ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, September 15, 2018

MAAFANDE WAWAPIGISHA KWATA WAUZA MBAO 0-1 CCM KIRUMBA MWANZA.



GSENGOtV/MWANZA
Bao pekee la mshambuliaji Abdalllah Ahmed ‘Shiboli’ dakika za nyongeza  likifungwa kwa njia ya penalti limeipa ushindi wa 1-0 JKT Tanzania dhidi ya wenyeji, Mbao FC Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.

DKT TIZEBA NA DKT MABULA WAMALIZA MGOGORO WA ARDHI WA CHAMA CHA USHIRIKA ULIODUMU KWA MIAKA 17


Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba akizungumza jambo kwa msisitizo wakati wa mkutano wa utatuzi wa mgogoro baina ya Chama Cha Ushirika Nyamatongo dhidi ya Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamatongo Ndg Itembwe Mnana uliodumu kwa miaka 17, Kushoto ni Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Angeline Mabula, Leo 8 Julai 2018. (Picha zote Na Mathias Canal-WK)
Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba akizungumza na wazee kijijini Nyamatongo wakati wa mkutano wa utatuzi wa mgogoro baina ya Chama Cha Ushirika Nyamatongo dhidi ya Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamatongo Ndg Itembwe Mnana uliodumu kwa miaka 17, Leo 8 julai 2018.
Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba, Naibu waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi Mhe. Dkt Angeline Mabula  wakiwa katika picha ya pamoja na wananchi wa kijiji cha Nyamatongo mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa utatuzi wa mgogoro baina ya Chama Cha Ushirika Nyamatongo dhidi ya Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamatongo Ndg Itembwe Mnana uliodumu kwa miaka 17, Leo 8 Julai 2018.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Angeline Mabula akizungumza jambo wakati wa mkutano wa utatuzi wa mgogoro baada ya Chama Cha Ushirika Nyamatongo dhidi ya Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamatongo Ndg Itembwe Mnana uliodumu kwa miaka 17, Leo 8 Julai 2018.
Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamatongo Ndg Itembwe Mnana (Kushoto) akisalimiana na Mwenyekiti wa Chama cha ushirika Nyamatongo Ndg Willium Elikana mara baada ya kuridhia mgogoro kumalizika.

Na Mathias Canal, Sengerema-Mwanza

Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba pamoja na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Angeline Mabula wametatua mgogoro baina ya Chama Cha Ushirika Nyamatongo dhidi ya Mwenyekiti wa kijiji cha Nyamatongo Ndg Itembwe Mnana uliodumu kwa miaka 17.

Mgogoro huo umemalizika kwa maelewano ya pande zote mbili kuwa na kauli moja ambapo Mwenyekiti wa kijiji hicho amekubali kuketi meza moja na Uongozi wa chama hicho cha ushirika ili kukubaliana namna bora ya kuchochea Maendeleo katika kijiji na Taifa kwa ujumla badala ya kuendeleza mgogoro usiokuwa na maslahi kwa pande zote.

Alisisitiza umuhimu wa ushirika nchini ambapo aliwaeleza wananchi hao kutoendeleza vita ya kutokuwa na maelewano kwani kufanya hivyo kunarudisha nyuma shughuli za Maendeleo ya kijiji na Taifa kwa ujumla wake.

Pia, Dkt Tizeba ametangaza Kiama kwa maafisa ugani wanaokaa maofisini badala ya kuwasaidia wakulima kwenye hatua muhimu za uandaaji wa shamba na hatimaye wakati wa Kilimo.

Katika mkutano huo Naibu Waziri wa Ardhi, nyumba na Maendeleo ya makazi Mhe Dkt Angelina Mabula aliwataka wananchi hao kuwa na utamaduni wa kuketi pamoja na kujadili changamoto zinazowakabili ili kuzitatua kwa manufaa yao binafsi na Taifa kwa ujumla.

Alisisitiza kuwa migogoro kama hiyo haihitaji sintofahamu ya mashitaka ya muda mrefu kwani kufanya hivyo ni kutengeneza uhasama usio kuwa na sababu ilihali wote ni watanzania.

Dkt Mabula aliongeza kuwa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli imekusudia kutatua changamoto zote zinazohusisha wananchi katika migogoro ya ardhi pamoja na kadhia zingine zote.

Mgogoro huo ambao ulianza tangu mwaka 2001 umekuwa na hatua za kushitakiana baina ya Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyamatongo dhidi ya Chama cha ushirika Nyamatongo katika maeneo mbalimbali tangu mwaka 2001 ambapo awali ulitolewa maamuzi katika ngazi ya baraza la kijiji baadae baraza la kata na hatimaye Baraza la Ardhi la Wilaya ya Sengerema ambalo ndilo liliamua kuvunja maamuzi yote ya baraza la kijiji na Kata ili kuanza upya usikilizwaji wa kesi hiyo.

Mara baada ya kumalizika kwa mgogoro huo wananchi kijijini hapo wamempongeza Waziri wa Kilimo Mhe Dkt Charles Tizeba pamoja na Naibu Waziri wa Ardhi, nyumba na Maendeleo ya makazi Mhe Dkt Angelina Mabula kwa kuzuru kijijini hapo hatimaye kutatua mgogoro huo ambao umekuwa sugu kwa miaka 17.

Aidha, katika mkutano huo wananchi wamepata nafasi ya kueleza kero mbalimbali zinazowakabili kijijini hapo ikiwemo ukosekanaji wa maji safi na salama, huku wengine wakieleza kusikitishwa na maafisa ugani kuketi maofisini pasina kuzuru kwa wakulima ili kuwafundisha mbinu bora za Kilimo.

DKT TIZEBA AITAKA CRDB KULIPA FEDHA ZA USHIRIKA (KCU)

Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akisisitiza jambo wakati akizungumza na wadau wa Kahawa Wilayani Muleba wakati wa ziara ya siku tatu ya kikazi Mkoani Kagera, Jana 12 Julai 2018. (Picha Zote Na Mathias Canal-WK)
Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akisalimiana na Mbunge wa Jimbo la Muleba kusini Mhe. Prof Anna Tibaijuka kabla ya mkutano na wadau wa Kahawa Wilayani Muleba wakati wa ziara ya siku tatu ya kikazi Mkoani Kagera, Jana 12 Julai 2018.
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage akimakabidhi muongozo wa ujenzi wa viwanda Mkuu wa Wilayani ya Muleba Mhe Richard Ruyango mara baada ya kuwasili Wilayani humo kwa ajili ya mkutano wa wadau wa Kahawa wakati wa ziara ya siku tatu ya kikazi Mkoani Kagera, Jana 12 Julai 2018. Mwingine pichani ni Mkurugenzi wa viwanda vidogo na biashara ndogo kutoka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Dkt Consolata Ishebali.
Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba akisisitiza jambo wakati akizungumza na wadau wa Kahawa Wilayani Muleba wakati wa ziara ya siku tatu ya kikazi Mkoani Kagera, Jana 12 Julai 2018. 

Na Mathias Canal-WK, Muleba-Kagera

Waziri wa Kilimo Mhe. Dkt Charles Tizeba Jana 12 Julai 2018 ameitaka Benki ya CRDB kulipa haraka malipo ya fedha za Ushirika za Chama Kikuu cha Kagera (KCU) kulingana na hatma ya kesi iliyokuwa mahakamani mwaka 2003 ambapo wakulima walikuwa wakikatwa kiasi cha shilingi 10 kwa kila kilo moja ya Kahawa ili kujenga mfuko wa Mazao kwa miaka mitatu kuanzia mwaka 1990 hadi 1993.

Dkt Tizeba ametoa agizo hilo wakati akizungumza kwenye mkutano uliowakutanisha wadau wa Kahawa Wilayani Muleba ikiwa ni siku ya tatu ya ziara ya kikazi mkoani Kagera iliyoanza Juzi 10 Julai 2018 na kuhudhuriwa pia na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage.

Swala la madai hayo katika mkutano huo liliibuka baada ya baadhi ya wakulima kuonyesha vitabu vya mfuko huo ambapo makato hayo ya shilingi 10 kwa kilo kwa kipindi cha miaka mitatu jinsi ambavyo yalikuwa yakifanyika.

Madai ya wakulima hao yamekuwa yakilalamikiwa kwa kipindi kirefu na kuchangia kwa kiasi kikubwa kupungua kwa imani ya wakulima kwa chama kikuu cha ushirika Kagera (KCU).

Chanzo cha kesi hiyo ni baada ya Benki ya CRDB kuzuia fedha za malipo yaliyotokana na mauzo ya Kahawa ili kulipia deni la msimu wa mwaka 1997/1998.

Hukumu ya kesi iliyotolewa tarehe 28 Octoba 2009 na mfuko wa Mazao wa wakulima Mkoani Kagera kupewa tahfifu ulizoomba ambapo tangu wakati huo Benki ya CRDB iliweza kulipa fedha za mfuko ilizochukua kiasi cha shilingi milioni 525 na fedha zilizobaki bado hazijalipwa kwa kisingizio cha kuwa na nia ya kukata rufaa ambayo bado haijakatwa ambapo hata hivyo hawawezi kukata rufaa kutokana na muda kuwa umepita.

Dkt Tizeba alisema kuwa Jumla ya madai hayo sambamba na riba ni shilingi Bilioni sita za kitanzania huku akisisitiza kuwa Benki hiyo ya CRDB inapaswa kuwa mfano wa Benki zingine nchini hivyo kushindwa kuwalipa wakulima kwa wakati ni kushindwa kwenda na serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli.

Wakati huo huo Waziri Tizeba aliagiza Halmashauri zote nchini zinazolima Kahawa kusimamia ukusanyaji wa Kahawa kwenda vya Msingi (AMCOS) kwani kutokana na usimamizi huo ndio hupata ushuru wa Halmshauri.

MWISHO.

MKUU WA WILAYA MISUNGWI AGOMA KUKABIDHI PIKIPIKI KWA AFISA ELIMU KATA KISA MIMBA ZA WANAFUNZI


NA GSENGOtV

MKUU wa Wilaya ya Misungwi Juma Sweda ameahirisha zoezi la kukabidhi pikipiki kwa Afisa Elimu kata ya Igokelo Baraka Dede Japhet  kufuatia shutuma zinazotajwa dhidi yake kuwalea na kuwakingia kifua watu wanaotajwa kuwapa mimba watoto wa shule za kata yake. 

Kwa wilaya ya Misungwi kata ya Igokelo inatajwa kuongoza kwa  vitendo vya wanafunzi kupata ujauzito wakiwa mashuleni hali inayosababisha wanafunzi hao kukatisha masomo.

Kwa upande wake Afisa huyo amejitetea kwa kusema kuwa hatua zote stahiki zilikuwa zikichukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwakama watuhumiwa kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria.

"Hata walionaswa jana, tumewakamata na kuwaripoti kwa vyombo vya dola na  taarifa zao tumeziandikia taarifa, tulikuwa na mtendaji wa kata lakini nashangaa kuambiwa kwamba sichukuwi hatua" alisema Dede

Ili kuwaondolea adha ya usafiri na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi, Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI ilikabidhi pikipiki 180 kwa kata mbalimbali za mkoa wa Mwanza, ambapo kwa wilaya ya Misungwi, pikipiki 26 zimekabidhiwa kwa maafisa hao huku pikipiki moja ikisalia kufanya idadi ya pikipiki 27 kwa kata hiyo yenye changamoto, mpaka pale uchunguzi utakapo kamilika. 

Friday, September 14, 2018

POLISI MWANZA WAMNASA JAMAA ANAYEWANYWESHA WANAWAKE DAWA ZA KULEVYA NA KUWABAKA



NA ZEPHANIA MANDIA/GSENGOtV

Mtu mmoja anashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza  kwa kujihusisha na vitendo vya kuwanywesha dawa za kulevya wanawake na kisha kuwabaka. 

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa  Mwanza, Jonathan Shanna, amemtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni  Kennedy Obworo, mwenye umri wa miaka 35, ambaye amekuwa akiwawekea wanawake dawa za kulevya katika vinywaji na kisha kuwabaka na kuwaibia vitu walivyonavyo.

Katika tukio jingine, jeshi hilo linamshikilia Sheshe Mazoya, anayedaiwa kuwa  mganga wa kienyeji mkazi wa Wilaya ya Magu kwa kosa la kukutwa na nyara mbalimbali za serikali ikiwemo mikia miwili ya nyumbu na pembe moja ya swala, kucha za Simba na miiba ya nungunungu ambavyo alikuwa anavimiliki kinyume na sheria.

Aidha, Kamanda Shanna amesema wanamshikilia mwanamke anayefahamika kwa jina la Sonia Fanuel kwa kosa la wizi wa kufungua milango kwa kutumia funguo bandia.

Kamanda Shanna ambaye amechukua nafasi ya Kamanda Ahmed Msangi aliyehamishiwa makao makuu, amesema watuhumiwa wote  wanatarajiwa kufikishwa Mahakamani Jumatatu ijayo kujibu  tuhuma zinazowakabili.

MAREKANI:- VIKWAZO DHIDI YA ZIMBABWE VITAENDELEA KUWEPO.

Marekani: Vikwazo dhidi ya Zimbabwe vitaendelea kuwepo
Manisha Singh.
Serikali ya Marekani haitaondoa vikwazo ilivyoiwekea Zimbabwe hadi pale serikali mpya ya Rais Emmerson Mnangagwa wa nchi hiyo itakapodhihirisha kuwa inabadili mielekeo yake. Hayo yameelezwa na afisa wa ngazi ya juu wa masuala ya uchumi wa Marekani.
Naibu Waziri wa Uchumi na Masuala ya Biashara wa Marekani, Manisha Singh amesema kuwa watu na taasisi 141 za Zimbabwe akiwemo Rais wa sasa Emmerson Mnangagwa na rais wa zamani wa nchi hiyo Robert Mugabe wako chini ya vikwazo vya Marekani.  Amesema mashinikizo ya Marekani kwa Zimbabwe bado yako palepale.

Amedai kuwa Washington inajaribu kutumia njia ya mashinikizo ili kushawishi mageuzi ya kisiasa na kiuchumi na kuheshimiwa haki za binadamu. Naibu Waziri wa Uchumi na Masuala ya Biashara wa Marekani ameongeza kuwa Washington itaanzisha tena uhusiano wa kawaida na Zimbabwe baada ya kushuhudia mabadiliko ya msingi nchini humo. 
Rais Emmerson Mnangagwa wa Zimbabwe.
Mnangagwa ametoa wito wa kuondolewa vikwazo hivyo vya Marekani dhidi ya maafisa wa chama tawala Zanu-pf, maafisa wa ngazi ya juu wa jeshi na baadhi ya mashirika yanayomilikiwa na serikali vilivyowekwa wakati wa utawala wa Mugabe kwa sababu ya kile ilichokitaja kuwa ni ukiukaji wa haki za binadamu na demokrasia.

BONDIA HASSAN MWAKINYO AMWAGIWA PESA BUNGENI.


Mtanzania kutoka Tanga, Bondia Hassan Mwakinyo leo ametembelea Bungeni Dodoma katika kikao chao cha mwisho  ambapo wabunge wameweza kumchangia T.sh 20,000 kwa kila mbunge kutoka kwenye posho zao na kufikisha Milioni 7.72 kama zawadi mara baada ya kuitangaza vyema Tanzania kimataifa alipoibuka na ushindi katika mchuano mkali uliomkutanisha na Bondia Sam Eggington wa Uingereza katika pambano lililochezewa Birmingham.

Hayo yamejiri baada ya Mbunge wa Sumbawanga Mjini (CCM), Aeshi Hilaly kuomba mwongozo wa kwa wa Spika, Job Ndugai.

“Tumekuwa tukiwachangia sana mamisi humu ndani, leo hii tunaomba mwongozo wako angalau tumchangie Tsh. 20,000 kila mmoja, naomba mwongozo wako spika,”alisema Aeshi.

Wabunge waliitika kwa makofi mengi kisha Spika Job Ndugai alipitisha mwongozo huo mara moja kila mbunge atakatwa posho yake.

Mwakinyo alimtwanga Eggington ambaye aliwahi kuwa Bondia namba moja wa Uingereza sekunde ya 45 ya mzunguko wa pili wa mchezo huo na kutangazwa Bingwa.

Aidha, Wabunge wamemtakia Hassan Mwakinyo mafanikio mema katika michuano inayoendelea na kumsihi aendelee kuiwakilisha vyema Tanzania kimataifa ili kuijengea nchi heshima.

MABONDIA WAPIMA UZITO KUPIGANA KESHO SEPTEMBA 15 UWANJA WA NDANI WATAIFA

Promota wa mchezo wa masumbwi nchini Rajabu mhamila 'Super D' katikati akiwainuwa mikono juu mabondia Georger Dimoso kushoto na Abdallah Pazi 'Dula Mbabe' baada ya kupima uzito kwa ajili ya kuzipiga kesho jumamosi Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa Picha zote na SUPER D BOXING NEWS

Mabondia Georger Dimoso kushoto akitambiana na Abdallah Pazi 'Dula Mbabe' baada ya upimaji wa uzito na Afya kwa ajili ya mpambano wao utakaofanyika Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa.

Mabondia Saidi Bakari 'Kidedea' kushoto akitunishiana misuli na Vicent Mbilinyi baada ya kumaliza kupima uzito katikati ni Promota Rajabu Mhamila 'Super D baada ya kupima uzito kwa ajili ya mpambano wao utakaofanyika jumamosi ya Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa 
Bondia Frank John kushoto akitunishiana misuli na Bakari Mbede wakati wa kupima uzito kwa mabondia hawo watazipiga siku ya jumamosi  Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa .
Mabondia Imani Mapambano kushoto akitambiana na Paul Kamata baada ya upimaji wa uzito na Afya kwa ajili ya mpambano wao utakaofanyika Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa.

Mabondia Saidi Zungu  kushoto akitambiana na Tonny Rashidi baada ya upimaji wa uzito na Afya kwa ajili ya mpambano wao utakaofanyika Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa.
Promota wa mchezo wa masumbwi nchini Rajabu mhamila 'Super D' katikati akiwainuwa mikono juu mabondia Saidi Zungu kushoto na Tonny Rashidi baada ya kupima uzito kwa ajili ya kuzipiga kesho jumamosi Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa 

Promota wa mchezo wa masumbwi nchini Rajabu mhamila 'Super D' katikati akiwainuwa mikono juu mabondia Fred Sayunu kushoto na Haidary Mchanjo baada ya kupima uzito kwa ajili ya kuzipiga kesho jumamosi Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa. 
Mabondia Frdy Sayuni  kushoto akitambiana na Haidary Mchanjo baada ya upimaji wa uzito na Afya kwa ajili ya mpambano wao utakaofanyika Septemba 15 katika uwanja wa ndani wa Taifa.

PROMOTA WA MPAMBANO WA MASUMBWI NCHINI RAJABU MHAMILA AKIZUNGUMZA NA WAANDISHI WA HABARI

Thursday, September 13, 2018

MISUNGWI YAPIGA MARUFUKU MADINI KUCHENJULIWA NJE YA WILAYA.


Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza imepiga marufuku usafirishaji wa madini ghafi kwenda wilaya nyingine kwa lengo la kuchenjuliwa.

Akzungumza kwenye Mkutano wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya Misungwi, Mkuu wa Wilaya Misungwi mkoani Mwanza Juma Sweda alipiga marufuku na kuwataka madiwani na watendaji kusimamia kikamilifu utekelezaji wake.

Alisema lengo la kuzuia usafirishaji wa madini ghafi hayo ikiwemo dhahabu na chuma ni kuhakikisha uchenjuaji unafanyikia ndani ya wilaya ya Misungwi ili kuongeza fursa ya ajira kwa wananchi pamoja na ukusanyaji mapato.

Naye  Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Kisena Mabuba alisema zuio hilo litasaidia kudhibiti mapato yanayopatikana kutokana na shughuli za uchenjuaji madini hivyo atashirikiana vyema na watendaji wake ili kutekeleza vyema zuio hilo.

Aidha Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Misungwi, Antony Bahebe aliwataka madiwani na watendaji wa halmashauri hiyo kuhakikisha wanasimamia vyema suala la ukusanyaji wa mapato ili kufikia lengo la asilimia 100 mwaka 2018/19 kutoka asilimia 80.16 mwaka 2017/18 huku wakihakikisha hakuna upotevu wa mapato ya halmashauri hiyo na kwamba watakaoshindwa kufanya hivyo hatua za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yao.

VIDEO: ANAYEKUFA AKIFANYA MAPENZI MBONA HAWAENDI KUCHOMA MOTO KITANDA? - WAZIRI LUGOLA


Waziri wa Mambo ya ndani ya nchi Kangi Lugola wakati akijibu maswali ya baadhi ya wabunge waliohoji Serikali inachukua hatua gani kwa kujitokeza mara kwa mara baadhi ya raia kufa wakiwa wameshikiliwa mahabusu na Polisi.

MHE. MAVUNDE NI MGENI RASMI FAINALI YA ANGELINE JIMBO CUP 2018



GSENGOtV

ALHAMISI YA TEREHE 13/09/2018
NUSU FAINALI YA KWANZA SHIBULA v/s IBUNGILO

IJUMAA YA TEREHE 14/09/2018
NUSU FAINALI YA PILI NYAKATO v/s KIRUMBA

JUMATATU YA TAREHE 17/09/2018
SAA 8 MCHANA - MCHEZO KUSAKA NAFASI YA 3
SAA 10 JIONI      - MCHEZO WAFAINALI KUMSAKA BINGWA

MGENI RASMI WA FAINALI YA ANGELINE JIMBO CUP 2018 NI NAIBU WAZIRI SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WALEMAVU MHE. ATHONY MAVUNDE.

NJAA MBAYA MAJANGILI WA WANYAMA PORI SASA WATUMIA NJIA ZA UCHOCHORONI.

Afisa Habari na Mawasiliano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA),Twaha Twaibu kushoto akiwa na Mkuu wa Kanda ya Kaskazini Magharibi-Msolwa Pori la Akiba Selous Augustine Ngimilanga wakiangalia baiskeli zilizotumiwa na majangiri kubebea wanyamapori.
 Ofisa Kampuni ya uwindaji wa Kitalii ya Mkwawa Hunting Safari Benson Kibonde akisisitiza jambo mbele ya Afisa Habari na Mawasiliano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA),Twaha Twaibu kushoto na Mkuu wa Kanda ya Kaskazini Magharibi - Msolwa Pori la Akiba Selous Augustine Ngimilanga.
 Mofisa wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA), katika Pori la Akiba Selous Kanda ya Kaskazini Magharibi -Msolwa wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi na Kijiji cha Msolwa Station Kilombero mkoani Morogoro mara baada ya kutembelea Shule ya Msingi Ukombozi kujionea mchango wa uhifadhi kutoka kampuni za uwindaji wa kitalii. 
 Mofisa wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA), katika Pori la Akiba Selous Kanda ya Kaskazini Magharibi -Msolwa wakiwa katika picha ya  na viongozi na Kijiji cha Msolwa Station Kilombero mkoani Morogoro baada ya kutembelea jengo la Ofisi ya Kijiji cha Msolwa Station linalojengwa kwa fedha kutoka kampuni za uwindaji wa kitalii. 
 Afisa habari na Mawasiliano wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA), Twaha Twahibu akisisitiza jambo mbele ya viongozi wa Kijiji cha Msolwa Station kinachopakana na Pori la Akiba Selous Kanda ya Kaskazini Magharibi-Msolwa mkoani Morogoro.

KILOMBERO
MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA), katika kipindi cha mwaka 2017/18 imekamata baiskeli 60 za watuhumiwa wa ujangiri zikiwamo Nyaya zaidi ya 100 ndani ya Pori la Akiba Selous Kanda ya Kaskazini Magharibi- Msolwa.
Hatua hiyo imekuja baada ya wananchi waishio jirani na Pori hilo la Akiba kubuni mbinu zaidi ya kuuwa wanyamapori ambapo sasa wameanza kutumia Vuvuzela zinazotumiwa na mashabiki kwenye michezo hususani mpira wa miguu.
Vifaa hivyo hutumiwa usiku na majangiri wakiwa na tochi ambapo hupuliza Vuvuzela kwa lengo la kuwachanganya wanyamapori huku wakiwa wamewamulika na mwanga wa tochi kisha kuwavamia na kuwakatakata miguu.
Mkuu wa Kanda hiyo, Augustine Ngimilanga akizungumzia zaidi anasema tayari wameweza kukabiliana na aina hiyo mpya ujangiri na kupitia askari wa doria walikamata watuhumiwa wa ujangiri waliofunguliwa kesi 92 zinazoendelea Mahakama ya wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro.
“Watuhumiwa 18 wameshasomewa kesi zao na kuhukumiwa baadhi wamefungwa miaka mitatu na wengine miaka tisa jela,” alisema Ngimilanga na kuongeza:
“Tumeweka mkakati wa kuhakikisha maeneo yote yanakuwa na ulinzi wa doria muda wote, hii ni pamoja na kukabiliana nao kabla hawajaingia na kufanya uharibifu,” alisema.
Ngimilanga alizitaja changamoto katika kukabiliana na ujangiri zinachangiwa na hali ya umasikini ya wananchi katika vijiji vinavyopakana na pori hilo.
“Baadhi ya wananchi wameona njia pekee ya kujipatia kipato ni kufanya ujangiri wa kuwinda wanyama na kuvua samaki kwenye mito ndani ya Pori la Akiba.
“Mbali ya kukamata tunaowakuta, tumeendelea pia kutoa elimu maeneo mbalimbali ya vijiji ikiwamo mikutano ya vijiji kwa kuwaelimisha na kuwapa mifano ya umuhimu wa kutunza haya maeneo,”alisema.
Alisema ili kuwasaidia kutoshiriki vitendo vya kijangiri wamekuwa wakiwapa elimu ya ujasiriamali wa ufugaji nyuki kwa ajili ya kuvuna asali na kuuza kwa lengo la kujiongezea kipato.

“Tumewasaidia kupata ufadhili wa mizinga kutoka kwa wawekezaji ili waendeshe shughuli za ufugaji kwenye msitu wa Magombela,” alisema Ngimilanga.

HOMA YA MPAMBANO WA MASUMBWI SEPTEMBA 15 TAIFA WAZIDI KUPAMBA MOTO


Na Mwandishi Wetu/GSENGOtV

YAKIWA wamebakia masaa machache sana kabla ya ule mtanange wa masumbwi utakao wakutanisha mabondia Haidary Mchanjo na Fredy Sayuni utakaofanyika Septemba 15 katika ukumbi wa uwanja wa ndani wa Taifa jumamosi hii

Mabondia hao wamendelea na mazoezi na sasa wapo tayali kwa mpambano uho akizungumza na mwandishi wa habari hizi mratibu wa mpambano uho Rajabu Mhamila 'Super D'  amesema kuwa maandalizi yote yamekamilika kwa sasa wanacho subili ni siku tu ya mpambano kwani mabondia wote wapo na molali ya hali ya juu ya kutaka kupigana

na akuna bondia yoyote alieleta malalamiko kuwa awezi kupanda ulingoni siku hiyo mabondia wote tulio ingia nao mkataba wa kuzipiga watapigana siku hiyo

mbali na mpambao uho unaosubiliwa kwa hamu na mashabiki lukuki kutakuwa na mapambano mengine ya kukata na shoka ambapo bondia

Abdallah Pazi 'Dula Mbabe' atazipiga na Georger Dimoso na Vicent Mbilinyi atavaana na Saidi Kidedea Hassani Mijugu na Martn Shekivuli Mohamedi Kashinde atakumbana na Sadiki Momba na Imani Mapambano na Paul Kamata wakati Frank John atazipiga na Bakari Mbede

Mpambano uhu umepewa Baraka zote na kamati ya kusimamia ngumi za kulipwa chini inayo ongozwa na Emanuel Saleh

mabondia wote watapima uzito na Afya katika soko la Vetenali lililopo Tazara siku ya Ijumaa na watacheza jumamosi katika uwanja wa ndani ya Taifa 'Indoor Stadium'

JOHN GUNINITA WA CCM HATUNAYE.


Aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana CCM (UVCCM), Taifa na baadaye akawa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita amefariki dunia leo Alhamisi, Septemba 13, 2018 alfajiri katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu.

Taarifa za msiba huo zimethibitishwa na mdogo wake na marehemu, Gerald Guninita ambaye naye aliyewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kilolo wakati wa Uongozi wa Awamu ya Nne.

Wednesday, September 12, 2018

DIWANI AZOMEWA MBELE YA MKUU WA WILAYA.





Na Ahmed Mmow, Kilwa
DIWANI wa kata ya Njinjo wilaya ya Kilwa, Ashura Kuchao amejikuta katika wakati mgumu kufuatia kuzomewa na wananchi mbele ya Mkuu wa Wilaya hiyo Christopher Ngubiagai.

Zomeazomea hiyo ilitokea  katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na Mkuu huyo wa wilaya ili kusikiliza kero za wananchi hao.

Ngubiagai alikwenda kijijini hapo kufuatia wananchi hao kumlalamikia mwenyekiti wao wa kijiji Abdulmalick Mnakatu kushindwa kuitisha mikutano mikuu ya kijiji tangu alipochaguliwa na wananchi.

Mwenyekiti ambaye alitangaza kujiuzulu siku moja baada ya kusikia ziara ya Mkuu wa Wilaya alipata fursa ya kusalimiana na Mkuu huyo wa wilaya na kumweleza kuwa mikutano ilikuwa haifanyiki kwa sababu wajumbe wake wengi wa Halmashauri ya kijiji walikuwa bize na kilimo hivyo alishindwa kuwapata kila alipokuwa akiwahitaji.

Wakati wa mkutano huo, Mkuu wa wilaya alianza kupokea kero za wananchi ambapo wananchi mbalimbali walieleza kuwa diwani wao hajaitisha mikutano na wananchi kutoa taarifa za mapato na matumizi na fedha zinazoletwa na serikali ngazi ya kata na kibaya zaidi hata kero za wananchi hazijui.

“Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya, sisi tunavyofahamu diwani anatakiwa akusanye kero kutoka kwetu lakini diwani wetu hajawahi kukutana na sisi hata siku moja na kila siku anakwenda kwenye vikao vya Halmashauri, hizo kero anazopeleka huko anazitoa wapi.” Alisema mwananchi mmoja na kusababisha wananchi wapige makofi.

Kutokana na kero hiyo, Mkuu wa Wilaya aliwaambia wananchi hao kuwa kero hiyo anatakiwa aijibu diwani mwenyewe ambapo alipompa nafasi hiyo, diwani huyo aliwaambia wananchi kuwa yeye anasikiliza kero kutoka kwa watendaji wa vijiji na anazipeleka Halmashauri.

“Mimi nasubiri kero kutoka kwa watendaji wa vijiji na ndio nazipeleka Halmashauri, habari ndio hiyo” alisema diwani huyo na kusababisha hasira kwa wananchi hao.

Wananchi hao waliendelea kumuuliza Mkuu wa Wilaya diwani huyo anazipata wapo kero za wananchi hao wakati vijiji vyenyewe havifanyi mikutano na ndio sababu ya kumuomba Mkuu wa Wilaya afike kijijini, hata hivyo diwani huyo aligoma kujibu swali hilo akidai ameshawazoea wananchi hao, hivyo hawamsumbui.

Hata hivyo, Mkuu wa Wilaya aliwaambia wananchi hao kuwa akili ziko kichwani mwao na kwamba uchaguzi unakuja, hivyo adhabu ya viongozi wa kuchaguliwa iko mikononi mwao.

MAGEUZI SEKTA YA UVUVI PANGANI,DC NA VIONGOZI WAKUTANA NA WAZIRI MPINA JIJINI DODOMA


 MKUU wa wilaya ya Pangani Zainabu Issa kulia akiwa na Katibu Tawala wa wilaya ya Pangani wakimsubiri Waziri wa Uvuvi na Mifugo Mh. Luhaga Mpina kufanya nae kikao ikiwa ni mpango mkakati wa kufanikisha changamoto na utekelezaji wa ubunifu katika sekta ya uvuvi inayoongoza kwa mapato na kutegemewa na wakazi wengi wa Pangani kulia ni Afisa Tawala wa wilaya ya Pangani Gipson
Waziri wa Uvuvi na Mifugo Mh. Luhaga Mpina kulia akimlaka Mkuu wa wilaya ya Pangani Zainabu Issa wakati alipofika ofisini kwake kwa mazungumzo kufanikisha changamoto na utekelezaji wa ubunifu katika sekta ya uvuvi inayoongoza kwa mapato na kutegemewa na wakazi wengi wa Pangani.
Waziri wa Uvuvi na Mifugo Mh. Luhaga Mpina akiwa na Mkuu wa wilaya ya Pangani wa pili kutoka kushoto na Katibu Tawala wa wilaya ya Pangani kulia akiwa na Afisa tawala wa wilaya hiyo Gipson mara baada ya kufanya mazungumzo nao leo Jijini Dodoma

Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Pangani ikiongozwa na Mh. Zainab Abdallah kwa ushirikiano na Ofisi ya Mbunge imefanya ziara ya kikazi makao makuu ya nchi mkoani Dodoma ikiwemo kukutana na kuwa na kikao na Waziri wa Uvuvi na Mifugo Mh. Luhaga Mpina na kufanikisha changamoto na utekelezaji wa ubunifu katika sekta ya uvuvi inayoongoza kwa mapato na kutegemewa na wakazi wengi wa Pangani.

Akizungumza baada ya kikao hicho Mkuu wa wilaya ya Pangani Zainabu Abdallah alisema kikao hicho kilihusisha agenda nne kubwa muhimu kwa ukombozi wa sekta ya Uvuvi wilayani Pangani ikiwemo Upatikanaji wa mashine ya Storage (Compressor) na Jokofu kwa ajili ya kuhifadhi mazao ya baharini kwa ajili ya soko kubwa la Samaki Pangani Mashariki ambalo ujenzi wake umefanikishwa na mapato ya ndani ya halmashauri.

Hatua hiyo imepelekea Waziri Mpina kuwapongeza kwa jitihada za awali na kuahidi kuwa Wizara yake itatoa fedha ili jokofu na compressor vipatikane mara moja na soko lianze kufanya kazi.

Alisema kuelekea utekelezaji wa kampeni ya “VIJANA NI WAKATI WETU” iliofanyika Wilaya ya Pangani; sekta ya uvuvi ndio iliongoza kwa uandikishaji wa Vijana wengi.

Hivyo pia Mkuu huyo wa wilaya aliwasilisha  ombi la kupata Engine za Boti za uvuvi kwa ajili ya vikundi vya vijana walio tayari kujiajiri na kujipatia kipato kupitia sekta hii. Wizara kupitia ruzuku yake itagharamia 40% na 60% igharamie halmashauri husika.

Ambapo kufuatilia ombo hilo Wizara hiyo  imeridhia kutoa Engine za kutosha kwa vijana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kupitia Halmashauri itatumia mfuko wa vijana na mfuko wa Jimbo kufanikisha upatikanaji wa Engine hizi ili vijana wapate vifaa hivi vya kisasa na utaratibu utawekwa kupitia Idara ya Vijana ya wilaya juu ya usimamizi na mafunzo. Hii ni ishara ya ukombozi kwa vijana wa Pangani.

Mkuu huyo wilaya alisema pia walizungumzia suala la kuanzishwe kwa  Chuo cha mafunzo na utaalamu kwa Sekta ya Uvuvi Pangani ikiwa ni kuelekea kupata muarobaini wa sintofahamu ya Chuo cha KIM kurudi mikononi mwa wananchi na kuwanufaisha zaidi ya ilivyo sasa.

Hatua hiyo ilimlazimu Waziri huyo kuamua kuunda timu ya wataalamu ambayo itakwenda Pangani mara moja kuchunguza suala hili ili ripoti itakayo wasilishwa aweze kuitolea maamuzi kwa maslahi mapana ya wana Pangani.
.
Sambamba na hilo liligusiwa suala la ujenzi wa  Soko la Samaki na Dagaa Kipumbwi ambapo Waziri Mpina ameweka wazi kuwa suala hili lipo sasa kwenye mipango ya Wizara na kilichobaki ni Utekelezaji wa haraka. na ikumbukwe mipango ilishawekwa sawa juu ya urasimishaji wa Bandari ya Kipumbwi.

" Sekta ya Mifugo nayo  haikuachwa nyuma kwa Waziri kuhahidi upatikanaji wa Rambo la malisho ya mifugo Pangani ikiwa ni faraja iliopotea muda mrefu kwa wafugaji wa Pangani "Alisema.

ASILIMIA KUBWA YA WATANZANIA HUPATA UPOFU KUTOKANA NA KUCHELEWA KUPATA TIBA


GSENGOtV


IMETAJWA kuwa asilimia kubwa ya watanzania hupata ulemevu wa macho au pengine upofu wa kudumu kutokana na kuchelewa kupata huduma au kuangukia mikononi mwa wahudumu wa afya wasio na sifa katika tasnia ya udaktari wa macho.

Hayo yamebainishwa hii leo na Rais wa Chama cha Madaktari wa Macho nchini Tanzania Dr. Joseph Masanja wakati wa utoaji huduma bure ya upimaji wa macho uliofanyika katika viwanja vya furahisha jijini Mwanza, huduma ikitolewa na Madaktari wanachama wa Otametria chini ya ufadhili wa Shirika lisilo la Kiserikali la Brien Holden Vision la nchini Marekani.

Amesema kuwa idadi kubwa ya wananchi mijini na vijijini wanapopatwa na changamoto yoyote ya afya ya macho wamekuwa wakikimbilia vituo vya huduma za bei nafuu bila kujali viwango au sifa za wauguzi  wanaowahudumia kwa kuwa inakuwa ngumu kwao kuwabaini.
Rais huyo wa Chama cha Madaktari wa Macho ameiomba Serikali kwa kutumia vyombo vyake vya ulinzi na usalama kuendesha oparesheni kuvibaini vituo vya afya vyenye wauguzi ‘Vishoka’ wanaojiingiza kwenye taaluma ya afya na kutoa huduma za ulaghai zisizo na viwango hali inayosababisha taifa kuwa na idadi kubwa ya watu wenye ulemavu wa macho.

“Vishoka wamekuwa wakiwavutia wateja kwenye vituo vyao kwa kigezo cha unafuu wa bei na hilo ndilo limekuwa tatizo linalosababisha baadhi ya wananchi wenye matatizo hata yaliyo madogo kukomaa na baadaye kuwa makubwa yanayopelekea ulemavu usiotibika, unaotokana na kuchelewa kuzipata huduma sahihi kwa muda na wakati” alisema Dr. Masanja

Kisha akaongeza “ Nawasihi wananchi wanaopata dalili au matatizo au pengine wale wanaotaka kujua afya ya macho, njia sahihi ni kwenda kwenye vituo vya afya vilivyosajiliwa ili wapate tiba iliyo sahihi”

 Mganga Mkuu wa Mkoa Mwanza Dr. Rutachunzibwa Thoma akitoa maelezo kwa wananchi jinsi ya kuzitumia vyema fursa mbalimbali za upimaji afya bure zinazotolewa na taasisi mbalimbali za Serikali na za kiraia. 

Licha ya kuahidi kulifikisha suala la ‘Oparesheni ya kubaini VISHOKA’ mbele ya  kamati ya Ulinzi na usalama inayoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, Mkuu wa wilaya ya Ilemela Dr. Severine Mlalika aliyekaimu ugeni rasmi  wa Mkuu wa Mkoa kwenye uzinduzi huo, amewataka wananchi kuwa na desturi ya kupima afya za uoni wao mara kwa mara ili kusaidia kujitambua ikiwa ni pamoja na kupata  huduma na ushauri  juu ya namna ya kuishi salama kwani asilimia kubwa ya utendaji na harakati za maisha ya mwanadamu hutegemea macho.

Amesema  kama wananchi watakuwa na mwamko wa kupima afya ya macho, itasaidia  jamii kutambua  na kujiepusha mazingira hatarishi yanavyoweza kuchangia madhara wanayoyapata na namna gani wanavyoweza kuishi salama kwa kujilinda.

Mkuu wa wilaya ya Ilemela Dr. Severine Mlalika akipima afya ya macho kwa moja ya madaktari viwanja vya Furahisha jijini Mwanza.
Dr. Moes Nasser ambaye ni mmoja wa wafadhili wa huduma hiyo ya upimaji wa macho akitoa ufafanuzi kwa mgeni rasmi  Mkuu wa wilaya ya Ilemela Dr. Severine Mlalika (kulia).
Edden Rodrick ambaye ni Mtaalam wa macho na Mwakilishi mkazi wa Shirika la Brien Holden Vision Institute la nchini Marekani akitoa maelezo kwa Mkuu wa wilaya ya Ilemela Dr. Severine Mlalika jinsi walivyojipanga katika suala la vitendea kazi kwa mpango huo wa upimaji.
Upimaji unaendelea....
Mmoja baada ya mwingine, wakubwa kwa wadogo.
Upimaji ukiendelea.
Kazi ikiendelea.
"Unaiona hii...." ni kama mmoja wa madaktari akimuuliza mwananchi aliyefika hapa kupima afya ya macho yake.


Mkuu wa wilaya ya Ilemela Dr. Severine Mlalika akikata utepe kuashiria uzinduzi wa upimaji afya kushoto ni Dr. Moes Nasser na Mganga Mkuu wa Mkoa Mwanza Dr. Rutachunzibwa Thoma.


Viwanja vya Furahisha.
Mwamko wa wananchi.
 Wananchi wanaozijali afya zao wamejitokeza hapa.
Maelezo mabanda mbalimbali ya utoaji huduma.
Vifaa vya upimaji...
Miwani...
Jicho limeona 'Selfie muhimu'
Huduma zikiendelea nao madaktari wakiendelea kuweka mikakati jinsi ya kufanikisha.
Picha ya pamoja.

ITAENDELEA TAKWIMU ZAJA