ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, April 11, 2025

IS SAMIA AKUTANA NA KUZUNGUMZA NA MMILIKI WA MANCHESTER UNITED IKULU JIJINI DAR ES SALAAM

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mmiliki wa Klabu ya Mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza Sir Jim Ratcliffe, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 11 Aprili, 2025. Katika mazungumzo yao Rais Dkt. Samia amemshukuru Sir Jim Ratcliffe kupitia Taasisi yake ya Six Rivers ambayo ina shughulika na masuala ya Uhifadhi, kwa namna inavyofanya vizuri katika kudhibiti muingiliano wa wanyamapori na binadamu kwa kushirikiana na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) pamoja na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI).

Kupitia Taasisi yake ya Six Rivers, Sir Jim Ratcliffe amebainisha kuwa Taasisi hiyo imedhamiria kurejesha hadhi ya Hifadhi ya Taifa ya Selous na kuwa na Wanyama wakubwa katika Hifadhi hiyo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Jezi ya Timu ya mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza iliyosainiwa na Wachezaji wa Timu hiyo kutoka kwa Mmiliki wa Klabu hiyo Sir Jim Ratcliffe, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 11 Aprili, 2025. Mmiliki wa Klabu hiyo Sir Jim Ratcliffe ameeleza dhamira yake ya kuitumia Klabu yake kutangaza utalii nchini Tanzania. Rais Dkt. Samia pia amemkaribisha Mmiliki huyo wa Club ya Manchester kuanzisha Vituo vya Mafunzo ya Michezo (Sports Academy) hapa nchini.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi zawadi ya picha, Mmiliki wa Klabu ya Mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza Sir Jim Ratcliffe, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 11 Aprili, 2025.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya mpira wa miguu kutoka kwa Sir Jim Ratcliffe Mmiliki wa Klabu ya Mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 11 Aprili, 2025.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiteta jambo na Mmiliki wa Klabu ya Mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza Sir Jim Ratcliffe, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 11 Aprili, 2025.

KANUNI ZA MAADILI YA UCHAGUZI KUSAINIWA KESHO.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Kailima Ramadhan.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Kailima Ramadhan.


Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, vyama vya siasa na Serikali kesho wanatarajiwa kusaini Kanuni za Maadili ya Uchaguzi yatakayotumika kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Akizungumza kwenye mahojiano maalum na vyombo vya habari mkoani Dodoma, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Kailima Ramadhan amesema chama cha siasa ambacho hakitasaini maadili hayo hakitaruhusiwa kushiriki kwenye uchaguzi huo.

Kailima amesema maadili hayo yameandaliwa kwa mujibu wa kifungu cha 162 (1), (2) na (3) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 ambacho kinaitaka Tume baada ya kushauriana na vyama vyote vya siasa na Serikali, kuandaa na kuchapisha katika Gazeti la Serikali Kanuni za Maadili ya Uchaguzi zitakazoainisha maadili ya vyama vya siasa, Serikali na Tume wakati wa kampeni za uchaguzi na uchaguzi na utaratibu wa utekelezaji wake.

Amesema kifungu hicho kinaelekeza kuwa kanuni za maadili zitasainiwa na kila chama cha siasa, kila mgombea kabla hajawasilisha fomu ya uteuzi, Serikali na Tume na zitapaswa kuzingatiwa na wahusika wote waliosaini. 

Ameongeza kuwa tayari maandalizi yote muhimu yameshafanyika na mawasiliano yameshafanyika baina ya Tume, Serikali na vyama vya siasa na kwamba kinachosubiriwa ni kuwasili kwa wahusika jijini Dodoma kwa ajili ya kusaini kanuni hizo za maadili kesho.

Amefafanua kuwa zoezi hilo litafanyika kwa siku moja tu na kwamba baada ya hapo chama ambacho hakijasaini kanuni hizo za maadili hakitapata fursa ya kusimamisha wagombea.

DKT. YONAZI AKUTANA NA UJUMBE WA IFAD NA TIMU YA WATAALAM NA WATEKELEZAJI WA PROGRAMU YA AFDP

 

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonaz akizungumza wakati wa kikao cha majumuisho (Wrap-Up Meeting) kilichohusisha Ujumbe Kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo(IFAD) na wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Posta Jijini Dodoma Tarehe 11 Aprili 2025


NA. MWANDISHI WETU - DODOMA

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughilikia Sera,Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi ameongoza kikao cha Majumuisho (wrap-up) cha Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo  (IFAD) na Timu ya Wataalamu wanaotekeleza Programu ya Kuendeleza  Kilimo na Uvuvi (AFDP) baada ya kukamilika kwa ziara ya kutembelea na kukagua maeneo yanayotekeleza programu hiyo.

Timu hiyo ya IFAD na wataalam ilitembelea maeneo mbalimbali ya utekelezaji wa Programu ya AFDP kwa sekta za kilimo na uvuvi Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar. Aidha, timu hiyo ilitembelea pia Mradi wa Kuimarisha na Kuendeleza Upatikanaji wa Lishe kwa Wafugaji Wadogo wa Viumbe Maji na Wakulima wa Mwani (ARNSA).

Kikao hicho kimefanyika tarehe 11 Aprili, 2025 katika Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopo mtaa wa Reli jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo Nchini (IFAD) Bw. Sakphouseth Meng akizungumza wakati wa kikao cha majumuisho (Wrap-Up Meeting) kilichohusisha Ujumbe Kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo(IFAD) na wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Posta Jijini Dodoma Tarehe 11 Aprili 2025

Katika kikao hicho Katibu Mkuu Dkt. Yonazi alipongeza maendeleo mazuri ya utekelezaji program hiyo na kusema kazi zinazofanywa na mradi kwa sasa zinaonekana huku akiwasihi kuendelea kuimarisha mafanikio hayo na kuahidi kushirikiana  na TAMISEMI kwa lengo la kuwafikia wanufaika wa program hii.

Baadhi ya wajumbe wakati wa kikao cha majumuisho (Wrap-Up Meeting) kilichohusisha Ujumbe Kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Posta Jijini Dodoma Tarehe 11 Aprili 2025
Baadhi ya wajumbe wakati wa kikao cha majumuisho (Wrap-Up Meeting) kilichohusisha Ujumbe Kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Posta Jijini Dodoma Tarehe 11 Aprili 2025


“Serikali kwa kushirikiana na IFAD itahakikisha inaleta matokeo chanya kwa kuzingatia mipango na mikakati inayotekelezwa na Program hii inawanufaisha walengwa,” Akisema Dkt. Yonazi 

Aidha, akieleza umuhimu wa Mradi Mkurugenzi Mkaazi wa IFAD Nchini Bw. Sakphouseth Meng amelezea kuwa upo umuhimu wa Ofisi ya Rais TAMISEMI kuwa sehemu ya utekelezaji wa programu ili kuwafikia walengwa na kueleza umuhimu wa sekta binafsi  kushirki katika Programu ili kuweza kuwafikia walengwa wengi zaidi na pia kuwa endelevu.


TANZANIA YASAINI MKATABA MPYA WA USAFIRI WA BAHARINI WA AFRIKA KATIKA MAKAO MAKUU YA UMOJA WA AFRIKA

 

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesaini rasmi Mkataba Mpya wa Usafiri wa Baharini wa Afrika wa mwaka 2010, hatua muhimu inayoashiria kuimarika kwa dhamira yake ya kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya sekta ya bahari kikanda na kimataifa. 


Hafla ya utiaji saini imefanyika, leo tarehe 11 Aprili 2025 katika Makao Makuu ya Umoja wa Afrika jijini Addis Ababa, Ethiopia, ambapo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Mashirika ya Meli Tanzania (TASAC), Bw. Mohamed Malick Salum, alisaini kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkataba huu ulipitishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1994 na Jumuiya ya Umoja wa Afrika (OAU), na ukafanyiwa marekebisho mwaka 2010 na Umoja wa Afrika ili kuakisi changamoto na matarajio mapya katika sekta ya usafiri wa baharini. Lengo kuu la Mkataba huu ni kukuza mfumo wa usafiri wa baharini barani Afrika ambao ni shirikishi, salama, unaotegemewa, unaozingatia mazingira na unaochochea maendeleo ya kiuchumi.

Kwa kusaini Mkataba huu, Tanzania inathibitisha upya kujitolea kwake kwa ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya bahari, sambamba na malengo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Baharini (IMO) ya kuimarisha usimamizi wa bahari duniani, usalama wa vyombo vya majini na ulinzi wa mazingira ya baharini.

Katika hotuba yake baada ya utiaji saini, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Bw. Mohamed Malick Salum, alisema:

“Hili ni tukio la kujivunia kwa Tanzania. Kwa kusaini Mkataba Mpya wa Usafiri wa Baharini wa Afrika, hatuchangii tu ajenda ya bara la Afrika bali pia tunafungua milango ya ushiriki mpana katika majukwaa ya kimkakati yanayokuza maslahi yetu ya kitaifa na kikanda. Ni tamko kuwa Tanzania iko tayari kushirikiana, kubuni na kuongoza katika sekta ya bahari barani Afrika.”

Moja ya manufaa makubwa ya kusaini Mkataba huu ni kwamba TASAC sasa inapata fursa ya kuwa mwanachama rasmi wa Chama cha Mamlaka za Usafiri wa Baharini Afrika (AAMA), taasisi iliyoanzishwa chini ya Mkataba huu kwa ajili ya kuratibu, kuoanisha na kukuza sera na utekelezaji wa usafiri wa baharini barani Afrika.



Thursday, April 10, 2025

YANGA SC YAICHAPA AZAM FC 2-1 CHAMAZI.

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji, Azam FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara leo Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Chachu ya ushindi wa Yanga ni leo mshambuliaji wa zamani wa Azam FC, Mzimbabwe Prince Dube Mpumelelo aliyetoa pasi ya bao la kwanza lililofungwa na kiungo Muivory Coast, Peodoh Pacome Zouzoua dakika ya 11, kabla ya yeye mwenyewe kufunga la pili dakika ya 34 akimalizia pasi ya kiungo Mudathir Yahya Abbas.

Bao pekee la Azam FC limefungwa na beki Lusajo Elukaga Mwaikenda dakika ya 81 akimalizia mpira wa adhabu uliopigwa na kiungo Feisal Salum Abdallah kutoka upande wa kulia wa Uwanja karibu kabisa na eneo la kupigia kona.

Kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi 67 katika mchezo wa 25 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi 10 zaidi ya Simba SC ambao hata hivyo wana mechi tatu mkononi.

Kwa upande wao Azam FC baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi zao 51 katika nafasi ya tatu wakiizidi pointi moja Singida Black Stars baada ya timu zote kucheza mechi 26.

COASTAL UNION YAICHARAZA SINGIDA BLACK STARS 2-1 MKWAKWANI


WENYEJI, Coastal Union wameibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga.

Mabao ya Coastal Union yamefungwa na viungo Josaphat Arthur Bada raia wa Ivory Coast aliyejifunga dakika ya 47 na Bakari Suleiman Msimu dakika ya 82, wakati bao pekee la Singida Bock Stars limefungwa na mshambuliaji Mghana, Jonathan Sowah kwa penalti dakika ya 76.

Kwa ushindi huo, Coastal Union inafikisha pointi 28 na kupanda kwa nafasi ya tatu hadi ya 10, wakati Singida Black Stars inabaki na pointi zake 50 nafasi ya nne baada ya timu zote kucheza mechi 26.

Wednesday, April 9, 2025

SIMBA WATINGA NUSU FAINALI SHIRIKISHO KWA MATUTA


Simba SC imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya ushindi wa penalti 4-1 dhidi ya Al Masry ya Misri jioni ya leo Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.

Hiyo ilifuatia Simba kushinda 2-0 ndani ya dakika 90, mabao ya winga Mkongo, Elie Mpanzu Kibisawala dakika ya 22 na mshambuliaji Mganda, Steven Dese Mukwala dakika ya 32.

Ushindi huo ulifanya matokeo ya jumla kuwa sare ya 2-2 kufuatia Al Masry kushinda 2-0 pia kwenye mchezo wa kwanza Aprili 2 mabao ya washambuliaji Mualgeria, Abderrahim Deghmoum dakika ya 16 na Mnigeria, John Okoye Ebuka dakika ya 89 Uwanja wa New Suez mjini Ismailia.

Kipa Mguinea wa Simba, Moussa Camara ameibuka shujaa kwa kuokoa mikwaju miwili ya penalti za viungo, Mohamed Gaber Tawfik Hussein ‘Mido Gaber’ na Mahmoud Hamada Awad, huku ya Fakhreddine Ben Youssef pekee ikimpita.
Waliofunga penalti za Simba ni Ahoua, Mukwala, kiungo mshambuliaji Kibu Denis Prosper na beki Shomari Salum Kapombe.

Simba sasa itakutana na mshindi wa jumla kati ya wenyeji, Zamalek na Stellenbosch ya Afrika Kusini zinazorudiana usiku huu Uwanja wa Cairo International Jijini Cairo baada ya timu hizo kutoka suluhu kwenye mchezo wa kwanza Aprili 2 pia Uwanja wa DHL Cape Town Jijini Cape Town. 

NI AL AHLY NA MAMELODI SUNDOWNS NUSU FAINALI LIGI YA MABINGWA AFRIKA

 


MABINGWA watetezi, Al Ahly ya Misri usiku wa kuamkia leo wamefanikiwa kutinga Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Al Hilal ya Sudan Uwanja wa Cheikha Ould Boïdiya Jijini Nouakchott nchini Mauritania.

Shujaa wa Al Ahly, mabingwa wa kihistoria wa michuano hiyo ni kiungo Emam Ashour Metwally Abdelghany dakika ya 80 akimalizia kazi nzuri ya Farao mwenzake, mshambuliaji Taher Mohamed Ahmed Taher Mohamed Mahmoud.
Al Ahly wanakwenda Nusu Fainali kwa ushindi wa jumla wa 2-0 kufuatia kushinda 1-0 pia kwenye mchezo wa kwanza Aprili 1 bao la beki Mmisri, Mohamed Hany Gamal Eldemerdash Uwanja wa Cairo International Jijini Cairo, Misri.

Ahly sasa itakutana na Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini ambayo imeitoa Espérance ya Tunisia kwa kuichapa 1-0 nyumbani, Uwanja wa  Venue Loftus Versfeld Jijini Pretoria, Tshwane kabla ya sare ya bila mabao jana Uwanja wa Olympique Hammadi-Agrebi mjini Radès, Tunisia.

Mechi nyingine ya marudiano ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika — Pyramids imekwenda Nusu Fainali licha ya kuchapwa 2-0 na wenyeji, FAR Rabat mabao ya washambuliaji, Mmoroco Youssef El Fahli dakika ya nane na Mkongo, 
Joël Beya dakika ya 82 Uwanja wa D'Honneur mjini Miknas.

Hata hivyo, Pyramids inakwenda Nusu Fainali kwa ushindi wa jumla wa 4-3 kufuatia ushindi wa 4-1 kwenye mchezo wa kwanza Aprili 1 Uwanja wa Jeshi la Anga la Misri Juni 30 Jijini Cairo.

Siku hiyo, mabao ya Pyramids yalifungwa na mshambuliaji Mkongo wa zamani wa Yanga ya Tanzania, Fiston Kalala Mayele mawili, dakika ya pili na 12 na mengine mawili, kiungo Mmisri, Ibrahim Adel 38 na 67, wakati bao la FAR Rabat lilifungwa na kiungo Mmorocco, Abdelfattah Hadraf dakika ya 45.

Pyramids sasa itakutana na mshindi wa jumla kati ya wenyeji, Orlando Pirates na MC Alger ya Algeria zinazorudiana leo Uwanja wa Orlando Jijini Johannesburg, Afrika Kusini.

Ikumbukwe mechi ya kwanza Orlando Pirates iliichapa 1-0  MC Alger bao pekee la kiungo chipukizi wa Kimataifa wa Afrika Kusini, Mohau Nkota dakika ya 65 Uwanja wa Julai 5, 1962 Jijini Algiers.

WAZIRI NDUMBARO ATAKA MIKAKATI YA PAMOJA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA

 


Na Oscar Assenga,Tanga

WAZIRI wa Katiba na Sheria Dkt Damas Ndumbaro amezitaka familia, viongozi wa dini na uongozi wa mkoa wa Tanga kuweka mikakati ya pamoja ya kupambana na ukatili wa kijinsia ili kukomesha tabia hiyo ambayo kwa mkoa huo ni tatizo kubwa tofauti na mikoa mingine nchini.

Akizungumza leo katika mkutano wa uzinduzi wa kampeni ya Msaada wa kisheria ya mama Samia (MSLAC), Waziri Dkt Ndumbaro alisema ukatili wa kijinsia ni tatizo kubwa linaloathiri jamii kwa njia nyingi, na ni muhimu kuwa na mikakati thabiti ya kutokomeza tabia hiyo ili kukomesha vikundi vinavyosababisha ukatili hususani kwa wanawake na watoto na hatimaye kuhakikisha kwamba wahanga wanapata msaada wa haraka.

Alisema Rais Dkt Samia Suluhu Hassan amemtuma alete salamu katika uzinduzi huo ili kuhakikisha kuwa masuala hayo yanashughulikiwa katika Kampeni hiyo kwa kutoa msaada wa kisheria bure kwa timu hiyo.


Alisema kampeni hiyo ipo katika ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi CCM ibara ya 120-123 ambayo inaelezea suala la utawala bora hivyo wahanga wanapopata haki jamii itakoma kufanya mambo hayo.

"Ilani Ile haikuandikwa bure, ukatili wa kijinsia unaofanywa kwa watoto na wanawake tunatakiwa kila mmoja katika familia tuweke mkakati wa kupambana nalo," alisema Waziri Ndumbaro na kuongeza,


"Tanga ni mkoa wenye imani ya dini, tutumie taasisi zetu za dini kukemea masuala ya ukatili,".


Amewataka watendaji wanaohusika na masuala ya haki, wasiogope kuamua kesi za ukatili kwa kutumia taratibu, kanuni, Sheria na taratibu.


Waziri Dkt Ndumbaro alisikiliza malalamiko mbalimbali ya wananchi na kupanga kukutana nao kusikiliza pande zote ili kufikia muafaka na haki kwa pande zinazokinzana.


Awali Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wanawake na makundi maalum, Wakili Msomi Amon Mpanju, alisema mkoa wa Tanga unaongoza kwa matukio ya ukatili ambapo jumla ya visa 7,320 yaliyoripotiwa mwaka jana mkoa huo ulikuwa na visa 457.


Mpanju alisema ili kupambana na matukio hayo viongozi wa dini wana nafasi kubwa ya kuepusha migogoro ya kifamilia katika jamii ikiwemo ukatili wa kijinsia.


Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Ustadh Rajab Abdarahman ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alimshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutumia maono yake ya kuanzisha kampeni hiyo ambayo itasaidia wananchi katika utatuzi na haki zao.


Aliwataka wananchi wa mkoa wa Tanga kutumia kampeni hizo kwa kuwa serikali imetumia fedha kuhakikisha migogoro ya kisheria inatatuliwa na wananchi kupata haki zao.


Mkuu wa mkoa wa Tanga, Balozi Dkt Batlida Burian, naye pia alimshukuru Rais Dkt Samia kwa mageuzi makubwa aliyofanya ya mabadiliko ya kiuchumi, kijamii na ya kisiasa na kampeni ya mama Samia itasaidia kupunguza migogoro iliyokuwepo.

Mwisho

Tuesday, April 8, 2025

SIMULIZI YA KUSISIMUA MZEE KARUME ALIVYOUAWA KWA RISASI.

 NA ALBERT G. SENGO

APRILI 7 mwaka 1972 visiwa viwili vya Unguja na Pemba pamoja na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, huzuni kubwa ilitanda kutokana na kuuawa kwa kupigwa risasi Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume.

Monday, April 7, 2025

PACOME AFUNGA BAO PEKEE YANGA YAILAZA COASTAL UNION 1-0 MWENGE

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union ya Tanga katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara leo Uwanja wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee leo, kiungo Muivory Coast, Peodoh Pacome Zouzoua kwa kichwa dakika ya 34 akimalizia krosi iliyochongwa na Max Nzengeli aliyepokea pande toka kwa beki Israel Patrick Mwenda kutoka upande wa kulia.

Kwa ushindi huo, Yanga inafikisha pointi 64 katika mchezo wa 24 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi saba zaidi ya watani wao, Simba SC ambao hata hivyo wana mechi mbili mkononi.

Kwa upande wao Coastal Union baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi zao 25 za mechi 25 sasa nafasi ya 13 kwenye Ligi ya timu 16, ambayo mwisho wa msimu mbili zitashuka daraja.

KAMPENI YA MSAADA WA KISHERIA YA RAIS DKT SAMIA SULUHU KUANZA RASMI MKOA WA TANGA APRILI 8 MWAKA HUU

 

Na Oscar Assenga, TANGA

KAMPENI ya Msaada wa kisheria ya Rais Dkt Samia Suluhu “Mama Samia Legal Aid Campaign” inatarajiwa kuanza kutoa huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi wanaokabiliwa na migogoro mbalimbali ikiwemo ya ardhi kuanzia Aprili 8 mwaka huu mkoani Tanga huku wananchi wakihimizwa kujitokeza kwa wingi.

Msaada huo wa kisheria utaongozwa na Jopo la wataalamu zaidi ya 40 kutoka kwenye Taasisi mbalimbali za Kisheria kupitia kliniki ya utatuzi wa msaada wa sheria ya Rais Dkt Samia Suluhu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian alisema uwepo wa kampeni hiyo katika Mkoa Tanga utasaidia kwa kiasi kikubwa kutatua migogoro iliyopo ambayo mingine imedumu kwa muda mrefu .


Mkuu huyo wa mkoa aliwataka wananachi kuchangamkia fursa hiyo na kwamba mkoa huo utatoa ratiba maalumu ya wapi wananchi watatakiwa kwenda kwajili ya kukutana na jopo hilo la wataalamu ili kupata ufumbuzi wa migogoro yao huduma ambayo itatolewa bila gharama yeyote

Aidha alisema kampeni hiyo itazinduliwa katika viwanja vya Tangamano na itajumuisha Halmashauri zote za Mkoa wa Tanga pamoja na kwensa kwenye ngazi za chini hadi ngazi ya kata,vijiji na mitaa.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga alisema lengo la kampeni hiyo ni kuongeza uelewa wa masuala mbalimbali ya kisheria ili jamii iweze kutambua hasa katika haki za wanawake, watoto, wazee, watu wenye ulemavu na makundi yote kwa ujumla wake.

Alisema jambo la pili kwenye kampeni hiyo ni kuimarisha huduma ya ushauri wa kisheria kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia, wengi wakiwa watoto, wakina mama na wakina baba.

Mkuu huyo wa mkoa alisema jambo la tatu ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu elimu ya sheria kwa uma, masuala ya haki na wajibu pamoja na misingi mizima ya utawala bora, hiku suala la nne likiwa kutoa elimu ya usimamizi wa mirathi na masuala mazima ya urithi wa ardhi ,haki ya kumiliki mali.

"Jambo la tano ni utatuzi wa migogoro kwa viongozi wa serikali za mitaa, watendai wa kata , vijiji, wajumbe wa mabaraza ya ardhi kwa kushirikiana na wazee maalumu , machifu, viongozi wa dini na serikali, nipongeze sana timu hii nimeambiwa kwambackambi hii arusha imeweza kutatua mgogoro uliodumu kwa takribani miaka 27,"Alisema Mkuu huyo wa Mkoa.



Akizungumza wakati wa mkutano huu na waandishi wa habari Mratibu wa Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia Mkoa Tanga ambaye ni Afisa Uchunguzi Mkuu kutoka Wizara ya Katiba ya Sheria Laurent Burilo alisema katika maeneo mengi waliyokwisha kuyafikia changamoto kubwa zilizojitokeza ni migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ni kilio kwenye maeneo mengi.

Aliongeza kwamba jambo jingine ni masula ya ndoa na matunzo ya watoto ikiwemo mirathi ambalo nalo limeweza kujitokeza kwenye maeneo mengi.

Akitolea mfano Burilo alisema Mikoa 23 ambayo wameifikia wamekumbana na migogoro mingi kwa mfano Mikoa 22 ambayo wameifikia wamefanikiwa kuwafikia wananchi zaidi ya milioni 2 huku wakikumbana na migogoro zaidi ya elfu ishirini kati ya migogoro hiyo migogoro zaidi ya 4000 imetatuliwa na kuisha kabisa ambapo wamekumbana na migogoro mingine ambayo imedumu kwa zaidi ya miaka kumi hadi 20