ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, March 28, 2015

TAIFA STARS TAYARI KUIKABILI MALAWI KESHO DIMBA LA CCM KIRUMBA MWANZA

Wakiongea na vyombo vya habari hii leo jijini Mwanza,  kutoka kushoto ni Daktari wa timu ya Taifa ya Tanzania Dr. Billy Haonga, Afisa Habari wa TFF Baraka Kizuguto, Kocha msaidizi wa Stars Salum Mayanga, mchezaji wa Stars Erasto Nyoni na nahodha wa timu hiyo Narub Canavaro.

NA ALBERT G. SENGO: MWANZA
KUELEKEA mchezo wa kesho timu ya Taifa ya Tanzania Taifa Stars, leo asubuhi imefanya mazoezi yake ya mwisho tayari kuikabili timu ya Taifa ya Malawi (The Flames) mchezo utakao chezwa kesho saa 10:30 jioni katika dimba la CCM Kirumba jijini Mwanza.

Tiketi za mchezo tayari zimekwishaanza kuuzwa katika kituo cha Uwanja wa Nyamagana kwa bei ya Tsh. 5,000/= kwa mzunguko, Tsh. 12,000/= kwa jukwaa kuu na Tsh. 20,000/= viti maalum jukwaa maalum.

Tayari mashabiki toka sehemu mbalimbali nchini wameanza kumiminika kwa wingi mjini hapa hasa ikizingatiwa kuwa safari hii wachezaji wa kimataifa Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wamejumuishwa kwenye kikosi hicho hivyo kuwa kivutio kwa mashabiki Kanda ya ziwa wenye uadimu wa michezo ya Kimataifa.

Kutoka kushoto ni Afisa Habari wa TFF Baraka Kizuguto, Kocha msaidizi wa Stars Salum Mayanga, mchezaji wa Stars Erasto Nyoni na nahodha wa timu hiyo Narub Canavaro.
Taifa Stars inashika nafasi ya 100 katika msimamo wa viwango vya FIFA uliotolewa mwezi March, huku Malawi ikiwa katika nafasi ya 91.

Akiongea na waandishi wa Habari katika Hoteli Lakairo jijini Mwanza, Kocha Msaidizi wa Taifa Stars Salum Mayanga amesema kikosi chake kiko katika hali nzuri na sasa kilichobaki nimchezo wenyewe wa kesho.

Mayanga amesema vijana wake wote 22 walioko kambini wako fiti na wamethibitishwa kiafya na daktari wa timu, wamefanya mazoezi ya siku tano katika dimba la CCM Kirumba wakiwa na ari na morali ya hali ya juu tayari kuusaka ushindi hiyo kesho.

Aidha Mayanga amewaomba wapenzi wa soka wa mkoa wa Mwanza na Kanda ya ziwa kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu yao muda wote wa mchezo.

Waandishi wa habari toka  vyombo mbalimbali.
Lakairo Hotel iliyopo Kirumba jijini Mwanza ambako Taifa Stars imeweka kambi.
Tayari waamuzi na makamisaa wa mchezo wamekwisha wasili jijini Mwanza, mwamuzi wa kati atakuwa Munyazinza Gervas kutoka nchini Rwanda, mshika kibendera namba moja ni Hakizimana Ambrose (Rwanda), mshika kibendera namba mbili Niyitegeka Bosco (Rwanda), mwamuzi wa akiba ni Martin Saanya kutoka Morogoro Tanzania huku kamishina wa mchezo ni Alfred Rwiza kutoka Mwanza. 

WALIMU WANAKWENDA KUJISAIDIA VICHAKANI KUTOKANA NA KUTOKUWA NA VYOO VYAO KUTITIA VYOTE

VICTOR MASANGU, KISARAWE PWANI
WALIMU wa shule ya msingi Mafizi iliyopo Wilayani Kisarawe, Mkoa wa Pwani wapo hatarini kupoteza maisha kutoka na vyoo walivyokuwa wanavitumia kutitia vyote kutokana na mvua ambazo zinaendelea kunyesha katika maeneo mbali mbali hapa nchini.
Kutokana na kuwepo kwa hali hiyo walimu hao kwa sasa wapo katika wakati mgumu kutokana na walimu  wengine kwenda kujisaidia katika vichakani na wengine kwenda kujisaidia katika zahanati ya mafizi.
Akizungumza na GSENGO BLOG shuleni hapo kuhusina na changamoto hiyo Mwalimu mkuu hiyo Manyama Philipo amesema kwamba miundombinu ya vyoo hivyo vipo katika hali mbaya sana ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa kwa  walimu hao.

Kwa upande wake mmoja wa walimu wanaofundisha katika shule hiyo Evelin Munisi  amesema kwamba kutokana na kuwepo kwa changamoto hiyo hususan kwa walimu wa kike wanalazimika kwenda porini uku wakiwa na majembe kwa ajili ya kujisaidia kitendo ambacho ni hatari kwa usalama wao kutokana na kuwepo kwa wanyama wakali katika maeneo hayo.
Aidha katika hatua nyingine Mwalimu huyo akusita kugusia  kero ambazo wanakumbana nazo wanafunzi wa shule hiyo, sambamba na kuiomba serikali kuliangalia suala la walimu  kwa jicho la tatu ili wawe na molali wa kufundisha katika shule za vijijini ambazo zimekuwa mara nyingi zikikimbiwa.
SHULE ya msingi Mafizi licha ya kukabiliwa na changamoto hiyo ya vyoo vyote kutitia pia wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji safi na salama, pamoja na upungufu wa vyoo vya wanafunzi hivyo kuwalazimu wanafunzi hao  kwenda kujisaidia kwa  kupanga foleni na ambao wapo karibu na shule  kwenda kujisaidia nyumbani  kwao.

WANANCHI ARUMERU WAVAMIA SHAMBA LA MWEKEZAJI LA KARAMU ESTATE.

Baaadhi ya mabango yaliyokutwa katika Karamu lililopo kijiji cha Nndatu wilayani Arumeru baada ya wananchi kuvamia shamaba hilo usiku wa manane na kuamua kuotesha migomba.
Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki ,Joshua Nassar akiwa ameongozana na baadhi ya wananchi wa jimbo hilo kutembelea eneo hilola Shamba akiungana mkono na hatua hiyo ya wananchi.
ARUMERU.

Baadhi ya wananchi katika kijiji cha Nkoaranga na Poli wameingia katika Shamba la Karamu (Karamu Estate) usiku wa manane na kuamua kuotesha migomba kwa kile wanachodai kuchoshwa na serikali kushindwa kusikia kilio chao cha kurudisha ardhi ya mashamba makubwa yaliyomilikiwa na walowezi wakati wa ukoloni.

Shamba hilo linalodaiwa kuwa na zaidi ya Hekari 3500 lilivamiwa na wananchi hao na kuanza zoezi la kuotesha migomba kabla ya kuning'iza  mabango yenye ujumbe mbalimbali katika maeneo tofauti ya shmaba hilo.

Wakizungumza kwa sharti la kutotaja majina yao,wananchi hao walisema mashamba hayo enzi za ukoloni yalipelekea Wananchi wa Meru kuchangia fedha kwenye Vyungu na kwamba mwaka 1952 alitumwa marehemu Shujaa Japhet Kirilo kwenda umoja a mataifa (UNO)kudai ardhi hiyo.

"Mwaka 1952 tulimtuma Shujaa wetu Kirilo kwenda umoja wa mataifa (UNO) huko New York nchini Marekani  kwenda kudai ardhi hii ya wana Meru lakini hadi leo hii mwaka 2015 maeneo mengi hayajarudi mikononi mwa wazawa."alisema mmoja wa wananchi hao.

Akizungumzia hatua hiyo Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki Joshua Nassari alisema amejaribu kupiga kelele Bungeni huku akisaidiwa na waziri kivuli wa Ardhi ,Nyumba na Maendeleo ya Makazi ,Halima Mdee lakini bado kelele zao hazijasikika.

"Binafsi nikisaidiwa na Halima Mdee,Waziri Kivuli wa Ardhi,tumepiga kelel vya kutosha Bungeni ,serukali sikivu bado haijasikia kelele zetu,Pengine sasa Waziri Lukuvi na serikali hii ya CCM itasikia kilio cha wananci hawa walioamua kuingia shambani na kuotesha Migomba"alisema Nassari.

Alisema Shamba la Karamu lilikuwa likitumika kwa kilimo cha Kahawa na kwamba kwa sasa limegeuka pori huku mwekezaji akidaiwa kuuza kuni kwa wenyeji na kukodishiwa kulima bustani ndogo ndogo za mboga.

Nassari alidai kuwa hivi karibuni mwekezaji alidaiwa kumega eneo la shamba hilo na kisha kuliuza kwa chuo kikuu cha Tumaini ,tawi la Makumira na kwa baadhi ya wageni kutokana na kile kinachodaiwa kumalizika kwa muda wa umiliki wa miaka 99.

Friday, March 27, 2015

UVCCM YAMCHARUKIA WAZIRI NYALANDU

Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana CCM Bw. Sixtus Mapunda akiongea na waandishi wa Habari(Hawapo pichani) wakati wa kutoa tamko juu ya msimamo wa Umoja huo wa kumtaka Waziri wa Mali asili na Utalii Bw. Lazaro Nyalandu kutekeleza sera za chama cha mapinduzi kwa kuhakikisha anatatua migogoro ya hifadhi na wananchi inayowatesa watanzania kwa muda mrefu na kupinga hatua ya Waziri huyo kutumia mitandao ya kijamii kutoa kauli za kejeli ambazo amekua akiungwa mkono na marafiki zake. Chama hicho pia kimemwagia pongezi tele Katibu Mkuu wa CCM Bw. Abdulrahman Kinana kwa kazi nzuri anayoifanya ya kujitolea ya kukiimarisha chama.( Kushoto) ni Katibu Mkuu Tawala Uchumi na fedha Bw. Omary Suleiman
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana CCM Bw. Sixtus Mapunda(Katikati) ,Katibu Mkuu Tawala Uchumi na fedha UVCCM Bw. Omary Suleiman(Kushoto) na Mjumbe wa NEC Bw. David Ismail wakisikiliza maswali kutoka kwa waandishi wa habari baada ya kumaliza kutoa tamko la kumtaka Waziri wa Mali asili na Utalii Bw. Lazaro Nyalandu kutekeleza sera za chama cha mapinduzi kwa kuhakikisha anatatua migogoro ya hifadhi na wananchi inayowatesa watanzania kwa muda mrefu. UVCCM pia ilitumia fursa hiyo kumpa pongezi tele Katibu Mkuu wa CCM Bw. Abdulrahman Kinana kwa kazi nzuri anayoifanya ya kujitolea na kukiimarisha chama.
UVCCM YAMCHARUKIA WAZIRI NYALANDU
Dar es salaam Machi 25 2015, Umoja wa vijana wa CCM (UVCCM), umemjia juu waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Lazaro Nyalandu kwa madai ya kwamba amekua akitoa kauli za kejeli kupitia mitandao ya kijamii na kuungwa mkono na baadhi ya marafiki zake.

Kauli hiyo ya UVCCM imekuja siku chache baada ya Katibu Mkuu wa chama cha mapinduzi (CCM), Abdulraham Kinana kumtaka Waziri Nyalandu aende kutatua migigoro ya wananchi wanaoishi jirani na hifadhi.

Alisema badala ya Waziri huyo kufanyia kazi ushauri wa Kinana, yeye ameibuka kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter na kuanza kutoa kauli za kejeli.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa UVCCM Taifa, Bw. Sixtus Raphael Mapunda alisema badala ya Waziri Nyalandu kwenda na kasi ya Kinana na sekretarieti ya CCM yeye amekua bize kujibizana kwenye mitandao.

“UVCCM inamtaka aende akatatute migogoro ya hifadhi na wananchi inayowatesa Watanzania kwa muda mrefu sasa, kila eneo la hifadhi kuna migogoro na wananchi”.

Umefika wakati sasa maliasili za Tanzania ziwanufaishe na kuwatumikia Watanzania badala ya hali ya sasa ambapo wananchi wanakuwa wanaumia kwa mali zao za asili nchini kwao wenyewe.

Haiwezekani tukalinda tembo na twiga wetu vizuri na tukashindwa kuwatetea Watanzania wanaonyanyasika katika maeneo ya hifadhi na tukatoka mbele za watu na kupaza sauti eti mmefanya kazi nzuri ya ulinzi wa tembo na mkaona hiyo ndio sifa” alisema Mapunda.

Pia aliongeza kuwa utendaji mzuri wa kazi ni kuwalina Tembo na Twiga na kutatua migogoro ya wananchi kwani vyote lazima viende pamoja na kumtaka Waziri Nyalandu kuiga mfano aliouonesha  Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe.William Lukuvi ambaye alikwenda haraka kusikiliza na kutafutia ufumbuzi kero za ardhi katika mikoa ya Dodoma, Manyara na Arusha baada ya ziara ya Katibu Mkuu wa CCM Kinana kubaini uwepo wa tatizo kubwa la migogoro hiyo, ni jambo la kupongezwa na kuigwa na viongozi wengine wa serikali. "Kutafuta mchawi badala ya kutekeleza wajibu husika kwa kiongozi wa serikali ni kujiondoshea sifa za kuendelea kuwa mtumishi kwa wadhifa unaoutumikia," alisema.

UVCCM inampongeza Katibu Kinana kwa ziara yake inayoendelea kufanywa  kwenye mikoa mbalimbali nchini kwa lengo la kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyoahidiwa katika ilani ya uchaguzi ya mwaka 2010-2015 na kuimarisha CCM.

"Kazi hii kubwa inayofanywa na Kinana na wajumbe wake imekirejeshea heshima kubwa Chama cha Mapinduzi katika kipindi hiki cha siasa za ushindani wa vyama vingi.

"Ili kufikia malengo ya kuwatumikia Watanzania kwa tija isiyo kifani, UVCCM chini ya ndugu Kinana na sekretarieti yake ni kutatua shida na kero za wananchi," alisema.

Aliongeza kuwa, UVCCM inaunga mkono kauli ya Kinana anayoitoa katika ziara yake inayoendelea hivi sasa mkoani Kilimanjaro ya kuhamasisha viongozi kutoka maofisini na kwenda vijijini kusikiliza kero za wananchi na kuzifanyia ufumbuzi, kwani kiongozi ni mfano wa kuigwa lazima aoneshe njia ili wanaomfuata wasijikwae.

MTATURU AWASHUKIA VIONGOZI WA CCM NA WATENDAJI WA SERIKALI . MTATURU AWASHUKIA VIONGOZI WA CCM NA WATENDAJI WA SERIKALI.

Miraji Mtaturu.
NA PETER FABIAN, SENGEREMA.
VIONGOZI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, wametakiwa kuacha ubinafsi, rushwa na makundi, ndani ya Chama ili wananchi waendelee kukiamini na kukichagua tena kushika dola.

Pia wametakiwa kuacha kuwania nafasi za uwakilishi wa wananchi wakiwa tayari ni viongozi wa Chama na kama watafanya hivyo  ni vyema wakajiuzuru nyadhifa zao kwanza ili kupicha wengine kuchukua kutokana na wao kupenda kura mkate mwingine.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa CCM mkoani Mwanza, Miraji Mtaturu wakati akizungumza na Halmashauri Kuu ya CCM ya wilaya ya Sengerema, jana wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani humo ambayo pamoja na kujitambulisha, alikagua utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Mtaturu amewaonya pia watendaji wa serikali wasiokuwa waaminifu na waliogeukia siasa na kuacha wajibu wao wa kutumikia wananchi, ole wao, Chama hakitawavumilia waendelee kukichafua. “Chama hiki tunakiua wenyewe kwa sababu ya ubinafsi wetu viongozi, unafiki, migawanyiko ya makundi na kundekeza rushwa hasa wakati kama huu wa uchaguzi, sasa iandaeni mioyo yenu kwanza muifanyie matengenezo na kaucha mambo hayo, Chama kwanza mtu baadaye,” alisema Katibu huyo.

Mtaturu alisema, watendaji wa serikali wanaokihujumu Chama wakidhani kitashindwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, wanaota ndoto za mcha kweupe. CCM ni Chama cha mfano barani Afrika, watanzania wengi wenye mapenzi na uchungu na nchi hii, hawana mpango na vyama vinavyotaka kuvuruga amani.

Alisema CCM kitaendelea kutawala iwapo viongozi na watendaji watatumikia wananchi waliowapa dhamana na siyo kuangalia masilahi yao binafisi na kuendekeza rushwa na kujali matumbo yao.

“Nimeambiwa hapa kuna mtumishi wa maji anakata maji kwa maksudi na kupeleka mgao katika eneo jingine kabla ya muda uliowekwa, akipewa rushwa ndiyo anatoa maji na kuacha mgao uendelee, ole wake,” alionya na kumuagiza Mkuu wa wilaya hiyo Zainabu Telaki amshughulikie na ikibidi ang’olewe wilayani humo kwani ni adui wa CCM na wananchi wote.

Katibu huyo aliwataka viongozi hao na watendaji wa serikali wajitambue na kuthamini dhamana waliyopewa na umma, watumie nyadhifa zao kuondoa kero na migigoro ya wananchi huku wakikubali kukosolewa, kushauriwa na wasiwe miungu watu katika ofisi zao kwani CCM hutafuta kura na kutukanwa wao wakila raha tu.

Awali mkuu wa wilaya hiyo, Telaki akitoa taarifa ya mradi wa maji mjini hapa alisema  ameiagiza wagawa maji waweke maji katika vioski vipya 20 kwa kutumia gari la boza ili wananchi wapate huduma na kuonya kuwa atapambana na watumishi wabovu akiwemo anayedaiwa kutoa maji kwa rushwa.

PICHA ZA HAPA NA PALE TOKA MAJINI ZIWA VICTORIA MWANZA

Rock City... 
Melikebu.
Soko kuu la biashara la kimataifa Mwaloni Kirumba Mwanza.
Bandari ya Mwaloni kwa Kitano.
Kutoka majini hadi eneo la kitongoji cha Nela na Isamilo kwa mbaaaali.
Usafirishaji wa bia kuelekea visiwani.
Usafirishaji wa dagaaa kuelekea masoko mbalimbali.
Mvuvi wa kienyeji.
Samma Three
Bandari ya Nansio Ukerewe.

MUDY MATUMLA MCHINA KUPAMBANA LEO IJUMAA DIAMOND JUBILEE

Bondia Wang Xin Hua kutoka China 'kushoto'  wakitunishiana misuli na Mohamed Matumla baada ya kupima uzito Dar es salaam jana kwa ajili ya mpambano wao leo katika ukumbi wa Diamond jubilee.

Bondia Wang Xin Hua kutoka China 'kushoto'  wakitazamana kwa usongo  na Mohamed Matumla baada ya kupima uzito Dar es salaam jana kwa ajili ya mpambano wao leo katika ukumbi wa Diamond jubilee katikati ni Jay Msangi Promota wa mpambano huo.
Promota wa mchezo wa masumbwi nchini Jay Msangi 'Jiwe Gumu' katikati akiwainuwa mikono juu mabondia Mfaume Mfaume kushoto na Cosmas Cheka baada ya kupima uzito jana kwa ajili ya mpambano wao wa leo .

Promota wa mchezo wa masumbwi nchini Jay Msangi 'Jiwe Gumu' katikati akiwainuwa mikono juu mabondia Bondia Wang Xin Hua kutoka China 'kushoto'  na Mohamedi Matumla baada ya kupima uzito jana kwa ajili ya mpambano wao wa leo 
Mabondia Japhert Kaseba Kushoto akitunishiana misuli na Mada Maugo baada ya kupima uzito kwa ajili ya mpambano wao wa leo Ijumaa katika ukumbi wa Diamond Jubilee Picha na SUPER D BOXING NEWS

Thursday, March 26, 2015

WAKAZI ZAIDI 48,100 WAKOSA MAJI SAFI NA SALAMA KWA UZEMBE WA HALMASHAURI KUTONUNUA LUKU YA UMEME.


NA PETER FABIAN, NANSIO.
HALMASHAURI imeshindwa kunua luku ya umeme kwa ajiri ya kuendeshwea mtambo wa kusukuma maji safi na salama na kusababisha wananchina wakazi wa mji wa Nansio wilayani Ukerewe Mkoani Mwanza kupata adha ya kukosa maji kwa miezi sita sasa.

Hayo yalibainshwa katika taarifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyosomwa kwa Katibu wa CCM mkoa wa Mwanza, Miraji Mtaturu wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezwaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kupitia ilani ya uchaguzi 2010 hadi 2015 pamoja na uhai wa chama.

Mtaturu alisema kuwa kutokana na taarifa za kuwepo baadhi ya watendaji wa halmashauri wasio waaminifu a mbao wamekuwa wakitumia nafasi zao kukwamisha utekelezwaji huo ni vyema vikao vya chama vikakaa na kuwaita kisha kuwajadiri na kuwasilisha mapendekezo yao Mkoani.

Awali alipotembelea chanzo cha maji mjini Nansio akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Joseph Mkirikiti na viongozi wa chama hicho ili kujionea tatizo linalosababisha mitambo kushindwa kusukuma maji, ambapo alipewa taarifa fupi na meneja wa Mamlka ya Maji Safi na Salama Edward Joseph aliyeonyesha kushitukizwa na kutakiwa kutoa taarifa na viongozi hao.


 “ tatizo hili limesababishwa na kukosekana kwa umeme wa luku na mamlaka kushindwa kukusanya fedha kutoka kwa wateja jambo ambalo limesababisha kusuasua utolewaji wa huduma ya maji safi katika mji wa Nansio pia wananchi hawana mwamko wa kulipia bili kwa wakati.” Joseph.

Baada ya taarifa hiyo Katibu Mtaturu aliuagiza uongozi wa Mamlaka ya Maji Safi na Halmashauri hiyo kuhakikisha inalekebisha kasoro zilizopo haraka ili wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na kuweka mipango mizuri ya ukusanyaji fedha ili kuwezesha uendeshaji wa Mamlaka hiyo.

. Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya Mkirikiti, licha ya kuletewa mita za kufungia wateja ili walipe
maji wanayotumia, mamlaka hiyo imeshindwa kufunga mita hizo na kukusanya ankara za maji, hivyo kukosa pesa za kununua umeme na wananchi kubaki wakisotea maji kwa baadhi yao kununua maji shilingi 3,000 kutoka kwenye mkokoteni wenye madumu kumi.

Pia Mkirikiti aliwaagiza Mameneja wa Mamlaka ya Maji Nansio, Tanesco na Mkurugenzi wa halmashauri kukutana naye na kumueleza mikakati ya kutatua kero ya maji haraka iwezekanvyo ili wananchi wa mji huo waanze kupata huduma ya maji safi na salama ndani ya muda uliotolewa na Katibu wa CCM na sitowavumilia watendaji wa serikali watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao kwa nafasi zao hapa wiliayani.

Hivi sasa mji wa Nansio wenye wakazi 48,100 wanaopata huduma maji ya bomba ni wakazi 919 tu hali ambayo imelalamikiwa na wananchi wakazi wa Nansio katika mkutano wa hadhara na viongozi hao wa chama na serikali uliofanyika katika viwanja vya stendi ya zamani mjini humo.

TAMKO LA UONGOZI WA SERIKALI ZA WANAFUNZI WA VYUO VIKUU DODOMA KULAANI KUHUSISHWA KWA WANAFUNZI WA VYUO VIKUU VYA DODOMA NA KUMUOMBA MH. LOWASA KUGOMBEA URAIS.

Ndugu Waandishi wa habari, Tunapenda kutanguliza shukrani za dhati kwenu kwa kufika katika eneo hili kutusikiliza.Mbele yenu ni viongozi wa serikali za wanafunzi kutoka Vyuo vikuu mbalimbali vilivyopo mkoani Dodoma.Ndugu waandishi wa habari,si kawaida na wala mazoea kwa marais na viongozi wa serikali za wanafunzi kutoka vyuo tofauti kukutana kwa pamoja na kuzungumza na nyie wanahabari kama inavyotokea hii leo.
Ndugu wanahabari,siku ya Jumapili ya tarehe 22 mwezi huu wa 3,kundi la watu waliojitambulisha kama ni wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma walijikusanya nyumbani kwa mh; Lowasa na kutoa matamko mbalimbali ikiwa pamoja na kuutangazia uma wa watanzania kuwa sisi wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma tunamuunga mkono na tunahitaji Lowasa awe rais wetu sambamba kumchangia pesa.
Ndugu wanahabari,Tunapenda kukanusha kuwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma kwa ujumla wetu hatukuhusika na jambo lile na kama viongozi wa serikali za wanafunzi kutoka vyuo vikuu vya mkoa huu wa Dodoma,Tunapinga na kulaani kitendo cha watu wachache kwenda kutuingiza sisi wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma katika jambo ambalo halituhusu na wala si lililotuleta hapa Dodoma.

Sisi kama wasomi ambao jamii inatutegemea kama kioo hatuwezi kuandamana na kujikusanya kwenye nyumba ya kiongozi na kumuomba agambee urais, wakati tunajua fika sisi hatuhusiki na uteuzi wa wagombea ndani ya taasisi yao.Kilichofanyika ni kuudanganya uma wa watanzania na taasiasi yake kupitia kivuli cha vijana wachache kutoka vyuo vya hapa Dodoma,waliolipwa pesa ili waweze kuwa kava la tukio lile.
Ndugu wanahabari,Mkoa wa Dodoma unavyuo vikuu visivyopungua 8,Na jumla ya wanafunzi wote tunaosoma katika vyuo vya Dodoma ni zaidi ya wanafunzi 35,000.Chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) pekee yake kinawanafunzi wasiopungua 22,000.

Idadi ya watu waliojikusanya nyumbani kwa Mh: Lowasa siku ya tarehe 22-03-2015 haizidi watu 230 wakiwemo Wamachinga na Wenyeviti wa Jumuiya za wazazi, kama vyombo vya habari vilivyoripoti. 

Ukiwatoa Wamachinga na Wenyeviti wa Jumuiya za wazazi waliotoka mikoa mbalimbali,idadi ya wanafunzi waliokuwepo kwenye tukio lile hawazidi 150.Idadi hii ni sawa na asilimia 0.4 ya wanafunzi wote wanaosoma vyuo vikuu vya Dodoma.Ndugu wanahabari,kwa akili ya kawaida kabisa asilimia 0.4 ya wanafunzi wa vyuo vikuu ndio waliokuwa pale.

Tunashangazwa na dhambi tusiyoitenda tunayobebeshwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma ambao kwa sasa tupo bize na msimu mpya ya masomo wenye changamoto mbalimbali.
Ndugu wanahabari,sisi kama vijana wasomi na watu tunaotegemewa na jamii zetu tutakusanyika katika kujadili na kuchambua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii yetu na sio kukusanyika kwa ajili ya mwanasiasa ambaye sifa zake na uhadilifu wake unatiliwa shaka katika jamii.

Tunaomba mlijulishe Taifa, kuwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma hatujahusika na tukio lile isipokuwa wanafunzi wachache walitumika kwa kupewa pesa na wahusika wa tukio lile.Tunataka Taifa lijue hatupo tayari kutumia elimu zetu kulitia upofu taifa letu.Waambieni mama zetu na baba zetu huku vijijini kwetu kuwa tumekuja kutafuta elimu ili ituwezeshe kuwakomboa wao na sio kutumika na Wanasiasa kwa malengo yao.

Tunatambua haki ya mwanafunzi kuamua na kufanya shughuli za kisiasa nje ya maeneo ya vyuo, lakini hatukubaliani na wanafunzi wachache kuchafua na kuwapaka matope maelfu ya wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma ambao hawajahusika na tukio lile.Hii sio haki na haikubaliki.
Vilevile tungependa kutumia fursa hii kuwaasa wanafunzi wenzetu popote pale nchini, makundi mbalimbali ya kijamii (wakulima, wafugaji, wavuvi, wamachinga, wasanii, n.k), zikiwemo taasisi za dini kwamba watu wachache kuzungumza kwa niaba ya makundi juu ya mambo yanayogusa maamuzi ya mtu binafsi. 
Mwisho tunatoa wito kwa wanafunzi wenzetu wote kujitambua na kutumie muda wetu kwa mambo ya msingi na muhimu kwa ustawi wa Nchi yetu. Na kuonesha jinsi wanafunzi wa Vyuo Vikuu vya Dodoma walivyokasilishwa na jambo hili, Tamko hili limesainiwa na wanafunzi 7821 toka vyuo mbali mbali vya Dodoma.Majina ya sahihi za wanafunzi zimeambatanishwa. Tusikubali kutumika na wanasiasa wa aina hii..
Asanteni Mungu ibariki Tanzania,Mungu vibariki vyuo vikuu vya Dodoma.
Kwa niaba ya wawakilishi wa serikali za Wanafunzi Chuo cha Mipango,Chuo cha Madini, Chuo cha Hombolo,Chuo kikuu cha Dodoma(UDOM) na CBE.
DANIEL DANIEL -Rais wa Saint Jonh’s University 26/03/2015

JEMBE FM MWANZA YAPEWA LESENI.

DSC_0644
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Profesa John Nkoma akizungumza kwenye hafla fupi ya kukabidhi leseni kwa redio ya Jembe FM ya jijini Mwanza kwenye ofisi za makao makuu ya TCRA jijini Dar es Salaam.(Picha zote na Zainul Mzige wa modewjiblog).
Na Mwandishi wetu
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Profesa John Nkoma ametaka matumizi sahihi ya masafa ya radio yanayatumiwa kurusha vipindi vya radio kwa ajili ya maendeleo ya umma.
Kauli hiyo ameitoa jana wakati akikabidhi leseni kwa radio Jembe FM.
Alisema  matumizi yasiyo sahihi yatasababisha mamlaka hiyo kunyang’anya leseni  walioitoa kwa ajili ya maslahi ya taifa.
Alisema pamoja na haja ya kushiriki katika ushindani, kituo hicho kipya kinatakiwa kufuata masharti ya utangazaji ambayo yamo katika leseni waliyoiomba.
Alisema radio hiyo ya Mwanza inaongeza ushindani katika eneo hilo katika jumla ya radio FM 12 zinazosikika mjini humo, radio za kitaifa saba, za kikanda 11 na radio ya jamii 1.
Aliwataka kuwa waangalifu na kufuata kanuni za kitaalamua kufanyakazi wanasotahili za kuelimisha na kuburudisha.
DSC_0650
Alisema si radio tu ambayo ina nguvu ndiyo inayoweza kuhimili ushindani lakini pia ufuataji wa kanuni na maadili katika utekelezaji wa majukumu yao.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Jembe FM, Dk. Sebastian Ndege amesema kwamba wameanzisha radio hiyo kwa lengo la zaidi ya kuburudisha na kuelimisha bali kusaidia vijana kushika hatamu na kujitengenezea uwezo wa ajira.
Alisema kwamba ili kuhakikisha kwamba wanafanyakazi kitaaluma wameajiri watu ambao wamesomea kazi husika ili kuhakikisha kwamba hawaendi kinyume na leseni yao.
Alisema kwamba wanaamini kwamba wana nafasi kubwa ya kujaza mapengo ambayo yapo katika urushaji wa matangazo kwa sasa ili kuhudumia mji wa Mwanza ambao unakua kwa kasi kwa sasa.
DSC_0676
Mkurugenzi wa sheria wa Mamlaka ya Mawasiliano Nchini (TCRA), Fortunata Mdachi (kushoto) akisisitiza jambo kwa uongozi wa JEMBE FM wakati wa hafla ya kukabidhi leseni kwa uongozi huo iliyofanyika jana jijini Dar es Salaam makao makuu ya ofisi za TCRA.
Alisema vipindi vyao vimezingatia haja ya jamii katika uchumi, elimu na afya.
Aidha amesema kwamba wanategemea kuwa na vipindi vizuri zaidi hasa kutokana na na uzoefu waliokuwa nao hasa wa uandaaji wa njia ya panda.
Jembe FM inamilikiwa na Jembe Media Limited.
DSC_0669
Mkurugenzi Mkuu wa Jembe FM Dk Sebastian Ndege (wa kwanza kushoto) na uongozi wa juu kabisa wa Jembe Media Limited wakimsikiliza kwa makini kabisa Mkurugenzi Mkuu wa TCRA (hayupo pichani) wakati wa hafla fupi ya kukabidhiwa leseni rasmi ya kurusha matangazo ya redio ya JEMBE FM ya jijini Mwanza.
DSC_0655
Baadhi ya wawakilishi wa kampuni ya Ndege Insurance inayomilikiwa na Dk. Sebastian Ndege waliojumuika kwenye hafla hiyo fupi.
DSC_0683
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Profesa John Nkoma (kulia) akimkabidhi rasmi leseni ya kurusha matangazo ya redio ya JEMBE FM ya jijini Mwanza, Mkurugenzi Mkuu wa Jembe FM, Dk Sebastian Ndege (katikati) katika hafla fupi iliyofanyika makao makuu ya ofisi za TCRA jijini Dar. Kushoto ni Mkurugenzi wa sheria wa Mamlaka ya Mawasiliano Nchini (TCRA), Fortunata Mdachi.
DSC_0712
Mkurugenzi Mkuu wa Jembe FM, Dk Sebastian Ndege akitoa neno la shukrani ambapo pia maeahidi kuwa atafuata masharti na kanuni zote zilizowekwa na mamlaka hiyo.
DSC_0725
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Profesa John Nkoma (wa pili kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na uongozi wa juu kabisa wa Jembe Media Limited. Kutoka kushoto ni Mwanasheria wa Jembe Media Ltd. Justine Ndege, Mkurugenzi Mkuu wa Jembe FM, Dk Sebastian Ndege pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Jembe Media Ltd, Renata Ndege.
DSC_0733
Mkurugenzi Mkuu wa Jembe FM, Dk Sebastian Ndege na Mwanasheria wa Jembe Media Ltd. Justine Ndege wakionyesha leseni hiyo iliyoambatanishwa na miongozi ya Mamlaka ya Mawasiliano ya TCRA kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) waliohudhuria hafla hiyo.