ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, January 6, 2026

HUYU HAPA KOCHA MPYA WA CHELSEA - JEH ATADUMU?

 


Kocha wa timu ya Strasbourg, Liam Rosenior ndiye kocha mpya wa klabu ya Ligi Kuu Uningereza, Chelsea.

Mwingereza huyo mwenye umri wa miaka 41 anatarajiwa kuchukua nafasi ya Enzo Maresca, ambaye aliondoka siku ya Mwaka Mpya.

Mapema Jumanne, katika mkutano wake wa mwisho na waandishi wa habari kama meneja wa Strasbourg, Rosenior alithibitisha kwamba "amekubali kwa maneno" kuwa kocha wa Chelsea.

"Siwezi kukataa fursa hii ya kujiunga na klabu kubwa, kikosi kikubwa ambacho ni mabingwa wa Kombe la Dunia la Klabu," Rosenior alisema.

"Sijasaini bado. Lakini tumeshakubaliana kwa kila kitu na huenda nikasaini saa chache zijazo," Rosenior alisema.

"Kukabidhiwa jukumu hili kunamaanisha jambo kubwa kwangu na nataka kuwashukuru wote waliohusika kwa fursa hii. Nitafanya kila kitu ili kuleta mafanikio ambayo klabu hii inastahili."

Rosenior amesema kocha msaidizi wa kikosi cha kwanza cha Strasbourg Kalifa Cisse, kocha mwingine msaidizi Justin Walker na mkuu wa uchambuzi Ben Warner watajiunga naye Chelsea.

Ronseior aliteuliwa na Strasbourg Julai 2024 na kuiongoza klabu hiyo ya Ufaransa hadi nafasi ya saba katika Ligue 1 msimu uliopita.

KWANINI MADURI ALIFUNGWA MACHO NA KUZIBWA MASIKIO ALIPOKAMATWA

 .

Picha ya kwanza ya Nicolás Maduro baada ya kuzuiliwa katika operesheni ya kijeshi ya Marekani Jumamosi hii itasalia katika kumbukumbu ya wengi.

Rekodi hiyo ya picha ilitolewa saa chache baada ya wanajeshi wa Marekani kumkamata mtu ambaye alikuwa kiongozi wa serikali ya Venezuela tangu 2013, katika operesheni iliyoamriwa na Donald Trump mwenyewe.

Ni Trump mwenyewe aliyechapisha picha ya Maduro kwenye mtandao wa Truth Social network, wakati ambapo Makamu wa Rais wa Venezuela wakati huo, Delcy Rodríguez, alikuwa akiuliza uthibitisho wa maisha baada ya kukamatwa kwa rais na mkewe.

Kufikia sasa inajulikana kuwa Maduro na mkewe, Cilia Flores, walikamatwa asubuhi na mapema huko Fort Tiuna, kusini-magharibi mwa Caracas, na kisha wakahamishwa kwa helikopta hadi kwenye meli ya kivita ya Iwo Jima ili kupelekwa -kupitia Cuba- hadi New York

Huko, wote wawili wameshtakiwa kwa tuhuma za kula njama za kutumia dawa za kulevya, kula njama ya kuingiza cocaine nchini Marekani, na makosa mengine yanayohusiana na silaha.

Katika BBC Mundo tulishauriana na wataalamu wa ulinzi na operesheni za kijeshi kuhusu hitimisho linaloweza kutolewa kutokana na picha hiyo ya kwanza ambayo Maduro anaonekana akiwa amevalia mavazi ya michezo, huku mikono yake ikiwa imefungwa pingu na huku hisi zake, kama vile kuona na kusikia, zikiwa zimezibwa.

Mbinu za Kawaida

Kwa Mark Cancian, kanali mstaafu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani na mshauri mkuu wa Idara ya Ulinzi na Usalama katika Kituo cha Mafunzo ya Kimkakati na Kimataifa (CSIS), "serikali imechukulia kukamatwa huku kama suala la utekelezaji wa sheria, sio operesheni ya kijeshi, kwa hivyo wamemchukulia Maduro kama mfungwa."

Monday, January 5, 2026

REFA AINYIMA WAZIWAZI PENATI TAIFA STARS IKITOLEWA AFCON 1-0 NA MOROCCO

 


SAFARI ya Tanzania katika Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 imeishia Hatua ya 16 Bora baada ya kutolewa na wenyeji, Morocco JANA jioni.

Mchezo huo uliopigwa kwenye Uwanja wa Prince Moulay Abdellah, Jijini Rabat, Morocco, bao pekee lilifungwa na winga wa Real Madrid, Brahim Díaz, dakika ya 64.

Kocha wa Taifa Stars, Miguel Angel Gamondi, na kikosi chake wameonesha kutoridhishwa na maamuzi ya refa Boubou Traore kutoka Mali, wakidai walinyimwa penalti ya wazi baada ya Iddi Suleiman ‘Nado’ kuangushwa ndani ya eneo la hatari dakika za lala salama.

Morocco sasa inaingia robo fainali na kukutana na Cameroon, waliowaondoa Afrika Kusini kwa ushindi wa mabao 2-1 katika mchezo wa usiku kwenye uwanja huo huo.