ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, June 28, 2025

ARAFAT HAJI : TULIDHARAULIWA WAKATI TUNAINGIA KWENYE MPIRA | HATUJAWAHI KUYUMBISHWA KWA LOLOTE

 “hapa katikati kulikuwa na misemo maarufu hawana uzoefu hawaujui mpira, mpira unaware wake”

Makamu wa Rais wa klabu ya Yanga Arafat anafunguka zaidi kupitia Almas Digital

YANGA SC NA MTIHANI MWINGINE KESHO DHIDI YA SINGIDA BLACK STARS

 

UONGOZI wa Yanga SC umeweka wazi kuwa unalitaka kombe lao la CRDB Federation Cup kwa kuwa wao ni watetezi licha ya kukutana na timu ngumu fainali. 

Kesho Juni 29 2025 Yanga SC itacheza na Singida Black Stars mchezo wa fainali.

Yanga SC imetoka kutwaa taji la 31 la Ligi Kuu Bara kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Simba SC. Ni pointi 82 imefikisha ikifunga jumla ya mabao 83 ikiwa ni timu namba moja kwenye kufunga mabao mengi na kufungwa mabao machache ambayo ni 10.

Simba SC imepishana na mataji yote ambayo ilikuwa inapambania na iliondolewa hatua ya nusu fainali na Singida Black Stars kwenye CRDB Federation Cup.

Ali Kamwe, Ofisa Habari wa Yanga SC amesema wanatambua ushindani ni mkubwa na fainali ya Jumapili Zanzibar haitakuwa nyepesi.

“Singida Black Stars walitusumbua kweli kwenye mechi zetu mbili za ligi. Kuelekea kweye mchezo wetu wa fainali tupo tayari na tunalitaka kombe letu licha ya ugumu ambao upo mbele yetu. Tunaamini benchi la ufundi na wachezaji watakamilisha majukumu yao.”

AIGLES DU CONGO BINGWA MPYA DRC, VIGOGO WOTE, AS VITA NA MAZEMBE WATUPWA NJE CAF

 


TIMU ya FC Les Aigles du Congo (Eagles of Congo) ya Kinshasa imefanikiwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ijulikanayo kama Linafoot kwa mara ya kwanza katika historia yake baada ya kutoa sare ya kufungana bao 1-1 na TP Mazembe Ijumaa ya jana (Juni 27, 2025) Uwanja wa Kamalondo, Lubumbashi.


Beki Heltone Kayembe alianza kuifungia Aigle du Congo ‘Des Samourais’, (The Samurai) dakika ya 35 akimtungua kipa Baggio Siadi Ngusia, kabla ya Patrick Mwaungulu kuisawazishia TP Mazembe dakika ya 47 akimtungua kipa Nathan Dibu kufuatia kazi nzuri ya Patient Mwamba.

Kipa Nathan Dibu akipongezwa na wachezaji wenzake jana baada ya kazi nzuri kwenye mchezo wa jana dhidi ya TP Mazembe

Kwa matokeo hayo, Aigles du Congo inayofundishwa na Kocha wa zamani wa Tabora United, Anicet Kiazayidi inamaliza na pointi 35 kileleni mwa Linafoot ikifuatiwa na FC Saint Eloi Lupopo ya Lubumbashi pia yenye pointi 33 baada ya mechi 16 kwenye ligi ya timu 12 na zote zinafuzu Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao.


Timu ya AS Maniema yenye maskani yake Kindu, jimbo la Maniema iliyomaliza nafasi ya tatu kwa pointi zake 32 inakwenda Kombe la Shirikisho Afrika katika msimu ambao umekuja na mageuzi makubwa katika Linafoot, kwani hata kigogo mmoja wa kihistoria, iwe Mazembe, AS Vita Club ya Kinshasa wala DC Motembab Pembe aliyepenya nafasi tatu za juu.


TP Mazembe yenye maskani yake Lubumbashi chini ya Kocha Msenegal, Lamine N’Diaye, waliokuwa mabingwa watetezi, wamemaliza nafasi ya nne kwa pointi zao 30 nyuma ya Motema Pembe ya Kinshasa iliyovuna pointi 31.

Mmiliki wa FC Les Aigles du Congo, Vidiye Tshipanda Tshimanga akiwa ofisini katika utendaji wa shughuli za kisiasa kama Mshauri wa Rais Felix Tshisekedi Tshilombo

FC Les Aigles du Congo ni klabu iliyoanzishwa na Mfanyabiashara na Mwanasiasa, Vidiye Tshipanda Tshimanga mwaka 2023 yenye maskani yake Jjini Kinshasa, ambaye aliinunua klabu ya Jeunesse Sportive de Kinshasa maarufu kama JSK na kuibadili jina.


Jukumu kubwa la Kisiasa la Vidiye Tshipanda Tshimanga (48) katika chama chake tawala cha United Congo Dynamics (DCU) kwa sasa ni Mshauri wa Rais wa DRC, Felix Tshisekedi Tshilombo juu ya masuala maalum ya kimkakati na msimu huu amefanikiwa kuizima TP Mazembe, timu inayomilikiwa na Mwanasiasa na Mfanyabiashara mwingine maarufu DRC, Moise Katumbi Chapwe (60) ambaye ni kiongozi wa Chama cha Together for the Republic.

Nje ya ofisi, huu ndio mwonekano wa ‘Tajiri’ Vidiye Tshipanda Tshimanga anayemiliki klabu ya Aigle du Congo

MAGRET SITA KUKABILIANA NA SHUGHULI PEVU YA MWAMBA HUYU HAPA JIMBO LA URAMBO TABORA

 

Afisa Mwandamizi katika sekta ya benki, Dkt. Danford Muyango ametangaza kugombea nafasi ya ubunge katika Jimbo la Urambo mkoani Tabora kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM).

Akizungumza na BMG Media, Dkt. Muyango amesema Urambo inamhitaji ili akashughulikie changamoto za wana Urambo ikiwemo uhaba wa masoko ya mazao ya biashara ikiwemo Tumbaku, kukuza sekta ya viwanda, upatikanaji wa maji safi na salama pamoja na miundombinu bora ya barabara.
Dkt. Danford Muyango anatarajiwa kuchuana na wagombea mbalimbali akiwemo mbunge anayemaliza muda wake, Mama Margaret Sitta.

Dkt. Muyango amesema "Urambo inahitaji mtu anayeijua na mwenye uwezo wa kutatua changamoto nne ambazo ni masoko ya zao la Tumbaku na mazao mengine ya niashara, kukuza viwanda wa mazao ya chakula na uongezaji thamani. Majisafi na salama kwa ngazi ya Mitaa na miundombinu inayofikika. Nimeyaishi maisha haya na nipo tayari kutatua changamoto hizi chini ya Chama cha Mapinduzi (CCM)".

Ifahamike kuwa Dkt. Muyango ni mbobevu wa mambo ya fedha na maendeleo kwa mgazi ya udaktari (PhD) kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM). 

Alizaliwa katika Kijiji cha Usoke Mission, Wilaya ya Urambo mkoani Tabora ambapo pia alipata elimu ya msingi na Sekondari miaka ya 1990.

Muyango ni Afisa Awandamizi katika masuala ya benki ambapo amehudumu kwa zaidi ya miaka 18 katika mabenki mbalimbali.
Kazi na Utu: Tuikomboe Urambo

Friday, June 27, 2025

'ATUPWA' JELA KWA KUMBAKA MTOTO WA MIAKA SITA.

 


NA DAWATI LA HABARI POLISI MOROGORO

Mrisho Mussa Nchemba (31) Mkulima mkazi wa Milama, Kata ya Dakawa wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro , amehukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kosa la kumbaka mtoto wa kike wa miaka 6.

Akisomewa hukumu hiyo Juni, 25, 2025 mbele ya Mheshimiwa Hakimu George Ngowi wa Mahakama ya Wilaya ya Mvomero ambaye alieleza, Mnamo Novemba 28, 2024 majira ya saa 2 asubuhi Mshitakiwa Nchemba alimvizia muhanga akiwa amelala kisha kuingia ndani ya nyumba, kumbaka na kumsababishia maumivu makali.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro amesema, vitendo hivi vya Ukatili vinasababishwa na mmomonyoko wa maadili kwenye jamii husika, hivyo mbali na kuchukua hatua za kisheria, Jeshi la Polisi mkoa wa Morogoro limeendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusiana na madhara ya vitendo vya ukatili.


CCM YAFUNGUKA SABABU ZA KUZUIA SHAMRASHAMRA UCHUKUAJI, UREJESHAJI FOMU

Katibu wa NEC Organaizesheni, Issa Haji Ussi
Katibu wa NEC Organaizesheni, Issa Haji Ussi.

 

Chama Cha Mapinduzi kimeeleza sababu za kuzuia shamrashamra za matarumbeta, ngoma,wapambe na pilipiki katika kuchukua na kurudisha fomu za ubunge na udiwani.

Taarifa kwa umma iliyotolewa na Katibu wa NEC Organaizesheni, Issa Haji Ussi kuhusu mwongozo wa na maelekezo kuhusu utaratibu wa uchukuaji na urejeshaji wa fomu kwa wanachama.

Amesema lengo la zuio ni kutoka na muhimu wa mchakato kwa chama katika kuwaunganisha wanachama wake ili kulinda misingi ya umoja, upendo, ushirikiano, mshikamano.

"Ili kusimamia misingi hiyo, inaelekezwa kwamba:- Ni, marufuku kwa mwanachama yeyote kualika kundi la wapambe kumsindikiza kwenda CCM kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea."amesema.

"Ni marufuku kwa mwanachama kuandaa msafara wa magari, pikipiki, baiskeli, ngoma na matarumbeta ya kumsindikiza kwenda CCM kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea, vitendo hivyo vinaleta viashiria vya makundi na mpasuko ndani ya Chama, havipaswi kufanywa na mwanachama yeyote."

Ussi amesema CCM inaelekeza usimamizi wa karibu mchakato huu, kuhakikisha kila mwanachama anaheshimu na anafuata maelekezo haya. 

"Mwanachama yeyote atakayepuuza na kukiuka maelekezo haya, hatua za kinidhamu zichukuliwe ipasavyo, kwa mujibu wa Kanuni za Uongozi na Maadili dhidi yake, bila upendeleo wala uonevu, ikiwemo ni pamoja na kumuondolea sifa za kuteuliwa kuwa mgombea.

"Maelekezo haya mnatakiwa kuyafikisha haraka sana kwa makatibu wote wa wilaya, na kata ili waweze kuwajulisha wanachama wanaokusudia kuchukua fomu za kugombea, nao waweze kufahamu juu ya katazo hili."

Thursday, June 26, 2025

HAJI MANARA AWASHUSHIA KIPIGO KIZITO SIMBA BAADA YA KUFUNGWA MARA 5 MFULULIZO / ATOA SIRI HII

 HAJI MANARA AWASHUSHIA KIPIGO KIZITO SIMBA BAADA YA KUFUNGWA MARA 5 MFULULIZO / ATOA SIRI HII

DMI MISSION TANZANIA YATUA KIBAHA KUWASAIDIA WATOTO WA KIKE JUU YA KUPAMBANA NA MIMBA ZA UTOTONI

 


NA VICTOR MASANGU,KIBAHA 


Jamii wakimemo walezi na wazazi wametakiwa kuhahakikisha wanaweka misingi imara na kuwa  mstari wa mbele katika kuwalinda watoto wa kike katika suala zima la ukatili wa kijinsia ikiwa pamoja na kutokomeza ndoa za utotoni.

Kauli hiyò imetolewa na Madina Mussa ambaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha wakati wa sherehe  maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika ambayo yameandaliwa na Shirika lisilokuwa la kiseŕikala la  DMI Mission Tanzania.

Mussa amesema kuwa ili kutekeleza mazingira rafiki kwa watoto waweze kupata haki hiyo ya msingi imejenga miundombinu mizuri ya watoto kujisomea.

"Katika kukabiliana na ukatili na ndoa za utotoni wazazi na walezi lazima washirikiane na serikali kuhakikisha haki za msingi za mtoto zinalindwa ikiwa ni pamoja na elimu, kumlinda na ukatili na kuishi katika mazingira mazuri kwani haki za mtoto zinaanzia nyumbani,"amesema Madina.

Awali Mkurugenzi wa DMI Mission Tanzania Sister Fathima Jacintha Ran amesema kuwa dhima ya siku hiyo ni Kupanga bajeti na kuweka bajeti kwa haki za watoto.

Ran amesema kuwa lengo ni kuhakikisha ustawi, elimu, na hatma njema za watoto ikiwa ni kukumbusha wajibu wa pamoja kuhakikisha watoto wa Afrika wanapata haki za msingi za elimu bora, huduma za afya, ulinzi na fursa ya kukua.

Naye Ofisa Maendeleo ya Jamii kitengo cha watoto Halmashauri ya Mji Kibaha Hanifa Mruma amesema kuwa mradi ulioanzishwa na shirika hilo wa kupambana na mimba za utotoni ni mzuri na utasaidia kukabiliana na changamoto hiyo.

Kwa upande wake moja ya wanufaika kwenye mradi huo wa Klabu za Wanawake Vijana Chiku Hamis amesema kuwa wanalishukuru shirika hilo kwa kuwapatia vifaa kwa ajili ya kutengeneza batiki na sabuni kwa ajili ya mafunzo ya utengenezaji vitu hivyo. 

Mradi huo wa kupunguza mimba za utotoni unatekelezwa kwenye Kata tatu za Pangani, Tumbi na Kongowe.

Wednesday, June 25, 2025

#LIVE - KARIAKOO DERBY JUNI 25, 2025 | Uchambuzi wa kina kabla ya mechi

 YANGA SC vs SIMBA SC | Pata Pata uchambuzi wa kina kutoka kwa Ramadhan Mbwaduke na Amri Kiemba wakiwa na Patrick Nyembera ndani ya studio....

Ni kuelekea mchezo wa NBC Premier League kati ya Yanga vs Simba, leo Juni 25, 2025 saa 11:00 jioni.

Monday, June 23, 2025

WAAMUZI WA DERBY YA KARIAKOO YANGA v SIMBA WANATOKA MISRI

 

 MWAMUZI Amin Mohamed Omar kutoka nchini Misri atasimamia sheria zote za soka katika pambano la watani wa jadi Yanga dhidi ya Simba Jumatano wiki hii Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Taarifa ya Bodi ya Ligi (TPLB, imeeleza kuwa mwamuzi huyo atasaidiwa na Mahmoud Ahmed Abo na Samir Gamal Saad, huku mwamuzi wa akiba akiwa ni Ahmed Mahrous wote kutoka Misri. Mtathimini waamuzi ni Ali Mohamed kutoka Somalia.

CCM YAZUIA ZIARA, MIKUTANO, SEMINA NA MAKONGAMANO.

 


Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesitisha mara moja ziara, mikutano, semina na makongamano, yanayohusisha wajumbe wa vikao vinavyopigia kura za maoni wagombea kwa ngazi zote mpaka baada ya kura za maoni.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi vikao hivyo ni kwa nafasi za ubunge, uwakilishi na udiwani ambavyo vimekuwa vikiendelea kwenye maeneo mbalimbali. 

“CCM inaendelea kusisitiza kuwa mwanachama yeyote anayetarajia kugombea au wakala wake kuepuka kufanya vitendo vyovyote vinavyoonekana dhahiri kuwa ni kinyume cha katiba, kanuni na miongozo ya chama chetu,”amesema Balozi Nchimbi.

MWENYEKITI UWT BAGAMOYO AWAASA WANAWAKE KUJIPANGA KUMPA SAPOTI DKT.SAMIA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU

 


NA VICTOR MASANGU,BAGAMOYO 

Mwenyekiti wa Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Wilaya  ya Bagamoyo Mariam Mkalì  amewaasa wanawake ķuhakikisha kwamba kuweka misingi mizuri ya kwenda kufanya kampeni za kistaarabu kwa kuzingatia kanuni na taratibu hasa  katika kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Kauli  hiyo ameitoa wakati wa kikao cha Baraza la kawaida la jumuiya ambalo limefanyika katika  Kata ya Msata na kuhudhuliwa na viongozi mbali mbali wa chama pamoja na jumuiya zake.

Mwenyekiti huyo amebainisha kwamba kwa sasa wanapaswa kuwa kitu kimoja  na kushikamana kwa hali ya upendo na amani   katika kipindi chote cha uchaguzi mkuu.

" Kikubwa ninachowaomba wanawake wenzangu  tushikamane hasa katika  kipindi chote  cha uchaguzi na kwamba uchaguzi  usiwe sababu za kutoleana lugha chafu,"amebainisha Mwenyekiti.

Kwa upande wake Katibu wa Jumuiya hiyo ya UWT Wilaya ya Bagamoyo  Catherine Makungwa amewahimiza wanawake kunitokeza kwa wingi katika kumpa  kura nyingi za kishindo Rais wa awamu ya sita Dkt.Samia Suluhu Hassan.

"Nawashukuru kwa dhati  Wabunge, Mjumbe wa Baraza Kuu la UWT Taifa Mariam Ulega na Madiwani wote  kwa michango yao mikubwa ambayo yameitoa  katika kusaidia Jumuiya hiyo kufanikisha shughuli zao  mbali mbali,"

"Pia namshukuru Mbunge wetu Muharami Mkenge, Ridhiwani, Hawa Mchafu, Dkt. Harris na Subira Mgalu ambao wamekuwa msaada mkubwa katika Jumuia yetu, wakiwemo wadau mbalimbali," amesema Makungwa.

Kwa upande wao Madiwani wastaafu  wa Viti Maalumu ambao wamemaliza  muda wao wamesoma taarifa zao za Utekelezaji katika kipindi cha miaka mitano cha kuanzia mwaka 2020 hadi 2025.

Sunday, June 22, 2025

NI SAHIHI KUMSIFIA RAIS SAMIA?



MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Chifu Hangaya, ambaye ni Mkuu wa Machifu nchini, akiwa kwenye Kituo cha Hifadhi ya Utamaduni wa Kabila la Wasukuma - Bujora, Magu, mkoani Mwanza,  Jumamosi, tarehe 21 Juni 2025. 

Na Emmanuel J. Shilatu

Utasikia "Mama anaupiga mwingi", wengineo "Mitano tena kwa Mama", hadi kufikia hatua ya Kila kitu kizuri kuonekana amefanya Mama nikiwa na Maana ya Mama Samia.

Wapo wanaosema anayoyafanya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake juu ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ni sehemu ya kutimiza wajibu wake, hapaswi kupongezwa; Wengine wanasema anayoyafanya hayastahili kutangazwa na wala hastahili kusifiwa kwani tutamfanya aanze kuharibu; ila wapo wengine wanaona anastahili kutiwa moyo na kupongezwa.

Kila Mtu ama kundi la Watu lina mitazamo yake. Nimekusanya mitazamo yote na mwisho wa siku nami nikajiuliza, Je ni sahihi kumsifia Rais Samia kwa yale anayoyafanya?

Nasema, 'Ni sahihi kabisa kwa Watanzania kumsifia Rais Magufuli' kutokana na sababu zifuatazo, twende sawa hapa;-

Mosi; Watanzania wanayo haki ya Kikatiba kwa mujibu wa Ibara 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inatoa uhuru wa kutoa maoni na mawazo. Kumsifia Rais Samia ni sehemu ya Wananchi kutimiza haki yao ya kikatiba ya kutoa maoni na mawazo yao.

Pili; Watanzania wana haki yao kabisa kumsifia Rais Samia anayetimiza wajibu wake wa kutekeleza ahadi zake alizozitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2020 - 2025 inayotokana na ilani ya uchaguzi. Kusema utafanya ni kitu kingine, kutekeleza ahadi yako ni jambo lingine. Kumpongeza Rais Samia kwa kutimiza ahadi zake ni sehemu ya kuonyesha, kukubali na kumuunga mkono kile anachokifanya.

Tatu; Wananchi wana haki ya 'kujivunia' kumpongeza Rais Samia ambaye anaiongoza vyema Serikali yake inayotokana na chama chake Chama Cha Mapinduzi (CCM) kukusanya kodi ipasavyo. Kodi hizo hizo zinazokusanywa ndizo hizo hizo zinazoenda kutuletea maendeleo Watanzania mfano ukamilishwaji wa miradi ya maendeleo ya kimkakati, ujenzi wa miradi ya maendeleo kwenye sekta za afya, elimu, maji nk.

Nne; Watanzania wanayo haki ya 'kujivunia' kumpongeza Rais Samia kwa kuhakikisha anatumia vyema kodi inayokusanywa kwa kuwaletea maendeleo Wananchi. Mathalani ununuzi wa ndege, vivuko, ujenzi wa reli ya kisasa ya standard gauge, ujenzi wa miundombinu ya madaraja, barabara, flyovers yote ni matunda ya matumizi sahihi na makini ya kodi zinazokusanywa. Sote ni mashuhuda miradi yote hiyo ameikamilisha ipasavyo na imeanza kutumika.

Narudia tena kusema, kumsifia Rais Samia kwa mema anayoyafanya kwa Taifa ni sahihi kabisa, ni sehemu ya uzalendo wenyewe wa Mtanzania kwa Taifa lako.

Kama tunaona barabara zinajengwa, madaraja yanajengwa, vivuko vipya vya kisasa vinazinduliwa, ndege mpya zinanunuliwa, reli ya kisasa imekamilika na nyingine inajengwa, flyovers zinajengwa, elimu bure inatolewa, dawa hospitalini zipo, umeme umesambazwa mpaka vijijini, hakika ametekeleza kwa vitendo ilani ya uchaguzi. Kwanini Watanzania tusijivunie kumpongeza Rais Samia?

Nahitimisha andiko hili kwa kumpongeza Rais Samia kwa uzalendo wake kwa Taifa, utekelezaji wa ilani ya uchaguzi inayowaletea maendeleo Watanzania na kuendesha nchi vyema kwa mujibu wa katiba ya nchi.

'Najivunia' kumsifia Rais Samia. Tuendelee kumpongeza na kumtia moyo kwa mema yake anayoyafanya kwa Taifa na kwa Watanzania, historia na vizazi vitamkumbuka kama ambavyo Leo hii tunamkumbuka Hayati Baba wa Taifa Mwl Julius Nyerere, Hayati Dk. John Pombe Magufuli na wengineo wengi.

Shilatu E.J

TWIGA STARS WATAWAZWA KUWA MABINGWA KOMBE LA CECAFA WANAWAKE

 TANZANIA imefanikiwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Women’s Challenge Cup baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Kenya Jana Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Bao pekee la Twiga Stars lililoizamisha Harambee Starlets limefungwa na kiungo mshambuliaji wa Al-Nassr ya Saudi Arabia, Clara Cleitus Luvanga dakika ya 49.
Mchezo mwingine uliotangulia jioni ya leo Sudan Kusini iliichapa Burundi mabao 3-1 hapo hapo Azam Complex.

Kwa matokeo hayo, wenyeji Tanzania wanamaliza na pointi 12 baada ya kushinda mechi zao zote nne, hivyo kutawazwa kuwa malkia wapya wa kandanda ukanda wa CECAFA.

Harambee Starlets inamaliza na pointi tisa katika nafasi ya pili baada ya kupoteza mchezo huo wa kwanza  kufuatia kushinda mechi tatu za awali, ikifuatiwa na Uganda, Burundi na Sudan Kusini ambazo kila moja imemaliza na pointi tatu.

Mshambuliaji Opa Clement Tukumbuke wa Tanzania anayechezea klabu ya wa Juárez ya Mexico ameibuka mfungaji bora wa michuano hiyo kwa mabao yake matano akifuatiwa na Martha Emedot wa Kenya aliyemaliza na mabao manne.


Naye kiungo Diana Lucas Msewa wa Trabzonspor ya Uturuki, amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa michuano hiyo huku Naijat Idirssa wa JKT Queens akichaguliwa Kipa wa CECAFA Women’s 2025.

INTER MILAN YATOKA NYUMA NA KUICHAPA URAWA RED DIAMONDS 2-1 MAREKANI

 

TIMU ya Inter Milan ya Italia jana ilitoka nyuma na kushinda mabao 2-1 dhidi ya Urawa Red Diamonds ya Japan katika mchezo wa Kundi E Kombe la Klabu Bingwa ya Dunia ya FIFA Uwanja Lumen Field, Seattle, Washington, Marekani.


Winga Ryōma Watanabe alianza kuifungia Urawa Red Diamonds dakika ya 11, kabla ya mabao ya Waargentina wawili kubadili mambo – kwanza mshambuliaji Lautaro Martínez akiisawazishia Inter Milan dakika ya 78 na kiungo Valentín Carboni kufunga la ushindi dakika ya 90’+2.


Mechi nyingine ya Kundi E jana River Plate ya Argentina ilitoka sare ya bila mabao na Monterrey ya Mexico Uwanja wa Rose Bowl, Pasadena.


Baada ya matokeo hayo, sasa River Plate inaongoza Kundi E kwa pointi zake nne ikiizidi tu bao moja Inter Milan, wakati Monterrey yenye pointi mbili inashika nafasi ya tatu na Urawa Red Diamonds inaburuza mkia kufuatia kupoteza mechi zote mbili za mwanzo.

MAMELODI SUNDOWNS YABAMIZWA 4-3 NA BORUSSIA DORTMUND KOMBE LA DUNIA LA VILABU

 

MAKOSA ya kizembe ya safu ya ulinzi jana yaliigharimu Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini kwa kuruhusu mabao mawili ya zawadi kwa wapinzani, Borussia Dortmund ya Ujerumani waliobuka na ushindi wa 4-2 katika mchezo wa Kundi F Kombe la Klabu Bingwa ya Dunia ya FIFA Uwanja wa TQL Stadium, Cincinnati, Hamilton, Ohio, Marekani.


Kwanza alikuwa ni kipa Ronwen Williams aliyetoa pasi fyongo ambayo ilinaswa na kiungo Felix Kalu Nmecha akaifungia bao la kusawazisha Borussia Dortmund dakika ya 16 kufuatia mshambuliaji Mbrazil, Lucas Ribeiro kuanza kuifungia Mamelodi Sundowns dakika ya 11 – kabla ya beki wa kulia, Khuliso Mudau kujifunga dakika ya 59 kuwapatia wapinzani bao la nne baada ya mshambuliaji Mguinea, Serhou Guirassy kufunga la pili dakika ya 34 na kiungo Jobe Bellingham wa England kufunga la tatu dakika ya 45.


Hata hivyo, Mamelodi ilipambana na kufaniikiwa kupata mabao zaidi yakifungwa na washambuliaji Iqraam Rayners dakika ya 62 na Lebogang Mothiba dakika ya 90.
Mechi nyingine ya Kundi F jana Fluminense ya Brazil iliichapa Ulsan HD ya Korea Kusini mabao 4-2 Uwanja wa MetLife, East Rutherford.


Mabao ya Fluminense yalifungwa na Arias dakika ya 27, Nonato dakika ya 66, Freytes dakika ya 83 na Keno dakika ya 90’+2, wakati ya Ulsan HD yalifungwa na Lee Jin-hyun dakika ya 37 na Um Won-sang dakika ya 45+3.


Msimamo wa Kundi F baada ya matokeo hayo ni Fluminense inaongoza kwa pointi zake nne ikiizidi bao moja tu Borussia Dortmund, wakati Mamelodi Sundowns inahamia nafasi ya tatu ikibaki na pointi zake tatu huku Ulsan iliyopoteza mechi zake zote mbili za awali inashika mkia.

WAZALISHAJI UMEME MKOANI NJOMBE WATAKIWA KUSHIRIKIANA

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu (kushoto) akikagua mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji uliopo katika Kijiji cha Masisiwe, Kata ya Ukwama, Wilaya ya Makete Mkoani Njombe unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala Juni 20, 2025. Pembeni yake ni Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kusini Kati, Wilson Sanga

 
Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu (katikati) katika picha ya pamoja na viongozi wa Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji uliopo katika Kijiji cha Masisiwe, Kata ya Ukwama, Wilaya ya Makete Mkoani Njombe unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala Juni 20, 2025. Kutoka kulia ni Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala kutoka REA, Mha. Advera Mwijage akifuatiwa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kusini Kati, Wilson Sanga. Kulia kwa Balozi Kingu ni Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Nishati Lutheran (DKK) Investment Ltd inayomiliki mradi huo, Elikana Kitahenga

 

Muonekano wa Bwawa la maji la kuzalisha umeme la mradi wa Ijangala wa kilowati 360 uliopo katika Kijiji cha Masisiwe, Kata ya Ukwama, Wilaya ya Makete Mkoani Njombe unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala.

 

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu (katikati) akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Nishati Lutheran (DKK) Investment Ltd inayozalisha umeme wa kilowati 360 wa Ijangala, Elikana Kitahenga (kushoto) wakati wa ziara yake kwenye mradi huo unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala Mkoani Njombe Juni 20, 2025. Kulia ni Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala kutoka REA, Mha. Advera Mwijage.


Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu (kulia) akifurahia jambo na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kusini Kati, Wilson Sanga (katikati) na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Nishati Lutheran (DKK) Investment Ltd inayozalisha umeme ka kutumia maporomoko ya maji ya Mto Ijangala, Elikana Kitahenga Juni 20, 2025 wakati wa ziara yake ya kukagua mradi huo uliopo katika Kijiji cha Masisiwe, Kata ya Ukwama, Wilaya ya Makete Mkoani Njombe unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala.

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu (kushoto)) akielekeza jambo kwa Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mha. Advera Mwijage wakati wa ziara yake ya kukagua Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji uliopo katika Kijiji cha Masisiwe, Kata ya Ukwama, Wilaya ya Makete Mkoani Njombe unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala Juni 20, 2025.-Washauriwa kuunda umoja wa kusaidiana na kubadilishana uzoefu



Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu ametoa wito kwa waendelezaji wa miradi ya Nishati Jadidifu Mkoani Njombe kufanya kazi kwa kushirikiana ili kuongeza tija kwenye shughuli zao na kuwa mfano bora kwa waendelezaji wa miradi katika mikoa mingine.

Ametoa wito huo Juni 20, 2025 akiwa katika ziara ya kukagua mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji uliopo katika Kijiji cha Masisiwe, Kata ya Ukwama, Wilaya ya Makete Mkoani Njombe unaomilikiwa na Dayosisi ya Kusini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupitia Kituo cha Udiakonia Tandala.

"Kwa wingi wa rasilimali ya maji iliyopo Mkoani hapa ni dhahiri uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 50 ndani ya Mkoa huu pekee upo, ni suala la nyinyi waendelezaji wa miradi kuunganisha nguvu kwa kufanya kazi kwa kushirikiana na kusaidiana," alisisitiza Balozi Kingu.

Hata hivyo alipongeza kwa jitihada zinazochukuliwa na waendelezaji wa miradi ya kuzalisha umeme katika miradi aliyoitembelea na aliwasisitiza kutoridhika na kiasi kidogo wanachozalisha badala yake wafikirie namna ya kutanua wigo wa uzalishaji ili watanzania waweze kunufaika na umeme wanaozalishwa.

Alisema shughuli nyingi zinahitaji umeme na kwamba Taifa linahitaji kuwa na umeme mwingi wenye kutosheleza ili kuwezesha maendeleo ya kichumi na kijamii hasa ikizingatiwa kuwa umeme ni kichocheo muhimu cha maendeleo na ni nguzo ya uchumi.

Aliwakumbusha kuwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) upo kwa ajili ya kuwaendeleza hivyo wahakikishe wanafanya kazi kwa karibu na Wakala ili kurahisisha shughuli zao na kufikia malengo waliyojiwekea.

"Serikali kupitia REA ipo kwa ajili yenu, hakikisheni kila hatua mnayopiga mnashirikiana kwa karibu na REA ili miradi iweze kwenda kwa kasi na kuleta tija inayokusidiwa," alisisitiza Balozi.

Kwa upande wake Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kusini Kati, Wilson Sanga aliishukuru Serikali kupitia REA kwa kuchangia uendelezaji wa mradi huo unaozalisha kilowati 360 ambazo zote zinaingizwa katika Gridi ya Taifa kwa makubaliano maalum ya kimkataba na TANESCO.

“Tunaishuru sana Serikali kupitia REA kwa kutuwezesha kutekeleza mradi huu ambao umekuwa na mchango mkubwa kwa jamii inayotuzunguka lakini na Taifa kwa ujumla,” alisema Askofu Sanga.

Naye Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage alisema mradi huo wa Ijangala umenufaika na ruzuku ya Jumla ya Shilingi Milioni 996.

Mbali na uwezeshwaji huo, Mhandisi Mwijage alisema Mwendelezaji mradi amewezeshwa na REA kupata mkopo nafuu wa muda wa miaka 12 uliyotolewa kupitia Benki ya Uwekezaji ya Tanzania (TIB) wenye thamani ya Shilingi Milioni 922 kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa miundombinu ya uzalishaji umeme na utekelezaji wa mradi kwa ujumla.


Mha. Mwijage alisisitiza kuwa milango ya Wakala ipo wazi kwa waendelezaji miradi ya Nishati Jadidifu na kwamba wasisite kuwasiliana na Wakala kwa jambo lolote linalokwamisha uendelezaji wa miradi. Vilevile aliwasisitiza wazalishaji umeme kuhakikisha mazingira yanatunzwa ili kuwa na miradi endelevu.

 

Benki ya CRDB yatoa zawadi kwa watoto Muhimbili, yamuaga Profesa Janabi

 


Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (kulia) akimkabidhi zawadi Mkurugenzi mteule wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Profesa Mohammed Janabi kumtakia utumishi mwema wa majukumu anayoenda kuyaanza hivi punde. Hafla hiyo fupi ilifanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili sambamba na kuwafungulia Akaunti ya Junior Jumbo Watoto 76 waliozaliwa hospitalini hapo.

Mkurugenzi mteule wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Profesa Mohammed Janabi (kushoto) akimsikiliza kwa umakini Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (kulia) alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kumuaga na kumtakia kazi njema katik amajukumu yake mapya anayotaraji akuyaanza hivikaribuni.



Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (kulia) na Balozi wa Akaunti ya Junior Jumbo ya Benki ya CRDB, Paula Masanja (kushoto) wakimkabidhi mmoja wa wanawake (katikati) waliojifungua katika Hospitali ya Taifa Muhimbili zawadi kwa ajili ya mtoto wake kuadhimisha Wiki ya Mtoto wa Afrika.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam. Tarehe 19 Juni 2025: Katika kusherehekea Siku ya Mtoto wa Afrika inayoadhimishwa Juni 16 kila mwaka, Benki ya CRDB imetembelea wodi ya watoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na kuwapongeza wazazi kwa kujifungua salama.

Licha ya ziara hiyo iliyofanyika katika wodi ya watoto njiti hospitali hapo, Benki ya CRDB pia imetumia nafasi hiyo kumuaga aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Profesa Mohammed Janabi kwa kushinda kiti cha Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika.

Akizungumza kwenye ziara hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela amesema siku zote wamekuwa wakitoa elimu ya fedha na kuwahamasisha wananchi kutumia huduma za benki tangu wakiwa wadogo ili kujenga msingi imara wa uchumi binafsi siku zijazo.

“Katika wiki hii ya kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika tumeona ni vyema kuja kuzungumza na wazazi hapa Muhimbili. Tunasisitiza elimu ya fedha ianze kutolewa tangu kwa watoto wadogo na ili kuliweka suala hili kwa vitendo, watoto wote waliopo hapa tutawafungulia Akaunti ya Junior Jumbo yenye shilingi 10,000 ya kuanzia ili mzazi akitoka hapa akaendeleze utaratibu wa kumtunzia mwanaye fedha zitakazomsaidia siku zijazo,” amesema Nsekela.

Kwa akiba yoyote iliyomo kwenye Akaunti ya Junior Jumbo, Benki ya CRDB hutoa riba ya mpaka asilimia 5 kwa mwaka hivyo kumpa uhakika mzazi au mlezi uhakika wa fedha za uhakika pindi mwanaye atakapoanza shule au atakapokuwa na mahitaji mengine yanayohitaji fedha.

“Akiba inawekwa kidogokidogo ingawa matumizi yake huwa makubwa pale yanapojitokeza. Ni vizuri kujenga utamaduni wa kuhifadhi fedha kidogo ambazo kadri muda unavyoenda zitazidi kuongezeka hivyo kutosha kwa ada na matumizi mengine ya shule au kwa jambo jingine ambalo mzazi atahitaji kulifanya kwa ajili ya mtoto wake,” amesema Nsekela.

Akimuaga Profesa Janabi anayetarajia kuondoa wiki ijayo kwenda kuanza majukumu yake mapya na Shirika la WHO hivi karibuni, Nsekela amemsifu kwa mikakati makini aliyonayo na kumuahidi kwamba Benki ya CRDB ipo tayari kushirikiana naye huko na anakokwenda na itaendeleza uhusiano mwema uliopo na Hospitali ya Taifa Muhimbili hata baada ya yeye kuondoka.

“Nilikusikiliza wakati wa kampeni za kuomba uchaguliwe kuiongoa WHO. Ulikuwa na mikakati 10 lakini mimi nimevutiwa na tatu ambazo ni utafiti na ubunifu, ubia pamoja na ufadhili wa huduma za afya kwa vyanzo vya ndani. Naamini vipaumbele hivi sio tu vitazifaa nchi zote 47 utakazokuwa unazihudumia bali vinato anafasi kwetu sekta binafsi kushiriki zaidi kuimarisha huduma za afya katika mataifa yetu. Benki ya CRDB itashirikiana nawe katika maeneo haya yote,” amesema Nsekela.

Kwa upande wake, Profesa Janabi ambaye ameimarisha ufanisi huduma hospitalini hapo tangu alipoteuliwa kuwa mkurugenzi mtendaji mwaka 2022, ameishukuru Benki ya CRDB kwa kwenda kumuaga akisema ni kampuni ya kwanza kufanya hivyo jambo linaloonyesha heshima kubwa ambayo taasisi hiyo kubwa ya fedha imempa.

“Uhusiano wangu na Benki ya CRDB ni wa muda mrefu. Tangu nilipokuwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) tulikuwa pamoja mkitusaidia kugharimia matibabu ya watoto. Nafurahi mmenikumbuka leo na kuja kuniaga,” amesema Profesa Janabi.

Akitarajiwa kuondoka wiki ijayo, Profesa Janabi anaiacha Tanzania akikumbukwa kwa utoaji wake wa elimu kupitia mitandao ya kijamii jambo lililoongeza hamasa ya kuepuka ulaji usiozingatia mahitaji ya kiafya unaoweza kumsababishia mtu magonjwa yasiyoambukiza.

Katika kuendeleza elimu hiyo, Profesa Janabi aliwaeleza wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwamba wangepata chakula cha mchana pamoja na akasisitiza: “Mlo wetu leo utakuwa tunda moja la apple (tufaa).”

Akiwa mkurugenzi mtendaji mwanzilishi wa JKCI, Profesa Janabi alifanikiwa kuifanya kuwa taasisi mahiri inayohudumia wagonjwa wa ndani na watokao nje ya nchi hivyo kuacha mchango ambao hautosahaulika.

Balozi wa Akaunti ya Junior Jumbo, Paula Masanja aliwatia moyo wazazi waliojifungua watoto njiti na kuwahamasisha kuitumia akauniti hiyo kwa ajili ya watoto yao akisema ni muhimu kuwa na akiba kwa ajili ya matumizi yatakayojitokeza wakati wowote.

“Nami ni mzazi mwenye mtoto mdogo kama ninyi. Akaunti ya Junior Jumbo ni nzuri, itumieni kwa ajili ya watoto wenu,” alihamasisha Paula.