ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, November 12, 2022

AJALI, UGONJWA AFYA YA AKILI VYAWEKWA KUNDI LA HATARI.

 


Ajali na magonjwa ya afya ya akili vimetajwa kuwa sehemu ya magonjwa yasiyoambukiza (NCDs).

Ni katika kongamano la nne la kisayansi la magonjwa yasiyoambukiza lililofanyika jana jijini Mwanza.

Akizungumza kwenye ufunguzi wa kongamano hilo, Profesa Paschal Ruggajo, mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Tiba katika Wizara ya Afya alisema ajali zinagharimu maisha ya watu wengi na ugonjwa wa afya ya akili unaathiri jamii.


“Ni vema tutambue kuwa magonjwa yasiyoambukiza yanaenda sambamba na ajali na ugojwa wa afya ya akili. Ni vema kuweka mkazo kwenye kupunguza magonjwa haya bila kuyaacha nyuma ili kupata suluhu ya pamoja,” alisema Profesa Ruggajo.


Ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza limechochewa na vihatarishi vinavyorekebishika, ambavyo ni mitindo isiyofaa ya maisha kama matumizi ya tumbaku, lishe duni, matumizi ya pombe kupita kiasi, kutoushughulisha mwili au kutofanya mazoezi ya viungo mara kwa mara bila kusahau unene uliokithiri.


Alisema utafiti wa mwaka 2018 unaonyesha hapa nchini watu wazima milioni 2.6 sawa na asilimia 8.7 wanatumia tumbaku, huku utafiti wa mwaka 2012 ukionyesha matumizi ya pombe kupita kiasi ni asilimia 29.3 na kuna asilimia 34.7 ya watu wenye unene uliokithiri.


Ingawa takwimu za polisi, kitengo cha Usalama Barabarani zinaonyesha kupungua kwa ajali za barabarani 2021 licha ya madhara ya ajali hizo hususani majeruhi, hali bado ni mbaya na madhara yake kwa jamii ni makubwa.


Kwa mujibu wa takwimu hizo, ajali za barabarani zilizorekodiwa zilifikia 1,864 mwaka 2021, ukilinganisha na 1,933 mwaka 2020.

Mwaka 2021 ajali hizo zilisababisha vifo vya Watanzania 1,368 na majeruhi 2,452, wakati 2020 kulikuwa na vifo 1,384 na majeruhi 2,362.


Ukiacha ajali, Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe katika kipindi cha Julai 2021 hadi Machi 2022 ilihudumia wagonjwa 28,325, kati yao 26,761 ni wagonjwa wa akili wa nje na wa ndani ni 1,564.


Wagonjwa wa msamaha waliopewa huduma walikuwa 3,985, ambao waliigharimu hospitali Sh60,2 milioni katika kipindi hicho.


Hali ikiwa hivyo, kwa ujumla magonjwa yasiyoambukiza yanazidi kuwa mzigo kwa taifa.


Agosti mwaka huu, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Bernard Konga alisema mfuko huo kwa mwaka 2021/22 ulitumia Sh99.09 bilioni kulipia huduma zilizotolewa kwa wagonjwa hao.


Kongamano kuhusu magonjwa hayo lilizinduliwa na Profesa James Mdoe, naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia aliyesisitiza juu ya umuhimu wa wanasayansi kufanya utafiti kwenye dawa za asili na endapo itathibitika kuwa ziko sawa zianze kutumika kwenye hospitali zetu.


Pia afya ya akili ikiwa ni kundi la magonjwa yasiyoambukiza, kwa takwimu za Ofisi ya Rais (Tamisemi), inakadiriwa Tanzania kuwa na wagonjwa milioni saba wenye matatizo na wengi wao wanaishi na sonona.


Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO zinaonyesha kuwa katika mwongo mmoja uliopita, kumekuwa na ongezeko la watu kwa asilimia 13, ambapo watu bilioni 1 wanaishi na tatizo hilo duniani.


Ajali, kundi lingine la magonjwa yasiyo ya kuambukiza, zinaelezwa na WHO kuwa kwa mwaka zinachukua uhai wa watu milioni 1.35 na wengine milioni 20 hadi 50 wakiachwa na majeraha na ulemavu wa kudumu.


Takwimu hizo zinaonyesha asilimia 74 ya watu duniani wanapoteza maisha kutokana na magonjwa yasiyoambukiza na asilimia 33 ya Watanzania wanapoteza maisha kwa magonjwa hayo ambayo idadi ya waathirika wake inaongezeka.


Katika kongamano hilo la kisayansi linalofanyika kwa wiki moja, kutakuwa na shughuli mbalimbali za kiafya zitakazohusisha upimaji wa afya bure kwenye viwanja vya CCM Kirumba.


Kongamano hilo limewaleta pamoja wadau mbalimbali wa afya zaidi ya 400 na litajadili mada mbalimbali za kitaaluma na kutoa matokeo ya tafiti mbalimbali za kiafya.


Pamoja na mada nyingine, mzigo wa magonjwa yasiyoambukiza kusini mwa Jangwa la Sahara na madhara ya mabadiliko ya tabianchi itakuwa miongoni.


Mada hii itawasilishwa na Profesa Harold Renz, Profesa wa dawa katika Chuo Kikuu cha Marburg Ujerumani.


Na mada nyingine ni magonjwa yasiyoambukiza kwa watoto na vijana; asiachwe mtu nyuma, itakayowasilishwa na Profesa Francis Furia wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Muhimbili.

KATIBU CHAMA CHA SOKA MWANZA AZUNGUMZIA MAANDALIZI KUELEKEA MTANANGE WA KAGERA DHIDI YA YANGA

 NA ALBERT G. SENGO /MWANZA

Leonard Malongo ni Katibu wa Chama cha soka mkoa wa Mwanza anaeleza jinsi maandalizi ya mchezo wa Kagera dhidi ya Yanga unaotaraji kuputwa dimba la CCM Kirumba.

KOCHA NABI: TUNA DENI NA HII KLABU AFUNGUKA KUTOKUWEPO KWA AZIZ KI NA AUCHO

 NA ALBERT G.SENGO/ MWANZA

Kocha Mkuu wa Yanga Sc Nasreddine Nabi pamoja na Kiungo Mshambuliaji Yusuph Athuman wamezungumza Maandalizi yao ya kuvaana na Kagera Sugar kwenye Mchezo wa kesho Jumapili, wa Ligi Kuu ya NBC, utakaochezwa dimba la CCM Kirumba jijini hapa.

KOCHA WA KAGERA "SITOKUBALI KUFUNGWA NA YANGA"

 NA ALBERT GSENGO/MWANZA

Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Mecky Maxime pamoja na Nahodha Charles Luhende wamezungumza maandalizi yao ya mchezo wa kesho Jumapili, wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Yanga Sc , utakaochezwa uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza. #SportsRipoti #michezolive #michezo #ligikuutanzaniabara

Friday, November 11, 2022

VIKOSI VYA TIMU MBALIMBALI ZA TAIFA KOMBE LA DUNIA

Ufaransa.


Ubalgiji


Uholanzi


Uingereza.


Hispania


Ujerumani.


Uruguay.
 

AJALI YA GARI TEGETA

 


Dar es Salaam. Watu kadhaa wanahofiwa kujeruhiwa kutokana na ajali iliyohusisha magari matatu iliyotokea eneo la Kitengule Tegema jijini Dar es Salaam leo Novemba 11, 2022.


Kamanda wa polisi mkoa wa Kinondoni, Mtatiro Kitinkwi amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo alipoulizwa kwa simu, hata hivyo amesema taarifa zaidi atazitoa kwani kwa sasa yupo nje ya ofisi.


“Nilikuwa nje ya ofisi kikazi ndiyo ninarudi, lakini hilo tukio lipo na limetokea…nikirudi ofisi nikiiandaa basi nitatoa taarifa,” amesema kamanda huyo.

Thursday, November 10, 2022

SERIKALI KUCHUNGUZA MWENENDO WA MIKOPO YA HALMASHAURI

 

Serikali imeunda timu ya uchunguzi kufuatilia mikopo ya asilimia kumi inayotolewa kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ili kubaini ikiwa fedha hizo zinawanufaisha walengwa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Angellah Kairuki amebainisha hayo Alhamisi Novemba 10, 2022 jijini Dodoma wakati akifunga kikao kazi cha Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Sekretarieti za Mikoa na Wakuu wa Idara za Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Waziri Kairuki amesema baada ya uchunguzi huo kukamilika, Serikali itachukua hatua za kisheria dhidi ya wote watakaobainika kukiuka kanuni, taratibu na sheria za utoaji wa mikopo hiyo ikiwemo kuanzisha vikundi hewa.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Zainabu Chaula amewataka maafisa maendeleo ya jamii kusimamia vyema majukumu yao ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mikopo inayotolewa na halmashauri inaleta tija kwa walengwa.

Kwa upande wake mdau wa maendeleo, Yassin Ally ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la kutetea haki za wanawake na watoto KIVULINI amesema usimamizi mzuri wa mikopo inayotolewa na halmashauri nchini utaimarisha kiwango cha uchumi wa kaya na hivyo kupunguza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Angellah Kairuki akihitimisha kikao kazi cha maafisa maendeleo ya jamii jijini Mwanza.
Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Zainabu Chaula akizungumza kwenye kikao hicho.
Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally akichagiza mada kwenye kikao hicho.
Maafisa Maendeleo ya Jamii wakiwa kwenye kikao hicho.
Washiriki wakifuatilia kikao hicho.
Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Sekretarieti za Mikoa na Wakuu wa Idara za Mamlaka za Serikali za Mitaa wakiwa kwenye kikao kazi cha siku tatu kuanzia Novemba 08-10, 2022 jijini Dodoma.
Picha ya pamoja.
Tazama BMG TV hapa chini

DC BULEMBO AWAONYA WENYE TABIA YA KUFANYA SHUGHULI ZA UCHIMBAJI WA MADINI KWENYE VYANZO VYA MAJI

 

MKUU wa wilaya ya Muheza Halima Bulembo akizungumza wakati wa ziara ya wadau kutembelea chanzo cha maji cha mto Zigi iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa mradi wa majaribio wa utunzaji wa vyanzo vya maji kijiji cha Kwemwewe kata ya Mbomole Tarafa ya Amani wilayani Muheza kushoto  ni Mkuu wa wilaya ya Pangani Ghalib RIngo
Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Mazingira y Asili ya Amani Fikiri Maiba  akizungumza wakati wa ziara hiyo
MKUU wa wilaya ya Pangani Ghalib Ringo akizungumza wakati wa ziara hito
 Afisa Mradi wa Mfuko wa Uhifadhi wa Milima ya Tao la Mashariki Magreth Victor akizungumza wakati wa ziara hiyo


Na Oscar Assenga, MUHEZA

MKUU wa wilaya ya Muheza Mkoani Tanga Halima Bulembo amewaonya wananchi wenye tabia za kuvamia vyanzo vya maji na kuchimba madini Tarafa ya Amani wilayani Muheza kuacha mara moja vitendo hivyo kabla hawaja kumbana na mkono wa sheria.


Bulembo aliyasema hayo wakati wa ziara ya wadau kutembelea chanzo cha maji cha mto Zigi iliyokwenda sambamba na uzinduzi wa mradi wa majaribio wa utunzaji wa vyanzo vya maji kijiji cha Kwemwewe kata ya Mbomole Tarafa ya Amani wilayani Muheza


Mkuu huyo wa wilaya alisema kwamba wamejipanga vilivyo kuhakikisha wanaohusika na vitendo vya namna hiyo wanashughulikiwa ili kuweza kuvimaliza kwa lengo la kuwezesha vyanzo vya maji vinaendelea kuwa salama.


"Kumekuwa na tabia ya wananchi kuvamia maeneo ya vyanzo vya maji wananchi kufanya shughuli za uchimbaji wa madini jambo ambalo lina sababisha uharibifu kwenye vyanzo hivyo ikiwemo uchafuzi"Alisema Mkuu huyo wa wilaya.


Alisema kutokana na uwepo wa athari hizo kubwa kwa jamii watahakikisha wanakula sahani moja na wahusika ili iweze kuwa fundisho kwa wengine ambao wame kuwa na tabia kama 
hizo.


" Uchimbaji wa madini ya dhahabu kwenye vyanzo vya maji kuna athari kubwa sana moja hivyo tutawashughulikia wote tutakao wakamata ili kuwezesha vyanzo hivyo vinatunzwa" Alisema.


Hata hivyo alitoa wito kwa wananchi kuacha kufanya uharibifu kwenye vyanzo vya maji na atayekamatwa na vyombo vya dola sheria itachukua mkondo wake.


"Lakini niwaombe wananchi mtakapowaona walio maeneo ya karibu wafichueni kwa maana vitendo hivyo vina madhara makubwa na kupelekea magonjwa hivyo tunaendelea kuvilinda vyanzo vya maji kwani maji ni uhai" Alisema.


Awali akizungumza wakati wa ziara hiyo ya wadau Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Mazingira y Asili ya Amani Fikiri Maiba alisema katika eneo hilo kuna chanzo cha maji cha mto Zigi ambacho kinalisha Tanga,Muheza na Mkinga.


Alisema katika vyanzo hivyo kuna uharibifu wa uchimbaji na utafutaji wa dhahabu hivyo jamii inapofuata madini na uharibu huo una madhara makubwa ambacho unapuguzua ubora wa maji kwenye mito.


Alisema katika matumizi hayo kunaleta shida kubwa na hivyo kutumia gharama kubwa kutibu maji hivyo lazima jamii ibadilike kwa ajili ya kulinda vyanzo vya maji.


Hata hivyo alisema kuna hatua mbalimbali zinchukuliwa ikiwemo operesheni na wamepata wahalifu ambao hivi Sasa wanaendelea na kesi hzao hiyo wanatoa wito kuhakikisha vyanzo vya maji ili viweze kuwa endelevu.


Awali akizungumza wakati w ziara hiyo ya wadau Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Tanga Uwasa Dkt Ally Fungo alisema kutokana na uharibifu wa vyanzo vya maji wamekuwa wakitumia zaidi ya Bilioni 1 kutibu maji kutokana na uchaguzi ambao umekuwa ukifanyika.

Naye kwa upande wake Afisa Mradi wa Mfuko wa Uhifadhi wa Milima ya Tao la Mashariki Magreth Victor alisema katika kipindi cha nyuma Serikali ilifanikiwa kudhibiti shughuli za uchimbaji wa Madini ya dhahabu kwenye vyanzo vya mto zigi.


Alisema lakini kwa siku za hivi karibuni baadhi ya wananchi wa eneo hilo la Amani wameanza tena shughuli za uchimbaji huo hivyo ipo haja ya hatua za makusudi kuchukuliwa ili kuweza kuendelea kudhibiti vitendo hivyo.

MAJAMBAZI WAAMURU KUPIKIWA KITOWEO CHA KUKU BAADA YA UVAMIZI


Wenyeji wa Kitengela wamelilia asasi za usalama kuwanusuru kutokana na utovu wa usalama unaoendelea kuwakosesha usingizi kila kukicha. 

Wenyeji wa eneo hilo wameripoti kwa polisi kuhusu kuvamiwa na majambazi wanaowashurutisha kuwapikia. 

 Wenyeji hao wameripoti kuwa majambazi wanaowavamia wana tabia za kiajabu, sana kwani huwalazimisha kuwapikia mlo kabla ya kuwaibia majumbani mwao. 

Mkazi wa kijiji cha Noonkopir alisimulia jinsi simu yake ilivyotwaliwa na kuamrishwa kupikaugali na kitoweo cha kuku na majambazi waliomvamia. 

Agatha Njogu aliiambia jarida la Nation.africa kuwa alipoendelea kuwapikia wavamizi hao, mmoja wao alikuwa akiwafuatilia yeye na wanao huku wengine wakizidi kuchokora nyumba na kuiba. 

 "Hawakuwa na haraka. Ni uvamizi uliopangwa kwa makini,” Njogu aliiambia the Nation. Wenyeji wamelaumu ongezeko la visa vya ujambazi, kwa utepetevu wa maafisa wa usalama eneo hilo. 

Wanadai kwamba maafisa wa kituo kidogo cha polisi cha Noonkopir, hujitokeza kwa saa chache hata ingawa wanahitajika kwa dharura. 

"Tuliamua kuweka kituo kidogo cha polisi kwa sababu ya visa vya uhalifu kwenye mtaa wetu. Ila maafisa kwenye kituo hicho huwekwa kwa saa chache kisha huondoka," mzee wa kijiji cha Noonkopir village Clement Njung'e alinukuliwa akisema.

WAZIRI DR CHANA AFUNGUA MAONYESHO YA UTALII KARIBU KUSINI MKOANI IRINGA.

 

 

Waziri wa maliasiali na utalii Balozi Dkt Pindi Chana amefungua maonyesho ya pili ya kimataifa ya karibu kusini kata viwanja vya kituo cha kikuu cha utalii kusini Kihesa Kilolo mkoani Iringa ikiwa na lengo la kutangaza vivutio vya kitalii vilivyo kusini.

Waziri wa maliasiali na utalii Balozi Dkt Pindi Chana akiteta jambo na mkuu wa mkoa wa Iringa Halima Dendego wakati wa ufunguzi wa maonyesho ya pili ya kimataifa ya karibu kusini kata viwanja vya kituo cha kikuu cha utalii kusini Kihesa Kilolo mkoani Iringa ikiwa na lengo la kutangaza vivutio vya kitalii vilivyo kusini.



Na Fredy Mgunda,Iringa.

WAZIRI wa maliasiali na utalii Balozi Dkt Pindi Chana amefungua maonyesho ya pili ya kimataifa ya karibu kusini kata viwanja vya kituo cha kikuu cha utalii kusini Kihesa Kilolo mkoani Iringa ikiwa na lengo la kutangaza vivutio vya kitalii vilivyo kusini.

akihutubia wananchi waliojitokeza wakati wa kufungua maeonyesho hayo, waziri wa  Balozi Dkt Pindi Chana alisema kuwa imefika zamu ya kuvitanga vivutio vya kitalii vilivyo kusini ili kuongeza watalii kutembelea na kuongeza pato la taifa.

Balozi Dkt Chana alisema kuwa serikali itatumia maonyesho ya kimataifa ya karibu kusini kama sehemu ya mkakati kutekeleza ilani ya CCM ya kufikisha watalii milioni tano ifikapo mwaka 2025 na wizara ya maliasili imejipanga kimkakati ili kufikia malengo hayo na ikiwezekana kuvuka idadi hiyo ya watalii.

alisema kuwa maonyesho hayo yamefunguliwa rasmi yakihusisha mikoa kumi ya kusini mwa Tanzania ikiwa ni sehemu muafaka yakutangaza utalii wa kusini.

Balozi Dkt Chana alisema kuwa mikoa inayoshiriki maonyesho hayo ni mkoa wa Iringa,Morogoro,Njombe,Mbeya,Songwe,Rukwa,Katavi,Ruvu Lindi na Mtwara ,mikoa hiyo kwa kutumia maonyesho hayo itasaidia katika kutangaza vivutio vya utalii kusini mwa Tanzania.

alisema kuwa maonyesho hayo ya karibu kusini yenye kaulimbiu inayosema “uwekezaji,kusinifahari yetu”ni jukwaa ambalo linawakutanisha wadau mbalimbali katika sekta ya utalii kwa lengo la kuuza bidhaa,kutafuta masoko pamoja na kujenga mahusiano ya kibiashara kwenye sekta mbalimbali za kitalii..

Balozi Dkt Chana alisema kuwa kutokana na kampeni ya filamu ya Tanzania The Royal Tour ilifanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kumesaidia kuongeza idadi ya watalii wa kimaoka watalii 922,692 mwaka 2019 hadi kufukia watalii 1,034,180.

alisema kuwa mikoa ya nyanda za juu kusini imebarikiwa kuwa na vivutio vingi vya kitalii hivy kupitia mradi wa REGROW utasaidia kuvitangaza vivuti hivyo na kujenga kituo cha utaliiwa kusini mwa Tanzania katika eneo la kihesa Kilolo ambacho kitatumia zaidi ya bilioni 12.

Balozi Dkt Chana alisema kuwa serikali ya awamu ya sita imeendelea kujenga viwanja vya ndege kwa lengo la kukuza na kuitanga sekta ya utalii ili kuongeza idadi ya watalii wa ndani na nje ya Tanzania.

MBWEMBWE ZA SHABIKI WA YANGA AKIMUENZI HAYATI BABA WA TAIFA

 


MAGOLI YA AZIZ KI YAFANANISHWA
Dhidi ya Simba Sc.


Dhidi ya Club Africain hii leo.

Wednesday, November 9, 2022

YANGA YATINGA MAKUNDI IKIWA UGENINI

 

YANGA wameandika historia kwa kupata ushindi ugenini na kutinga hatua ya makundi kwenye Kombe la Shirikisho Afrika.

Ushindi pekee umepatikana kipindi cha pili kupitia kwa kiungo wa Yanga Aziz KI ambaye alianzia benchi kwenye mchezo wa leo.

Dakika 45 za awali ni beki Kibwana Shomar alikuwa ni mwiba kwa wapinzani wao Club Africain ambapo alipiga mashuti mawili ambayo yalilenga lango.

Kiungo Bernard Morrison na Sure Boy walikuwa na kazi kubwa uchezesha timu ya Yanga iliyocheza soka la pasi nyingi kipindi cha kwanza na cha pili.

Bao la ushindi limepachikwa dakika ya 79 kwa nyota huyo kuwatungua Waarabu wa Tunisia kwa shuti lilimshinda mlinda mlango baada ya kupokea pasi ya kichwa kutoka kwa mshambuliaji wao mahiri Fiston Mayele.

Pongezi kwa kipa namba moja wa Yanga, Diarra Djigui ambaye alifanya kazi kubwa kuwakikisha anaweka mazingira ya lango lake linakuwa salama kwa dakika zote.

ALIYEKUWA MKE WA BILL GATES MELINDA APATA MPENZI MIEZI 6 BAADA YA KUTALIKIANA NA BILIONEA HUYO


Mke wa zamani wa Bill Gates Melinda yuko kwenye uhusiano mpya wa mapenzi mwaka mmoja baada ya kukamilisha talaka yake na bilionea huyo. 

Hapo awali Melinda aliolewa na Bill Gates, lakini walitalikiana rasmi mnamo Agosti 2021. 

Bill na Melinda waliushangaza ulimwengu walipotangaza kuwa wanaachana rasmi baada ya kuishi kwenye ndoa kwa miaka 27.

 Wengi walijiuliza ni nini kilisababisha wawili hao kutengana, huku wengine wakisema kuwa kweli pesa haziwezi kununua mapenzi. 

Wengi walikuwa na wasiwasi kuhusu jinsi talaka ya wawili hao ingeathiri mamia ya miradi ulimwenguni ambayo walianzisha pamoja. 

 Hata hivyo, kwa mujibu wa TMZ, Melinda kwa sasa anachumbiana na mara kwa mara amekuwa akionekana na aliyekuwa mwandishi wa habari kwenye Televisheni anayedaiwa kuwa mpenzi wake. 

Duru zinaarifu kwamba Melinda amekuwa akichumbiana na Jon Du Pre kwa miezi michache au hata zaidi ikizangatiwa nyakati ambazo wameonekana pamoja. 

Mke wa zamani wa bilionea huyo alionekana akiwa na mwandishi huyo kwenye mechi ya mpira wa vikapu mnamo mwezi wa Aprili, swala lililowaacha wengi na masali chungu nzima. 

Ingawa hakuna anayejua jinsi walivyokutana kwa mara ya kwanza, kilicho wazi ni kwamba wawili hao na baadhi ya jamaa zao hivi majuzi walikuwa na likizo ya pamoja. 

Melinda alifanya mahojiano yake ya kwanza tangu yeye na bilionea wake wa zamani walipotengana mapema mwaka huu, na alizungumzia jinsi ilivyoathiri maisha yake. 

Mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 58 alisema alifikia hatua katika ndoa yake hakuweza kuvumilia tena na ikabidi aondoke kwa sababu ilikuwa imeingia doa. 

 Aliongeza kuwa roho yake inapona na alihisi kwamba anafungua ukurasa mpya huku akisubiri kuona jinsi siku zilizoko usoni mwake zitakavyokuwa. .

ALIYEFARIKI AJALI YA NDEGE AZIKWA SIKU YA BIRTHDAY YAKE.

 

Enzi za uhai wake Zaituni Mohamed Shillah.

SIMANZI na majonzi vimetawala katika mazishi ya mmoja kati ya abiria 19 waliofariki katika ajali ya ndege iliyotokea Ziwa Victoria mkoani Kagera, Zaituni Mohamed Shillah (28), ambaye amezikwa tarehe ambayo inafanana na siku aliyozaliwa.

Leo Jumatano Novemba 9, 2022 tofauti na misiba mingine ulinzi ulikuwa umeimarishwa na ilikuwa marufuku kupiga picha wala kurekodi tukio lolote.

Familia hiyo ilikumbwa na majonzi kwani leo Zaituni alitarajia kusherekea kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa ambapo alizaliwa Novemba 9, 1994, mkoani Dodoma.

Ibada ya mazishi ya Zaituni imeongozwa na Mchungaji Loserian Kambei wa Kanisa la The Mountain Hebron Ministry.


Marehemu ambaye alikuwa akifanya kazi jijini Dar es Salaam na alikuwa anakwenda kikazi mkoani Kagera hata hivyo hakuna aliyekuwa tayari kueleza sehemu aliyokuwa anafanya kazi.


Katika ibada hiyo iliyofanyika nyumbani kwa Idd wilayani Arumeru kabla ya kwenda kuzikwa katika eneo la TPRI, ilihudhuriwa na watu wachache.


Katibu Tawala wa Wilaya  ya Arumeru, James Mchembe, aliongoza waombolezaji katika mazishi hayo ambayo pia yalihudhuriwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Arusha, Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Suleiman Msumi, kamati ya ulinzi na usalama na ndugu na jamaa wa karibu wa familia hiyo.


Zaituni ambaye alizaliwa mkoani Dodoma Novemba 9, 2022, alikuwa akijishughulisha na kazi ya ofisa masoko wa kidigitali jijini Dar es Salaam.


Akihubiri katika ibada hiyo ya maziko, Mchungaji Kambei, amesema ajali hiyo imekuwa pigo kubwa kwa taifa kwani imepoteza nguvu kazi ambayo ilikuwa ikitegemewa


Kuhusu vijana alisema ni wakati wa jamii na taifa kwa ujumla kuombea kundi la vijana ambalo kwa asilimia kubwa wamekiuka maadili na kujihusisha na vitendo viovu.


"Tunalia kama kanisa, watu wanapenda anasa kuliko Mungu,vijana wanajishughulisha na matukio ya ajabu ikiwemo panya road,taifa linaelekea wapi?"Wazazi tuombe kwa ajili ya vijana,watu wamejisahau, tunalia juu ya vijana ni lazima kama jamii tukemee vitendo viovu kwani kizazi kinaangamia,msiba huu ni huzuni kwani leo tunamzika Zaituni na ingekuwa maadhimisho ya siku yake ya kuzaliwa,"aliongeza


Kuhusu mvuvi Jackson Majaliwa, ambaye aliokoa manusura wa ajali hiyo ambaye alitumia kasia kuufungua mlango wa ndege  na kuwezesha watu 24 kuokolewa, amesema ni muhimu jamii kuhakikisha inatenda mema na kusaidiana bila kujali hali zao.


"Jiulize kijana aliyefanya uokoaji ni kijana ni mdogo sana inawezekana alikuwa anatamani kuwa jeshi la uokoaji,lakini hakupata nafasi hiyo.Watu wanalia,yeye imekuwa fursa kwake dunia inamjua leo kwa alichokifanya,labda alikata tamaa lakini Mungu amemsaidia,"amesema

MAAFISA MAENDELEO WATAKIWA KUSAIDIA MAPAMBANO DHIDI YA VITENDO VYA UKATILI.

 

Maafisa Maendeleo ya Jamii wametakiwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ili kusaidia kupambana na matukio ya vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto ambayo yameendelea kuripotiwa nchini.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima alitoa rai hiyo Jumanne Novemba 08, 2022 jijini Dodoma wakati akifungua kikao kazi cha siku tatu cha Maafisa Maedeleo ya Jamii wa Sektretarieti za Mikoa na Wakuu wa Idara za Maendeleo ya Jamii kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa Tanzania Bara.

Dkt. Gwajima alisema wataalamu hao wa maendeleo ya jamii wanao mchango mkubwa katika ustawi wa jamii hivyo baada ya kikao hicho wakaweke mikakati itakayosaidia kuwalinda wanawake na watoto ambao ni wahanga wakubwa wa vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Katika kikao hicho, Mratibu wa mpango wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto (MTAKUWWA), Joel Mangi alisema vitendo vya ukatili wa kijinsia vimezidi kuongezeka nchini ambapo matukio 20,306 yakiwemo elfu nane ya ukatili dhidi ya watoto yameripotiwa katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Septemba mwaka huu.

Mangi alibainisha kuwa matukio ya ukatili yalioongoza katika kipindi hicho ni mimba kwa wanafunzi yaliyofikia 1,115 pamoja na udhalilishaji wa kijinsia ambapo ubakaji ni matukio 4,797 na ulawiti matukio 1,044.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji shirika la kutetea haki za wanawake na watoto KIVULINI la jijini Mwanza, Yassin Ally alisema utendaji kazi wa maafisa maendeleo ya jamii ngazi ya wilaya, mkoa na halmashauri ukiimarishwa watasaidia kuelimisha jamii kupitia vikao mbalimbali na hivyo kusaidia kutokomeza matukio ya ukatili.

Alisema ni vyema ukawepo mkakati wa kuwawezesha maafisa maendeleo ya jamii na kuhakikisha wanawafikia wananchi angalau mara mbili kwa kila wiki badala ya kukaa maofisini muda wote huku wakiacha kulalamika kwamba wamenyang’anywa majukumu yao na kada nyingine.

Yassin pia alishauri kuimarishwa kwa mikakati ya ulinzi wa watoto wa jinsia zote kufuatia idadi ya watoto wa kiume wanaolawitiwa kuongozeka, akisema changamoto hiyo imetokana na nguvu kuelekezwa zaidi kwa watoto wa kike.

Awali Rais wa Chama cha Wataalam wa Maendeleo ya Jamii (CODEPATA) Angela Mvaa alisema tayari mchakato wa kuanzisha Sheria ya Maendeleo ya Jamii umeanza ambapo kukamilika kwake kutasaidia wataalamu hao kutimiza kwa weledi majukumu yao.

Takwimu za matukio ya ukatili wa kijinsia zilizotolewa kwenye kikao hicho katika kipindi cha mwezi Januari hadi Septemba mwaka huu, zinaonyesha kuwa Mkoa wa Mbeya unaongoza kwa matukio 301 ya ubakaji, Morogoro na Mwanza kila mmoja matukio 114 ya mimba kwa wanafunzi na Mkoa wa kipolisi Kinondoni ukiongoza kwa matukio 96 ya ulawiti.
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima akifungua kikao kazi cha Maafisa Maedeleo ya Jamii wa Sektretarieti za Mikoa na Wakuu wa Idara za Maendeleo ya Jamii kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa Tanzania Bara kinachofanyika jijini Dodoma, Novemba 08-10, 2022.
Mratibu wa Mpango wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA), Joel Mangi akitoa takwimu za ukatili kwa kipindi cha Januari hadi Septemba 2022.
Wataalamu wa Maendeleo ya Jamii wakifuatilia kikao kazi hicho.
Mkurugenzi Mtendaji Shirila la Kutetea Haki za Wanawake na Watoto KIVULINI, Yassin Ally akitoa salamu kwenye kikao hicho.
Washiriki wa kikao hicho wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally wakati akiwasilisha mada kwenye kikao kazi hicho.
Washiriki wakifuatilia kikao hicho.
Maafisa Maedeleo ya Jamii wa Sektretarieti za Mikoa na Wakuu wa Idara za Maendeleo ya Jamii kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa Tanzania Bara wakifuatilia kikao hicho.
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima (kushoto) akizindua Mwongozo wa Taifa wa uendeshaji majadiliano kuhusu Mila na Desturi zenye Madhara kwa Jamii.
Viongozi mbalimbali meza kuu akiwemo mgeni rasmi, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima (wa tatu kushoto).