ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, March 31, 2020

WAZIRI MPINA ASHTUKIA UPIGAJI WA BILIONI 2.6 UJENZI MAABARA YA UVUVI, AAGIZA TAKUKURU KUCHUNGUZA NDANI YA SIKU 7

 Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akipata maelezo ya namna ya shughuli ya ujenzi wa mradi wa jengo la Maabara ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Kituo cha Dar es Salaam  kutoka kwa Mkandarasi wa Kampuni ya Petra Constuction co. Limited, Nicholaus Mlayi alipotembelea mradi huo Kunduchi Dar es Salaam. Picha na Mpiga Picha Wetu.
 Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akipata ufafanuzi kutoka kwa Mshauri Mwelekezi wa Kampuni ya Y&P Architect inayosimamia Mradi wa Ujenzi wa Maabara ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Kituo cha Dar es Salaam, Anna Shayo alipotembelea mradi huo Kunduchi Dar es Salaam. Picha na Mpiga Picha Wetu
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akiangalia ramani ya mradi wa jengo la Maabara ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (TAFIRI) Kituo cha Dar es Salaam baada ya kutembelea kukagua maendeleo ya ujenzi wa majengo hayo na kuunda tume kuchunguza mradi huo. Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa TAFIRI, Dk. Ismael Kimerei . Picha na Mpiga Picha Wetu.
Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amesimamisha malipo yote kwa Mkandarasi wa Kampuni ya Petra Construction co. Limited inayojenga maabara ya kisasa ya Taasisi ya Uvuvi Tanzania (TAFIRI) kituo cha Dar es Salaam hadi uhakiki wa gharama halisi za mradi huo utakapokamilika baada ya kubaini kuwepo matumizi mabaya ya fedha za umma kiasi cha shilingi bilioni 2.6
Hivyo Waziri Mpina ameunda tume ya kiuchunguzi itakayofanya kazi kwa siku saba na kuwahusisha wataalamu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili kubaini ukweli wa gharama halisi za mradi huo.
Akizungumza mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa Maabara ya  Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI)  jijini Dar es Salaam, Waziri Mpina alisema amebaini mradi unaojengwa miundombinu yake ni midogo ikilinganishwa na mkataba ulioridhiwa  wa sh. bilioni 2.6 na kwamba taarifa ya uhakiki ya mradi huo itawasilishwa wizarani ikiwa na mapendekezo ya hatua za kuchukua dhidi ya wizi huo wa fedha za umma.
Waziri Mpina alisema thamani halisi ya mradi huo hailingani na fedha zilizotolewa na Serikali huku akitolea mfano baadhi ya miradi ya ujenzi wa majengo mbalimbali ikiwemo vituo vya afya na hospitali za wilaya zinazojengwa maeneo mbalimbali nchini.
Hata hivyo wakati wa mjadala ukiendelea wa kuhoji matumizi ya fedha hizo kwenye mradi huo, mmoja wa wakandarasi wanaojenga majengo hayo alimweleza Waziri Mpina kuwa hadi mradi utakapomika kutabaki ‘chenji’ kiasi cha shilingi milioni 500 jambo lililotilia mashaka na kuibua maswali mengi juu ya gharama halisi za mradi huo.
Kufuatia mkanganyiko huo wa maelezo ya mkandarasi na hali halisi iliyoonekana kwenye mradi huo ndipo Waziri Mpina akalazimika kutangaza uamuzi huo wa kuundwa tume hiyo ili iweze kufanya tathmini ya gharama ya mradi iliyofanywa na Mshauri mwelezi wa mradi, namna zabuni ya kumpata mkandarasi ilivyotangazwa na namna mshauri mwelekezi alivyopatikana na hali ya ujenzi unavyoendelea kwa sasa ili kujua dosari ilisababishwa na nani.

Hivyo Waziri Mpina akabainisha kuwa baada ya kazi hiyo ya uhakiki kukamilika ndani ya siku saba ukweli utajulikana na hatua zote zilizopitiwa katika mradi huo ili kubaini  kama Sheria ya Manunuzi ya Mwaka 2004 ilikiukwa ili hatua ziweze kuchukuliwa kwa wote watakaohusika na ubadhirifu huo wa fedha za umma.
 “Sikubaliani na hizi gharama za mradi majengo na miundombinu ni midogo ikilinganishwa na mkataba wa bilioni 2.6, BOQ ilihakikiwa na wahandisi wa wizara, washauri waelekezi walijiridhisha kwamba iko sawa na ujenzi ukaenda hadi bilioni 2.6 mtu yeyote akija anakataa” alihoji Waziri Mpina
Hivyo Waziri Mpina ameagiza ujenzi wa mradi huo uendelee bila kusimama na ukamilike ifikapo Aprili 20 mwaka huu kama mkataba unavyoeleeza na baada ya jengo litazinduliwa ikiwa ni sehemu ya kuleta mageuzi makubwa ya sekta ya uvuvi kupitia eneo hilo muhimu la utafiti.
“Nitaleta timu ya ukaguzi itakayofanya uhakiki wa thamani ya fedha katika ujenzi wa jengo hili, kuanzia kwenye kutangaza tenda yenyewe, thamani ya mradi, kumpata mkandarasi mwenyewe, cost estimates zilizofanywa na wizara na baadae watafanya uhakiki wa kinachoendelea kujengwa hapa na kujua thamani halisi inayotakiwa na kwanini mradi huu upitishwe hadi kusainiwa”alihoji Waziri Mpina.
Meneja wa Mradi wa Swiofish, Flora Luhanga alisema mradi huo wa ujenzi wa Jengo la Maabara ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi ulianza Juni 10, 2019 kwa gharama ya shilingi bilioni 2, 609,491,754 unajengwa na Mkandarasi Kampuni ya Petra Construction Limited na kusimamiwa na Kampuni ya YP Architect.
Luhanga alisema mradi huo unajumuisha  pia ujenzi wa uzio, ofisi ya walinzi, kuchimba kisima cha maji, ujenzi wa tenki la maji ya mvua na kujenga mnara wa maji.
Mkandarasi wa Mradi huo, Nicholaus Mlayi alisema hadi sasa ujenzi wa mradi huo umefikia asilimia 70 na tayari ameshalipwa shilingi milioni 963 na unatarajia kukamilika mwezi Aprili.
Mwakilishi wa Katibu Mkuu Uvuvi, Magese Bulayi alimhakikishia Waziri Mpina kuwa maagizo yote aliyoyatoa atayasimamia kikamilifu hasa katika kuangalia thamani ya fedha ‘value for money’ katika mradi huo na kwamba hatua stahiki zitachukuliwa kwa wote watakaobainika kuhusika katika mchakato huo.

MAUAJI YA MTOTO WA MIAKA 13 KIAMAIKO.


Kiongozi wa mashtaka ya umma Noordin Haji ameagiza uchunguzi wa kisa cha mauaji ya kijana mmoja wa miaka 13 anayedaiwa kupigwa risasi na maafisa wa polisi katika eneo la Kiamaiko hapa Nairobi jana usiku.

Kijana huyu anasemekana kuwa kwenye roshani ya nyumba yao akitazama yaliyokuwa yakiendelea. Kwa sasa kijana huyo anatazamiwa kuzikwa katika maziara ya Kariako hapa Nairobi.

KOFFI OLOMIDE ATOA WIMBO KUHUSU UGONJWA WA CORONA.



Koffi Olomide - Coronavirus Assassin (Clip Officiel)

HHALIMA MDEE ATAKA WABUNGE WOTE WAPIMWE CORONA.


Mbunge wa Kawe Halima Mdee amependekeza wabunge wote wapimwe CoronaVirus ili wale watakaobainika kuwa na maambukizi ya Corona wakawekwe karantini, na wale ambao hawana maambukii waendelee kufanya kazi bungeni.

Amezungumza hayo alipopata nafasi ya kuuliza swali kwaajili ya ufafanuzi baada ya taarifa iliyotolewa na Spika wa bunge, Job Ndugai juu ya utaratibu mpya wa vikao vya bunge utakavyokuwa ili kukinga maambukizi ya virusi vya covid 19 kwa wabunge.

“Leo wabunge wapo kwenye vyumba (utaratibu mpya wanaoingia bungeni ni 150 kati ya wabunge zaidi ya 300) kwanini tusianze na sisi tupimwe wote tukijijua tupo salama tukae hapa tu ‘debate’, hili ndio bunge la mwisho mh. kuelekea uchaguzi mkuu” Amesema Mdee.

Aidha Spika Ndugai amesema kuwa wazo hilo ni zuri na litafikiriwa jinsi ya kulifanyia kazi, huku awali wakati akitoa taarifa yake amesema wabunge ambao hawatapata nafasi ya kuingia bungeni watafuatilia shughuli za bunge kupitia runinga katika kumbi na maeneo mengine yaliyopangwa.

Sambamba na hayo Ndugai amesema tahadhari zinazoendelea kuchukuliwa katika nchi yetu kukinga maambukizi ya virusi vya Covid 19 hatizaweza kuendana moja kwa moja na zile za nchi nyingize zilizoendelea kwani watanzania wana mfumo tofauti wa maisha.

NDUGU WATHIBITISHA CORONA ILIVYOONDOA UHAI WA IDDY MBITA.

Ibrahim Mbita amesema mdogo wake, Iddy amefariki kwa ugonjwa wa corona leo Jumanne Machi 31, 2020 katika kituo cha matibabu ya wanaougua ugonjwa huo kilichopo Hospitali ya Mloganzila, Dar es Salaam.

"Familia ya Marehemu Alhaj Brigedia Generali Hashim Mbita kwa huzuni kubwa inasikitika kuarifu msiba wa mdogo wetu mpendwa IDDI HASHIM MBITA uliotokea usiku wa kuamkia leo hospitalini Mloganzila.

Kutokana na tatizo lililopelekea kifo chake, CORONA, serikali itamzika mpendwa wetu leo mchana. Wawakilishi wachache sana wa familia wataruhusiwa kuhudhuria mazishi. Hakutakuwa na msiba wala matanga ya pamoja kuepuka kueneza maambukizi. Kila mtu aomboleze kwake.
Dua nyingi tumuombee Iddi Allah amuweke pema peponi. Amina."

Leo taarifa iliyotolewa na Waziri wa Afya wa Tanzania, Ummy Mwalimu imethibitisha kifo hicho na kubainisha kuwa alikuwa akipatiwa matibabu katika kituo hicho.

"Marehemu ni Mtanzania mwanaume mwenye umri wa miaka 49 ambaye pia alikuwa akisumbuliwa na maradhi mengine."