ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, February 25, 2026

SIMBA YAKWAA KISIKI DODOMA

 


TIMU ya Simba SC imetoa sare ya bila kufungana na wenyeji, Dodoma Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

Kwa matokeo hayo, Simba SC inafikisha pointi 23 katika mchezo wa 10 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya tatu, wakati Dodoma Jiji FC inafikisha pointi 21 katika mchezo wa 16, ingawa inabaki nafasi ya sita. 

YANGA YATUMA SALAMU KWA 'KUIGAGADUA' JKT GOLI TANO MTUNGI

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya JKT Tanzania katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na beki Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ dakika ya saba, mshambuliaji Muangola Laurindo Dilson Maria Aurelio ‘Depu’ dakika ya 60, kiungo Mudathir Yahya Abbas dakika ya 63, mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Mpumelelo Dube dakika ya 84 na kiungo Shekhan Ibrahim Khamis dakika ya 89.

Kwa ushindi huo, Yanga wanafikisha pointi 28 katika mchezo wa 10 na kupanda kileleni ikiizidi tu wastani wa mabao JKT Tanzania, ambayo pia imecheza mechi saba zaidi. 

Mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo Dube ndiye Mchezaji Bora wa Mechi leo

STAMICO, PLANTCOR WASAINI UBIA UTAFITI NA UCHIMBAJI MADINI BUKOMBE

 NA ALBERT G.SENGO/BUKOMBE/GEITA

Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imeingia makubaliano ya ushirikiano na kampuni ya uchimbaji madini ya Plantcor ya Afrika Kusini kwa lengo la kufanya utafiti na baadaye uchimbaji wa madini katika Pori na Hifadhi ya Msitu wa Kigosi, wilayani Bukombe mkoani Geita. Makubaliano hayo yamesainiwa Jumanne, Februari 24, 2026 katika Ukumbi wa CCM Bukombe, hafla iliyohudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa kama mgeni rasmi. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Kiruswa amesisitiza umuhimu wa mwekezaji kuhakikisha kuwa zoezi la utafiti, litakalotumia teknolojia ya kisasa ya ndege nyuki (drones) kabla ya kuanza rasmi uchimbaji wa dhahabu, linafanyika kwa uwazi na kwa kutoa taarifa sahihi kwa wananchi ili waweze kushirikishwa na kunufaika na matokeo ya utafiti huo. Aidha, amemtaka mwekezaji huyo kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya eneo husika, hususan barabara, kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), ili kurahisisha upatikanaji wa maeneo ya uchimbaji kwa wachimbaji wadogo. Ameeleza kuwa hali ya miundombinu ilivyo sasa hairidhishi na inahitaji maboresho ya haraka. Mradi huo unatarajiwa kuwa chachu ya uchumi katika wilaya hiyo kupitia kodi za mirabaha, uboreshaji wa miundombinu na huduma za kijamii kwa wananchi pamoja na ajira za muda mfupi na mrefu zipatazo 2,000.