ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Sunday, April 26, 2026

YANGA WATINGA FAINALI, MACHO SASA KWA DABI NZITO INAYOFUATA?

 


Mabingwa watetezi, Young Africans SC wamefanikiwa kutinga Fainali ya Kombe la Muungano 2026 baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC katika mchezo wa nusu fainali uliopigwa usiku wa Jumamosi, Aprili 25, 2026 kwenye dimba la New Amaan Complex, Zanzibar.

Yanga walionyesha dhamira mapema baada ya mshambuliaji wao raia wa Zimbabwe, Prince Mpumelelo Dube kufungua ukurasa wa mabao dakika ya 9 akiitungua timu yake ya zamani. Kiungo mahiri raia wa DR Congo, Maxi Mpia Nzengeli akaongeza bao la pili dakika ya 25, akiipa Yanga utulivu wa mchezo.

Kwa upande wa Azam FC, kiungo mshambuliaji Feisal Salum Abdallah alifunga bao la kufutia machozi dakika ya 78, naye akiiumiza klabu yake ya zamani, lakini halikutosha kuizuia Yanga kusonga mbele.

Sasa Yanga wanasubiri kumjua mpinzani wao wa fainali atakayepatikana katika mchezo wa nusu fainali ya pili kati ya Simba SC na Mlandege FC utakaopigwa leo kuanzia saa 2:15 usiku, uwanja huo huo wa Amaan.

Fainali ya Kombe la Muungano 2026 imepangwa kupigwa Jumatano, Aprili 29, saa 2:15 usiku katika Uwanja wa Amaan .

Hata hivyo, macho ya mashabiki wengi tayari yanaelekezwa mbele zaidi kwani siku tatu tu baada ya fainali hiyo, kunatarajiwa kuchezwa dabi kubwa ya watani wa jadi, Simba SC dhidi ya Young Africans SC mchezo unaotarajiwa kuwa na presha, ushindani mkali, na huenda ukaathiriwa moja kwa moja na matokeo ya fainali ya Muungano.

'LEO WANAUME WA MWANZA MMEFIKIWA' KARIBU KIKAONI

 NA ALBERT G.SENGO/MWANZA

Jumapili hii, yaani LEO - tarehe 26 Aprili 2026, jiji la Mwanza linakuwa kitovu cha mjadala muhimu unaomhusu mwanaume wa kizazi cha sasa. Ndani ya Ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT – Capri Point), tukio maalum la Mwanza Wanaume Summit 2026 linafanyika, likiwaleta pamoja wanaume kutoka pande mbalimbali za Kanda ya Ziwa na kwingineko. Kuanzia saa 8 mchana hadi saa 12 jioni, washiriki watapata fursa ya kipekee ya kujifunza, kuhamasishana na kujenga mtazamo mpya unaoendana na changamoto na fursa za maisha ya leo kuanzia majukumu ya kifamilia hadi mchango wao katika jamii na taifa. Katika mazungumzo haya yenye uzito, Maxwell Stanslaus Shing’oma, Rais wa Taasisi ya Wanaume Tanzania (Men At Work Global), anafungua pazia kwa kueleza kwa kina dhamira ya kongamano hili na kwa nini ni muhimu kwa maendeleo ya mwanaume wa kizazi hiki.......