ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, July 27, 2024

UVCCM KIBAHA MJI YAUNGANA NA DAS KIBAHA KUTAMBULISHA CLUB YA JOGGING

 


NA VICTOR MASANGU, KIBAHA

 
Ofisi ya Wilaya ya Kibaha kwa kushirikiana na Umoja wa vijana (UVCCM)  Kibaha mjini katika kutekeleza agizo la serikali la kufanya  usafi wa mazingira ifikapo kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi  imeamua kutambulisha rasmi  Club ya Jogging pamoja na  kufanya  mazoezi kwa ajili ya kujenga afya zao na ili kuweza kujikinga na kuepukana na magonjwa yasiyoambukiza.

Utambulisho huo wa Jogging inayotambulika kwa jina la Kibaha Fitness Club umekwenda sambamba na zoezi la ufanyaji wa  usafi katika kituo cha afya Mkoani kilichopo Wilaya ya Kibaha pamoja na uchangiaji wa damu kwa ajili ya kuweza kuwasaidia wagonjwa mbali mbali wenye uhitaji hususan wakinamama wajawazito.


Akizungumza  kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Katibu Tawala wa Wilaya ya Kibaha  Moses Magogwa amesema kwamba wameamua kuungana na  vijana wa UVCCM  kufanya usafi wa mazingira ikiwa ikiwa ni moja ya utekelezaji wa agizo la serikali la kufanya usafi ifikapo kila jumamosi ya mwisho wa mwezi.

"Sisi kama serikali ya Wilaya ya Kibaha tumeamua kushirikiana na vijana wetu wa UVCCM, katika kufanya utambulisho wa Club ya Jogging ambayo pia imeambatana na suala la usafi wa mazingira na nipo hapa kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kibaha na kwamba tumeweza kusafisha maeneo mbali mbali ya kituo cha afya Mkoani pamoja na uchangiaji wa damu,"alisema.

Aidha Katibu Tawala huyo aliwapongeza kwa dhati vijana hao wa UVCCM Wilaya ya Kibaha mji kwa maamuzi yao kwa kujitokeza kwa wingi katika zoezi la uchangiaji wa wa damu,kufanya usafi wa mazingira pamoja na kuweza kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali katika wodi ya wazazi katika kituo hicho cha afya Mkoani.
Katika hatua nyingine Katibu huyo alibaisha kwamba lengo lao kubwa kama Wilaya ya Kibaha ni kuendelea kutekeleza kwa hali na mali agizo la serikali katika kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ikiwa pamoja na kuanzisha Club za Jogging ambazo zitaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa  kupunguza magonjwa yasiyoambukiza.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa umoja wa vijana  (UVCCM) Wilaya ya Kibaha mjini Ramadhani Kazembe amesema kwamba  wao kama vijana wameungana na Ofisi ya Wilaya ya Kibaha  na kufanya mazoezi ya pamoja ambayo pia yameambatana na uchangiaji wa damu, pamoja na kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali katika wodi ya wazazi.

"Tumeamua kuungana na ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kibaha katika kuunga mkono juhudi za serikali katika jambo zima la usafi wa mazingira na tumefanya mazoezi ambayo pia yameambatana na uchangiaji wa damu ikiwa sambamba na utoaji wa mahitaji mbali mbali ambayo yatawasaidia wakinamama wajawazito,"alisema Kazembe.

Kadhalika Kazembe alimpongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji ya viwanda ikiwa pamoja na kuboresha miundombinu ya barabara, maji,pamoja na huduma ya afya.

Naye Mganga mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha mjini Catherine Saguti  ameishukuru Ofisi ya Mkuu wa Wilaya pamoja na vijana wa UVCCM kwa kwenda kutoa msaada wa kuchangia damu na kuwatembelewa wakinamama waliojifungua na kuwapatia mahitaji mbali mbali ikiwemo sabuni za kufulia.

Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kibaha kwa kushirikiana na umoja wa vijana (UVCCM) Wilaya ya Kibaha mjini imeweza kutambulisha Club ya Jogging na kufanya mazoezi ambayo yamekwenda sambamba na uchangiaji wa damu, kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali ikiwa sambamba na kufanya usafi wa mazingira katika katika kituo cha afya.

Tuesday, July 23, 2024

VIJANA WAKUMBUSHWA KUJIKITA KATIKA MIDAHALO KUONGEZA UELEWA WA MAISHA.

 


NA VICTOR MASANGU

Vijana wametakiwa kushiriki  katika midahalo mbalimbali itakayowawezesha kuwa na mawazo chanya juu ya mustakabali wa maisha yao.

Hayo yamesemwa na Mwanzilishi wa jukwaa la Power of Sentence ambalo ni jukwaa la uwezeshaji kwa vijana kupitia simulizi za maneno ambapo, jukwaa hilo linatoa nafasi kwa vijana kupata nafasi ya kutambua athari za maneno zinavyoweza kuathiri maamuzi yako na zingine zinazoweza kuwajenga kifikra.

Mwanzilishi wa jukwaa la Power Of Sentence, Jackline Christopher amesema jukwaa hili limewakutanisha vijana mbalimbali na kufanya midahalo juu ya maneno yanavyoweza kuathiri maamuzi yao.

Jackline amesema, huu ni mwaka wa tano toka kuanzishwa kwa jukwaa hilo na limewawezesha vijana wengi kufikia malengo yao baada ya kuweka wazi hisia na fikra zilizopo ndani ya mawazo baada ya kuyawasilisha mbele ya jamii.

“Hii powe of sentence ni namna ambayo mtu anaweza kutumia maneno yake kuweza kumletea mafanikio na muda mwingine yanaweza yakaathiri maisha yake kwa namna moja ama nyingine,” amesema Jackline.

“Unaweza kuwa na mawazo yakawa ni mazuri au mabaya kulingana na utakavyochukulia, zaidi unapokuwa na mawazo usiyaache kuyatumia na kuyaishi kwa sababu maneno hayo yanayopita ndani ya kichwa chako yanaweza kukujenga zaidi na kufikia malengo yako,” amesema


Akizungumzia msimu wa tano wa jukwaa hilo linalotarajia kufanyika Julai 27, mwaka huu Jackline amewaomba vijana wajitokeze kwa wingi kwa kununua tiketi kwani dhamira ya jukwaa hilo ni kuona linafika mbali zaidi katika mikoa mingine ikiwemo Kigoma.

Jackline ni mwandishi wa vitabu mbalimbali ambapo tayari ameshazindua kitabu chake cha 100 Power of Sentence na Amnesia ambavyo vyote kwa sasa vinapatikana.

RC KUNENGE AKABIDHI MAGARI MAPYA YA SERIKALI KWA DC KISARAWE NA BAGAMOYO

 


NA VICTOR MASANGU,PWANI 


Mkuu wa mkoa wa Pwani Alhaji  Abubakari Kunenge amekabidhi Magari mawili mapya  kwa wakuu wa Wilaya za Kisarawe na Bagamoyo ambayo yataweza  kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika utekelezaji wa kuwahudumia wananchi wao kwa urahisi zaidi.

Akikabidhi Magari hayo kwa wakuu hao wa Wilaya Mkuu huyo wa mkoa wa Pwani amemshukuru kwa dhati  Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa Magari hayo yatakayokuwa ni mkombozi mkubwa katika suala zima la usafiiri kwa wakuu hao wa Wilaya.


Kunenge alisema kupatikana kwa magari hayo mapya kutaweza ni juhudi kubwa ambazo amezifanya Rais wa awamu ya sita Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha anaboresha mazingira ya kazi kwa wakuu wake wa Wilaya.

Alisema katika Mkoa wa Pwani kuna jumla ya Wilaya sana na kwamba Rais kwa awamu hii ameshatoa magari mapya  matatu ambayo mawili yamekabidhiwa leo rasmi na mengine yatakabidhiwa katika awamu nyingine.


Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Petro Magoti amempongeza kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa  kuwapatia magari hayo ambayo yatakwenda kuwa msaada mkubwa.

Magoti alisema kwamba hapo awali alikuwa anatekeleza majukumu yake kwa kutumia gari nyingine lakini kwa sasa anashukuru kupata gari jipya ambalo litamuwezesha kuwafikia wananchi kwa urahisi zaidi.

"Kwa kweli napenda kumshukuru kwa dhati Mkuu wa Mkoa wa Pwani pamoja na Rais wangu Dkt.Samis Suluhu Hassan kwa kuweza kutupatia magari haya ambayo kwa kweli mm nilikuwa naenda vijijini kwa usafiri wa gari aina ya Pick up,:alisema Magoti.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo  Halima Okash   hakusita kumpongeza Mkuu wa Mkos wa Pwani kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na  Rais Samia  kuwapatia magari mapya kwa ajili ya kurahisisha usafiri na utekelezaji wa majukumu yao ya kuwatumikia wananchi.

Monday, July 22, 2024

NHC YATUMIA ZAIDI YA MILIONI 300 KUBORESHA MAJENGO YAO TANGA

 


Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkoani Tanga Mhandisi Mussa Kamendu

Na Oscar Assenga, TANGA

SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) katika kipindi cha mwaka wa fedha uliopita 2023/2024 wametumia zaidi ya Milioni 300 kwa ajili ya matengenezo makubwa ya majengo yao katika Jiji la Tanga.

Hayo yalibainishwa leo na Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkoani Tanga Mhandisi Mussa Kamendu wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema kwamba matengenezo hayo yatahusisha nyumba za Ngamiani, Nguvumali, Bombo mpaka Raskazone.

Mhandisi Kamendu alisema kwamba shirika hilo limefanya mkakati huo maalumu makusudi kuhakikisha majengo yao yanaboreshwa na kuwa na muonekano mzuri ikiwemo kupakwa rangi ili wapangaji wao waishi kwenye mazingira mazuri.

“Katika miji yote ya Tanzania Shirika hilo linamiliki nyumba katikati ya Miji na Majiji kwa hiyo nyumba zinapokuwa kwenye hali mbaya zinafanya miji ionekane vibaya na taswira ya majiji inakuwa haipo vizuri kwa kuliona hilo shirika limekuja na mkakati maalumu wa kuzipaka rangi ili ziweze kuwa na muonekano mzuri na kubadilisha mifumo ya maji taka na maji safi “Alisema

Aidha allisema pia katika matengenezo hayo wamebadilisha pia mifumo ya umeme ambayo imechakaa na kurekebisha miundombinu mbalimbali mingine ikiwemo milango na madirisha ili kuhakikisha wanapangaji wanakuwa kwenye mazingira mazuri.

Katika hatua nyengine Meneja huyo aliwataka wapangaji wao kuhakikisha wanabadilika na kufuata mikataba yao inavyowataka walipe kodi kwa wakati ili waweze kuepukana na usumbufu wanataokumbana nao.

Mhandisi Kamendu alisema kwamba mikataba yao inawataka wapangaji wao kuhakikisha wanalipa kodi kwa wakati na pia waweze kuepukana usumbufu watakaoupata maana pale ambao hawajalipa kodi kufuatia na mikataba yao itafikia wakati watatolewa kwenye nyumba hizo.

“Wapangaji wasumbufu ambao wanasubiri mpaka kufuatwa na madadali kwenye kwenye nyumba sasa wanapotelewa kwenye nyumba ni usumbufu na aibu kwa familia na jamii inaweza kuona ni mtu wa ajabu tusisburi mpaka kufukia hatua hii”Alisema

Katika hatua nyengine Meneja huyo alisema kwamba shirika hilo limejiwekea malengo la kukusanya Sh. Bilioni 2,444,183,556.96 katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2024/2025 kutokana na makusanyo yao ya Pango la Kodi kutoka katika nyumba zao.

Alisema kwamba hayo ndio malengo yao na mwaka huu wa fedha kwa sababu hiyo kama mkoa wanaendelela kuboresha huduma zao.

Alisema kwamba wanafanya hivyo kama shirika ili kuhakikisha wapangaji wanakuwa kwenye mazingira mazuri na kuwa sawa ili kodi zao wanazolipa ziendane na thamani ya mahali wanapoishi.

Maneja huyo alisema kwamba malengo yao ya Bajeti katika Mwaka wa Fedha wa 2023/2024 waliweza kukusanya kiasi cha Bilioni 2,040,727,435 kutokana na kodi ya pango kutoka kwa wapangaji wao walioishi kwenye nyumba za shirika hilo.

Alisema katika mwaka wa fedha kuanzia Julai 2023 mpaka June 2024 waliweza kukusanya kiasi cha Bilioni 2,040,727,435 na malengo waliokuwa wamejiwekea kwenye bajeti yao ya mwaka 2023/2024 ilikuwa ni kukusanya kodi Bilioni 2,046 ,528,000 .

“Kwa hiyo utaona ukiangalia kiasi tulichokusanya wao Biloni 2,040,727,435 tumekusanya kwa asilimia 99.7 ya malengo ya bajeti yetu ya mwaka 2023/2024 kwa hiyo katika majengo yetu na idadi ya wapangaji wao na kodi tunavyokusanya kwa ufupi tumefikia malengo ya kwa sababu asilimia 99.7 ni sawa asilimia 100 kiasi cha 5,856,400 ndio ambacho hakijaweza kukusanywa”Alisema

Aidha alisema na hivyo inatokana na madeni ya wapangaji wao ambao wanadaiwa na ni wajibu wao kuendelea kuyadai na kuchukua nafasi hiyo kuwapongeza wapangaji ambao wanalipa vizuri huku wakiendelea kuwasisitizia kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi.

Sunday, July 21, 2024

UWT KIBAHA MJINI YATEMA CHECHE KWA KATA YA MBWAWA NA MSANGANI JUU YA KUWALINDA WATOTO.


 NA VICTOR MASANGU,KIBAHA 


Mwenyekiti wa Umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha Elina Mgonja amewahimiza wazazi na walezi kuhakikisha wanaungana kwa pamoja katika kukabiliana na wimbi la vitendo vya utekaji wa watoto.

Mgonja ameyasema hayo wakati akizungumza na wanawake wa UWT katika kata za Mbwawa na Msangani wakati wa ziara yake ya kikazi ya kuangalia uhai wa chama pamoja na kuhimiza wanawake kuchukua fomu za kugombea nafasi za uongozi.

Mwenyekiti huyo alisema kwamba kumekuwepo na matukio mbali mbali ya baadhi ya watoto kufanyiwa vitendo vya kutekwa na wengine kufanyiwa vitendo vya kulawitiwa.


"Wanawake,wazazi pamoja na walezi mnapaswa kuhakikisha kwamba mnawalinda na kuwatunza watoto wao kwani kuna wimbi kubwa la utekaji kwa watoto kwa hivyo inabidi tuwe makini sana,"alisema Mgonja.

Aidha aliwahimiza wanawake kuhakikisha kwamba wanaungana kwa pamoja katika kujitokeza kwa wingi kuchukua fomu kwa ajili ya kugombea katika uchaguzi wa serikali za mitaa ambao unatarajiwa kufanyika mwaka huu.

Kadhalika aliwakumbusha wanawake kuweka utaratibu wa kuwachunguza kwa kina watoto wao ili kuweza kubaini kama wamefanyiwa vitendo mbali mbali vya ukatili ikiwemo kulawitiwa.


 Kwa upande wake mjumbe wa kamati ya utekelezaji ya UWT Kibaha mjini Dkt.Zainabu Gama amewataka wanawake kutokuwa waoga kabisa na kuchukua maamuzi ya kuwa Jasiri.

Naye Diwani wa viti maalumu wa Halmashauri ya mji Kibaha Lidia Mgaya amewaomba wanawake kuwa na umoja na upendo na kuwa mstari wa mbele hasa katika kipindi cha kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa.

Ziara ya Mwenyekiti wa umoja wa wanawake (UWT)  Wilaya ya Kibaha mjini imelenga kupita katika kata zote za 14 kwa lengo la kuwahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi katika kugombea nafasi za uongozi.