ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, March 23, 2019

MATAIFA YAVUTIWA NA MRADI MWANZA

 Ugeni kutoka Brazili, Afrika Kusini, Kenya na Uganda ukiwa katika moja ya eneo lenye mradi wa majitaka wa simplified sewerage Jijini Mwanza. Huu ni ugeni wa pili kutoka nje ya Tanzania uliyotembelea mradi huo kwa Mwaka huu 2019.


Mradi wa majitaka Mwanza wavutia wageni kutoka nchi mbalimbali ulimwenguni. 

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jijini Mwanza (MWAUWASA) imepokea ugeni kutoka Asasi zisizo za Kiserikali kutoka Brazil, Afrika Kusini, Kenya na Uganda ambao umevutiwa na ubunifu uliyotumika katika ujenzi wa mradi wa Mfumo rahisi wa uondoshaji majitaka kwenye maeneo ya milimani unaofahamika kitaalam kama 'Simplified Sewerage System'.

Hayo yamebainishwa Machi 22, 2019 na Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali linalojishughulisha na masuala ya Kijamii nchini (CCI) Dkt. Tim Ndezi ambaye alikuwa mwenyeji wa ugeni huo kwa hapa nchini.

Dkt. Ndezi alisema mradi wa majitaka wa simplified sewerage umeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa mataifa mbalimbali kote ulimwenguni.

Alisema taasisi zinazojishugulisha na masuala ya usafi wa mazingira kutoka nchi mbalimbali baada ya kupata sifa za mradi huo wa Mwanza zimevutika kujifunza zaidi ubunifu uliotumika katika utekelezaji wake ili pia kuutumia katika nchi wanazotoka. 

"Wageni hawa wamekuja kujifunza namna ambavyo mradi huu umejengwa ili nao wakaandae mradi wa namna hii kwenye nchi zao," alisema Dkt. Ndezi.

Mradi huo wa Simplified Sewerage umeendelea kutembelewa na wageni kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kujifunza namna ukivyotekelezwa na namna ambavyo unaendeshwa.

Kwa mujibu wa Dkt. Ndezi ni kwamna ugeni huo vilevile ulilenga kuzungumza na wanufaika wa mradi huo ili kufahamu wajibu wao na namna ambavyo waliupokea na njia wanazotumia kuutunza. 

Hii ni mara ya pili kwa mwaka huu 2019 mradi huo kutembelewa na ugeni kutoka nje ya nchi kwani hivi karibuni MWAUWASA ilipokea ugeni kutoka Kenya ambao ulifika kwa ajili ya kujifunza namna bora ya kutekeleza mradi wa majitaka hususan kwa maeneo yasiyo rasmi. 

Ugeni huo wa awali kutoka Nchini Kenya ulieleza namna ulivyovutiwa na ubunifu mkubwa uliyotumika katika ujenzi wa mradi wa majitaka kwenye maeneo ya milimani na kuahidi kurejea tena na wataalam wa mamlaka zinazohusika ili kujenga miradi ya namna hiyo nchini mwao. 

Akizungumza mmoja ya wageni hao kutoka Uganda, Mundamba Omar alisema nchini humo ipo changamoto ya wananchi hususan wa kipato duni kukosa mfumo bora na rasmi wa uondoaji wa majitaka na kwamba ziara hiyo waliyoifanya Jijini Mwanza imewapatia uzoefu na ujuzi wa namna ya kujenga na kusimamia mradi mzuri wa majitaka. 

"Tunaipongeza MWAUWASA, kazi iliyofanyika hapa ni ya kipekee hatuna budi nasi kuiga," alisema Omar. 
Itakumbukwa kuwa Mradi huo wa Simplified Sewerage ulikuwa miongoni mwa miradi miwili bora zaidi kuwahi kutekelezwa Barani Afrika chini ya ufadhili wa African Infrastructure Trust Fund (EU-AITF).

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendeji wa MWAUWASA, Mhandisi Anthony Sanga ujenzi wa mradi huo ulianza Mwaka 2016 na umenufaisha Kaya zipatazo 415.

Mhandisi Sanga alisema mradi huo wa Simplified Sewerage ulijengwa kwa majaribio kwenye maeneo matatu ambayo ni Kilimahewa, Mabatini na Igogo. 

Katika maeneo hayo matatu, Mhandisi Sanga alisema mwitikio ulikua mzuri na alitolea mfano kwa Kilimahewa ambapo MWAUWASA ilipanga kuunganisha Kaya 68 lakini kutokana na mwitikio kuwa mkubwa Kaya 117 ziliunganishwa na kwa upande wa Mabatini mpango ulikua ni kuungnisha Kaya 88 hata hivyo zaidi ya Kaya 178 ziliunganishwa na kufikia jumla ya Kaya 415 kwenye maeneo yote matatu.

Hata hivyo Mhandisi Sanga anabainisha kwamba awamu ya pili ya ujenzi wa mradi huo itahusisha maeneo mengi zidi ambayo ni Kabuhoro, Ibungilo, Kawekamo na Isamilo. 

"Maeneo ambayo tulianza nayo kwenye awamu ya kwanza nayo hatujamaliza, kwahiyo haya ni maeneo mapya lakini pia tutarudi kwenye hayo maeneo ya awali tukaunganishe Kaya zilizosalia," alibainisha Mhandisi Sanga. 

Akielezea sababu za mradi huo kuitwa simplified, Mhandisi Sanga alisema kwamba mradi ulipunguza baadhi ya vigezo kwenye miongozo ya usanifu miradi kutoka Wizara ya Maji. 

"Ukivifuata vigezo vyote kama vilivyo kwenye miongozo inakua ngumu kutekeleza mradi kwenye maeneo ya namna hiyo," alisema Mhandisi Sanga. 
Aliongeza kwamba changamoto iliyopo kwenye Jiji la Mwanza ni kwamba zaidi ya asilimia 70 ya maeneo hususan ya milimani hayajapimwa na hivyo kusababisha ujenzi wa miradi kuwa mgumu. 

Alibainisha kwamba kwa Tanzania, Jiji la Mwanza ni la kwanza kutekeleza miradi ya namna hiyo na kwamba kwa duniani miradi ya namna hiyo inapatikana Nchini Brazili. 

Mhandisi Sanga alisema lengo mahsusi la mradi huo ni kuondosha majitaka kwa njia rahisi kutoka kwenye maeneo ya milimani ili kuwaepusha wakazi na maradhi yanayoweza kutokea kutokana na mfumo usio rasmi wa uondoshaji wake. 

"Lazima tuhakikishe majitaka yanatolewa na yanatibiwa kwakuwa haya yanaweza kuwa ni hatari kwani mara nyingine hua ni chanzo kikuu cha maradhi," alisema. 

Alimalizia kwamba hapo awali uondoshaji wa majitaka kwenye maeneo ya milimani Jijini Mwanza ulionekana kuwa mgumu na kutowezekana." Ni lazima tuwe na majawabu kwenye maeneo ambayo hapo zamani ilionekana hayawezekani kabisa," alisema Mhandisi Sanga.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mbugani, Athumani Jama alisema hapo zamani kabla ya mradi hali ilikuwa ni chafu hasa ikizingatiwa hali halisi ya kijiografia ya maeneo hayo ya milimani. 

“Walikuwa wakichimba vyoo vifupi na wakati wa mvua hali inakuwa tete sana, maji yalikuwa yanatiririka ovyo na magonjwa ya mlipuko yalikuwa ya kufikia tu,” alisema Jama. 

Wananchi waliozungumza wakati wa ziara ya ugeni huo waliiomba MWAUWASA kuharakisha ujenzi wa mradi mpya ili Kaya nyingi zaidi zinufaike. 

Wafungwa Gereza Songwe Walima Ekari 750 za Mahindi

 Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni (kulia), akielekea kukagua mahindi yanayolimwa na wafungwa katika Gereza la Kilimo Songwe kwa ajili ya chakula cha wafungwa nchini. Kushoto ni Mkuu wa Gereza hilo, Mrakibu Mwandamizi, Peter Anatory. Ziara hiyo imefanyika leo jijini Mbeya. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni , akizungumza na Mkuu wa Gereza la Kilimo Songwe, Mrakibu Mwandamizi, Peter Anatory (kushoto) wakati wa ziara ya kukagua shamba katika gereza hilo  kwa ajili ya chakula cha wafungwa nchini. Ziara hiyo imefanyika leo jijini Mbeya. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Na Mwandishi Wetu
Jumla ya ekari 750 za mahindi zimelimwa katika Gereza la Kilimo Songwe ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais Dkt. John Magufuli la kutaka magereza yatumike kwa shughuli za uzalishaji ikiwemo kilimo kwa kutumia nguvu kazi ya wafungwa waliopo magerezani.
Akisoma taarifa mbele ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, Mkuu wa Gereza hilo ,Mrakibu Mwandamizi, Peter Anatory alisema kwa kutumia nguvu kazi ya wafungwa jumla ya ekari 750 za mahindi zimelimwa ikiwa ni kwa matumizi ya chakula kwa wafungwa ambapo wanatarajia kulisha na magereza mengine.
“Tunaendelea vizuri na kilimo na kama maelekezo ya Mheshimiwa Rais yalivyotufikia ni kweli tunatumia wafungwa ambao tumewapangia zamu katika shughuli hizi za kilimo,tunategemea kulisha magereza saba baada ya mavuno huku jumla ya ekari 750 zimelimwa mahindi hapa” alisema SSP Anatory
Pia aliitaka serikali kuwasaidia kutatua changamoto ya zana za kilimo ikiwepo matrekta ili kukamilisha ekari 250 zilizobaki ili kuweza kukamilisha ekari 1000 zilizopo katika gereza hilo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, alisema Gereza la Songwe ni moja kati ya magereza kumi nchini yaliyoteuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano kuendeleza kilimo cha mkakati lengo ni kuwezesha magereza yote nchini kuzalisha vyakula kwa ajili ya kulisha wafungwa na mazao yanayoweza kuwaletea kipato badala ya kutegemea ruzuku kutoka serikalini.
“Agizo la Rais Dkt.Magufuli ni kuona magereza yanajitosheleza kwa chakula kupitia wafungwa, nawapongeza kwa ekari mlizolima mahindi na kama wizara tunaahidi kulishughulikia suala la zana za kilimo ikiwemo matrekta, na gereza lenu ni moja kati ya magereza kumi ya kimkakati na mnaendelea vizuri” alisema Masauni
Mbali ya kilimo Gereza la Songwe pia linajishughulisha na ufugaji wa ng’ombe, mbuzi, kondoo, kuku, sungura  na  simbilisi.

"ENDELEA KUOTA SISI TUNAKUACHA"


Mkuu wa mkoa wa Mwanza John Mongella mwishoni mwa wiki (Ijumaa ya tarehe 22 Machi 2019) ameongoza kikao cha kamati ya ushauri cha mkoa (RCC) ambacho kimepitia na kushauri mpango wa rasmi ya bajeti ya halmashauri na manispaa za wilaya mbalimbali mkoani hapa kwa mwaka 2019/2020.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Makatibu Tawala,  Wakuu wa wilaya, Wenyeviti, Wakurugenzi pamoja na Wataalamu wa Sekretarieti ya mkoa, Viongozi wa vyama vya siasa, Wakuu wa idara, Maofisa tarafa, Watendaji wa Kata na Kamati ya Ulinzi na Usalama.

Aidha Wajumbe wakikao hicho wamepata nafasi ya kujadili kwa uwazi rasimu ya bajeti, wameshauri miradi viporo ya muda mrefu ipewe kipaumbele katika mwaka huu na ikamilike kwa wakati.

GsengoTv inakuletea sehemu ya majumuisho upande wa hitimisho ambapo msemaji wa kwanza anayeonekana katika video ni Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Salum Kali na msemaji wa pili ni Mwenyekiti wa kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella.

Taarifa ya ukusanyaji wa mapato ya ndani ya Mamlaka za Serikali za mitaa kwa kipindi cha mwaka 2018/2019 halmashauri za Mkoa wa Mwanza zilijiwekea malengo ya kukusanya jumla ya Ts. 35,086,833,000/= Hadi kufikia mwezi Februari, 2019 Jumla ya Tsh. 21,173,018,080/15 sawa na 60.34% ya lengo.

Makusanyo hayo yameongezeka kwa Tsh. 6,340,121,731/30 sawa na asiliamia 42.74 ukilinganisha na kipindi kama hiki kwa Mwaka 2017/18.

Moja ya Changamoto katika ukusanyaji wa mapato ni pamoja na Baadhi ya wakusanyaji kutumia fedha hizo kabla ya kuingia benki na kusababisha Halmashauri kushindwa kutambua mapato hayo.

Sababu nyingine inayotajwa ni baadhi ya mashine za kielektoniki (POS) zinazotumika kukusanya mapato kuzimwa (Off-line) kwa kisingizio cha kukosa 'bundle'. 

Hotuba ya ACT Wazalendo kwa Viongozi wa Wilaya, Mkoa wa Kusini Pemba


Ndugu zangu mliokuwa  viongozi wa matawi, kata, majimbo na wilaya wa wilaya ya Mkoani, ninapenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wananchi wa Pemba kwa kumuunga mkono Maalim Seif katika uamuzi alioufanya yeye na wenzake kujiunga na chama cha ACT Wazalendo.

Pemba ilikuwa ngome ya CUF chini ya uongozi wa Maalim Seif. Kwa hivyo, kitendo cha mliokuwa wanachama wa CUF nyote kwa umoja wenu kujiunga na jukwaa jipya la siasa la ACT Wazalendo kinaifanya Pemba sasa kuwa ngome ya ACT. Hili ni jambo kubwa sana kwa chama chetu.

Tumewapokea kwa moyo mkunjufu na mjihisi mmefika na mko nyumbani ndani ya ACT. Karibuni sana!

Kisiwa cha Pemba na wananchi wa Pemba mna historia kubwa sana katika mapambano ya kupigania haki, demokrasia na utu. Pemba imekuwa ALAMA ya mapambano ya kupigania haki na demokrasia kabla na baada ya mfumo wa vyama vingi.

Pemba mmekuwa Walimu na mmetufundisha Watanzania maana ya kuwa na Msimamo. Mmetufundisha maana ya ukweli katika kusimamia jambo mnaloliamini. Mmetufundisha maana ya kuwa utiifu kwa kiongozi mnayeamini anawakilisha na kusimamia kile mnachokiamini nyinyi.

Kwa sababu ya Msimamo wenu, ukweli wenu na utiifu wenu kwa mnaloliamini na kulipigania, mmepitia katika hilaki na mateso makubwa sana. Pengine katika Tanzania hakuna eneo ambalo limeshuhudia hayo zaidi ya Pemba. Tunakuhakikishieni kuwa kujitoa kwenu si kwa bure na siku haiko mbali kile mlichokipigania mtakipata Inshallah kupitia jukwaa hili la ACT.

Kuhusu suala la nafasi ya Zanzibar kwenye muungano, ninapenda kuwahakikishia kuwa Chama chetu kinaamini kuwa ili muungano wetu uwe wenye tija ni lazima kuwe na usawa baina ya pande zote mbili za muungano. Ndio maana katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya mwaka 2015, tuliweka bayana kuwa Chama chetu kinaamini katika Rasimu ya Tume ya Jaji Warioba ambayo ilishakamilisha wajibu wake wa kukusanya maoni ya wananchi kabla CCM na serikali yake haijayavuruga. Hivyo basi ninapenda kuwahakikishia Wazanzibar kuwa chama hiki kitakuwa jukwaa madhubuti la kuendeleza mapambano ya Wazanzibar katika kupigania muungano wa haki na usawa.

Pemba ina matatizo mengi lakini kubwa ni ugumu wa maisha kutokana na kisiwa hichi kufungwa kisiweze kufurukuta. Vijana hawana ajira na mzunguko wa pesa ni mdogo sana. Tumekuwa watu wa kungoja kusaidiana tu. Haya ni maumivu kwa jamii ya watu inayojitambua na kuwa na fakhari ya utu wao. Maisha kama haya yanatufanya tuwe dhalili na kuudhalilisha utu wetu. 
Pemba ni kisiwa chenye fursa nyingi na watu wabunifu tena wachapa kazi. Pemba inahitaji kufunguliwa kiuchumi kwa kuunganishwa na Unguja, Dar es Salaam, Tanga na Mombasa. Pemba inahitaji kuunganishwa na dunia kibiashara. Haya hayawezi kufanywa na CCM. Tunahitaji mabadiliko ili tupate Serikali inayothamini watu na kuziona fursa zilizopo Pemba na kuzifungua.

Tumekuja kukitambulisha Chama na kukupeni kadi za uanachama. Tutakuja tena kwa kazi ya kisiasa. Huku hamhitaji maelekezo. Nyinyi ndiyo walimu. Tutakuja tu kupeana hamasa ili kuhakikisha lengo lenu wananchi wa Zanzibar linafanikishwa.

Friday, March 22, 2019

"DAWA NI USHINDI TU KWA STARS, TUKIFUATILIA MATOKEO YA CAPE VERDE Vs TUTAPATA MAKENGEZA"



Taifa la Tanzania liko kwenye kampeni ya kusaka ushindi yaani pointi zote tatu za mchezo wa Jumapili dhidi ya Timu ya Taifa ya Uganda 'The Cranes' mchezo utakaopigwa Uwanja wa Taifa Jijini Dar es salaam, lakini wakati huo huo kusonga mbele kwa Stars, kunategemea matokeo ya upande wa pili,  mchezo wa Cape Verde dhidi ya Lesotho.

Mchambuzi wa michezo, mwanahabari ambaye pia kajikita zaidi katika soka Saleh Ally (Jembe) anasema Dawa yake Watanzania wajikite katika kuusaka ushindi tu kwa Stars kwani tukifuatilia matokeo ya Cape Verde tutapata makengeza...... Msikilize wakati akichonga kwa njia ya simu na Gsengo wa kipindi cha KAZI NA NGOMA ya Jembe Fm Mwanza.

CUF YATANGAZA KUJITOA UKAWA.


Katibu Mkuu mpya wa Chama Cha Wananchi CUF, Khalifa Suleiman Khalifa, amesema wao kama chama cha Wananchi wameshajitoa kwenye mwamvuli wa Umoja wa Katiba ya Wananchi 'UKAWA' kwa madai upo hoi na hauna msaada kwao
Khalifa amesema kwamba, msimamo wa CUF ni kutoshirikiana na UKAWA kwasababu wabunge wa CHADEMA na wafuasi wake wameshindwa kuwa na ushirikiano katika matatizo waliyokuwa nayo

Ameongeza kwamba kwa muda mrefu Wabunge wa CHADEMA wamekuwa wasemaji waliokuwa wakimuunga mkono, aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho Maalim Seif Sharif

Umoja wa Katiba ya Wananchi, (UKAWA) uliundwa na vyama vya NCCR-Mageuzi, NLD, CUF na CHADEMA ambapo baadaye waliungana katika uchaguzi mkuu wa 2015

Thursday, March 21, 2019

SIMBA USO KWA USO NA TP MAZEMBE :ROBO FAINALI KLABU BINGWA AFRIKA

Droo ya Total CAF Confederation Cup

Nkana (Zambia) vs CS Sfaxien (Tunisia)
Etoile du Sahel (Tunisia) vs El Hilal (Sudan)
Hassania Agadir (morocco) vs Zamalek (Egypt)
Gor Mahia (Kenya) vs RS Berkane (Morocco)
CS Constantine (Algeria) vs Esperance (Tunisia)
Mamelodi Sundowns (South Africa) vs Al Ahly (Egypt)
Horoya (Guinea) vs Wydad Athletic Club (Morocco)
Simba (Tanzania) vs TP Mazembe (DR Congo)

WANAFUNZI WALIOCHORA PICHA YA KUMDHIHAKI RAIS WA BURUNDI WASHITAKIWA.

Wanafunzi waliochora picha ya kumdhihaki Rais wa Burundi washitakiwa

Wanafunzi watatu wa kike wamefunguliwa mashitaka ya kumdhihaki Rais wa Burundi Pierre Nkurunziza, na huenda wakahukumiwa kifungo cha hadi miaka mitano jela.
Msemaji wa Mahakama ya Juu ya Burundi, Agnès Bangiricenge amesema leo Alkhamisi kuwa, wanafunzi hao wameshitakiwa kwa kumdhalilisha rais wa nchi, kwa kuchora picha yake na kisha kuichafua kwa kuipaka rangi.
Wanafunzi hao walikamatwa juma lililopita kwa kosa la kuchora na kupaka rangi picha ya Rais Nkurunziza katika vitabu vyao vya shule, kitendo ambacho vyombo vya mahakama vinasema ni kuidhihaki na kuidhalilisha shakhsia ya rais, ambaye ni nembo ya umoja wa kitaifa.
Shirika la kutetea haki za kibinadamu la Human Rights Watch (HRW) limesema wanafunzi saba walikamatwa wakihusishwa na kitendo hicho, lakini wanne wakaachiwa huru.

Burundi imekuwa ikituhumiwa na UN kuwa inakiuka haki za binadamu

David Ninganza, mtetezi wa haki za watoto nchini humo amesema ingawaje ni kinyume cha sheria kumvunjia heshima kiongozi wa nchi kwa namna yoyote ile, lakini kwa kuwa kosa hilo (la kuchora na kupaka rangi picha ya rais) limefanywa na wanafunzi, hawakupaswa kufunguliwa mashitaka kwa kuwa kitendo hicho hakikuwa cha kisiasa.
Mwaka 2016, watoto 11 walifungwa jela kwa tuhuma za kuchora vibonzo vya kumdhalilisha Rais Nkurunziza katika vitabu vyao vya shule. Mwaka huohuo, wanafunzi wengine 300 walifukuzwa shule baada ya kuchora picha za kumdhihaki rais.

WADAU WA UWEKEZAJI SEKTA YA UTALII TANZANIA SASA WAJA NA MKAKATI HUU KUINUA UTALII KANDA YA ZIWA.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Profesa. Adolf Mkenda, ameongoza timu ya wawekezaji kutembelea Mapori ya Akiba ya Biharamuro, Burigi na Kimisi, kuangalia fursa za uwekezaji katika sekta ya Utalii ikiwa ni mkakati wa kuongeza pato la Utalii nchini. 

Wednesday, March 20, 2019

HUDSON KAMOGA AZUNGUMZIA UMUHIMU WA MAAFISA UHUSIANO WA SERIKALI KUPIGWA MSASA


Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Hudson Kamoga amefunguka umuhimu wa Maafisa Mawasiliano wa Taasisi mbalimbali nchini kushiriki Kazi Darasa kupitia kikao cha wadau hao kinachoendelea katika ukumbi wa Chuo Cha Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Mwanza.

Mada mbalimbali zimewasilishwa ndani ya kikao kazi hicho, zikiwemo mada kuhusu Vichocheo na Mazingira ya Rushwa kwa Maafisa Habari na Namna ya Kukabiliana Navyo, Wajibu wa Maafisa Habari Kuzingatia Usalama wa Nchi Katika Kutekeleza Kazi zao, pamoja na mada ya TUNATEKELEZA2019-Mageuzi Katika Utekelezaji wa Serikali Mikoani na Mbinu zinazotumika Kuuhabarisha Umma.

Mada nyingine zilizo kwenye ratiba ambazo zinategemewa kuwasilishwa ni pamoja na Mjadala wa Kujadili "FAKE NEWS" katika Kazi za Maafisa Habari na jinsi ya kukabiliana nazo na mwisho wadau hao watafungua jukwaa la kuainisha Changamoto za Kada yao na kusaka utatuzi wake.

Kikao Kazi hicho kinatarajiwa kufungwa ijumaa ya wiki hii.

MAJALIWA AFUNGUA KITUO CHA AFYA KOROMIJE AKITOA ONYO KWA WASIMAMIZI


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa amefungua kituo cha Afya cha Koromije kilichopo wilayani Misungwi mkoani Mwanza, kilichofanyiwa ukarabati mkubwa na kuhutubia wananchi.

RAIS FILIPE NYUSI: IDADI YA VIFO MSUMBIJI VINAWEZA KUFIKIA 1000

Rais Filipe Nyusi: Idadi ya vifo Msumbiji vinaweza kufikia 1000

Rais Filipe Nyusi wa Msumbiji amesema kuwa, kuna uwezekano idadi ya watu waliopoteza maisha kutokana na kimbunga cha Idai kilichoikumba nchi hiyo ya kusini mwa Afrika ikafikia watu 1000.
Rais huyo wa Msumbiji alisema hayo jana Jumatatu wakati alipozungumza na taifa kwa njia ya redio na kuongeza kuwa, maafa yaliyosababishwa na kimbunga hicho ni makubwa mno ikilinganishwa na idadi ya watu waliothibitishwa kufariki dunia hadi hivi sasa kutokana na maafa hayo ya kimaumbile.
Jana mashirika ya habari yalikuwa yametangaza kwamba, idadi ya watu waliothibitishwa kupoteza maisha kutokana na kimbunga cha Idai kilichopiga katikati ya Msumbiji wiki iliyopita imeshafikia 215. Kimbunga hicho kilichoziathiri pia nchi za Zimbabwe na Malawi kimesababisha mafuriko na uharibifu mkubwa.



Kwa mujibu wa vyombo hivyo vya habari, hadi jana Jumatatu watu wasiopungua 126 walikuwa wamethibitishwa kufariki dunia katika nchi mbili za Msumbiji na Malawi huku waziri wa habari wa Zimbabwe akisema hiyo jana kuwa watu 89 wamepoteza maisha nchini humo kutokana na maafa hayo ya kimaumbile.

Kwa mujibu wa televisheni ya al Jazeera ya Qatar, uharibifu wa janga hilo la kimaumbile ni mkubwa sana kiasi kwamba umefika umbali wa kilomita 300 kutoka eneo kilipopiga kimbunga cha Idai. Mamia ya nyumba zimeharibiwa kikamilifu katika mji wa Beira. Watu wengi wamekimbilia katika maeneo ya shule na wengine kwa majirani zao.

Tuesday, March 19, 2019

NONDO 6 ZA WAZIRI MKUU KWA MAAFISA MAWASILIANO SERIKALINI



Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewaagiza viongozi wa serikali kuwawezesha Maafisa Habari kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kwa wakati.

Waziri Mkuu amebainisha hayo jana wakati wa Kikao Kazi Cha Maafisa Mawasiliano wa Serikali kilichofanyika mkoani Mwanza ambapo amewataka maafisa hao kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao ipasavyo.

Pia Waziri Mkuu ameonya kwa kusema kuwa "Maafisa Habari ambao hawatekelezi majukumu yao hao ni mizigo, wachukuliwe hatua kwa mujibu wa Sheria. Naiagiza Wizara ya Habari kufanya tathmini za mara kwa mara kwa Maafisa Habari na Mawasiliano Serikalini ili kubaini mapungufu na madhaifu yaliyopo".












WAKAZI WA MAJOHE NA VITONGOJI VYAKE JIJINI DAR KUPATA MAJI SAFI NA SALAMA

Katibu Tawala DAS Ilala Sheila Edward aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Ilala Sophia Mjema akitoa neno wakati wa sherehe ya uzinduzi na uwekaji wa jiwe la msingi Ujenzi wa Tanki la Maji katika eneo la Majohe jijini Dar es Salaam. Picha zote na Cathbert Kajuna- Kajunason/MMG.
 Kaimu Mkurugenzi Manispaa ya Ilala Upendo Lugongo akizungumza wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi katika ujenzi wa tanki la maji lenye ujazo wa Lita 150,000 litakalohudumia wananchi laki saba (700,000) leo Jijini Dar es Salaam.
 Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala Charles Kuyeko akizungumza na wananchi wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa Tanki la maji lenye ujazo wa Lita 150,000 litakalohudumia wananchi laki saba (700,000) leo Jijini Dar es Salaam. Diwani wa Mtaa Kichangani Mwenevyale Waziri akitoa neno.
Wakazi wa Majohe na vitongoji vyake wakisikiliza kwa makini.
Katibu Tawala DAS Ilala Sheila Edward akiwa sambamba na Diwani wa Mtaa Kichangani Mwanevyale Waziri wakiweka jiwe la Msingi katika ujenzi wa tanki la maji lenye ujazo wa Lita 150,000 litakalohudumia wananchi laki saba (700,000) leo Jijini Dar es Salaam.
Shamla Shamla zilitanda.
Na Cathbert Kajuna - Kajunason/MMG.
Wakazi zaidi ya 700,000 wa Majohe na vitongoji vyake jijini Dar es Salaam wanatarajia kupatiwa majiSafi na Salama ifikapo mwishoni mwa mwezi Aprili 2019.

Serikali kuwajengea Tanki la Maji lenye uwezo wa kuhifadhi Lita 150,000 kwa siku katika Mtaa wa Kichangani. Akiweka jiwe la Msingi kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Ilala Sophia Mjema, Katibu Tawala DAS Sheila Edward amesema kuwa mradi huu utawasaidia wananchi wa eneo hilo kwa kuwapunguzia kero ya maji waliyonayo kwa muda mrefu. 

 Amesema, serikai inaendelea kutekeleza ahadi za serikali ya mapinduzi ili kufikia malengo ya kumtua mama ndoo kichwani na wamekuwa wanashirikiana na madiwani kwani maendeleo hayana chama. DAS amesema, Uwekaji wa jiwe la msingi Mradi wa maji Mtaa wa Kichangani Majohe utasaidia wananchi takribani laki saba (700,000) kuondokana na kero na amezitaka mamlaka husika kusimamia mradi huo pindi utakapomalizika ili uweze kujiendeleza. 

 Kaimu Mkurugenzi Wa Manispaa ya Ilala Mhandisi Upendo Lugongo amesema kuwa mradi huo wa maji unajengwa kwa kushirikiana na Mamlaka ya Majisafi na Majitaka DAWASA na utawasaidia wananchi wote wanaoishi mtaa wa Kichangani Mahoje. 

 Amesema kuwa, gharama za mradi huo ni takribani milioni 230 na unatarajiwa kumalizika mwishoni mwa mwezi wa nne na lengo kuu ni kupunguza kero ya maji kwa wananchi. 

 Upendo amesema, serikali kwa kushirikiana na mamlaka za maji wanaendelea kushirikiana kwa pamoja kupeleka maji kwenye maeneo ambayo hayakuwa na mtandao wa maji na kufikia lengo la asilimia 95 mwaka 2020. “Kuna mradi mwingine wa maji unaosimamiwa na DAWASA wa Ujenzi wa tanki la Kisarawe ambapo kufikia mwishoni mwa mwaka huu wananchi wote wa Majohe na Gongo la Mboto kwa ujumla watapata majisafi na salama,” amesema Upendo.

 Diwani wa Kata ya Kichangani Mwenevyale Waziri ameishukuru ofisi ya Mkurugenzi kwa kufanikisha kuja kwa mradi huo kwani wana muda mrefu wananchi wa eneo hilo hawajapata majisafi na salama. Mradi huo wa maji wa Mtaa wa Kichangani utakapomalizika kutajengwa vizima saba vya kuchotea maji kwa ajili ya kuwarahishia wananchi wa maeneo hayo. 

 DAWASA wanaendelea kuadhimisha wiki ya maji iliyoanza Machi 16 na itamalizika Machi 22 ikiwa na kauli mbiu ya Hakuna atakayeachwa.

MAJALIWA AUPOKEA MWILI WA MAMA YAKE VICKY KAMATA.


Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa mapema asubuhi  ya leo jumanne majira ya saa 3 katika uwanja wa ndege wa Mwanza ameshiriki kuupokea mwili wa marehemu Mama Paulina Kasama Selemani ambaye ni Mama Mzazi wa Mbunge wa Viti Maalumu wa Geita Mhe. Vicky Kamata na pia ni dada yake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo.

Hivi ndivyo hali ilivyokuwa katika katika eneo la mapokezi la uwanja wa Airport Mwanza.

Mhe. Majaliwa yupo jijini hapa kwa ziara yake ya siku tatu aliyoianza jana kwa kufungua Kikao Kazi cha 15 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki na Uhusiano Serikalini kilichofanyika ukumbi wa Benki Kuu Mwanza.

Leo Mhe. Waziri Mkuu ameendelea ziara yake kwa kufungua Ofisi ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) Kanda ya Ziwa na kukabidhi matrekta 16 kwa vyama vya  Ushirika vya Msingi, kisha baada ya hapo ameelekea Kijiji cha Kolomije Wilayani Misungwi kufungua Kituo cha Afya, kuweka jiwe la msingi katika mradi wa maji Misungwi kwenye chanzocha maji kilichopo kijiji cha Nyahiti na kuhutubia wananchi.

ZANTEL YAENDELEA KUWAPA NEEMA WATEJA WAKE KUPITIA PROMOSHENI YA EZYPESA

Promosheni ya Tumia EzyPesa kwa watumiaji wa mtandao wa Zantel kutuma na kupokea fedha ambayo iliazinduliwa mwezi uliopita na itakayodumu kwa kipindi cha miezi 3 inaendelea kuwanufaisha wateja wa huduma hiyo ambapo wanaendelea kujishindia zawadi za simu za kisasa za Smartphone kupitia droo za kila wiki na fedha taslimu kupitia droo za kila mwezi.
Meneja wa Zantel Kanda ya Pemba, Yakub Fadhil (kulia) akimkabidhi mshindi wa kwanza wa mwezi wa promosheni ya Tumia EzyPesa Ushinde, Bw. Abdallah Salum (kushoto) kitita cha shilingi milioni 
Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Zantel, Sakyi Opuku (kulia) akimkabidhi akimkabidhi zawadi ya simu ya Smartphone mmoja wa washindi wa promosheni ya Tumia Ezypesa ushinde, Juma Omar mkazi wa Unguja, katika hafla iliyofanyika Darajani mjini Unguja hivi karibuni
Afisa Mauzo wa Zantel kanda ya Pemba, Said Masoud Ali (kulia) akimkabidhi kitita cha shilingi laki mbili mmoja wa washindi kupitia promosheni ya Tumia EzyPesa Ushinde, Mohamed Nassor, katika hafla iliyofanyika katika ofisi za Zantel ChakeChake Pemba.
Meneja Mawasiliano wa Zantel, Rukia Mtingwa (kulia) akikabidhi simu ya Smartphone kwa mmoja wa washindi kupitia promosheni ya Tumia EzyPesa Ushinde, Aza Joseph mkazi wa Pemba Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Zantel, Sakyi Opuku (kulia) akimkabidhi akimkabidhi zawadi ya simu ya Smartphone mmoja wa washindi wa promosheni ya Tumia Ezypesa ushinde, Juma Omar mkazi wa Unguja.
Mkuu wa Huduma na bidhaa wa Zantel, Aneth Muga, akimkabidhi zawadi ya simu ya Smartphone mmoja wa washindi wa promosheni ya Tumia Ezypesa ushinde, Asha Hamim Juma mkazi wa Unguja.
Mkuu wa Huduma na Bidhaa wa Zantel, Aneth Muga (katikati) akimkabidhi zawadi ya simu ya Smartphone mmoja wa washindi wa promosheni ya Tumia Ezypesa ushinde, Khadija Ali Makame mkazi waChukwani.
Mkuu wa Huduma na bidhaa wa Zantel, Aneth Muga (katikati) akiwa na baadhi ya washindi wa simu za Smartphone kupitia promosheni inayoendelea ya Tumia ezyPesa Ushinde baada ya kuwakabidhi zawadi zao katika hafla iliyofanyika Darajani mjini Unguja mwishoni mwa wiki.

Monday, March 18, 2019

MAJALIWA NMGENI RASMI 'KIKAO KAZI CHA MAAFISA MAWASILIANO WA SERIKALI MWANZA'.


⚒ - - "Utoaji habari sahihi na kwa wakati ni Chachu ya Kuifikia Tanzania ya kipato cha Kati" #Jembe fm tupo live kutokea kwenye  ukumbi wa Benki kuu ya Tanzania (BOT)
@jembenijembe @jembefm @gsengotv @harrisonmwakyembe @myna_400 @hamadsongora @djkflipmichael @harith_jaha @mansourjumanne @msemajimkuuwaserikali @rcmwanza @john_mongella  @kikotifredy @djmike_beatz @jerrymuro1980