ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, March 12, 2026

TATHIMINI YA ZOEZI LA UHAMAJI WA HIARI WA WAKAZI WA ENEO LA HIFADHI YA NGORONGORO

 

Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka akizungumza katika hafla ya kupokea Taarifa za Tume ya Rais ya Kutathmini Mgogoro wa Ardhi katika Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Tume ya Rais ya Kutathmini Zoezi la Uhamaji wa Hiari wa Wakazi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, tarehe 12 Machi, 2026.

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kutathmini Zoezi la Uhamaji wa Hiari wa Wakazi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Katibu Mkuu Mstaafu, Mhandisi Musa Iyombe akizungumza na kukabidhi Taarifa ya Tume hiyo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, tarehe 12 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kwenye hafla ya kupokea Taarifa za Tume ya Rais ya Kutathmini Mgogoro wa Ardhi katika Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Tume ya Rais ya Kutathmini Zoezi la Uhamaji wa Hiari wa Wakazi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 12 Machi, 2026.

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kutathmini Masuala ya Ardhi katika Wilaya ya Ngorongoro, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani Dkt. Gerald Ndika akizungumza na kukabidhi Taarifa ya Tume hiyo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, tarehe 12 Machi, 2026.




PROFESA KABUDI ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA JUMUIYA YA MADOLA JIJINI LONDON.

LONDON-Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba Kabudi, ameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Jumuiya ya Madola yaliyofanyika jijini London, Uingereza, yakihusisha nchi wanachama 56 wa jumuiya hiyo.
Sherehe hiyo ilijumuisha matukio mbalimbali, ikiwemo hafla ya kupandisha bendera katika Bunge la Uingereza, uwekaji wa shada la maua katika Milango ya Kumbukumbu ya Jumuiya ya Madola, pamoja na ibada ya waumini wa dini mbalimbali iliyofanyika katika Kanisa la Westminster Abbey.
Kaulimbiu ya mwaka huu ilikuwa “Kufungua Fursa kwa Ajili ya Jumuiya ya Madola Yenye Mafanikio,” ikilenga kuhimiza diplomasia, kubadilishana tamaduni na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola.

Hafla hiyo pia iliwakutanisha wanadiplomasia, mawaziri, viongozi wa kimataifa pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo, waliotafakari kuhusu mshikamano wa muda mrefu wa Jumuiya ya Madola na umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kukuza maendeleo endelevu. huku ikichangia kuimarisha sauti na ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya kimataifa.

Wednesday, March 11, 2026

MPANZU ATOKEA BENCHI SINGIDA NA KUIPA POINTI TATU SIMBA SC

 


TIMU ya Simba SC imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars katika mchezo wa Ligi Ali ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Mwigulu Airtel mkoani Singida.

Pongezi kwa winga kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Elie Mpanzu Kibisawala aliyeifungia bao la ushindi Simba SC dakika ha 84 akimalizia pasi nzuri ya kiungo Mzambia, Clatous Chotta Chama.

Mpanzu alifunga bao hilo dakika tano tu tangu aingie kuchukua nafasi ya kiungo kutoka Kongo-Brazzaville, Inno Jospin Loemba.

Hadi mapumziko timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1 winga wa kushoto, Muivory Coast, Alain Anicet Oura akianza kuifungia Simba dakika ya saba, kabla ya winga wa kulia, Mossi Nduwumwe kuisawazishia Singida Black Stars dakika ya 38.

Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 27 na kusogea nafasi ya pili ilizidiwa pointi tano na mabingwa watetest, Yanga baada ya wote kucheza mechi 12, wakati Singida Black Stars inabaki na pointi zake 19 za mechi 13 sasa na kushuka kwa nafasi moja hadi ya 10.

RAIS SAMIA AMUASILI MTOTO MCHANGA ALIYETELEKEZWA NZEGA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemuasili mtoto mchanga wa kike leo tarehe 11 Machi, 2026, katika makazi yake, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.


Mtoto huyo aliyepewa jina la Grace Samia Suluhu Hassan alitelekezwa mjini Nzega, mkoani Tabora, na amekabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai.


Akizungumza wakati wa kumkabidhi mtoto huyo, Mkuu wa Wilaya Tukai alisema mtoto huyo aliokotwa tarehe 17 Januari, 2026 akiwa ametelekezwa katika eneo jirani na nyumba ya wageni ya Kasulu, Nzega Mjini. 


Alieleza kuwa baada ya kupokea taarifa hizo, alishirikiana na Jeshi la Polisi kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitalini kwa uchunguzi na uangalizi, huku juhudi za kumtafuta mama yake zikiendelea bila mafanikio.


Rais Dkt. Samia amemkaribisha mtoto huyo katika familia yake na kuahidi kumpatia malezi, ulinzi na huduma zote muhimu ili akue katika mazingira salama na yenye upendo.


“Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina, na hatuijui kesho yake,” alisema Rais Dkt. Samia.

Profesa Kabudi akutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Canada

 LONDON-Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof Paramagamba Kabudi, amefanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Canada, Mhe. Rober Oliphant..

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Machi 8, 2026.

Viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kati ya Tanzania na Canada pamoja na kuendeleza uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola kwa kuzingatia misingi na tunu za jumuiya hiyo katika kukuza ushirikiano na maendeleo ya pamoja.
Aidha,viongozi hao wamebainisha kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Canada umejengwa juu ya msingi wa urafiki wa kihistoria, ushirikiano wa kiuchumi pamoja na uanachama wao ndani ya Jumuiya ya Madola, hali inayofungua fursa zaidi za kupanua ushirikiano katika nyanja za biashara, uwekezaji na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Pia, viongozi hao wameangazia mchango wa diaspora wa Tanzania na Canada katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi zao.

Walieleza kuwa kupitia uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola, diaspora imeendelea kuwa kiungo muhimu kinachoimarisha uhusiano wa watu kwa watu na kufungua fursa zaidi za ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.
Katika mazungumzo hayo, Prof. Kabudi aliambatana na Mshauri wa Rais katika Masuala ya Diplomasia, Balozi Lazaro Nyalandu; Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki; pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Noel Kaganda.

TANZIA SSEBO AFARIKI DUNIA

 


Mkurugenzi Wa Uendeshaji Na Biashara wa EFM TV E Bwana Denis Busulwa (Ssebo) amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika hospital ya Taifa Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu.


Taarifa za kifo cha Ssebo zimethibitishwa na Mkurugenzi wa EFM TVE Francis Majizo kupitia kurasa zake rasmi za mitandao ya kijamii akeeleza kuwa taratibu zingine zinaendelea na taarifa zaidi zitatolewa.

"Kwa moyo mzito na machozi mengi, nasikitika kutangaza kifo cha rafiki, kaka, aliyekuwa msimamizi wa ndoa yangu, na mfanyakazi mwenzangu aliyeitumikia EFM na TVE kwa nguvu zake zote, ndugu yangu Ssebo.

Tuesday, March 10, 2026

DC Makilagi: HAKUNA VIFO, UPOTEVU WA MALI MAFURIKO MWANZA

 Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza, Amina Makilagi.

Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza, Amina Makilagi amesema kuwa hadi sasa hakuna tukio la kifo na upotevu wa mali ya mwananchi yeyote katika hekaheka za mvua kubwa iliyonyesha leo Machi 10, 2026 jijini Mwanza.

Mvua hiyo imenyesha mfululizo kwa takribani saa nane kuanzia saa 10 alfajiri hadi saa saba mchana na kuathiri maeneo mengi ya wilaya ya Nyamagana (jiji la Mwanza) hususan Kata ya Mkuyuni na kusababisha kubomoa kuta za majengo, magari kuzama, nyumba kuzingirwa na maji, na wananchi kushindwa kufanya shughuli ikiwamo kwenda kazini kutokana na maji kujaa barabarani.

Akizungumza leo na waandishi wa habari baada ya kutembelea eneo la Mkuyuni lililoathirika na mvua hizo, Amina amelipongeza jeshi la polisi na zimamoto kwa juhudi kubwa za kuhakikisha wananchi hawaathiriki na mvua hizo.

“Mpaka sasahivi ninavyozungumza hakuna mwananchi yeyote aliyepata tukio ama kifo chochote kilichotokea kwenye wilaya yetu, mtu aliyepoteza mali zake wala mtu yeyote kupata tatizo lolote la kiusalama, nashukuru jeshi la zimamoto wamefika kwa wakati na wameingia majini ndiyo maana utaona hata wale walioteleza wakaanguka kwenye maji waliokolewa,” amesema Amina.

Aliwataka wananchi kuwa makini na kuzingatia taarifa za utabiri wa hali ya hewa zinazotolewa kuhusu uwepo wa mvua kubwa, huku akiwataka wakazi wa mabondeni kuchukua hatua mapema kwa kutafuta maeneo yenye usalama.

Baadhi ya wakazi wa jiji la Mwanza, wakizungumzia hali hiyo walisema imewaathiri kwa kiasi kikubwa kwa kusababishwa washindwe kwenye kwenye maeneo yao ya kazi na kurudia njiani, kupoteza mali, biashara na kuhangaika kupata usafiri.

Abel Zabron, mkazi wa Nyegezi alisema changamoto hiyo ilimpata asubuhi wakati akielekea kazini ndipo alipofika Mkuyuni na kukuta maji yamejaa barabarani na kwenye makazi ya watu na kushindwa kuvuka kwenda upande wa pili (mjini).

Zabron alishauri serikali kuona namna ya kutengeneza miundombinu bora ikiwemo mito itakayokuwa inatiririsha maji vizuri ili barabara ziwe safi kwa ajili ya watu kuwahi makazini kwao.

Mkazi wa Butimba, Getrude Jacob alisema; “Hali ya leo imetuathiri sana tulikuwa na zana zetu lakini zote zimeondoka, hapa tulipo hatuan hata mbele wala nyuma nimeathirika sana na hii mvua na imeharibu vitu vingi sana. Nilikuwa natunzia vitu vyangu hapo garden lakini vimeenda vyote hapa nilipo sina mtaji yaani natetemeka tu,”


MAAFA YA MVUA YAFUNGA MTAA MKUYUNI, WAFANYABIASHARA WASAFIRI WAHAHA.

 🚨𝗠𝗸𝘂𝘆𝘂𝗻𝗶: 𝗠𝗮𝗮𝗳𝗮 𝘆𝗮 𝗺𝘃𝘂𝗮 𝘆𝗮𝗺𝗳𝘂𝗻𝗴𝗮 𝗺𝘁𝗮𝗮, 𝘄𝗮𝗳𝗮𝗻𝘆𝗮𝗯𝗶𝗮𝘀𝗵𝗮𝗿𝗮 𝘄𝗮𝗸𝗮𝘁𝗮 '𝗛𝗮𝘁𝘂𝗺𝘄𝗶 𝗺𝘁𝗼𝘁𝗼 𝗱𝘂𝗸𝗮𝗻𝗶'

.
Majira ya asubuhi ya leo tarehe 10/03/2026 eneo la Mkuyuni lilishuhudia mafuriko makubwa baada ya mvua kuendelea kunyesha, hali iliyofanya barabara zisipitike na maji kujaa kwa kiwango kinachoharibu biashara na maduka kandokando ya barabara.
.
Mvua ilianza mdogomdogo mapema alfajiri na kuongezeka kuanzia saa 2:30 hadi 4:00 asubuhi, ikichapa ile yenyewe, ikisababisha wateja kukosa uwezo wa kufika sokoni na wafanyabiashara kulazimika kufunga maduka.
.
“Maji yalikuja ghafla na kujaa dukani nikalazimika kupandisha juu bidhaa zote nilizokuwa nimeziweka chini sakafuni — hatumwi mtoto dukani,” alisema mfanyabiashara mmoja wa sokoni, akieleza wasiwasi wa wafanyabiashara waliokuwa wameweka bidhaa mafuta za mauzo.
.
Hadi sasa mamlaka za mkoa au wilaya hazijatoa taarifa rasmi kuhusu uzito wa uharibifu au idadi ya wahasiriwa.
.
#jembehabari
#DriveMix

MWANAFUNZI ALIYEDAIWA KUBEBWA NA MAMBA APATIKANA HAI BAADA YA SIKU SABA

Mwanafunzi huyo (aliyefunikwa uso) akiondolewa Katika Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe na ofisa wa jeshi la polisi dawati la jinsia.
Mwanafunzi huyo (aliyefunikwa uso) akiondolewa Katika Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe na ofisa wa jeshi la polisi dawati la jinsia.

 Katika tukio la kushangaza na lisilo la kawaida, mwanafunzi wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari Colnel Magembe iliyopo Wilaya ya Ukerewe, Mkoa wa Mwanza (jina limehifadhiwa), amepatikana akiwa hai baada ya kudaiwa kushambuliwa na kuchukuliwa na mamba takribani wiki moja iliyopita.

Tukio la kutoweka kwa mwanafunzi huyo lilitokea Machi 2, 2026 katika kitongoji cha Ilondo Magharibi, kijiji cha Buzegwe, Kata ya Kagunguli wilayani Ukerewe. Inadaiwa kuwa saa 11 alfajiri alipokuwa akioga katika Ziwa Victoria akijiandaa kwenda shuleni, alishambuliwa na mamba na kubebwa majini.

Hata hivyo, jana Jumatatu Machi 9, 2026, majira ya saa 11 alfajiri, mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 18 amepatikana akiwa hai katika eneo lile lile alikodaiwa kuchukuliwa na mamba. Cha kushangaza zaidi ni kwamba alikutwa bila majeraha wala michubuko yoyote mwilini.

Kwa mujibu wa taarifa, wavuvi waliokuwa wakifanya shughuli zao kandokando ya Ziwa Victoria ndiyo waliomkuta binti huyo akiwa amelala karibu na ufukwe wa ziwa. Hata hivyo, hakuwa na uwezo wa kuzungumza. Wananchi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi walimchukua na kumpeleka katika Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe (Bomani) iliyopo Nansio kwa ajili ya matibabu na uchunguzi zaidi.

Akizungumza hospitalini hapo Machi 9, 2026, baba wa mwanafunzi huyo, Deonatus Salvatory, amesema familia ilishakata tamaa baada ya juhudi za kumtafuta kugonga mwamba. Alieleza kuwa walikuwa tayari wameanza maandalizi ya msiba na jamii ilikuwa imeanza taratibu za maombolezo kama ilivyo katika misiba mingine.

Salvatory amesema walipokea simu kutoka kwa wavuvi alfajiri wakitoa taarifa kuwa binti yao amepatikana kandokando ya ziwa akiwa hai, jambo lililowashangaza sana.

“Matumaini ya kumpata yalikuwa yamekwisha kabisa. Baada ya kutoonekana kwa muda mrefu tuliweka msiba na kufanya matanga, watu walikuwa tayari wameanza kutawanyika. Tangu nizaliwe katika eneo hili, sijawahi kushuhudia tukio kama hili. Tunaamini si jambo la kawaida,” amesema Salvatory.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe (Bomani), Dk. Bunhya Kayila, amesema walimpokea mwanafunzi huyo majira ya saa 1 asubuhi akiwa dhaifu. Uchunguzi wa awali umeonyesha hana majeraha yoyote yanayoashiria kuwa alishambuliwa na mamba.

Dk. Kayila amesema vipimo mbalimbali vinaendelea kufanywa ili kubaini hali yake kiafya, huku akieleza kuwa kwa sasa mwanafunzi huyo anaweza kutambua mazingira yanayomzunguka lakini bado hana uwezo wa kuzungumza. Amewekwa wodini chini ya uangalizi wa karibu kwa angalau saa 24.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe, Goodluck Mtigandi, amesema uchunguzi wa awali haujaonyesha dalili za uwepo wa mnyama hatarishi katika eneo alikodaiwa kushambuliwa mwanafunzi huyo.

Amesema tangu Machi 2 hadi sasa hakukuwa na ushahidi wowote wa kuthibitisha kuwa mnyama pori alimshambulia binadamu katika eneo hilo. Hivyo, mamlaka zinasubiri mwanafunzi huyo apate nafuu ili aweze kueleza kwa undani kilichotokea katika kipindi chote alichokuwa hajulikani alipo.

Aidha, Jeshi la Polisi Wilaya ya Ukerewe kupitia dawati la jinsia na watoto limezuia vyombo vya habari kumuona mwanafunzi huyo au kupiga picha zake. Kwa sasa amehamishwa wodini na anaendelea kuwa chini ya uangalizi wa karibu wa vyombo vya usalama pamoja na wataalamu wa afya huku uchunguzi zaidi ukiendelea kubaini ukweli wa tukio hilo.


Monday, March 9, 2026

Naibu Waziri Maghembe azungumza na Wawakilishi wa Heshima wa Tanzania nchini Nepal, mjini Mumbai, Chennai na Kolkata

 NEW DELHI-Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe amekutana kwa mazungumzo na Wawakilishi wa Heshima wa Tanzania katika maeneo ya Nepal, Mumbai, Chennai na Kolkata ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi nchini India.

Katika mazungumzo yao yaliyofanyika jijini New Delhi hivi karibuni wamejadili umuhimu wa wawakilishi hao kushirikiana na Serikali katika kuimarisha sekta ya utalii, kilimo, elimu na biashara na uwekezaji ili kutekeleza dhana ya Diplomasia ya Uchumi.
Akizungumza, kwenye kikao kilichofanyika jijini New Delhi hivi karibuni, Mhe. Dkt. Maghembe aliwapongeza wawakilishi hao kwa kuiwakilisha Tanzania kikamilifu kwenye maeneo yao na kwamba Serikali inathamini mchango wao kwenye uwakilishi huo na itaendelea kushirikiana nao.

Kwa upande wao, wawakilishi hao Mhe. Rajesh Chaudhary wa Nepal, Mhe. Nayan Patel wa Mumbai, Mhe. Krishna Pimple wa Chennai na Mhe. Pradeep Singhania wa Kolkata wamemshukuru Mhe. Naibu Waziri kwa kukutenga muda wa kukutana nao na kwamba wataendelea kuiwakilisha Tanzania kikamilifu kwenye maeneo yao hususan katika kutangaza fursa mbalimbali zilizopo nchini ikiwemo utalii biashara na uwekezaji.