ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, February 26, 2026

AZAM FC YAILAMBA MTIBWA SUGAR 3-0

 

Presha katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara inazidi kuongezeka baada ya Azam FC kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Mtibwa Sugar, usiku huu ni katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, jijini Dar es Salaam.

Mabao ya Azam FC yamefungwa na kiungo Feisal Salum Abdallah dakika ya tatu tu ya mchezo na mshambuliaji mpya, Jean-Jacques Ngita Kamanga raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), aliyesajiliwa dirisha dogo kutoka Aris Limassol ya Cyprus akitupia magoli mawili dakika ya 19 na 59. 

Kwa ushindi huo, Azam FC wanafikisha pointi 22 katika mchezo wa 10 na kupanda kwa nafasi tatu hadi ya tano, wakati Mtibwa Sugar inabaki na pointi zake 21 za mechi 16 nafasi ya nne. 

CCM YATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA ASKOFU MKUU RUWA’ICHI KUFUATIA KIFO CHA KADINALI PENGO

 

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetoa salamu za rambirambi kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddeus Ruwa’ichi OFMCap, kufuatia kifo cha Askofu Mkuu mstaafu wa Jimbo hilo, Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo, aliyefariki dunia Februari 19, 2026, katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) alipokuwa akipatiwa matibabu.


Akizungumza Februari 26, 2026 baada ya kusaini kitabu cha maombolezo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu, Dar es Salaam, Katibu Mkuu CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro, alisema amewasilisha salamu za rambirambi kwa niaba ya Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Dkt. Migiro alisema marehemu Kadinali Pengo atakumbukwa kama mchungaji wa faraja na tumaini, kiongozi wa kiroho mwenye hekima, unyenyekevu na msimamo thabiti wa maadili.

Alijipambanua si tu kwa huduma ya Kanisa, bali pia kwa mchango wake katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa, maadili ya jamii, malezi ya vijana na uwajibikaji wa viongozi.


“Kadinali Pengo ameacha alama inayodumu ya utumishi wa Mungu, utumishi wa Taifa na utumishi wa jamii. Maisha na mafundisho yake yataendelea kuwa dira kwa vizazi vijavyo,” alisema Dkt. Migiro.

CCM imesema inaliombea Kanisa Katoliki na waumini wote wapate faraja katika kipindi hiki cha maombolezo na Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Kwa mujibu wa ratiba ya mazishi, mwili wa marehemu utawasili Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Februari 27, 2026 kwa ajili ya waumini kutoa heshima zao za mwisho, na Ibada ya Misa ya Mazishi itafanyika Februari 28, 2026 katika Kituo cha Hija Pugu, Dar es Salaam.



MBOZI WAFANYA UCHAGUZI MWINGINE BAADA YA DIWANI ALIYEKUWEPO KUJIUWA.

 


ZOEZI la upigaji kura katika uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Shiwinga, Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, linaendelea leo Februari 26, 2026, huku wananchi wakijitokeza kwa wingi.

Uchaguzi huo umeitishwa kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wa kata hiyo, Lusekelo Mwalukomo, kilichotokea Novemba 26, 2025, baada ya kunywa maji ya betri, zikiwa zimebaki siku chache kabla ya kuapishwa rasmi kushika wadhifa huo.

Kwa mujibu wa Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi katika kata hiyo, Selestin Luambano, jumla ya wapiga kura 6,854 wanatarajiwa kushiriki zoezi hilo katika vituo 19 vilivyotengwa kwa ajili ya kupigia kura.

Amesema jumla ya vyama nane vya siasa vimesimamisha wagombea kuwania nafasi hiyo.

Wagombea hao ni Menati Mzumbwe (CCM), Matias Dulle (ADC), Elly Shitindi (ADA-TADEA), Mary Daud (UPDP), Neema Abadallah (UMD), Emily Siwale (SAU), Mussa Dulle (Chama-Makin) na Cosam Mwakyusa (TLP).

BARABARA MLIMA KITONGA KUPANULIWA NA KUWA NJIA NNE

news

WAZIRI wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema serikali iko katika hatua za mwisho za kuanza upanuzi wa barabara inayopita Mlima Kitonga mkoani Iringa ambayo sasa itakuwa ya njia nne na yenye taa za barabarani.

Amesema hatua hiyo ni uamuzi wa Rais Samia Suluhu Hassan ili kupunguza foleni na kuboresha usalama wa watumiaji wa barabara katika njia hiyo inayotumiwa na magari mengi. 

Akizungumza jana baada ya kutembelea eneo hilo, Waziri Ulega, alisema barabara hiyo ni ya kimkakati kwa uchumi wa nchi kwa sababu inatumiwa pia na magari yanayokwenda katika nchi zinazotumia bandari ya Dar wa Salaam kubeba mizigo yao. 

Akitoa picha ya ongezeko la uhitaji wa upanuzi wa barabara hiyo, Waziri Ulega alisema idadi ya magari yanayopita katika Barabara Kuu ya TANZAM imeongezeka kutoka magari 1,700 hadi 3,400 kwa siku, hali inayosababisha njia hiyo kuzidiwa.

Waziri wa Ujenzi Abdala Ulega akizungumzia upanuzi wa barabara Mlima Kitonga.

“Nimepokea mapendekezo kutoka kwa Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Iringa ya kuhakikisha tunaondoa msongamano wa magari katika Mlima Kitonga, na nimeelekeza kwa wataalamu wetu kupanua hii barabara kwa kilometa saba. Kwa sasa hivi barabara ina njia mbili kwa hiyo tutatanua na kuwa njia nne,” alisema Ulega.

Waziri Ulega aliongeza kuwa ni maelekezo ya Rais Samia kwamba kila mradi wa barabara uende sambamba na uwekaji wa taa za barabarani ili kuhakikisha usalama wa watumiaji ikiwemo wananchi, wafanyabiashara na madereva pamoja na kuweka kingo pembezoni mwa barabara ili kuzuia magari yasianguke kwenye makorongo.

“Ninaagiza manunuzi yaanze mara moja ili kuhakikisha kwamba barabara hii inatanuliwa kwani ina umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi hivyo hatuwezi kuiacha katika hali hii na kutimiza pia maelekezo ya rais kutatua changamoto zote,” alisema Ulega. 

Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Ritha Kabati, alisema barabara hiyo ni ya uchumi wa kimataifa hivyo ikitengenezwa itainua zaidi uchumi wa Mkoa wa Iringa na taifa kwa ujumla pamoja na kuwasaidia wananchi ambao hupata changamoto ya kufuata huduma za kijamii ikiwemo matibabu Iringa mjini. 

Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa Eng. Yudas Msangi alisema gharama ya upanuzi wa kilometa saba kwa njia mbili katika barabara hiyo ni bilioni 59.2 na ukarabati wa njia mbili zilizopo ni bilioni 16.2.

Wednesday, February 25, 2026

SIMBA YAKWAA KISIKI DODOMA

 


TIMU ya Simba SC imetoa sare ya bila kufungana na wenyeji, Dodoma Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

Kwa matokeo hayo, Simba SC inafikisha pointi 23 katika mchezo wa 10 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya tatu, wakati Dodoma Jiji FC inafikisha pointi 21 katika mchezo wa 16, ingawa inabaki nafasi ya sita. 

YANGA YATUMA SALAMU KWA 'KUIGAGADUA' JKT GOLI TANO MTUNGI

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya JKT Tanzania katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na beki Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ dakika ya saba, mshambuliaji Muangola Laurindo Dilson Maria Aurelio ‘Depu’ dakika ya 60, kiungo Mudathir Yahya Abbas dakika ya 63, mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Mpumelelo Dube dakika ya 84 na kiungo Shekhan Ibrahim Khamis dakika ya 89.

Kwa ushindi huo, Yanga wanafikisha pointi 28 katika mchezo wa 10 na kupanda kileleni ikiizidi tu wastani wa mabao JKT Tanzania, ambayo pia imecheza mechi saba zaidi. 

Mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo Dube ndiye Mchezaji Bora wa Mechi leo

STAMICO, PLANTCOR WASAINI UBIA UTAFITI NA UCHIMBAJI MADINI BUKOMBE

 NA ALBERT G.SENGO/BUKOMBE/GEITA

Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imeingia makubaliano ya ushirikiano na kampuni ya uchimbaji madini ya Plantcor ya Afrika Kusini kwa lengo la kufanya utafiti na baadaye uchimbaji wa madini katika Pori na Hifadhi ya Msitu wa Kigosi, wilayani Bukombe mkoani Geita. Makubaliano hayo yamesainiwa Jumanne, Februari 24, 2026 katika Ukumbi wa CCM Bukombe, hafla iliyohudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa kama mgeni rasmi. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Kiruswa amesisitiza umuhimu wa mwekezaji kuhakikisha kuwa zoezi la utafiti, litakalotumia teknolojia ya kisasa ya ndege nyuki (drones) kabla ya kuanza rasmi uchimbaji wa dhahabu, linafanyika kwa uwazi na kwa kutoa taarifa sahihi kwa wananchi ili waweze kushirikishwa na kunufaika na matokeo ya utafiti huo. Aidha, amemtaka mwekezaji huyo kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya eneo husika, hususan barabara, kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), ili kurahisisha upatikanaji wa maeneo ya uchimbaji kwa wachimbaji wadogo. Ameeleza kuwa hali ya miundombinu ilivyo sasa hairidhishi na inahitaji maboresho ya haraka. Mradi huo unatarajiwa kuwa chachu ya uchumi katika wilaya hiyo kupitia kodi za mirabaha, uboreshaji wa miundombinu na huduma za kijamii kwa wananchi pamoja na ajira za muda mfupi na mrefu zipatazo 2,000.

Saturday, February 21, 2026

KUKAMILIKA KWA DARAJA LA BUGELENGA (MITA 60.54) KUFUNGUA FURSA ZA KIUCHUMI BUKOMBE NA MBOGWE

 

Na, Ernest Magashi

Kukamilika kwa Daraja la Bugelenga lenye urefu wa mita 60.54 kunatarajiwa kufungua fursa mpya za kiuchumi kwa wananchi wa Wilaya za Bukombe na Mbogwe mkoani Geita, hasa katika kurahisisha usafirishaji wa mazao na mawasiliano kati ya wilaya hizo mbili.

Akizungumza wakati wa kukagua daraja hilo, Diwani wa Kata ya Bugelenga, Donald Lubigisa, alimpongeza Mbunge wa Jimbo la Bukombe na Naibu Waziri Mkuu mstaafu, Dkt. Doto Biteko, kwa kutekeleza ahadi yake ya kuhakikisha daraja hilo linajengwa na kukamilika kwa wakati.Lubigisa alisema mradi huo umegharimu Shilingi milioni 583.83 zilizotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufuatia maombi yaliyowasilishwa na mbunge huyo baada ya kuombwa na diwani pamoja na wananchi.Alieleza kuwa daraja hilo linaunganisha moja kwa moja Wilaya ya Bukombe na Mbogwe, na limeondoa changamoto ya usafiri hasa kipindi cha masika, ambapo awali wananchi walipata shida kubwa kusafirisha mazao yao kwenda sokoni.“Ninamshukuru Mbunge Dkt. Biteko kwa kuwa msikivu na kufuatilia kwa karibu changamoto za wananchi. Pia nampongeza Meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Bukombe, Mhandisi Msoka Msumba, kwa usimamizi mzuri wa mradi huu hadi kukamilika kwake,” alisema Lubigisa.Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Bukombe, Mhandisi Msoka Msumba, alisema ujenzi wa daraja hilo umekamilika kwa wakati kama ilivyopangwa, na kubainisha kuwa lenye urefu wa mita 60.54 ni miongoni mwa madaraja marefu ya mawe katika Mkoa wa Geita. Aliongeza kuwa mradi huo umegharimu jumla ya Shilingi milioni 583.83.Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Bugelenga walitoa shukrani kwa Serikali kwa kuboresha miundombinu hiyo, wakisema daraja hilo limekuwa suluhisho la kudumu kwa changamoto za usafirishaji wa mazao, hasa wakati wa mvua kubwa.Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Mkange, Timbola Kasungwa, aliipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mradi huo, akieleza kuwa daraja hilo limekuwa mhimili muhimu wa uchumi kwa vijiji vya mpakani, na linatarajiwa kuongeza kipato cha wananchi mmoja mmoja pamoja na taifa kwa ujumla.

DKT. JAFO AWEZESHA ELIMU YA UFUNDI, AKABIDHI VYEREHANI VINNE CHUO CHA FDC KISARAWE-MZENGA

 
Na Mwandishi Wetu

Taasisi ya Jafo Education Foundation imefadhili jumla ya vijana 51 kusoma katika Chuo cha FDC Kisarawe - Mzenga, kwa lengo la kuwawezesha kupata ujuzi wa fani mbalimbali za ufundi.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi na kuzungumza na wananchi katika Kata ya Mzenga, Mbunge wa Jimbo la Kisarawe Mhe.Dkt. Selemani Jafo, amesema vijana hao 51 watatoka katika kata zote 17 za wilaya hiyo na taasisi hiyo itagharamia ada zao za masomo.

"Hii ni fursa muhimu kwa vijana wa Kisarawe kujipatia ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kuajiriwa, hasa katika kipindi hiki ambacho soko la ajira linahitaji wataalamu wenye ujuzi wa vitendo."amesema Dkt. Jafo

Dkt.Jafo amesema kuwa Chuo cha FDC Kisarawe – Mzenga ni chuo kipya kilichojengwa wilayani humo na tayari kinatoa mafunzo katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ushonaji, ujenzi, mapishi, umeme, kompyuta pamoja na mafunzo ya muda mfupi.


Aidha, Dkt. Jafo ameeleza kuwa tangu mwaka 2010 amefanikiwa kusaidia zaidi ya vijana 500 kutoka familia zenye changamoto kusoma katika ngazi mbalimbali, ikiwemo kidato cha tano, astashahada, stashahada na shahada.

Katika kuendeleza juhudi za kukuza elimu ya ufundi, tarehe 20 Februari, Dkt. Jafo kupitia taasisi yake amekabidhi msaada wa vyerehani vinne vya umeme katika chuo hicho, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuwa dhamira kuu ni kuwawezesha vijana katika fani za ufundi ili kujenga msingi imara wa ajira rasmi na zisizo rasmi, pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo katika Wilaya ya Kisarawe.

SONGORO MARINE UBORA WA KIMATAIFA UJENZI MELI


Kampuni ya kizawa ya Songoro Marine iliyojikita katika ujenzi wa meli ndani na nje ya Tanzania inatajwa ni kampuni inayojenga meli kwa viwango vya kimataifa.


Kampuni hiyo, imekuwa ikipewa zabuni na serikali za ujenzi wa vivuko, kutokana na kuonyesha uzalendo katika kutekeleza miradi kwa viwango vya kimataifa.


Kwa miaka zaidi ya 30 Tangu kuanza kwa kampuni hii ya kizalendo imeonyesha dira kwa kampuni za kizawa baada ya kuaminiwa na serikali katika ujenzi wa vivuko.


Kampuni hii iliyoanza kazi mwaka 1993 kwa sasa imeendeleza mizizi ya ujenzi wa meli za kisasa zinazotumiwa ziwani na baharini kwa kufungua matawi nje ya mipaka ya Tanzania.


Inaelezwa kuanza kufungua matawi nje ya mipaka ya Tanzania ni hatua iliyotokana na kazi iliyotukuka kwa kujenga meli na vivuko vya umma na binafsi kwa viwango vya kimataifa.


Serikali ya Tanzania mara kwa mara imekuwa ikitangaza zabuni za ujenzi wa meli, ambapo kampuni hii ya kizalendo imekuwa ikiibuka kidedea.


Songoro Marine yenye makao makuu yake Ilemela mkoani Mwanza, kwa sasa inaendelea na ujenzi wa Meli tano ambazo zipo katika hatua mbalimbali.


Kati ya hizo meli tano, Meli ya Mv. Ukerewe ambayo imekamilika kwa asilimia 99 itakuwa inafanya safari zake kati ya Rugezi - Kisorya.


Kampuni ya Songoro Marine imekuwa ni mkombozi kwa Taifa kutokana na kujikita katika ujenzi wa meli na kuipa Taifa sofa nje ya Tanzania baada ya nchi ya Uganda kuipa kazi ha ujenzi wa meli.


Songoro Marine yenye tawi lingine, jijini Dar es Salaam ambako ujenzi wa vivuko inaendelea kwa kasi na viwango vinavyohitaji kulingana na mamlaka zinazosimamia sekta hiyo.


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi mkuu wa kampuni hiyo, Meja Songoro, Mratibu miradi wa Songoro, Hawa Isakiya, amesema kampuni hiyo imekuwa ikishirikiana na serikali katika ujenzi wa vivuko.


Anasema serikali kupitia  Wakala wa Ufundi na Umeme - Temesa, asilimia 75-80 kazi nyingi wanazofanya na za Umma, ambapo kazi chache zilizobaki ni kutoka nje ya nchi na watu binafsi.


Isakiya anasema kukuwa kwa kampuni wamefanikiwa kuongeza wigo kwa kufungua  tawi lingine nchini Uganda kwa ajili ya kusogeza huduma karibu.


Anaeleza mafanikio hayo yamesababishwa na serikali ya Tanzania kwa kujali wawekezaji wazawa kwa kuwapa nafasi ya kuonyesha uwezo wao.


Isakiya amesema, “kampuni kwa sasa inaendelea na vivuko vingine vinne, ikiwemo Kivuko cha Kome kitakachofanya safari zake Nyakalilo - Kome, Kivuko cha Mv. Bukondo kitafanya safari Bwiro - Bukondo ambacho kipo asilimia 99,”.


Friday, February 20, 2026

RC MTANDA AZINDUA MADUKA MATANO YA NGUVU YA AIRTEL JIJINI MWANZA

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA 

Mwanza ni kitovu cha uchumi katika Kanda ya Ziwa. Shughuli kuu za uchumi wetu ni pamoja na uvuvi katika Ziwa Victoria, biashara ndogo na za kati, kilimo cha pamba na mazao ya chakula, uchimbaji wa madini, pamoja na sekta ya huduma na utalii.

Kwa wavuvi wanaofanya kazi katika mwambao wa Ziwa Victoria, mawasiliano ya uhakika yanarahisisha biashara ya samaki, kupanga masoko, na kufanya malipo kwa njia ya kidijitali.

Kwa wafanyabiashara wa masoko kama Soko Kuu la Mwanza, Soko kuu la Samaki Kirumba na maeneo mengine huduma za Airtel Money zinarahisisha miamala, kupokea malipo, na hata kuagiza bidhaa kutoka maeneo mengine ya nchi.

Kwa wakulima wa pamba na mpunga katika wilaya za mkoa wa Mwanza, huduma za mawasiliano zinawaunganisha na masoko na taasisi za kifedha.

Hivyo basi, uwekezaji huu wa Airtel Tanzania unaenda moja kwa moja kuunga mkono shughuli hizi muhimu za kiuchumi zinazofanywa na serikali

Thursday, February 19, 2026

DKT. MWIGULU AIPA WIZARA YA MAJI WIKI MBILI.

 Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ameipa Wizara ya Maji kipindi cha wiki mbili kuhakikisha inakamilisha mchakato wa upatikanaji wa mkandarasi wa ujenzi wa mradi wa maji kutoka chanzo cha Ziwa Chala.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wananchi wa kata ya Marangu-Kitowo, Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro baada ya kupokea taarifa za ujenzi wa Mradi wa Maji kutoka chanzo cha ziwa Chala, Ujenzi wa mradi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi), pamoja kuweka jiwe la msingi la Shule ya Sekondari Stephen Moshi Technical.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa ujenzi wa mradi huo unapaswa kuanza kutekelezwa kwani unategemewa kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji katika Wilaya nzima ya Rombo.

Kwa upande wake Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa Wizara haitakuwa kikwazo katika utekelezaji wa mradi huo na watahakikisha katika kipindi cha siku 14 wanampata mkandarasi wa mradi huo.

Mradi wa maji ziwa Chala unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 8.66 na utanufaisha wananchi 34,104 katika vijiji 14 vya wilaya ya Rombo.

Kadhalika Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amemuagiza Waziri wa Fedha kuhakikisha anatafuta fedha kwa ajili ya kufanya malipo ya awali kwa mkandarasi ili aanze ujenzi wa mradi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi) kilomita 52.8
Mradi huo ambao utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 28 unapita mpakani mwa Tanzania na Kenya na unategemewa kusaidia kukuza shughuli za kijamii, kiuchumi pamoja na utalii.

Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari Stephen Moshi Technical ambayo itagharimu shilingi bilioni 1.6 Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa shule hiyo ni kielelezo cha uwepo wa kiongozi mwenye maono na mipango.

“Ndani ya muda mchache sana zimejengwa shule zaidi ya 103 za aina hii nchi nzima” Amesema Dkt. Mwigulu.

Mradi huo utahusisha Ujenzi wa madarasa 08, ofisi 02, chumba 01 cha TEHAMA, maabara ya kemia na baiolojia, mabweni 4 ya wasichana na wavulana, bwalo 01, karakana 01 ya magari, matundu 08 ya vyoo vya wasichana na wavulana na Kichomea taka.

Pia utahusisha uchimbaji wa kisima cha maji cha ardhini, jengo la utawala na nyumba 01 ya mtumishi.


    YANGA SC YAICHAPA COSMO 2-0 NA KUSONGA MBELE KOMBE LA CRDB

     


    MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Cosmopolitan katika mchezo wa Raundi ya Pili Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) usiku wa jana 18 February 2026 Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

    Mabao yote ya Yanga leo yamefungwa na mchezaji mpya, winga Mgambia, Buba Jammeh aliyesajiliwa dirisha dogo kutoka Interclube ya Angola dakika ya 13 na 23 ya mchezo huo wa Hatua ya Timu 64.

    Yanga sasa wanasonga mbele ya Raundi ya Tatu ya michuano hiyo itakayohusisha timu 32 katika kampeni ya kutwaa taji la michuano hiyo kwa Mara ya tano mfululizo.

    KAMATI YA BUNGE YAITA WAWEKEZAJI UJENZI WA VITUO VYA GESI ASILIA ILIYOSHINDILIWA (CNG)

     

    Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, kupitia Mwenyekiti wake Mhe. Subira Mgalu, imetoa wito kwa wawekezaji kuunga mkono Serikali katika ujenzi wa vituo vya gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG) ili kurahisisha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi katika Jiji la Dar es Salaam na mikoa mingine ikiwemo Morogoro na Dodoma.

    Wito huo umetolewa tarehe 19 Februari 2026 wakati Kamati hiyo ilipotembelea Kituo Mama cha Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG) kilichopo eneo la Mlimani jijini Dar es Salaam.

    “Tumeona Serikali tayari ina mpango wa kuongeza ujenzi wa vituo hivi kutokana na uhitaji wa wananchi kuendelea kuongezeka pamoja na unafuu unaopatikana ukitumia CNG kwenye vyomvbo vya usafiri kama vile magari na bajaji, kwani gharama zinapungua kwa asilimia 40 ukilinganisha na mafuta. Hii hii ni fursa kwa sekta binafsi kushirikiana na Serikali kujenga vituo vingi zaidi,” amesema Mhe. Mgalu

    Aidha, kamati hiyo imetoa wito kwa Serikali kufunga mfumo wa CNG katika magari yake, jambo litakalosaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa vyombo hivyo vya usafiri.

    Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini pia imeipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa uwekezaji inaoufanya katika ujenzi wa vituo vya CNG na kupelekea vyombo vya usafiri vipatavyo 15,000 kutumia CNG.


    Vilevile, imepongeza shughuli za utafiti na uendelezaji wa gesi asilia zinazoendelea; ikisema kuwa upatikanaji wa gesi asilia ya kutosha utawezesha kuendelea kuboresha huduma nyinginezo ikiwemo kupikia majumbani na viwandani.

    Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema tangu kuanza kwa vituo vya CNG nchini, Serikali imekuwa ikiona tija yake na ndiyo maana inaongeza kasi ya usogezaji wa huduma hiyo kwa wananchi kwa kuhusisha pia sekta binafsi mfano ukiwa ni uzinduzi wa hivi karibuni wa kituo cha CNG cha Puma kilichopo Salasala ambacho kwa Afrika ndicho kituo kikubwa.

    Amesema Serikali pia katika mwaka huu wa fedha imeagiza magari makubwa matano yatakayobeba gesi asilia iliyoshindiliwa na kuisambaza katika vituo vilivyopo katika maeneo ya mbali ikiwemo Dodoma, Morogoro, Arusha na Tanga, lengo likiwa ni kuhakikisha huduma hiyo inapatikana kutoka eneo moja kwenda jingine.

    Kuhusu kubadilisha mfumo wa magari ya Serikali kwenda kwenye CNG, ameeleza kuwa, tayari Serikali imeanza kufanyia kazi suala hilo na moja ya vielelezo ni mabasi mapya ya mwendo kasi ambayo yote yanatumia mfumo wa CNG, jambo ambalo limefanya utoaji wa huduma kwa abiria kuboreka.

    Kituo cha CNG Mlimani kina uwezo wa kujaza gesi asilia kwenye magari 1,200 kwa siku huku kikiwa na pampu maalum tatu kwa ajili ya kujaza magari maalum ya kusafirisha CNG kwenda kwenye vituo vidogo vya kujaza gesi kwenye magari (Offline CNG Filling Stations), viwandani, katika taasisi na majumbani.

    Wednesday, February 18, 2026

    SIMBA SC YACHUMPA RAUNDI YA TATU KOMBE LA CRDB, KMC NJE

     


    VIGOGO, Simba SC wamefanikiwa kwenda Raundi ya Tatu ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), michuano inayodhaminiwa na Benki ya CRDB baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Greenland ya Kagera usiku huu Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam.

    Mabao ya Simba SC yamefumgwa na Baraka Mwangosi dakika ya 13, beki Anthony Mligo dakika ya 45’+3 na kiungo wa Kimataifa wa Afrika Kusini, Neo Maema dakika ya 90.

    Mechi nyingine ya leo Kombela CRDB wenyeji, KMC FC wameaga mashindano baada ya kuchapwa 3-2 na Bandari Tanzania jioni ya Jana Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

    Jumla ya timu 64 zinashiriki hatua hii na leo mabingwa watetezi, Yanga wataanza kampeni yao ya kutetea taji lao hilo kwa mwaka wa tano mfululizo watakapomenyana na mabingwa wa kwanza wa Ligi Kuu ya nchi, Cosmopolitan ya Dar es Salaam pia. 

    WAZIRI MKUU AMALIZA ZIARA TANGA, AAGIZA FAGIO LIPITE MUHEZA

     
    WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemwagiza Waziri wa Nchi (OWM – TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe arudi Halmashauri ya Muheza na kusafisha watumishi wote waliohusika na ubadhirifu wa fedha za mradi wa jengo la ofisi.
    Ametoa agizo hilo jana (Jumanne, Februari 17, 2026) wakati akizungumza na viongozi na watumishi wa Mkoa wa Tanga katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku tano mkoani humo yaliyofanyika kwenye Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).

    “Muheza ndiyo wilaya iliyonidisappoint sana kwa sababu huku kwingine nimekuta upungufu bali kule Muheza ni uharibifu. Mheshimiwa Waziri kesho rudi Muheza, nenda kachukue hatua. Shirikiana na Waziri wa Utumishi, mchukue hatua,” alisisitiza.

    Dkt. Mwigulu amesema kuna baadhi ya vifaa vilinunuliwa lakini havikufika site (eneo la mradi). “Nondo zenye thamani ya shilingi milioni 9.2 zililipwa kwa mzabuni Saifi Store wa Tanga lakini hazikufikishwa site, maana yake zimechepushwa.”
    “Kuna marine boards vipande 192 vyenye thamani ya shilingi milioni 7.8 havikufika site. Wanaohusika ni Mhasibu, Rajab Mushi na Mhandisi Abdalla Jaha na Afisa anayehusika kupokea vifaa.”

    Alisema mbali ya hivyo, kuna malipo mengine ya sh. milioni 4.4 yalifanywa ili kulipia mifuko 3,800 ya saruji lakini mifuko 300 haikufika kwenye eneo la ujenzi. “Afisa manunuzi na Afisa utumishi ambaye alikuwa ni mwenyekiti wa kamati ya mapokezi ya vifaa vya mradi watafutwe hawa pamoja na Mkurugenzi wa Mwanambonde General Enterprises.”

    Waziri Mkuu alisema kuna ukiukwaji wa taratibu za serikali ambao ulifanyika ikiwemo kumlipa mshauri mwelekezi bila ya kuwa na mkataba wowote. “Kuna huyu AG Engineering amelipwa shilingi milioni 98.7 bila kuwa na mkataba. Huyu kalipwa za nini? Kuna mshauri mwelekezi kalipwa shilingi milioni 11.9 bila mkataba.”

    “Kibaya zaidi, shilingi milioni 343 zimetumika nje ya mradi kwa kulipana posho. Mheshimiwa Waziri nenda kasafishe wote pale. Safisha wote pale hii wilaya ianze upya. Ongea na Waziri wa Utumishi kila mmoja apate adhabu anayostahili,” alisisitiza.
    Kwa ujumla, Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa mkoa huo wakamilishe hoja za sekta mbalimbali zilizoibuliwa na wananchi kwenye wilaya na Halmashauri zote alizopita. “Wakuu wa Wilaya wafanye ziara katika kata na kusikiliza kero za wananchi. Wao wanataka kusikia majibu ya serikali. Wanataka jambo lao litatuliwe na serikali.”

    Mapema, Mkuu wa Mkoa Tanga, Dkt. Batilda Burian alimshukuru Waziri Mkuu kwa kufanya ziara kwenye wilaya zote saba za mkoa huo, Halmashauri 11 na majimbo 12 ambako alikagua na kuzindua miradi yenye thamani ya sh. bilioni 751.

    “Ziara yako ni darasa ambalo limetupa namna mpya ya kuwatumikia wananchi. Sisi tunabaki na kauli yako kwamba tusizoee matatizo ya wananchi, tutaifanyia kazi kwa kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi,” alisema.

    Tuesday, February 17, 2026

    MTUNZI WA TANZANIA YETU MZEE STEVEN HIZZA AFARIKI DUNIA TANGA

     


    Mwanamuziki mkongwe nchini Tanzania, Mzee Steven Hizza, aliyepata umaarufu mkubwa kupitia wimbo wa kizalendo wa “Tanzania Yetu Ndiyo Nchi ya Furaha,” amefariki dunia jioni ya Jumatatu, tarehe 16 Februari 2026, katika eneo la Mwanzange, jijini Tanga.

    Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na watu wa karibu wa familia, wakieleza kuwa msanii huyo mkongwe amefariki akiwa nyumbani kwake Mwanzange, ambako aliishi kwa muda mrefu baada ya kustaafu rasmi jukwaani.

    Mzee Hizza anakumbukwa kama miongoni mwa wanamuziki waliotumia kipaji chao kuhubiri uzalendo, mshikamano wa kitaifa na mapenzi kwa nchi. Wimbo wake maarufu wa “Tanzania Yetu Ndiyo Nchi ya Furaha” uliwahi kutamba katika vipindi mbalimbali vya redio na matukio ya kitaifa, ukiimbwa pia mashuleni na katika sherehe za kitaifa kama sehemu ya kuhamasisha ari ya uzalendo kwa vizazi vipya.

    Katika historia ya muziki wa Tanzania, Mzee Hizza alijijengea heshima kama msanii wa maadili, aliyeamini kuwa muziki ni chombo cha kuelimisha na kuunganisha jamii. Mbali na wimbo huo maarufu, alishiriki pia katika matamasha ya kitaifa na shughuli za kijamii zilizolenga kuhamasisha amani, umoja na maendeleo.

    Wadau wa muziki wanamkumbuka kwa sauti yake ya kipekee na mashairi yenye ujumbe mzito yaliyoakisi uzalendo wa dhati. Kwa miaka mingi, kazi zake zimeendelea kurushwa hewani na kubaki sehemu ya kumbukumbu muhimu ya muziki wa kizazi cha zamani uliobeba maadili na utambulisho wa Taifa.

    Mara ya mwisho Mzee Stephen kusikika ilikuwa ni mwaka 2011 alipohojiwa kipindi Tanzania ilipokuwa ikitimiza miaka 50 ya uhuru.

    Kifo chake kinaacha pengo kubwa katika tasnia ya muziki wa kizalendo nchini, huku wengi wakiamini kuwa mchango wake utaendelea kuishi kupitia kazi zake zilizogusa mioyo ya Watanzania wengi.

    Hadi sasa, taarifa rasmi kuhusu chanzo cha kifo chake pamoja na ratiba ya mazishi zinatarajiwa kutolewa na familia pamoja na viongozi wa tasnia ya muziki nchini.

    • RAIS ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI


    Wakati huo huo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ametuma salamu zake za rambirambi kwa nguli huyo akisema:-

    "Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mzee Steven Hiza, nguli wa muziki na mtunzi wa wimbo, “Tanzania Yetu.”


    Tunatambua na tutaendelea kuenzi mchango wake mkubwa katika sekta ya muziki, ambapo wimbo wake wa Tanzania Yetu umeipamba nchi yetu, umetukumbusha wajibu wetu kwa Taifa letu, umetuelimisha na kutuburudisha kwa takribani miaka 60 sasa.


    Ninawaombea subra na uvumilivu familia, ndugu, jamaa, marafiki na wote walioguswa na msiba huu. Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. 


    Amina.

    Nukuu ya Rais wetu mpendwa Mhe.dkt.Samia Suluhu Hassan

    KILI TRUST YAANDAA WARSHA KUWAJENGEA UWEZO WANUFAIKA WAKE ILI KUIMARISHA UWAJIBIKAJI NA UHAKIKI WA KINA

    Kwa uongozi wa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. Omar Sukari (aliesimama pichani), wadau (ikiwemo GGML, TACAIDS, LGAs, na washirika wengine)  wanaratibu mbinu zitakazokuwa za kijamii, endelevu na zenye matokeo yanayopimika.


    Mwanza, Tanzania

    Geita Gold Mining Limited kupitia mpango wake wa Kilimanjaro Challenge Against HIV and AIDS Trust (Kili Trust) imeandaa warsha ya kuwajengea uwezo wanufaika wake, inayofanyika jijini Mwanza kuanzia Februari 16–20, 2026. Warsha hiyo inawakutanisha wanufaika, wadau wa utekelezaji, washirika na wadhamini kwa lengo la kuimarisha utawala bora, uwajibikaji wa kifedha na kuongeza matokeo chanya ya programu.



    Warsha hii ni hatua muhimu ya kiutawala kabla ya utoaji wa fedha kupitia Kili Grants Portfolio ya mwaka 2024/2025, inayolenga kusaidia miradi ya uwezeshaji wa kiuchumi, uimarishaji wa afya za jamii na mipango endelevu. Kupitia mpa…


    Majadiliano ya kimkakati yakiendelea ili kubuni afua mahsusi zitakazowafikia wachimbaji wadogo katika Mkoa wa Geita, kundi lenye changamoto na hatari za kipekee katika mapambano dhidi ya VVU.

    MSIBA WA ASKARI WA USALAMA BARABARANI WAACHA SIMANZI MWANZA

     

    Na, Ernest Magashi

    Jijini Mwanza kumeghubikwa na simanzi kufuatia kifo cha askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Koplo wa Polisi (CPL) Tumsifu Wilson Kileo (F7768), ambaye mwili wake umeagwa na mamia ya waombolezaji kabla ya kusafirishwa kwenda Lyamungo mkoani Kilimanjaro kwa mazishi.Marehemu alifariki dunia baada ya kugongwa na daladala iliyopoteza mwelekeo wakati akiwa kazini akiongoza magari na kusimamia usalama barabarani. Ajali hiyo ilitokea Februari 10, 2026 majira ya saa 2:00 asubuhi katika mzunguko wa Mwanza Hotel katikati ya Jiji la Mwanza.Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Buhongwa, Lucas Baskely, aliyeongoza ibada ya kuuaga mwili wa marehemu, aliwataka madereva kuacha uzembe barabarani na kutotumia vyombo vya moto kama silaha ya kuhatarisha maisha ya wengine. Alisisitiza kuwa hakuna safari iliyo na thamani kuliko uhai wa binadamu.Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Wilbrod Mutafungwa, alitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, akieleza kuwa CPL Tumsifu alikuwa askari mwenye nidhamu, weledi wakati wote kazini, ambaye Jeshi la Polisi bado lilikuwa linamuhitaji katika kulinda usalama wa raia na mali zao.Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda, Februari 16, 2026 aliongoza mamia ya maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali pamoja na wananchi katika kuuaga mwili wa marehemu. CPL Tumsifu alifariki dunia Februari 13, 2026 katika hospitali ya Rufaa Bugando alipokuwa akipatiwa matibabu.Akizungumza na waombolezaji, Mkuu huyo wa Mkoa aliwahimiza askari na wananchi kuenzi maisha ya marehemu kwa kuendeleza mema aliyoyaacha katika kulitumikia Jeshi la Polisi na jamii kwa ujumla.