ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, March 18, 2026

SALA YA EID KWA NGAZI YA MKOA KUFANYIKA NYAMAGANA.

 


Baraza Kuu la Waislam Mkoa wa Mwanza limetangaza kuwa Swala ya Eid itafanyika kimkoa katika Uwanja wa Nyamagana uliopo Wilaya ya Nyamagana, Mkoa wa Mwanza.


Katika taarifa hiyo, Waislam wote mkoani Mwanza wanaombwa kuhudhuria swala hilo kwa pamoja ili kushiriki ibada hiyo muhimu ya sikukuu.


Baraza hilo limehimiza umoja, mshikamano na nidhamu wakati wa ibada hiyo, pamoja na kuzingatia maelekezo yatakayotolewa na viongozi wa dini na mamlaka husika.

VIKUNDI 41 VIJANA, WANAWAKE NA WATU WENYE ULEMAVU VYANUFAIKA NA MIKOPO YA ASILIMIA 10 ILEMELA

 


Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza , Amir Mkalipa, amevitaka vikundi vilivyopata mikopo ya asilimia 10 katika wilaya hiyo kuhakikisha vinarejesha fedha hizo kwa wakati ili kutoa fursa kwa vikundi vingine kunufaika na mpango huo.


Akizungumza hii leo wakati wa hafla ya utoaji wa mikopo hiyo iliyofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Mkalipa amesema kuwa halmashauri itafuatilia kwa karibu vikundi vyote vilivyopata mikopo ili kuhakikisha vinarejesha kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa.


Aidha, Mkalipa amewataka maafisa maendeleo wa kata kutoa elimu mara kwa mara kwa vikundi hivyo pamoja na kuvitembelea ili kubaini mapema vikundi vinavyosuasua katika marejesho, na kuchukua hatua stahiki kwa wakati.


Kwa upande wake, Meya wa Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Bi. Salah Ngw'ani, ameishukuru halmashauri hiyo kwa utoaji wa mikopo hiyo, akisema kuwa itakuwa chachu ya maendeleo kwa wakazi wa wilaya hiyo.


Jumla ya vikundi 41 vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu katika wilaya ya ilemela vimenufaika na mikopo hiyo  ya alimia 10 yenye thamani ya shilingi milioni 463.

YANGA SC YAAMBULIA SULUHU NYINGINE KWA TRA UNITED ARUSHA

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wametoa sare ya bila kufungana na wenyeji, TRA United katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania jioni ya leo Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha.

TRA United ilicheza pungufu kwa dakika 10 za mwisho kufuatia kiungo wake, Muzamil Yassin Selemba kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 76 baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano.

 

Majeruhi bado yanaiandama Yanga huku Dube na beki wa kulia Israel Mwenda wote wakitoka uwanjani kutokana na kugongana. Sare hiyo inaifanya Yanga ibaki kileleni kwa pointi zake 37, tisa mbele ya Azam inayoshika nafasi ya pili na JKT Tanzania inayoshika nafasi ya tatu, wakiwa na pointi 28 kila mmoja, huku Simba wakishika nafasi ya nne kwa pointi 27 nayo TRA nafasi ya 10.


Huu unakuwa mchezo wa pili mfululizo kwa Yanga wa ligi bila bao, kufuatia sare ya 0-0 dhidi ya Azam wikendi iliyopita. Baada ya mechi 15 za mzunguko wa kwanza, Yanga imeshinda 11 na kutoa sare nne, huku ikiwa haijafungwa.


Azam wamecheza mechi 14, mechi inayofuata dhidi ya Mashujaa mjini Kigoma kesho, huku Simba wakicheza mechi yao ya 13 dhidi ya Pamba ya Jiji, hiyo ikimaanisha kuonyesha kwa nguvu kwenye michezo hii kunaweza kuwafanya kupunguza pengo la pointi moja tu nyuma ya wapinzani wao hao wa jadi.


SENEGAL WAVULIWA UBINGWA WA AFCON, MOROCCO WAPEWA USHNDI WA 3-0

 


BODI ya Rufaa ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) imeivua Senegal ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) na kuwapa wenyeji, Morocco.

Senegal ilitawazwa kuwa bingwa wa AFCON ya 2025 baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Morocco Januari 18, mwaka huu bao pekee la kiungo wa ulinzi, Pape Alassane Gueye anayechezea Villarreal ya Hispania dakika ya 94 katika mchezo uliodumu kwa dakika 120 Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat.

Hata hivyo, CAF imesema kwamba Senegal imepoteza mechi hiyo na Morocco wamepewa ushindi wa mabao 3-0  kwa kutumia Kifungu cha 84 cha Kanuni za AFCON kwa kitendo chao cha kuondoka uwanjani kupinga Penalti waliyopewa Morocco na kusababisha mchezo kusima akwa dakika 14, kabla ya kurejea kumalizia.

Mshambuliaji Brahim Díaz wa Morocco ambaye yeye mwenyewe alichezewa rafu na beki wa Senegal, El Hadji Malick Diouf – alikwenda kupiga penalti kwa staili ya Panenka bahati mbaya ikaokolewa na kipa Édouard Mendy na kuzima ndoto za Simba wa Atlasi kutwaa taji kwa jasho uwanjani.

Tuesday, March 17, 2026

JPM

Monday, March 16, 2026

MIAKA MITANO TANZANIA BILA JPM

 


Miaka Mitano Siku Zaidi ya Siku 1800 Tangu kifo cha Rais Wa Awamu ya Tano Hayati Dkt, John Pombe Magufuli 


#kazinangoma ya 93.7 Jembe Fm inaungana na Familia ya Dkt, John Pombe Magufuli na Watanzania wote katika kumbukizi hiyo 

Kuzifungua kurasa za kumbukumbu, mijadala na simulizi.

Kuanzia Leo.

📅 16–17 Machi 2026

📻 93.7 Mwanza


Usikose.  Kusikiliza vipindi mbalimbali kupitia Jembe Fm🔥📻 Na Kutufatilia kwenye mitandao ya kijamii @jembefmtz 


Follow Us On Social Media

‎Instagram - @jembefmtz

‎Facebook - @jembefmtz

‎X(Twitter) - @jembefmtz

‎TikTok - @jembefmtz

‎Thread - @jembefmtz


#AhsanteKwaTime 

#Familiamoja

#10yrsjembefm 


#JembeFMKurasa1800LiveChato

MVUA MOROGORO YASABABISHA VIFO VINNE

 


Mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Morogoro zimesababisha vifo vya watu wanne katika matukio tofauti, huku wengine wakijeruhiwa baada ya kupigwa na radi.

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, SACP Alex Mkama, amesema watu wawili walifariki dunia baada ya kupigwa na radi wakati wa mvua kubwa katika Kijiji cha Kilosa Mpepo wilayani Malinyi.

Amewataja waliofariki kuwa ni Nindi Masele (15) na Marwa Mwanzilwa (2), wote wakazi wa kijiji hicho, waliopoteza maisha usiku wa Machi 13, 2026 wakati mvua kubwa ikiendelea kunyesha.

Aidha, amesema watu wengine wanne wa familia moja walijeruhiwa katika tukio hilo akiwemo Milembe Dase (27), Kulwa Malembe (38), Milembe Samwel (39) pamoja na Ngolo Nchimwe (1), ambao wanaendelea kupatiwa matibabu.

Ndani ya mwezi mmoja uliopita, tukio jingine la radi lilitokea Februari 23 mwaka huu katika Kitongoji cha Mbesi, Kijiji na Kata ya Utengule, Halmashauri ya Mlimba wilayani Kilombero.

Katika tukio hilo, watu wawili Tano Leonard Lunasi (36) na Ngimila Ndombeji Mashana (27), wote wakulima na wakazi wa eneo hilo, walipoteza maisha huku wengine wawili wakijeruhiwa walipokuwa wakirejea nyumbani kutoka matembezini.

Katika tukio jingine, watu wawili Hamis Yahaya Waziri (45), mkulima mkazi wa Kisaye na Nyerere Katebeka Kidagati (50), mfugaji mkazi wa Mkono wa Mara wilayani Morogoro, wamefariki dunia baada ya kusombwa na maji ya mvua.

Kamanda Mkama amesema watu hao walifariki katika kata za Tegetero na Mkambarani walipokuwa wakijaribu kuvuka maeneo yaliyofurika maji lakini walizidiwa nguvu na kusombwa na maji.

KAMATI BUNGE YARIDHISHWA MRADI FARU MWEUSI, MBWA MWITU

 Faru mweusi ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi.Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imesema imeridhishwa na uwekezaji wa mradi wa uhifadhi wa faru mweusi na mbwa mwitu katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, na kuiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na mamlaka husika kuendelea kuwalinda wanyama hao ambao walikuwa hatarini kutoweka.

Akizungumza Machi 15 baada ya kutembelea na kukagua mradi huo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mary Masanja, amesema kamati imefurahishwa na maendeleo ya mradi huo huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwalinda na kuwahifadhi wanyama hao adimu.

Alisema pia ni muhimu kuangalia uwezekano wa kuwahamishia faru katika hifadhi nyingine kadri idadi yao inavyozidi kuongezeka, ili kuwapa nafasi zaidi ya kuishi na kuongeza fursa kwa watalii kuwaona katika maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini.

“Mradi kwa sasa unaridhisha na ukizingatia kwamba faru ni mnyama aliyekuwa kwenye hatari ya kutoweka. Tunaendelea kuwaalika wananchi watembelee hifadhi hii, na kikubwa tumeielekeza Wizara kuwa mradi huu unahitaji matunzo endelevu. Pale ambapo idadi ya faru itaongezeka, waweze kusambazwa katika hifadhi nyingine ili watalii wanaotembelea maeneo hayo waweze kuwaona kwa urahisi zaidi,” alisema Masanja.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Hassan Abbasi, alisema mradi huo wa faru uliogharimu zaidi ya shilingi bilioni 3.4 unalenga kuwahifadhi wanyama hao adimu ili waweze kuzaliana na kulinda urithi wa taifa.

Alisema pamoja na juhudi za uhifadhi, mradi huo pia umeongeza thamani ya utalii katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, kwani watalii sasa wanaweza kufika katika eneo maalumu lenye uzio wa umeme na kupata fursa ya kuwaona faru kwa ukaribu zaidi.

“Kamati wameridhishwa na mradi huu na kutupa maelekezo ya kuendelea kuwalinda wanyama hawa pamoja na kuboresha zaidi mradi huu. Faru waliopo katika mradi huu wamefikia idadi ya 50, hivyo eneo la sasa linaanza kuwa finyu. Kamati imesisitiza kuongeza eneo la uzio, na sisi pamoja na mamlaka husika tunakwenda kulifanyia kazi kwa haraka ili wanyama wapate eneo kubwa zaidi la kuishi na utalii uendelee kuimarika,” alisema Abbasi.

Aidha, aliongeza kuwa Wizara pia inapanga kuongeza magari kwa ajili ya kuwahudumia watalii wanaotembelea eneo la faru pamoja na hifadhi kwa ujumla, kutokana na ongezeko kubwa la watalii wanaotembelea Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, hususan wale wanaokuja kuona faru.

Kwa upande wake, mjumbe wa kamati hiyo, Asia Halamga, alisema juhudi za Serikali zimewezesha kuongezeka kwa wanyama waliokuwa adimu kama faru na mbwa mwitu katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi.

Alitoa wito kwa Watanzania kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini ili kufurahia na kuthamini urithi wa rasilimali za asili uliopo Tanzania.

YANGA SC YAAMBULIA SULUHU DHIDI YA AZAM FC

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wamelazimishwa sare ya bila mabao na Azam FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku wa Jumapili ya tarehe 15 Machi 2026, Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Kwa matokeo hayo, Yanga SC inafikisha pointi 36 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 28 baada ya timu zote kucheza mechi 14.

Friday, March 13, 2026

DARAJA LA RUHEMBE LAKATIKA SAFARI ZASIMAMA

Daraja la Ruhembe. Wananchi wanaotumia barabara ya Mikumi kuelekea Ifakara, Ulanga, Mlimba na Malinyi wamelazimika kusitisha kwa mara nyingine safari baada ya Daraja la Ruhembe lililopo wilayani Kilosa mkoani Morogoro kuharibika kwa kukatika kingo zake.

Taarifa zinaeleza kuwa tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Machi 13 na kusababisha magari pamoja na vyombo vingine vya usafiri kushindwa kupita katika eneo hilo.

Barabara hiyo ni kiungo muhimu kwa wakazi wa wilaya za Kilosa, Kilombero, Ulanga pamoja na Malinyi ambao hutegemea njia hiyo kusafirisha abiria na bidhaa mbalimbali.
Kutokana na hali hiyo, wananchi wamelazimika kusubiri hatua za dharura huku baadhi yao wakitumia njia mbadala kufikia maeneo yao.

Awali daraja jingine katika barabara hiyo eneo la Kijiji cha Mhenda lilikatika  Kingo zake usiku wa kuamkia Machi 09 mwaka huu ambapo Uongozi wa Mkoa wa Morogoro uliwataka wataalamu wa wakala wa barabara TANROADS kuchukua hatua za haraka kujenga kivuko cha muda ili kurahisisha wananchi kuvuka kwa miguu wakati jitihada za kurekebisha daraja la kudumu zikiendelea.

Thursday, March 12, 2026

TATHIMINI YA ZOEZI LA UHAMAJI WA HIARI WA WAKAZI WA ENEO LA HIFADHI YA NGORONGORO

 

Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka akizungumza katika hafla ya kupokea Taarifa za Tume ya Rais ya Kutathmini Mgogoro wa Ardhi katika Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Tume ya Rais ya Kutathmini Zoezi la Uhamaji wa Hiari wa Wakazi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, tarehe 12 Machi, 2026.

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kutathmini Zoezi la Uhamaji wa Hiari wa Wakazi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Katibu Mkuu Mstaafu, Mhandisi Musa Iyombe akizungumza na kukabidhi Taarifa ya Tume hiyo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, tarehe 12 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kwenye hafla ya kupokea Taarifa za Tume ya Rais ya Kutathmini Mgogoro wa Ardhi katika Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Tume ya Rais ya Kutathmini Zoezi la Uhamaji wa Hiari wa Wakazi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 12 Machi, 2026.

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kutathmini Masuala ya Ardhi katika Wilaya ya Ngorongoro, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani Dkt. Gerald Ndika akizungumza na kukabidhi Taarifa ya Tume hiyo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma, tarehe 12 Machi, 2026.
Rais Dk Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wananchi katika utekelezaji wa mapendekezo ya Tume za Rais kuhusu mgogoro wa ardhi na uhamaji wa hiari Ngorongoro kwa maslahi yao na nchi kwa ujumla.

Samia ametoa kauli hiyo, leo Alhamisi Machi 12, 2026, wakati wa hotuba yake, katika hafla ya kupokea taarifa ya Tume za Rais kuhusu mgogoro wa ardhi na uhamaji wa hiari, Ngorongoro.

“Tumesikia kwamba Serikali tulifanya kwa nia njema lakini tulikosea baadhi ya maeneo na hayo ndio ya kukaa kutafakari na kuona namna ya kurekebisha,” amesema.

Amesema ni matumaini yake mapendekezo yaliyomo ndani ya taarifa hiyo, yataiongoza Serikali kupata namna bora ya kushughulikia jambo hilo kwa maslahi ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Ameitaka Ofisi ya Waziri Mkuu isimamie utekelezaji wa mapendekezo hayo na yaratibiwe kwa kushirikiana na Katibu Mkuu Kiongozi.

Amesema anatambua mchakato wa utekelezaji wa baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na tume unaweza kuibua mitazamo tofauti katika jamii hasa kutoka kwa wale wanaofaidika.



PROFESA KABUDI ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA JUMUIYA YA MADOLA JIJINI LONDON.

LONDON-Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba Kabudi, ameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Jumuiya ya Madola yaliyofanyika jijini London, Uingereza, yakihusisha nchi wanachama 56 wa jumuiya hiyo.
Sherehe hiyo ilijumuisha matukio mbalimbali, ikiwemo hafla ya kupandisha bendera katika Bunge la Uingereza, uwekaji wa shada la maua katika Milango ya Kumbukumbu ya Jumuiya ya Madola, pamoja na ibada ya waumini wa dini mbalimbali iliyofanyika katika Kanisa la Westminster Abbey.
Kaulimbiu ya mwaka huu ilikuwa “Kufungua Fursa kwa Ajili ya Jumuiya ya Madola Yenye Mafanikio,” ikilenga kuhimiza diplomasia, kubadilishana tamaduni na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola.

Hafla hiyo pia iliwakutanisha wanadiplomasia, mawaziri, viongozi wa kimataifa pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo, waliotafakari kuhusu mshikamano wa muda mrefu wa Jumuiya ya Madola na umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kukuza maendeleo endelevu. huku ikichangia kuimarisha sauti na ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya kimataifa.

Wednesday, March 11, 2026

MPANZU ATOKEA BENCHI SINGIDA NA KUIPA POINTI TATU SIMBA SC

 


TIMU ya Simba SC imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars katika mchezo wa Ligi Ali ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Mwigulu Airtel mkoani Singida.

Pongezi kwa winga kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Elie Mpanzu Kibisawala aliyeifungia bao la ushindi Simba SC dakika ha 84 akimalizia pasi nzuri ya kiungo Mzambia, Clatous Chotta Chama.

Mpanzu alifunga bao hilo dakika tano tu tangu aingie kuchukua nafasi ya kiungo kutoka Kongo-Brazzaville, Inno Jospin Loemba.

Hadi mapumziko timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1 winga wa kushoto, Muivory Coast, Alain Anicet Oura akianza kuifungia Simba dakika ya saba, kabla ya winga wa kulia, Mossi Nduwumwe kuisawazishia Singida Black Stars dakika ya 38.

Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 27 na kusogea nafasi ya pili ilizidiwa pointi tano na mabingwa watetest, Yanga baada ya wote kucheza mechi 12, wakati Singida Black Stars inabaki na pointi zake 19 za mechi 13 sasa na kushuka kwa nafasi moja hadi ya 10.

RAIS SAMIA AMUASILI MTOTO MCHANGA ALIYETELEKEZWA NZEGA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemuasili mtoto mchanga wa kike leo tarehe 11 Machi, 2026, katika makazi yake, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.


Mtoto huyo aliyepewa jina la Grace Samia Suluhu Hassan alitelekezwa mjini Nzega, mkoani Tabora, na amekabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai.


Akizungumza wakati wa kumkabidhi mtoto huyo, Mkuu wa Wilaya Tukai alisema mtoto huyo aliokotwa tarehe 17 Januari, 2026 akiwa ametelekezwa katika eneo jirani na nyumba ya wageni ya Kasulu, Nzega Mjini. 


Alieleza kuwa baada ya kupokea taarifa hizo, alishirikiana na Jeshi la Polisi kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitalini kwa uchunguzi na uangalizi, huku juhudi za kumtafuta mama yake zikiendelea bila mafanikio.


Rais Dkt. Samia amemkaribisha mtoto huyo katika familia yake na kuahidi kumpatia malezi, ulinzi na huduma zote muhimu ili akue katika mazingira salama na yenye upendo.


“Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina, na hatuijui kesho yake,” alisema Rais Dkt. Samia.

Profesa Kabudi akutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Canada

 LONDON-Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof Paramagamba Kabudi, amefanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Canada, Mhe. Rober Oliphant..

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Machi 8, 2026.

Viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kati ya Tanzania na Canada pamoja na kuendeleza uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola kwa kuzingatia misingi na tunu za jumuiya hiyo katika kukuza ushirikiano na maendeleo ya pamoja.
Aidha,viongozi hao wamebainisha kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Canada umejengwa juu ya msingi wa urafiki wa kihistoria, ushirikiano wa kiuchumi pamoja na uanachama wao ndani ya Jumuiya ya Madola, hali inayofungua fursa zaidi za kupanua ushirikiano katika nyanja za biashara, uwekezaji na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Pia, viongozi hao wameangazia mchango wa diaspora wa Tanzania na Canada katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi zao.

Walieleza kuwa kupitia uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola, diaspora imeendelea kuwa kiungo muhimu kinachoimarisha uhusiano wa watu kwa watu na kufungua fursa zaidi za ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.
Katika mazungumzo hayo, Prof. Kabudi aliambatana na Mshauri wa Rais katika Masuala ya Diplomasia, Balozi Lazaro Nyalandu; Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki; pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Noel Kaganda.