ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, February 18, 2026

SIMBA SC YACHUMPA RAUNDI YA TATU KOMBE LA CRDB, KMC NJE

 


VIGOGO, Simba SC wamefanikiwa kwenda Raundi ya Tatu ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), michuano inayodhaminiwa na Benki ya CRDB baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Greenland ya Kagera usiku huu Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam.

Mabao ya Simba SC yamefumgwa na Baraka Mwangosi dakika ya 13, beki Anthony Mligo dakika ya 45’+3 na kiungo wa Kimataifa wa Afrika Kusini, Neo Maema dakika ya 90.

Mechi nyingine ya leo Kombela CRDB wenyeji, KMC FC wameaga mashindano baada ya kuchapwa 3-2 na Bandari Tanzania jioni ya Jana Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Jumla ya timu 64 zinashiriki hatua hii na leo mabingwa watetezi, Yanga wataanza kampeni yao ya kutetea taji lao hilo kwa mwaka wa tano mfululizo watakapomenyana na mabingwa wa kwanza wa Ligi Kuu ya nchi, Cosmopolitan ya Dar es Salaam pia. 

WAZIRI MKUU AMALIZA ZIARA TANGA, AAGIZA FAGIO LIPITE MUHEZA

 
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemwagiza Waziri wa Nchi (OWM – TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe arudi Halmashauri ya Muheza na kusafisha watumishi wote waliohusika na ubadhirifu wa fedha za mradi wa jengo la ofisi.
Ametoa agizo hilo jana (Jumanne, Februari 17, 2026) wakati akizungumza na viongozi na watumishi wa Mkoa wa Tanga katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku tano mkoani humo yaliyofanyika kwenye Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).

“Muheza ndiyo wilaya iliyonidisappoint sana kwa sababu huku kwingine nimekuta upungufu bali kule Muheza ni uharibifu. Mheshimiwa Waziri kesho rudi Muheza, nenda kachukue hatua. Shirikiana na Waziri wa Utumishi, mchukue hatua,” alisisitiza.

Dkt. Mwigulu amesema kuna baadhi ya vifaa vilinunuliwa lakini havikufika site (eneo la mradi). “Nondo zenye thamani ya shilingi milioni 9.2 zililipwa kwa mzabuni Saifi Store wa Tanga lakini hazikufikishwa site, maana yake zimechepushwa.”
“Kuna marine boards vipande 192 vyenye thamani ya shilingi milioni 7.8 havikufika site. Wanaohusika ni Mhasibu, Rajab Mushi na Mhandisi Abdalla Jaha na Afisa anayehusika kupokea vifaa.”

Alisema mbali ya hivyo, kuna malipo mengine ya sh. milioni 4.4 yalifanywa ili kulipia mifuko 3,800 ya saruji lakini mifuko 300 haikufika kwenye eneo la ujenzi. “Afisa manunuzi na Afisa utumishi ambaye alikuwa ni mwenyekiti wa kamati ya mapokezi ya vifaa vya mradi watafutwe hawa pamoja na Mkurugenzi wa Mwanambonde General Enterprises.”

Waziri Mkuu alisema kuna ukiukwaji wa taratibu za serikali ambao ulifanyika ikiwemo kumlipa mshauri mwelekezi bila ya kuwa na mkataba wowote. “Kuna huyu AG Engineering amelipwa shilingi milioni 98.7 bila kuwa na mkataba. Huyu kalipwa za nini? Kuna mshauri mwelekezi kalipwa shilingi milioni 11.9 bila mkataba.”

“Kibaya zaidi, shilingi milioni 343 zimetumika nje ya mradi kwa kulipana posho. Mheshimiwa Waziri nenda kasafishe wote pale. Safisha wote pale hii wilaya ianze upya. Ongea na Waziri wa Utumishi kila mmoja apate adhabu anayostahili,” alisisitiza.
Kwa ujumla, Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa mkoa huo wakamilishe hoja za sekta mbalimbali zilizoibuliwa na wananchi kwenye wilaya na Halmashauri zote alizopita. “Wakuu wa Wilaya wafanye ziara katika kata na kusikiliza kero za wananchi. Wao wanataka kusikia majibu ya serikali. Wanataka jambo lao litatuliwe na serikali.”

Mapema, Mkuu wa Mkoa Tanga, Dkt. Batilda Burian alimshukuru Waziri Mkuu kwa kufanya ziara kwenye wilaya zote saba za mkoa huo, Halmashauri 11 na majimbo 12 ambako alikagua na kuzindua miradi yenye thamani ya sh. bilioni 751.

“Ziara yako ni darasa ambalo limetupa namna mpya ya kuwatumikia wananchi. Sisi tunabaki na kauli yako kwamba tusizoee matatizo ya wananchi, tutaifanyia kazi kwa kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi,” alisema.

Tuesday, February 17, 2026

MTUNZI WA TANZANIA YETU MZEE STEVEN HIZZA AFARIKI DUNIA TANGA

 


Mwanamuziki mkongwe nchini Tanzania, Mzee Steven Hizza, aliyepata umaarufu mkubwa kupitia wimbo wa kizalendo wa “Tanzania Yetu Ndiyo Nchi ya Furaha,” amefariki dunia jioni ya Jumatatu, tarehe 16 Februari 2026, katika eneo la Mwanzange, jijini Tanga.

Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na watu wa karibu wa familia, wakieleza kuwa msanii huyo mkongwe amefariki akiwa nyumbani kwake Mwanzange, ambako aliishi kwa muda mrefu baada ya kustaafu rasmi jukwaani.

Mzee Hizza anakumbukwa kama miongoni mwa wanamuziki waliotumia kipaji chao kuhubiri uzalendo, mshikamano wa kitaifa na mapenzi kwa nchi. Wimbo wake maarufu wa “Tanzania Yetu Ndiyo Nchi ya Furaha” uliwahi kutamba katika vipindi mbalimbali vya redio na matukio ya kitaifa, ukiimbwa pia mashuleni na katika sherehe za kitaifa kama sehemu ya kuhamasisha ari ya uzalendo kwa vizazi vipya.

Katika historia ya muziki wa Tanzania, Mzee Hizza alijijengea heshima kama msanii wa maadili, aliyeamini kuwa muziki ni chombo cha kuelimisha na kuunganisha jamii. Mbali na wimbo huo maarufu, alishiriki pia katika matamasha ya kitaifa na shughuli za kijamii zilizolenga kuhamasisha amani, umoja na maendeleo.

Wadau wa muziki wanamkumbuka kwa sauti yake ya kipekee na mashairi yenye ujumbe mzito yaliyoakisi uzalendo wa dhati. Kwa miaka mingi, kazi zake zimeendelea kurushwa hewani na kubaki sehemu ya kumbukumbu muhimu ya muziki wa kizazi cha zamani uliobeba maadili na utambulisho wa Taifa.

Mara ya mwisho Mzee Stephen kusikika ilikuwa ni mwaka 2011 alipohojiwa kipindi Tanzania ilipokuwa ikitimiza miaka 50 ya uhuru.

Kifo chake kinaacha pengo kubwa katika tasnia ya muziki wa kizalendo nchini, huku wengi wakiamini kuwa mchango wake utaendelea kuishi kupitia kazi zake zilizogusa mioyo ya Watanzania wengi.

Hadi sasa, taarifa rasmi kuhusu chanzo cha kifo chake pamoja na ratiba ya mazishi zinatarajiwa kutolewa na familia pamoja na viongozi wa tasnia ya muziki nchini.

  • RAIS ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI


Wakati huo huo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ametuma salamu zake za rambirambi kwa nguli huyo akisema:-

"Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mzee Steven Hiza, nguli wa muziki na mtunzi wa wimbo, “Tanzania Yetu.”


Tunatambua na tutaendelea kuenzi mchango wake mkubwa katika sekta ya muziki, ambapo wimbo wake wa Tanzania Yetu umeipamba nchi yetu, umetukumbusha wajibu wetu kwa Taifa letu, umetuelimisha na kutuburudisha kwa takribani miaka 60 sasa.


Ninawaombea subra na uvumilivu familia, ndugu, jamaa, marafiki na wote walioguswa na msiba huu. Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. 


Amina.

Nukuu ya Rais wetu mpendwa Mhe.dkt.Samia Suluhu Hassan

KILI TRUST YAANDAA WARSHA KUWAJENGEA UWEZO WANUFAIKA WAKE ILI KUIMARISHA UWAJIBIKAJI NA UHAKIKI WA KINA

Kwa uongozi wa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. Omar Sukari (aliesimama pichani), wadau (ikiwemo GGML, TACAIDS, LGAs, na washirika wengine)  wanaratibu mbinu zitakazokuwa za kijamii, endelevu na zenye matokeo yanayopimika.


Mwanza, Tanzania

Geita Gold Mining Limited kupitia mpango wake wa Kilimanjaro Challenge Against HIV and AIDS Trust (Kili Trust) imeandaa warsha ya kuwajengea uwezo wanufaika wake, inayofanyika jijini Mwanza kuanzia Februari 16–20, 2026. Warsha hiyo inawakutanisha wanufaika, wadau wa utekelezaji, washirika na wadhamini kwa lengo la kuimarisha utawala bora, uwajibikaji wa kifedha na kuongeza matokeo chanya ya programu.



Warsha hii ni hatua muhimu ya kiutawala kabla ya utoaji wa fedha kupitia Kili Grants Portfolio ya mwaka 2024/2025, inayolenga kusaidia miradi ya uwezeshaji wa kiuchumi, uimarishaji wa afya za jamii na mipango endelevu. Kupitia mpa…


Majadiliano ya kimkakati yakiendelea ili kubuni afua mahsusi zitakazowafikia wachimbaji wadogo katika Mkoa wa Geita, kundi lenye changamoto na hatari za kipekee katika mapambano dhidi ya VVU.

MSIBA WA ASKARI WA USALAMA BARABARANI WAACHA SIMANZI MWANZA

 

Na, Ernest Magashi

Jijini Mwanza kumeghubikwa na simanzi kufuatia kifo cha askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Koplo wa Polisi (CPL) Tumsifu Wilson Kileo (F7768), ambaye mwili wake umeagwa na mamia ya waombolezaji kabla ya kusafirishwa kwenda Lyamungo mkoani Kilimanjaro kwa mazishi.Marehemu alifariki dunia baada ya kugongwa na daladala iliyopoteza mwelekeo wakati akiwa kazini akiongoza magari na kusimamia usalama barabarani. Ajali hiyo ilitokea Februari 10, 2026 majira ya saa 2:00 asubuhi katika mzunguko wa Mwanza Hotel katikati ya Jiji la Mwanza.Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Buhongwa, Lucas Baskely, aliyeongoza ibada ya kuuaga mwili wa marehemu, aliwataka madereva kuacha uzembe barabarani na kutotumia vyombo vya moto kama silaha ya kuhatarisha maisha ya wengine. Alisisitiza kuwa hakuna safari iliyo na thamani kuliko uhai wa binadamu.Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Wilbrod Mutafungwa, alitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, akieleza kuwa CPL Tumsifu alikuwa askari mwenye nidhamu, weledi wakati wote kazini, ambaye Jeshi la Polisi bado lilikuwa linamuhitaji katika kulinda usalama wa raia na mali zao.Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda, Februari 16, 2026 aliongoza mamia ya maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali pamoja na wananchi katika kuuaga mwili wa marehemu. CPL Tumsifu alifariki dunia Februari 13, 2026 katika hospitali ya Rufaa Bugando alipokuwa akipatiwa matibabu.Akizungumza na waombolezaji, Mkuu huyo wa Mkoa aliwahimiza askari na wananchi kuenzi maisha ya marehemu kwa kuendeleza mema aliyoyaacha katika kulitumikia Jeshi la Polisi na jamii kwa ujumla.

DC AWATAKA MADIWANI KUHAMASISHA WAZAZI KUPELEKA WATOTO SHULENI KABLA YA KUANZA MUSAKO

 

Na, Ernest Magashi

Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe mkoani Geita wametakiwa kuhamasisha wazazi na walezi kuhakikisha watoto waliofikia umri wa kuanza shule wanaripoti kwa wakati, kabla ya kuanza kwa msako wa kuwachukulia hatua wazazi watakaokaidi agizo hilo.Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Mhadis Paskas Mragili, wakati akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani. Amesema amepokea taarifa kuwa kasi ya uandikishaji na uripoti wa wanafunzi, hususan wa darasa la awali, darasa la kwanza na kidato cha kwanza, bado hairidhishi.Ameeleza kuwa idadi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza walioripoti shuleni iko chini ya asilimia 80 ukilinganisha na idadi ya waliofaulu darasa la saba mwaka jana.“Waheshimiwa madiwani, nawaombeni sana muhamasishe wazazi na walezi wapeleke watoto shule. Tumeanza mwaka vizuri tangu shule zilipofunguliwa Januari 2026, lakini mwitikio wa darasa la awali, la kwanza na kidato cha kwanza bado ni mdogo. Kuanzia wiki ijayo, kila mzazi au mlezi mwenye mtoto aliyeandikishwa na hajafika shule atachukuliwa hatua kupitia serikali za vijiji na kata,” alisisitiza Mragili.Aliongeza kuwa Serikali imeboresha miundombinu ya kujifunzia na inaendelea kutekeleza Sera ya Elimu Bila Malipo, hivyo jukumu la mzazi ni kuhakikisha mtoto anapata haki yake ya elimu. Alionya kuwa Serikali haitavumilia kuona watoto wanabaki nyumbani bila sababu za msingi, na wazazi watakaobainika watawajibishwa kwa mujibu wa sheria.Mkuu huyo wa wilaya alisema licha ya Bukombe kufanya vizuri kitaaluma mkoani Geita, juhudi zaidi zinahitajika kuhakikisha wanafunzi wote wanaripoti shuleni ili kufikia lengo la Serikali la kutoa elimu bora kwa kila mtoto.Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Bukombe na Naibu Waziri Mkuu Mstaafu, Dkt. Doto Biteko, aliwapongeza wataalamu wa idara mbalimbali, hususan za elimu ya msingi na sekondari, kwa juhudi zao zilizoifanya wilaya hiyo kushika nafasi ya kwanza kimkoa katika matokeo ya mitihani.

Dkt. Biteko aliwahimiza madiwani na wataalamu kuendelea kushirikiana katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhamasisha wazazi kusomesha watoto wao ili kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ambayo imeendelea kupeleka fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo, ikiwemo sekta ya elimu.Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Adelina Mfikwa, aliahidi kuwa wataalamu wataendelea kushirikiana na madiwani kuhakikisha malengo ya elimu yanafikiwa.Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri, Erick Kagoma, aliwataka madiwani kwenda kufanya mikutano ya hadhara katika maeneo yao kuhamasisha wazazi na walezi kupeleka watoto shule kabla ya kuanza rasmi kwa msako huo.

Saturday, February 14, 2026

MAHUNDI : SAYANSI NI SULUHUSHO LA AJIRA KWA WASICHANA


Naibu Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhandisi Maryprisca Mahundi, amewahimiza wanafunzi wa kike nchini kuwekeza juhudi katika masomo ya Sayansi, akisisitiza kuwa kusoma masomo hayo ni njia muhimu ya kupambana na tatizo la ukosefu wa ajira.


Naibu Waziri Mahundi ameyasema hayo leo, Februari 11, 2026, wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake na Wasichana Katika Sayansi, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.

“Watoto wa kike, ninawaambia kusoma Sayansi inawezekana. Ukifaulu vizuri, itakuwa msaada mkubwa katika mapambano ya kujenga taifa,” amesema Naibu Waziri Mahundi.


Ameongeza kuwa jukumu kuu la wizara ni kuhakikisha wanawake na wasichana wanahamasishwa na kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Sayansi, kupitia maboresho ya sera na miongozo inayowarahisishia kushiriki ipasavyo katika fursa za maendeleo ya Sayansi.


Aidha, Naibu Waziri Mahundi amesisitiza kuwa wanapowahimiza wasichana kusoma Sayansi, wizara haimuachii nyuma mtoto wa kiume, ili kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza za kutowapa fursa sawa watoto wa kiume katika nyanja za elimu na Sayansi.




RAIS SAMIA ASHIRIKI MKUTANO WA WAKUU WA NCHI WA UMOJA WA AFRIKA MJINI ADDIS ABABA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika ambao unaongozwa na Kaulimbiu ya Mwaka 2026 inayosema: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Huduma Salama za Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza hatua za pamoja za bara katika kuhakikisha usalama wa rasilimali maji, afya ya jamii, na maendeleo endelevu.

NA ALBERT G.SENGO

Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika kwa mwaka 2026 umeongozwa na kaulimbiu isemayo, “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Huduma Salama za Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063"


Kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza hatua za pamoja barani Afrika katika kulinda rasilimali maji, kuboresha afya za wananchi na kuhakikisha maendeleo endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa Tanzania, ajenda hii inaleta manufaa makubwa katika nyanja mbalimbali.

Kidiplomasia, ushiriki wa Tanzania katika utekelezaji wa ajenda ya maji na usafi wa mazingira unaimarisha nafasi ya nchi katika majukwaa ya kikanda na kimataifa. Pia unatoa fursa ya kupanua ushirikiano kupitia jumuiya za kikanda kama Jumuiya ya Afrika Mashariki, hususan katika usimamizi wa vyanzo vya maji vya pamoja.

Kiuchumi, uwekezaji katika miundombinu ya maji unachochea ajira, unaimarisha sekta ya kilimo kwa kuongeza umwagiliaji, pamoja na kukuza viwanda vinavyotegemea upatikanaji wa maji ya uhakika. Hali hiyo pia huchochea ukuaji wa pato la taifa.

Katika sekta ya afya, upatikanaji wa maji safi na huduma bora za usafi wa mazingira unapunguza magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu na kuhara, hivyo kupunguza gharama za matibabu kwa familia na serikali kwa ujumla.

Kwa upande wa maendeleo endelevu, ajenda hiyo inalinda mazingira, inaongeza usawa wa kijinsia kwa kupunguza muda unaotumika kutafuta maji, na kusaidia kufikia malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya bara la Afrika.

Kwa ujumla, kaulimbiu ya mwaka 2026 si tu wito wa kisera, bali ni fursa kwa Tanzania kuimarisha diplomasia, kukuza uchumi, kuboresha afya za wananchi na kusukuma mbele gurudumu la maendeleo endelevu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika ambao unaongozwa na Kaulimbiu ya Mwaka 2026 inayosema: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Huduma Salama za Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza hatua za pamoja za bara katika kuhakikisha usalama wa rasilimali maji, afya ya jamii, na maendeleo endelevu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika ambao unaongozwa na Kaulimbiu ya Mwaka 2026 inayosema: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Huduma Salama za Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza hatua za pamoja za bara katika kuhakikisha usalama wa rasilimali maji, afya ya jamii, na maendeleo endelevu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri Mkuu wa Ethiopia Mheshimiwa Abiy Ahmed huku waandamizi wake wakifuatilia maelekezo hatua pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika, tarehe 14 Februari, 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri Mkuu wa Ethiopia Mheshimiwa Abiy Ahmed pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika, tarehe 14 Februari, 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri Mkuu wa Ethiopia Mheshimiwa Abiy Ahmed pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika, tarehe 14 Februari, 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri Mkuu wa Ethiopia Mheshimiwa Abiy Ahmed pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika, tarehe 14 Februari, 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia.

HOTUBA NZIMA YA NAIBU WAZIRI WA HABARI AKITOA TAMKO LA SERIKALI KUSHUSHA GHARAMA ZA USAJILI MITANDAO

 NA ALBERT G.SENGO/DODOMA

SERIKALI imechukua hatua ya kihistoria ya kuchochea ukuaji wa sekta ya habari za kidijitali nchini kwa kupunguza kwa kiwango kikubwa ada za leseni kwa wanablogu na wakusanyaji wa maudhui mtandaoni, hatua inayolenga kuondoa vikwazo vya gharama na kufungua fursa zaidi kwa wabunifu wa maudhui. Hatua hiyo imetangazwa na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji (ABC) Februari 12, 2026 jijini Dodoma. Kwa mujibu wa tangazo hilo, ada ya leseni kwa wakusanyaji wa maudhui mtandaoni imepunguzwa kutoka Shilingi 1,000,000 hadi Shilingi 100,000 kwa mwaka, huku ada ya fomu ya usajili ikishuka kutoka Shilingi 100,000 hadi Shilingi 20,000. Aidha, ada ya leseni kwa blogu imepungua kutoka Shilingi 500,000 hadi Shilingi 50,000 kwa mwaka, na fomu ya usajili kushuka kutoka Shilingi 50,000 hadi Shilingi 10,000.

SEKTA YA HABARI YASISITA ITHIBATI KUIMARISHA UWAJIBIKAJI.

 

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesema utekelezaji wa mfumo wa ithibati kwa waandishi na watangazaji wa habari nchini ni hatua ya kimkakati ya kuimarisha uaminifu, weledi na ushindani wa sekta ya habari katika uchumi wa kisasa unaotegemea taarifa sahihi na zenye kuaminika.


Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji (ABC) uliofanyika Februari 13, 2026 jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema ithibati inalenga kujenga taaluma yenye misingi imara ya kitaaluma, maadili na uwajibikaji kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.

Kwa mujibu wa Wakili Kipangula, ithibati si chombo cha kudhibiti maudhui, bali ni utaratibu wa kuweka viwango vinavyolinda hadhi ya taaluma na kuimarisha imani ya umma kwa vyombo vya habari na kwamba katika mazingira ya sasa ya ushindani wa kidijitali, uaminifu wa chanzo cha habari ndiyo mtaji mkubwa wa chombo husika.

Ameongeza kuwa vyombo vya utangazaji vinavyowekeza katika weledi wa rasilimali watu wake vinajiweka katika nafasi bora ya kuvutia wawekezaji, matangazo na ushirikiano wa kimataifa, kwa kuwa soko la habari linazidi kuthamini ubora na uwajibikaji.

Kwa upande wa wadau wa mkutano huo ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imeelezwa kuwa ushirikiano kati ya msimamizi wa maudhui na wadau wa tasnia ni nguzo muhimu katika kujenga sekta imara, inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Hatua ya kuimarisha ithibati inaonekana kuwa sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kukuza taaluma za ubunifu na mawasiliano kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya kitaifa na kimataifa, huku ikihakikisha kuwa sekta ya habari inabaki kuwa mhimili wa uwazi, uwajibikaji na maendeleo endelevu.

Waandishi zaidi ya 3,200 kati ya 3,900 walioomba vitambulisho vya uandishi wa habari (Press Card) wamethibitishwa baada ya kukidhi vigezo vya kisheria, hali inayoonesha mwitikio chanya wa wadau na utayari wa sekta kujiimarisha kitaaluma.


Friday, February 13, 2026

SERIKALI YATOA NAFUU KWA WAWEKEZAJI WA MAUDHUI YA HABARI MTANDAONI

 

SERIKALI imechukua hatua ya kihistoria ya kuchochea ukuaji wa sekta ya habari za kidijitali nchini kwa kupunguza kwa kiwango kikubwa ada za leseni kwa wanablogu na wakusanyaji wa maudhui mtandaoni, hatua inayolenga kuondoa vikwazo vya gharama na kufungua fursa zaidi kwa wabunifu wa maudhui.

Hatua hiyo imetangazwa na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji (ABC) Februari 12, 2026 jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa tangazo hilo, ada ya leseni kwa wakusanyaji wa maudhui mtandaoni imepunguzwa kutoka Shilingi 1,000,000 hadi Shilingi 100,000 kwa mwaka, huku ada ya fomu ya usajili ikishuka kutoka Shilingi 100,000 hadi Shilingi 20,000.

Aidha, ada ya leseni kwa blogu imepungua kutoka Shilingi 500,000 hadi Shilingi 50,000 kwa mwaka, na fomu ya usajili kushuka kutoka Shilingi 50,000 hadi Shilingi 10,000.


Akizungumza katika mkutano huo, Naibu Waziri Mwinjuma amesema hatua hiyo imefikiwa baada ya utafiti wa kina na majadiliano ya kimkakati yaliyodumu kwa takribani mwaka mmoja kati ya Mtandao wa Mabloga Tanzania (TBN) na Tanzania Communications Regulatory Authority (TCRA), yakilenga kuondoa changamoto za gharama zilizokuwa zikikwaza ukuaji wa uandishi wa habari za kidijitali nchini.


Katika hatua nyingine, Meneja wa Huduma za Utangazaji wa TCRA, Andrew Kisaka, alitangaza msamaha wa ada ya leseni kwa mwaka mmoja kwa waandishi wa habari wanaoanzisha mitandao ya habari watakaotambulika kama “amateur”, ili kuwapa nafasi ya kujitambulisha rasmi na kukuza vipaji vyao bila mzigo wa kifedha.

Awali, mwombaji wa kuanzisha mtandao wa habari alitakiwa kulipa ada ya maombi ya Shilingi 50,000 na ada ya leseni ya Shilingi 500,000 kwa mwaka.

Tangazo hilo limepokelewa kwa furaha kubwa na wamiliki wa mitandao waliohudhuria mkutano huo wa siku mbili, ambapo baada ya kutangazwa rasmi walishangilia na kupiga makofi kuonyesha kuunga mkono hatua hiyo.


Miongoni mwa washiriki wa mkutano huo ni wanachama wa Mtandao wa Mabloga Tanzania (TBN), Jumuiya ya Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA), Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), MOAT, NIBA, Wakongwe RTD, Baraza la Habari Tanzania (MCT), MISA Tanzania na EACO.