ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, March 10, 2026

DC Makilagi: HAKUNA VIFO, UPOTEVU WA MALI MAFURIKO MWANZA

 Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza, Amina Makilagi.

Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza, Amina Makilagi amesema kuwa hadi sasa hakuna tukio la kifo na upotevu wa mali ya mwananchi yeyote katika hekaheka za mvua kubwa iliyonyesha leo Machi 10, 2026 jijini Mwanza.

Mvua hiyo imenyesha mfululizo kwa takribani saa nane kuanzia saa 10 alfajiri hadi saa saba mchana na kuathiri maeneo mengi ya wilaya ya Nyamagana (jiji la Mwanza) hususan Kata ya Mkuyuni na kusababisha kubomoa kuta za majengo, magari kuzama, nyumba kuzingirwa na maji, na wananchi kushindwa kufanya shughuli ikiwamo kwenda kazini kutokana na maji kujaa barabarani.

Akizungumza leo na waandishi wa habari baada ya kutembelea eneo la Mkuyuni lililoathirika na mvua hizo, Amina amelipongeza jeshi la polisi na zimamoto kwa juhudi kubwa za kuhakikisha wananchi hawaathiriki na mvua hizo.

“Mpaka sasahivi ninavyozungumza hakuna mwananchi yeyote aliyepata tukio ama kifo chochote kilichotokea kwenye wilaya yetu, mtu aliyepoteza mali zake wala mtu yeyote kupata tatizo lolote la kiusalama, nashukuru jeshi la zimamoto wamefika kwa wakati na wameingia majini ndiyo maana utaona hata wale walioteleza wakaanguka kwenye maji waliokolewa,” amesema Amina.

Aliwataka wananchi kuwa makini na kuzingatia taarifa za utabiri wa hali ya hewa zinazotolewa kuhusu uwepo wa mvua kubwa, huku akiwataka wakazi wa mabondeni kuchukua hatua mapema kwa kutafuta maeneo yenye usalama.

Baadhi ya wakazi wa jiji la Mwanza, wakizungumzia hali hiyo walisema imewaathiri kwa kiasi kikubwa kwa kusababishwa washindwe kwenye kwenye maeneo yao ya kazi na kurudia njiani, kupoteza mali, biashara na kuhangaika kupata usafiri.

Abel Zabron, mkazi wa Nyegezi alisema changamoto hiyo ilimpata asubuhi wakati akielekea kazini ndipo alipofika Mkuyuni na kukuta maji yamejaa barabarani na kwenye makazi ya watu na kushindwa kuvuka kwenda upande wa pili (mjini).

Zabron alishauri serikali kuona namna ya kutengeneza miundombinu bora ikiwemo mito itakayokuwa inatiririsha maji vizuri ili barabara ziwe safi kwa ajili ya watu kuwahi makazini kwao.

Mkazi wa Butimba, Getrude Jacob alisema; “Hali ya leo imetuathiri sana tulikuwa na zana zetu lakini zote zimeondoka, hapa tulipo hatuan hata mbele wala nyuma nimeathirika sana na hii mvua na imeharibu vitu vingi sana. Nilikuwa natunzia vitu vyangu hapo garden lakini vimeenda vyote hapa nilipo sina mtaji yaani natetemeka tu,”


MAAFA YA MVUA YAFUNGA MTAA MKUYUNI, WAFANYABIASHARA WASAFIRI WAHAHA.

 🚨𝗠𝗸𝘂𝘆𝘂𝗻𝗶: 𝗠𝗮𝗮𝗳𝗮 𝘆𝗮 𝗺𝘃𝘂𝗮 𝘆𝗮𝗺𝗳𝘂𝗻𝗴𝗮 𝗺𝘁𝗮𝗮, 𝘄𝗮𝗳𝗮𝗻𝘆𝗮𝗯𝗶𝗮𝘀𝗵𝗮𝗿𝗮 𝘄𝗮𝗸𝗮𝘁𝗮 '𝗛𝗮𝘁𝘂𝗺𝘄𝗶 𝗺𝘁𝗼𝘁𝗼 𝗱𝘂𝗸𝗮𝗻𝗶'

.
Majira ya asubuhi ya leo tarehe 10/03/2026 eneo la Mkuyuni lilishuhudia mafuriko makubwa baada ya mvua kuendelea kunyesha, hali iliyofanya barabara zisipitike na maji kujaa kwa kiwango kinachoharibu biashara na maduka kandokando ya barabara.
.
Mvua ilianza mdogomdogo mapema alfajiri na kuongezeka kuanzia saa 2:30 hadi 4:00 asubuhi, ikichapa ile yenyewe, ikisababisha wateja kukosa uwezo wa kufika sokoni na wafanyabiashara kulazimika kufunga maduka.
.
“Maji yalikuja ghafla na kujaa dukani nikalazimika kupandisha juu bidhaa zote nilizokuwa nimeziweka chini sakafuni — hatumwi mtoto dukani,” alisema mfanyabiashara mmoja wa sokoni, akieleza wasiwasi wa wafanyabiashara waliokuwa wameweka bidhaa mafuta za mauzo.
.
Hadi sasa mamlaka za mkoa au wilaya hazijatoa taarifa rasmi kuhusu uzito wa uharibifu au idadi ya wahasiriwa.
.
#jembehabari
#DriveMix

MWANAFUNZI ALIYEDAIWA KUBEBWA NA MAMBA APATIKANA HAI BAADA YA SIKU SABA

Mwanafunzi huyo (aliyefunikwa uso) akiondolewa Katika Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe na ofisa wa jeshi la polisi dawati la jinsia.
Mwanafunzi huyo (aliyefunikwa uso) akiondolewa Katika Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe na ofisa wa jeshi la polisi dawati la jinsia.

 Katika tukio la kushangaza na lisilo la kawaida, mwanafunzi wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari Colnel Magembe iliyopo Wilaya ya Ukerewe, Mkoa wa Mwanza (jina limehifadhiwa), amepatikana akiwa hai baada ya kudaiwa kushambuliwa na kuchukuliwa na mamba takribani wiki moja iliyopita.

Tukio la kutoweka kwa mwanafunzi huyo lilitokea Machi 2, 2026 katika kitongoji cha Ilondo Magharibi, kijiji cha Buzegwe, Kata ya Kagunguli wilayani Ukerewe. Inadaiwa kuwa saa 11 alfajiri alipokuwa akioga katika Ziwa Victoria akijiandaa kwenda shuleni, alishambuliwa na mamba na kubebwa majini.

Hata hivyo, jana Jumatatu Machi 9, 2026, majira ya saa 11 alfajiri, mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 18 amepatikana akiwa hai katika eneo lile lile alikodaiwa kuchukuliwa na mamba. Cha kushangaza zaidi ni kwamba alikutwa bila majeraha wala michubuko yoyote mwilini.

Kwa mujibu wa taarifa, wavuvi waliokuwa wakifanya shughuli zao kandokando ya Ziwa Victoria ndiyo waliomkuta binti huyo akiwa amelala karibu na ufukwe wa ziwa. Hata hivyo, hakuwa na uwezo wa kuzungumza. Wananchi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi walimchukua na kumpeleka katika Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe (Bomani) iliyopo Nansio kwa ajili ya matibabu na uchunguzi zaidi.

Akizungumza hospitalini hapo Machi 9, 2026, baba wa mwanafunzi huyo, Deonatus Salvatory, amesema familia ilishakata tamaa baada ya juhudi za kumtafuta kugonga mwamba. Alieleza kuwa walikuwa tayari wameanza maandalizi ya msiba na jamii ilikuwa imeanza taratibu za maombolezo kama ilivyo katika misiba mingine.

Salvatory amesema walipokea simu kutoka kwa wavuvi alfajiri wakitoa taarifa kuwa binti yao amepatikana kandokando ya ziwa akiwa hai, jambo lililowashangaza sana.

“Matumaini ya kumpata yalikuwa yamekwisha kabisa. Baada ya kutoonekana kwa muda mrefu tuliweka msiba na kufanya matanga, watu walikuwa tayari wameanza kutawanyika. Tangu nizaliwe katika eneo hili, sijawahi kushuhudia tukio kama hili. Tunaamini si jambo la kawaida,” amesema Salvatory.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe (Bomani), Dk. Bunhya Kayila, amesema walimpokea mwanafunzi huyo majira ya saa 1 asubuhi akiwa dhaifu. Uchunguzi wa awali umeonyesha hana majeraha yoyote yanayoashiria kuwa alishambuliwa na mamba.

Dk. Kayila amesema vipimo mbalimbali vinaendelea kufanywa ili kubaini hali yake kiafya, huku akieleza kuwa kwa sasa mwanafunzi huyo anaweza kutambua mazingira yanayomzunguka lakini bado hana uwezo wa kuzungumza. Amewekwa wodini chini ya uangalizi wa karibu kwa angalau saa 24.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe, Goodluck Mtigandi, amesema uchunguzi wa awali haujaonyesha dalili za uwepo wa mnyama hatarishi katika eneo alikodaiwa kushambuliwa mwanafunzi huyo.

Amesema tangu Machi 2 hadi sasa hakukuwa na ushahidi wowote wa kuthibitisha kuwa mnyama pori alimshambulia binadamu katika eneo hilo. Hivyo, mamlaka zinasubiri mwanafunzi huyo apate nafuu ili aweze kueleza kwa undani kilichotokea katika kipindi chote alichokuwa hajulikani alipo.

Aidha, Jeshi la Polisi Wilaya ya Ukerewe kupitia dawati la jinsia na watoto limezuia vyombo vya habari kumuona mwanafunzi huyo au kupiga picha zake. Kwa sasa amehamishwa wodini na anaendelea kuwa chini ya uangalizi wa karibu wa vyombo vya usalama pamoja na wataalamu wa afya huku uchunguzi zaidi ukiendelea kubaini ukweli wa tukio hilo.


Monday, March 9, 2026

Naibu Waziri Maghembe azungumza na Wawakilishi wa Heshima wa Tanzania nchini Nepal, mjini Mumbai, Chennai na Kolkata

 NEW DELHI-Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe amekutana kwa mazungumzo na Wawakilishi wa Heshima wa Tanzania katika maeneo ya Nepal, Mumbai, Chennai na Kolkata ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi nchini India.

Katika mazungumzo yao yaliyofanyika jijini New Delhi hivi karibuni wamejadili umuhimu wa wawakilishi hao kushirikiana na Serikali katika kuimarisha sekta ya utalii, kilimo, elimu na biashara na uwekezaji ili kutekeleza dhana ya Diplomasia ya Uchumi.
Akizungumza, kwenye kikao kilichofanyika jijini New Delhi hivi karibuni, Mhe. Dkt. Maghembe aliwapongeza wawakilishi hao kwa kuiwakilisha Tanzania kikamilifu kwenye maeneo yao na kwamba Serikali inathamini mchango wao kwenye uwakilishi huo na itaendelea kushirikiana nao.

Kwa upande wao, wawakilishi hao Mhe. Rajesh Chaudhary wa Nepal, Mhe. Nayan Patel wa Mumbai, Mhe. Krishna Pimple wa Chennai na Mhe. Pradeep Singhania wa Kolkata wamemshukuru Mhe. Naibu Waziri kwa kukutenga muda wa kukutana nao na kwamba wataendelea kuiwakilisha Tanzania kikamilifu kwenye maeneo yao hususan katika kutangaza fursa mbalimbali zilizopo nchini ikiwemo utalii biashara na uwekezaji.

WANAWAKE WA SF GROUP WATUMIA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI KUFANYA MATENDO YA HURUMA NA KUTOA MSAADA

NA VICTOR MASANGU/PWANI - SAUTI NA FLORENCIA PETER

Katika kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita ya kuboresha sekta ya elimu wafanyakazi wanawake wa Kampuni ya Sf Group wameamua kuungana kwa pamoja kuitumia siku ya maadhimisho ya siku ya mwanamke duniani kufanya matendo mbali mbali huruma ikiwemo kutoa msaada wa kompyuta, madaftari, na taulo za kike katika shule ya Koka sekondari na kutembelea vituo vya watoto yatima katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha.

Akizungumza katika sherehe za maadhimisho hayo ambayo yamefanyika katika Jimbo la Kibaha mjini Mkurugenzi wa Rasirimali watu na utawala wa kampuni ya SF Group Marygoreth Faustinen amebainisha kwamba wameamua kuitumia siku hiyo katika kutoa misaada mbali mbali ikiwa ni njia moja wapo ya kurudisha fadhila kwa jamii ambayo inawazunguka sambamba na kusaidia kutatua changamoto za wananchi katika baadhi ya maeneo.

Sunday, March 8, 2026

JUMANNE HII 'SEED OF LIFE' WAJA NA IBADA KUBWA YA VIJANA MWANZA

 Jumanne hii ya Tarehe 10 Machi 2026 kuanzia saa 11 jioni, tutakua na ibada ya vijana (GLORIOUS REVIVAL). IT’S A LIFE CHANGING SERVICE 🔥

Tutakua na praise & worship session, tukiongozwa na watumishi wa Mungu seed of life na waimbaji wengine; Mtumishi wa Mungu Pastor Panta atakuwepo kutuhudumia. KARIBU SANA, USIPANGE KUKOSA🔥

CHAMA NA LOEMBA WAFUNGA SIMBA SC YASONGA MBELE KOMBE LA CRDB

 


VIGOGO, Simba SC wamejikatia tiketi ya Hatua ya 16 Bora Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), michuano inayodhaminiwa na Benki ya CRDB baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya B19 usiku wa jana Jumamosi katika Uwanja wa Meja Jenerali Charles Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam.

Mabao ya Simba SC yamefungwa na viungo, Mkongo-Brazzaville, Inno Jospin Loemba dakika ya 22 na Mzambia, Clatous Chotta Chama dakikia ya 77.

Mechi nyingine za Hatua ya 32 Bora Kombe la CRDB leo timu ya Namungo FC imefanikiwa kutinga 16 Bora baada ya ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya kagera Sugar jioni ya leo Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Lindi.

Nyota wa mchezo huo ni kiungo, Jacob Raymond Massawe aliyefunga mabao matatu peke yake dakika ya 11, 28 na 45, huku bao lingine likifungwa na winga Hassan Salum Kabunda dakika ya 89 baada ya Kagera Sugar kutangulia na bao la Hamisi Adam dakika ya nane. 

Nayo Pamba Jiji FC imesonga mbele kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Transit Camp ya Dar es Salaam jioni ya Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza, wakati Geita Gold imeichapa Nyika ya Pwani 4-1 Uwanja wa shule ya sekondari ya Wasichana ya Nyankumbu mjini Geita na Mashujaa FC imeitoa KegGold ya Mbeya kwa penalti 5-3 baada ya sare ya bila mabao ndani ya dakika 90 Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.

Friday, March 6, 2026

ULAJI HOLELA WA VYAKULA CHANZO CHA MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA.

Jamii imetakiwa kupunguza ulaji holela wa vyakula ili kuepuka magonjwa yasiyoambukizwa kama vile Kisukari,Kiharusi na presha kutokana na ulaji holela wa chakula bila kufuata utaratibu wa kiafya na mazoezi ya mwili ya kupunguza uzito

Rai hiyo imetolewa na Oda Isac Sekiromba mwakilishi wa kampuni ya Edmark tawi la Mwanza leo wakati wa siku ya mwanamke Jembe iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Edmark iliyoambatana na utolewaji wa elimu ya Afya na ujasiriamali iliyoandaliwa na kampuni ya Edmark kwa kushirikiana na Jembe FM

 

Je, vyakula vya ovyo husababisha magonjwa?
Madaktari wengi wanatambua kuwa ulaji wa chakula kisicho na chakula unahusishwa na ugonjwa wa moyo wa mapema. Makubaliano ya jumla ni kwamba uhusiano huu unaweza kuelezewa na mafuta yaliyojaa katika vyakula hivi kuongeza fetma, hatari ya kisukari na hyperlipidemia na maudhui ya juu ya chumvi kuongeza shinikizo la damu.  
Je, ni nini kitatokea ikiwa unakula kila siku?
Ulaji mwingi wa vyakula vya kuchukua unahusishwa na kuongezeka kwa hatari ya ugonjwa wa moyo kwa watu wazima . Inasababisha unene wa kupindukia, shinikizo la damu, na viwango vya juu vya kolesteroli kwa sababu ya utajiri wake wa kalori, mali duni ya virutubishi, inayoongezwa kwa ukosefu wa matunda na mboga mboga.
Kwa nini ni muhimu kula vyakula vyenye afya?
Inakulinda dhidi ya magonjwa mengi sugu yasiyoambukiza, kama vile ugonjwa wa moyo, kisukari na saratani . Kula vyakula mbalimbali na kutumia chumvi kidogo, sukari na mafuta yaliyoshiba na yanayozalishwa viwandani, ni muhimu kwa lishe yenye afya.

Ni tabia gani mbaya zaidi za kula?
Haya yanaweza kujumuisha kula kabla ya kulala, kuruka milo, kula haraka sana, kula bila akili, au kula mkazo . Hebu tuzungumze kuhusu jinsi tabia hizo zinaweza kuathiri afya yako na baadhi ya mapendekezo ya kuzidhibiti.

Nini kinatokea kwa mwili wako unapoacha kula vyakula vilivyosindikwa?
Ni nini hufanyika ninapokata vyakula vilivyosindikwa? Unaweza kupata dalili za kujiondoa kama vile uchovu na kuwashwa, lakini pia kuna uwezekano wa kupunguza uzito na kujisikia nguvu zaidi .

Nini kinatokea kwa mwili wako unapoanza kula afya?
Kula chakula bora - kama vile kufuata lishe ya Mediterania yenye mazao na nyuzinyuzi au lishe ya DASH - kunaweza kupunguza hatari yako ya kupata ugonjwa mbaya. Ulaji mbaya umehusishwa na magonjwa sugu kama vile ugonjwa wa moyo, kisukari cha aina ya 2, shinikizo la damu na hata saratani fulani, pamoja na saratani ya utumbo mpana.

AFCON 2027: ULINZI NI CHUMA, AMANI YETU NDIO FURSA KWA VIJANA!

 

WAKATI hamu ya michuano ya AFCON 2027 ikizidi kupanda, Serikali imetuma ujumbe mzito: "Tanzania ni salama na ulinzi ni chuma!" 

Katika kikao kizito kilichofanyika Dar es Salaam Machi 4, Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi imekutana na Mkuu wa Kitengo cha Usalama wa Michezo kutoka Umoja wa Mataifa (UN), Valerio de Divitiis, kupigilia msumari mkakati wa kuhakikisha kila mgeni na mwenyeji anakuwa salama kama yuko nyumbani kwake.

Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo, Boniface Tamba, ameweka wazi kuwa usalama si suala la polisi pekee, bali ni mazingira tulivu yatakayowawezesha vijana na wafanyabiashara kuchangamkia fursa bila hofu. 

Tamba alisisitiza kuwa mifumo ya kudhibiti umati na usimamizi wa viwanja itakuwa ya viwango vya dunia, jambo linaloashiria kuwa Tanzania iko tayari kuishangaza Afrika kwa ukarimu na utulivu wa kipekee.

Hivi karibuni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) Gianni Infantino katika ofisi za FIFA zilizopo mjini Rabat nchini Morroco ambapo moja kati ya masuala waliyozungumza ni pamoja na maandalizi ya AFCON 2027.

Kwa upande wake,  Leodegar Tenga, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi, amepigilia msumari kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha AFCON 2027 inavunja rekodi. 

Alibainisha kuwa mashindano haya hayataishia kwenye ufundi wa uwanjani pekee, bali yataacha alama ya usalama wa hali ya juu, jambo ambalo ni msingi wa kuvutia wawekezaji na watalii wanaotafuta maeneo yenye amani ya kudumu.

Huu ni ujumbe tosha kwa vijana wanaopoteza muda kusononeka: Usalama huu unaoandaliwa na Serikali kwa kushirikiana na UN ni "uwanja mweupe" kwenu.  Badala ya kuendekeza chuki mitandaoni, ni wakati wa kuthamini utulivu huu na kujiandaa kuvuna "mapesa" ya mashindano hayo makubwa barani Afrika.

WANAWAKE WATAKIWA KUVAA UJASIRI WA KUPIMA AFYA ZAO.

 Wanawake watakiwa kuvaa ujasiri wa kupima afya zao


Hofu ya kupima afya imetajwa kuwa kitanzi kwa wanawake wengi, kwa kuwa imesababisha baadhi kuteseka hata kupoteza maisha kwa magonjwa makubwa ikiwamo kansa, ambayo yakigundulika mapema wangepata tiba.

Imeelezwa kuwa wengi hulazimika kupima wakiwa tayari kwenye hali mbaya, ikiambatana na maumivu.
 
 Hivyo wanawake wametakiwa kubadili mtazamo, na kujenga tabia ya kwenda kufanyiwa uchunguzi wa afya mapema.

Akizungumza katika kongamano la afya ya wanawake lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Mkemia na Mtafiti wa Miti Dawa, Prof. Faith Mabiki, alisema bado kuna hofu kubwa miongoni mwa wanawake kuhusu vipimo vya afya licha ya maendeleo ya teknolojia katika sekta ya tiba.

Prof.Mabiki alisema magonjwa kama saratani ya shingo ya kizazi na saratani ya matiti yanaweza kudhibitiwa kwa kiwango kikubwa, endapo yatagunduliwa mapema kupitia vipimo vya mara kwa mara.

“Wanawake wengi huweka afya zao kama jambo la pili, lakini ukweli ni kwamba afya njema ndiyo msingi wa ustawi wa familia na maendeleo ya jamii,” alisema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa RAAWU Tawi la SUA, Faraja Kamendu, alisema taasisi hiyo inaendelea kushirikiana na menejimenti ya chuo kuhakikisha wafanyakazi wanawake wanapata elimu ya afya na huduma muhimu za kitabibu.

Kamendu alisema semina hiyo imewapa wanawake fursa ya kujifunza kuhusu changamoto mbalimbali za kiafya pamoja na njia za kujikinga nazo.

Naye Daktari bingwa wa magonjwa ya watoto katika Hospitali ya SUA, Dk.Graca Chotamawe, alisema magonjwa yasiyoambukiza yanaendelea kuongezeka duniani, ikiwamo barani Afrika kutokana na mabadiliko ya mtindo wa maisha.

Alisema takribani watu milioni 41 hufariki kila mwaka duniani kutokana na magonjwa hayo, huku sababu zake zikitajwa kuwa ni pamoja na kupungua kwa mazoezi, matumizi ya vyombo vya usafiri kama magari na bodaboda, pamoja na matumizi ya dawa za kulevya.

Aliongeza kuwa magonjwa hayo huongeza mzigo wa kiuchumi kwa familia nyingi, kwa kuwa matibabu yake huchukua muda mrefu na kugharimu fedha nyingi.

Kongamano hilo lilihusisha watumishi wanawake wa SUA na wanafunzi, huku pia likitoa fursa ya upimaji wa afya kwa magonjwa mbalimbali ikiwemo presha na sukari.

DARAJA LA UBAGWE LAONDOA ADHA YA MAFURIKO USHETU.

Daraja la Ubagwe laondoa  adha ya mafuriko Ushetu
Daraja la Ubagwe laondoa adha ya mafuriko Ushetu

 

Wananchi wa Wilaya ya Ushetu sasa wana sababu ya kutabasamu baada ya kukamilika kwa Daraja la Ubagwe, mradi muhimu wa miundombinu uliokuja kuondoa changamoto ya muda mrefu ya kukatika kwa mawasiliano wakati wa msimu wa mvua.

Kwa miaka mingi wakazi wa eneo hilo walikuwa wakikumbwa na adha kubwa hasa kipindi cha mvua kali. Mafuriko yaliyosababishwa na mvua za El-Nino yaliwahi kuharibu miundombinu ya barabara na kukata kabisa mawasiliano kati ya maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo pamoja na mikoa jirani ya Tabora, Geita na Shinyanga. Hali hiyo ilifanya shughuli za kiuchumi kudorora huku wananchi wakipata hasara kubwa.

Wakulima walishindwa kusafirisha mazao yao kwenda sokoni, wafugaji walikwama kuvusha mifugo yao na wafanyabiashara walipoteza fursa za kibiashara kutokana na kukosekana kwa njia salama ya kuvuka. Changamoto hiyo pia iliathiri huduma za kijamii, ambapo baadhi ya wagonjwa walishindwa kufikishwa hospitalini kwa wakati.

Kwa mujibu wa wananchi wa eneo hilo, hali hiyo ilikuwa hatari zaidi kwa akina mama wajawazito ambao wakati mwingine walilazimika kuvuka katika mazingira magumu au kushindwa kabisa kuvuka, jambo lililosababisha vifo katika baadhi ya matukio.

Hata hivyo, matumaini mapya yameanza kuonekana baada ya kukamilika kwa Daraja la Ubagwe, mradi uliogharimu shilingi bilioni 13.5. Daraja hilo linatajwa kuwa mkombozi wa wananchi wa Ushetu na maeneo ya jirani kwa kuwa sasa linahakikisha mawasiliano yanakuwepo wakati wote wa mwaka bila kujali msimu wa mvua.

Akizungumza na wananchi mara baada ya kukagua daraja hilo, Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenan Kihongosi, amesema kukamilika kwa daraja hilo kumesaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zilizokuwa zikiwakumba wananchi kwa muda mrefu.

Ameeleza kuwa mradi huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha miundombinu ya barabara na madaraja ili kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi kwa wananchi.

Kihongosi amebainisha kuwa ujenzi wa Daraja la Ubagwe umefanyika sambamba na ujenzi wa madaraja mengine mawili ya Kasenga na Ng’hwande, hatua inayolenga kuboresha zaidi mtandao wa usafiri na mawasiliano katika ukanda huo.

Amesema kwa sasa daraja hilo lipo katika kipindi cha majaribio ili kuhakikisha linakidhi viwango vya ubora na thamani ya fedha iliyotumika kabla ya kukabidhiwa rasmi kwa matumizi ya wananchi.

Akizungumzia ubora wa mradi huo, Kihongosi amesema thamani ya fedha inaonekana wazi kupitia ubora wa ujenzi wake, huku akiwataka wananchi kulinda na kutunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kuwanufaisha kizazi cha sasa na kijacho.

Katika ziara hiyo pia amesisitiza umuhimu wa kudumisha amani na utulivu nchini, akieleza kuwa maendeleo ya miundombinu na ustawi wa shughuli za kiuchumi kama kilimo, ufugaji na biashara hutegemea uwepo wa amani.

Kwa kukamilika kwa Daraja la Ubagwe, wananchi wa Ushetu wanatarajia kuona ongezeko la shughuli za kiuchumi, urahisi wa usafiri na mawasiliano pamoja na kuboreshwa kwa upatikanaji wa huduma za kijamii, jambo litakalosaidia kuharakisha maendeleo ya eneo hilo na ukanda wa Ziwa kwa ujumla.

Ujenzi wa daraja hilo ni mfano wa namna uwekezaji katika miundombinu unavyoweza kubadilisha maisha ya wananchi kwa kuondoa vikwazo vya kijiografia na kuleta fursa mpya za maendeleo.

Thursday, March 5, 2026

AZAM FC YATOSHANA NGUVU NA TANZANIA PRISONS

 


TIMU ya Azam FC imetoa sare ya bila kufungana na wenyeji, Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.

Kwa matokeo hayo, Azam FC wanafikisha pointi 24 katika mchezo wa 12 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya nne, wakati Tanzania Prisons inafikisha pointi 13 katika mchezo wa 15, ingawa inabaki nafasi ya 15 kwenye ligi ya timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.  

YANGA SC 'YAITWANGA' SINGIDA BLACK STARS 3-0

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya wenyeji, Singida Black Stars katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Mwigulu Airtel Complex, Singida.

Mabao ya Yanga SC leo yamefungwa na mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Mpumelelo Dube dakika ya 39, winga Mganda, Allan Okello kwa penalti dakika ya 45’+2 na kiungo Mudathir Yahya Abbas dakika ya 56.

Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 32 katika mchezo wa 12 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi nne zaidi ya JKT Tanzania ambayo pia imecheza mechi tano zaidi.

Kwa upande wao Singida Black Stars wanabaki na pointi zao 19 za mechi 12 pia nafasi ya tisa.

TAZAMA GOLI LA ALLAN OKELLO VS SINGIDA BLACK STARS

BARA LA AFRIKA; ATHARI KUU VITA VYA MASHARIKI YA KATI

Eneo la Strait Hormuz
Eneo la Strait Hormuz

 Vita inayoendelea Mashariki ya Kati, iliyoanzishwa na Marekani pamoja na mshirika wake Isarel, dhidi ya Iran, tayari wachumi wametaja athari za mapema zitakazoanza kushuhudiwa barani Afrika.

Miongoni mwaka ni nishati ya mafuta. Kwa siku takribani mapipa ya mafuta milioni 20 hupita katika korido ya mlango wa ‘Strait of Hormuz’. Huo ni mlango mwembamba wa bahari unaounganisha Ghuba ya Persian na Ghuba ya Oman.

Kwa mujibu wa ukurasa Firstpost mtandao wa instagram, unaeleza hayo na kwamba hali hiyo inatokana na kukosekana kwa hali ya kiusalama kutokana na vita hivyo, kwa sasa usafirishaji huo utasitishwa.

Athari za kukosekana kwa nishati hiyo, mchambuzi wa kupitia mtandao huo anasema, kwa Afrika, gharama za maisha zitapanda, ikiwamo bei za vyakula.

Kinachoendelea sasa si mzozo mwingine tu wa kawaida katika eneo la Asia Magharibi, bali ni mshtuko wa moja kwa moja kwa uchumi wa dunia. 

Katikati ya yote haya eneo hilo ni muhimu na Mlango wa Bahari wa uitwao ‘Hormuz’. Ni njia nyembamba ya baharini kati ya Iran na Oman, ambako karibu theluthi moja ya tano ya mafuta ya dunia hupita.

Baada ya mashambulizi mapya ya Marekani na Israel, pamoja na hatua za kulipiza kisasi za Iran, inaripotiwa kuwa baadhi ya meli zilipokea maonyo ya redio yakidai kuwa upitishaji unaweza kuzuiwa. 

Hakuna tangazo rasmi la kufungwa kwa njia hiyo, lakini masoko hayasubiri taratibu za kisheria.

Bei za mafuta zinaanza kupanda, kampuni za bima zinaongeza gharama za bima ya hatari ya vita, na maamuzi ya usafirishaji kwa njia ya meli yanasimama kwa tahadhari. Iran imekwishafunga mlango huo muhimu.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Uingereza Reuters, Umoja wa Ulaya (EU), meli zake zimekuwa zikipokea ujumbe kutoka Jeshi la Iran, likisema hakuna meli inayoruhusiwa kupita katika Mlango wa Bahari wa Hormuz.

Mlango huu ni njia muhimu ya kusafirisha mafuta duniani, takribani mapipa milioni 20 ya mafuta kwa siku hupitia, yakiwakilisha asilimia 20-25 ya biashara ya mafuta ya baharini duniani na moja ya tano ya matumizi ya mafuta duniani.

ATHARI ZA AWALI

Kuongezeka kwa mapigano kunahatarisha kuharibu zaidi utulivu wa dunia, Mashariki ya Kati kuna athari kubwa kwa biashara ya nishati, usalama wa chakula na uchumi, hasa barani Afrika, ambako migogoro na misukosuko ya kiuchumi bado ni mikali.

Umoja wa Afrika (AU), baada ya taarifa Israel na Marekani kuanzisha mashambulio dhidi ya Iran, umezitaka pande zinazopigana kujizuia, kupunguza mvutano na kuendelea na mazungumzo

Athari hizo kwa Afrika, pia ziliguswa na  mgogoro wa Russia na Ukraine miezi ya mwanzoni mwaka 2022. 


Afrika ilianza kuona makali ya vita hivyo baada kutokea mgogoro wa chakula, ikiwamo kupanda kwa gharama ya chakula hasa ngano na mafuta.

Katika ripoti ya Shirika la Fedha Duniani (IMF) iliyochapishwa Aprili mwaka huo, ilisema, baadhi ya mataifa ambayo yanaathirika moja kwa moja na vita vya Ukraine kwa kutegemea uagizwaji wa ngano kutoka nchi hiyo na Russia kwa asililia 85 ni pamoja na Tanzania, Ivory Coast, Senegal na Msumbiji.

Haikuwa Afrika pekee, dunia nzima iliona makali ya vita hivyo ambavyo bado vinaendelea. Ni kutokana na ukweli kwamba hadi vita vinaanza, Russia ndiyo nchi inayoongoza katika mauzo ya ngano duniani ikifuatiwa na Ukraine.

Bei ya mafuta inatarajiwa kupanda kwa kasi siku ya Jumatatu licha ya ahadi ya nchi kubwa zinazozalisha mafuta kuongeza uzalishaji, huku vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran pamoja na kufungwa kwa vitendo kwa Mlango wa Bahari wa Hormuz vikitetemesha wawekezaji.

Mafuta ghafi ya Marekani yanatarajiwa kupanda kwa karibu asilimia tisa biashara itakaporejea, kulingana na takwimu za dalali IG. 

Ongezeko hilo linakuja licha ya kundi la wazalishaji mafuta la OPEC+ kukubaliana Jumapili kuongeza uzalishaji kwa kiwango kikubwa zaidi ya ilivyotarajiwa ili kupunguza athari za mzozo.

Walinda Mapinduzi wa Iran (Revolutionary Guards) wanaripotiwa kuziambia meli kwamba kupita katika 

Meli moja ya mafuta ilishambuliwa Jumapili leo katika mlango huo na angalau meli 150 zilizobeba mafuta ghafi, gesi asilia iliyoyeyushwa (LNG) na bidhaa za mafuta zilisimamisha safari na kutia nanga katika maji ya wazi katika Ghuba ya Mashariki ya Kati, kulingana na Reuters.

Tehran imekuwa ikionya kwa muda mrefu kwamba inaweza kutumia nafasi yake ya kijiografia kuufunga mlango huo kujibu uchokozi wa kijeshi. 

Tamsin Hunt, mchambuzi mwandamizi wa kampuni ya ujasusi na usalama wa mtandao ya S-RM, alisema kufunga kabisa njia hiyo “kungedhoofisha sana uchumi wa Iran yenyewe.”

Masoko ya wikendi ya IG yanaonesha kuwa mafuta ghafi ya Marekani yanaweza kupanda hadi zaidi ya dola 73 kwa pipa biashara itakaporejea New York, kutoka dola 67 Ijumaa usiku, kiwango cha juu zaidi tangu Juni 2025 wakati Marekani ilipoanzisha mashambulizi dhidi ya vituo vya nyuklia vya Iran.

Wachambuzi wa Barclays walisema bei ya mafuta inaweza kufikia dola 80 kwa pipa endapo kutakuwa na “usumbufu mkubwa wa usambazaji.” Nao wachambuzi wa Royal Bank of Canada walionya kuwa mafuta ya zaidi ya dola 100 kwa pipa ni hatari halisi iwapo mzozo utaongezeka.

Kupanda kwa bei ya jumla ya mafuta kunatarajiwa kuathiri bei za rejareja. Bei ya wastani ya petroli nchini Uingereza ni pensi 132.9 kwa lita na dizeli 142.4p, kulingana na The AA, ambayo imeonya kuwa athari za Iran zinaweza kuungana na mpango wa serikali kurejesha ushuru wa mafuta wa 5p kwa lita na hivyo kuongeza bei zaidi.

Katika soko la London, faharasa ya FTSE 100 inatarajiwa kushuka kwa karibu asilimia 0.5, Jumatatu asubuhi baada ya kufikia rekodi Ijumaa.

Wawekezaji duniani wanatarajiwa kukimbilia mali salama. Dhahabu, ambayo imepanda kwa wiki nne mfululizo, imeongezeka kwa asilimia 2.25 hadi karibu dola 5,400 kwa wakia katika masoko ya wikendi ya IG, huku fedha (silver) nayo ikipanda kwa 3.2.

Nchi nane za OPEC+ zilikubaliana kimsingi kuongeza uzalishaji kwa mapipa 206,000 kwa siku mwezi April, zaidi ya matarajio ya awali ya mapipa 137,000.

Kampuni ya bandari ya DP World imesimamisha shughuli katika Bandari ya Jebel Ali, Dubai na kampuni ya Mediterranean Shipping Company imesitisha upokeaji wa mizigo inayoelekezwa Mashariki ya Kati hadi itakapotangazwa vinginevyo.

Gharama za bima ya meli katika eneo hilo zimeongezeka, kulingana na Dylan Mortimer wa kampuni ya usimamizi wa hatari ya Marsh, akionya kuwa hatari kuu ni pamoja na kukamatwa kwa meli na vikosi vya Iran na uwezekano wa kufungwa kwa Mlango wa Hormuz.

Masoko mengi ya hisa katika eneo la Ghuba yalishuka Jumapili. Soko la Saudi Arabia lilipoteza asilimia 2.5, ingawa hisa za Saudi Aramco zilipanda kwa 2.5 kufuatia matarajio ya kupanda kwa bei ya mafuta ghafi. Soko la hisa la Kuwait lilisimamisha biashara hadi itakapotangazwa tena, likitaja “hali za kipekee” zinazoikabili nchi hiyo.

KUUAWA KIONGOZI IRAN

Taarifa kutoka Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, vyombo kadhaa vya habari vya serikali nchini Iran vilithibitisha kifo cha Ayatollah Khamenei, jana.

Ayatollah Khamenei.


Rais wa Marekani, Donald Trump saa chache zilizopita alisema Kiongozi Mkuu huyo aliuawa wakati wa shambulio la pamoja na Israel katika maeneo kadhaa kote Iran.

Katika taarifa hiyo, haikutajwa ni jinsi gani Khamenei mwenye umri wa miaka 86 alivyofariki, au ni nani anayeweza kuchukua nafasi ya kiongozi.

Jamaa wa Khamenei pia wameuawa katika mashambulizi hayo

Hapo awali, vyombo vya habari vya serikali vilisema kwamba binti wa Khamenei, mkwewe na mjukuu wake pia waliuawa katika mashambulizi hayo.

Kulingana na Shirika la Habari la Fars, ambalo lina uhusiano na Kikosi cha Revolutionary Guard, kuna ripoti kwamba mmoja wa mabinti wa Khamenei ameuawa pia.