ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, April 17, 2026

MALEMA AHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA MI-5 JELA

Kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini, Julius Malema
Kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini, Julius Malema.

 

Kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini, Julius Malema, ameripotiwa kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano jela baada ya kupatikana na hatia ya kumiliki silaha kinyume cha sheria pamoja na kufyatua risasi hadharani.

Tukio Lilivyotokea

Hukumu hiyo inatokana na tukio la mwaka 2018 wakati wa maadhimisho ya miaka mitano ya chama cha EFF yaliyofanyika katika jimbo la Eastern Cape. Katika tukio hilo, video iliyosambaa mitandaoni ilimuonyesha Malema akifyatua risasi kadhaa hewani kwa kutumia bunduki ya nusu otomatiki mbele ya umati wa wafuasi wake waliokuwa wakishangilia.

Mamlaka za usalama zilichukulia kitendo hicho kama ukiukwaji wa sheria za silaha za moto nchini Afrika Kusini, hali iliyosababisha kuanzishwa kwa uchunguzi na hatimaye kufunguliwa kwa mashtaka dhidi yake.

Utetezi Wake Mahakamani

Akiwasilisha utetezi wake, Malema alidai kuwa silaha iliyotumika haikuwa mali yake na kwamba kitendo hicho kilikuwa sehemu ya kuhamasisha umati katika tukio la kisiasa. Hata hivyo, upande wa mashtaka uliwasilisha ushahidi ulioridhisha mahakama kwamba kitendo hicho kilikiuka sheria za nchi, na hivyo kumfanya kupatikana na hatia.

Athari za Kisiasa

Hukumu hiyo inatarajiwa kuwa na athari kubwa katika siasa za Afrika Kusini, hasa kutokana na nafasi ya Malema kama mmoja wa viongozi wakuu wa upinzani. Chama chake cha EFF kimekuwa na ushawishi mkubwa miongoni mwa vijana na tabaka la wafanyakazi, hivyo hukumu hiyo inaweza kuathiri mwenendo wa kisiasa ndani ya chama na taifa kwa ujumla.

Wachambuzi wa siasa wanaamini kuwa kesi hiyo inaweza kufungua mjadala mpana kuhusu nidhamu ya viongozi wa kisiasa, utawala wa sheria na matumizi sahihi ya silaha za moto nchini humo.

KOCHA BILO AFARIKI AKIWA UWANJANI JIJINI MWANZA

aa

  Athuman Bilali maarufu kama Billo.

Picha: Mtandao
Athuman Bilali maarufu kama Billo.

Aliyewahi kuwa kocha wa timu mbalimbali za soka nchini, ikiwamo Stand United ‘Chama la Wana’ na Pamba (sasa Pamba Jiji), Athuman Bilali maarufu kama Billo, amefariki dunia huku chanzo cha kifo chake kikiwa bado hakijafahamika.

Marehemu Billo hadi mauti yanamkuta alikuwa mmiliki wa kituo cha michezo pamoja na timu ya wanawake ya Bilo Queens inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania.

Katibu wa Chama cha Soka Mkoa wa Mwanza (MZFA), Leonard Malongo, amethibitisha kifo hicho, akieleza kuwa ni pigo kubwa kwa wadau wa soka mkoani Mwanza na nchini kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Malongo, taarifa za awali zinaeleza kuwa kocha huyo aliendelea na majukumu yake ya kawaida ya mazoezi na timu ya Bilo Queens katika Uwanja wa Shule ya Msingi Nyasaka jijini Mwanza hadi jioni ya Aprili 15, 2026. Hata hivyo, baada ya wachezaji kuondoka, aliachwa akiwa amekaa uwanjani na baadaye alikutwa amefariki eneo hilo asubuhi iliyofuata.

“Jana alikuwa uwanjani akifanya mazoezi na timu yake, lakini hadi wachezaji wanaondoka walimwacha amekaa. Asubuhi ndipo alikutwa amefariki hapohapo. Bado hatujajua chanzo cha kifo, kwani mwili wake umehifadhiwa hospitalini kwa uchunguzi zaidi,” amesema Malongo.

Ameongeza kuwa taarifa zaidi kuhusu chanzo cha kifo pamoja na ratiba ya mazishi zitatolewa baada ya taratibu za kitabibu kukamilika.

Kifo cha Billo kimeacha pengo kubwa katika maendeleo ya soka, hususan katika kuinua vipaji vya wanawake kupitia timu yake ya Bilo Queens. Wadadau wa michezo wanatarajiwa kuendelea kutoa salamu za rambirambi huku wakikumbuka mchango wake mkubwa katika tasnia ya soka nchini.

Thursday, April 16, 2026

BALAA LA YANGA KWA MBEYA CITY LEO


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo mawili dakika ya saba na 82, kiungo Muivory Coast, Pacome Peodoh Zouzoua dakika ya 10 na 44, kiungo Mkongo Maxi Mpia Nzengeli dakika ya 16 na beki mzawa, Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ dakika ya 45’+2.

Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 47 katika mchezo wa 19 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi nane zaidi ya watani, Simba SC ambao hata hivyo wana mechi moja mkononi.

Kwa upande wao Mbeya City baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi zao 17 za mechi 19 pia nafasi ya 13 kwenye ligi ya timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.  

Wednesday, April 15, 2026

WANANCHI WASHIRIKI UJENZI WA JENGO LA HUDUMA ZA UZAZI

 

Na, Ernest Magashi

Wananchi wa Kata ya Katente, Wilaya ya Bukombe mkoani Geita, wamejitokeza kwa wingi kushiriki zoezi la kusafisha eneo litakalojengwa jengo la huduma za uzazi katika Hospitali ya Wilaya ya Bukombe. Ushiriki huo unaakisi mwamko mkubwa wa jamii katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuboresha huduma za afya, hususan kwa mama na mtoto.Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Marycelina Mbohoma, ametoa shukrani za dhati kwa Rais kwa kuidhinisha utoaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo muhimu. Amesema uwekezaji huo ni hatua madhubuti katika kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga.Aidha, Mbohoma amewataka wananchi kuendelea kuwa walinzi wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao.“Mradi huu ni wetu sote. Ni wajibu wetu kuulinda, kuuthamini na kutoa taarifa mapema pale tutakapoona viashiria vya hujuma,” amesisitiza.Kwa upande wake, Mhandisi wa Ujenzi wa Wilaya, Haruni Fashe, amesema jengo hilo la kisasa litagharimu shilingi milioni 660 na linatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi minne.Amefafanua kuwa jengo hilo litakuwa na miundombinu muhimu ikiwemo wodi za wazazi, vyumba vya kujifungulia, chumba cha upasuaji, pamoja na huduma za watoto wachanga.Mradi huu unatarajiwa kuleta mapinduzi makubwa katika utoaji wa huduma za afya wilayani Bukombe, kwa kuhakikisha akina mama wanapata huduma salama na bora wakati wa kujifungua, na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo vinavyoweza kuzuilika.Ushiriki wa wananchi katika hatua za awali za utekelezaji wa mradi huu ni ishara ya umiliki wa kweli wa miradi ya maendeleo na msingi imara wa mafanikio endelevu ya sekta ya afya.Mkazi wa Katente, Evodia Simon,alisema wamejitokeza kujitolea nguvu zao kama sehemu ya kuitikia wito wa maendeleo unaotolewa mara kwa mara na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, na viongozi wengine wa serikali katika mikutano ya hadhara.

SIMBA SC YAIBAMIZA FOUNTAIN GATE 3-0

 


TIMU ya Simba SC imeonyesha ubabe wake jioni ya leo kwa kuibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Fountain Gate FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara uliopigwa kwenye dimba la Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha. 


Simba ilianza kuonesha makali yake mwishoni mwa kipindi cha kwanza, ambapo kiungo fundi kutoka Zambia, Clatous Chama alifungua ukurasa wa mabao dakika ya 45+7 kwa mpira uliowaacha mabeki wa Fountain Gate wakitazamana. 


Kipindi cha pili hakikuwa na huruma, kwani winga hatari kutoka Senegal, Libasse Gueye aliongeza bao la pili dakika ya 53, akimalizia shambulizi la kasi lililoacha mashabiki wa Simba wakishangilia kwa furaha kubwa. 


Shinikizo la Simba liliendelea kuwa kubwa na kuwavuruga wapinzani wao, hali iliyosababisha kiungo mzawa, Shaaban Mgunda kujifunga dakika ya 71 wakati akijaribu kuokoa hatari langoni kwake—bao lililozika matumaini ya Fountain Gate kabisa. 


Kwa ushindi huo, Simba SC sasa imefikisha pointi 39, ikiendelea kushikilia nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi, ikiwa nyuma kwa pointi tano dhidi ya vinara na mabingwa watetezi, Young Africans SC baada ya kila timu kucheza mechi 18. 


Kwa upande wa Fountain Gate, hali inaendelea kuwa tete baada ya kupoteza mchezo wao wa 10 kati ya 18 walizocheza hadi sasa. 


Wakiwa na sare nne na ushindi nne pekee, wanabaki na pointi 16, wakishika nafasi ya 14 katika ligi yenye timu 16—eneo hatarishi kabisa. 


Vita ya kushuka daraja yazidi kupamba moto 

Kwa mujibu wa kanuni za ligi, timu mbili za mwisho zitashuka moja kwa moja daraja. 

Hata hivyo, zile zitakazomaliza nafasi ya 13 na 14 zitapata nafasi ya kupambana kujiokoa kupitia mechi za mtoano za nyumbani na ugenini. 

Mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu, huku atakayeshindwa akilazimika kupambana tena na timu kutoka Ligi ya Championship katika hatua nyingine ya mchujo—mapambano ya mwisho yatakayobainisha nani atasalia kwenye ligi kuu msimu ujao.

WIZARA YA MAMBO YA NJE KUANDAA UTARATIBU WA KUVUNA MAARIFA YA MABALOZI WASTAAFU


Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imetakiwa kutumia hazina ya maarifa na uzoefu kutoka kwa Mabalozi Wastaafu katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuimarisha diplomasia ya nchi. 


Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo wakati anafungua kikao cha mashauriano kati ya uongozi wa Wizara na Mabalozi Wastaafu kilichofanyika jijini Dar Es Salaam Aprili 15, 2026. 

"Wizara tumeanzisha utaratibu wa kuwa na vikao vya mara kwa mara na Mabalozi Wastaafu ili kuvuna maarifa na uzoefu wao kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia ili ulete nanufaa katika nyanja mbalimbali kama vile, siasa, ulinzi na usalama, uchumi, biashara, uwekezaji na utalii". Balozi Kombo alisema.


Balozi Kombo ametaja mifano ya maeneo ambayo angependa Mabalozi Wastaafu wachangie maarifa na uzoefu walio kuwa nao ili maeneo hayo yaendelee kuwa na manufaa zaidi kwenye nchi..


Maeneo hayo ni pamoja na mwenendo wa ufanyaji wa biashara baina ya Tanzania na nchi nyingine, hususan zilizopo barani Afrika.


Utekelezaji wa Dira 2050 ambayo inalenga uchumi wa Dola bilioni moja, ni eneo lingine muhimu ambalo maarifa ya Mabalozi Wastaafu yanahitajika ili kuhakikisha 

utekelezaji wake unakuwa wa ufanisi.


Waziri Kombo ameongeza kuwa mabadiliko yanayoendelea duniani 

hususan, maendeleo ya kidigitali yanahitaji mikakati thabiti ili nchi iweze kunufaika na kuwa na mipango madhubuti ya kukabiliana na athari zake. Haya yote yanahitaji mawazo ya pamoja ili kuyaendeea kwa ufanisi.


Eneo lingine ambalo Waziri  Kombo alisisitiza umuhimu wa kupata uzoefu wa Mabalozi Wastaafu ni siasa za ulimwengu ambazo zimekuwa hazitabiriki na zinasababisha madhara mbalimbali, hususan katika nchi zinazoendelea kama Tanzania.


Aidha, uzoefu wa Mabalozi Wastaafu unahitajika katika kuendeleza na kuimarisha taswira nzuri ya nchi na hasa nchi inapopewa dhamana ya majukumu ya kimataifa. Balozi Kombo alisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika mwaka 2028 na hivyo maarifa yao ni muhimu ili kuhakikisha nchi inatekeleza jukumu hilo kwa ufanisi. 

Awali, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alisema Wizara inaangalia uwezekano wa kuanzisha utaratibu rasmi kupitia   Ofisi ya Rais-UTUMISHI ili ushirikishwaji wa Mabalozi Wastaafu uwe unatambulika rasmi.



Monday, April 13, 2026

HORMUZ | MAZUNGUMZO YA HORMUZ NI "MECHI ILIYOISHA KABLA HAIJAANZA"

 AZAM MEDIA LTD

Friday, April 10, 2026

SERIKALI YAKUTANA NA MHE. CHAKWERA

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi (kushoto), akiwa  na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera,

Na Mwandishi wetu

Ujumbe wa Serikali ya Tanzania ukingozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi, imekutana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera, na kujadiliana kuhusu namna Tanzania ilivyojidhatiti katika kudumisha umoja, amani na mshikamano miongoni mwa Watanzania.

Kikao hicho kilifanyika katika Kituo cha Mikutano cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyrere (JNICC) siku ya Alhamisi Aprili 9, 2026 mchana baada ya Mheshimiwa Chakwera kumtembelea Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahamoud Thabit Kombo, ikiwa ni ishara ya kuanza rasmi kwa ziara ya Mjumbe huyo Maalum nchini Tanzania.


Katika kikao hicho, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mjumbe huyo Maalum, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchululiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka mssisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.

“Tumekutana na Mheshimiwa Chakwera na tumemueleza mambo mengi kuhusu Tanzania na historia ya nchi hii tangu ipate uhuru mwaka 1961, hali ya siasa na demokrasia nchni, na hatua ambazo serikali inaendelea kuchukua ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo”, ameeleza Waziri Kabudi.

Waziri kabudi ameeleza kuwa kikao hicho kimekuwa kizuri na chenye mafanikio kutokana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola kupata ufafanuzi wa kutosha juu ya masuala mbalimbali yanayoendelea nchini hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania.


Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera anatarajiwa kukutana na wadau mbalimbali ambapo jana Aprili 10, 2026 alikutana na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi pamoja na vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.

Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).


Katika ziara yake hii, Mheshimiwa Chakwera anatarajia pia kukutana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.

Aidha, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, atakutana pia na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

JEH ALAMA ZILIZOPO KWENYE NOTI YA DOLA 1YA MAREKANI ZINAMAANISHA NINI?

Illustration of U.S. $1 bill symbols

Bila shaka unaifahamu noti ya dola 1 ya Marekani. Huenda umeiona maelfu ya mara, na ni mojawapo ya sarafu zinazotambulika zaidi duniani. Inawezekana hata una kadhaa kwenye pochi yako hivi sasa.


Lakini ni mara ngapi umeiangalia kwa makini na kujiuliza maana ya muundo wake na alama zilizopo juu yake?


Kwanza kabisa, alama hizo hazikuchaguliwa kwa bahati. Kwa mfano, picha ya George Washington haikuwa kwenye dola tangu mwanzo. Noti ya kwanza halali ya dola 1 ilitolewa wakati wa Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Marekani, na ilikuwa na picha ya Salmon P. Chase ambaye alikuwa Waziri wa Fedha wakati huo. Washington aliwekwa kwenye dola hiyo mwaka 1869.


Upande wa Mbele wa Dola

Tuanzie upande wa mbele wa noti, ambao una picha ya Washington. Upande huu una vitu vingi, ikiwa ni pamoja na:

Great Seal


Muhuri wa Wilaya ya Benki Kuu (Federal Reserve)

- Herufi na namba ya nafasi ya noti

- Namba ya mfululizo (serial number)

- Muhuri wa Hazina ya Marekani

- Namba ya sahani ya uchapishaji

- Mwaka wa toleo (series)


Kwa mfano, kila noti ya dola 1 ina muhuri wa Wilaya ya Federal Reserve System. Huu ni namba (kama 1 au 2) unaoonekana mara nne kwenye noti. Namba hiyo inaonyesha ni benki ipi ya Federal Reserve iliyochapisha noti hiyo. Mfano, namba 2 ina maana ilichapishwa New York. Pia kuna herufi (kama B) inayobainisha wilaya husika.


Herufi na namba ya nafasi ya noti (mfano B3) inaonyesha nafasi halisi ya noti kwenye sahani ya uchapishaji. Pia kuna namba ya sahani (plate number) inayotumika kutambua sahani iliyotumika kuchapisha noti hiyo.


Namba ya mfululizo (serial number) ni mchanganyiko wa herufi na tarakimu 11, na kila noti ina namba yake ya kipekee. Herufi ya kwanza lazima ifanane na ile ya muhuri wa Federal Reserve; ikiwa haifanani, kuna uwezekano noti hiyo ni bandia.


Mwaka wa toleo (series), kwa mfano 2009, hauonyeshi mwaka noti ilipochapishwa, bali ni mwaka ambao muundo huo ulianza kutumika. Mabadiliko hutokea pale kunapokuwa na mabadiliko kama kuteuliwa kwa Waziri mpya wa Fedha.


Muhuri wa Hazina ya Marekani pia upo upande wa mbele. Umebaki karibu sawa tangu 1789, ukiwa na mizani ya haki, ufunguo, na nyota 13. Muundo wa awali uliundwa na Francis Hopkinson.


Upande wa Nyuma wa Dola

Upande wa nyuma una alama muhimu sana, ikiwemo pande mbili za Muhuri Mkuu wa Marekani (Great Seal), pamoja na namba ya sahani ya uchapishaji.

Muhuri Mkuu wa Marekani (Great Seal)

Muhuri huu ulianzishwa na waanzilishi wa taifa la Marekani. Mnamo 1776, kabla ya Continental Congress kuvunjwa, kamati iliundwa yenye watu kama:

- John Adams

- Thomas Jefferson

- Benjamin Franklin

Lengo lao lilikuwa kubuni muhuri unaoonyesha maadili ya taifa jipya. Muundo wa mwisho uliidhinishwa miaka mitano baadaye, ukibuniwa na Charles Thomson.Great Seal

Upande wa mbele wa muhuri:

Una tai wa Marekani akiwa na Tawi la mzeituni (amani) Mishale (vita)

Kauli mbiu “E Pluribus Unum” (Kutoka wengi, kuwa mmoja)


Juu yake kuna nyota 13 zinazoashiria makoloni 13 ya awali. Mistari ya ngao pia ina maana ya umoja wa majimbo hayo.


Upande wa nyuma wa muhuri:

Una piramidi isiyokamilika yenye safu 13 za mawe, ikionyesha nguvu na uimara. Juu yake kuna jicho lenye mwanga (ishara ya ulinzi wa Mungu).


Maneno yaliyoandikwa ni:

- “Annuit Coeptis” (Mungu ameibariki juhudi yetu)

- “Novus Ordo Seclorum” (Mpangilio mpya wa zama)

Chini kuna namba za Kirumi (1776), kuashiria mwaka wa kuanzishwa kwa taifa.


Hitimisho.

Muundo wa dola 1 una maana nyingi na historia ndefu. Kila alama ina ujumbe wake maalum kuhusu umoja, nguvu, amani na mwanzo wa taifa la Marekani. Na jambo la kuvutia zaidi ni kwamba, kuna sheria inayozuia kubadilishwa kwa muundo wa noti ya dola 1 — hivyo utaendelea kubaki kama ulivyo kwa muda mrefu.

Thursday, April 9, 2026

MODULI YA RUFAA KUBORESHA MNYORORO WA UGAVI WAZINDULIWA

Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.
Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma. 

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema ujenzi wa moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST utachangia kuongeza uwajibikaji, uwazi na ufanisi kwenye mnyororo wa ugavi.

Katibu Mtendaji wa PPAA, James Sando amebainisha hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 na kuongeza kuwa Moduli hiyo imewaunganisha wazabuni wote na Taasisi nunuzi nchini ili kuongeza uwajibikaji katika utatuzi wa migogoro inayotokana na michakato ya ununuzi wa umma. 

“PPAA ni moja kati ya taasisi zinazosimamia ununuzi wa umma nchini, matumizi ya moduli hiyo katika mnyororo wa ugavi yatachangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati uliokusudiwa,” amesema Sando.

Pamoja na mambo mengine, Sando amebainisha kuwa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma yatasaidia kuongeza uwazi, kupunguza gharama, kuokoa muda, utunzaji wa nyaraka na hivyo kuongeza ufanisi katika hukumu zinazotolewa kutokana na michakato mbalimbali ya zabuni za umma.

Sando ameongeza kuwa, PPAA imefanikiwa kushiriki katika utungwaji wa Sera ya Taifa ya Mnyororo wa Ugavi, Sheria ya Ununuzi wa Umma, Kanunuzi za Ununuzi wa Umma na Kanuni za Rufaa za Ununuzi wa Umma ambapo yote ni michango wa Mamlaka ya Rufani katika mnyororo wa ugavi.

Kadhalika, Mamlaka ya Rufani inatarajia kuboresha kipengele cha makundi maalum na vijana ambapo inategemea kuboresha gharama au tozo za kesi kwa makundi maalum pamoja na kuelekeza nguvu kwa vijana na kuhakikisha wanapata fursa ya kudai haki zao katika michakato ya ununuzi wa umma.

Awali akizindua Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba amezielekeza mamlaka, taasisi na wadau wote wanaosimamia utekelezaji wa Sera hiyo kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora, uwazi na utawala wa sheria.‎

‎Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo wakati akizundua Sera hiyo kwa niaba ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Dk. Nchemba amesema changamoto zinazoikumba sekta ya ununuzi wa umma hazitokani na sera au sheria zilizopo, bali ni uzembe na mitazamo ya baadhi ya watendaji.‎

‎Ameongeza kuwa taarifa za ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zinaonesha wazi kuwa kasoro nyingi zinasababishwa na utekelezaji dhaifu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

“Sehemu kubwa ya changamoto hizo zinatokana na hulka, tabia na mitazamo ya watendaji. Hivyo, ni lazima tubadilike ili kufikia malengo ya sera hii,” amesisitiza Dk. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu, amezitaka wizara, taasisi na mamlaka zote kufanya mapitio ya sera, sheria na kanuni zinazokinzana na sera hiyo ili kuweka mazingira rafiki ya utekelezaji wake.

Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar amesema sera hiyo ni mwongozo muhimu utakaosaidia kuimarisha mifumo ya ugavi katika sekta ya umma, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kudhibiti vitendo vya rushwa.‎

Balozi Khamis ameongeza kuwa utekelezaji wa sera hiyo utaongeza ajira, kuimarisha mnyororo wa thamani na kuchochea mageuzi makubwa ya kiuchumi kuelekea dira ya maendeleo ya mwaka 2050.


Sehemu ya viongozi mbalimbali walioshiriki katika uzinduzi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), wakati alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), (Katikati Kulia), akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na viongozi wengine wakisikiliza maelezo kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Bw. James Sando (kushoto), kuhusu mchango wa PPAA katika Mnyororo wa Ugavi, wakati Mhe. Waziri Mkuu alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.

SIMBA SC NAYO YACHANGIA MAPATO KWA TRA UNITED ARUSHA, ZATOKA SULUHU

 


TIMU ya Simba SC imetoa sare ya bila mabao na wenyeji, TRA United katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha. 

Kwa matokeo hayo, TRA inayofundishwa na Kocha Mrundi, Ettienne Ndayiragijje inafikisha pointi 24 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya saba ikiizidi tu wastani wa mabao Dodoma Joni FC baada ya wote kucheza mechi 18. 

Kwa upande wao Simba SC wanafikisha pointi 36 katika mchezo wa 17, ingawa wanabaki nafasi ya pili wakizidiwa pointi nane na mabingwa watetezi, Yanga ambao hata hivyo wamecheza mechi moja zaidi.




AZAM FC YALAZIMISHWA SARE V/s MBEYA CITY

 


TIMU ya Azam FC imelazimishwa sare ya bila kufungana na wenyeji, Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, Babati mkoani Manyara.

Kwa matokeo hayo, Azam FC inafikisha pointi 34 katika mchezo wa 18, ikibaki nafasi ya tatu, wakati Mbeya City inafikisha pointi 17 katika mchezo wa 18 pia, nayo ikibaki nafasi ya 12 kwenye Ligi Kuu inayoshirikisha timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao. 

IRAN YATANGAZA VIPENGELE 10 INAVYODAI KUWA MSINGI WA MAZUNGUMZO YA KUSITISHA MAPIGANO

Men in orange outfits clean up rubble from a destroyed building.
Iran ilitangaza hadharani Jumatano kile ilichodai kuwa ni mfumo wa vipengele 10 kwa ajili ya mazungumzo, ambao Rais Trump aliuelezea kama “msingi unaoweza kufanyiwa mazungumzo” ili kumaliza vita. 

Sehemu kubwa ya vipengele hivyo ilijumuisha madai ya juu sana ambayo yanaonekana kuwa magumu, kama siyo yasiyowezekana, kupatanishwa na malengo ya Marekani.

Afisa mmoja wa Ikulu ya White House alisema vipengele hivyo haviendani na kile alichokuwa anakimaanisha Trump. Afisa huyo alizungumza kwa sharti la kutotajwa jina ili kujadili mazungumzo ya ndani ya White House.

Iran ilitoa toleo lake la pendekezo hilo asubuhi baada ya Marekani na Iran kukubaliana kusitisha mapigano kwa wiki mbili, na linataka wanajeshi wa Marekani kuondoka katika eneo hilo, linarejesha msisitizo wa udhibiti wa Iran juu ya Mlango wa Hormuz wenye umuhimu wa kimkakati, na linadumisha haki ya Iran ya kurutubisha nyuklia.

Mengi ya madai hayo yana uwezekano mkubwa wa kugongana na pendekezo la vipengele 15 lililotolewa na wapatanishi wa Marekani mwezi uliopita.

Pendekezo hilo halikuwahi kuwekwa hadharani, lakini maafisa waliopata taarifa zake, waliozungumza na gazeti la The New York Times kwa sharti la kutotajwa majina kutokana na unyeti wa taarifa, walisema lilihusu programu ya makombora ya balestiki ya Iran na mpango wake wa nyuklia, pamoja na biashara ya baharini. Katika mazungumzo ya awali, wapatanishi wa Marekani walisisitiza kupunguza umbali wa makombora ya balestiki ya Iran na kusitisha kabisa urutubishaji wa nyuklia.

Trump alionekana kurejea mpango huo wa Marekani siku ya Jumatano, akiandika kwenye mitandao ya kijamii kuwa “vipengele vingi kati ya vile 15 tayari vimekubaliwa,” na kurudia msimamo wake wa “kutokuwepo kabisa kwa urutubishaji wa urani.”


MASHARTI 10 YA IRAN AMBAYO NI MWIBA KWA MAREKANI

1. Dhamana ya Marekani ya kutofanya uchokozi dhidi ya Iran

Katika pendekezo la awali la vipengele 15 kutoka kwa wapatanishi wa Marekani, kulikuwa na pendekezo la kusitisha mapigano tu. Maafisa wa Iran wanataka kuhakikisha kuna mwisho rasmi na wa kudumu zaidi wa uhasama.
Hili ni moja ya madai makuu ambayo Iran inalenga kulipa kipaumbele.

2. Iran kudumisha udhibiti wa Mlango wa Hormuz
Hili linaweza kuwa suala gumu sana kufikiwa mwafaka. Uwezo wa Iran kudhibiti au kuzuia usafiri wa meli katika mlango huo, ambako hupita takriban theluthi moja ya mafuta ya dunia, umekuwa ukitikisa uchumi wa dunia. Ni vigumu sana kwa Marekani au nchi za Kiarabu za Ghuba kukubali hilo.

3. Kumaliza vita vya kikanda katika nyanja zote, ikiwemo dhidi ya mshirika wa Iran, Hezbollah nchini Lebanon
Hili linaweza kuwa eneo la kufikia muafaka baadaye.


Marekani na Israel zinataka Tehran kudhibiti mtandao wa makundi ya wanamgambo inayounga mkono katika eneo hilo, unaoitwa “Axis of Resistance.” Baadhi ya makundi hayo yameishambulia Marekani, nchi za Ghuba na Israel kwa kutumia ndege zisizo na rubani na makombora.


Miongoni mwao ni Hezbollah ya Lebanon, ambayo ilishambuliwa vikali na Israel, ambayo baadaye ilitangaza mipango ya kukalia sehemu za kusini mwa Lebanon.
Israel imesema usitishaji wa mapigano hauhusu operesheni zake nchini Lebanon, hivyo bado haijulikani kama suala hilo linaweza kuingizwa kwenye makubaliano ya muda mrefu.

4. Kuondolewa kwa majeshi ya Marekani katika vituo vyote vya kijeshi katika eneo hilo
Marekani ina vituo vya kijeshi katika nchi za Ghuba, Israel na Iraq. Ni vigumu kufikiria hali ambayo Marekani itakubali sharti hili.

5. Fidia kwa Iran kutokana na uharibifu wa vita
Iran imepata uharibifu mkubwa, si tu kwenye maeneo ya kijeshi bali pia miundombinu muhimu kama viwanda vya dawa, chuma, madaraja, vyuo vikuu na nishati.
Hakuna dalili kwamba Marekani iko tayari kulipa fidia hiyo.

6. Kutambuliwa kwa haki ya Iran ya kurutubisha nyuklia
Hili linapingana kabisa na msimamo wa Trump, ambaye amesisitiza kutokuwepo kabisa kwa urutubishaji wa urani.


Baadhi ya wanadiplomasia wa kikanda wamependekeza Iran iruhusiwe urutubishaji mdogo sana kwa matumizi ya kiraia, lakini bado haijulikani kama Marekani itakubali.

7. Kuondolewa kwa vikwazo vya moja kwa moja (primary sanctions)
Marekani imeweka vikwazo mbalimbali vya kifedha dhidi ya Iran tangu mapinduzi ya mwaka 1979.

Katika mazungumzo ya awali, kulikuwa na wazo la kuondoa baadhi ya vikwazo hivyo badala ya Iran kufanya mabadiliko kwenye mpango wake wa nyuklia. Trump pia aligusia uwezekano wa kupunguza ushuru na vikwazo.

8. Kuondolewa kwa vikwazo vya sekondari (secondary sanctions)
Hivi ni vikwazo vinavyolenga pia nchi au kampuni nyingine zinazofanya biashara na Iran.
Kipengele hiki kinaweza kujadiliwa kulingana na makubaliano yatakayofikiwa.

9. Kufutwa kwa maazimio yote dhidi ya Iran na Bodi ya Magavana ya Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA)
Mwaka jana, shirika hilo lilipitisha azimio dhidi ya Iran likidai haitekelezi wajibu wake wa kudhibiti usambazaji wa silaha za nyuklia. Iran ililaani hatua hiyo kama ya kisiasa.
Marekani haiwezi kulazimisha kufutwa kwa maazimio hayo moja kwa moja, lakini inaweza kushawishi washirika wake.

10. Kufutwa kwa maazimio yote ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa dhidi ya Iran
Kumekuwa na maazimio kadhaa dhidi ya Iran, hasa kuhusu nyuklia. Mwaka uliopita, Umoja wa Mataifa ulirejesha vikwazo dhidi ya Iran kwa kukiuka makubaliano ya mwaka 2015.


Marekani inaweza kujaribu kushawishi washirika wake, lakini hilo litahitaji makubaliano mapana zaidi na Iran.

KILA MWENYE PUMZI AKAPELA - AIC Chang'ombe Choir (CVC)

 Kipindi cha Pasaka ya Mwaka huu 2026 tumepata nafasi ya kuwafikia AIC Chang'ombe Choir ya Jijini Dar es salaam, waliokuwa na mwaliko wa kushiriki ibada ya uimbaji katika kanisa la AICT Makongoro jijini Mwanza.

Wednesday, April 8, 2026

MUDA ATUPIA MBILI YANGA SC IKIICHAPA PAMBA 3-0 KIRUMBA

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya wenyeji, Pamba Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na viungo Mudathir Yahya Abbas mawili dakika ya nane na 34 na Mkongo, Maxi Mpia Nzengeli dakika ya 67.


Kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi 44 katika mchezo wa 18 kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi tisa zaidi ya watani wao, Simba SC ambao pia wana mechi mbili mkononi.

Kwa upande wao, Pamba Jiji FC baada ya kupoteza mchezo wa leo wanabaki na pointi zao 26 za mechi 18 sasa wakishuka kwa nafasi moja hadi ya sita.

Tuesday, April 7, 2026

KOCHA PEDRO AIVULIA KOFIA PAMBA JIJI ILA ASEMA ALAMA TATU UHAKIKA.

NA ALBERT G. SENGO, MWANZA Kuelekea mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Pamba Jiji na Young Africans (Yanga SC) utakaopigwa katika dimba la CCM Kirumba jijini Mwanza, Kocha Mkuu wa Yanga, Pedro Goncalves, amesema timu yake inatarajia upinzani mkali kutoka kwa wenyeji hao. Goncalves ameeleza kuwa Pamba Jiji ni timu imara inapocheza nyumbani, ikiwa bado haijapoteza mchezo wowote katika uwanja wake, huku timu kadhaa kubwa zikishindwa kuondoka na alama tatu hali inayoashiria ugumu wa mchezo huo. “Tunatarajia mazingira magumu ya mchezo. Uwanja hautaruhusu soka la kuvutia, lakini hilo halibadilishi malengo yetu. Tunapaswa kuwa imara, makini na kupambana ili kupata alama tatu,” amesema kocha huyo. Ameongeza kuwa wapinzani wao wanacheza kwa nguvu na kasi, wakitumia vyema faida ya uwanja wa nyumbani pamoja na sapoti kubwa kutoka kwa mashabiki wao. “Ni timu inayocheza kwa msukumo mkubwa wa mashabiki wake. Wanajua namna ya kutumia mazingira yao kwa faida yao, hivyo nasi tumelazimika kujiandaa kisaikolojia na kimkakati kukabiliana na hali hiyo,” aliongeza. Kocha huyo ameonyesha imani kubwa kwa kikosi chake, akisisitiza kuwa wachezaji wake wamekuwa wakionyesha ari, nidhamu na uwezo wa kujiboresha kila siku. “Nina imani kubwa na wachezaji wangu. Kesho tunahitaji kuonyesha moyo wa upambanaji, ushindani, nidhamu na umoja ili kufanikisha malengo yetu,” amesema. Kwa upande wake, beki wa Yanga, Israel Mwenda, aliyewakilisha wachezaji, amesema wanatambua umuhimu wa mchezo huo pamoja na ubora wa mpinzani wao. “Kwa niaba ya wachezaji wenzangu, tunatambua umuhimu wa mchezo wa kesho. Utakuwa na ushindani mkubwa na kila mmoja wetu analitambua hilo. Tumerejea katika ari ya ushindi na tunakusudia kuendeleza mwenendo huo,” amesema Mwenda. Aidha, ametoa wito kwa mashabiki wa Mwanza na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kuisapoti timu hiyo. “Tunawaalika Wananchi kujitokeza kwa wingi kutupa sapoti. Tunawahakikishia kuwa tutapambana kwa nguvu zote ili waondoke wakiwa na furaha,” aliongeza. Akijibu swali la waandishi wa habari kuhusu presha ya mchezo huo, Mwenda amesema hawana presha yoyote, akisisitiza kuwa kucheza katika klabu kubwa kama Yanga kunahitaji uzoefu wa kukabiliana na mazingira yoyote. “Hatuna presha. Unapocheza Yanga lazima uwe tayari kukabiliana na hali yoyote. Tumejielekeza katika maandalizi sahihi na umakini mkubwa tukitambua umuhimu wa mchezo huu,” alihitimisha.

NI ZAIDI YA NUSU KARNE SASA TANGU MAUAJI YA KARUME.

 


🏴Leo ni kumbukizi ya miaka 54 tangu kuuawa kwa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Sheikh Abeid Amani Karume, kiongozi aliyebeba alama ya mapambano, mageuzi na ujenzi wa taifa jipya visiwani humo.


Karume aliuawa Aprili 7, 1972, kwa kupigwa risasi katika eneo la Kisiwandui, Unguja, yalipokuwa Makao Makuu ya Chama cha Afro-Shiraz. Tukio hilo liliacha pengo kubwa katika uongozi wa Zanzibar na historia ya siasa za Tanzania kwa ujumla.

Miaka zaidi ya nusu karne baadaye, wadau wa siasa na wananchi kwa ujumla wanaendelea kumkumbuka kwa misingi aliyoiasisi ikiwemo msisitizo wa usawa wa kijamii, uzalendo, na ujenzi wa uchumi unaowajali wananchi wa kawaida. Hata hivyo, baadhi yao wanahoji kuwa dira na maono hayo yameanza kufifia au kupuuzwa kadri nyakati zinavyobadilika.

Kumbukizi hii si tu ya kuenzi maisha yake, bali pia ni fursa ya kutafakari juu ya misingi aliyosimamia, na kujiuliza kama bado ina nafasi katika kuongoza maendeleo ya Zanzibar ya leo.
.
.
#KarumeDay