ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, March 30, 2026

NEMC KUPEWA NGUVU ZAIDI KUDHIBITI MAZINGIRA-MASAUN

 

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamo wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Yusuf Masauni, amesema serikali inatarajia kufanya maboresho ya sheria ili kuipa mamlaka zaidi Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kushughulikia moja kwa moja wanaokiuka sheria za mazingira, bila kujali kama ni taasisi za umma au binafsi.

Akizungumza Machi 30, 2026 katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha usimamizi wa taka ili kulinda mazingira na afya za wananchi.

Aidha, Masauni amewataka wananchi kutumia kilele cha maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri kama fursa ya kujifunza namna ya kubadilisha taka kuwa rasilimali yenye tija, hatua itakayosaidia kuongeza kipato na kukuza uchumi wa taifa.

Ameongeza kuwa NEMC inahitaji kupatiwa vitendea kazi vya kisasa, ikiwemo helikopta na droni, ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake na kudhibiti uchafuzi wa mazingira.

Sambamba na hilo, ametoa onyo kali kwa wote wanaochafua mazingira, wakiwemo wazalishaji wa mifuko ya plastiki, wanaotupa taka hovyo, wanaomwaga maji machafu baharini na wanaosababisha kelele mitaani, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa bila upendeleo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amesema mkoa wa Dar es Salaam umeanza mpango wa kufundisha somo la uhifadhi wa mazingira kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari, ambapo tayari shule 10 zimechaguliwa kuanza utekelezaji wake.

RAIS DKT.SAMIA APOKEA RIPOTI YA CAG, TAKUKURU NA PPRA LEO IKULU JIJINI DAR ES SALAAM.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali mara baada ya kupokea Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha 2024/25, Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) pamoja na Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye hafla ya kupokea Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha 2024/25, Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) pamoja na Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Bw. Charles Kichere akisoma Muhtasri wa Ripoti yake kwa Mwaka wa Fedha 2024/25, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha 2024/25 kutoka kwa Bw. Charles Kichere, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Bw. Crispin Chalamila akisoma Muhtasari wa Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi hiyo, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo, Bw. Crispin Chalamila, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 30 Machi, 2026.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) Bw. Dennis Simba akisoma Muhtasari wa Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi hiyo, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) kutoka kwa Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo Bw. Dennis Simba, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.

MAFURIKO SIMANJIRO 169,638 WAOMBA MSAADA WA DHARURA

news

TAKRIBANI wananchi 169,638 wa Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara wamekumbwa na mafuriko makubwa yaliyosababisha uharibifu wa makazi, mali na mashamba, hali inayozidi kuongeza ugumu wa maisha kwa wakazi wa eneo hilo.

Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Fakii Lulandala, amesema licha ya idadi hiyo ya wananchi walioathirika lakini pia mafuriko hayo yameharibu zaidi ya ekari 97,429 za mashamba kwa kujaa maji.

Imeelezwa kuwa mafuriko hayo yameathiri kwa kiasi kikubwa kata za Shambalai, Nduruma, Mirerani na Naisinyai, ambako maji yameingia ndani ya nyumba na kusomba mali mbalimbali pamoja na kuharibu vyanzo vya chakula, huku ukihitajika msaada wa dharura.

“Athari hizo zimeacha wananchi wengi bila makazi, chakula na mahitaji muhimu, na wengine wamelazimika kuishi kwa ndugu na jamaa wakati wakisubiri msaada zaidi,” amesema.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, mkazi wa Mererani, Henson Loy, amesema tatizo la mafuriko limekuwepo kwa muda mrefu lakini mwaka huu limeongezeka kwa kiwango kikubwa zaidi.

“Moja ya sababu kuu ya hali hiyo ni miundombinu mibovu ya mifereji ya maji pamoja na barabara kuwa chini, hali inayosababisha maji kushindwa kupita na hivyo kuelekezwa moja kwa moja kwenye makazi ya wananchi,” amesema.

Mkazi wa Utupendana, Jonathan Mkali, amesema mafuriko hayo hujitokeza mara kwa mara kila msimu wa mvua na hudumu kwa muda mrefu, hali inayosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi ikiwemo kukatika kwa mawasiliano na shughuli za kiuchumi.

Katika juhudi za kusaidia waathirika, kampuni ya Permanent Minerals imetoa msaada wa vifaa mbalimbali ikiwemo chakula vifaa vya shule vya watoto,vyandarua,venye thamani ya takriban Sh. milioni 22, ikiwa ni sehemu ya mchango wa wadau katika kukabiliana na athari za mafuriko hayo.

Hata hivyo, Mkuu wa Wilaya ameendelea kutoa wito kwa taasisi mbalimbali, mashirika na wananchi kujitokeza kusaidia zaidi, akisisitiza kuwa mahitaji bado ni makubwa kutokana na ukubwa wa janga hilo.

Aidha, wananchi wameiomba serikali kuchukua hatua za kudumu kwa kuboresha miundombinu ya mifereji ya maji, kupanua mitaro na kuinua barabara ili kuzuia kujirudia kwa mafuriko hayo katika siku zijazo.

"HAPAKUWA NA MTU WAKATI AJALI IKITOKEA MGODINI" - RIPOTI YASEMA

 

Taarifa ya Odisi ya Madini Mbogwe, Geita.


OFISI ya Afisa Madini Mkazi Mbogwe imetoa ufafanuzi kuhusu tukio la ajali lililotokea katika Mgodi wa Dhahabu wa Msasa kwamba wakati tukio linatokea hapakuwa na shughuli zozote za uzalishaji katika eneo husika kwakuwa watendakazi wote walikuwa tayari wameondolewa kupisha ukarabati.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na ofisi hiyo ya madini Mbogwe, katika mgodi huo uliopo katika Kijiji cha Msasa, Runzewe, Wilaya ya Bukombe, Mkoa wa Geita, Machi 29, 2026 majira ya saa 4:00 asubuhi, katika eneo la Area A kulitokea mpasuko wa ardhi ulioathiri maduara manne yenye namba KO 46A, 47A, 48A na 49A.

“Hadi sasa, kwa mujibu wa taarifa ya pamoja ya timu ya uokozi, wakaguzi wa migodi na vyombo vya usalama, hakuna mtu aliyeripotiwa kupata majeraha wala kupoteza maisha kutokana na tukio hilo,” imesema sehemu ya taarifa hiyo.

 Imesema maduara hayo yalikuwa yamesimamishwa uzalishaji kufuatia maelekezo ya wakaguzi wa mgodi yaliyotolewa Machi 27, 2026 ili kufanyiwa ukarabati wa kiusalama. Na kwamba mpasuko huo ulisababisha maduara hayo kutitia ardhini, hali inayohusishwa na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini na kusababisha kulegea kwa udongo na miamba.

“Baada ya kubainika dalili za hatari, wakaguzi wa mgodi walichukua hatua za haraka kuwaondoa mafundi waliokuwa chini ya ardhi pamoja na watu waliokuwa jirani na eneo hilo ambapo wote waliweza kutoka salama.

“Vikosi vya uokozi vilivyohusisha Ofisi ya Mgodi, Ofisi ya Madini, Kikosi cha Uokozi na Zimamoto, Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya usalama vilifika mara moja katika eneo la tukio na kusimamisha shughuli zote za mgodi kwa muda, kuweka utepe wa tahadhari katika eneo lililoathirika na kudhibiti wananchi waliokuwa wakijaribu kusogea katika eneo la hatari,” Imesema sehemu ya taarifa hiyo.

 Imeongeza kuwa shughuli za ukaguzi katika mgodi huo hufanyika kila siku kupitia Ofisi ya Ukaguzi wa Mgodi inayoongozwa na Mkaguzi Mkuu wa Mgodi akisaidiwa na takribani wakaguzi 200 waliopo muda wote katika eneo la mgodi, chini ya usimamizi wa karibu wa Ofisi ya Ofisa Madini Mkazi Mbogwe, Mkaguzi Mkuu wa Migodi Tanzania pamoja na taasisi nyingine za serikali kwa mujibu wa sheria.


Friday, March 27, 2026

MATATANI KWA KUJIFANYA BUBU NA KUTAPELI MTWARA.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, SACP Issa Suleiman.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara limemkamata Ibrahimu Nzumbi Mugendi (31), mkazi wa Kijiji cha Makere, Wilaya ya Kasulu, kwa tuhuma za kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, mtuhumiwa aliwasili mkoani Mtwara Februari 18, 2026 na kufikia katika nyumba ya kulala wageni (jina limehifadhiwa). Februari 26, 2026 alifika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mtwara kupitia Ofisi ya Katibu Tawala wa Wilaya, ambapo aliomba kibali cha kukusanya michango kutoka kwa watu binafsi na taasisi mbalimbali akidai kuwa ana changamoto ya kuongea (bubu).

Alifanikiwa kupatiwa kibali hicho chenye kumbukumbu namba B58/274/03/123, na kuanza kuzunguka katika taasisi za serikali pamoja na kwa watu binafsi akiomba michango.

Hata hivyo, baada ya uchunguzi wa kina, ilibainika kuwa mtuhumiwa hana tatizo lolote la ulemavu wa kuongea, bali alitumia kigezo hicho kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

Mtuhumiwa alikamatwa katika nyumba hiyo ya kulala wageni akiwa na kiasi cha Shilingi 1,800,000 alizokuwa amechangiwa na taasisi pamoja na watu binafsi ndani ya Wilaya ya Mtwara.

Uchunguzi wa awali umeonesha kuwa alifanikiwa kufika katika jumla ya taasisi 10 za serikali na binafsi. Polisi wamesema upelelezi unaendelea, na ukikamilika mtuhumiwa atafikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa hatua zaidi.

Wednesday, March 25, 2026

NI RASMI SASA MO SALAH ATAONDOKA RASMI LIVERPOOL

  Mohamed Salah poses with the Premier League trophy

Mohamed Salah ataondoka Liverpool msimu huu akiwa miongoni mwa wachezaji bora kabisa kuwakilisha klabu hiyo na kung'ara katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL)


Takwimu za Salah zinaonyesha mafanikio yake kwa uwazi, lakini zaidi ya hiyo, kuna hadithi kubwa nyuma ya namba hizo. Mashabiki zake pale Anfield, ambao wanamuita 'Egyptian King' (Mfalme wa Misri), wanakumbuka kila goli lake alilofunga na kila mchango wake kwenye klabu hiyo, jambo ambalo limeifanya historia yake kuwa ya kipekee.

Salah alijiunga na Liverpool kutoka AS Roma mnamo Juni 23, 2017 kwa ada ya pauni milioni 34, kiasi kinachoonekana sasa kama fedha ndogo ikilinganishwa na mafanikio aliyoyapata baada ya kuhamia Liverpool.


Kama Kevin de Bruyne, Salah alikuwa Chelsea awali lakini hakufanya alichotarajiwa, akifunga mabao mawili tu katika mechi 19, akianza katika michezo 10 tu.

Awali aliikataa Liverpool pale alipoondoka Basel na kujiunga na Chelsea Januari 2014. Kumbukumbu yake ya kwanza Anfield ilikuwa pale alipoanza kwenye jezi ya Chelsea katika ushindi wa 2-0 mnamo Aprili 2014, mchezo unaokumbukwa kwa kosa la Steven Gerrard kosa lililozima ndoto za ubingwa uliokwenda Manchester City.

Hata hivyo, tangu alipojiunga rasmi na Liverpool, Salah ameacha kumbukumbu zisizosahaulika, akisaidia klabu hiyo kushinda Ligi ya Mabingwa Ulaya, mataji mawili ya Ligi Kuu, Kombe la FA, EFL Cup sasa Kombe la Carabao, UEFA Super Cup na Kombe la dunia la vilabu, akiboresha historia ya Anfield.


Safari ya maana ya Salah kutoka Basel mpaka Liverpool

Salah alianza safari yake yake polepole Basel, ambapo kocha Murat Yakin aligusia kwamba atakuwa mchezaji nyota pale alipoifunga Tottenham katika robo fainali ya Europa League 2013.


"Kama Mohamed ataendelea kufunga mabao zaidi, hatasalia hapa," Yakin alisema. Na kweli hakusalia, akaendelea kuwa kwenye kiwango bora. Baada ya kuondoka Chelsea, baadaye kwa mkopo Fiorentina kisha AS Roma, Salah alijitengenezea jina kubwa kabla ya kuwasili Anfield, na hata Klopp huenda hakuwa amejua anamchukua mtu wa mwenye kiwango gani hasa.


Goli lake la kwanza akiwa na Liverpool lilikuwa katika sare ya 3-3 dhidi ya Watford. Tangu hapo, hakukoma kufunga. Salah ameifungia Liverpool jumla ya mabao 255 katika mechi 435, akishika nafasi ya tatu kwenye orodha ya wafungaji bora wa klabu hiyo, nyuma ya Ian Rush na Roger Hunt. Katika Ligi Kuu, amecheza mechi 310, akifunga mabao 189 na kutoa pasi za mabao 92, akichangia jumla ya mabao 281, mchango mkubwa zaidi kwa klabu moja katika historia ya Ligi Kuu.


Salah alikuwa mchezaji mwenye ubinafsi wa kipekee lakini pia alichangia kikamilifu kwa timu. Msimu wake wa kwanza ulikuwa mzuri sana, akifunga mabao 44 na kutoa pasi 14 katika mechi 52. Hata hivyo, aliumia kwenye fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Real Madrid, akicheza dakika 31 tu. Mwaka mmoja baadaye, alirekebisha hilo pale Liverpool iliposhinda 2-0 dhidi ya Tottenham, akifunga penati ya mapema.


Salah alikuwa sehemu ya safu bora ushambuliaji akiwa na Sadio Mane na Roberto Firmino, wakiwa na kasi, mbinu na ufanisi wa timu. Alishambulia kutoka upande wa kulia, Mane upande wa kushoto, na Firmino akibadilisha nafasi akicheza kama shambuliaji ama nyuma ya mshambuliaji, ambaye ufundi wake ulisaidia kuboresha viwango vya kila mmoja.


Kila msimu, Salah aliendelea kuwa na uthabiti mkubwa. Katika mechi 310 za Ligi Kuu, kiwango cha ushindi wa Liverpool kilikuwa 63.9%, na katika jumla ya mechi 435, kilikuwa 62.7%. Hii inaonyesha miaka ya heshima kwa klabu na mchezaji.


Hata hivyo mwishoni mwa zama zake hizi, kabla ya michuano ya AFCON, Salah alikabiliana na changamoto ya kocha mpya Arne Slot, baada ya Klopp kuondoka. Kukawa na malumbano kwa sababu ya kuwekwa benchi, lakini mara zote alithibitisha ni bora alipopata nafasi. Baada ya msimu huu wa mwisho, Salah ataondoka akiwa amejenga urithi usioweza kuharibiwa.


Hakuna anayekinzana na ukweli kwamba Mohamed Salah amekuwa miongoni mwa wachezaji bora kabisa kuwahi kuvaa jezi nyekundu ya Liverpool.

MWAKILISHI JIMBO LA CHWAKA AWAKOMBOA WANAFUNZI KWA KUTOA MSAADA WA VIFAA VYA ELIMU

 


NA MWANDISHI WETU, CHWAKA

 
Katika kuboresha sekta ya elimu  Mwakilishi wa Jimbo la Chwaka Mhe. Issa Gavu leo machi 25 amekabidhi vitabu kwa ajili ya kujisomea pamoja na vifaa mbali mbali vya elimu lengo ikiw ni kuleta mabadiliko katika suala zima la kukuza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa skuli  zote la Jimbo hilo.

Akikabidhi msaada huo Mwakilishi wa Jimbo hilo la Chwaka Mhe Gavu amebainisha kwamba wameamua kutoa msaada wa vifaaa mbali mbali kwa wanafunzi hao ikiwemo kompyuta mapakato,Printer, vitabu m,bali mbalin pamoja na mashine ya kubuluzia karatasi (Photocopy mashine)  vyote vikiwa vimegharimu kiasi cha shilingi milioni 12 msaada ambao umetolewa kutoka kwa marafiki wema kwa watu wa Jimbo la Chwaka.


"Leo tumejumuika hapa kwa ajili ya kuweza kukabidhi vifaa mbali mbali kwa wanafunzi ambao wanasoma katika Jimbo la Chwaka na katika siku ya leo tumeweza kukabidhi vifaa mbali mbali ikiwemo vitabu kwa ajili ya kujisomea wanafunzi, Photocopy mashine, pamoja Printer ambavyo vitaweza kuwa ni mkombozi mkubwa kwa wanafunzi kuweza kuongeza kasi ya ufaulu katika masomo yao,"amebainisha Mhe. Gavu.

 Aidha katika tukio hilo pia Mhe. Gavu kwa kushirukiana na marafiki zake wa Jimbo hilo pia wameweza kutoa msaada wa  kugawa  mabati katiika  Skuli ya Mrembo Uroa, washing machine, tanki  la maji na mipira Jendele, pamoja na mafeni na vifaa vya umeme kwa Kituo cha Afya Cheju.


Mhe  amesema  kwamba wameamua kutoa misaada hiyo katika nyanja mbali mbali ikiwa ni moja ya hatua ya kuweza  kuimarisha suala la  elimu kwa wanafunzi  pamoja na kuboresha afya kwa jamii ambayo inawazunguka hasa katika Jimbo la Chwaka na kuwasihi wanafunzi waweze kusoma kwa bidii lengo ikiwa ni kupata na kuongeza maharifa  ambayo yatawasaidia katika siku za usoni.

AUA NA KUJERUHI KISA USHABIKI WA SIMBA NA YANGA

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbrod Mutafungwa.


Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linamtafuta kijana mmoja (jina limehifadhiwa) kwa tuhuma za kumuua Abel Mganga Mazuri (25), mkazi wa Nyamahengo wilayani Kwimba, kwa kumchoma na kitu chenye ncha kali kifuani, pamoja na kuwajeruhi watu wawili.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Machi 25, 2026 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbrod Mutafungwa, tukio hilo lilitokea Machi 24, 2026 majira ya saa 5:30 usiku katika kitongoji cha Nyamahengo, kata ya Sumve.

Inaelezwa kuwa mtuhumiwa alifanya shambulio hilo wakati akiwa na wenzake wakinywa pombe na kuangalia mpira katika banda la maonesho ya mpira, ambapo ugomvi ulizuka kutokana na ushabiki wa timu za Simba SC na Yanga SC.

Kamanda Mutafungwa amesema mtuhumiwa aliwashambulia watu watatu kwa kutumia kitu chenye ncha kali kufuatia mabishano makali yaliyochochewa na ushabiki huo, na kusababisha kifo cha Abel Mazuri.

Waliopata majeraha katika tukio hilo wametajwa kuwa ni Semen Juma Cherehani (26) na Ndubu Mkoi Chagula (26), ambao walijeruhiwa katika maeneo ya mikononi.

Jeshi la Polisi limeeleza kuwa majeruhi wote wamepatiwa fomu za matibabu (PF3) na wanaendelea kupatiwa huduma katika Hospitali Teule ya Sumve, huku hali zao zikiripotiwa kuimarika.

Aidha, Polisi wanaendelea na msako mkali wa kumkamata mtuhumiwa ili afikishwe katika vyombo vya sheria, huku wakitoa wito kwa wananchi kuepuka vurugu zinazotokana na ushabiki wa mpira uliopitiliza mipaka.

Tuesday, March 24, 2026

KAMANDA MURILO AONYA POLISI KUINGILIA MAJUKUMU YA TRA

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro (anayeongoza msafara)

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro, amewataka askari wa Jeshi la Polisi kuacha mara moja kuingilia majukumu ya mamlaka nyingine, ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kufuatia malalamiko ya wafanyabiashara wa Kariakoo kuhusu kunyanyaswa.

Akizungumza wakati wa ziara yake katika eneo la Kariakoo, Kamanda Murilo alikutana na wafanyabiashara wa Jumuiya ya Raha Square kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto za kiusalama. Alisisitiza kuwa si jukumu la polisi kukagua mizigo ya wafanyabiashara wala kushughulikia masuala ya kodi, na kuonya kuwa askari watakaokiuka maelekezo hayo watachukuliwa hatua kali.

Awali, wafanyabiashara walilalamikia tabia ya baadhi ya askari kusimamisha mizigo yao katika makutano ya barabara na kukagua risiti za biashara, wakieleza kuwa hali hiyo imekuwa kero na chanzo cha usumbufu mkubwa.

Akizungumza kwa niaba ya wafanyabiashara, Mwenyekiti wa Kijiwe cha Raha Square, Rweyemamu Erasto, alisema licha ya changamoto hiyo, pia wanakabiliwa na hali duni ya usalama hasa nyakati za usiku wanapofunga biashara zao. Alibainisha kuwa baadhi ya barabara bado hazijafunguliwa ipasavyo, hali inayochangia vitendo vya uporaji, huku biashara zinazofanyika barabarani zikiziba njia na kuongeza hatari ya ajali.

Aidha, wafanyabiashara walieleza wasiwasi wao kuhusu ongezeko la watoto wa mitaani wanaozagaa nyakati za usiku pamoja na uwepo wa watu wasiokuwa na utambulisho unaoeleweka, wakidai hali hiyo inahatarisha usalama wao na mali zao.

Katika mapendekezo yao, waliomba kufunguliwa kwa barabara zote za Kariakoo, kuondolewa kwa biashara zisizo rasmi barabarani, pamoja na kufungwa kwa mifumo ya kamera za ulinzi (CCTV) ili kusaidia kudhibiti uhalifu.

Akijibu hoja hizo, Kamanda Murilo amesema Jeshi la Polisi linaendelea kushirikiana na mamlaka mbalimbali kuhakikisha eneo la Kariakoo linakuwa salama. Aliahidi kufanyia kazi changamoto zote zilizotolewa na wafanyabiashara.

Kuhusu tatizo la watoto wa mitaani, alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na taasisi husika inaendelea kutafuta suluhisho la kudumu kwa kuchunguza chanzo cha tatizo hilo. Pia alionya juu ya matumizi holela ya bajaji na maguta katika barabara kuu, akisema hatua madhubuti zitachukuliwa kudhibiti hali hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya usalama.

Kamanda Murilo amesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia ya kamera za ulinzi, akibainisha kuwa zimekuwa msaada mkubwa katika kubaini na kudhibiti uhalifu.

Amemalizia kwa kuwahakikishia wafanyabiashara wa Kariakoo kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kutoa ulinzi wa saa 24 ili kuhakikisha usalama wa watu na mali zao.

TRA PWANI YAWAKUMBUKA WATOTO YATIMA NA MAKUNDI MAALUMU KWENYE TUKIO MAALUM LA IFTAR

 


NA VICTOR MASANGU, PWANI

Mamlaka ya mapato (TRA) Mkoa wa Pwani katika kurudisha fadhila kwa jamii imeamua kuandaa Iftar maalumu kwa ajili ya kufuturisha makundi mbali mbali ikiwemo watoto yatima, viongozi wa madhehebu ya dini, viongozi wa serikali ikiwa pamoja na wananchi kutoka maeneo ya Mkoa wa Pwani.

Tukio hilo  maalumu la Iftar limefanyika katika viwanja vya nje ya Ofisi ya TRA na kuongozwa na Sheikh wa Mkoa wa Pwani Khamis Mtupa pamoja na kuhudhuliwa na viongozi wengine wa dini pamoja na watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu kutoka kituo cha Fadhila kilichopo kata ya Misigusugu Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha.

Katika  tuki hilo Sheikh wa Mkoa wa Pwani Khamis Mtupa ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi hakusita kuupongeza kwa dhati uongozi mzima wa TRA Mkoa wa Pwani kwa kuamua kurudish fadhila kwa jamii na kukusanya makundi mbali mbali ikiwemo watoto yatima na kula nao chakula cha jioni ikiwa ni moja na nguzo muhimu sana hasa katika kipindi hiki  cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

"Kwa upande wangu mimi kipekee nipende kuchukua  fursa hii kuwashukuru kwa dhati uongozi mzima wa TRA pamoja na meneja wake kwa kuona umuhimu mkubwa wa kutukutanisha siku ya leo katika hili tuko la Iftari kwa kweli mmefanya jambo la msingi sana na kingine nimependa mmekusanya makundi tofauti ikiwemo na watoto yatima ambao tumejumuika nao hapa katika tukio hilo na Mungu awabariki sana na muendelee na moyo huu wa kujitolea,"amebainisha Sheikh Mtupa.

Pia katika hatua  nyingine amebaainisha kwamba katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadani taasisis na watu mbali mbali wanapaswa kufanya matendo ya huruma kwa wahitaji ikiwemo suala la kuwafuturisha watu    wenye uhitaji na kuweza kutoa misaada mbaali mbali ambayo itaweza kuwasaidia walengwa na kwamba zoezi hilo liwe endelevu ikiwemo kusaidia jamii.

Kadhalika Sheikh Mtupa ameipongeza TRA Mkoa wa Pwani kwa kuweka mikakati madhubuti ambayo imeweza kusaidia kwa kiassi kikubwa katika suala zima la kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mapato ambayo yanapelekea kuleta mabadiliko makubwa katika maendeleo kwa wananchi.

Kwa   upande wake Meneja wa mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani Masawa Masawa amesema kwamba wameamua kufanya tukio la Iftar hiiyo na kuwakutanisha makundi mbali mbali ikiwa ni moja ya kurudisha fadhila kwa jamii pamoja na kukutana na watoto yatima na kula nao chakula cha jioni.

Meneja huyo amesema kwamba lengo kubwa la TRA Mkoa wa Pwani ni kuendelea kushirikiana begaa kwa bega na jamii katika mambo mbali mbali ikiwemo kukutana kwa pamoja na kubadilishanaa mawazo pamoja naa kula cha jioni kwani ni moja ya kuongeza wigo mpana ya katika kujenga mahusiano mazuri kwa jamii.

Nao baadhi ya watoto yatima ambao wamehudhulia      katika tukio hilo  wamesema wamefurahishwa na uongozi  mzima wa TRA kwa kuweza kuwakumbuka katika kuwakutanisha katika Iftar hiyo na kusema kwamba wamejisikia furaha na amani ya kukutana na jamii nyingine.

Monday, March 23, 2026

MANCHESTER CITY YAICHAPA ARSENAL 2-0 NA KUTWAA CAFRABAO CUP

 

SHEREHE: Manchester City WAKINYANYUA JUU KOMBE LA Carabao BAADA YA KUITANDIKA Arsenal KATIKA UWANJA WA Wembley

TIMU ya Manchester City FC jana ilifanikiwa kutwaa Kombe la Ligi England baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Arsenal katika mchezo wa Fainali uliofanyika Jumapili ya terehe 22 Machi 2026 Uwanja wa Wembley Jijini London.

Mabao yaliyoipa Manchester City taji la ya Carabao Cup yalifungwa na beki chipukizi wa kushoto wa umri wa miaka 21 ambaye pia hucheza nafasi za kiungo, Nico O'Reilly yote mawili dakika ya 60 na 64.

Hilo linakuwa taji la tisa la Carabao kwa Manchester City baada ya awali kulibeba katika misimu ya 1970, 1976, 2014, 2016, 2018, 2019, 2020 na 2021.

Mara ya mwisho Arsenal kutwaa taji iliuwa ni Agosti mwaka 2020 walipobeba Kombe la FA Cup chini ya kocha wa sasa, Mikel Arteta kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Chelsea kwenye Fainali hapo hapo Uwanja wa Wembley.

ZAMALEK HIYOOoo NUSU FANALI KOMBE LA SHIRIKISHO AFRIKA

 


TIMU ya Zamalek SC ya Misri imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya ushindi wa mabao 2-1 na AS Otoho d'Oyo ya Kongo-Brazzaville katika mchezo wa marudiano wa Robo Fainali jana Uwanja wa Cairo International Jijini Cairo nchini Misri.

Kwa matoke ohayo, Zamalek inakwenda Nusu Fainali kwa ushindi wa jumla wa 3-2 kufuatia sare ya kufungana bao 1-1 katika mchezo wa kwanza Machi 14 Uwanja wa Alphonse Massamba-Débat Jijini Brazzaville.

Mambo hayakuwa mazuri kwa timu za Wydad Athletic ya Morocco na AS Maniema Union ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ambazo zote zilitolewa kwa mabao ya ugenini zote.

Wydad Athletic ilitoa sare ya kufungana mabao 2-2 na Olympic Club de Safi, zote za Morocco jana Uwanja wa Mfalme Mohammed wa Tano Jijini Casablanca.
Kwa matokeo hayo, Olympic Club de Safi inakwenda Nusu Fainali kwa faida ya mabao ya ugenini katika sare hiyo ya jumla ya 3-3 baada ya awali timu hizo kufungana bao 1-1 kwenye mchezo wa kwanza Machi 16 Uwanja wa El Massira mjini Safi.

Nayo AS Maniema Union ilichapwa 1-0 USM Alger bao pekee la kiungo Brahim Benzaza dakika ya 30 Uwanja wa Julai 5, 1962 Jijini Algiers nchini Algeria.

USM Alger inakwenda Nusu Fainali kwa faida ya mabao ya ugenini katika sare hiyo ya jumla ya 2-2 kufuatia kufungwa 2-1 na AS Maniema Union kwenye mchezo wa kwanza wa Robo Fainali Machi 15 Uwanja wa TP Mazembe Jijini Lubumbashi.
Mechi za kwanza za Nusu Fainali zitachezwa Aprili 10 na marudano Aprili 17, Zamalek ikimenyana na CR Belouizdad iliyoitoa Al Masry ya Misri pia na USM Alger ikicheza na Olympic Safi.

MV LIEMBA MELI YENYE HISTORIA DUNIANI ZAIDI YA MIAKA 100 YAKARABATIWA KWAAJILI YA USAFIRI NA UTALII

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

Meli kongwe zaidi inayobaki duniani na bado inaendelea kutoa huduma, MV Liemba, yenye umri wa zaidi ya miaka 100, inaendelea kufanyiwa ukarabati mkubwa unaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 32. Uamuzi wa kuikarabati umetokana na tathmini iliyoonesha kuwa kujenga meli mpya kungehitaji zaidi ya shilingi bilioni 80. Kutokana na umuhimu wake wa kihistoria na kiuchumi, Serikali ya Tanzania imechagua kuirudishia uhai meli hiyo ili iendelee kutumika katika usafiri na usafirishaji katika Ziwa Tanganyika, huku pia ikibaki kuwa kivutio muhimu cha historia na utalii. Akizungumza kuhusu umuhimu wa meli hiyo mbele ya vyombo vya habari jijini Mwanza, Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa amesema kuwa MV Liemba ni hazina ya kipekee duniani, akibainisha kuwa watu kutoka nchi mbalimbali na hata mabara tofauti husafiri kuja kuiona. "Watu wanasafiri kutoka nchi za mbali na mabara tofauti kuja tu kuiangalia meli hii ambayo, licha ya kuwa na umri wa zaidi ya karne moja, bado inaendelea kutoa huduma," amesema. #mvliemba #samiasuluhuhassan #GersonMsigwa #tanzania

SERIKALI YAWEKEZA ZAIDI YA TRILIONI 1 KUBORESHA USAFIRI WA MAJINI

NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

Serikali ya awamu ya Sita imewekeza zaidi ya shilingi trilioni moja katika kuimarisha sekta ya usafiri wa majini nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo pamoja na kukuza uchumi wa Taifa.


Hayo yameelezwa na Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa wakati akizungumza na vyombo vya habari jijini Mwanza, ambapo amesema uwekezaji huo umehusisha ununuzi wa meli mpya, ukarabati wa meli zilizopo pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya bandari katika maziwa makuu na ukanda wa Bahari ya Hindi.

Amesema hatua hizo zinalenga kuongeza usalama wa usafiri majini, kurahisisha usafirishaji wa mizigo na abiria, pamoja na kuimarisha biashara kati ya Tanzania na nchi jirani.

Msigwa amesema miongoni mwa mafanikio ya uwekezaji huo ni kuanza kwa huduma za meli ya MV Mwanza, ambayo ina uwezo wa kubeba abiria 1,200, tani 400 za mizigo pamoja na magari makubwa matatu na magari madogo 20.


Ameeleza kuwa Serikali pia inaendelea na ukarabati wa meli ya MV Umoja pamoja na meli ya MT Ukerewe, huku ikiendelea na ujenzi wa meli mpya ya mizigo yenye uwezo wa kubeba tani 3,000 katika Ziwa Victoria.


Katika Ziwa Tanganyika, Serikali inaendelea na ukarabati wa meli ya MV Liemba ili kuboresha huduma za usafiri kwa wakazi wa maeneo ya mwambao na nchi jirani.

Mbali na miradi hiyo, Serikali pia inaendelea kuboresha bandari mbalimbali katika maziwa makuu, kujenga bandari mpya pamoja na kuimarisha mifumo ya uokoaji majini kwa kujenga vituo vya utafutaji na uokoaji na kununua boti maalum za uokoaji.


Msigwa amesema hatua hizo zinaonyesha dhamira ya Serikali ya kuifanya sekta ya usafiri wa majini kuwa ya kisasa, salama na yenye mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Taifa.