ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, February 10, 2026

DKT. MWIGULU AONGOZA KIKAO CHA KAMATI YA KITAIFA YA AFCON 2027.


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amekutana na Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa ajili ya kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.

 

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amefanya kikao hicho leo Jumanne (Februari 10, 2026) Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam.

 


Katika mazungumzo hayo, Waziri Mkuu amepongeza kazi kubwa inayofanywa na kamati hiyo, akieleza kuridhishwa na kasi na mwelekeo wa maandalizi yanayoendelea. 

 

“Maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa yanaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha Tanzania inakuwa mwenyeji bora wa michuano hiyo”.

 


Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ni muhimu kuwepo kwa ushirikishwaji wa sekta zote, “mawaziri, makatibu wakuu pamoja na watendaji wengine hakikisheni mnazishirikisha sekta zetu kila mmoja katika eneo lake, tunataka kuona matokeo chanya katika michuano hii”.

 


Aidha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewataka wajumbe wa kamati hiyo kuhakikisha kila mmoja anasimamia kikamilifu eneo lake la uwajibikaji, ili hatua zote za maandalizi zikamilike kwa muda uliopangwa na kwa viwango vinavyokubalika.

ULEGA AWAAGIZA WAKANDARASI: LIPENI WAFANYAKAZI KWA MUJIBU WA SHERIA

 

Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewaagiza wakandarasi wote nchini kuhakikisha wanalipa watumishi wao kwa kuzingatia sheria za kazi za Tanzania, akisisitiza kuwa Serikali haitavumilia vitendo vya kuwapunja wafanyakazi.


Waziri Ulega alitoa agizo hilo wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Same–Kisiwani–Mkomazi yenye urefu wa kilometa 100.5, mradi unaotekelezwa na mkandarasi M/S China Communication Construction Company Ltd.


Katika ukaguzi huo, Waziri alipokea malalamiko kutoka kwa wafanyakazi wakidai kuwa wanalipwa mishahara midogo isiyokidhi viwango vya kisheria. Hali hiyo ilimlazimu Waziri Ulega kutoa onyo kali kwa mkandarasi huyo kuhakikisha anarekebisha mara moja dosari hizo.


Ingawa msimamizi wa kampuni hiyo alimwahidi Waziri kuwa suala hilo litafanyiwa kazi, Mbunge wa Mkuranga alisema hatasita kulifikisha suala hilo kwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ili wamiliki wa kampuni hiyo waitwe nchini na kupewa maelekezo ya kufuata sheria za Tanzania kuhusu malipo ya wafanyakazi.


Aidha, Waziri Ulega alionesha kutoridhishwa na kasi ndogo ya utekelezaji wa mradi huo ambao ulianza Januari mwaka jana, akisisitiza kuwa ucheleweshaji haukubaliki kutokana na umuhimu wa barabara hiyo kwa wananchi.


Hata hivyo, aliwahakikishia wananchi wa Same kuwa ujenzi wa barabara hiyo utaambatana na ujenzi wa vituo pamoja na uwekaji wa taa za barabarani ili kuleta mwanga na kuchochea shughuli za kibiashara katika maeneo hayo.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu, alisema matarajio makubwa ya wananchi wa Same ni kuona barabara hiyo inakamilika kwa wakati ili kurahisisha shughuli za kiuchumi na kuchangia maendeleo ya wilaya hiyo pamoja na Taifa kwa ujumla.

TANZANIA YATAJWA MIONGONI MWA NCHI 17 DUNIANI ZENYE MIFUMO BORA YA HIFADHI YA JAMII

 

Tanzania imeandika rekodi mpya ya kihistoria katika sekta ya Kinga ya Jamii! Hatua hii imekuja baada ya nchi yetu kutajwa rasmi kuwa miongoni mwa nchi 17 duniani zenye mifumo bora zaidi ya hifadhi ya jamii. 

Mafanikio haya si ya bahati mbaya, bali ni matokeo ya utekelezaji thabiti wa maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yanayolenga kuinua ustawi wa kila Mtanzania.

Kauli hiyo imetolewa na Nchi Ofisi ya Rais,Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete , wakati akihitimisha mkutano wa siku mbili wa wadau wa sekta ya Kinga ya Jamii jijini Arusha, Februari 10, 2026.
Waziri Kikwete ametaka kuwepo kwa utekelezaji wa kina wa maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan kuhusu kinga ya jamii kwani tayari maono yake Rais Samia yamesababisha mafanikio makubwa .

Amewataka watekelezaji wa sera hiyo kujipanga vyema na kuweka nguvu katika kutekeleza dira na maono yaliyotolewa ili kufikia malengo yaliyokusudiwa. 

Aidha ametoa wito kwa watendaji wote kuyaishi maelekezo ya Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa wakati wa kuhitimisha Bunge la kumi na mbili tarehe 27 Juni 2025 pamoja na kuzingatia ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na dira ya maendeleo.Amesema utekelezaji wa miongozo hiyo utasaidia kupata matokeo chanya katika kuimarisha mifumo ya hifadhi ya jamii nchini. 

Mh Kikwete alisema kwambaTanzania inatekeleza misingi yote tisa ya hifadhi ya jamii ikiwemo fao la familia ambalo huko nyuma lilikuwa halijawekwa sawa lakini sasa linatekelezwa kupitia huduma za kijamii.

Alisema kwamba fao hilo la familia linajumuisha utoaji wa elimu bure, matibabu kwa wazee, matibabu kwa watoto pamoja na akina mama ambapo yote haya ni sehemu ya mchango wa Serikali kwa wananchi wake. 
Alisema ndoto ya Watanzania kuwa ndani ya mfumo wa hifadhi ya jamii sasa inakwenda kukamilika huku akipongeza taasisi mbalimbali zikiwemo za Serikali kwa kazi nzuri ya kuandaa nyaraka na miongozo muhimu kuhusu kinga ya jamii.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mary Maganga akimkaribisha waziri Kikwete alisema Mkutano huo wa siku mbili ulitoa fursa ya kipekee kwa wadau kujadili kwa kina kubadilishana uzoefu na maarifa yenye lengo la kuboresha sekta hiyo kwa ajili ya maendeleo ya taifa. 

Aidha alisema kwamba katika mkutano huo washiriki walijengeana uelewa wa pamoja kuhusu umuhimu wa Kinga ya Jamii kwa maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja na Taifa na kuangalia namna ya kuimarisha ushirikiano na uratibu kati ya Serikali, Sekta Binafsi na Wadau wa Maendeleo katika kuimarisha mifumo ya kinga.

Katika kipindi cha siku mbili, washiriki wamepata fursa ya kupokea na kujadili mada mbalimbali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, pamoja na taasisi za PSSSF, NSSF, WCF, NHIF na TASAF. Vilevile, tulipata mafunzo muhimu kuhusu uzingatiwaji wa mienendo ya maisha, hususan mapambano dhidi ya msongo wa mawazo na afya ya akili maeneo ya kazi.

Mkutano huo ulifunguliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Clement Sangu,ambaye alibainisha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta ya kinga ya jamii nchini, ambapo thamani ya mifuko yote ya hifadhi ya jamii imeongezeka maradufu kutoka shilingi trilioni 10.43 mwaka 2020 hadi kufikia shilingi trilioni 24.20 mwezi Desemba 2025. 

Aidha alisema mafanikio hayo yameenda sambamba na uimarishaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), ambao katika awamu ya pili pekee umeweza kunufaisha zaidi ya kaya milioni 1.37 zenye takribani watu milioni 5.5 kwa ruzuku ya zaidi ya shilingi trilioni 1.55.

SHINDA BODA: PIGABET YAGEUZA MICHEZO YA KUBAHATISHA KUWA FURSA YA KIUCHUMI KWA VIJANA

 

Dar es Salaam, Februari 10, 2026: Katika hatua inayoonesha mwelekeo mpya wa michezo ya kubahatisha nchini, PigaBet imezindua kampeni ya “SHINDA BODA” inayolenga si burudani pekee, bali pia kuwawezesha wachezaji—hasa vijana—kujipatia mtaji wa kujiajiri na kujiongezea kipato kupitia ushindi wa pikipiki mpya kila wiki.

Kampeni hiyo inawapa wachezaji wawili kila wiki fursa ya kushinda boda boda, zawadi ambayo kwa wengi imekuwa nyenzo muhimu ya kujiajiri au kuongeza kipato cha kila siku. Kupitia mfumo wa PigaPoints, kila mchezaji anayeshiriki michezo ya PigaBet ikiwemo Sports Betting, Casino na Aviator hujikusanyia pointi kwa kila bet au raundi, hali inayoongeza nafasi yake ya kuingia kwenye droo ya ushindi.

Akizungumza kuhusu dira ya kampeni hiyo, Meneja Masoko wa PigaBet, Arthur Kazora, alisema kampeni ya Shinda Boda inalenga kuwafanya wachezaji waone thamani ya muda na ushiriki wao.

“Tumelenga kumwezesha mchezaji kubadili ushindi kuwa fursa ya maisha. Boda si zawadi tu, ni chombo cha ajira, ni mtaji na ni mwanzo wa safari ya kujitegemea kiuchumi,” alisema Kazola.

Tofauti na kampeni nyingi za awali, Shinda Boda imebuniwa kuunganisha burudani, ushindi na uwezeshaji wa kiuchumi. Wachezaji hawazuiliwi na mchezo mmoja pekee, bali wanaruhusiwa kucheza michezo mbalimbali ndani ya jukwaa la PigaBet, jambo linalowawezesha kukusanya pointi zaidi na kuongeza nafasi ya ushindi.

PigaBet pia imeendelea kuvutia wachezaji kwa promosheni zinazolinda na kuongeza thamani ya mchezaji, ikiwemo 10% Cashback kila Jumatatu kwa bet zilizopotea, Win Boost hadi 1000%, pamoja na huduma ya 2UP na Cashout, vinavyompa mchezaji udhibiti zaidi wa michezo yake.

Kwa kutambua nguvu ya mitandao ya kijamii, kampeni hiyo pia imefungua milango kwa content creators kupitia PigaBet Content Creator Challenge, itakayoratibiwa na mshirika wao WAKA.WIN. Kupitia mpango huo, wabunifu wa maudhui watapata nafasi ya kunufaika kifedha kwa kushiriki kikamilifu katika kuhamasisha kampeni.

Wadau wa michezo ya kubahatisha na vijana kwa ujumla wamehimizwa kujisajili kupitia www.pigabet.co.tz na kushiriki kampeni hiyo, huku PigaBet ikisisitiza umuhimu wa kucheza kwa uwajibikaji kwa watu wenye umri wa miaka 18 na kuendelea.

Kwa mtazamo mpya unaoangazia ajira na uwezeshaji, Shinda Boda imejipambanua kama kampeni inayotazama mbali zaidi ya ushindi wa muda mfupi, na kuweka msingi wa matumaini mapya kwa vijana wanaotafuta fursa za kujikwamua kiuchumi.

>

JKT TANZANIA YAWAGONGA MASHUJAA FC 1-0 MBWENI

 


WENYEJI, JKT Tanzania wameibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mashujaa FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jana jioni Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni Jijini Dar es Salaam.

Bao pekee la JKT Tanzania katika mchezo huo limefungwa na beki Laurian Omar Makame aliyeiadhibu timu yake ya zamani dakika ya 40.

Kwa ushindi huo, JKT Tanzania inafikisha pointi 27 katika mchezo wa 15 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu, wakati Mashujaa inabaki na pointi zake 14 za mechi 14 nafasi ya tisa kwenye msimamo wa ligi yenye timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini  na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.

Wednesday, February 4, 2026

GGML YAKABIDHI NYUMBA KWA JESHI LA POLISI GEITA.

Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela (kati kati) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa nyumba za makazi zilizojengwa na mgodi wa dhahabu wa Geita (GGML) mkoani humo. Kushoto kwake ni Mkuu wa Polisi mkoani humo BI. Safia Jongo na kulia kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa GGML, Duan Campbell

KAMPUNI ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) imekamilisha ujenzi wa nyumba mbili (nyumba pacha) za polisi katika mtaa wa Mgusu kata ya Mgusu wilayani Geita mkoani hapa.

Ujenzi wa nyumba hizo uliofanywa na GGML umehusisha ufadhili wa kiasi cha sh milioni 77 kwa zilizotumika kukamilisha maboma yaliyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi lengo likiwa ni kuboresha makazi ya askari polisi.

Kaimu Mkurugenzi wa GGML, Duan Campbell akiongea katika uzinduzi huo.

Akiongea wakati wa hafla ya kukabidhi nyumba hizo kwa jeshi la Polisi mkoani Geita, Kaimu Mkurugenzi wa GGML, Duan Campbell amesema  kuwa mbali na uchimbaji dhahabu, mgodi huo pia unashiriki katika maendeleo mbalimbali ya kijamii.

Bw.Duan alisema kukamilika kwa mradi huo huo ni muhimu kwani siyo tu unajenga mahusiano ya mgodi na jamii, lakini pia kuimarisha ulinzi na usalama kwenye maeneo yanayozunguka mgodi na wananchi kwa ujumla.


Alisema sera ya GGML inaamini kuwa Jamii imara inategemea taasisi imara za ndani, na moja ya taasisi zinazoshikilia uimara na ustawi wa jamii kila siku ni jeshi la polisi.


"Askari polisi wanaposaidiwa kwa kupata makazi bora, utulivu na heshima, uwezo wao wa kuitumikia jamii unaimarika zaidi, hali hii huongeza utayari wa kazi na kuimarisha usalama wa raia na mali zao. 


"Kampuni ya GGML tunaamini kwamba  Geita salama na yenye ulinzi wa uhakika inachangia moja kwa moja uendelevu wa shughuli zetu", alisema na kuongeza;


"Usalama hauishii ndani ya mgodi pekee, bali usalama upo pia majumbani, barabarani, shuleni, na mitaani ambako watu wanaishi na kufanya kazi", alisisitiza Duan.


Naye Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Mgusu, Nazoro Marcel alisema mradi ulianza kutekelezwa mwaka wa fedha 2019/20 kupitia nguvu za wananchi na wadau wa maendeleo kwa kuchangia ujenzi wa msingi na boma kwa thamani ya sh milioni 19.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Safia Jongo alisema ushirikiano kati ya wananchi, wadau wa maendeleo na viongozi wa Serikali imeleta matokeo chanya kupunguza matukio ya uharifu Geita.


Kamanda Jongo alikiri kuwa mchango GGML kwenye sekta ya ulinzi na usalama inawafanya kuwa wadau wakubwa wa amani ambapo wamesaidia kuboresha utendaji wa polisi mkoani humo.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Bw. Martine Shigela.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela aliipongeza GGML kwa msaada huo huku akiwaomba kutenga bajeti ya ujenzi wa kituo bora cha polisi cha kata ya Mgusui li kukidhi mahitaji ya eneo hilo.

Friday, January 30, 2026

SHABIKI KINDAKINDAKI WA MAN CITY ATUA SERENGETI

 


𝗛𝗔𝗧𝗜𝗠𝗔𝗬𝗘 ile kiu na ndoto ya kuitembelea Tanzania imetimia kwa mwanahabari wa michezo na shabiki sugu wa klabu ya Manchester City ya nchini Uingereza, Braydon Bent.

.
Akiwa katika ziara ya kitalii ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, picha na video za Braydon zimekuwa zikisambaa katika mitandao ya kijamii, zikimuonesha akifurahia kwa karibu vivutio mbalimbali vya wanyamapori pamoja na mandhari ya kuvutia yanayoburudisha macho na kuigusa roho.
.


Katika safari hiyo, Braydon ameambatana na rafiki yake wa muda mrefu na mwalimu wake wa lugha ya Kiswahili, ambaye pia ni mwanahabari na mtangazaji wa kujitegemea, John Jackson maarufu kama JJ. @johnjackson_jj 
.



Kupitia ujumbe aliouandika kwenye mitandao yake ya kijamii, Braydon aliandika:-

“LIONS 🦁 & HOT AIR BALLOON IN SERENGETI 🎈🇹🇿
ASANTE SERENGETI ☀️
SERENGETI NI NOMA! 🇹🇿
DAY 2 @serengeti_national_park
.
Safari hiyo imeendelea kuonesha jinsi Tanzania inavyoendelea kuwa kivutio kikubwa cha utalii wa kimataifa, huku Serengeti ikiendelea kuthibitisha hadhi yake kama moja ya hifadhi bora zaidi duniani.
.
📸 Captures by @infocusstudio.tz

CC: @braydonbentpage

#visittanzani
#visitzanzibar






Thursday, January 29, 2026

SIMBA YAIKUNYUGA MASHUJAA 2-0

 


TIMU ya Simba SC imeibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mashujaa FC ya Kigoma katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam.

Mabao ya Simba SC leo yamefungwa na winga mpya wa kushoto, Libasse Gueye (22) aliyesajiliwa mwezi huu katika dirisha dogo kutoka Teungueth FC ya kwao, Senegal dakika ya 27 na mshambuliaji Suleiman Abdallah Mwalimu 'Gomez' anayecheza kwa mkopo tangu mwanzo wa msimu kutoka Wydad Athletics dakika ya 76.

Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 16 katika mchezo wa saba na kusogea nafasi ya nne, wakati Mashujaa FC inabaki na pointi zake 13 za mechi 11 sasa nafasi ya nane.

Baada ya mchezo huo, Simba SC inarejea kambini kujiandaa na mchezo wa Kundi D Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Espérance ya Tunisia Jumapili kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Ili kufufua matumaini ya kwenda Robo Fainali, Simba inahitaji kushinda Jumapili ikitoka kufungwa mechi zote tatu za mwanzio ikiwemo ya Jumamosi ambayo walifungwa 1-0 na Espérance Uwanja wa Hammadi Agrebi Jijini Tunis nchini Tunisia.

Bao lililoizamisha Simba SC siku hiyo lilifungwa na winga chipukizi wa umri wa miaka 19 wa Burkina Faso, Jack Diarra dakika ya 21 akimtungua kipa wa Kimataifa wa Niger, Mahamadou Tanja Djibrilla Kassali Djibo.

TFF YALIFUNGIA DIMBA LA KMC

 


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeufungia Uwanja wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, maarufu kama KMC Complex, uliopo Mwenge Jijini Dar es Salaam kutotumika kwa mechi za Ligi Kuu kufuatia kupoteza sifa za kikanuni.

Taarifa ya TFF iliyotolewa leo ikiwa na saini ya Meneja Habari na Mawasiliano wa shirikisho hilo, Clifford Mario Ndimbo imezielekeza klabu zinazotumia Uwanja huo mwingine hadi hapo KMC Complex itakapofunguliwa tena baada ya mapungufu yaliyoibainika kufanyiwa marekebisho.

Mbali na wenye mali yao, KMC FC timu nyingine ambayo inatumia Uwanja huo rasmi kama wa nyumbani ni mabingwa wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara kwa miaka minne mfululizo, Yanga SC walioanza kuutumia msimu uliopita. 

WAFANYABIASHARA WAONYWA UPANDISHAJI BEI KIPINDI CHA RAMADHANI


Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba amewataka wafanyabiashara nchini kutowaumiza Watanzania kwa kupandisha bei za bidhaa hususani kipindi hiki cha kuelekea Mwezi Mtukufu wa Ramadhani pamoja na mfungo wa Kwaresma kwa kuwa nchi kwa sasa haina upungufu wa chakula.


Amesema licha ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) nchini kutangaza kuwepo kwa upungufu wa mvua katika maeneo mengi nchini lakini nchi inautoshelevu wa chakula hivyo hakuna sababu ya kupandisha bei za vyakula.


Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Januari 29, wakati akijibu swali la Nancy Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum katika kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. 


Mbunge huyo alitaka kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha nchi inakuwa na utoshelevu wa chakula na kuzuia mfumuko wa bei kuelekea kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na Kwaresma.


“…Kwa sasa tuna chakula cha kutosha, mahitaji ya chakula cha akiba kwa nchi ni takribani tani 150,000 na sasa nchi ina zaidi ya tani 400,000 za akiba ya chakula rai ambayo niliitoa hata nilipokutana na wakuu wa mikoa ni kuendelea kuwahamasisha wananchi  kuzingatia ushauri wa aina ya mazao ya kupanda.”


Pia, Waziri Mkuu amewaelekeza Wakuu wa Mikoa yote nchini wawaelimishe wananchi kuendelea kutumia vizuri chakula walichonacho kutokana na tahadhari ya upungufu wa mvua iliyotolewa na TMA. 


Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameielekeza Wizara ya Afya kuzingatia viwango rasmi vya gharama za huduma na kuharakisha mpango wa kutunga sheria itakayoweka viwango vinavyofanana nchini kote, ili kuondoa hali ya baadhi ya maeneo kuwa na viwango tofauti.


Ametoa maelekezo hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani ambaye alitaka kupata kauli ya Serikali kuhusu viwango wanavyotozwa wananchi kama gharama ya kumuona daktari ambaye ni mwajiriwa na analipwa mshahara na Serikali.

Waziri Mkuu amesema kwa mujibu wa utaratibu wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, wananchi wanahimizwa kujiunga na mifumo ya bima ili kupunguza changamoto ya kuchangia gharama wanapohitaji huduma hospitalini.

Wednesday, January 28, 2026

DEPU AFUNGA MAWILI YANGA YAICHAPA DODOMA JIJI FC 3-1 MWENGE

 


MABINGWA watetezi, Young Africans, maarufu tu kama Yanga SC wametoka nyuma na kushinda mabao 3-1 dhidi ya Dodoma Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara uliochezwa jana usiku katika  Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao Yanga SC yamefungwa na washambuliaji wake wa kigeni, Muangola Laurindo Dilson Maria Aurélio ‘Depu’ mawili kwa penalti dakika ya 45’+2 na la kichwa dakika ya 60 na Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo dakika ya baada ya 66, na hiyo ilikuwa baada ya mshambuliaji mzawa, William Edgar kuanza kuifungia Dodoma Jiji FC dakika ya 41 akiwatoka kwa ustadi mkubwa mabeki wa Yanga kabla ya kumtungua kipa namba moja wa Mali, Djigui Diarra.


Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 22 katika mchezo  wa nane na kurejea kileleni ikiishushia nafasi ya pili JKT Tanzania yenye pointi 21 za mechi 12.


Kwa upande wao Dodoma Jiji baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi 10 za mechi 10 nafasi ya 11.


Baada ya mchezo huo Yanga wanakwenda Zanzibar kujiandaa na mchezo wa marudiano wa Kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri Jumamosi ya Januari 31 Uwanja wa New Amaan Complex.


Ikumbukwe Yanga ilichapwa 2-0 na wenyeji, Al Ahly Ijumaa ya Januari 23 mabao ya winga wa kushoto, Mahmoud Ahmed Ibrahim Hassan ‘Trézéguet’ moja kila kipindi, dakika ya 45’+3 na 75 Ijumaa usiku huu Uwanja wa Borg El Arab Jijini Alexandria, Misri.


Saturday, January 24, 2026

YANGA SC YATELEZA UGENINI, YACHAPWA 2-0 NA AHLY ALEXANDRIA

 


TIMU ya Yanga imeteleza ugenini baada ya kuchapwa mabao 2-0 na wenyeji, Al Ahly katika mchezo wa Kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika usiku huu Uwanja wa Borg El Arab Jijini Alexandria, Misri. 

Mabao yaliyoizamisha Yanga SC jana yote yamefungwa na winga wa kushoto, Mahmoud Ahmed Ibrahim Hassan ‘Trézéguet’ moja kila kipindi, dakika ya 45’+3 na 75.

Kwa ushindi huo, Al Ahly inafikisha pointi saba kufuatia ushindi wa 4-1 dhidi ya JS Kabylie ya Algeria nyumbani na sare ya 1-1 ugenini dhidi ya wenyeji, AS FAR Rabat nchini Morocco.

Yanga wanabaki na pointi zao nne walizovuna kwenye mechi mbili za awali wakishinda 1-0 nyumbani dhidi ya FAR Rabat na sare ya bila mabao, 0-0 ugenini na JS Kabylie.

Mchezo mwingine wa Kundi B leo, JS Kabylie watawakaribisha AS FAR Rabat Uwanja wa Hocine Aït Ahmed mjini Tizi Ouzou.

Yanga wanarejea nyumbani kuwasubiri Al Ahly kwa mchezo wa marudiano Januari 31 Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

𝗦𝗘𝗥𝗜𝗞𝗔𝗟𝗜 𝗬𝗔𝗢𝗠𝗕𝗪𝗔 𝗞𝗨𝗣𝗨𝗡𝗚𝗨𝗭𝗔 𝗭𝗔𝗜𝗗𝗜 𝗚𝗛𝗔𝗥𝗔𝗠𝗔 𝗭𝗔 𝗨𝗦𝗔𝗝𝗜𝗟𝗜 𝗪𝗔 𝗢𝗡𝗟𝗜𝗡𝗘 𝗠𝗘𝗗𝗜𝗔.

Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko (kulia) akimkabidhi Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, tuzo maalum kutoka YouTube baada ya BMG Media kufikisha zaidi ya wafuasi (subscribers) laki moja.

Serikali imeombwa kuendelea kupunguza gharama za usajili wa vyombo vya habari mtandaoni (Online Media) ili kuongeza fursa za ajira na kujiajiri kwa vijana nchini.

.
Ombi hilo limetolewa Jumamosi Januari 24, 2026 na Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, wakati wa hafla fupi ya kupokea tuzo maalum kutoka YouTube baada ya BMG Media kufikisha zaidi ya wafuasi (subscribers) laki moja.
.
Akizungumza katika hafla hiyo, Binagi amesema licha ya Serikali kupunguza gharama za usajili wa Online Media kutoka shilingi milioni moja hadi shilingi laki tano, bado kiwango hicho ni kikubwa kwa vijana wengi, hususan wahitimu wa taaluma ya uandishi wa habari na wabunifu wa maudhui, hivyo ameomba gharama hizo zishushwe hadi shilingi laki moja.
 

Ameeleza kuwa hatua hiyo itachochea vijana wengi zaidi kuanzisha vyombo vya habari mtandaoni na kujiajiri, jambo litakalosaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira nchini.
.
Aidha, Binagi amesema kuanzia mwaka 2026, watengeneza maudhui mtandaoni wameanza kukatwa asilimia tano ya mapato yao na kuwasilishwa serikalini, huku wakiendelea kulipa kodi nyingine mbalimbali, hali ambayo imewaongezea mzigo wa kodi na kusababisha kile alichokitaja kama kulipa kodi mara mbili.
.
 Kutokana na hilo, ameomba Serikali kulitafutia ufumbuzi suala hilo.
.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko, amesema mitandao ya kijamii imeendelea kuwa fursa muhimu kwa vijana katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira, hivyo amewahimiza vijana kutumia mitandao hiyo kwa njia sahihi na yenye tija.
.
Kuhusu gharama za usajili na masuala ya kodi, Soko amesema atayawasilisha kwa mamlaka husika kupitia vikao mbalimbali vya wadau wa habari ambavyo vinaendelea kufanyika kwa lengo la kuboresha na kukuza sekta ya habari nchini.
.
#YouTube 
#mwanza 
#Habari 
CC: @bmgonlinetv 

Wednesday, January 21, 2026

JKT YATANGAZA NASAFI MAFUNZO YA KUJITOLEA.

news
Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jeneral Hassan Mabena

 

JESHI la Kujenga Taifa (JKT) imetangaza nafasi za kujiunga na mafunzo ya kujitolea kwa vijana wa Tanzania Bara na visiwani kwa mwaka 2026 huku likisisitiza nafasi hizo ni bure kwa vijana watakaoomba.

Akizungumza katika Makao Makuu ya JKT, Chamwino Dodoma, Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jeneral Hassan Mabena, amesema usahili wa vijana hao utaanza Januari 26 mwaka huu katika mikoa yote ya bara na visiwani.

Amesema utaratibu wa vijana kuomba mafunzo hayo unaratibiwa chini ya ofisi za wakuu wa mikoa na wilaya na vijana wenye elimu ya kuanzia darasa la saba hadi chuo kikuu wanazo sifa za kuomba, akisema watakaochaguliwa wataanza kujiunga katika kambi mbalimbali za JKT kuanzia February 27 hadi Machi nne mwaka huu.

"Mafunzo haya ni bure wazazi au walezi wasikubali kurubuniwa kutoa fedha ili vijana wao wapate nafasi za kujiunga na mafunzo hayo," amesema Brigedia Jenerali Hassan Mabena.

Amezitaja kozi ambazo wanazipa kipaumbele ni zile za taaluma ya Stashahada ya Teknolojia ya Habari, Stashahada ya Mifumo ya Taarifa za Biashara, Stashahada ya Sayansi ya Kompyuta, Stashahada ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT), Stashahada ya Usalama Mtandaoni.

Nyingine ni Shahada ya Sayansi katika Sayansi ya Kompyuta, Shahada ya Sayansi katika Teknolojia ya Habari, Shahada ya Sayansi katika Uhandisi wa Kompyuta, Shahada ya Sayansi katika Teknolojia ya Habari za Biashara,Shahada ya Sayansi katika Usalama wa Mtandao na Forensics ya kidigitali.

"Nitoe wito kwa Watanzania wenye sifa waende kwenye vijiji kata,tarafa zao ili waweze kujiandikisha, nasisitiza  nafasi hizi haziiuzwi ni fursa iliyotolewa bure kwa Watanzania wote," amesema Brigedia Jenerali Mabena 

Mabena amesema Vijana watakaopewa kipaumbele kuchanguliwa ni waliosoma kozi za masulala ya Sayansi pia akawatahadharisha wazazi kuepuka matapeli.

MBOWE: MZEE MTEI HAKUWA NA SHARI NA MTU.

Mbowe: Mtei hakuwa na shari na mtu

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Freeman Mbowe, amesema Hayati Mzee Edwin Mtei (94), alikuwa ni mtu aliyejenga uhusiano mwema na watu wakati wote.

Mbowe ameeleza hayo Jana Jumanne Januari 20 jijini Arusha, wakati akizungumza na waandishi wa habari alipokuwa msibani.

Akisimulia namna alivyomfahamu Mzee Mtei, Mbowe, amesema hakuwa mtu wa shari, kila alikofanya kazi, alikuwa amejipanga na alikuwa hachagui rafiki ndani na nje ya chama.

Mtei, alifariki dunia usiku wa kuamkia Januari 19 mwaka huu, wakati akikimbizwa kupatiwa matibabu katika Hospitali  ya Selian Jijini Arusha, inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).

"Hakuwa mtu mwenye njaa, alikuwa ni mtu anayejiweza, akifanya siasa za mageuzi katika mazingira yale...misingi mikuu ambayo mzee huyu ametuachia ni sera. Tulikuwa na waasisi 12 wa CHADEMA." amesema Mbowe.

Mbowe amesema Mtei aliwasaidi kupata uzoefu ndani ya chama husuani masuala ya kifedha.

Amesema alikuwa na ujuzi mkubwa wa masuala ya kodi na sera pamoja na uzoefu mkubwa wa masuala ya kidiplomasia.


Wakati wa uhai wake, Hayati Edwin Mtei aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Kanda ya Afrika, Katibu

Mkuu wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC), Gavana wa kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Waziri wa Fedha wakati wa uongozi wa Hayati Julius Nyerere.

MWASISI WA SARAFU

Mbowe amesema: "Mzee Mtei, ndiye aliyekuwa mwasisi wa kwanza wa sarafu ya Tanzania, baada ya ile sarafu ya Afrika ya Mashariki baada ya sisi kuanzisha Benki Kuu ya Tanzania (BoT)".

KUUGUA

Mbowe amesema Mzee Mtei ameugua kwa muda mrefu na familia imepokea kwa uzito msiba huo kutokana na rekodi iliyotukuka, aliyoiweka ndani ya chama na Taifa.

Kwa mujibu wa Mbowe, Mzee Mtei alikuwa akipatiwa matibabu katika hospitali mbalimbali, ikiwemo Hospitali ya Nairobi-Kenya, Dar es Salaam na maeneo mengine kadha wa kadha.

Mbowe alisema: "Natambua CHADEMA  wametuma ujumbe katika msiba huu ili kuungana na familia kwa sababu mzee alikuwa ni mwasisi wa chama chetu. Ni kiongozi ambaye bado tulikuwa tunamuheshimu sana katika njia mbalimbali, kwa sababu misingi yote ya CHADEMA huyu ndiye aliyeianzisha"