ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, February 27, 2026

VIJANA 336 WAHITIMU VETA MWANZA.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa

Jumla ya vijana 336 kutoka Wilaya za Ilemela na Nyamagana mkoani Mwanza wamehitimu mafunzo ya stadi za maisha na ufundi stadi katika fani mbalimbali, na kukabidhiwa vifaa vya kuanzia kazi ili kuwawezesha kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Vijana hao wamehitimu leo Februari 27, 2026 katika VETA Mwanza, ambapo wamekabidhiwa vyeti baada ya kupatiwa mafunzo ya uselemala, uashi, uchomeleaji, ufundi bomba, aluminium, umeme wa magari na majumbani, ufundi magari na upishi. Aidha, walipata elimu ya stadi za maisha, biashara, fedha, ujasiriamali, usawa wa kijinsia pamoja na teknolojia na TEHAMA.

Wahitimu hao ni sehemu ya vijana 400 walioandikishwa katika awamu ya pili ya mradi wa Vijana Elimu, Malezi na Ajira (VEMA) unaotekelezwa na Plan International mkoani Mwanza, kwa lengo la kuwawezesha vijana kutoka familia zisizojiweza kupata ujuzi wa kujiajiri au kuajiriwa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa, amewataka vijana hao kuendeleza ujuzi walioupata na kuvitunza vifaa walivyokabidhiwa. Ameonya kuwa yeyote atakayebainika kuuza vifaa hivyo atachukuliwa hatua za kisheria.

“Huu ni mwanzo wa safari. Mmepewa elimu na vifaa vya kuanzia kazi, hatutarajii kuona mnaishia njiani. Hatutakubali kuona unauza cherehani; utakuwa hujatimiza wajibu wako,” amesema Mkalipa.

Mratibu wa mradi wa VEMA, Gadiel Kayanda, amesema shirika limetumia zaidi ya shilingi milioni 160 kulipia ada za mafunzo na kununua vifaa vya kujifunzia. Aidha, wahitimu hao wamekabidhiwa vifaa vya kuanzia kazi vyenye thamani ya shilingi milioni 69 kulingana na fani walizosoma.

Kwa mujibu wake, tayari vijana 58 kati ya walionufaika wameajiriwa, huku 30 wakijiajiri katika shughuli mbalimbali za uzalishaji.

Mwakilishi wa wahitimu, Raina Revelian, mhitimu wa umeme majumbani, amesema wenzao 64 walishindwa kumaliza mafunzo kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo utoro, kukosa ruhusa kutoka kwa wazazi, ujauzito, magonjwa, umbali na muda mfupi wa mafunzo.

Amesema mafunzo hayo yamewapa ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko na kuwafungua milango ya kujiajiri na kuajiriwa, akitaja siku ya mahafali kuwa ni ya kihistoria kwao.

RAIS DKT. SAMIA AKISHIRIKI MISA TAKATIFU YA KUAGA MWILI WA MWADHAMA POLYCARP KARDINALI PENGO

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini Kitabu cha Maombolezo kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo mara baada ya kuwasili katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa pamoja na viongozi mbalimbali kwenye Misa Takatifu ya kumuombea na kumuaga Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Marehemu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Februari, 2026.




Kengele ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph ililia kwa dakika kumi mfululizo, mara tu baada ya mwili wa Askofu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Hayati Polycarp Kardinali Pengo, kuwasili kanisani hapo.

Na haya ni mambo machache kumuhusu;

1. Jina lake halisi ni nani? Kuna watu wanadhani Mwadhama ni jina lake? Wengine wanadhani Polycarp ni cheo chake. Jina lake ni Polycarp Pengo. Kardinali ni cheo cha Kanisa, na Mwadhama ni kivumishi cha sifa, kama ambavyo Maaskofu huitwa Mhashamu au Mbunge kuitwa Mheshimiwa.

2. Kwanini neno Kardinali lipo katikati ya majina yake na sio mwanzoni? Kwanini hakuitwa Kardinali Polycarp Pengo, akaitwa Polycarp Kardinali Pengo? Kanisa Katoliki lina utaratibu wa majina. Utaratibu huo huitwa modus titulorum ama style of titulature kwa kingereza. Kwa Makardinali wote, neno Kardinali hukaa katikati ya majina yao. Ndiyo maana Kardinali mpya anaitwa Protase Kardinali Rugambwa. Hata Papa Leo XIV kabla ya kuwa Papa aliitwa Robert Kardinali Prevost.

3. Kardinali Pengo ni miongoni mwa Maaskofu wachache kutoka Tanzania waliowekwa wakfu na Papa mwenyewe. Alipoteuliwa kuwa Askofu wa Nachingwea, aliitwa Vatican na kuwekwa wakfu na Papa John Paul II January 6, mwaka 1984 katika Basilika Kuu la Mtakatifu Petro.

4. Watu wengi wanashangaa kumbe Pengo alikuwa msomi wa kiwango cha PhD? Mbona alikuwa hajiiti Dr? Jibu ni kwamba katika Kanisa Katoliki, vyeo vya kitaaluma havipewi kipaumbele kuliko vyeo vya kiroho. Kuna doctrine ya unyenyekevu (humility) ambayo inasisitiza watawa wasijikweze kwa vyeo vya kisomi, bali wajitambulishe kwa nafasi zao za kiroho (Askofu, Kardinali, Padre etc).

Kardinali Pengo alikuwa na PhD ya Moral Theology kutoka Chuo Kikuu kinachoheshimika sana duniani cha Lateran, lakini maisha yake yote hakuwahi kujiita Dokta. Na hata pale TEC karibu Maaskofu wote ni PhD lakini huwezi kusikia wakijiita Dokta. Ni kwa sababu ya doctrine of humility.

5. Kwanini hakuzikwa kijijini kwao Mwazye, Kalambo? Ukiwa Mkleri utazikwa kwa utaratibu wa Kanisa. Mkleri ni mtu aliyepokea sakramenti ya daraja Takatifu. Hata hivyo angeweza kuzikwa Jimbo Katoliki Lindi au Tunduru-Masasi alipokuwa Askofu wa kwanza wa jimbo hilo. Lakini alishajiandalia kaburi lake kule Pugu. Na alichagua Pugu kwa sababu maisha yake ya utume yamekua zaidi Dar kuliko mahali pengine. Na pia alitamani kuzikwa pamoja na Wamisionari wa kale waliozikwa Pugu.!

Chanzo:  Malisa GJ 



KAMATI YA UONGOZI WA MRADI WA JNHPP YAKAGUA MAENDELEO YA BWAWA LA JULIUS NYERERE

 

📌Yasema mradi umesimamiwa na kutekelezwa kwa ufanisi

📌Yasisitiza ni kichocheo muhimu katika za fursa za kiuchumi na kijamii

Kamati ya Uongozi wa Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), tarehe 26 Februari 2026, imekagua maendeleo ya uzalishaji wa umeme katika mradi huo na kueleza kuridhishwa na usimamizi pamoja na utekelezaji wake, uliokidhi viwango vya ubora vinavyoendana na thamani ya fedha iliyowekezwa na Serikali.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi , amesema kamati imefurahishwa na namna bwawa hilo linavyochochea ukuaji wa uchumi kwa kuongeza uzalishaji wa umeme unaosambazwa katika maeneo mbalimbali nchini, hatua inayochangia kuimarika kwa upatikanaji wa nishati ya umeme.

“Tumeridhishwa na jinsi mradi huu ulivyosimamiwa na kutekelezwa kwa ufanisi mkubwa.

 Ukilinganisha na miradi mingine barani Afrika, mradi huu umejengwa kwa ubora wa hali ya juu na umeleta unafuu katika huduma ya umeme nchini. Haya ni mafanikio makubwa kwa Taifa,” alieleza Dkt. Yonazi.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Bw. Petro Lyatuu, amesema mradi huo umekamilika  kwa asilimia 100 na mchango wake tayari umeanza kuonekana. 

Amefafanua kuwa mwaka 2021, gridi ya taifa ilikuwa na jumla ya megawati 1,600, lakini kwa sasa uwezo wa uzalishaji umefikia zaidi ya megawati 4,000, zaidi ya mara mbili ya kiwango cha awali.

“Kwa sasa bwawa linazalisha umeme na tija yake imeonekana wazi. Kuongezeka kwa uzalishaji kumeimarisha gridi ya taifa na tunaendelea kuongeza nguvu katika sekta ya nishati kwa ajili ya maendeleo ya nchi na ustawi wa wananchi,” alisisitiza Bw. Lyatuu.

Aidha kwa hatua nyingine Kamati hiyo ilitembelea kituo cha kupokea na kupoza umeme cha Chalinze, kinachopokea umeme kutoka Bwawa la Julius Nyerere na kusambaza katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Naibu Mkurugenzi Mtendaji Uzalishaji, Mhandisi Antony Mbushi, amesema kituo hicho kimekamilika na tayari kinafanya kazi.

Ameongeza kuwa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma umefikia asilimia 71.58, huku mradi wa kusafirisha umeme kutoka Chalinze kupitia Kinyerezi hadi Mkuranga umefikia asilimia 59.76.

‘’Kamati imeridhishwa na maendeleo ya miradi hiyo na kusisitiza kuwa mpango uliopo ni kuendelea kuongeza uzalishaji ili kuhakikisha nishati ya umeme inakuwa ya uhakika na endelevu’,’Aliongeza Mha. Mbushi

Katika hitimisho la ziara hiyo, Kamati imeeleza kuwa utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya umeme unaifanya Tanzania kuwa kivutio cha uwekezaji na kitovu cha usambazaji wa umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini.

Thursday, February 26, 2026

AZAM FC YAILAMBA MTIBWA SUGAR 3-0

 

Presha katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara inazidi kuongezeka baada ya Azam FC kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Mtibwa Sugar, usiku huu ni katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, jijini Dar es Salaam.

Mabao ya Azam FC yamefungwa na kiungo Feisal Salum Abdallah dakika ya tatu tu ya mchezo na mshambuliaji mpya, Jean-Jacques Ngita Kamanga raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), aliyesajiliwa dirisha dogo kutoka Aris Limassol ya Cyprus akitupia magoli mawili dakika ya 19 na 59. 

Kwa ushindi huo, Azam FC wanafikisha pointi 22 katika mchezo wa 10 na kupanda kwa nafasi tatu hadi ya tano, wakati Mtibwa Sugar inabaki na pointi zake 21 za mechi 16 nafasi ya nne. 

CCM YATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA ASKOFU MKUU RUWA’ICHI KUFUATIA KIFO CHA KADINALI PENGO

 

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetoa salamu za rambirambi kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddeus Ruwa’ichi OFMCap, kufuatia kifo cha Askofu Mkuu mstaafu wa Jimbo hilo, Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo, aliyefariki dunia Februari 19, 2026, katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) alipokuwa akipatiwa matibabu.


Akizungumza Februari 26, 2026 baada ya kusaini kitabu cha maombolezo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu, Dar es Salaam, Katibu Mkuu CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro, alisema amewasilisha salamu za rambirambi kwa niaba ya Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Dkt. Migiro alisema marehemu Kadinali Pengo atakumbukwa kama mchungaji wa faraja na tumaini, kiongozi wa kiroho mwenye hekima, unyenyekevu na msimamo thabiti wa maadili.

Alijipambanua si tu kwa huduma ya Kanisa, bali pia kwa mchango wake katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa, maadili ya jamii, malezi ya vijana na uwajibikaji wa viongozi.


“Kadinali Pengo ameacha alama inayodumu ya utumishi wa Mungu, utumishi wa Taifa na utumishi wa jamii. Maisha na mafundisho yake yataendelea kuwa dira kwa vizazi vijavyo,” alisema Dkt. Migiro.

CCM imesema inaliombea Kanisa Katoliki na waumini wote wapate faraja katika kipindi hiki cha maombolezo na Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Kwa mujibu wa ratiba ya mazishi, mwili wa marehemu utawasili Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Februari 27, 2026 kwa ajili ya waumini kutoa heshima zao za mwisho, na Ibada ya Misa ya Mazishi itafanyika Februari 28, 2026 katika Kituo cha Hija Pugu, Dar es Salaam.



MBOZI WAFANYA UCHAGUZI MWINGINE BAADA YA DIWANI ALIYEKUWEPO KUJIUWA.

 


ZOEZI la upigaji kura katika uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Shiwinga, Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, linaendelea leo Februari 26, 2026, huku wananchi wakijitokeza kwa wingi.

Uchaguzi huo umeitishwa kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wa kata hiyo, Lusekelo Mwalukomo, kilichotokea Novemba 26, 2025, baada ya kunywa maji ya betri, zikiwa zimebaki siku chache kabla ya kuapishwa rasmi kushika wadhifa huo.

Kwa mujibu wa Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi katika kata hiyo, Selestin Luambano, jumla ya wapiga kura 6,854 wanatarajiwa kushiriki zoezi hilo katika vituo 19 vilivyotengwa kwa ajili ya kupigia kura.

Amesema jumla ya vyama nane vya siasa vimesimamisha wagombea kuwania nafasi hiyo.

Wagombea hao ni Menati Mzumbwe (CCM), Matias Dulle (ADC), Elly Shitindi (ADA-TADEA), Mary Daud (UPDP), Neema Abadallah (UMD), Emily Siwale (SAU), Mussa Dulle (Chama-Makin) na Cosam Mwakyusa (TLP).

BARABARA MLIMA KITONGA KUPANULIWA NA KUWA NJIA NNE

news

WAZIRI wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema serikali iko katika hatua za mwisho za kuanza upanuzi wa barabara inayopita Mlima Kitonga mkoani Iringa ambayo sasa itakuwa ya njia nne na yenye taa za barabarani.

Amesema hatua hiyo ni uamuzi wa Rais Samia Suluhu Hassan ili kupunguza foleni na kuboresha usalama wa watumiaji wa barabara katika njia hiyo inayotumiwa na magari mengi. 

Akizungumza jana baada ya kutembelea eneo hilo, Waziri Ulega, alisema barabara hiyo ni ya kimkakati kwa uchumi wa nchi kwa sababu inatumiwa pia na magari yanayokwenda katika nchi zinazotumia bandari ya Dar wa Salaam kubeba mizigo yao. 

Akitoa picha ya ongezeko la uhitaji wa upanuzi wa barabara hiyo, Waziri Ulega alisema idadi ya magari yanayopita katika Barabara Kuu ya TANZAM imeongezeka kutoka magari 1,700 hadi 3,400 kwa siku, hali inayosababisha njia hiyo kuzidiwa.

Waziri wa Ujenzi Abdala Ulega akizungumzia upanuzi wa barabara Mlima Kitonga.

“Nimepokea mapendekezo kutoka kwa Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Iringa ya kuhakikisha tunaondoa msongamano wa magari katika Mlima Kitonga, na nimeelekeza kwa wataalamu wetu kupanua hii barabara kwa kilometa saba. Kwa sasa hivi barabara ina njia mbili kwa hiyo tutatanua na kuwa njia nne,” alisema Ulega.

Waziri Ulega aliongeza kuwa ni maelekezo ya Rais Samia kwamba kila mradi wa barabara uende sambamba na uwekaji wa taa za barabarani ili kuhakikisha usalama wa watumiaji ikiwemo wananchi, wafanyabiashara na madereva pamoja na kuweka kingo pembezoni mwa barabara ili kuzuia magari yasianguke kwenye makorongo.

“Ninaagiza manunuzi yaanze mara moja ili kuhakikisha kwamba barabara hii inatanuliwa kwani ina umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi hivyo hatuwezi kuiacha katika hali hii na kutimiza pia maelekezo ya rais kutatua changamoto zote,” alisema Ulega. 

Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Ritha Kabati, alisema barabara hiyo ni ya uchumi wa kimataifa hivyo ikitengenezwa itainua zaidi uchumi wa Mkoa wa Iringa na taifa kwa ujumla pamoja na kuwasaidia wananchi ambao hupata changamoto ya kufuata huduma za kijamii ikiwemo matibabu Iringa mjini. 

Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa Eng. Yudas Msangi alisema gharama ya upanuzi wa kilometa saba kwa njia mbili katika barabara hiyo ni bilioni 59.2 na ukarabati wa njia mbili zilizopo ni bilioni 16.2.

Wednesday, February 25, 2026

SIMBA YAKWAA KISIKI DODOMA

 


TIMU ya Simba SC imetoa sare ya bila kufungana na wenyeji, Dodoma Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.

Kwa matokeo hayo, Simba SC inafikisha pointi 23 katika mchezo wa 10 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya tatu, wakati Dodoma Jiji FC inafikisha pointi 21 katika mchezo wa 16, ingawa inabaki nafasi ya sita. 

YANGA YATUMA SALAMU KWA 'KUIGAGADUA' JKT GOLI TANO MTUNGI

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya JKT Tanzania katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na beki Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ dakika ya saba, mshambuliaji Muangola Laurindo Dilson Maria Aurelio ‘Depu’ dakika ya 60, kiungo Mudathir Yahya Abbas dakika ya 63, mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Mpumelelo Dube dakika ya 84 na kiungo Shekhan Ibrahim Khamis dakika ya 89.

Kwa ushindi huo, Yanga wanafikisha pointi 28 katika mchezo wa 10 na kupanda kileleni ikiizidi tu wastani wa mabao JKT Tanzania, ambayo pia imecheza mechi saba zaidi. 

Mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo Dube ndiye Mchezaji Bora wa Mechi leo

STAMICO, PLANTCOR WASAINI UBIA UTAFITI NA UCHIMBAJI MADINI BUKOMBE

 NA ALBERT G.SENGO/BUKOMBE/GEITA

Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imeingia makubaliano ya ushirikiano na kampuni ya uchimbaji madini ya Plantcor ya Afrika Kusini kwa lengo la kufanya utafiti na baadaye uchimbaji wa madini katika Pori na Hifadhi ya Msitu wa Kigosi, wilayani Bukombe mkoani Geita. Makubaliano hayo yamesainiwa Jumanne, Februari 24, 2026 katika Ukumbi wa CCM Bukombe, hafla iliyohudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa kama mgeni rasmi. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Kiruswa amesisitiza umuhimu wa mwekezaji kuhakikisha kuwa zoezi la utafiti, litakalotumia teknolojia ya kisasa ya ndege nyuki (drones) kabla ya kuanza rasmi uchimbaji wa dhahabu, linafanyika kwa uwazi na kwa kutoa taarifa sahihi kwa wananchi ili waweze kushirikishwa na kunufaika na matokeo ya utafiti huo. Aidha, amemtaka mwekezaji huyo kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya eneo husika, hususan barabara, kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), ili kurahisisha upatikanaji wa maeneo ya uchimbaji kwa wachimbaji wadogo. Ameeleza kuwa hali ya miundombinu ilivyo sasa hairidhishi na inahitaji maboresho ya haraka. Mradi huo unatarajiwa kuwa chachu ya uchumi katika wilaya hiyo kupitia kodi za mirabaha, uboreshaji wa miundombinu na huduma za kijamii kwa wananchi pamoja na ajira za muda mfupi na mrefu zipatazo 2,000.

Saturday, February 21, 2026

KUKAMILIKA KWA DARAJA LA BUGELENGA (MITA 60.54) KUFUNGUA FURSA ZA KIUCHUMI BUKOMBE NA MBOGWE

 

Na, Ernest Magashi

Kukamilika kwa Daraja la Bugelenga lenye urefu wa mita 60.54 kunatarajiwa kufungua fursa mpya za kiuchumi kwa wananchi wa Wilaya za Bukombe na Mbogwe mkoani Geita, hasa katika kurahisisha usafirishaji wa mazao na mawasiliano kati ya wilaya hizo mbili.

Akizungumza wakati wa kukagua daraja hilo, Diwani wa Kata ya Bugelenga, Donald Lubigisa, alimpongeza Mbunge wa Jimbo la Bukombe na Naibu Waziri Mkuu mstaafu, Dkt. Doto Biteko, kwa kutekeleza ahadi yake ya kuhakikisha daraja hilo linajengwa na kukamilika kwa wakati.Lubigisa alisema mradi huo umegharimu Shilingi milioni 583.83 zilizotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufuatia maombi yaliyowasilishwa na mbunge huyo baada ya kuombwa na diwani pamoja na wananchi.Alieleza kuwa daraja hilo linaunganisha moja kwa moja Wilaya ya Bukombe na Mbogwe, na limeondoa changamoto ya usafiri hasa kipindi cha masika, ambapo awali wananchi walipata shida kubwa kusafirisha mazao yao kwenda sokoni.“Ninamshukuru Mbunge Dkt. Biteko kwa kuwa msikivu na kufuatilia kwa karibu changamoto za wananchi. Pia nampongeza Meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Bukombe, Mhandisi Msoka Msumba, kwa usimamizi mzuri wa mradi huu hadi kukamilika kwake,” alisema Lubigisa.Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Bukombe, Mhandisi Msoka Msumba, alisema ujenzi wa daraja hilo umekamilika kwa wakati kama ilivyopangwa, na kubainisha kuwa lenye urefu wa mita 60.54 ni miongoni mwa madaraja marefu ya mawe katika Mkoa wa Geita. Aliongeza kuwa mradi huo umegharimu jumla ya Shilingi milioni 583.83.Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Bugelenga walitoa shukrani kwa Serikali kwa kuboresha miundombinu hiyo, wakisema daraja hilo limekuwa suluhisho la kudumu kwa changamoto za usafirishaji wa mazao, hasa wakati wa mvua kubwa.Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Mkange, Timbola Kasungwa, aliipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mradi huo, akieleza kuwa daraja hilo limekuwa mhimili muhimu wa uchumi kwa vijiji vya mpakani, na linatarajiwa kuongeza kipato cha wananchi mmoja mmoja pamoja na taifa kwa ujumla.

DKT. JAFO AWEZESHA ELIMU YA UFUNDI, AKABIDHI VYEREHANI VINNE CHUO CHA FDC KISARAWE-MZENGA

 
Na Mwandishi Wetu

Taasisi ya Jafo Education Foundation imefadhili jumla ya vijana 51 kusoma katika Chuo cha FDC Kisarawe - Mzenga, kwa lengo la kuwawezesha kupata ujuzi wa fani mbalimbali za ufundi.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi na kuzungumza na wananchi katika Kata ya Mzenga, Mbunge wa Jimbo la Kisarawe Mhe.Dkt. Selemani Jafo, amesema vijana hao 51 watatoka katika kata zote 17 za wilaya hiyo na taasisi hiyo itagharamia ada zao za masomo.

"Hii ni fursa muhimu kwa vijana wa Kisarawe kujipatia ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kuajiriwa, hasa katika kipindi hiki ambacho soko la ajira linahitaji wataalamu wenye ujuzi wa vitendo."amesema Dkt. Jafo

Dkt.Jafo amesema kuwa Chuo cha FDC Kisarawe – Mzenga ni chuo kipya kilichojengwa wilayani humo na tayari kinatoa mafunzo katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ushonaji, ujenzi, mapishi, umeme, kompyuta pamoja na mafunzo ya muda mfupi.


Aidha, Dkt. Jafo ameeleza kuwa tangu mwaka 2010 amefanikiwa kusaidia zaidi ya vijana 500 kutoka familia zenye changamoto kusoma katika ngazi mbalimbali, ikiwemo kidato cha tano, astashahada, stashahada na shahada.

Katika kuendeleza juhudi za kukuza elimu ya ufundi, tarehe 20 Februari, Dkt. Jafo kupitia taasisi yake amekabidhi msaada wa vyerehani vinne vya umeme katika chuo hicho, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuwa dhamira kuu ni kuwawezesha vijana katika fani za ufundi ili kujenga msingi imara wa ajira rasmi na zisizo rasmi, pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo katika Wilaya ya Kisarawe.

SONGORO MARINE UBORA WA KIMATAIFA UJENZI MELI


Kampuni ya kizawa ya Songoro Marine iliyojikita katika ujenzi wa meli ndani na nje ya Tanzania inatajwa ni kampuni inayojenga meli kwa viwango vya kimataifa.


Kampuni hiyo, imekuwa ikipewa zabuni na serikali za ujenzi wa vivuko, kutokana na kuonyesha uzalendo katika kutekeleza miradi kwa viwango vya kimataifa.


Kwa miaka zaidi ya 30 Tangu kuanza kwa kampuni hii ya kizalendo imeonyesha dira kwa kampuni za kizawa baada ya kuaminiwa na serikali katika ujenzi wa vivuko.


Kampuni hii iliyoanza kazi mwaka 1993 kwa sasa imeendeleza mizizi ya ujenzi wa meli za kisasa zinazotumiwa ziwani na baharini kwa kufungua matawi nje ya mipaka ya Tanzania.


Inaelezwa kuanza kufungua matawi nje ya mipaka ya Tanzania ni hatua iliyotokana na kazi iliyotukuka kwa kujenga meli na vivuko vya umma na binafsi kwa viwango vya kimataifa.


Serikali ya Tanzania mara kwa mara imekuwa ikitangaza zabuni za ujenzi wa meli, ambapo kampuni hii ya kizalendo imekuwa ikiibuka kidedea.


Songoro Marine yenye makao makuu yake Ilemela mkoani Mwanza, kwa sasa inaendelea na ujenzi wa Meli tano ambazo zipo katika hatua mbalimbali.


Kati ya hizo meli tano, Meli ya Mv. Ukerewe ambayo imekamilika kwa asilimia 99 itakuwa inafanya safari zake kati ya Rugezi - Kisorya.


Kampuni ya Songoro Marine imekuwa ni mkombozi kwa Taifa kutokana na kujikita katika ujenzi wa meli na kuipa Taifa sofa nje ya Tanzania baada ya nchi ya Uganda kuipa kazi ha ujenzi wa meli.


Songoro Marine yenye tawi lingine, jijini Dar es Salaam ambako ujenzi wa vivuko inaendelea kwa kasi na viwango vinavyohitaji kulingana na mamlaka zinazosimamia sekta hiyo.


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi mkuu wa kampuni hiyo, Meja Songoro, Mratibu miradi wa Songoro, Hawa Isakiya, amesema kampuni hiyo imekuwa ikishirikiana na serikali katika ujenzi wa vivuko.


Anasema serikali kupitia  Wakala wa Ufundi na Umeme - Temesa, asilimia 75-80 kazi nyingi wanazofanya na za Umma, ambapo kazi chache zilizobaki ni kutoka nje ya nchi na watu binafsi.


Isakiya anasema kukuwa kwa kampuni wamefanikiwa kuongeza wigo kwa kufungua  tawi lingine nchini Uganda kwa ajili ya kusogeza huduma karibu.


Anaeleza mafanikio hayo yamesababishwa na serikali ya Tanzania kwa kujali wawekezaji wazawa kwa kuwapa nafasi ya kuonyesha uwezo wao.


Isakiya amesema, “kampuni kwa sasa inaendelea na vivuko vingine vinne, ikiwemo Kivuko cha Kome kitakachofanya safari zake Nyakalilo - Kome, Kivuko cha Mv. Bukondo kitafanya safari Bwiro - Bukondo ambacho kipo asilimia 99,”.


Friday, February 20, 2026

RC MTANDA AZINDUA MADUKA MATANO YA NGUVU YA AIRTEL JIJINI MWANZA

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA 

Mwanza ni kitovu cha uchumi katika Kanda ya Ziwa. Shughuli kuu za uchumi wetu ni pamoja na uvuvi katika Ziwa Victoria, biashara ndogo na za kati, kilimo cha pamba na mazao ya chakula, uchimbaji wa madini, pamoja na sekta ya huduma na utalii.

Kwa wavuvi wanaofanya kazi katika mwambao wa Ziwa Victoria, mawasiliano ya uhakika yanarahisisha biashara ya samaki, kupanga masoko, na kufanya malipo kwa njia ya kidijitali.

Kwa wafanyabiashara wa masoko kama Soko Kuu la Mwanza, Soko kuu la Samaki Kirumba na maeneo mengine huduma za Airtel Money zinarahisisha miamala, kupokea malipo, na hata kuagiza bidhaa kutoka maeneo mengine ya nchi.

Kwa wakulima wa pamba na mpunga katika wilaya za mkoa wa Mwanza, huduma za mawasiliano zinawaunganisha na masoko na taasisi za kifedha.

Hivyo basi, uwekezaji huu wa Airtel Tanzania unaenda moja kwa moja kuunga mkono shughuli hizi muhimu za kiuchumi zinazofanywa na serikali

Thursday, February 19, 2026

DKT. MWIGULU AIPA WIZARA YA MAJI WIKI MBILI.

 Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ameipa Wizara ya Maji kipindi cha wiki mbili kuhakikisha inakamilisha mchakato wa upatikanaji wa mkandarasi wa ujenzi wa mradi wa maji kutoka chanzo cha Ziwa Chala.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wananchi wa kata ya Marangu-Kitowo, Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro baada ya kupokea taarifa za ujenzi wa Mradi wa Maji kutoka chanzo cha ziwa Chala, Ujenzi wa mradi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi), pamoja kuweka jiwe la msingi la Shule ya Sekondari Stephen Moshi Technical.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa ujenzi wa mradi huo unapaswa kuanza kutekelezwa kwani unategemewa kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji katika Wilaya nzima ya Rombo.

Kwa upande wake Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa Wizara haitakuwa kikwazo katika utekelezaji wa mradi huo na watahakikisha katika kipindi cha siku 14 wanampata mkandarasi wa mradi huo.

Mradi wa maji ziwa Chala unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 8.66 na utanufaisha wananchi 34,104 katika vijiji 14 vya wilaya ya Rombo.

Kadhalika Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amemuagiza Waziri wa Fedha kuhakikisha anatafuta fedha kwa ajili ya kufanya malipo ya awali kwa mkandarasi ili aanze ujenzi wa mradi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi) kilomita 52.8
Mradi huo ambao utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 28 unapita mpakani mwa Tanzania na Kenya na unategemewa kusaidia kukuza shughuli za kijamii, kiuchumi pamoja na utalii.

Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari Stephen Moshi Technical ambayo itagharimu shilingi bilioni 1.6 Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa shule hiyo ni kielelezo cha uwepo wa kiongozi mwenye maono na mipango.

“Ndani ya muda mchache sana zimejengwa shule zaidi ya 103 za aina hii nchi nzima” Amesema Dkt. Mwigulu.

Mradi huo utahusisha Ujenzi wa madarasa 08, ofisi 02, chumba 01 cha TEHAMA, maabara ya kemia na baiolojia, mabweni 4 ya wasichana na wavulana, bwalo 01, karakana 01 ya magari, matundu 08 ya vyoo vya wasichana na wavulana na Kichomea taka.

Pia utahusisha uchimbaji wa kisima cha maji cha ardhini, jengo la utawala na nyumba 01 ya mtumishi.


    YANGA SC YAICHAPA COSMO 2-0 NA KUSONGA MBELE KOMBE LA CRDB

     


    MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Cosmopolitan katika mchezo wa Raundi ya Pili Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) usiku wa jana 18 February 2026 Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

    Mabao yote ya Yanga leo yamefungwa na mchezaji mpya, winga Mgambia, Buba Jammeh aliyesajiliwa dirisha dogo kutoka Interclube ya Angola dakika ya 13 na 23 ya mchezo huo wa Hatua ya Timu 64.

    Yanga sasa wanasonga mbele ya Raundi ya Tatu ya michuano hiyo itakayohusisha timu 32 katika kampeni ya kutwaa taji la michuano hiyo kwa Mara ya tano mfululizo.