ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, March 6, 2026

ULAJI HOLELA WA VYAKULA CHANZO CHA MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA.

Jamii imetakiwa kupunguza ulaji holela wa vyakula ili kuepuka magonjwa yasiyoambukizwa kama vile Kisukari,Kiharusi na presha kutokana na ulaji holela wa chakula bila kufuata utaratibu wa kiafya na mazoezi ya mwili ya kupunguza uzito

Rai hiyo imetolewa na Oda Isac Sekiromba mwakilishi wa kampuni ya Edmark tawi la Mwanza leo wakati wa siku ya mwanamke Jembe iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Edmark iliyoambatana na utolewaji wa elimu ya Afya na ujasiriamali iliyoandaliwa na kampuni ya Edmark kwa kushirikiana na Jembe FM

 

Je, vyakula vya ovyo husababisha magonjwa?
Madaktari wengi wanatambua kuwa ulaji wa chakula kisicho na chakula unahusishwa na ugonjwa wa moyo wa mapema. Makubaliano ya jumla ni kwamba uhusiano huu unaweza kuelezewa na mafuta yaliyojaa katika vyakula hivi kuongeza fetma, hatari ya kisukari na hyperlipidemia na maudhui ya juu ya chumvi kuongeza shinikizo la damu.  
Je, ni nini kitatokea ikiwa unakula kila siku?
Ulaji mwingi wa vyakula vya kuchukua unahusishwa na kuongezeka kwa hatari ya ugonjwa wa moyo kwa watu wazima . Inasababisha unene wa kupindukia, shinikizo la damu, na viwango vya juu vya kolesteroli kwa sababu ya utajiri wake wa kalori, mali duni ya virutubishi, inayoongezwa kwa ukosefu wa matunda na mboga mboga.
Kwa nini ni muhimu kula vyakula vyenye afya?
Inakulinda dhidi ya magonjwa mengi sugu yasiyoambukiza, kama vile ugonjwa wa moyo, kisukari na saratani . Kula vyakula mbalimbali na kutumia chumvi kidogo, sukari na mafuta yaliyoshiba na yanayozalishwa viwandani, ni muhimu kwa lishe yenye afya.

Ni tabia gani mbaya zaidi za kula?
Haya yanaweza kujumuisha kula kabla ya kulala, kuruka milo, kula haraka sana, kula bila akili, au kula mkazo . Hebu tuzungumze kuhusu jinsi tabia hizo zinaweza kuathiri afya yako na baadhi ya mapendekezo ya kuzidhibiti.

Nini kinatokea kwa mwili wako unapoacha kula vyakula vilivyosindikwa?
Ni nini hufanyika ninapokata vyakula vilivyosindikwa? Unaweza kupata dalili za kujiondoa kama vile uchovu na kuwashwa, lakini pia kuna uwezekano wa kupunguza uzito na kujisikia nguvu zaidi .

Nini kinatokea kwa mwili wako unapoanza kula afya?
Kula chakula bora - kama vile kufuata lishe ya Mediterania yenye mazao na nyuzinyuzi au lishe ya DASH - kunaweza kupunguza hatari yako ya kupata ugonjwa mbaya. Ulaji mbaya umehusishwa na magonjwa sugu kama vile ugonjwa wa moyo, kisukari cha aina ya 2, shinikizo la damu na hata saratani fulani, pamoja na saratani ya utumbo mpana.

AFCON 2027: ULINZI NI CHUMA, AMANI YETU NDIO FURSA KWA VIJANA!

 

WAKATI hamu ya michuano ya AFCON 2027 ikizidi kupanda, Serikali imetuma ujumbe mzito: "Tanzania ni salama na ulinzi ni chuma!" 

Katika kikao kizito kilichofanyika Dar es Salaam Machi 4, Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi imekutana na Mkuu wa Kitengo cha Usalama wa Michezo kutoka Umoja wa Mataifa (UN), Valerio de Divitiis, kupigilia msumari mkakati wa kuhakikisha kila mgeni na mwenyeji anakuwa salama kama yuko nyumbani kwake.

Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo, Boniface Tamba, ameweka wazi kuwa usalama si suala la polisi pekee, bali ni mazingira tulivu yatakayowawezesha vijana na wafanyabiashara kuchangamkia fursa bila hofu. 

Tamba alisisitiza kuwa mifumo ya kudhibiti umati na usimamizi wa viwanja itakuwa ya viwango vya dunia, jambo linaloashiria kuwa Tanzania iko tayari kuishangaza Afrika kwa ukarimu na utulivu wa kipekee.

Hivi karibuni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) Gianni Infantino katika ofisi za FIFA zilizopo mjini Rabat nchini Morroco ambapo moja kati ya masuala waliyozungumza ni pamoja na maandalizi ya AFCON 2027.

Kwa upande wake,  Leodegar Tenga, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi, amepigilia msumari kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha AFCON 2027 inavunja rekodi. 

Alibainisha kuwa mashindano haya hayataishia kwenye ufundi wa uwanjani pekee, bali yataacha alama ya usalama wa hali ya juu, jambo ambalo ni msingi wa kuvutia wawekezaji na watalii wanaotafuta maeneo yenye amani ya kudumu.

Huu ni ujumbe tosha kwa vijana wanaopoteza muda kusononeka: Usalama huu unaoandaliwa na Serikali kwa kushirikiana na UN ni "uwanja mweupe" kwenu.  Badala ya kuendekeza chuki mitandaoni, ni wakati wa kuthamini utulivu huu na kujiandaa kuvuna "mapesa" ya mashindano hayo makubwa barani Afrika.

WANAWAKE WATAKIWA KUVAA UJASIRI WA KUPIMA AFYA ZAO.

 Wanawake watakiwa kuvaa ujasiri wa kupima afya zao


Hofu ya kupima afya imetajwa kuwa kitanzi kwa wanawake wengi, kwa kuwa imesababisha baadhi kuteseka hata kupoteza maisha kwa magonjwa makubwa ikiwamo kansa, ambayo yakigundulika mapema wangepata tiba.

Imeelezwa kuwa wengi hulazimika kupima wakiwa tayari kwenye hali mbaya, ikiambatana na maumivu.
 
 Hivyo wanawake wametakiwa kubadili mtazamo, na kujenga tabia ya kwenda kufanyiwa uchunguzi wa afya mapema.

Akizungumza katika kongamano la afya ya wanawake lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Mkemia na Mtafiti wa Miti Dawa, Prof. Faith Mabiki, alisema bado kuna hofu kubwa miongoni mwa wanawake kuhusu vipimo vya afya licha ya maendeleo ya teknolojia katika sekta ya tiba.

Prof.Mabiki alisema magonjwa kama saratani ya shingo ya kizazi na saratani ya matiti yanaweza kudhibitiwa kwa kiwango kikubwa, endapo yatagunduliwa mapema kupitia vipimo vya mara kwa mara.

“Wanawake wengi huweka afya zao kama jambo la pili, lakini ukweli ni kwamba afya njema ndiyo msingi wa ustawi wa familia na maendeleo ya jamii,” alisema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa RAAWU Tawi la SUA, Faraja Kamendu, alisema taasisi hiyo inaendelea kushirikiana na menejimenti ya chuo kuhakikisha wafanyakazi wanawake wanapata elimu ya afya na huduma muhimu za kitabibu.

Kamendu alisema semina hiyo imewapa wanawake fursa ya kujifunza kuhusu changamoto mbalimbali za kiafya pamoja na njia za kujikinga nazo.

Naye Daktari bingwa wa magonjwa ya watoto katika Hospitali ya SUA, Dk.Graca Chotamawe, alisema magonjwa yasiyoambukiza yanaendelea kuongezeka duniani, ikiwamo barani Afrika kutokana na mabadiliko ya mtindo wa maisha.

Alisema takribani watu milioni 41 hufariki kila mwaka duniani kutokana na magonjwa hayo, huku sababu zake zikitajwa kuwa ni pamoja na kupungua kwa mazoezi, matumizi ya vyombo vya usafiri kama magari na bodaboda, pamoja na matumizi ya dawa za kulevya.

Aliongeza kuwa magonjwa hayo huongeza mzigo wa kiuchumi kwa familia nyingi, kwa kuwa matibabu yake huchukua muda mrefu na kugharimu fedha nyingi.

Kongamano hilo lilihusisha watumishi wanawake wa SUA na wanafunzi, huku pia likitoa fursa ya upimaji wa afya kwa magonjwa mbalimbali ikiwemo presha na sukari.

DARAJA LA UBAGWE LAONDOA ADHA YA MAFURIKO USHETU.

Daraja la Ubagwe laondoa  adha ya mafuriko Ushetu
Daraja la Ubagwe laondoa adha ya mafuriko Ushetu

 

Wananchi wa Wilaya ya Ushetu sasa wana sababu ya kutabasamu baada ya kukamilika kwa Daraja la Ubagwe, mradi muhimu wa miundombinu uliokuja kuondoa changamoto ya muda mrefu ya kukatika kwa mawasiliano wakati wa msimu wa mvua.

Kwa miaka mingi wakazi wa eneo hilo walikuwa wakikumbwa na adha kubwa hasa kipindi cha mvua kali. Mafuriko yaliyosababishwa na mvua za El-Nino yaliwahi kuharibu miundombinu ya barabara na kukata kabisa mawasiliano kati ya maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo pamoja na mikoa jirani ya Tabora, Geita na Shinyanga. Hali hiyo ilifanya shughuli za kiuchumi kudorora huku wananchi wakipata hasara kubwa.

Wakulima walishindwa kusafirisha mazao yao kwenda sokoni, wafugaji walikwama kuvusha mifugo yao na wafanyabiashara walipoteza fursa za kibiashara kutokana na kukosekana kwa njia salama ya kuvuka. Changamoto hiyo pia iliathiri huduma za kijamii, ambapo baadhi ya wagonjwa walishindwa kufikishwa hospitalini kwa wakati.

Kwa mujibu wa wananchi wa eneo hilo, hali hiyo ilikuwa hatari zaidi kwa akina mama wajawazito ambao wakati mwingine walilazimika kuvuka katika mazingira magumu au kushindwa kabisa kuvuka, jambo lililosababisha vifo katika baadhi ya matukio.

Hata hivyo, matumaini mapya yameanza kuonekana baada ya kukamilika kwa Daraja la Ubagwe, mradi uliogharimu shilingi bilioni 13.5. Daraja hilo linatajwa kuwa mkombozi wa wananchi wa Ushetu na maeneo ya jirani kwa kuwa sasa linahakikisha mawasiliano yanakuwepo wakati wote wa mwaka bila kujali msimu wa mvua.

Akizungumza na wananchi mara baada ya kukagua daraja hilo, Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenan Kihongosi, amesema kukamilika kwa daraja hilo kumesaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zilizokuwa zikiwakumba wananchi kwa muda mrefu.

Ameeleza kuwa mradi huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha miundombinu ya barabara na madaraja ili kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi kwa wananchi.

Kihongosi amebainisha kuwa ujenzi wa Daraja la Ubagwe umefanyika sambamba na ujenzi wa madaraja mengine mawili ya Kasenga na Ng’hwande, hatua inayolenga kuboresha zaidi mtandao wa usafiri na mawasiliano katika ukanda huo.

Amesema kwa sasa daraja hilo lipo katika kipindi cha majaribio ili kuhakikisha linakidhi viwango vya ubora na thamani ya fedha iliyotumika kabla ya kukabidhiwa rasmi kwa matumizi ya wananchi.

Akizungumzia ubora wa mradi huo, Kihongosi amesema thamani ya fedha inaonekana wazi kupitia ubora wa ujenzi wake, huku akiwataka wananchi kulinda na kutunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kuwanufaisha kizazi cha sasa na kijacho.

Katika ziara hiyo pia amesisitiza umuhimu wa kudumisha amani na utulivu nchini, akieleza kuwa maendeleo ya miundombinu na ustawi wa shughuli za kiuchumi kama kilimo, ufugaji na biashara hutegemea uwepo wa amani.

Kwa kukamilika kwa Daraja la Ubagwe, wananchi wa Ushetu wanatarajia kuona ongezeko la shughuli za kiuchumi, urahisi wa usafiri na mawasiliano pamoja na kuboreshwa kwa upatikanaji wa huduma za kijamii, jambo litakalosaidia kuharakisha maendeleo ya eneo hilo na ukanda wa Ziwa kwa ujumla.

Ujenzi wa daraja hilo ni mfano wa namna uwekezaji katika miundombinu unavyoweza kubadilisha maisha ya wananchi kwa kuondoa vikwazo vya kijiografia na kuleta fursa mpya za maendeleo.

Thursday, March 5, 2026

AZAM FC YATOSHANA NGUVU NA TANZANIA PRISONS

 


TIMU ya Azam FC imetoa sare ya bila kufungana na wenyeji, Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya.

Kwa matokeo hayo, Azam FC wanafikisha pointi 24 katika mchezo wa 12 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya nne, wakati Tanzania Prisons inafikisha pointi 13 katika mchezo wa 15, ingawa inabaki nafasi ya 15 kwenye ligi ya timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.  

YANGA SC 'YAITWANGA' SINGIDA BLACK STARS 3-0

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya wenyeji, Singida Black Stars katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Mwigulu Airtel Complex, Singida.

Mabao ya Yanga SC leo yamefungwa na mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Mpumelelo Dube dakika ya 39, winga Mganda, Allan Okello kwa penalti dakika ya 45’+2 na kiungo Mudathir Yahya Abbas dakika ya 56.

Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 32 katika mchezo wa 12 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi nne zaidi ya JKT Tanzania ambayo pia imecheza mechi tano zaidi.

Kwa upande wao Singida Black Stars wanabaki na pointi zao 19 za mechi 12 pia nafasi ya tisa.

TAZAMA GOLI LA ALLAN OKELLO VS SINGIDA BLACK STARS

BARA LA AFRIKA; ATHARI KUU VITA VYA MASHARIKI YA KATI

Eneo la Strait Hormuz
Eneo la Strait Hormuz

 Vita inayoendelea Mashariki ya Kati, iliyoanzishwa na Marekani pamoja na mshirika wake Isarel, dhidi ya Iran, tayari wachumi wametaja athari za mapema zitakazoanza kushuhudiwa barani Afrika.

Miongoni mwaka ni nishati ya mafuta. Kwa siku takribani mapipa ya mafuta milioni 20 hupita katika korido ya mlango wa ‘Strait of Hormuz’. Huo ni mlango mwembamba wa bahari unaounganisha Ghuba ya Persian na Ghuba ya Oman.

Kwa mujibu wa ukurasa Firstpost mtandao wa instagram, unaeleza hayo na kwamba hali hiyo inatokana na kukosekana kwa hali ya kiusalama kutokana na vita hivyo, kwa sasa usafirishaji huo utasitishwa.

Athari za kukosekana kwa nishati hiyo, mchambuzi wa kupitia mtandao huo anasema, kwa Afrika, gharama za maisha zitapanda, ikiwamo bei za vyakula.

Kinachoendelea sasa si mzozo mwingine tu wa kawaida katika eneo la Asia Magharibi, bali ni mshtuko wa moja kwa moja kwa uchumi wa dunia. 

Katikati ya yote haya eneo hilo ni muhimu na Mlango wa Bahari wa uitwao ‘Hormuz’. Ni njia nyembamba ya baharini kati ya Iran na Oman, ambako karibu theluthi moja ya tano ya mafuta ya dunia hupita.

Baada ya mashambulizi mapya ya Marekani na Israel, pamoja na hatua za kulipiza kisasi za Iran, inaripotiwa kuwa baadhi ya meli zilipokea maonyo ya redio yakidai kuwa upitishaji unaweza kuzuiwa. 

Hakuna tangazo rasmi la kufungwa kwa njia hiyo, lakini masoko hayasubiri taratibu za kisheria.

Bei za mafuta zinaanza kupanda, kampuni za bima zinaongeza gharama za bima ya hatari ya vita, na maamuzi ya usafirishaji kwa njia ya meli yanasimama kwa tahadhari. Iran imekwishafunga mlango huo muhimu.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Uingereza Reuters, Umoja wa Ulaya (EU), meli zake zimekuwa zikipokea ujumbe kutoka Jeshi la Iran, likisema hakuna meli inayoruhusiwa kupita katika Mlango wa Bahari wa Hormuz.

Mlango huu ni njia muhimu ya kusafirisha mafuta duniani, takribani mapipa milioni 20 ya mafuta kwa siku hupitia, yakiwakilisha asilimia 20-25 ya biashara ya mafuta ya baharini duniani na moja ya tano ya matumizi ya mafuta duniani.

ATHARI ZA AWALI

Kuongezeka kwa mapigano kunahatarisha kuharibu zaidi utulivu wa dunia, Mashariki ya Kati kuna athari kubwa kwa biashara ya nishati, usalama wa chakula na uchumi, hasa barani Afrika, ambako migogoro na misukosuko ya kiuchumi bado ni mikali.

Umoja wa Afrika (AU), baada ya taarifa Israel na Marekani kuanzisha mashambulio dhidi ya Iran, umezitaka pande zinazopigana kujizuia, kupunguza mvutano na kuendelea na mazungumzo

Athari hizo kwa Afrika, pia ziliguswa na  mgogoro wa Russia na Ukraine miezi ya mwanzoni mwaka 2022. 


Afrika ilianza kuona makali ya vita hivyo baada kutokea mgogoro wa chakula, ikiwamo kupanda kwa gharama ya chakula hasa ngano na mafuta.

Katika ripoti ya Shirika la Fedha Duniani (IMF) iliyochapishwa Aprili mwaka huo, ilisema, baadhi ya mataifa ambayo yanaathirika moja kwa moja na vita vya Ukraine kwa kutegemea uagizwaji wa ngano kutoka nchi hiyo na Russia kwa asililia 85 ni pamoja na Tanzania, Ivory Coast, Senegal na Msumbiji.

Haikuwa Afrika pekee, dunia nzima iliona makali ya vita hivyo ambavyo bado vinaendelea. Ni kutokana na ukweli kwamba hadi vita vinaanza, Russia ndiyo nchi inayoongoza katika mauzo ya ngano duniani ikifuatiwa na Ukraine.

Bei ya mafuta inatarajiwa kupanda kwa kasi siku ya Jumatatu licha ya ahadi ya nchi kubwa zinazozalisha mafuta kuongeza uzalishaji, huku vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran pamoja na kufungwa kwa vitendo kwa Mlango wa Bahari wa Hormuz vikitetemesha wawekezaji.

Mafuta ghafi ya Marekani yanatarajiwa kupanda kwa karibu asilimia tisa biashara itakaporejea, kulingana na takwimu za dalali IG. 

Ongezeko hilo linakuja licha ya kundi la wazalishaji mafuta la OPEC+ kukubaliana Jumapili kuongeza uzalishaji kwa kiwango kikubwa zaidi ya ilivyotarajiwa ili kupunguza athari za mzozo.

Walinda Mapinduzi wa Iran (Revolutionary Guards) wanaripotiwa kuziambia meli kwamba kupita katika 

Meli moja ya mafuta ilishambuliwa Jumapili leo katika mlango huo na angalau meli 150 zilizobeba mafuta ghafi, gesi asilia iliyoyeyushwa (LNG) na bidhaa za mafuta zilisimamisha safari na kutia nanga katika maji ya wazi katika Ghuba ya Mashariki ya Kati, kulingana na Reuters.

Tehran imekuwa ikionya kwa muda mrefu kwamba inaweza kutumia nafasi yake ya kijiografia kuufunga mlango huo kujibu uchokozi wa kijeshi. 

Tamsin Hunt, mchambuzi mwandamizi wa kampuni ya ujasusi na usalama wa mtandao ya S-RM, alisema kufunga kabisa njia hiyo “kungedhoofisha sana uchumi wa Iran yenyewe.”

Masoko ya wikendi ya IG yanaonesha kuwa mafuta ghafi ya Marekani yanaweza kupanda hadi zaidi ya dola 73 kwa pipa biashara itakaporejea New York, kutoka dola 67 Ijumaa usiku, kiwango cha juu zaidi tangu Juni 2025 wakati Marekani ilipoanzisha mashambulizi dhidi ya vituo vya nyuklia vya Iran.

Wachambuzi wa Barclays walisema bei ya mafuta inaweza kufikia dola 80 kwa pipa endapo kutakuwa na “usumbufu mkubwa wa usambazaji.” Nao wachambuzi wa Royal Bank of Canada walionya kuwa mafuta ya zaidi ya dola 100 kwa pipa ni hatari halisi iwapo mzozo utaongezeka.

Kupanda kwa bei ya jumla ya mafuta kunatarajiwa kuathiri bei za rejareja. Bei ya wastani ya petroli nchini Uingereza ni pensi 132.9 kwa lita na dizeli 142.4p, kulingana na The AA, ambayo imeonya kuwa athari za Iran zinaweza kuungana na mpango wa serikali kurejesha ushuru wa mafuta wa 5p kwa lita na hivyo kuongeza bei zaidi.

Katika soko la London, faharasa ya FTSE 100 inatarajiwa kushuka kwa karibu asilimia 0.5, Jumatatu asubuhi baada ya kufikia rekodi Ijumaa.

Wawekezaji duniani wanatarajiwa kukimbilia mali salama. Dhahabu, ambayo imepanda kwa wiki nne mfululizo, imeongezeka kwa asilimia 2.25 hadi karibu dola 5,400 kwa wakia katika masoko ya wikendi ya IG, huku fedha (silver) nayo ikipanda kwa 3.2.

Nchi nane za OPEC+ zilikubaliana kimsingi kuongeza uzalishaji kwa mapipa 206,000 kwa siku mwezi April, zaidi ya matarajio ya awali ya mapipa 137,000.

Kampuni ya bandari ya DP World imesimamisha shughuli katika Bandari ya Jebel Ali, Dubai na kampuni ya Mediterranean Shipping Company imesitisha upokeaji wa mizigo inayoelekezwa Mashariki ya Kati hadi itakapotangazwa vinginevyo.

Gharama za bima ya meli katika eneo hilo zimeongezeka, kulingana na Dylan Mortimer wa kampuni ya usimamizi wa hatari ya Marsh, akionya kuwa hatari kuu ni pamoja na kukamatwa kwa meli na vikosi vya Iran na uwezekano wa kufungwa kwa Mlango wa Hormuz.

Masoko mengi ya hisa katika eneo la Ghuba yalishuka Jumapili. Soko la Saudi Arabia lilipoteza asilimia 2.5, ingawa hisa za Saudi Aramco zilipanda kwa 2.5 kufuatia matarajio ya kupanda kwa bei ya mafuta ghafi. Soko la hisa la Kuwait lilisimamisha biashara hadi itakapotangazwa tena, likitaja “hali za kipekee” zinazoikabili nchi hiyo.

KUUAWA KIONGOZI IRAN

Taarifa kutoka Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, vyombo kadhaa vya habari vya serikali nchini Iran vilithibitisha kifo cha Ayatollah Khamenei, jana.

Ayatollah Khamenei.


Rais wa Marekani, Donald Trump saa chache zilizopita alisema Kiongozi Mkuu huyo aliuawa wakati wa shambulio la pamoja na Israel katika maeneo kadhaa kote Iran.

Katika taarifa hiyo, haikutajwa ni jinsi gani Khamenei mwenye umri wa miaka 86 alivyofariki, au ni nani anayeweza kuchukua nafasi ya kiongozi.

Jamaa wa Khamenei pia wameuawa katika mashambulizi hayo

Hapo awali, vyombo vya habari vya serikali vilisema kwamba binti wa Khamenei, mkwewe na mjukuu wake pia waliuawa katika mashambulizi hayo.

Kulingana na Shirika la Habari la Fars, ambalo lina uhusiano na Kikosi cha Revolutionary Guard, kuna ripoti kwamba mmoja wa mabinti wa Khamenei ameuawa pia.


Tuesday, March 3, 2026

UKARABATI MV LIEMBA WAFIKIA ASILIMIA 57

 Ukarabati wa MV Liemba wafika asilima 57 Serikali kupitia Kampuni ya Meli Tanzania, (TASHICO) imesema ukarabati wa meli kongwe ya abiria na mizigo, MV Liemba, umefikia asilimia 57, huku ikieleza kuwa kukamilika kwake kutaleta mapinduzi ya kiuchumi katika nchi za ukanda wa maziwa makuu.

Akizungumza Mhandisi wa mradi huo Elias Kivara amesema vifaa vyote vinavyotakiwa kukamilisha ukarabati wa meli hiyo tayari vimefika akitaja kuwa kinachoendelea sasa ni kukamilisha zoezi la kupaka rangi na kwamba maboresho ya meli hiyo yataifanya iwe katika hali ya upya na usasa.

“Meli imeboreshwa kutoka ilivyokuwa wakati ule, tumeweka siti za kisasa, kutakuwa na sehemu ya starehe, ambayo inaweza kuchukua watu 53 na vyumba vyote vitakuwa na kiyoyozi, vitu vyote vimewekwa vipya na tumezingatia vifaa vya usalama, vyote vitakuwepo ndani ya meli,"amesema Kivara.

Amesema mpaka sasa wapo wafanyakazi 45 wakiwemo wazawa 43 na kutoka Korea wawili.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TASHICO, Daniel Mwambungu amesema kuwa kati ya jumla ya dola milioni 13, sawa na Sh. bilioni 29 za mradi huo kiasi cha dola milioni 7.8 kimeshalipwa.

Amesema ukarabati wa meli hiyo ulianza Julai 2024 huku ikitarajiwa kuanzia safari za majaribio mnamo mwezi Juni mwaka huu na kuanza safari rasmi mwezi Julai 2026

MV Liemba ilikuwa inafanya kazi zake kuzunguka mwambao wa ziwa Tanganyika ikiwemo Kigoma, Katavi, Rukwa na nchi jirani za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 600 na tani 200 za mzigo, ilisimama safari zake mwaka 2018 kutokana na uchakavu wa mitambo yake.



PAMBA V/S AZAM NGOMA SARE 2-2 FEI TOTO ALIMWA UMEME


TIMU ya Azam FC imelazimisha sare ya kufungana mabao 2-2 na wenyeji, Pamba Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya jana Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza.


Ni Pamba Jiji waliouanza vyema mchezo huo na kupata mabao mawili ya uongozi kupitia kwa kiungo wa Azam FC, Himid Mao Mkami aliyejifunga dakika ya 45 na mshambuliaji wake, Mganda John Ben Nakibinge dakika ya 48.


Lakini Azam FC ikazinduka kipindi cha pili na kusawazisha mabao yote kupitia kwa mshambuliaji Mkongo, Jean-Jacques Ngita dakika ya 56 na kiungo Feisal Salum Abdallah kwa penalti dakika ya 59, kabla ya kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 62.


Kwa matokeo hayo, Azam FC inafikisha pointi 23 katika mchezo wa 11, ingawa inabaki nafasi ya tano ikizidiwa pointi moja na Pamba Jiji FC ambayo pia imecheza mechi nne zaidi.

TAHADHARI KUBWA! WANANCHI USHOROBA WA SGR KANDA YA ZIWA WAKUMBUSHWA USALAMA WA VIVUKO.

 NA ALBERT G.SENGO/FELA/MISUNGWI/MWANZA

Tahadhari imetolewa na Wataalamu wa Shirika la Reli Tanzania ( TRC ) katika mkutano wa hadhara wa kutoa elimu ya usalama kwa wakazi wa Kijiji cha Fela wilayani Misungwi, ambako mradi huo wa kimkakati unatekelezwa na serikali. Afisa Usalama Mahali Pa Kazi wa TRC Richard Msungu amesema lengo la shirika hilo kutoa elimu ya usalama kwa wananchi wanaoishi katika ushoroba wa reli ya SGR ni kuona wanakuwa salama ikiwa watazingatia alama za usalama kwa kutumia vivuko sahihi vya kuvukia binadamu, wanyama na magari. Kwa mujibu wa mhandisi ujenzi wa TRC, Nastra Chusi mradi wa SGR kipande cha 5 hadi sasa umetekelezwa kwa asilmia 68.28, hivyo elimu hiyo kwa wananchi wa mikoa ya Mwanza, Simiyu na Shinyanga ni endelevu.

Sunday, March 1, 2026

KIFO CHA KIONGOZI MKUU NI TUKIO KUBWA NA IRAN INAJIBU KWA NGUVU.

 Khamenei

Kuuawa jana kwa mtu ambaye ameiongoza Iran kwa karibu miaka 40 kulithibitishwa usiku na televisheni ya taifa. Hili ni tukio kubwa sana kwa taifa hilo la Kiislamu.

Kulikuwa na sherehe katika baadhi ya mitaa ya miji ya Iran kutoka kwa watu waliopinga utawala wake. Hali hiyo itazitia moyo Israel na Marekani, ambazo zimewahimiza Wairani kutumia fursa hii kuamka na kuiondoa serikali.

Usiku kucha, jeshi la Israel lilifanya wimbi jingine la mashambulizi ya mabomu, likisema lililenga hifadhi na vituo vya kurushia makombora ya masafa marefu ya Iran pamoja na mifumo yake ya ulinzi wa anga.

Zaidi ya watu 200 wameuawa kote Iran, kulingana na Iranian Red Crescent Society, Shirika la misaada ya kibinadamu nchini Iran.

Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi la Iran limesema litajibu kifo cha Kiongozi Mkuu kwa operesheni yenye uharibifu mkubwa zaidi katika historia yake.

Asubuhi hii nchini Israel, ving’ora vya tahadhari ya mashambulizi ya anga vimesikika tena huku Iran ikiendelea kurusha makombora ya masafa marefu. Karibu yote yamedunguliwa na mfumo wa ulinzi wa anga wa Israel.

Hata hivyo, baadhi yalipenya: mjiniTel Aviv, shambulizi la kombora lilimuua mwanamke mmoja, ambaye ni kifo cha kwanza cha raia wa Israel katika vita hivi. Huduma ya ambulensi imesema watu wengine 120 wamejeruhiwa, wengi wao wakiwa na majeraha madogo.

Saturday, February 28, 2026

WAZIRI MKUU ASHIRIKI MAZISHI YA KARDINALI PENGO, DAR ES SALAAM

 


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Februari 28, 2026 ameshiriki mazishi ya Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Marehemu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, yaliyofanyika katika Kanisa la Hija ya Bikira Maria – Pugu, jijini Dar es Salaam.


Mazishi hayo yameongozwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi na kuhudhuriwa na viongozi wengine wa Serikali pamoja na viongozi wa dini mbalimbali.


VIDEO:- VIJANA 336 WAHITIMU VETA MWANZA, WANAOUZA VITENDEA KAZI WAONYWA.

 NA ALBERT G.SENGO/MWANZA

Jumla ya vijana 336 kutoka Wilaya za Ilemela na Nyamagana mkoani Mwanza wamehitimu mafunzo ya stadi za maisha na ufundi stadi katika fani mbalimbali, na kukabidhiwa vifaa vya kuanzia kazi ili kuwawezesha kujiajiri na kujikwamua kiuchumi. Vijana hao wamehitimu Februari 27, 2026 katika VETA Mwanza, ambapo wamekabidhiwa vyeti baada ya kupatiwa mafunzo ya uselemala, uashi, uchomeleaji, ufundi bomba, aluminium, umeme wa magari na majumbani, ufundi magari na upishi. Aidha, walipata elimu ya stadi za maisha, biashara, fedha, ujasiriamali, usawa wa kijinsia pamoja na teknolojia na TEHAMA. Wahitimu hao ni sehemu ya vijana 400 walioandikishwa katika awamu ya pili ya mradi wa Vijana Elimu, Malezi na Ajira (VEMA) unaotekelezwa na Plan International mkoani Mwanza, kwa lengo la kuwawezesha vijana kutoka familia zisizojiweza kupata ujuzi wa kujiajiri au kuajiriwa. Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa, amewataka vijana hao kuendeleza ujuzi walioupata na kuvitunza vifaa walivyokabidhiwa. Ameonya kuwa yeyote atakayebainika kuuza vifaa hivyo atachukuliwa hatua za kisheria.

NAMUNGO YATOA SARE 1-1 NA SINGIDA BLACK STARS RUANGWA

 

Mshambuliaji Mkenya, Elvis Baranga Rupia akishangilia baada ya kuifungia Singida Black Stars bao la kuongoza

TIMU ya Namungo FC imetoa sare ya kufungana bao 1-1 na Singida Black Stars katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Lindi.

Mkenya, Elvis Baranga Rupia alianza kuifungia Singida Black Stars dakika ya 58 kwa penalti, kabla ya mshambuliaji mwenzake, Mkongo - Fabrice Ngoy wa Ngoy kuisawazishia Namungo FC dakika ya 90’+1.

Kwa matokeo hayo, Namungo FC inafikisha pointi 21 katika mchezo wa 16 na kupanda kwa nafasi mbili hadi ya sita, wakati Singida Black Stars inafikisha pointi 16 katika mchezo wa 10 na kupanda kwa nafasi mbili pia hadi ya 10.

Friday, February 27, 2026

VIJANA 336 WAHITIMU VETA MWANZA.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa

Jumla ya vijana 336 kutoka Wilaya za Ilemela na Nyamagana mkoani Mwanza wamehitimu mafunzo ya stadi za maisha na ufundi stadi katika fani mbalimbali, na kukabidhiwa vifaa vya kuanzia kazi ili kuwawezesha kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Vijana hao wamehitimu leo Februari 27, 2026 katika VETA Mwanza, ambapo wamekabidhiwa vyeti baada ya kupatiwa mafunzo ya uselemala, uashi, uchomeleaji, ufundi bomba, aluminium, umeme wa magari na majumbani, ufundi magari na upishi. Aidha, walipata elimu ya stadi za maisha, biashara, fedha, ujasiriamali, usawa wa kijinsia pamoja na teknolojia na TEHAMA.

Wahitimu hao ni sehemu ya vijana 400 walioandikishwa katika awamu ya pili ya mradi wa Vijana Elimu, Malezi na Ajira (VEMA) unaotekelezwa na Plan International mkoani Mwanza, kwa lengo la kuwawezesha vijana kutoka familia zisizojiweza kupata ujuzi wa kujiajiri au kuajiriwa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amiri Mkalipa, amewataka vijana hao kuendeleza ujuzi walioupata na kuvitunza vifaa walivyokabidhiwa. Ameonya kuwa yeyote atakayebainika kuuza vifaa hivyo atachukuliwa hatua za kisheria.

“Huu ni mwanzo wa safari. Mmepewa elimu na vifaa vya kuanzia kazi, hatutarajii kuona mnaishia njiani. Hatutakubali kuona unauza cherehani; utakuwa hujatimiza wajibu wako,” amesema Mkalipa.

Mratibu wa mradi wa VEMA, Gadiel Kayanda, amesema shirika limetumia zaidi ya shilingi milioni 160 kulipia ada za mafunzo na kununua vifaa vya kujifunzia. Aidha, wahitimu hao wamekabidhiwa vifaa vya kuanzia kazi vyenye thamani ya shilingi milioni 69 kulingana na fani walizosoma.

Kwa mujibu wake, tayari vijana 58 kati ya walionufaika wameajiriwa, huku 30 wakijiajiri katika shughuli mbalimbali za uzalishaji.

Mwakilishi wa wahitimu, Raina Revelian, mhitimu wa umeme majumbani, amesema wenzao 64 walishindwa kumaliza mafunzo kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo utoro, kukosa ruhusa kutoka kwa wazazi, ujauzito, magonjwa, umbali na muda mfupi wa mafunzo.

Amesema mafunzo hayo yamewapa ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko na kuwafungua milango ya kujiajiri na kuajiriwa, akitaja siku ya mahafali kuwa ni ya kihistoria kwao.

RAIS DKT. SAMIA AKISHIRIKI MISA TAKATIFU YA KUAGA MWILI WA MWADHAMA POLYCARP KARDINALI PENGO

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaini Kitabu cha Maombolezo kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo mara baada ya kuwasili katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa pamoja na viongozi mbalimbali kwenye Misa Takatifu ya kumuombea na kumuaga Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Marehemu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Februari, 2026.




Kengele ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph ililia kwa dakika kumi mfululizo, mara tu baada ya mwili wa Askofu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Hayati Polycarp Kardinali Pengo, kuwasili kanisani hapo.

Na haya ni mambo machache kumuhusu;

1. Jina lake halisi ni nani? Kuna watu wanadhani Mwadhama ni jina lake? Wengine wanadhani Polycarp ni cheo chake. Jina lake ni Polycarp Pengo. Kardinali ni cheo cha Kanisa, na Mwadhama ni kivumishi cha sifa, kama ambavyo Maaskofu huitwa Mhashamu au Mbunge kuitwa Mheshimiwa.

2. Kwanini neno Kardinali lipo katikati ya majina yake na sio mwanzoni? Kwanini hakuitwa Kardinali Polycarp Pengo, akaitwa Polycarp Kardinali Pengo? Kanisa Katoliki lina utaratibu wa majina. Utaratibu huo huitwa modus titulorum ama style of titulature kwa kingereza. Kwa Makardinali wote, neno Kardinali hukaa katikati ya majina yao. Ndiyo maana Kardinali mpya anaitwa Protase Kardinali Rugambwa. Hata Papa Leo XIV kabla ya kuwa Papa aliitwa Robert Kardinali Prevost.

3. Kardinali Pengo ni miongoni mwa Maaskofu wachache kutoka Tanzania waliowekwa wakfu na Papa mwenyewe. Alipoteuliwa kuwa Askofu wa Nachingwea, aliitwa Vatican na kuwekwa wakfu na Papa John Paul II January 6, mwaka 1984 katika Basilika Kuu la Mtakatifu Petro.

4. Watu wengi wanashangaa kumbe Pengo alikuwa msomi wa kiwango cha PhD? Mbona alikuwa hajiiti Dr? Jibu ni kwamba katika Kanisa Katoliki, vyeo vya kitaaluma havipewi kipaumbele kuliko vyeo vya kiroho. Kuna doctrine ya unyenyekevu (humility) ambayo inasisitiza watawa wasijikweze kwa vyeo vya kisomi, bali wajitambulishe kwa nafasi zao za kiroho (Askofu, Kardinali, Padre etc).

Kardinali Pengo alikuwa na PhD ya Moral Theology kutoka Chuo Kikuu kinachoheshimika sana duniani cha Lateran, lakini maisha yake yote hakuwahi kujiita Dokta. Na hata pale TEC karibu Maaskofu wote ni PhD lakini huwezi kusikia wakijiita Dokta. Ni kwa sababu ya doctrine of humility.

5. Kwanini hakuzikwa kijijini kwao Mwazye, Kalambo? Ukiwa Mkleri utazikwa kwa utaratibu wa Kanisa. Mkleri ni mtu aliyepokea sakramenti ya daraja Takatifu. Hata hivyo angeweza kuzikwa Jimbo Katoliki Lindi au Tunduru-Masasi alipokuwa Askofu wa kwanza wa jimbo hilo. Lakini alishajiandalia kaburi lake kule Pugu. Na alichagua Pugu kwa sababu maisha yake ya utume yamekua zaidi Dar kuliko mahali pengine. Na pia alitamani kuzikwa pamoja na Wamisionari wa kale waliozikwa Pugu.!

Chanzo:  Malisa GJ