ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, April 10, 2026

SERIKALI YAKUTANA NA MHE. CHAKWERA

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi (kushoto), akiwa  na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera,

Na Mwandishi wetu

Ujumbe wa Serikali ya Tanzania ukingozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi, imekutana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera, na kujadiliana kuhusu namna Tanzania ilivyojidhatiti katika kudumisha umoja, amani na mshikamano miongoni mwa Watanzania.

Kikao hicho kilifanyika katika Kituo cha Mikutano cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyrere (JNICC) siku ya Alhamisi Aprili 9, 2026 mchana baada ya Mheshimiwa Chakwera kumtembelea Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahamoud Thabit Kombo, ikiwa ni ishara ya kuanza rasmi kwa ziara ya Mjumbe huyo Maalum nchini Tanzania.


Katika kikao hicho, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mjumbe huyo Maalum, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchululiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka mssisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.

“Tumekutana na Mheshimiwa Chakwera na tumemueleza mambo mengi kuhusu Tanzania na historia ya nchi hii tangu ipate uhuru mwaka 1961, hali ya siasa na demokrasia nchni, na hatua ambazo serikali inaendelea kuchukua ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo”, ameeleza Waziri Kabudi.

Waziri kabudi ameeleza kuwa kikao hicho kimekuwa kizuri na chenye mafanikio kutokana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola kupata ufafanuzi wa kutosha juu ya masuala mbalimbali yanayoendelea nchini hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania.


Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera anatarajiwa kukutana na wadau mbalimbali ambapo jana Aprili 10, 2026 alikutana na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi pamoja na vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.

Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).


Katika ziara yake hii, Mheshimiwa Chakwera anatarajia pia kukutana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.

Aidha, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, atakutana pia na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

JEH ALAMA ZILIZOPO KWENYE NOTI YA DOLA 1YA MAREKANI ZINAMAANISHA NINI?

Illustration of U.S. $1 bill symbols

Bila shaka unaifahamu noti ya dola 1 ya Marekani. Huenda umeiona maelfu ya mara, na ni mojawapo ya sarafu zinazotambulika zaidi duniani. Inawezekana hata una kadhaa kwenye pochi yako hivi sasa.


Lakini ni mara ngapi umeiangalia kwa makini na kujiuliza maana ya muundo wake na alama zilizopo juu yake?


Kwanza kabisa, alama hizo hazikuchaguliwa kwa bahati. Kwa mfano, picha ya George Washington haikuwa kwenye dola tangu mwanzo. Noti ya kwanza halali ya dola 1 ilitolewa wakati wa Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Marekani, na ilikuwa na picha ya Salmon P. Chase ambaye alikuwa Waziri wa Fedha wakati huo. Washington aliwekwa kwenye dola hiyo mwaka 1869.


Upande wa Mbele wa Dola

Tuanzie upande wa mbele wa noti, ambao una picha ya Washington. Upande huu una vitu vingi, ikiwa ni pamoja na:

Great Seal


Muhuri wa Wilaya ya Benki Kuu (Federal Reserve)

- Herufi na namba ya nafasi ya noti

- Namba ya mfululizo (serial number)

- Muhuri wa Hazina ya Marekani

- Namba ya sahani ya uchapishaji

- Mwaka wa toleo (series)


Kwa mfano, kila noti ya dola 1 ina muhuri wa Wilaya ya Federal Reserve System. Huu ni namba (kama 1 au 2) unaoonekana mara nne kwenye noti. Namba hiyo inaonyesha ni benki ipi ya Federal Reserve iliyochapisha noti hiyo. Mfano, namba 2 ina maana ilichapishwa New York. Pia kuna herufi (kama B) inayobainisha wilaya husika.


Herufi na namba ya nafasi ya noti (mfano B3) inaonyesha nafasi halisi ya noti kwenye sahani ya uchapishaji. Pia kuna namba ya sahani (plate number) inayotumika kutambua sahani iliyotumika kuchapisha noti hiyo.


Namba ya mfululizo (serial number) ni mchanganyiko wa herufi na tarakimu 11, na kila noti ina namba yake ya kipekee. Herufi ya kwanza lazima ifanane na ile ya muhuri wa Federal Reserve; ikiwa haifanani, kuna uwezekano noti hiyo ni bandia.


Mwaka wa toleo (series), kwa mfano 2009, hauonyeshi mwaka noti ilipochapishwa, bali ni mwaka ambao muundo huo ulianza kutumika. Mabadiliko hutokea pale kunapokuwa na mabadiliko kama kuteuliwa kwa Waziri mpya wa Fedha.


Muhuri wa Hazina ya Marekani pia upo upande wa mbele. Umebaki karibu sawa tangu 1789, ukiwa na mizani ya haki, ufunguo, na nyota 13. Muundo wa awali uliundwa na Francis Hopkinson.


Upande wa Nyuma wa Dola

Upande wa nyuma una alama muhimu sana, ikiwemo pande mbili za Muhuri Mkuu wa Marekani (Great Seal), pamoja na namba ya sahani ya uchapishaji.

Muhuri Mkuu wa Marekani (Great Seal)

Muhuri huu ulianzishwa na waanzilishi wa taifa la Marekani. Mnamo 1776, kabla ya Continental Congress kuvunjwa, kamati iliundwa yenye watu kama:

- John Adams

- Thomas Jefferson

- Benjamin Franklin

Lengo lao lilikuwa kubuni muhuri unaoonyesha maadili ya taifa jipya. Muundo wa mwisho uliidhinishwa miaka mitano baadaye, ukibuniwa na Charles Thomson.Great Seal

Upande wa mbele wa muhuri:

Una tai wa Marekani akiwa na Tawi la mzeituni (amani) Mishale (vita)

Kauli mbiu “E Pluribus Unum” (Kutoka wengi, kuwa mmoja)


Juu yake kuna nyota 13 zinazoashiria makoloni 13 ya awali. Mistari ya ngao pia ina maana ya umoja wa majimbo hayo.


Upande wa nyuma wa muhuri:

Una piramidi isiyokamilika yenye safu 13 za mawe, ikionyesha nguvu na uimara. Juu yake kuna jicho lenye mwanga (ishara ya ulinzi wa Mungu).


Maneno yaliyoandikwa ni:

- “Annuit Coeptis” (Mungu ameibariki juhudi yetu)

- “Novus Ordo Seclorum” (Mpangilio mpya wa zama)

Chini kuna namba za Kirumi (1776), kuashiria mwaka wa kuanzishwa kwa taifa.


Hitimisho.

Muundo wa dola 1 una maana nyingi na historia ndefu. Kila alama ina ujumbe wake maalum kuhusu umoja, nguvu, amani na mwanzo wa taifa la Marekani. Na jambo la kuvutia zaidi ni kwamba, kuna sheria inayozuia kubadilishwa kwa muundo wa noti ya dola 1 — hivyo utaendelea kubaki kama ulivyo kwa muda mrefu.

Thursday, April 9, 2026

MODULI YA RUFAA KUBORESHA MNYORORO WA UGAVI WAZINDULIWA

Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.
Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma. 

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema ujenzi wa moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST utachangia kuongeza uwajibikaji, uwazi na ufanisi kwenye mnyororo wa ugavi.

Katibu Mtendaji wa PPAA, James Sando amebainisha hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 na kuongeza kuwa Moduli hiyo imewaunganisha wazabuni wote na Taasisi nunuzi nchini ili kuongeza uwajibikaji katika utatuzi wa migogoro inayotokana na michakato ya ununuzi wa umma. 

“PPAA ni moja kati ya taasisi zinazosimamia ununuzi wa umma nchini, matumizi ya moduli hiyo katika mnyororo wa ugavi yatachangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati uliokusudiwa,” amesema Sando.

Pamoja na mambo mengine, Sando amebainisha kuwa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma yatasaidia kuongeza uwazi, kupunguza gharama, kuokoa muda, utunzaji wa nyaraka na hivyo kuongeza ufanisi katika hukumu zinazotolewa kutokana na michakato mbalimbali ya zabuni za umma.

Sando ameongeza kuwa, PPAA imefanikiwa kushiriki katika utungwaji wa Sera ya Taifa ya Mnyororo wa Ugavi, Sheria ya Ununuzi wa Umma, Kanunuzi za Ununuzi wa Umma na Kanuni za Rufaa za Ununuzi wa Umma ambapo yote ni michango wa Mamlaka ya Rufani katika mnyororo wa ugavi.

Kadhalika, Mamlaka ya Rufani inatarajia kuboresha kipengele cha makundi maalum na vijana ambapo inategemea kuboresha gharama au tozo za kesi kwa makundi maalum pamoja na kuelekeza nguvu kwa vijana na kuhakikisha wanapata fursa ya kudai haki zao katika michakato ya ununuzi wa umma.

Awali akizindua Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba amezielekeza mamlaka, taasisi na wadau wote wanaosimamia utekelezaji wa Sera hiyo kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora, uwazi na utawala wa sheria.‎

‎Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo wakati akizundua Sera hiyo kwa niaba ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Dk. Nchemba amesema changamoto zinazoikumba sekta ya ununuzi wa umma hazitokani na sera au sheria zilizopo, bali ni uzembe na mitazamo ya baadhi ya watendaji.‎

‎Ameongeza kuwa taarifa za ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zinaonesha wazi kuwa kasoro nyingi zinasababishwa na utekelezaji dhaifu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

“Sehemu kubwa ya changamoto hizo zinatokana na hulka, tabia na mitazamo ya watendaji. Hivyo, ni lazima tubadilike ili kufikia malengo ya sera hii,” amesisitiza Dk. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu, amezitaka wizara, taasisi na mamlaka zote kufanya mapitio ya sera, sheria na kanuni zinazokinzana na sera hiyo ili kuweka mazingira rafiki ya utekelezaji wake.

Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar amesema sera hiyo ni mwongozo muhimu utakaosaidia kuimarisha mifumo ya ugavi katika sekta ya umma, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kudhibiti vitendo vya rushwa.‎

Balozi Khamis ameongeza kuwa utekelezaji wa sera hiyo utaongeza ajira, kuimarisha mnyororo wa thamani na kuchochea mageuzi makubwa ya kiuchumi kuelekea dira ya maendeleo ya mwaka 2050.


Sehemu ya viongozi mbalimbali walioshiriki katika uzinduzi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), wakati alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), (Katikati Kulia), akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na viongozi wengine wakisikiliza maelezo kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Bw. James Sando (kushoto), kuhusu mchango wa PPAA katika Mnyororo wa Ugavi, wakati Mhe. Waziri Mkuu alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.

SIMBA SC NAYO YACHANGIA MAPATO KWA TRA UNITED ARUSHA, ZATOKA SULUHU

 


TIMU ya Simba SC imetoa sare ya bila mabao na wenyeji, TRA United katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha. 

Kwa matokeo hayo, TRA inayofundishwa na Kocha Mrundi, Ettienne Ndayiragijje inafikisha pointi 24 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya saba ikiizidi tu wastani wa mabao Dodoma Joni FC baada ya wote kucheza mechi 18. 

Kwa upande wao Simba SC wanafikisha pointi 36 katika mchezo wa 17, ingawa wanabaki nafasi ya pili wakizidiwa pointi nane na mabingwa watetezi, Yanga ambao hata hivyo wamecheza mechi moja zaidi.




AZAM FC YALAZIMISHWA SARE V/s MBEYA CITY

 


TIMU ya Azam FC imelazimishwa sare ya bila kufungana na wenyeji, Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, Babati mkoani Manyara.

Kwa matokeo hayo, Azam FC inafikisha pointi 34 katika mchezo wa 18, ikibaki nafasi ya tatu, wakati Mbeya City inafikisha pointi 17 katika mchezo wa 18 pia, nayo ikibaki nafasi ya 12 kwenye Ligi Kuu inayoshirikisha timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao. 

IRAN YATANGAZA VIPENGELE 10 INAVYODAI KUWA MSINGI WA MAZUNGUMZO YA KUSITISHA MAPIGANO

Men in orange outfits clean up rubble from a destroyed building.
Iran ilitangaza hadharani Jumatano kile ilichodai kuwa ni mfumo wa vipengele 10 kwa ajili ya mazungumzo, ambao Rais Trump aliuelezea kama “msingi unaoweza kufanyiwa mazungumzo” ili kumaliza vita. 

Sehemu kubwa ya vipengele hivyo ilijumuisha madai ya juu sana ambayo yanaonekana kuwa magumu, kama siyo yasiyowezekana, kupatanishwa na malengo ya Marekani.

Afisa mmoja wa Ikulu ya White House alisema vipengele hivyo haviendani na kile alichokuwa anakimaanisha Trump. Afisa huyo alizungumza kwa sharti la kutotajwa jina ili kujadili mazungumzo ya ndani ya White House.

Iran ilitoa toleo lake la pendekezo hilo asubuhi baada ya Marekani na Iran kukubaliana kusitisha mapigano kwa wiki mbili, na linataka wanajeshi wa Marekani kuondoka katika eneo hilo, linarejesha msisitizo wa udhibiti wa Iran juu ya Mlango wa Hormuz wenye umuhimu wa kimkakati, na linadumisha haki ya Iran ya kurutubisha nyuklia.

Mengi ya madai hayo yana uwezekano mkubwa wa kugongana na pendekezo la vipengele 15 lililotolewa na wapatanishi wa Marekani mwezi uliopita.

Pendekezo hilo halikuwahi kuwekwa hadharani, lakini maafisa waliopata taarifa zake, waliozungumza na gazeti la The New York Times kwa sharti la kutotajwa majina kutokana na unyeti wa taarifa, walisema lilihusu programu ya makombora ya balestiki ya Iran na mpango wake wa nyuklia, pamoja na biashara ya baharini. Katika mazungumzo ya awali, wapatanishi wa Marekani walisisitiza kupunguza umbali wa makombora ya balestiki ya Iran na kusitisha kabisa urutubishaji wa nyuklia.

Trump alionekana kurejea mpango huo wa Marekani siku ya Jumatano, akiandika kwenye mitandao ya kijamii kuwa “vipengele vingi kati ya vile 15 tayari vimekubaliwa,” na kurudia msimamo wake wa “kutokuwepo kabisa kwa urutubishaji wa urani.”


MASHARTI 10 YA IRAN AMBAYO NI MWIBA KWA MAREKANI

1. Dhamana ya Marekani ya kutofanya uchokozi dhidi ya Iran

Katika pendekezo la awali la vipengele 15 kutoka kwa wapatanishi wa Marekani, kulikuwa na pendekezo la kusitisha mapigano tu. Maafisa wa Iran wanataka kuhakikisha kuna mwisho rasmi na wa kudumu zaidi wa uhasama.
Hili ni moja ya madai makuu ambayo Iran inalenga kulipa kipaumbele.

2. Iran kudumisha udhibiti wa Mlango wa Hormuz
Hili linaweza kuwa suala gumu sana kufikiwa mwafaka. Uwezo wa Iran kudhibiti au kuzuia usafiri wa meli katika mlango huo, ambako hupita takriban theluthi moja ya mafuta ya dunia, umekuwa ukitikisa uchumi wa dunia. Ni vigumu sana kwa Marekani au nchi za Kiarabu za Ghuba kukubali hilo.

3. Kumaliza vita vya kikanda katika nyanja zote, ikiwemo dhidi ya mshirika wa Iran, Hezbollah nchini Lebanon
Hili linaweza kuwa eneo la kufikia muafaka baadaye.


Marekani na Israel zinataka Tehran kudhibiti mtandao wa makundi ya wanamgambo inayounga mkono katika eneo hilo, unaoitwa “Axis of Resistance.” Baadhi ya makundi hayo yameishambulia Marekani, nchi za Ghuba na Israel kwa kutumia ndege zisizo na rubani na makombora.


Miongoni mwao ni Hezbollah ya Lebanon, ambayo ilishambuliwa vikali na Israel, ambayo baadaye ilitangaza mipango ya kukalia sehemu za kusini mwa Lebanon.
Israel imesema usitishaji wa mapigano hauhusu operesheni zake nchini Lebanon, hivyo bado haijulikani kama suala hilo linaweza kuingizwa kwenye makubaliano ya muda mrefu.

4. Kuondolewa kwa majeshi ya Marekani katika vituo vyote vya kijeshi katika eneo hilo
Marekani ina vituo vya kijeshi katika nchi za Ghuba, Israel na Iraq. Ni vigumu kufikiria hali ambayo Marekani itakubali sharti hili.

5. Fidia kwa Iran kutokana na uharibifu wa vita
Iran imepata uharibifu mkubwa, si tu kwenye maeneo ya kijeshi bali pia miundombinu muhimu kama viwanda vya dawa, chuma, madaraja, vyuo vikuu na nishati.
Hakuna dalili kwamba Marekani iko tayari kulipa fidia hiyo.

6. Kutambuliwa kwa haki ya Iran ya kurutubisha nyuklia
Hili linapingana kabisa na msimamo wa Trump, ambaye amesisitiza kutokuwepo kabisa kwa urutubishaji wa urani.


Baadhi ya wanadiplomasia wa kikanda wamependekeza Iran iruhusiwe urutubishaji mdogo sana kwa matumizi ya kiraia, lakini bado haijulikani kama Marekani itakubali.

7. Kuondolewa kwa vikwazo vya moja kwa moja (primary sanctions)
Marekani imeweka vikwazo mbalimbali vya kifedha dhidi ya Iran tangu mapinduzi ya mwaka 1979.

Katika mazungumzo ya awali, kulikuwa na wazo la kuondoa baadhi ya vikwazo hivyo badala ya Iran kufanya mabadiliko kwenye mpango wake wa nyuklia. Trump pia aligusia uwezekano wa kupunguza ushuru na vikwazo.

8. Kuondolewa kwa vikwazo vya sekondari (secondary sanctions)
Hivi ni vikwazo vinavyolenga pia nchi au kampuni nyingine zinazofanya biashara na Iran.
Kipengele hiki kinaweza kujadiliwa kulingana na makubaliano yatakayofikiwa.

9. Kufutwa kwa maazimio yote dhidi ya Iran na Bodi ya Magavana ya Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA)
Mwaka jana, shirika hilo lilipitisha azimio dhidi ya Iran likidai haitekelezi wajibu wake wa kudhibiti usambazaji wa silaha za nyuklia. Iran ililaani hatua hiyo kama ya kisiasa.
Marekani haiwezi kulazimisha kufutwa kwa maazimio hayo moja kwa moja, lakini inaweza kushawishi washirika wake.

10. Kufutwa kwa maazimio yote ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa dhidi ya Iran
Kumekuwa na maazimio kadhaa dhidi ya Iran, hasa kuhusu nyuklia. Mwaka uliopita, Umoja wa Mataifa ulirejesha vikwazo dhidi ya Iran kwa kukiuka makubaliano ya mwaka 2015.


Marekani inaweza kujaribu kushawishi washirika wake, lakini hilo litahitaji makubaliano mapana zaidi na Iran.

KILA MWENYE PUMZI AKAPELA - AIC Chang'ombe Choir (CVC)

 Kipindi cha Pasaka ya Mwaka huu 2026 tumepata nafasi ya kuwafikia AIC Chang'ombe Choir ya Jijini Dar es salaam, waliokuwa na mwaliko wa kushiriki ibada ya uimbaji katika kanisa la AICT Makongoro jijini Mwanza.

Wednesday, April 8, 2026

MUDA ATUPIA MBILI YANGA SC IKIICHAPA PAMBA 3-0 KIRUMBA

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya wenyeji, Pamba Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na viungo Mudathir Yahya Abbas mawili dakika ya nane na 34 na Mkongo, Maxi Mpia Nzengeli dakika ya 67.


Kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi 44 katika mchezo wa 18 kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi tisa zaidi ya watani wao, Simba SC ambao pia wana mechi mbili mkononi.

Kwa upande wao, Pamba Jiji FC baada ya kupoteza mchezo wa leo wanabaki na pointi zao 26 za mechi 18 sasa wakishuka kwa nafasi moja hadi ya sita.

Tuesday, April 7, 2026

KOCHA PEDRO AIVULIA KOFIA PAMBA JIJI ILA ASEMA ALAMA TATU UHAKIKA.

NA ALBERT G. SENGO, MWANZA Kuelekea mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Pamba Jiji na Young Africans (Yanga SC) utakaopigwa katika dimba la CCM Kirumba jijini Mwanza, Kocha Mkuu wa Yanga, Pedro Goncalves, amesema timu yake inatarajia upinzani mkali kutoka kwa wenyeji hao. Goncalves ameeleza kuwa Pamba Jiji ni timu imara inapocheza nyumbani, ikiwa bado haijapoteza mchezo wowote katika uwanja wake, huku timu kadhaa kubwa zikishindwa kuondoka na alama tatu hali inayoashiria ugumu wa mchezo huo. “Tunatarajia mazingira magumu ya mchezo. Uwanja hautaruhusu soka la kuvutia, lakini hilo halibadilishi malengo yetu. Tunapaswa kuwa imara, makini na kupambana ili kupata alama tatu,” amesema kocha huyo. Ameongeza kuwa wapinzani wao wanacheza kwa nguvu na kasi, wakitumia vyema faida ya uwanja wa nyumbani pamoja na sapoti kubwa kutoka kwa mashabiki wao. “Ni timu inayocheza kwa msukumo mkubwa wa mashabiki wake. Wanajua namna ya kutumia mazingira yao kwa faida yao, hivyo nasi tumelazimika kujiandaa kisaikolojia na kimkakati kukabiliana na hali hiyo,” aliongeza. Kocha huyo ameonyesha imani kubwa kwa kikosi chake, akisisitiza kuwa wachezaji wake wamekuwa wakionyesha ari, nidhamu na uwezo wa kujiboresha kila siku. “Nina imani kubwa na wachezaji wangu. Kesho tunahitaji kuonyesha moyo wa upambanaji, ushindani, nidhamu na umoja ili kufanikisha malengo yetu,” amesema. Kwa upande wake, beki wa Yanga, Israel Mwenda, aliyewakilisha wachezaji, amesema wanatambua umuhimu wa mchezo huo pamoja na ubora wa mpinzani wao. “Kwa niaba ya wachezaji wenzangu, tunatambua umuhimu wa mchezo wa kesho. Utakuwa na ushindani mkubwa na kila mmoja wetu analitambua hilo. Tumerejea katika ari ya ushindi na tunakusudia kuendeleza mwenendo huo,” amesema Mwenda. Aidha, ametoa wito kwa mashabiki wa Mwanza na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kuisapoti timu hiyo. “Tunawaalika Wananchi kujitokeza kwa wingi kutupa sapoti. Tunawahakikishia kuwa tutapambana kwa nguvu zote ili waondoke wakiwa na furaha,” aliongeza. Akijibu swali la waandishi wa habari kuhusu presha ya mchezo huo, Mwenda amesema hawana presha yoyote, akisisitiza kuwa kucheza katika klabu kubwa kama Yanga kunahitaji uzoefu wa kukabiliana na mazingira yoyote. “Hatuna presha. Unapocheza Yanga lazima uwe tayari kukabiliana na hali yoyote. Tumejielekeza katika maandalizi sahihi na umakini mkubwa tukitambua umuhimu wa mchezo huu,” alihitimisha.

NI ZAIDI YA NUSU KARNE SASA TANGU MAUAJI YA KARUME.

 


🏴Leo ni kumbukizi ya miaka 54 tangu kuuawa kwa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Sheikh Abeid Amani Karume, kiongozi aliyebeba alama ya mapambano, mageuzi na ujenzi wa taifa jipya visiwani humo.


Karume aliuawa Aprili 7, 1972, kwa kupigwa risasi katika eneo la Kisiwandui, Unguja, yalipokuwa Makao Makuu ya Chama cha Afro-Shiraz. Tukio hilo liliacha pengo kubwa katika uongozi wa Zanzibar na historia ya siasa za Tanzania kwa ujumla.

Miaka zaidi ya nusu karne baadaye, wadau wa siasa na wananchi kwa ujumla wanaendelea kumkumbuka kwa misingi aliyoiasisi ikiwemo msisitizo wa usawa wa kijamii, uzalendo, na ujenzi wa uchumi unaowajali wananchi wa kawaida. Hata hivyo, baadhi yao wanahoji kuwa dira na maono hayo yameanza kufifia au kupuuzwa kadri nyakati zinavyobadilika.

Kumbukizi hii si tu ya kuenzi maisha yake, bali pia ni fursa ya kutafakari juu ya misingi aliyosimamia, na kujiuliza kama bado ina nafasi katika kuongoza maendeleo ya Zanzibar ya leo.
.
.
#KarumeDay

YANGA TAWI LA NYAMANORO WATISHA KUELEKEA MCHEZO DHIDI YA PAMBA FC

 Mkurugenzi wa Wanachama na Masoko @i_sammjr kwenye uzinduzi wa Tawi la Yanga Nyamanoro ikiwa ni Tawi la Kwanza kati ya matawi Saba yanayozinduliwa leo hii hapa Jijini Mwanza.

Monday, April 6, 2026

AZAM FC Vs SIMBA SC 'NGOMA NYAU NYAU'

 


TIMU za Azam FC na Simba SC zimetoshana nguvu kwa sare ya bila mabao katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya Jumapili ya Tarehe 05 April 2026 Uwanja wa Azam Complex, Chamazi Jijini Dar es Salaam.

Ulikuwa mchezo mzuri wa kiufundi na maarifa, timu zote — Azam FC inayofundishwa na Kocha Mkongo Jean-Florent Ikwange Ibenge na Simba SC ya Kocha raia wa Afrika Kusini, Steven Robert Barker zikishambuliana kwa zamu.
Kwa matokeo hayo, Azam FC inafikisha pointi 33 katika mchezo wa 17, ingawa inabaki nafasi ya tatu ikizidwa pointi mbili na Simba SC ambayo pia ina mechi moja mkononi.

Ikumbukwe, mabingwa watetezi, Yanga SC ndio wanaongoza Ligi Kuu kwa pointi zao 41 za mechi 17.

HIGHLIGHTS: YANGA SC 3-0 TZ PRISONS | MAGOLI YA KIUFUNDI YALIVYOFUNGWA KWENYE DIMBA LA KMC

 

 
MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara katika mchezo uliopigwa Jumamosi ya tarehe 4 April 2026 Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao ya Yanga SC leo yote yamefungwa na viungo, Mganda, Allan Jolly Okello ‘Star Boy’ dakika ya 50, mzawa Mudathir Yahya Abbas dakika ya 68 na Muivory Coast, Peodoh Pacome Zouzoua dakika ya 86.

Kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi 41 katika mchezo wa 17 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu ikifuatiwa na watani wao, Simba SC wenye pointi 35 za mechi 16.

Kwa upande wao Tanzania Prisons baada ya kupoteza mchezo wa leo inabaki na pointi zake 13 za mechi 18 sasa nafasi ya 15 kwenye ligi ya timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.    

Friday, April 3, 2026

AKINAMAMA CHANGAMKIENI FURSA ZA MIKOPO NAFUU AKIBA COMMERCIAL BANK

 

Na Albert G. Sengo | Mwanza

Katika juhudi za kuimarisha uchumi jumuishi na kukuza ujasiriamali miongoni mwa wanawake, Benki ya Akiba (Akiba Commercial Bank) imeendelea kujenga ukaribu wa karibu na wateja wake kupitia mikutano ya moja kwa moja. Moja ya hatua hizo ni mkutano maalum uliowakutanisha akinamama wajasiriamali wa Mwanza, uliofanyika tarehe 31 Machi 2026 katika ukumbi wa ARCH Mayala, Nyakahoja.


Tukio hilo lilihudhuriwa na zaidi ya washiriki 100, wengi wao wakiwa ni akinamama wanaojishughulisha na biashara ndogo na za kati katika maeneo mbalimbali ya Kanda ya Ziwa Victoria kuanzia biashara za vyakula, usindikaji wa mazao ya kilimo, uuzaji wa samaki, hadi huduma za kijamii kama elimu na urembo.

POLISI MWANZA YASISITIZA MARUFUKU DISKO TOTO

news 

JESHI la Polisi Mkoa wa Mwanza limesisitiza marufuku ya kuandaa burudani za watoto katika kumbi za starehe (disko toto) likisema marufuku hiyo inalenga kulinda rika hilo na vitendo vya uvunjifu wa amani na kupotea.

Marufuku hiyo imesisitizwa leo Aprili 3, 2026 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbrod Mutafungwa, wakati akizungumzia maandalizi ya kuimarisha ulinzi na usalama kuelekea sikukuu hizo.

Pia Mutafungwa amepiga marufuku wazazi kuwaruhusu watoto kwenda kwenye matembezi ama sehemu za burudani bila uangalizi wa watu wazima, huku akisisitiza kila mzazi kuhakikisha anaangalia watoto ili washerehekee wakiwa na ulinzi wa kutosha.

“Niwatake wamiliki wa nyumba za kulala wageni na kumbi za starehe kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia masharti ya leseni zao kwa kutoendesha na kuandaa matamasha ya watoto (disko toto) na kuhakikisha maeneo hayo yamewekewa ulinzi wa kutosha.

“Na tunaelekeza kwa namna yoyote mambo ya kuburudisha watoto disko toto mambo hayo ni marufuku na hatutasita kuchukua hatua za sheria kwa wafanyabiashara watakaofanya hivyo hata kama wana leseni, na tunaomba wazazi wasiwaruhusi kwenda huko,” amesema Mutafungwa.

Hata hivyo, ametoa wito kwa familia zinazosherehekea sikukuu nje ya makazi yao kutoacha nyumba zao zikiwa hazina uangalizi wowote.


“Wanapotoka wahakikishe nyumba ina ulinzi. Pia tunashauri wasitoke wote ndani ya nyumba, wabaki baadhi ya watu wanaoangalia nyumba ili kuepuka kupata changamoto,” amesema.

Amesema jeshi hilo limeimarisha ulinzi maeneo yote kwa kuwapanga askari wanaotumia doria za magari, pikipiki, magari ya wazi, askari wa kiraia, askari wanaotumia wanyama, na limeshaweka mpango kazi wa doria za boti katika visiwa vinavyozungika mkoa huo.

“Tunaomba kila mwananchi awe na utii mkubwa wa sheria na kuepuka mambo ambayo yanaweza kuwaweka kwenye migogoro na vyombo ambavyo vinasimamia sheria,” amesema Mutafungwa.

Vile vile, amewataka viongozi wa makanisa yatakayokuwa na ibada za asubuhi na usiku kuendelea kushirikiana na polisi katika ngazi ya wilaya na vituo ili kuhakikisha katika ibada zote askari wanakuwepo.

MWENYEKITI MANGUNGU NA KAMANDA MULIRO WAGUSA NA KUSIKITISHWA NA KIFO CHA EMMANUEL MACHA

 
NA VICTOR MASANGU, DAR

Maelfu ya wananchi mbali mbali wakiwemo viongozi wa serikali, viongozi wa dini,  taasisi na mashirika binafsi ,mashabiki wa soka na mziki wa dansi pamoja na wananchi mbali mbali .... wamejitokeza kwa wingi   katika makaburi ya Kinonddoni Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya  kuhudhuria mazishi ya mfanyabiashara maarufu na mshabiki mkubwa  wa klabu ya soka ya Simba Emmanuel  Nderimo almaarufu Macha ambaye alifariki dunia  machi 30 mwaka huu.

Katika mazishi hayo ambayo yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa serikali pamoja na chama cha mapinduzi (CCM) yalikubikwa na  vilio na majonzi makubwa ambayo yalipelekea baadhi ya watu kushindwa kujizuia kwa kutokwa na machozi  wakati wa zoezi la kuuga mwili huo.



Moja kati ya viongozi maarufu ambao walihudhulia katika  msiba huo ni Mwenyekiti wa klabu ya soka ya Simba Murtaza  Mangungu pamoja ambapo aliambatana na viongozi wengine mbali mbali wa klabu hiyo ambapo amesema marehemu Emmanuel alikuwa  na mchango mkubwa sana  katika klabu hiyo kwani alikuwa mstari wa mbela katika kusaidia mambo mbali mbali.


Pia Kamanda wa Polisi Kanda maalumu ya  Dar es Salaam SACP Jumanne Muliro naye alikuwa ni mmoja wa viongozi wa ulinzi na usalama ambaye naye  alifika kwa ajili ya kutoa heshima zake za mwisho  kwa Marehemu Emmaanuel Nderimo.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Mhe,Silvestry  Koka ambaye marehemu ni  shemeji yake hakusita  kumwelezea marehemu jinsi alivyokuwa ni mpambanaji katika mambo mbali nmbali na kwamba alikuwa ni mtu wa kusamehe sana pindi unapomkosea na kwamba alikuwa ni mstari wa mbele katika kutoa ushauri wenye kujenga.

"Kwa kweli mimi nimesimama hapa kwannza kabisa namshukuru mwenyezi Mungu muumba wa mbingu na nchi kwa kutukutanisha hapa katika msiba wa ndugu yetu Emmanuel lakini kitu ambacho nataka kukisema inapaswa tuishi kwa kupendana sana na ndio maana marehemu alikuwa na upendo mkubwa sana  na watu mbali mbali na alikuwa ni mwepesi sana katika suala la kusamehe kwa hivyo inapaswa tujifunze mazuri ambayo ametuachia."amebainisha Mhe. Koka.


Nao baadhi ya  viongozi na mashabiki akiwemo Mama Asha Baraka ambaye pia ni Mbunge wa viti maalumu kupitia tiketi ya chama cha mapinduzi (CCM) amesema kwamba ameguswa na kusikitishwa sana na msiba huo mzito kwani marehemu kwa upande wake alikuwa ni moja ya mtu muhimu sana katika kuleta chachu ya maendeleo katika ttimu pamoja na kuweza kusaidia mtu mmoja mmoja kwa hivyo ni pengo kubwa sana ambalo ameliacha.


Pia mwimbaji maarufu wa mziki wa dansi hapa nchini Ally Choki ni moja kati ya wasanii maarufu ambao walihudhulia katika msiba huo hadi kuweza kufika katika makaburi hayo ya Kinondoni kwa lengo la kumpumzisha ndugu yao na rafiki mkubwa wa burudani ya mziki wa dansi hapa nchini katika bendi mbali mbali.


Mazishi hayo ya marehemu Emmanule Nderimo  ambayo  yamefanyika katika makaburi ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam  yameweza kuhudhuliwa na umati wa  maelfu ya watu kutoka sehemu  mbali mbali wakiwemo viongozi wa serikali, viongozi wa chama, viongozi wa madhehebu ya  dini, taaasisi wezeshi,wasanii maarufu, pamoja na wananchi ambao wamewza kufika na kumuhifadhi katika nyumba yake ya milele.

AKINAMAMA WA KANDA YA ZIWA VICTORIA WANAVYOCHOCHEA UCHUMI KUPITIA UJASILIAMALI NA HUDUMA ZA KIFEDHA

 


Akinamama wa Kanda ya Ziwa Victoria Wanavyochochea Uchumi Kupitia Ujasiriamali na Huduma za Kifedha

Na Albert G. Sengo | Mwanza

Katika juhudi za kuimarisha uchumi jumuishi na kukuza ujasiriamali miongoni mwa wanawake, Benki ya Akiba (Akiba Commercial Bank) imeendelea kujenga ukaribu wa karibu na wateja wake kupitia mikutano ya moja kwa moja. Moja ya hatua hizo ni mkutano maalum uliowakutanisha akinamama wajasiriamali wa Mwanza, uliofanyika tarehe 31 Machi 2026 katika ukumbi wa ARCH Mayala, Nyakahoja.

Tukio hilo lilihudhuriwa na zaidi ya washiriki 100, wengi wao wakiwa ni akinamama wanaojishughulisha na biashara ndogo na za kati katika maeneo mbalimbali ya Kanda ya Ziwa Victoria kuanzia biashara za vyakula, usindikaji wa mazao ya kilimo, uuzaji wa samaki, hadi huduma za kijamii kama elimu na urembo.

Afisa Mkuu wa Biashara wa benki hiyo, Bi. Wezi Mwanzani,


Ni dhahiri kuwa wanawake wa Kanda ya Ziwa wanachangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa eneo hili. Kupitia ujasiriamali, wamekuwa wakitoa ajira, kuongeza thamani ya mazao ya ndani, na kuzungusha mzunguko wa fedha katika jamii.

Hata hivyo, pamoja na juhudi zao, bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa mitaji, elimu ya kifedha, pamoja na ugumu wa kupata huduma rasmi za kifedha. Hapa ndipo nafasi ya taasisi za kifedha kama Benki ya Akiba inakuwa muhimu zaidi.

Jukwaa la Kusikilizana na Kujifunza

Katika mkutano huo, washiriki walipata fursa ya kipekee ya kuzungumza ana kwa ana na viongozi waandamizi wa benki, kutoa maoni yao, na kueleza changamoto wanazokutana nazo katika safari yao ya ujasiriamali.

Afisa Mkuu wa Biashara wa benki hiyo, Bi. Wezi Mwanzani, alieleza kuwa mwitikio mkubwa wa wanawake wa Mwanza unaonyesha wazi imani waliyonayo kwa benki hiyo pamoja na uhitaji mkubwa wa huduma za kifedha zilizo karibu na mahitaji yao halisi.

“Tunaona wazi nguvu ya akinamama katika uchumi wa Mwanza. Kama benki, tunalenga kutoa huduma bunifu zinazomgusa mteja moja kwa moja kwenye uhalisia wa biashara yake,” alisema Bi. Wezi.

Aliongeza kuwa Mwanza ni eneo muhimu katika mkakati wa benki wa kuhakikisha huduma za kifedha zinawafikia wananchi wengi zaidi, hasa wale waliopo katika sekta isiyo rasmi.

Mkurugenzi wa Faith Junior School, Bi. Shiide Nyanda Lugoba.


Miongoni mwa washiriki waliotoa ushuhuda ni Mkurugenzi wa Faith Junior School, Bi. Shiide Nyanda Lugoba, ambaye alieleza namna mkopo kutoka Benki ya Akiba ulivyomsaidia kukuza taasisi yake ya elimu.

“Nimefanikiwa kuendesha shule kwa ufanisi zaidi kutokana na mkopo nilioupata. Leo hii, kupata huduma za kifedha si changamoto tena kama ilivyokuwa awali,” alisema.

Aidha, alibainisha kuwa matumizi ya mifumo ya kidijitali kama Lipa Namba yamerahisisha malipo kwa wateja wake, hasa wazazi, kwa kuwaondolea usumbufu wa foleni benki.

Elimu ya Fedha na Fursa za Mikopo



Mbali na majadiliano, washiriki walipata elimu muhimu kuhusu:

  • Usimamizi wa fedha binafsi na za biashara
  • Matumizi salama ya huduma za kidijitali
  • Njia bora za kukuza biashara kwa uendelevu
  • Fursa za mikopo nafuu kwa wajasiriamali


Elimu hii ni nyenzo muhimu inayoweza kuwasaidia akinamama kubadili biashara zao kutoka kiwango cha kawaida hadi kuwa miradi yenye tija kubwa kiuchumi.




Umuhimu wa Kurasimisha Biashara

Wakili Msomi Rose Ndege.

Kwa upande wake, Wakili Msomi Rose Ndege alisisitiza umuhimu wa kurasimisha biashara kama hatua ya msingi ya kufungua milango ya fursa za kifedha.

“Bila kurasimisha biashara, ni vigumu kupata imani ya taasisi za kifedha. Rasmi ni ufunguo wa kupata mitaji, kujenga uaminifu, na kukuza biashara,” alieleza.


Kwa ujumla, mkutano huu umeonesha wazi kuwa akinamama wa Kanda ya Ziwa si tu washiriki wa uchumi, bali ni injini muhimu ya maendeleo. Kupitia ushirikiano kati yao na taasisi za kifedha, kuna fursa kubwa ya kukuza biashara, kuongeza kipato, na hatimaye kuinua uchumi wa jamii nzima.

Kadri elimu ya kifedha inavyozidi kuenea na huduma za kifedha zinavyokuwa rafiki zaidi, ndivyo ndoto za wanawake wengi wajasiriamali zinavyoweza kutimia—kutoka biashara ndogo hadi kuwa himaya kubwa za kiuchumi.



Picha ya pamoja.