ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, February 4, 2026

GGML YAKABIDHI NYUMBA KWA JESHI LA POLISI GEITA.

Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela (kati kati) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa nyumba za makazi zilizojengwa na mgodi wa dhahabu wa Geita (GGML) mkoani humo. Kushoto kwake ni Mkuu wa Polisi mkoani humo BI. Safia Jongo na kulia kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa GGML, Duan Campbell

KAMPUNI ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) imekamilisha ujenzi wa nyumba mbili (nyumba pacha) za polisi katika mtaa wa Mgusu kata ya Mgusu wilayani Geita mkoani hapa.

Ujenzi wa nyumba hizo uliofanywa na GGML umehusisha ufadhili wa kiasi cha sh milioni 77 kwa zilizotumika kukamilisha maboma yaliyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi lengo likiwa ni kuboresha makazi ya askari polisi.

Kaimu Mkurugenzi wa GGML, Duan Campbell akiongea katika uzinduzi huo.

Akiongea wakati wa hafla ya kukabidhi nyumba hizo kwa jeshi la Polisi mkoani Geita, Kaimu Mkurugenzi wa GGML, Duan Campbell amesema  kuwa mbali na uchimbaji dhahabu, mgodi huo pia unashiriki katika maendeleo mbalimbali ya kijamii.

Bw.Duan alisema kukamilika kwa mradi huo huo ni muhimu kwani siyo tu unajenga mahusiano ya mgodi na jamii, lakini pia kuimarisha ulinzi na usalama kwenye maeneo yanayozunguka mgodi na wananchi kwa ujumla.


Alisema sera ya GGML inaamini kuwa Jamii imara inategemea taasisi imara za ndani, na moja ya taasisi zinazoshikilia uimara na ustawi wa jamii kila siku ni jeshi la polisi.


"Askari polisi wanaposaidiwa kwa kupata makazi bora, utulivu na heshima, uwezo wao wa kuitumikia jamii unaimarika zaidi, hali hii huongeza utayari wa kazi na kuimarisha usalama wa raia na mali zao. 


"Kampuni ya GGML tunaamini kwamba  Geita salama na yenye ulinzi wa uhakika inachangia moja kwa moja uendelevu wa shughuli zetu", alisema na kuongeza;


"Usalama hauishii ndani ya mgodi pekee, bali usalama upo pia majumbani, barabarani, shuleni, na mitaani ambako watu wanaishi na kufanya kazi", alisisitiza Duan.


Naye Ofisa Mtendaji wa Mtaa wa Mgusu, Nazoro Marcel alisema mradi ulianza kutekelezwa mwaka wa fedha 2019/20 kupitia nguvu za wananchi na wadau wa maendeleo kwa kuchangia ujenzi wa msingi na boma kwa thamani ya sh milioni 19.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Safia Jongo alisema ushirikiano kati ya wananchi, wadau wa maendeleo na viongozi wa Serikali imeleta matokeo chanya kupunguza matukio ya uharifu Geita.


Kamanda Jongo alikiri kuwa mchango GGML kwenye sekta ya ulinzi na usalama inawafanya kuwa wadau wakubwa wa amani ambapo wamesaidia kuboresha utendaji wa polisi mkoani humo.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Bw. Martine Shigela.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela aliipongeza GGML kwa msaada huo huku akiwaomba kutenga bajeti ya ujenzi wa kituo bora cha polisi cha kata ya Mgusui li kukidhi mahitaji ya eneo hilo.

Friday, January 30, 2026

SHABIKI KINDAKINDAKI WA MAN CITY ATUA SERENGETI

 


𝗛𝗔𝗧𝗜𝗠𝗔𝗬𝗘 ile kiu na ndoto ya kuitembelea Tanzania imetimia kwa mwanahabari wa michezo na shabiki sugu wa klabu ya Manchester City ya nchini Uingereza, Braydon Bent.

.
Akiwa katika ziara ya kitalii ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, picha na video za Braydon zimekuwa zikisambaa katika mitandao ya kijamii, zikimuonesha akifurahia kwa karibu vivutio mbalimbali vya wanyamapori pamoja na mandhari ya kuvutia yanayoburudisha macho na kuigusa roho.
.


Katika safari hiyo, Braydon ameambatana na rafiki yake wa muda mrefu na mwalimu wake wa lugha ya Kiswahili, ambaye pia ni mwanahabari na mtangazaji wa kujitegemea, John Jackson maarufu kama JJ. @johnjackson_jj 
.



Kupitia ujumbe aliouandika kwenye mitandao yake ya kijamii, Braydon aliandika:-

“LIONS 🦁 & HOT AIR BALLOON IN SERENGETI 🎈🇹🇿
ASANTE SERENGETI ☀️
SERENGETI NI NOMA! 🇹🇿
DAY 2 @serengeti_national_park
.
Safari hiyo imeendelea kuonesha jinsi Tanzania inavyoendelea kuwa kivutio kikubwa cha utalii wa kimataifa, huku Serengeti ikiendelea kuthibitisha hadhi yake kama moja ya hifadhi bora zaidi duniani.
.
📸 Captures by @infocusstudio.tz

CC: @braydonbentpage

#visittanzani
#visitzanzibar






Thursday, January 29, 2026

SIMBA YAIKUNYUGA MASHUJAA 2-0

 


TIMU ya Simba SC imeibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mashujaa FC ya Kigoma katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam.

Mabao ya Simba SC leo yamefungwa na winga mpya wa kushoto, Libasse Gueye (22) aliyesajiliwa mwezi huu katika dirisha dogo kutoka Teungueth FC ya kwao, Senegal dakika ya 27 na mshambuliaji Suleiman Abdallah Mwalimu 'Gomez' anayecheza kwa mkopo tangu mwanzo wa msimu kutoka Wydad Athletics dakika ya 76.

Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 16 katika mchezo wa saba na kusogea nafasi ya nne, wakati Mashujaa FC inabaki na pointi zake 13 za mechi 11 sasa nafasi ya nane.

Baada ya mchezo huo, Simba SC inarejea kambini kujiandaa na mchezo wa Kundi D Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Espérance ya Tunisia Jumapili kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Ili kufufua matumaini ya kwenda Robo Fainali, Simba inahitaji kushinda Jumapili ikitoka kufungwa mechi zote tatu za mwanzio ikiwemo ya Jumamosi ambayo walifungwa 1-0 na Espérance Uwanja wa Hammadi Agrebi Jijini Tunis nchini Tunisia.

Bao lililoizamisha Simba SC siku hiyo lilifungwa na winga chipukizi wa umri wa miaka 19 wa Burkina Faso, Jack Diarra dakika ya 21 akimtungua kipa wa Kimataifa wa Niger, Mahamadou Tanja Djibrilla Kassali Djibo.

TFF YALIFUNGIA DIMBA LA KMC

 


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeufungia Uwanja wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, maarufu kama KMC Complex, uliopo Mwenge Jijini Dar es Salaam kutotumika kwa mechi za Ligi Kuu kufuatia kupoteza sifa za kikanuni.

Taarifa ya TFF iliyotolewa leo ikiwa na saini ya Meneja Habari na Mawasiliano wa shirikisho hilo, Clifford Mario Ndimbo imezielekeza klabu zinazotumia Uwanja huo mwingine hadi hapo KMC Complex itakapofunguliwa tena baada ya mapungufu yaliyoibainika kufanyiwa marekebisho.

Mbali na wenye mali yao, KMC FC timu nyingine ambayo inatumia Uwanja huo rasmi kama wa nyumbani ni mabingwa wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara kwa miaka minne mfululizo, Yanga SC walioanza kuutumia msimu uliopita. 

WAFANYABIASHARA WAONYWA UPANDISHAJI BEI KIPINDI CHA RAMADHANI


Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba amewataka wafanyabiashara nchini kutowaumiza Watanzania kwa kupandisha bei za bidhaa hususani kipindi hiki cha kuelekea Mwezi Mtukufu wa Ramadhani pamoja na mfungo wa Kwaresma kwa kuwa nchi kwa sasa haina upungufu wa chakula.


Amesema licha ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) nchini kutangaza kuwepo kwa upungufu wa mvua katika maeneo mengi nchini lakini nchi inautoshelevu wa chakula hivyo hakuna sababu ya kupandisha bei za vyakula.


Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Januari 29, wakati akijibu swali la Nancy Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum katika kipindi cha Maswali ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu. 


Mbunge huyo alitaka kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha nchi inakuwa na utoshelevu wa chakula na kuzuia mfumuko wa bei kuelekea kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na Kwaresma.


“…Kwa sasa tuna chakula cha kutosha, mahitaji ya chakula cha akiba kwa nchi ni takribani tani 150,000 na sasa nchi ina zaidi ya tani 400,000 za akiba ya chakula rai ambayo niliitoa hata nilipokutana na wakuu wa mikoa ni kuendelea kuwahamasisha wananchi  kuzingatia ushauri wa aina ya mazao ya kupanda.”


Pia, Waziri Mkuu amewaelekeza Wakuu wa Mikoa yote nchini wawaelimishe wananchi kuendelea kutumia vizuri chakula walichonacho kutokana na tahadhari ya upungufu wa mvua iliyotolewa na TMA. 


Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameielekeza Wizara ya Afya kuzingatia viwango rasmi vya gharama za huduma na kuharakisha mpango wa kutunga sheria itakayoweka viwango vinavyofanana nchini kote, ili kuondoa hali ya baadhi ya maeneo kuwa na viwango tofauti.


Ametoa maelekezo hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani ambaye alitaka kupata kauli ya Serikali kuhusu viwango wanavyotozwa wananchi kama gharama ya kumuona daktari ambaye ni mwajiriwa na analipwa mshahara na Serikali.

Waziri Mkuu amesema kwa mujibu wa utaratibu wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, wananchi wanahimizwa kujiunga na mifumo ya bima ili kupunguza changamoto ya kuchangia gharama wanapohitaji huduma hospitalini.

Wednesday, January 28, 2026

DEPU AFUNGA MAWILI YANGA YAICHAPA DODOMA JIJI FC 3-1 MWENGE

 


MABINGWA watetezi, Young Africans, maarufu tu kama Yanga SC wametoka nyuma na kushinda mabao 3-1 dhidi ya Dodoma Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara uliochezwa jana usiku katika  Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao Yanga SC yamefungwa na washambuliaji wake wa kigeni, Muangola Laurindo Dilson Maria Aurélio ‘Depu’ mawili kwa penalti dakika ya 45’+2 na la kichwa dakika ya 60 na Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo dakika ya baada ya 66, na hiyo ilikuwa baada ya mshambuliaji mzawa, William Edgar kuanza kuifungia Dodoma Jiji FC dakika ya 41 akiwatoka kwa ustadi mkubwa mabeki wa Yanga kabla ya kumtungua kipa namba moja wa Mali, Djigui Diarra.


Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 22 katika mchezo  wa nane na kurejea kileleni ikiishushia nafasi ya pili JKT Tanzania yenye pointi 21 za mechi 12.


Kwa upande wao Dodoma Jiji baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi 10 za mechi 10 nafasi ya 11.


Baada ya mchezo huo Yanga wanakwenda Zanzibar kujiandaa na mchezo wa marudiano wa Kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri Jumamosi ya Januari 31 Uwanja wa New Amaan Complex.


Ikumbukwe Yanga ilichapwa 2-0 na wenyeji, Al Ahly Ijumaa ya Januari 23 mabao ya winga wa kushoto, Mahmoud Ahmed Ibrahim Hassan ‘Trézéguet’ moja kila kipindi, dakika ya 45’+3 na 75 Ijumaa usiku huu Uwanja wa Borg El Arab Jijini Alexandria, Misri.


Saturday, January 24, 2026

YANGA SC YATELEZA UGENINI, YACHAPWA 2-0 NA AHLY ALEXANDRIA

 


TIMU ya Yanga imeteleza ugenini baada ya kuchapwa mabao 2-0 na wenyeji, Al Ahly katika mchezo wa Kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika usiku huu Uwanja wa Borg El Arab Jijini Alexandria, Misri. 

Mabao yaliyoizamisha Yanga SC jana yote yamefungwa na winga wa kushoto, Mahmoud Ahmed Ibrahim Hassan ‘Trézéguet’ moja kila kipindi, dakika ya 45’+3 na 75.

Kwa ushindi huo, Al Ahly inafikisha pointi saba kufuatia ushindi wa 4-1 dhidi ya JS Kabylie ya Algeria nyumbani na sare ya 1-1 ugenini dhidi ya wenyeji, AS FAR Rabat nchini Morocco.

Yanga wanabaki na pointi zao nne walizovuna kwenye mechi mbili za awali wakishinda 1-0 nyumbani dhidi ya FAR Rabat na sare ya bila mabao, 0-0 ugenini na JS Kabylie.

Mchezo mwingine wa Kundi B leo, JS Kabylie watawakaribisha AS FAR Rabat Uwanja wa Hocine Aït Ahmed mjini Tizi Ouzou.

Yanga wanarejea nyumbani kuwasubiri Al Ahly kwa mchezo wa marudiano Januari 31 Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

𝗦𝗘𝗥𝗜𝗞𝗔𝗟𝗜 𝗬𝗔𝗢𝗠𝗕𝗪𝗔 𝗞𝗨𝗣𝗨𝗡𝗚𝗨𝗭𝗔 𝗭𝗔𝗜𝗗𝗜 𝗚𝗛𝗔𝗥𝗔𝗠𝗔 𝗭𝗔 𝗨𝗦𝗔𝗝𝗜𝗟𝗜 𝗪𝗔 𝗢𝗡𝗟𝗜𝗡𝗘 𝗠𝗘𝗗𝗜𝗔.

Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko (kulia) akimkabidhi Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, tuzo maalum kutoka YouTube baada ya BMG Media kufikisha zaidi ya wafuasi (subscribers) laki moja.

Serikali imeombwa kuendelea kupunguza gharama za usajili wa vyombo vya habari mtandaoni (Online Media) ili kuongeza fursa za ajira na kujiajiri kwa vijana nchini.

.
Ombi hilo limetolewa Jumamosi Januari 24, 2026 na Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, wakati wa hafla fupi ya kupokea tuzo maalum kutoka YouTube baada ya BMG Media kufikisha zaidi ya wafuasi (subscribers) laki moja.
.
Akizungumza katika hafla hiyo, Binagi amesema licha ya Serikali kupunguza gharama za usajili wa Online Media kutoka shilingi milioni moja hadi shilingi laki tano, bado kiwango hicho ni kikubwa kwa vijana wengi, hususan wahitimu wa taaluma ya uandishi wa habari na wabunifu wa maudhui, hivyo ameomba gharama hizo zishushwe hadi shilingi laki moja.
 

Ameeleza kuwa hatua hiyo itachochea vijana wengi zaidi kuanzisha vyombo vya habari mtandaoni na kujiajiri, jambo litakalosaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira nchini.
.
Aidha, Binagi amesema kuanzia mwaka 2026, watengeneza maudhui mtandaoni wameanza kukatwa asilimia tano ya mapato yao na kuwasilishwa serikalini, huku wakiendelea kulipa kodi nyingine mbalimbali, hali ambayo imewaongezea mzigo wa kodi na kusababisha kile alichokitaja kama kulipa kodi mara mbili.
.
 Kutokana na hilo, ameomba Serikali kulitafutia ufumbuzi suala hilo.
.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko, amesema mitandao ya kijamii imeendelea kuwa fursa muhimu kwa vijana katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira, hivyo amewahimiza vijana kutumia mitandao hiyo kwa njia sahihi na yenye tija.
.
Kuhusu gharama za usajili na masuala ya kodi, Soko amesema atayawasilisha kwa mamlaka husika kupitia vikao mbalimbali vya wadau wa habari ambavyo vinaendelea kufanyika kwa lengo la kuboresha na kukuza sekta ya habari nchini.
.
#YouTube 
#mwanza 
#Habari 
CC: @bmgonlinetv 

Wednesday, January 21, 2026

JKT YATANGAZA NASAFI MAFUNZO YA KUJITOLEA.

news
Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jeneral Hassan Mabena

 

JESHI la Kujenga Taifa (JKT) imetangaza nafasi za kujiunga na mafunzo ya kujitolea kwa vijana wa Tanzania Bara na visiwani kwa mwaka 2026 huku likisisitiza nafasi hizo ni bure kwa vijana watakaoomba.

Akizungumza katika Makao Makuu ya JKT, Chamwino Dodoma, Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jeneral Hassan Mabena, amesema usahili wa vijana hao utaanza Januari 26 mwaka huu katika mikoa yote ya bara na visiwani.

Amesema utaratibu wa vijana kuomba mafunzo hayo unaratibiwa chini ya ofisi za wakuu wa mikoa na wilaya na vijana wenye elimu ya kuanzia darasa la saba hadi chuo kikuu wanazo sifa za kuomba, akisema watakaochaguliwa wataanza kujiunga katika kambi mbalimbali za JKT kuanzia February 27 hadi Machi nne mwaka huu.

"Mafunzo haya ni bure wazazi au walezi wasikubali kurubuniwa kutoa fedha ili vijana wao wapate nafasi za kujiunga na mafunzo hayo," amesema Brigedia Jenerali Hassan Mabena.

Amezitaja kozi ambazo wanazipa kipaumbele ni zile za taaluma ya Stashahada ya Teknolojia ya Habari, Stashahada ya Mifumo ya Taarifa za Biashara, Stashahada ya Sayansi ya Kompyuta, Stashahada ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT), Stashahada ya Usalama Mtandaoni.

Nyingine ni Shahada ya Sayansi katika Sayansi ya Kompyuta, Shahada ya Sayansi katika Teknolojia ya Habari, Shahada ya Sayansi katika Uhandisi wa Kompyuta, Shahada ya Sayansi katika Teknolojia ya Habari za Biashara,Shahada ya Sayansi katika Usalama wa Mtandao na Forensics ya kidigitali.

"Nitoe wito kwa Watanzania wenye sifa waende kwenye vijiji kata,tarafa zao ili waweze kujiandikisha, nasisitiza  nafasi hizi haziiuzwi ni fursa iliyotolewa bure kwa Watanzania wote," amesema Brigedia Jenerali Mabena 

Mabena amesema Vijana watakaopewa kipaumbele kuchanguliwa ni waliosoma kozi za masulala ya Sayansi pia akawatahadharisha wazazi kuepuka matapeli.

MBOWE: MZEE MTEI HAKUWA NA SHARI NA MTU.

Mbowe: Mtei hakuwa na shari na mtu

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Freeman Mbowe, amesema Hayati Mzee Edwin Mtei (94), alikuwa ni mtu aliyejenga uhusiano mwema na watu wakati wote.

Mbowe ameeleza hayo Jana Jumanne Januari 20 jijini Arusha, wakati akizungumza na waandishi wa habari alipokuwa msibani.

Akisimulia namna alivyomfahamu Mzee Mtei, Mbowe, amesema hakuwa mtu wa shari, kila alikofanya kazi, alikuwa amejipanga na alikuwa hachagui rafiki ndani na nje ya chama.

Mtei, alifariki dunia usiku wa kuamkia Januari 19 mwaka huu, wakati akikimbizwa kupatiwa matibabu katika Hospitali  ya Selian Jijini Arusha, inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).

"Hakuwa mtu mwenye njaa, alikuwa ni mtu anayejiweza, akifanya siasa za mageuzi katika mazingira yale...misingi mikuu ambayo mzee huyu ametuachia ni sera. Tulikuwa na waasisi 12 wa CHADEMA." amesema Mbowe.

Mbowe amesema Mtei aliwasaidi kupata uzoefu ndani ya chama husuani masuala ya kifedha.

Amesema alikuwa na ujuzi mkubwa wa masuala ya kodi na sera pamoja na uzoefu mkubwa wa masuala ya kidiplomasia.


Wakati wa uhai wake, Hayati Edwin Mtei aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Kanda ya Afrika, Katibu

Mkuu wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC), Gavana wa kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Waziri wa Fedha wakati wa uongozi wa Hayati Julius Nyerere.

MWASISI WA SARAFU

Mbowe amesema: "Mzee Mtei, ndiye aliyekuwa mwasisi wa kwanza wa sarafu ya Tanzania, baada ya ile sarafu ya Afrika ya Mashariki baada ya sisi kuanzisha Benki Kuu ya Tanzania (BoT)".

KUUGUA

Mbowe amesema Mzee Mtei ameugua kwa muda mrefu na familia imepokea kwa uzito msiba huo kutokana na rekodi iliyotukuka, aliyoiweka ndani ya chama na Taifa.

Kwa mujibu wa Mbowe, Mzee Mtei alikuwa akipatiwa matibabu katika hospitali mbalimbali, ikiwemo Hospitali ya Nairobi-Kenya, Dar es Salaam na maeneo mengine kadha wa kadha.

Mbowe alisema: "Natambua CHADEMA  wametuma ujumbe katika msiba huu ili kuungana na familia kwa sababu mzee alikuwa ni mwasisi wa chama chetu. Ni kiongozi ambaye bado tulikuwa tunamuheshimu sana katika njia mbalimbali, kwa sababu misingi yote ya CHADEMA huyu ndiye aliyeianzisha"

ASKOFU ROSEMARY AMPONGEZA DKT. BITEKO

 

Na, Ernest Magashi

Askofu wa Kanisa la Ufunuo Jimbo la Geita, Rosemary Mashauri Bendera, amempongeza Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, kwa juhudi zake za kuwaletea wananchi maendeleo, huku akiwahimiza wananchi kushirikiana kwa pamoja katika kuijenga na kuendeleza Wilaya ya Bukombe.Pongezi hizo zilitolewa Jumapili ya Tarehe 19 Jan 2026 wakati wa ibada ya shukrani kwa Mungu baada ya kuvuka mwaka 2025 na kuukaribisha mwaka 2026, iliyofanyika katika Kanisa la Ufunuo mjini Ushirombo, wilayani Bukombe.Katika ibada hiyo, Askofu Rosemary aliwaomba waumini kuendelea kuiombea Serikali na viongozi wake ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. Alitaja baadhi ya miradi ya maendeleo inayoendelea kutekelezwa wilayani humo, ikiwemo ujenzi wa soko la kisasa, stendi ya mabasi na uwanja wa mpira wa miguu, kama vielelezo vya dhamira ya Serikali katika kuboresha maisha ya wananchi.Aidha, Askofu Rosemary aliwatunuku wachungaji 12 daraja la uchungaji kamili na kuwakabidhi vifaa vya kazi, akiwahimiza kumtumikia Mungu kwa uaminifu kwa kushirikiana na Serikali pamoja na jamii zinazowazunguka katika maeneo watakayopangiwa.Vilevile, aliwasisitiza wazazi na walezi kuwekeza katika elimu ya watoto wao kwa kuhakikisha watoto waliofikia umri wa kuandikishwa darasa la awali na kidato cha kwanza wanaandikishwa na kuhudhuria shule, sambamba na jitihada za Serikali za kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya elimu.Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, katika ziara zake za kikazi hivi karibuni amekuwa akihamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika miradi ya maendeleo kwa kuchangia nguvu kazi, hususan katika ujenzi wa zahanati na shule.Dkt. Biteko amesema Serikali inatarajia kukarabati shule 23 pamoja na miundombinu yake, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuboresha huduma za elimu wilayani Bukombe, huku akisisitiza kuwa jukumu la wazazi na walezi ni kuhakikisha watoto wote wanapelekwa shule kwa wakati.

Monday, January 19, 2026

NI SENEGAL BINGWA AFCON, MOROCCO YALALA NYUMBANI 1-0

 

TIMU ya Senegal ‘Simba wa Teranga’ imefanikiwa kutwaa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Morocco usiku huu Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat.


Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee, kiungo wa ulinzi wa Villarreal ya Hispania, Pape Alassane Gueye dakika ya 94 katika mchezo uliodumu kwa dakika 120.


Hilo linakuwa taji la pili la AFCON kwa Senegal baada ya awali kulibeba mwaka 2021 nchini Cameroon Waliofunga Misri kwa penalti 4-2 baada ya sare ya 0-0 Uwanja wa Olembe Yaoundé.


Nyota wa Senegal, Sadio Mane wa Senegal amechaguliwa Mchezaji Bora wa michuano hiyo (MVP), Mfungaji Bora Brahim Diaz wa Morocco mabao matano, Kipa Bora Yassine Bounou wa Morocco na Timu iliyoonyesha Mchezo wa Kiungwana, Morocco. 

Friday, January 16, 2026

YANGA SC YAACHANA NA KOCHA MSAIDIZI, YAAJIRI MWINGINE NAYE MRENO

 


KLABU ya Yanga imempa mkono wa kwaheri Kocha wake Maaidizi, Filipe Duarte da Silva Pedro baada ya  miezi miwili na ushei tangu awasili na nafasi yake inachukuliwa na Mreno mwingine, Marques Pereira Da Silva.

Filipe Pedro aliwasili Yanga kwa pamoja na Kocha Mkuu, Mreno mwenzake, Pedro Valdemar Soares Gonçalves Oktoba 25 mwaka jana.

Ni uamuzi wa ghafla unaokuja siku chache baada ya Yanga kutwaa Kombe la Mapinduzi wakiiifuga Azam FC kwa penalti 5-4 kufuatia sare ya 0-0 Jumanne Januari 13 Uwanja wa Gombani, Pemba.

Taarifa mbili za Yanga zimeambatana jioni hii — kuondoka kwa Pedro na ujio wa Da Silva ambaye ni Msaidizi wa pili pamoja na Mmalawi, Patrick Mabedi ambaye yupo hata kabla ya ujio wa Kocha Mkuu, Pedro Gonçalves.  
Da Silva

TANZANIA YAVUKA DOLA BILIONI 4 ZA UTALII; YAIPIGA CHINI "DIPLOMASIA YA KIKI" YA MAJIRANI

 

Wakati Kanda ya Afrika Mashariki ikishuhudia ushindani mkali wa kutafuta umaarufu kupitia influencers (washawishi) wa mitandaoni, Tanzania imesisitiza kuwa mafanikio yake katika sekta ya utalii yanatokana na uhalisia na rasilimali zake zisizohitaji 'kupambwa mno' na gharama za serikali.

Kumekuwa na mjadala baada ya ziara ya YouTuber maarufu IShowSpeed nchi jirani,  kuwa ziara hiyo ilikuwa ya kulazimisha ili kupandisha sifa za utalii wa majirani. 

Pamoja na kelele zao za mtandaoni  takwimu za Tanzania zinaonesha kutomhitaji  IshowSpeed katika kutangaza utalii wake.

"Hatuogopi mbinu za kutafuta umaarufu, kwani ukweli wa mazingira yetu, kutoka Zanzibar hadi Serengeti, hauwezi kununuliwa kwa helikopta ya kukodi," alimalizia mchambuzi mmoja wa masuala ya utalii.

Hata hivyo, Rais Samia Suluhu Hassan, katika hotuba yake ya Sherry Party, ametoa jibu la kishindo kupitia takwimu.

 "Tanzania haihitaji kutengeneza hadithi za kufikirika," alisema Rais Samia huku akionyesha kuwa mapato ya utalii yamefikia Dola bilioni 4 mwaka 2025. Huku majirani wakihaha kutafuta umaarufu kupitia TikTok na YouTube, Tanzania imejikita katika kuboresha miundombinu kama SGR na viwanja vya ndege ili kumfanya mtalii wa kawaida awe balozi wa nchi.

Kilimanjaro ni Moja, na Ipo Tanzania 

Ni kama akijibu hoja za baadhi ya nchi jirani kujaribu kujimilikisha alama za Tanzania kama Mlima Kilimanjaro na utamaduni wa Kimaasai, Rais amesisitiza kuwa Dira ya 2050 italinda rasilimali hizo kama mali ya taifa. "Tunajiuza kwa kile tulichonacho. Utulivu wetu na asili yetu ndiyo sumaku kubwa zaidi duniani," aliongeza.

Mkakati wa 'Royal Tour' Unadunda 

Wakati ziara za mastaa wa mtandaoni kama IShowSpeed zikiwa na maisha mafupi (viral for a day), mkakati wa Tanzania kupitia The Royal Tour unaendelea kuleta watalii wa kudumu na wawekezaji wakubwa. 

UCHAGUZI UGANDA 2026: MUSEVENI KINARA WA KURA ZILIZOHESABIWA HADI SASA

 


Uchaguzi Uganda 2026: Museveni achukua uongozi wa mapema wa kura zilizohesabiwa kufikia sasa

Jaji Simon Byabakama, mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Uganda amesema matokeo hayo yanazingatia vituo 133 vya kupiga kura na yanawakilisha asilimia 0.26 ya jumla ya kura zilizopigwa.

Wakati huo huo Rais Museveni amewaonya raia wanaopanga kuandamana siku ya Jumanne akisema kwamba 'wanacheza na moto'.


Mgongano unaokuja  baada ya wimbi la maandamano ya kupingana na serikali yaliyoigonga nchi ya jirani ya Kenya, ambapo watu wasiopunguwa 50 walipoteza maisha katika mapambano na vyombo vya usalama, kulingana na takwimu zilizo chapishwa na Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu.

Rais Yoweri Museveni, 79, aliyekuwa akitawala taifa la Uganda kwa karibu miongo minne kwa mkono wa chuma, alisema katika hotuba iliyorushwa hewani Jumamosi kuwa maandamano ya kupambana na ufisadi hayataruhusiwa.

“Ana haki gani… unao nayo wa kuleta tabia ya maangamizi? … Tunaanza kuzalisha chakula cha bei rahisi, watu wengine katika sehemu nyingine za dunia wanaachu (kuwa na njaa)… wewe unataka kutulazimisha kuvuruga. Unacheza na moto kwa sababu hatuwezi kukuruhusu kutuvuruga,” Museveni aliweka maneno yake katika hotuba iliyotumia saa tatu.

Wengi wa vijana wa Uganda wanasema kupitia mitandao ya kijamii kuwa wanapanga kuendelea na maandamano hadi ofisi za bunge la taifa, licha ya jeshi la polisi kukataa kutoa vibali vya maandamano.

Jeshi la Polisi wa Uganda liliutanabaisha umma kwa maandamano yaliyopangwa kuwa “yanayoweza kusababisha vurugu” katika taarifa ya Jumatatu, likionya kwamba “hawatahimili tabia ya utulivu mbovu.”

Baadhi ya waandamanaji vijana waliodhamiria kujiunga na maandamano hayo ya Jumanne wameanza kutupia picha zao kwenye mitandao ya kijamii, wakihanikiza  raia wenzao nao wafanye vivyo hivyo ili wapate kuwataja wakirudi salama nyumbani. 

Na hata ikitokea wakapotea basi ijulikane ni kipi kiliwapoteza.



HILI HAPA - BONGE MOJA LA RAGGA LA KUFUNGULIA MWAKA 2026

Thursday, January 15, 2026

YANGA SC YATAMBULISHA STRAIKA MUANGOLA ALIKUWA ANACHEZA ULAYA

 

𝙔𝙖𝙣𝙜𝙖 𝙎𝙘 imemtambulisha mshambuliaji wa Kimataifa wa Angola Lauren do Dilson Maria 'Depu' kuwa mchezaji wake mpya akitokea Radomiak Radom ya Poland.

Je, Depu ana rekodi ya kuthibitisha uwezo wa kufunga mabao?
Depu ana uzoefu mkubwa wa kimataifa akiwa ni mshambuliaji wa timu ya taifa ya Angola, ambapo amefunga mabao mengi kwa nchi yake takwimu zinaonyesha ana takribani 15 mabao katika michezo 18 za kimataifa kwa Angola. 

Pia, katika mashindano ya COSAFA Cup, Depu amekuwa mfungaji bora na mchezaji muhimu sana, akisaidia Angola kushinda mataji na kupata tuzo za Golden Boot. 

Confédération Africaine de Football
Kwa timu za vilabu (club), rekodi yake ya mabao haionekani kuwa ya juu sana katika baadhi ya ligi za Ulaya kama Poland kwa mfano katika Ekstraklasa mwaka wa 2025/26, Depu aliweza kufunga mchezo mmoja kwenye mechi tisa akiwa Radomiak Radom. 

Transfer Feed
Hitimisho: Yanga SC imepata mshambuliaji mwenye uzoefu wa kimataifa na rekodi nzuri ya kufunga mabao kwa timu yake ya taifa, hasa katika mashindano ya COSAFA Cup. Hata hivyo, kiwango chake cha mabao katika vilabu vya Ulaya hakikuwa cha juu sana hivi karibuni hivyo mafanikio yake kama mwarobaini wa uhakika wa mabao kwa Yanga yatategemea jinsi atakavyoweza kuendana na ligi ya Tanzania na uwezo wa benchi la ufundi kulifanya afanikiwe ipasavyo