ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, March 25, 2026

NI RASMI SASA MO SALAH ATAONDOKA RASMI LIVERPOOL

  Mohamed Salah poses with the Premier League trophy

Mohamed Salah ataondoka Liverpool msimu huu akiwa miongoni mwa wachezaji bora kabisa kuwakilisha klabu hiyo na kung'ara katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL)


Takwimu za Salah zinaonyesha mafanikio yake kwa uwazi, lakini zaidi ya hiyo, kuna hadithi kubwa nyuma ya namba hizo. Mashabiki zake pale Anfield, ambao wanamuita 'Egyptian King' (Mfalme wa Misri), wanakumbuka kila goli lake alilofunga na kila mchango wake kwenye klabu hiyo, jambo ambalo limeifanya historia yake kuwa ya kipekee.

Salah alijiunga na Liverpool kutoka AS Roma mnamo Juni 23, 2017 kwa ada ya pauni milioni 34, kiasi kinachoonekana sasa kama fedha ndogo ikilinganishwa na mafanikio aliyoyapata baada ya kuhamia Liverpool.


Kama Kevin de Bruyne, Salah alikuwa Chelsea awali lakini hakufanya alichotarajiwa, akifunga mabao mawili tu katika mechi 19, akianza katika michezo 10 tu.

Awali aliikataa Liverpool pale alipoondoka Basel na kujiunga na Chelsea Januari 2014. Kumbukumbu yake ya kwanza Anfield ilikuwa pale alipoanza kwenye jezi ya Chelsea katika ushindi wa 2-0 mnamo Aprili 2014, mchezo unaokumbukwa kwa kosa la Steven Gerrard kosa lililozima ndoto za ubingwa uliokwenda Manchester City.

Hata hivyo, tangu alipojiunga rasmi na Liverpool, Salah ameacha kumbukumbu zisizosahaulika, akisaidia klabu hiyo kushinda Ligi ya Mabingwa Ulaya, mataji mawili ya Ligi Kuu, Kombe la FA, EFL Cup sasa Kombe la Carabao, UEFA Super Cup na Kombe la dunia la vilabu, akiboresha historia ya Anfield.


Safari ya maana ya Salah kutoka Basel mpaka Liverpool

Salah alianza safari yake yake polepole Basel, ambapo kocha Murat Yakin aligusia kwamba atakuwa mchezaji nyota pale alipoifunga Tottenham katika robo fainali ya Europa League 2013.


"Kama Mohamed ataendelea kufunga mabao zaidi, hatasalia hapa," Yakin alisema. Na kweli hakusalia, akaendelea kuwa kwenye kiwango bora. Baada ya kuondoka Chelsea, baadaye kwa mkopo Fiorentina kisha AS Roma, Salah alijitengenezea jina kubwa kabla ya kuwasili Anfield, na hata Klopp huenda hakuwa amejua anamchukua mtu wa mwenye kiwango gani hasa.


Goli lake la kwanza akiwa na Liverpool lilikuwa katika sare ya 3-3 dhidi ya Watford. Tangu hapo, hakukoma kufunga. Salah ameifungia Liverpool jumla ya mabao 255 katika mechi 435, akishika nafasi ya tatu kwenye orodha ya wafungaji bora wa klabu hiyo, nyuma ya Ian Rush na Roger Hunt. Katika Ligi Kuu, amecheza mechi 310, akifunga mabao 189 na kutoa pasi za mabao 92, akichangia jumla ya mabao 281, mchango mkubwa zaidi kwa klabu moja katika historia ya Ligi Kuu.


Salah alikuwa mchezaji mwenye ubinafsi wa kipekee lakini pia alichangia kikamilifu kwa timu. Msimu wake wa kwanza ulikuwa mzuri sana, akifunga mabao 44 na kutoa pasi 14 katika mechi 52. Hata hivyo, aliumia kwenye fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Real Madrid, akicheza dakika 31 tu. Mwaka mmoja baadaye, alirekebisha hilo pale Liverpool iliposhinda 2-0 dhidi ya Tottenham, akifunga penati ya mapema.


Salah alikuwa sehemu ya safu bora ushambuliaji akiwa na Sadio Mane na Roberto Firmino, wakiwa na kasi, mbinu na ufanisi wa timu. Alishambulia kutoka upande wa kulia, Mane upande wa kushoto, na Firmino akibadilisha nafasi akicheza kama shambuliaji ama nyuma ya mshambuliaji, ambaye ufundi wake ulisaidia kuboresha viwango vya kila mmoja.


Kila msimu, Salah aliendelea kuwa na uthabiti mkubwa. Katika mechi 310 za Ligi Kuu, kiwango cha ushindi wa Liverpool kilikuwa 63.9%, na katika jumla ya mechi 435, kilikuwa 62.7%. Hii inaonyesha miaka ya heshima kwa klabu na mchezaji.


Hata hivyo mwishoni mwa zama zake hizi, kabla ya michuano ya AFCON, Salah alikabiliana na changamoto ya kocha mpya Arne Slot, baada ya Klopp kuondoka. Kukawa na malumbano kwa sababu ya kuwekwa benchi, lakini mara zote alithibitisha ni bora alipopata nafasi. Baada ya msimu huu wa mwisho, Salah ataondoka akiwa amejenga urithi usioweza kuharibiwa.


Hakuna anayekinzana na ukweli kwamba Mohamed Salah amekuwa miongoni mwa wachezaji bora kabisa kuwahi kuvaa jezi nyekundu ya Liverpool.

MWAKILISHI JIMBO LA CHWAKA AWAKOMBOA WANAFUNZI KWA KUTOA MSAADA WA VIFAA VYA ELIMU

 


NA MWANDISHI WETU, CHWAKA

 
Katika kuboresha sekta ya elimu  Mwakilishi wa Jimbo la Chwaka Mhe. Issa Gavu leo machi 25 amekabidhi vitabu kwa ajili ya kujisomea pamoja na vifaa mbali mbali vya elimu lengo ikiw ni kuleta mabadiliko katika suala zima la kukuza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa skuli  zote la Jimbo hilo.

Akikabidhi msaada huo Mwakilishi wa Jimbo hilo la Chwaka Mhe Gavu amebainisha kwamba wameamua kutoa msaada wa vifaaa mbali mbali kwa wanafunzi hao ikiwemo kompyuta mapakato,Printer, vitabu m,bali mbalin pamoja na mashine ya kubuluzia karatasi (Photocopy mashine)  vyote vikiwa vimegharimu kiasi cha shilingi milioni 12 msaada ambao umetolewa kutoka kwa marafiki wema kwa watu wa Jimbo la Chwaka.


"Leo tumejumuika hapa kwa ajili ya kuweza kukabidhi vifaa mbali mbali kwa wanafunzi ambao wanasoma katika Jimbo la Chwaka na katika siku ya leo tumeweza kukabidhi vifaa mbali mbali ikiwemo vitabu kwa ajili ya kujisomea wanafunzi, Photocopy mashine, pamoja Printer ambavyo vitaweza kuwa ni mkombozi mkubwa kwa wanafunzi kuweza kuongeza kasi ya ufaulu katika masomo yao,"amebainisha Mhe. Gavu.

 Aidha katika tukio hilo pia Mhe. Gavu kwa kushirukiana na marafiki zake wa Jimbo hilo pia wameweza kutoa msaada wa  kugawa  mabati katiika  Skuli ya Mrembo Uroa, washing machine, tanki  la maji na mipira Jendele, pamoja na mafeni na vifaa vya umeme kwa Kituo cha Afya Cheju.


Mhe  amesema  kwamba wameamua kutoa misaada hiyo katika nyanja mbali mbali ikiwa ni moja ya hatua ya kuweza  kuimarisha suala la  elimu kwa wanafunzi  pamoja na kuboresha afya kwa jamii ambayo inawazunguka hasa katika Jimbo la Chwaka na kuwasihi wanafunzi waweze kusoma kwa bidii lengo ikiwa ni kupata na kuongeza maharifa  ambayo yatawasaidia katika siku za usoni.

AUA NA KUJERUHI KISA USHABIKI WA SIMBA NA YANGA

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbrod Mutafungwa.


Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linamtafuta kijana mmoja (jina limehifadhiwa) kwa tuhuma za kumuua Abel Mganga Mazuri (25), mkazi wa Nyamahengo wilayani Kwimba, kwa kumchoma na kitu chenye ncha kali kifuani, pamoja na kuwajeruhi watu wawili.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Machi 25, 2026 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbrod Mutafungwa, tukio hilo lilitokea Machi 24, 2026 majira ya saa 5:30 usiku katika kitongoji cha Nyamahengo, kata ya Sumve.

Inaelezwa kuwa mtuhumiwa alifanya shambulio hilo wakati akiwa na wenzake wakinywa pombe na kuangalia mpira katika banda la maonesho ya mpira, ambapo ugomvi ulizuka kutokana na ushabiki wa timu za Simba SC na Yanga SC.

Kamanda Mutafungwa amesema mtuhumiwa aliwashambulia watu watatu kwa kutumia kitu chenye ncha kali kufuatia mabishano makali yaliyochochewa na ushabiki huo, na kusababisha kifo cha Abel Mazuri.

Waliopata majeraha katika tukio hilo wametajwa kuwa ni Semen Juma Cherehani (26) na Ndubu Mkoi Chagula (26), ambao walijeruhiwa katika maeneo ya mikononi.

Jeshi la Polisi limeeleza kuwa majeruhi wote wamepatiwa fomu za matibabu (PF3) na wanaendelea kupatiwa huduma katika Hospitali Teule ya Sumve, huku hali zao zikiripotiwa kuimarika.

Aidha, Polisi wanaendelea na msako mkali wa kumkamata mtuhumiwa ili afikishwe katika vyombo vya sheria, huku wakitoa wito kwa wananchi kuepuka vurugu zinazotokana na ushabiki wa mpira uliopitiliza mipaka.

Tuesday, March 24, 2026

KAMANDA MURILO AONYA POLISI KUINGILIA MAJUKUMU YA TRA

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro (anayeongoza msafara)

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Jumanne Muliro, amewataka askari wa Jeshi la Polisi kuacha mara moja kuingilia majukumu ya mamlaka nyingine, ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kufuatia malalamiko ya wafanyabiashara wa Kariakoo kuhusu kunyanyaswa.

Akizungumza wakati wa ziara yake katika eneo la Kariakoo, Kamanda Murilo alikutana na wafanyabiashara wa Jumuiya ya Raha Square kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto za kiusalama. Alisisitiza kuwa si jukumu la polisi kukagua mizigo ya wafanyabiashara wala kushughulikia masuala ya kodi, na kuonya kuwa askari watakaokiuka maelekezo hayo watachukuliwa hatua kali.

Awali, wafanyabiashara walilalamikia tabia ya baadhi ya askari kusimamisha mizigo yao katika makutano ya barabara na kukagua risiti za biashara, wakieleza kuwa hali hiyo imekuwa kero na chanzo cha usumbufu mkubwa.

Akizungumza kwa niaba ya wafanyabiashara, Mwenyekiti wa Kijiwe cha Raha Square, Rweyemamu Erasto, alisema licha ya changamoto hiyo, pia wanakabiliwa na hali duni ya usalama hasa nyakati za usiku wanapofunga biashara zao. Alibainisha kuwa baadhi ya barabara bado hazijafunguliwa ipasavyo, hali inayochangia vitendo vya uporaji, huku biashara zinazofanyika barabarani zikiziba njia na kuongeza hatari ya ajali.

Aidha, wafanyabiashara walieleza wasiwasi wao kuhusu ongezeko la watoto wa mitaani wanaozagaa nyakati za usiku pamoja na uwepo wa watu wasiokuwa na utambulisho unaoeleweka, wakidai hali hiyo inahatarisha usalama wao na mali zao.

Katika mapendekezo yao, waliomba kufunguliwa kwa barabara zote za Kariakoo, kuondolewa kwa biashara zisizo rasmi barabarani, pamoja na kufungwa kwa mifumo ya kamera za ulinzi (CCTV) ili kusaidia kudhibiti uhalifu.

Akijibu hoja hizo, Kamanda Murilo amesema Jeshi la Polisi linaendelea kushirikiana na mamlaka mbalimbali kuhakikisha eneo la Kariakoo linakuwa salama. Aliahidi kufanyia kazi changamoto zote zilizotolewa na wafanyabiashara.

Kuhusu tatizo la watoto wa mitaani, alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na taasisi husika inaendelea kutafuta suluhisho la kudumu kwa kuchunguza chanzo cha tatizo hilo. Pia alionya juu ya matumizi holela ya bajaji na maguta katika barabara kuu, akisema hatua madhubuti zitachukuliwa kudhibiti hali hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya usalama.

Kamanda Murilo amesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia ya kamera za ulinzi, akibainisha kuwa zimekuwa msaada mkubwa katika kubaini na kudhibiti uhalifu.

Amemalizia kwa kuwahakikishia wafanyabiashara wa Kariakoo kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kutoa ulinzi wa saa 24 ili kuhakikisha usalama wa watu na mali zao.

TRA PWANI YAWAKUMBUKA WATOTO YATIMA NA MAKUNDI MAALUMU KWENYE TUKIO MAALUM LA IFTAR

 


NA VICTOR MASANGU, PWANI

Mamlaka ya mapato (TRA) Mkoa wa Pwani katika kurudisha fadhila kwa jamii imeamua kuandaa Iftar maalumu kwa ajili ya kufuturisha makundi mbali mbali ikiwemo watoto yatima, viongozi wa madhehebu ya dini, viongozi wa serikali ikiwa pamoja na wananchi kutoka maeneo ya Mkoa wa Pwani.

Tukio hilo  maalumu la Iftar limefanyika katika viwanja vya nje ya Ofisi ya TRA na kuongozwa na Sheikh wa Mkoa wa Pwani Khamis Mtupa pamoja na kuhudhuliwa na viongozi wengine wa dini pamoja na watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu kutoka kituo cha Fadhila kilichopo kata ya Misigusugu Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha.

Katika  tuki hilo Sheikh wa Mkoa wa Pwani Khamis Mtupa ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi hakusita kuupongeza kwa dhati uongozi mzima wa TRA Mkoa wa Pwani kwa kuamua kurudish fadhila kwa jamii na kukusanya makundi mbali mbali ikiwemo watoto yatima na kula nao chakula cha jioni ikiwa ni moja na nguzo muhimu sana hasa katika kipindi hiki  cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

"Kwa upande wangu mimi kipekee nipende kuchukua  fursa hii kuwashukuru kwa dhati uongozi mzima wa TRA pamoja na meneja wake kwa kuona umuhimu mkubwa wa kutukutanisha siku ya leo katika hili tuko la Iftari kwa kweli mmefanya jambo la msingi sana na kingine nimependa mmekusanya makundi tofauti ikiwemo na watoto yatima ambao tumejumuika nao hapa katika tukio hilo na Mungu awabariki sana na muendelee na moyo huu wa kujitolea,"amebainisha Sheikh Mtupa.

Pia katika hatua  nyingine amebaainisha kwamba katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadani taasisis na watu mbali mbali wanapaswa kufanya matendo ya huruma kwa wahitaji ikiwemo suala la kuwafuturisha watu    wenye uhitaji na kuweza kutoa misaada mbaali mbali ambayo itaweza kuwasaidia walengwa na kwamba zoezi hilo liwe endelevu ikiwemo kusaidia jamii.

Kadhalika Sheikh Mtupa ameipongeza TRA Mkoa wa Pwani kwa kuweka mikakati madhubuti ambayo imeweza kusaidia kwa kiassi kikubwa katika suala zima la kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mapato ambayo yanapelekea kuleta mabadiliko makubwa katika maendeleo kwa wananchi.

Kwa   upande wake Meneja wa mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani Masawa Masawa amesema kwamba wameamua kufanya tukio la Iftar hiiyo na kuwakutanisha makundi mbali mbali ikiwa ni moja ya kurudisha fadhila kwa jamii pamoja na kukutana na watoto yatima na kula nao chakula cha jioni.

Meneja huyo amesema kwamba lengo kubwa la TRA Mkoa wa Pwani ni kuendelea kushirikiana begaa kwa bega na jamii katika mambo mbali mbali ikiwemo kukutana kwa pamoja na kubadilishanaa mawazo pamoja naa kula cha jioni kwani ni moja ya kuongeza wigo mpana ya katika kujenga mahusiano mazuri kwa jamii.

Nao baadhi ya watoto yatima ambao wamehudhulia      katika tukio hilo  wamesema wamefurahishwa na uongozi  mzima wa TRA kwa kuweza kuwakumbuka katika kuwakutanisha katika Iftar hiyo na kusema kwamba wamejisikia furaha na amani ya kukutana na jamii nyingine.

Monday, March 23, 2026

MANCHESTER CITY YAICHAPA ARSENAL 2-0 NA KUTWAA CAFRABAO CUP

 

SHEREHE: Manchester City WAKINYANYUA JUU KOMBE LA Carabao BAADA YA KUITANDIKA Arsenal KATIKA UWANJA WA Wembley

TIMU ya Manchester City FC jana ilifanikiwa kutwaa Kombe la Ligi England baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Arsenal katika mchezo wa Fainali uliofanyika Jumapili ya terehe 22 Machi 2026 Uwanja wa Wembley Jijini London.

Mabao yaliyoipa Manchester City taji la ya Carabao Cup yalifungwa na beki chipukizi wa kushoto wa umri wa miaka 21 ambaye pia hucheza nafasi za kiungo, Nico O'Reilly yote mawili dakika ya 60 na 64.

Hilo linakuwa taji la tisa la Carabao kwa Manchester City baada ya awali kulibeba katika misimu ya 1970, 1976, 2014, 2016, 2018, 2019, 2020 na 2021.

Mara ya mwisho Arsenal kutwaa taji iliuwa ni Agosti mwaka 2020 walipobeba Kombe la FA Cup chini ya kocha wa sasa, Mikel Arteta kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Chelsea kwenye Fainali hapo hapo Uwanja wa Wembley.

ZAMALEK HIYOOoo NUSU FANALI KOMBE LA SHIRIKISHO AFRIKA

 


TIMU ya Zamalek SC ya Misri imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya ushindi wa mabao 2-1 na AS Otoho d'Oyo ya Kongo-Brazzaville katika mchezo wa marudiano wa Robo Fainali jana Uwanja wa Cairo International Jijini Cairo nchini Misri.

Kwa matoke ohayo, Zamalek inakwenda Nusu Fainali kwa ushindi wa jumla wa 3-2 kufuatia sare ya kufungana bao 1-1 katika mchezo wa kwanza Machi 14 Uwanja wa Alphonse Massamba-Débat Jijini Brazzaville.

Mambo hayakuwa mazuri kwa timu za Wydad Athletic ya Morocco na AS Maniema Union ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ambazo zote zilitolewa kwa mabao ya ugenini zote.

Wydad Athletic ilitoa sare ya kufungana mabao 2-2 na Olympic Club de Safi, zote za Morocco jana Uwanja wa Mfalme Mohammed wa Tano Jijini Casablanca.
Kwa matokeo hayo, Olympic Club de Safi inakwenda Nusu Fainali kwa faida ya mabao ya ugenini katika sare hiyo ya jumla ya 3-3 baada ya awali timu hizo kufungana bao 1-1 kwenye mchezo wa kwanza Machi 16 Uwanja wa El Massira mjini Safi.

Nayo AS Maniema Union ilichapwa 1-0 USM Alger bao pekee la kiungo Brahim Benzaza dakika ya 30 Uwanja wa Julai 5, 1962 Jijini Algiers nchini Algeria.

USM Alger inakwenda Nusu Fainali kwa faida ya mabao ya ugenini katika sare hiyo ya jumla ya 2-2 kufuatia kufungwa 2-1 na AS Maniema Union kwenye mchezo wa kwanza wa Robo Fainali Machi 15 Uwanja wa TP Mazembe Jijini Lubumbashi.
Mechi za kwanza za Nusu Fainali zitachezwa Aprili 10 na marudano Aprili 17, Zamalek ikimenyana na CR Belouizdad iliyoitoa Al Masry ya Misri pia na USM Alger ikicheza na Olympic Safi.

MV LIEMBA MELI YENYE HISTORIA DUNIANI ZAIDI YA MIAKA 100 YAKARABATIWA KWAAJILI YA USAFIRI NA UTALII

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

Meli kongwe zaidi inayobaki duniani na bado inaendelea kutoa huduma, MV Liemba, yenye umri wa zaidi ya miaka 100, inaendelea kufanyiwa ukarabati mkubwa unaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 32. Uamuzi wa kuikarabati umetokana na tathmini iliyoonesha kuwa kujenga meli mpya kungehitaji zaidi ya shilingi bilioni 80. Kutokana na umuhimu wake wa kihistoria na kiuchumi, Serikali ya Tanzania imechagua kuirudishia uhai meli hiyo ili iendelee kutumika katika usafiri na usafirishaji katika Ziwa Tanganyika, huku pia ikibaki kuwa kivutio muhimu cha historia na utalii. Akizungumza kuhusu umuhimu wa meli hiyo mbele ya vyombo vya habari jijini Mwanza, Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa amesema kuwa MV Liemba ni hazina ya kipekee duniani, akibainisha kuwa watu kutoka nchi mbalimbali na hata mabara tofauti husafiri kuja kuiona. "Watu wanasafiri kutoka nchi za mbali na mabara tofauti kuja tu kuiangalia meli hii ambayo, licha ya kuwa na umri wa zaidi ya karne moja, bado inaendelea kutoa huduma," amesema. #mvliemba #samiasuluhuhassan #GersonMsigwa #tanzania

SERIKALI YAWEKEZA ZAIDI YA TRILIONI 1 KUBORESHA USAFIRI WA MAJINI

NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

Serikali ya awamu ya Sita imewekeza zaidi ya shilingi trilioni moja katika kuimarisha sekta ya usafiri wa majini nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo pamoja na kukuza uchumi wa Taifa.


Hayo yameelezwa na Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa wakati akizungumza na vyombo vya habari jijini Mwanza, ambapo amesema uwekezaji huo umehusisha ununuzi wa meli mpya, ukarabati wa meli zilizopo pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya bandari katika maziwa makuu na ukanda wa Bahari ya Hindi.

Amesema hatua hizo zinalenga kuongeza usalama wa usafiri majini, kurahisisha usafirishaji wa mizigo na abiria, pamoja na kuimarisha biashara kati ya Tanzania na nchi jirani.

Msigwa amesema miongoni mwa mafanikio ya uwekezaji huo ni kuanza kwa huduma za meli ya MV Mwanza, ambayo ina uwezo wa kubeba abiria 1,200, tani 400 za mizigo pamoja na magari makubwa matatu na magari madogo 20.


Ameeleza kuwa Serikali pia inaendelea na ukarabati wa meli ya MV Umoja pamoja na meli ya MT Ukerewe, huku ikiendelea na ujenzi wa meli mpya ya mizigo yenye uwezo wa kubeba tani 3,000 katika Ziwa Victoria.


Katika Ziwa Tanganyika, Serikali inaendelea na ukarabati wa meli ya MV Liemba ili kuboresha huduma za usafiri kwa wakazi wa maeneo ya mwambao na nchi jirani.

Mbali na miradi hiyo, Serikali pia inaendelea kuboresha bandari mbalimbali katika maziwa makuu, kujenga bandari mpya pamoja na kuimarisha mifumo ya uokoaji majini kwa kujenga vituo vya utafutaji na uokoaji na kununua boti maalum za uokoaji.


Msigwa amesema hatua hizo zinaonyesha dhamira ya Serikali ya kuifanya sekta ya usafiri wa majini kuwa ya kisasa, salama na yenye mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Taifa.




Sunday, March 22, 2026

UWANJA MKUBWA NA MRADI WA MICHEZO WAPANGWA KUJENGWA JIJINI MWANZA

NA ALBERT G.SENGO/MWANZA 

Serikali imetangaza mpango wa kujenga eneo changamani la michezo litakalokuwa kubwa zaidi nchini, litakalojengwa jijini Mwanza.

Akizungumza hii leo na waandishi wa habari, katika ukumbi wa juu ndani ya MV New Mwanza, Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa amesema Serikali imeomba takribani hekari elfu moja katika eneo la Wilaya ya Ilemela District kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo.

Eneo hilo linatarajiwa kujumuisha uwanja mkubwa wa mpira wa miguu, uwanja wa riadha, viwanja vya michezo ya ndani (indoor arena) kwa michezo kama mpira wa kikapu na mpira wa wavu, pamoja na miundombinu ya mafunzo na kukuza vipaji vya wanamichezo.

Wednesday, March 18, 2026

SALA YA EID KWA NGAZI YA MKOA KUFANYIKA NYAMAGANA.

 


Baraza Kuu la Waislam Mkoa wa Mwanza limetangaza kuwa Swala ya Eid itafanyika kimkoa katika Uwanja wa Nyamagana uliopo Wilaya ya Nyamagana, Mkoa wa Mwanza.


Katika taarifa hiyo, Waislam wote mkoani Mwanza wanaombwa kuhudhuria swala hilo kwa pamoja ili kushiriki ibada hiyo muhimu ya sikukuu.


Baraza hilo limehimiza umoja, mshikamano na nidhamu wakati wa ibada hiyo, pamoja na kuzingatia maelekezo yatakayotolewa na viongozi wa dini na mamlaka husika.

VIKUNDI 41 VIJANA, WANAWAKE NA WATU WENYE ULEMAVU VYANUFAIKA NA MIKOPO YA ASILIMIA 10 ILEMELA

 


Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza , Amir Mkalipa, amevitaka vikundi vilivyopata mikopo ya asilimia 10 katika wilaya hiyo kuhakikisha vinarejesha fedha hizo kwa wakati ili kutoa fursa kwa vikundi vingine kunufaika na mpango huo.


Akizungumza hii leo wakati wa hafla ya utoaji wa mikopo hiyo iliyofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Mkalipa amesema kuwa halmashauri itafuatilia kwa karibu vikundi vyote vilivyopata mikopo ili kuhakikisha vinarejesha kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa.


Aidha, Mkalipa amewataka maafisa maendeleo wa kata kutoa elimu mara kwa mara kwa vikundi hivyo pamoja na kuvitembelea ili kubaini mapema vikundi vinavyosuasua katika marejesho, na kuchukua hatua stahiki kwa wakati.


Kwa upande wake, Meya wa Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Bi. Salah Ngw'ani, ameishukuru halmashauri hiyo kwa utoaji wa mikopo hiyo, akisema kuwa itakuwa chachu ya maendeleo kwa wakazi wa wilaya hiyo.


Jumla ya vikundi 41 vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu katika wilaya ya ilemela vimenufaika na mikopo hiyo  ya alimia 10 yenye thamani ya shilingi milioni 463.

YANGA SC YAAMBULIA SULUHU NYINGINE KWA TRA UNITED ARUSHA

 


MABINGWA watetezi, Yanga SC wametoa sare ya bila kufungana na wenyeji, TRA United katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania jioni ya leo Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha.

TRA United ilicheza pungufu kwa dakika 10 za mwisho kufuatia kiungo wake, Muzamil Yassin Selemba kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 76 baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano.

 

Majeruhi bado yanaiandama Yanga huku Dube na beki wa kulia Israel Mwenda wote wakitoka uwanjani kutokana na kugongana. Sare hiyo inaifanya Yanga ibaki kileleni kwa pointi zake 37, tisa mbele ya Azam inayoshika nafasi ya pili na JKT Tanzania inayoshika nafasi ya tatu, wakiwa na pointi 28 kila mmoja, huku Simba wakishika nafasi ya nne kwa pointi 27 nayo TRA nafasi ya 10.


Huu unakuwa mchezo wa pili mfululizo kwa Yanga wa ligi bila bao, kufuatia sare ya 0-0 dhidi ya Azam wikendi iliyopita. Baada ya mechi 15 za mzunguko wa kwanza, Yanga imeshinda 11 na kutoa sare nne, huku ikiwa haijafungwa.


Azam wamecheza mechi 14, mechi inayofuata dhidi ya Mashujaa mjini Kigoma kesho, huku Simba wakicheza mechi yao ya 13 dhidi ya Pamba ya Jiji, hiyo ikimaanisha kuonyesha kwa nguvu kwenye michezo hii kunaweza kuwafanya kupunguza pengo la pointi moja tu nyuma ya wapinzani wao hao wa jadi.


SENEGAL WAVULIWA UBINGWA WA AFCON, MOROCCO WAPEWA USHNDI WA 3-0

 


BODI ya Rufaa ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) imeivua Senegal ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) na kuwapa wenyeji, Morocco.

Senegal ilitawazwa kuwa bingwa wa AFCON ya 2025 baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Morocco Januari 18, mwaka huu bao pekee la kiungo wa ulinzi, Pape Alassane Gueye anayechezea Villarreal ya Hispania dakika ya 94 katika mchezo uliodumu kwa dakika 120 Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat.

Hata hivyo, CAF imesema kwamba Senegal imepoteza mechi hiyo na Morocco wamepewa ushindi wa mabao 3-0  kwa kutumia Kifungu cha 84 cha Kanuni za AFCON kwa kitendo chao cha kuondoka uwanjani kupinga Penalti waliyopewa Morocco na kusababisha mchezo kusima akwa dakika 14, kabla ya kurejea kumalizia.

Mshambuliaji Brahim Díaz wa Morocco ambaye yeye mwenyewe alichezewa rafu na beki wa Senegal, El Hadji Malick Diouf – alikwenda kupiga penalti kwa staili ya Panenka bahati mbaya ikaokolewa na kipa Édouard Mendy na kuzima ndoto za Simba wa Atlasi kutwaa taji kwa jasho uwanjani.

Tuesday, March 17, 2026

JPM

Monday, March 16, 2026

MIAKA MITANO TANZANIA BILA JPM

 


Miaka Mitano Siku Zaidi ya Siku 1800 Tangu kifo cha Rais Wa Awamu ya Tano Hayati Dkt, John Pombe Magufuli 


#kazinangoma ya 93.7 Jembe Fm inaungana na Familia ya Dkt, John Pombe Magufuli na Watanzania wote katika kumbukizi hiyo 

Kuzifungua kurasa za kumbukumbu, mijadala na simulizi.

Kuanzia Leo.

📅 16–17 Machi 2026

📻 93.7 Mwanza


Usikose.  Kusikiliza vipindi mbalimbali kupitia Jembe Fm🔥📻 Na Kutufatilia kwenye mitandao ya kijamii @jembefmtz 


Follow Us On Social Media

‎Instagram - @jembefmtz

‎Facebook - @jembefmtz

‎X(Twitter) - @jembefmtz

‎TikTok - @jembefmtz

‎Thread - @jembefmtz


#AhsanteKwaTime 

#Familiamoja

#10yrsjembefm 


#JembeFMKurasa1800LiveChato

MVUA MOROGORO YASABABISHA VIFO VINNE

 


Mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Morogoro zimesababisha vifo vya watu wanne katika matukio tofauti, huku wengine wakijeruhiwa baada ya kupigwa na radi.

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, SACP Alex Mkama, amesema watu wawili walifariki dunia baada ya kupigwa na radi wakati wa mvua kubwa katika Kijiji cha Kilosa Mpepo wilayani Malinyi.

Amewataja waliofariki kuwa ni Nindi Masele (15) na Marwa Mwanzilwa (2), wote wakazi wa kijiji hicho, waliopoteza maisha usiku wa Machi 13, 2026 wakati mvua kubwa ikiendelea kunyesha.

Aidha, amesema watu wengine wanne wa familia moja walijeruhiwa katika tukio hilo akiwemo Milembe Dase (27), Kulwa Malembe (38), Milembe Samwel (39) pamoja na Ngolo Nchimwe (1), ambao wanaendelea kupatiwa matibabu.

Ndani ya mwezi mmoja uliopita, tukio jingine la radi lilitokea Februari 23 mwaka huu katika Kitongoji cha Mbesi, Kijiji na Kata ya Utengule, Halmashauri ya Mlimba wilayani Kilombero.

Katika tukio hilo, watu wawili Tano Leonard Lunasi (36) na Ngimila Ndombeji Mashana (27), wote wakulima na wakazi wa eneo hilo, walipoteza maisha huku wengine wawili wakijeruhiwa walipokuwa wakirejea nyumbani kutoka matembezini.

Katika tukio jingine, watu wawili Hamis Yahaya Waziri (45), mkulima mkazi wa Kisaye na Nyerere Katebeka Kidagati (50), mfugaji mkazi wa Mkono wa Mara wilayani Morogoro, wamefariki dunia baada ya kusombwa na maji ya mvua.

Kamanda Mkama amesema watu hao walifariki katika kata za Tegetero na Mkambarani walipokuwa wakijaribu kuvuka maeneo yaliyofurika maji lakini walizidiwa nguvu na kusombwa na maji.

KAMATI BUNGE YARIDHISHWA MRADI FARU MWEUSI, MBWA MWITU

 Faru mweusi ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi.Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imesema imeridhishwa na uwekezaji wa mradi wa uhifadhi wa faru mweusi na mbwa mwitu katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, na kuiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na mamlaka husika kuendelea kuwalinda wanyama hao ambao walikuwa hatarini kutoweka.

Akizungumza Machi 15 baada ya kutembelea na kukagua mradi huo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mary Masanja, amesema kamati imefurahishwa na maendeleo ya mradi huo huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwalinda na kuwahifadhi wanyama hao adimu.

Alisema pia ni muhimu kuangalia uwezekano wa kuwahamishia faru katika hifadhi nyingine kadri idadi yao inavyozidi kuongezeka, ili kuwapa nafasi zaidi ya kuishi na kuongeza fursa kwa watalii kuwaona katika maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini.

“Mradi kwa sasa unaridhisha na ukizingatia kwamba faru ni mnyama aliyekuwa kwenye hatari ya kutoweka. Tunaendelea kuwaalika wananchi watembelee hifadhi hii, na kikubwa tumeielekeza Wizara kuwa mradi huu unahitaji matunzo endelevu. Pale ambapo idadi ya faru itaongezeka, waweze kusambazwa katika hifadhi nyingine ili watalii wanaotembelea maeneo hayo waweze kuwaona kwa urahisi zaidi,” alisema Masanja.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Hassan Abbasi, alisema mradi huo wa faru uliogharimu zaidi ya shilingi bilioni 3.4 unalenga kuwahifadhi wanyama hao adimu ili waweze kuzaliana na kulinda urithi wa taifa.

Alisema pamoja na juhudi za uhifadhi, mradi huo pia umeongeza thamani ya utalii katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, kwani watalii sasa wanaweza kufika katika eneo maalumu lenye uzio wa umeme na kupata fursa ya kuwaona faru kwa ukaribu zaidi.

“Kamati wameridhishwa na mradi huu na kutupa maelekezo ya kuendelea kuwalinda wanyama hawa pamoja na kuboresha zaidi mradi huu. Faru waliopo katika mradi huu wamefikia idadi ya 50, hivyo eneo la sasa linaanza kuwa finyu. Kamati imesisitiza kuongeza eneo la uzio, na sisi pamoja na mamlaka husika tunakwenda kulifanyia kazi kwa haraka ili wanyama wapate eneo kubwa zaidi la kuishi na utalii uendelee kuimarika,” alisema Abbasi.

Aidha, aliongeza kuwa Wizara pia inapanga kuongeza magari kwa ajili ya kuwahudumia watalii wanaotembelea eneo la faru pamoja na hifadhi kwa ujumla, kutokana na ongezeko kubwa la watalii wanaotembelea Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, hususan wale wanaokuja kuona faru.

Kwa upande wake, mjumbe wa kamati hiyo, Asia Halamga, alisema juhudi za Serikali zimewezesha kuongezeka kwa wanyama waliokuwa adimu kama faru na mbwa mwitu katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi.

Alitoa wito kwa Watanzania kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini ili kufurahia na kuthamini urithi wa rasilimali za asili uliopo Tanzania.