ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, April 24, 2026

SIMBA WALEEEE NUSU FAINALI KOMBE LA MUUNGANO 2026

 


TIMU ya Simba SC imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya Kombe la Muungano baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mafunzo usiku wa tarehe 23 Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

Bao pekee la Simba SC katika mchezo huo limefungwa na mshambuliaji wake tegemeo kwa sasa, Suleiman Abdallah Mwalimu ‘Gomez’ dakika ya 54.

Simba SC sasa itakutana na Mlandege FC katika Nusu Fainali Jumapili, baada ya mabingwa watetezi, Yanga kucheza na Azam FC katika Nusu Fainali ya kwanza Jumamosi, mechi zote zikianza kuanzia Saa 2:15 usiku hapo hapo Uwanja wa New Amaan Complex 

Mlandege FC imetinga Nusu Fainali baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars mchezo uliocheza jioni ya tarehe 23 April 2026 hapo hapo Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

Mabao ya Mlandege yamefungwa na Omar Juma’Samatta’ dakika ya 28 na Mussan Hassan ‘Mbappe’ dakika ya 45’+1, baada ya Mishamo Daudi kuanza kuifungia Singida Black Stars dakika ya tisa.

Wakati Yanga iliitoa Muembe Makumbi City FC kwa kuichapa mabao 4-0 juzi, Azam FC iliitupa nje KVZ FC KWA kuichapa mabao 2-0 hapo hapo Amaan Complex.

BETIKA WAZINDUA JEZI YA MSIMU WA 10 WA TULIA MARATHON MBEYA

 


KAMPUNI ya ubashiri, Betika Tanzania ikishirikiana na Taasisi ya Tulia trust kupitia Betika Mbeya Tulia Marathon imezindua rasmi jezi ambayo itatumika Msimu wa 10 wa Mashindano Jijini Mbeya mwaka huu.

Akizungumza na Wanahabari  Jijini Dar es Salaam Meneja Mkuu wa Betika Tanzania Samuel Mcheru amesema Betika inathamini sana michezo na itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa kupitia Taasisi ya Tulia trust Kuhakikisha mbio hizo za Betika Mbeya Tulia Marathon zinafanyika kwa ufanisi mkubwa.

Hata hivyo, ameongeza kuwa mashirikiano hayo yanalenga kuwaweka wananchi karibu na kushiriki michezo ili kuweka miili yao imara zaidi,kurudisha tabasamu kwa jamii na kutoa fursa za kibiashara kwa Wananchi wa Jiji hilo.

Mcheru ametoa wito kwa Makampuni mengine yawe yenye tija katika jamii kwani uwepo wa Betika Tulia Marathon ni kiashiria tosha kuwepo kwa ongezeko la kipato kila inapofanyika kutokana na jamii kukusanyika eneo moja hivyo inawapa fursa betika pia kujitangaza zaidi na Wafanyabiashara kuendesha shughuli zao.

Kwa upande wake Mbunge wa Mbeya na Spika wa Bunge Mstaafu Dkt.Tulia Ackson amesema Kampuni ya Betika imekuwa na mchango mkubwa wa kuhakikisha mbio hizo zinafanyika kwa ufanisi mkubwa hasa kwa mchango wao wa vifaa vya kushiriki mbio hizo pamoja na miundombinu mbalimbali pindi linapokuja shindano hilo kutokana na kuweka udhamini wao kwa zaidi ya Miaka mitatu.

Ackson amesema kwa mwaka huu shindano hilo linatimiza miaka 10 tangu kuanzishwa kwake na kwa mwaka huu wanategemea kukusanya kiasi cha fedha shilingi milioni 300 ili kugusa Maeneo ya Kijamii mbalimbali ikiwemo Kuboresha makazi ya Wahitaji, eneo la Afya hususani kujenga baadhi ya wodi hitajika, vifaa pamoja na eneo la Elimu Mashuleni.

Hata hivyo amesema Mbio hizo za kipekee zilizopewa chachu na hali ya hewa ya jiji hilo itatimua vumbi Mei 15 na 16 zikiambatana na burudani mbalimbali.

Aidha amevipongeza vyombo vya habari kwa kuendelea kutoa habari juu ya Taasisi ya hiyo ambayo kutokana na michango ya wadau mbalimbali katika kujikita kusaidia jamii.

Pia ametoa wito kwa Watanzania kujiandikisha kushiriki katika mbio hizo kupitia Ofisi zilizopo Jijini Mbeya pamoja na kujisajili mtandao kwenye kurasa za Taasisi hiyo.

Nae Afisa Habari wa Kampuni ya Betika Juvenalius Rugambwa aliongeza kuwa Jezi hiyo iliozinduliwa itatumika rasmi kwenye mbio hizo huku akisherehesha kuwa jezi hizo zimepambwa na rangi zenye mvuto zaidi zenye michoro ya vivutio vilivyopo Tanzania ikiwemo bendera ya Taifa.

Thursday, April 23, 2026

SAKATA LA MAHANDAKI MWANZA: MFANYABIASHARA AKAMATWA KWA UJENZI USIOFUATA SHERIA.

 news

Katika tukio linalozua maswali ya kiusalama na ufuatiliaji wa shughuli za ujenzi, mfanyabiashara Evance Bisesagu (47), mkazi wa Bupumula, Kata ya Nyamhongolo, Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kuchimba mahandaki sita kinyume cha sheria.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, mtuhumiwa huyo alikamatwa jioni ya Aprili 22, 2026, kufuatia taarifa za wananchi waliokuwa na hofu juu ya uwepo wa mahandaki hayo karibu na makazi yao. Wananchi hao walieleza kuwa shughuli hizo zilikuwa zikifanyika kwa siri na bila maelezo ya wazi, jambo lililozua wasiwasi mkubwa wa usalama.

Uchunguzi wa Polisi Wabaini Ukiukwaji wa Sheria

Akizungumza Aprili 23, 2026, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa, alisema uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa ujenzi huo ulikuwa unafanyika bila vibali halali kutoka mamlaka husika.

Mbali na mmiliki wa eneo hilo, watu wengine wawili Ngasa Kasuka na Hamad Kashinje pia wanashikiliwa wakidaiwa kuwa walikuwa wakifanya kazi kama vibarua katika mradi huo.

 “Msako unaendelea kuwatafuta mafundi na watu wengine wote waliohusika katika shughuli hizi,” alieleza Kamanda Mutafungwa.


Hofu ya Usalama kwa Wananchi

Tukio hili limeibua mjadala mpana kuhusu usalama wa makazi ya wananchi, hasa pale shughuli za ujenzi zinapofanyika bila uwazi na ufuatiliaji wa karibu. Mahandaki kama hayo yanaweza kusababisha hatari kubwa, ikiwemo kuporomoka kwa ardhi au majengo, pamoja na uwezekano wa kutumika kwa shughuli zisizo halali.

Wito kwa Viongozi na Mamlaka

Jeshi la Polisi limetoa rai kwa viongozi wa serikali za mitaa na mamlaka za ujenzi kuhakikisha wanafuatilia kwa karibu shughuli zote za maendeleo katika maeneo yao.

Kamanda Mutafungwa alisisitiza kuwa ni lazima kila ujenzi ufuate taratibu zote za kisheria, ikiwa ni pamoja na kupata vibali vinavyohitajika kabla ya kuanza kazi yoyote.

 “Hatutavumilia ujenzi holela. Kila anayekiuka sheria atachukuliwa hatua kali,” alionya.


Wednesday, April 22, 2026

ALIYEMUUA MUMEWE BAADA YA FUMANIZI AHUKUMIWA KIFUNGO CHA NJE.

 Mahakama

ELIZABETH Sylvester maarufu kama Sosomo, mkazi wa Kijiji cha Chudeko, Wilaya ya Songwe, amehukumiwa kifungo cha nje cha miezi 18, baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kumuua mumewe, Ally Masanja, bila kukusudia.

Hukumu hiyo imetolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songwe, imemhukumu Katika kesi hiyo namba 7304/2026, mshitakiwa alikiri kosa la kuua bila kukusudia kinyume na vifungu vya  195 na 198 vya kanuni ya adhabu, Sura ya 16, kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2023.

Kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo na wakili wa Serikali, Elbariki Mpinga, tukio hilo lilitokea Januari 3, 2026 katika Kijiji cha Chudeko, wilayani Songwe, ambapo mshitakiwa alimchoma mumewe kisu ubavuni wakati wa ugomvi uliotokana na wivu wa mapenzi.

Ilielezwa kuwa ugomvi huo ulizuka baada ya mshitakiwa kumkuta mumewe akiwa  nyumbani kwa mwanamke anayedaiwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi. 

Hali  hiyo  iliyoibua ugomvi kati yao watatu hao, hadi kufikia  kwenye shambulio hilo lililosababbisha mauti ya mwanaume huyo. 

Akisoma hukumu Aprili 21, 2026, Jaji Mfawidhi wa mahakama hiyo, Jaji Gabriel Malata, amesema mahakama imezingatia mazingira ya tukio, ikiwemo hali ya mshtakiwa kabla, wakati na baada ya tukio pamoja na ungamo lake.

Alisema mahakama ilimtia hatiani kwa kosa hilo na kuamua kumpa adhabu hiyo ya kifungo cha nje cha miezi 18 kwa kuzingatia masharti ya kisheria.

Kwa mujibu wa hukumu hiyo, mshitakiwa hataruhusiwa kutenda kosa lolote la jinai katika kipindi hicho, na endapo atakiuka masharti hayo atalazimika kutumikia kifungo hicho gerezani.

Kesi hiyo ni miongoni mwa kesi tatu za mwanzo kutolewa hukumu na Mahakama Kuu Kanda ya Songwe tangu kuanza rasmi kwa shughuli zake za kimahakama Machi 30, 2026.

Awali, Wakili wa utetezi, Moses Mwampashi, aliomba mahakama imuonee huruma mshitakiwa, akieleza kuwa hilo ni kosa lake la kwanza na halikupangwa bali lilitokana na mazingira ya tukio.

Aliongeza kuwa mshitakiwa ana watoto wanne aliowazaa na mumewe,ambao kwa sasa  ndiye mtu wa kuwalea na wanamtegemea, hivyo kuiomba mahakama izingatie maslahi yao katika utoaji wa hukumu.

KONGAMANO LA WANAUME (MEN AT WORK) KUFANYIKA MWANZA

 

Men at Work ni jukwaa maalum linalowakutanisha wanaume kutoka maeneo mbalimbali kwa lengo la kujifunza, kujadili na kujengeana uwezo katika safari ya maisha. 

Kupitia kongamano hili, washiriki hupata fursa ya kuimarika katika nyanja muhimu kama uchumi, ndoa na mahusiano pamoja na kukuza nidhamu binafsi na uwajibikaji katika nafasi zao kama wanaume ndani ya familia na jamii kwa ujumla.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2015, Men at Work imeendelea kuwa chachu ya mabadiliko kwa wanaume wengi, ikiwa imefanikiwa kuandaa makongamano yenye tija ndani na nje ya Mwanza. 

Athari yake imekuwa kubwa kiasi cha kuibua majukwaa mengine yenye mwelekeo sawa, ikiwemo "Kikao cha Wanaume", lakini chimbuko lake ni Men at Work. 

Ushuhuda wa mafanikio na mabadiliko ya maisha ya washiriki ni mwingi na unaendelea kuongezeka kila mwaka na unatarajiwa kutolewa katika kongamano la wanaume jijini Mwanza.

Kongamano hilo la wanaume (Men at Work) linatarakiwa kufanyika jumamosi tarehe 26 Aprili 2026 katika ukumbi wa Chuo cha BOT, Capripoint jijini Mwanza kuanzia saa mbili asubuhi.

Mwandaaji wa kongamano hilo, Maxwell Chaila amesema jukwaa hilo ni linatoa fursa kwa wanaume kufahamiana na kujifunza safari ya mabadiliko chanya katika maisha yao.

Men at Work- Mwanaume Bora, Jamii Imara.

Friday, April 17, 2026

MALEMA AHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA MI-5 JELA

Kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini, Julius Malema
Kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini, Julius Malema.

 

Kiongozi wa chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini, Julius Malema, ameripotiwa kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano jela baada ya kupatikana na hatia ya kumiliki silaha kinyume cha sheria pamoja na kufyatua risasi hadharani.

Tukio Lilivyotokea

Hukumu hiyo inatokana na tukio la mwaka 2018 wakati wa maadhimisho ya miaka mitano ya chama cha EFF yaliyofanyika katika jimbo la Eastern Cape. Katika tukio hilo, video iliyosambaa mitandaoni ilimuonyesha Malema akifyatua risasi kadhaa hewani kwa kutumia bunduki ya nusu otomatiki mbele ya umati wa wafuasi wake waliokuwa wakishangilia.

Mamlaka za usalama zilichukulia kitendo hicho kama ukiukwaji wa sheria za silaha za moto nchini Afrika Kusini, hali iliyosababisha kuanzishwa kwa uchunguzi na hatimaye kufunguliwa kwa mashtaka dhidi yake.

Utetezi Wake Mahakamani

Akiwasilisha utetezi wake, Malema alidai kuwa silaha iliyotumika haikuwa mali yake na kwamba kitendo hicho kilikuwa sehemu ya kuhamasisha umati katika tukio la kisiasa. Hata hivyo, upande wa mashtaka uliwasilisha ushahidi ulioridhisha mahakama kwamba kitendo hicho kilikiuka sheria za nchi, na hivyo kumfanya kupatikana na hatia.

Athari za Kisiasa

Hukumu hiyo inatarajiwa kuwa na athari kubwa katika siasa za Afrika Kusini, hasa kutokana na nafasi ya Malema kama mmoja wa viongozi wakuu wa upinzani. Chama chake cha EFF kimekuwa na ushawishi mkubwa miongoni mwa vijana na tabaka la wafanyakazi, hivyo hukumu hiyo inaweza kuathiri mwenendo wa kisiasa ndani ya chama na taifa kwa ujumla.

Wachambuzi wa siasa wanaamini kuwa kesi hiyo inaweza kufungua mjadala mpana kuhusu nidhamu ya viongozi wa kisiasa, utawala wa sheria na matumizi sahihi ya silaha za moto nchini humo.

KOCHA BILO AFARIKI AKIWA UWANJANI JIJINI MWANZA

aa

  Athuman Bilali maarufu kama Billo.

Picha: Mtandao
Athuman Bilali maarufu kama Billo.

Aliyewahi kuwa kocha wa timu mbalimbali za soka nchini, ikiwamo Stand United ‘Chama la Wana’ na Pamba (sasa Pamba Jiji), Athuman Bilali maarufu kama Billo, amefariki dunia huku chanzo cha kifo chake kikiwa bado hakijafahamika.

Marehemu Billo hadi mauti yanamkuta alikuwa mmiliki wa kituo cha michezo pamoja na timu ya wanawake ya Bilo Queens inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania.

Katibu wa Chama cha Soka Mkoa wa Mwanza (MZFA), Leonard Malongo, amethibitisha kifo hicho, akieleza kuwa ni pigo kubwa kwa wadau wa soka mkoani Mwanza na nchini kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Malongo, taarifa za awali zinaeleza kuwa kocha huyo aliendelea na majukumu yake ya kawaida ya mazoezi na timu ya Bilo Queens katika Uwanja wa Shule ya Msingi Nyasaka jijini Mwanza hadi jioni ya Aprili 15, 2026. Hata hivyo, baada ya wachezaji kuondoka, aliachwa akiwa amekaa uwanjani na baadaye alikutwa amefariki eneo hilo asubuhi iliyofuata.

“Jana alikuwa uwanjani akifanya mazoezi na timu yake, lakini hadi wachezaji wanaondoka walimwacha amekaa. Asubuhi ndipo alikutwa amefariki hapohapo. Bado hatujajua chanzo cha kifo, kwani mwili wake umehifadhiwa hospitalini kwa uchunguzi zaidi,” amesema Malongo.

Ameongeza kuwa taarifa zaidi kuhusu chanzo cha kifo pamoja na ratiba ya mazishi zitatolewa baada ya taratibu za kitabibu kukamilika.

Kifo cha Billo kimeacha pengo kubwa katika maendeleo ya soka, hususan katika kuinua vipaji vya wanawake kupitia timu yake ya Bilo Queens. Wadadau wa michezo wanatarajiwa kuendelea kutoa salamu za rambirambi huku wakikumbuka mchango wake mkubwa katika tasnia ya soka nchini.

Thursday, April 16, 2026

BALAA LA YANGA KWA MBEYA CITY LEO


MABINGWA watetezi, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam.

Mabao ya Yanga SC yamefungwa na mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo mawili dakika ya saba na 82, kiungo Muivory Coast, Pacome Peodoh Zouzoua dakika ya 10 na 44, kiungo Mkongo Maxi Mpia Nzengeli dakika ya 16 na beki mzawa, Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ dakika ya 45’+2.

Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 47 katika mchezo wa 19 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi nane zaidi ya watani, Simba SC ambao hata hivyo wana mechi moja mkononi.

Kwa upande wao Mbeya City baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi zao 17 za mechi 19 pia nafasi ya 13 kwenye ligi ya timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.  

Wednesday, April 15, 2026

WANANCHI WASHIRIKI UJENZI WA JENGO LA HUDUMA ZA UZAZI

 

Na, Ernest Magashi

Wananchi wa Kata ya Katente, Wilaya ya Bukombe mkoani Geita, wamejitokeza kwa wingi kushiriki zoezi la kusafisha eneo litakalojengwa jengo la huduma za uzazi katika Hospitali ya Wilaya ya Bukombe. Ushiriki huo unaakisi mwamko mkubwa wa jamii katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuboresha huduma za afya, hususan kwa mama na mtoto.Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Marycelina Mbohoma, ametoa shukrani za dhati kwa Rais kwa kuidhinisha utoaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo muhimu. Amesema uwekezaji huo ni hatua madhubuti katika kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga.Aidha, Mbohoma amewataka wananchi kuendelea kuwa walinzi wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao.“Mradi huu ni wetu sote. Ni wajibu wetu kuulinda, kuuthamini na kutoa taarifa mapema pale tutakapoona viashiria vya hujuma,” amesisitiza.Kwa upande wake, Mhandisi wa Ujenzi wa Wilaya, Haruni Fashe, amesema jengo hilo la kisasa litagharimu shilingi milioni 660 na linatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi minne.Amefafanua kuwa jengo hilo litakuwa na miundombinu muhimu ikiwemo wodi za wazazi, vyumba vya kujifungulia, chumba cha upasuaji, pamoja na huduma za watoto wachanga.Mradi huu unatarajiwa kuleta mapinduzi makubwa katika utoaji wa huduma za afya wilayani Bukombe, kwa kuhakikisha akina mama wanapata huduma salama na bora wakati wa kujifungua, na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo vinavyoweza kuzuilika.Ushiriki wa wananchi katika hatua za awali za utekelezaji wa mradi huu ni ishara ya umiliki wa kweli wa miradi ya maendeleo na msingi imara wa mafanikio endelevu ya sekta ya afya.Mkazi wa Katente, Evodia Simon,alisema wamejitokeza kujitolea nguvu zao kama sehemu ya kuitikia wito wa maendeleo unaotolewa mara kwa mara na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, na viongozi wengine wa serikali katika mikutano ya hadhara.

SIMBA SC YAIBAMIZA FOUNTAIN GATE 3-0

 


TIMU ya Simba SC imeonyesha ubabe wake jioni ya leo kwa kuibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Fountain Gate FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara uliopigwa kwenye dimba la Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha. 


Simba ilianza kuonesha makali yake mwishoni mwa kipindi cha kwanza, ambapo kiungo fundi kutoka Zambia, Clatous Chama alifungua ukurasa wa mabao dakika ya 45+7 kwa mpira uliowaacha mabeki wa Fountain Gate wakitazamana. 


Kipindi cha pili hakikuwa na huruma, kwani winga hatari kutoka Senegal, Libasse Gueye aliongeza bao la pili dakika ya 53, akimalizia shambulizi la kasi lililoacha mashabiki wa Simba wakishangilia kwa furaha kubwa. 


Shinikizo la Simba liliendelea kuwa kubwa na kuwavuruga wapinzani wao, hali iliyosababisha kiungo mzawa, Shaaban Mgunda kujifunga dakika ya 71 wakati akijaribu kuokoa hatari langoni kwake—bao lililozika matumaini ya Fountain Gate kabisa. 


Kwa ushindi huo, Simba SC sasa imefikisha pointi 39, ikiendelea kushikilia nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi, ikiwa nyuma kwa pointi tano dhidi ya vinara na mabingwa watetezi, Young Africans SC baada ya kila timu kucheza mechi 18. 


Kwa upande wa Fountain Gate, hali inaendelea kuwa tete baada ya kupoteza mchezo wao wa 10 kati ya 18 walizocheza hadi sasa. 


Wakiwa na sare nne na ushindi nne pekee, wanabaki na pointi 16, wakishika nafasi ya 14 katika ligi yenye timu 16—eneo hatarishi kabisa. 


Vita ya kushuka daraja yazidi kupamba moto 

Kwa mujibu wa kanuni za ligi, timu mbili za mwisho zitashuka moja kwa moja daraja. 

Hata hivyo, zile zitakazomaliza nafasi ya 13 na 14 zitapata nafasi ya kupambana kujiokoa kupitia mechi za mtoano za nyumbani na ugenini. 

Mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu, huku atakayeshindwa akilazimika kupambana tena na timu kutoka Ligi ya Championship katika hatua nyingine ya mchujo—mapambano ya mwisho yatakayobainisha nani atasalia kwenye ligi kuu msimu ujao.

WIZARA YA MAMBO YA NJE KUANDAA UTARATIBU WA KUVUNA MAARIFA YA MABALOZI WASTAAFU


Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imetakiwa kutumia hazina ya maarifa na uzoefu kutoka kwa Mabalozi Wastaafu katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuimarisha diplomasia ya nchi. 


Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo wakati anafungua kikao cha mashauriano kati ya uongozi wa Wizara na Mabalozi Wastaafu kilichofanyika jijini Dar Es Salaam Aprili 15, 2026. 

"Wizara tumeanzisha utaratibu wa kuwa na vikao vya mara kwa mara na Mabalozi Wastaafu ili kuvuna maarifa na uzoefu wao kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia ili ulete nanufaa katika nyanja mbalimbali kama vile, siasa, ulinzi na usalama, uchumi, biashara, uwekezaji na utalii". Balozi Kombo alisema.


Balozi Kombo ametaja mifano ya maeneo ambayo angependa Mabalozi Wastaafu wachangie maarifa na uzoefu walio kuwa nao ili maeneo hayo yaendelee kuwa na manufaa zaidi kwenye nchi..


Maeneo hayo ni pamoja na mwenendo wa ufanyaji wa biashara baina ya Tanzania na nchi nyingine, hususan zilizopo barani Afrika.


Utekelezaji wa Dira 2050 ambayo inalenga uchumi wa Dola bilioni moja, ni eneo lingine muhimu ambalo maarifa ya Mabalozi Wastaafu yanahitajika ili kuhakikisha 

utekelezaji wake unakuwa wa ufanisi.


Waziri Kombo ameongeza kuwa mabadiliko yanayoendelea duniani 

hususan, maendeleo ya kidigitali yanahitaji mikakati thabiti ili nchi iweze kunufaika na kuwa na mipango madhubuti ya kukabiliana na athari zake. Haya yote yanahitaji mawazo ya pamoja ili kuyaendeea kwa ufanisi.


Eneo lingine ambalo Waziri  Kombo alisisitiza umuhimu wa kupata uzoefu wa Mabalozi Wastaafu ni siasa za ulimwengu ambazo zimekuwa hazitabiriki na zinasababisha madhara mbalimbali, hususan katika nchi zinazoendelea kama Tanzania.


Aidha, uzoefu wa Mabalozi Wastaafu unahitajika katika kuendeleza na kuimarisha taswira nzuri ya nchi na hasa nchi inapopewa dhamana ya majukumu ya kimataifa. Balozi Kombo alisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika mwaka 2028 na hivyo maarifa yao ni muhimu ili kuhakikisha nchi inatekeleza jukumu hilo kwa ufanisi. 

Awali, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alisema Wizara inaangalia uwezekano wa kuanzisha utaratibu rasmi kupitia   Ofisi ya Rais-UTUMISHI ili ushirikishwaji wa Mabalozi Wastaafu uwe unatambulika rasmi.



Monday, April 13, 2026

HORMUZ | MAZUNGUMZO YA HORMUZ NI "MECHI ILIYOISHA KABLA HAIJAANZA"

 AZAM MEDIA LTD

Friday, April 10, 2026

SERIKALI YAKUTANA NA MHE. CHAKWERA

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi (kushoto), akiwa  na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera,

Na Mwandishi wetu

Ujumbe wa Serikali ya Tanzania ukingozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi, imekutana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera, na kujadiliana kuhusu namna Tanzania ilivyojidhatiti katika kudumisha umoja, amani na mshikamano miongoni mwa Watanzania.

Kikao hicho kilifanyika katika Kituo cha Mikutano cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyrere (JNICC) siku ya Alhamisi Aprili 9, 2026 mchana baada ya Mheshimiwa Chakwera kumtembelea Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahamoud Thabit Kombo, ikiwa ni ishara ya kuanza rasmi kwa ziara ya Mjumbe huyo Maalum nchini Tanzania.


Katika kikao hicho, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mjumbe huyo Maalum, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchululiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka mssisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.

“Tumekutana na Mheshimiwa Chakwera na tumemueleza mambo mengi kuhusu Tanzania na historia ya nchi hii tangu ipate uhuru mwaka 1961, hali ya siasa na demokrasia nchni, na hatua ambazo serikali inaendelea kuchukua ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo”, ameeleza Waziri Kabudi.

Waziri kabudi ameeleza kuwa kikao hicho kimekuwa kizuri na chenye mafanikio kutokana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola kupata ufafanuzi wa kutosha juu ya masuala mbalimbali yanayoendelea nchini hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania.


Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera anatarajiwa kukutana na wadau mbalimbali ambapo jana Aprili 10, 2026 alikutana na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi pamoja na vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.

Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).


Katika ziara yake hii, Mheshimiwa Chakwera anatarajia pia kukutana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.

Aidha, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, atakutana pia na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

JEH ALAMA ZILIZOPO KWENYE NOTI YA DOLA 1YA MAREKANI ZINAMAANISHA NINI?

Illustration of U.S. $1 bill symbols

Bila shaka unaifahamu noti ya dola 1 ya Marekani. Huenda umeiona maelfu ya mara, na ni mojawapo ya sarafu zinazotambulika zaidi duniani. Inawezekana hata una kadhaa kwenye pochi yako hivi sasa.


Lakini ni mara ngapi umeiangalia kwa makini na kujiuliza maana ya muundo wake na alama zilizopo juu yake?


Kwanza kabisa, alama hizo hazikuchaguliwa kwa bahati. Kwa mfano, picha ya George Washington haikuwa kwenye dola tangu mwanzo. Noti ya kwanza halali ya dola 1 ilitolewa wakati wa Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Marekani, na ilikuwa na picha ya Salmon P. Chase ambaye alikuwa Waziri wa Fedha wakati huo. Washington aliwekwa kwenye dola hiyo mwaka 1869.


Upande wa Mbele wa Dola

Tuanzie upande wa mbele wa noti, ambao una picha ya Washington. Upande huu una vitu vingi, ikiwa ni pamoja na:

Great Seal


Muhuri wa Wilaya ya Benki Kuu (Federal Reserve)

- Herufi na namba ya nafasi ya noti

- Namba ya mfululizo (serial number)

- Muhuri wa Hazina ya Marekani

- Namba ya sahani ya uchapishaji

- Mwaka wa toleo (series)


Kwa mfano, kila noti ya dola 1 ina muhuri wa Wilaya ya Federal Reserve System. Huu ni namba (kama 1 au 2) unaoonekana mara nne kwenye noti. Namba hiyo inaonyesha ni benki ipi ya Federal Reserve iliyochapisha noti hiyo. Mfano, namba 2 ina maana ilichapishwa New York. Pia kuna herufi (kama B) inayobainisha wilaya husika.


Herufi na namba ya nafasi ya noti (mfano B3) inaonyesha nafasi halisi ya noti kwenye sahani ya uchapishaji. Pia kuna namba ya sahani (plate number) inayotumika kutambua sahani iliyotumika kuchapisha noti hiyo.


Namba ya mfululizo (serial number) ni mchanganyiko wa herufi na tarakimu 11, na kila noti ina namba yake ya kipekee. Herufi ya kwanza lazima ifanane na ile ya muhuri wa Federal Reserve; ikiwa haifanani, kuna uwezekano noti hiyo ni bandia.


Mwaka wa toleo (series), kwa mfano 2009, hauonyeshi mwaka noti ilipochapishwa, bali ni mwaka ambao muundo huo ulianza kutumika. Mabadiliko hutokea pale kunapokuwa na mabadiliko kama kuteuliwa kwa Waziri mpya wa Fedha.


Muhuri wa Hazina ya Marekani pia upo upande wa mbele. Umebaki karibu sawa tangu 1789, ukiwa na mizani ya haki, ufunguo, na nyota 13. Muundo wa awali uliundwa na Francis Hopkinson.


Upande wa Nyuma wa Dola

Upande wa nyuma una alama muhimu sana, ikiwemo pande mbili za Muhuri Mkuu wa Marekani (Great Seal), pamoja na namba ya sahani ya uchapishaji.

Muhuri Mkuu wa Marekani (Great Seal)

Muhuri huu ulianzishwa na waanzilishi wa taifa la Marekani. Mnamo 1776, kabla ya Continental Congress kuvunjwa, kamati iliundwa yenye watu kama:

- John Adams

- Thomas Jefferson

- Benjamin Franklin

Lengo lao lilikuwa kubuni muhuri unaoonyesha maadili ya taifa jipya. Muundo wa mwisho uliidhinishwa miaka mitano baadaye, ukibuniwa na Charles Thomson.Great Seal

Upande wa mbele wa muhuri:

Una tai wa Marekani akiwa na Tawi la mzeituni (amani) Mishale (vita)

Kauli mbiu “E Pluribus Unum” (Kutoka wengi, kuwa mmoja)


Juu yake kuna nyota 13 zinazoashiria makoloni 13 ya awali. Mistari ya ngao pia ina maana ya umoja wa majimbo hayo.


Upande wa nyuma wa muhuri:

Una piramidi isiyokamilika yenye safu 13 za mawe, ikionyesha nguvu na uimara. Juu yake kuna jicho lenye mwanga (ishara ya ulinzi wa Mungu).


Maneno yaliyoandikwa ni:

- “Annuit Coeptis” (Mungu ameibariki juhudi yetu)

- “Novus Ordo Seclorum” (Mpangilio mpya wa zama)

Chini kuna namba za Kirumi (1776), kuashiria mwaka wa kuanzishwa kwa taifa.


Hitimisho.

Muundo wa dola 1 una maana nyingi na historia ndefu. Kila alama ina ujumbe wake maalum kuhusu umoja, nguvu, amani na mwanzo wa taifa la Marekani. Na jambo la kuvutia zaidi ni kwamba, kuna sheria inayozuia kubadilishwa kwa muundo wa noti ya dola 1 — hivyo utaendelea kubaki kama ulivyo kwa muda mrefu.

Thursday, April 9, 2026

MODULI YA RUFAA KUBORESHA MNYORORO WA UGAVI WAZINDULIWA

Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.
Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma. 

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema ujenzi wa moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST utachangia kuongeza uwajibikaji, uwazi na ufanisi kwenye mnyororo wa ugavi.

Katibu Mtendaji wa PPAA, James Sando amebainisha hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 na kuongeza kuwa Moduli hiyo imewaunganisha wazabuni wote na Taasisi nunuzi nchini ili kuongeza uwajibikaji katika utatuzi wa migogoro inayotokana na michakato ya ununuzi wa umma. 

“PPAA ni moja kati ya taasisi zinazosimamia ununuzi wa umma nchini, matumizi ya moduli hiyo katika mnyororo wa ugavi yatachangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati uliokusudiwa,” amesema Sando.

Pamoja na mambo mengine, Sando amebainisha kuwa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma yatasaidia kuongeza uwazi, kupunguza gharama, kuokoa muda, utunzaji wa nyaraka na hivyo kuongeza ufanisi katika hukumu zinazotolewa kutokana na michakato mbalimbali ya zabuni za umma.

Sando ameongeza kuwa, PPAA imefanikiwa kushiriki katika utungwaji wa Sera ya Taifa ya Mnyororo wa Ugavi, Sheria ya Ununuzi wa Umma, Kanunuzi za Ununuzi wa Umma na Kanuni za Rufaa za Ununuzi wa Umma ambapo yote ni michango wa Mamlaka ya Rufani katika mnyororo wa ugavi.

Kadhalika, Mamlaka ya Rufani inatarajia kuboresha kipengele cha makundi maalum na vijana ambapo inategemea kuboresha gharama au tozo za kesi kwa makundi maalum pamoja na kuelekeza nguvu kwa vijana na kuhakikisha wanapata fursa ya kudai haki zao katika michakato ya ununuzi wa umma.

Awali akizindua Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba amezielekeza mamlaka, taasisi na wadau wote wanaosimamia utekelezaji wa Sera hiyo kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora, uwazi na utawala wa sheria.‎

‎Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo wakati akizundua Sera hiyo kwa niaba ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Dk. Nchemba amesema changamoto zinazoikumba sekta ya ununuzi wa umma hazitokani na sera au sheria zilizopo, bali ni uzembe na mitazamo ya baadhi ya watendaji.‎

‎Ameongeza kuwa taarifa za ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zinaonesha wazi kuwa kasoro nyingi zinasababishwa na utekelezaji dhaifu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

“Sehemu kubwa ya changamoto hizo zinatokana na hulka, tabia na mitazamo ya watendaji. Hivyo, ni lazima tubadilike ili kufikia malengo ya sera hii,” amesisitiza Dk. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu, amezitaka wizara, taasisi na mamlaka zote kufanya mapitio ya sera, sheria na kanuni zinazokinzana na sera hiyo ili kuweka mazingira rafiki ya utekelezaji wake.

Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar amesema sera hiyo ni mwongozo muhimu utakaosaidia kuimarisha mifumo ya ugavi katika sekta ya umma, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kudhibiti vitendo vya rushwa.‎

Balozi Khamis ameongeza kuwa utekelezaji wa sera hiyo utaongeza ajira, kuimarisha mnyororo wa thamani na kuchochea mageuzi makubwa ya kiuchumi kuelekea dira ya maendeleo ya mwaka 2050.


Sehemu ya viongozi mbalimbali walioshiriki katika uzinduzi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), wakati alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), (Katikati Kulia), akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na viongozi wengine wakisikiliza maelezo kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Bw. James Sando (kushoto), kuhusu mchango wa PPAA katika Mnyororo wa Ugavi, wakati Mhe. Waziri Mkuu alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.

SIMBA SC NAYO YACHANGIA MAPATO KWA TRA UNITED ARUSHA, ZATOKA SULUHU

 


TIMU ya Simba SC imetoa sare ya bila mabao na wenyeji, TRA United katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha. 

Kwa matokeo hayo, TRA inayofundishwa na Kocha Mrundi, Ettienne Ndayiragijje inafikisha pointi 24 na kupanda kwa nafasi moja hadi ya saba ikiizidi tu wastani wa mabao Dodoma Joni FC baada ya wote kucheza mechi 18. 

Kwa upande wao Simba SC wanafikisha pointi 36 katika mchezo wa 17, ingawa wanabaki nafasi ya pili wakizidiwa pointi nane na mabingwa watetezi, Yanga ambao hata hivyo wamecheza mechi moja zaidi.




AZAM FC YALAZIMISHWA SARE V/s MBEYA CITY

 


TIMU ya Azam FC imelazimishwa sare ya bila kufungana na wenyeji, Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, Babati mkoani Manyara.

Kwa matokeo hayo, Azam FC inafikisha pointi 34 katika mchezo wa 18, ikibaki nafasi ya tatu, wakati Mbeya City inafikisha pointi 17 katika mchezo wa 18 pia, nayo ikibaki nafasi ya 12 kwenye Ligi Kuu inayoshirikisha timu 16.

Ikumbukwe mwisho wa msimu timu mbili zitashuka Daraja na mbili zitakazomaliza nafasi ya 14 na 13 zitamenyana baina yao kwa mechi mbili za nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla atasalia Ligi Kuu.

Timu itakayofungwa itakwenda kumenyana na timu kutoka Ligi ya Championship katika mechi nyingine mbili za mchujo nyumbani na ugenini na mshindi wa jumla ndiye atacheza Ligi Kuu msimu ujao.