 |
| Eneo la Strait Hormuz |
Vita inayoendelea Mashariki ya Kati, iliyoanzishwa na Marekani pamoja na mshirika wake Isarel, dhidi ya Iran, tayari wachumi wametaja athari za mapema zitakazoanza kushuhudiwa barani Afrika.
Miongoni mwaka ni nishati ya mafuta. Kwa siku takribani mapipa ya mafuta milioni 20 hupita katika korido ya mlango wa ‘Strait of Hormuz’. Huo ni mlango mwembamba wa bahari unaounganisha Ghuba ya Persian na Ghuba ya Oman.
Kwa mujibu wa ukurasa Firstpost mtandao wa instagram, unaeleza hayo na kwamba hali hiyo inatokana na kukosekana kwa hali ya kiusalama kutokana na vita hivyo, kwa sasa usafirishaji huo utasitishwa.
Athari za kukosekana kwa nishati hiyo, mchambuzi wa kupitia mtandao huo anasema, kwa Afrika, gharama za maisha zitapanda, ikiwamo bei za vyakula.
Kinachoendelea sasa si mzozo mwingine tu wa kawaida katika eneo la Asia Magharibi, bali ni mshtuko wa moja kwa moja kwa uchumi wa dunia.
Katikati ya yote haya eneo hilo ni muhimu na Mlango wa Bahari wa uitwao ‘Hormuz’. Ni njia nyembamba ya baharini kati ya Iran na Oman, ambako karibu theluthi moja ya tano ya mafuta ya dunia hupita.
Baada ya mashambulizi mapya ya Marekani na Israel, pamoja na hatua za kulipiza kisasi za Iran, inaripotiwa kuwa baadhi ya meli zilipokea maonyo ya redio yakidai kuwa upitishaji unaweza kuzuiwa.
Hakuna tangazo rasmi la kufungwa kwa njia hiyo, lakini masoko hayasubiri taratibu za kisheria.
Bei za mafuta zinaanza kupanda, kampuni za bima zinaongeza gharama za bima ya hatari ya vita, na maamuzi ya usafirishaji kwa njia ya meli yanasimama kwa tahadhari. Iran imekwishafunga mlango huo muhimu.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Uingereza Reuters, Umoja wa Ulaya (EU), meli zake zimekuwa zikipokea ujumbe kutoka Jeshi la Iran, likisema hakuna meli inayoruhusiwa kupita katika Mlango wa Bahari wa Hormuz.
Mlango huu ni njia muhimu ya kusafirisha mafuta duniani, takribani mapipa milioni 20 ya mafuta kwa siku hupitia, yakiwakilisha asilimia 20-25 ya biashara ya mafuta ya baharini duniani na moja ya tano ya matumizi ya mafuta duniani.
ATHARI ZA AWALI
Kuongezeka kwa mapigano kunahatarisha kuharibu zaidi utulivu wa dunia, Mashariki ya Kati kuna athari kubwa kwa biashara ya nishati, usalama wa chakula na uchumi, hasa barani Afrika, ambako migogoro na misukosuko ya kiuchumi bado ni mikali.
Umoja wa Afrika (AU), baada ya taarifa Israel na Marekani kuanzisha mashambulio dhidi ya Iran, umezitaka pande zinazopigana kujizuia, kupunguza mvutano na kuendelea na mazungumzo
Athari hizo kwa Afrika, pia ziliguswa na mgogoro wa Russia na Ukraine miezi ya mwanzoni mwaka 2022.
Afrika ilianza kuona makali ya vita hivyo baada kutokea mgogoro wa chakula, ikiwamo kupanda kwa gharama ya chakula hasa ngano na mafuta.
Katika ripoti ya Shirika la Fedha Duniani (IMF) iliyochapishwa Aprili mwaka huo, ilisema, baadhi ya mataifa ambayo yanaathirika moja kwa moja na vita vya Ukraine kwa kutegemea uagizwaji wa ngano kutoka nchi hiyo na Russia kwa asililia 85 ni pamoja na Tanzania, Ivory Coast, Senegal na Msumbiji.
Haikuwa Afrika pekee, dunia nzima iliona makali ya vita hivyo ambavyo bado vinaendelea. Ni kutokana na ukweli kwamba hadi vita vinaanza, Russia ndiyo nchi inayoongoza katika mauzo ya ngano duniani ikifuatiwa na Ukraine.
Bei ya mafuta inatarajiwa kupanda kwa kasi siku ya Jumatatu licha ya ahadi ya nchi kubwa zinazozalisha mafuta kuongeza uzalishaji, huku vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran pamoja na kufungwa kwa vitendo kwa Mlango wa Bahari wa Hormuz vikitetemesha wawekezaji.
Mafuta ghafi ya Marekani yanatarajiwa kupanda kwa karibu asilimia tisa biashara itakaporejea, kulingana na takwimu za dalali IG.
Ongezeko hilo linakuja licha ya kundi la wazalishaji mafuta la OPEC+ kukubaliana Jumapili kuongeza uzalishaji kwa kiwango kikubwa zaidi ya ilivyotarajiwa ili kupunguza athari za mzozo.
Walinda Mapinduzi wa Iran (Revolutionary Guards) wanaripotiwa kuziambia meli kwamba kupita katika
Meli moja ya mafuta ilishambuliwa Jumapili leo katika mlango huo na angalau meli 150 zilizobeba mafuta ghafi, gesi asilia iliyoyeyushwa (LNG) na bidhaa za mafuta zilisimamisha safari na kutia nanga katika maji ya wazi katika Ghuba ya Mashariki ya Kati, kulingana na Reuters.
Tehran imekuwa ikionya kwa muda mrefu kwamba inaweza kutumia nafasi yake ya kijiografia kuufunga mlango huo kujibu uchokozi wa kijeshi.
Tamsin Hunt, mchambuzi mwandamizi wa kampuni ya ujasusi na usalama wa mtandao ya S-RM, alisema kufunga kabisa njia hiyo “kungedhoofisha sana uchumi wa Iran yenyewe.”
Masoko ya wikendi ya IG yanaonesha kuwa mafuta ghafi ya Marekani yanaweza kupanda hadi zaidi ya dola 73 kwa pipa biashara itakaporejea New York, kutoka dola 67 Ijumaa usiku, kiwango cha juu zaidi tangu Juni 2025 wakati Marekani ilipoanzisha mashambulizi dhidi ya vituo vya nyuklia vya Iran.
Wachambuzi wa Barclays walisema bei ya mafuta inaweza kufikia dola 80 kwa pipa endapo kutakuwa na “usumbufu mkubwa wa usambazaji.” Nao wachambuzi wa Royal Bank of Canada walionya kuwa mafuta ya zaidi ya dola 100 kwa pipa ni hatari halisi iwapo mzozo utaongezeka.
Kupanda kwa bei ya jumla ya mafuta kunatarajiwa kuathiri bei za rejareja. Bei ya wastani ya petroli nchini Uingereza ni pensi 132.9 kwa lita na dizeli 142.4p, kulingana na The AA, ambayo imeonya kuwa athari za Iran zinaweza kuungana na mpango wa serikali kurejesha ushuru wa mafuta wa 5p kwa lita na hivyo kuongeza bei zaidi.
Katika soko la London, faharasa ya FTSE 100 inatarajiwa kushuka kwa karibu asilimia 0.5, Jumatatu asubuhi baada ya kufikia rekodi Ijumaa.
Wawekezaji duniani wanatarajiwa kukimbilia mali salama. Dhahabu, ambayo imepanda kwa wiki nne mfululizo, imeongezeka kwa asilimia 2.25 hadi karibu dola 5,400 kwa wakia katika masoko ya wikendi ya IG, huku fedha (silver) nayo ikipanda kwa 3.2.
Nchi nane za OPEC+ zilikubaliana kimsingi kuongeza uzalishaji kwa mapipa 206,000 kwa siku mwezi April, zaidi ya matarajio ya awali ya mapipa 137,000.
Kampuni ya bandari ya DP World imesimamisha shughuli katika Bandari ya Jebel Ali, Dubai na kampuni ya Mediterranean Shipping Company imesitisha upokeaji wa mizigo inayoelekezwa Mashariki ya Kati hadi itakapotangazwa vinginevyo.
Gharama za bima ya meli katika eneo hilo zimeongezeka, kulingana na Dylan Mortimer wa kampuni ya usimamizi wa hatari ya Marsh, akionya kuwa hatari kuu ni pamoja na kukamatwa kwa meli na vikosi vya Iran na uwezekano wa kufungwa kwa Mlango wa Hormuz.
Masoko mengi ya hisa katika eneo la Ghuba yalishuka Jumapili. Soko la Saudi Arabia lilipoteza asilimia 2.5, ingawa hisa za Saudi Aramco zilipanda kwa 2.5 kufuatia matarajio ya kupanda kwa bei ya mafuta ghafi. Soko la hisa la Kuwait lilisimamisha biashara hadi itakapotangazwa tena, likitaja “hali za kipekee” zinazoikabili nchi hiyo.
KUUAWA KIONGOZI IRAN
Taarifa kutoka Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, vyombo kadhaa vya habari vya serikali nchini Iran vilithibitisha kifo cha Ayatollah Khamenei, jana.
Rais wa Marekani, Donald Trump saa chache zilizopita alisema Kiongozi Mkuu huyo aliuawa wakati wa shambulio la pamoja na Israel katika maeneo kadhaa kote Iran.
Katika taarifa hiyo, haikutajwa ni jinsi gani Khamenei mwenye umri wa miaka 86 alivyofariki, au ni nani anayeweza kuchukua nafasi ya kiongozi.
Jamaa wa Khamenei pia wameuawa katika mashambulizi hayo
Hapo awali, vyombo vya habari vya serikali vilisema kwamba binti wa Khamenei, mkwewe na mjukuu wake pia waliuawa katika mashambulizi hayo.
Kulingana na Shirika la Habari la Fars, ambalo lina uhusiano na Kikosi cha Revolutionary Guard, kuna ripoti kwamba mmoja wa mabinti wa Khamenei ameuawa pia.