Iran ilitangaza hadharani Jumatano kile ilichodai kuwa ni mfumo wa vipengele 10 kwa ajili ya mazungumzo, ambao Rais Trump aliuelezea kama “msingi unaoweza kufanyiwa mazungumzo” ili kumaliza vita. Sehemu kubwa ya vipengele hivyo ilijumuisha madai ya juu sana ambayo yanaonekana kuwa magumu, kama siyo yasiyowezekana, kupatanishwa na malengo ya Marekani.
Afisa mmoja wa Ikulu ya White House alisema vipengele hivyo haviendani na kile alichokuwa anakimaanisha Trump. Afisa huyo alizungumza kwa sharti la kutotajwa jina ili kujadili mazungumzo ya ndani ya White House.
Iran ilitoa toleo lake la pendekezo hilo asubuhi baada ya Marekani na Iran kukubaliana kusitisha mapigano kwa wiki mbili, na linataka wanajeshi wa Marekani kuondoka katika eneo hilo, linarejesha msisitizo wa udhibiti wa Iran juu ya Mlango wa Hormuz wenye umuhimu wa kimkakati, na linadumisha haki ya Iran ya kurutubisha nyuklia.
Mengi ya madai hayo yana uwezekano mkubwa wa kugongana na pendekezo la vipengele 15 lililotolewa na wapatanishi wa Marekani mwezi uliopita.
Pendekezo hilo halikuwahi kuwekwa hadharani, lakini maafisa waliopata taarifa zake, waliozungumza na gazeti la The New York Times kwa sharti la kutotajwa majina kutokana na unyeti wa taarifa, walisema lilihusu programu ya makombora ya balestiki ya Iran na mpango wake wa nyuklia, pamoja na biashara ya baharini. Katika mazungumzo ya awali, wapatanishi wa Marekani walisisitiza kupunguza umbali wa makombora ya balestiki ya Iran na kusitisha kabisa urutubishaji wa nyuklia.
Trump alionekana kurejea mpango huo wa Marekani siku ya Jumatano, akiandika kwenye mitandao ya kijamii kuwa “vipengele vingi kati ya vile 15 tayari vimekubaliwa,” na kurudia msimamo wake wa “kutokuwepo kabisa kwa urutubishaji wa urani.”
MASHARTI 10 YA IRAN AMBAYO NI MWIBA KWA MAREKANI
1. Dhamana ya Marekani ya kutofanya uchokozi dhidi ya IranKatika pendekezo la awali la vipengele 15 kutoka kwa wapatanishi wa Marekani, kulikuwa na pendekezo la kusitisha mapigano tu. Maafisa wa Iran wanataka kuhakikisha kuna mwisho rasmi na wa kudumu zaidi wa uhasama.
Hili ni moja ya madai makuu ambayo Iran inalenga kulipa kipaumbele.
2. Iran kudumisha udhibiti wa Mlango wa Hormuz
Hili linaweza kuwa suala gumu sana kufikiwa mwafaka. Uwezo wa Iran kudhibiti au kuzuia usafiri wa meli katika mlango huo, ambako hupita takriban theluthi moja ya mafuta ya dunia, umekuwa ukitikisa uchumi wa dunia. Ni vigumu sana kwa Marekani au nchi za Kiarabu za Ghuba kukubali hilo.
3. Kumaliza vita vya kikanda katika nyanja zote, ikiwemo dhidi ya mshirika wa Iran, Hezbollah nchini Lebanon
Hili linaweza kuwa eneo la kufikia muafaka baadaye.
Marekani na Israel zinataka Tehran kudhibiti mtandao wa makundi ya wanamgambo inayounga mkono katika eneo hilo, unaoitwa “Axis of Resistance.” Baadhi ya makundi hayo yameishambulia Marekani, nchi za Ghuba na Israel kwa kutumia ndege zisizo na rubani na makombora.
Miongoni mwao ni Hezbollah ya Lebanon, ambayo ilishambuliwa vikali na Israel, ambayo baadaye ilitangaza mipango ya kukalia sehemu za kusini mwa Lebanon.
Israel imesema usitishaji wa mapigano hauhusu operesheni zake nchini Lebanon, hivyo bado haijulikani kama suala hilo linaweza kuingizwa kwenye makubaliano ya muda mrefu.
4. Kuondolewa kwa majeshi ya Marekani katika vituo vyote vya kijeshi katika eneo hilo
Marekani ina vituo vya kijeshi katika nchi za Ghuba, Israel na Iraq. Ni vigumu kufikiria hali ambayo Marekani itakubali sharti hili.
5. Fidia kwa Iran kutokana na uharibifu wa vita
Iran imepata uharibifu mkubwa, si tu kwenye maeneo ya kijeshi bali pia miundombinu muhimu kama viwanda vya dawa, chuma, madaraja, vyuo vikuu na nishati.
Hakuna dalili kwamba Marekani iko tayari kulipa fidia hiyo.
6. Kutambuliwa kwa haki ya Iran ya kurutubisha nyuklia
Hili linapingana kabisa na msimamo wa Trump, ambaye amesisitiza kutokuwepo kabisa kwa urutubishaji wa urani.
Baadhi ya wanadiplomasia wa kikanda wamependekeza Iran iruhusiwe urutubishaji mdogo sana kwa matumizi ya kiraia, lakini bado haijulikani kama Marekani itakubali.
7. Kuondolewa kwa vikwazo vya moja kwa moja (primary sanctions)
Marekani imeweka vikwazo mbalimbali vya kifedha dhidi ya Iran tangu mapinduzi ya mwaka 1979.
Katika mazungumzo ya awali, kulikuwa na wazo la kuondoa baadhi ya vikwazo hivyo badala ya Iran kufanya mabadiliko kwenye mpango wake wa nyuklia. Trump pia aligusia uwezekano wa kupunguza ushuru na vikwazo.
8. Kuondolewa kwa vikwazo vya sekondari (secondary sanctions)
Hivi ni vikwazo vinavyolenga pia nchi au kampuni nyingine zinazofanya biashara na Iran.
Kipengele hiki kinaweza kujadiliwa kulingana na makubaliano yatakayofikiwa.
9. Kufutwa kwa maazimio yote dhidi ya Iran na Bodi ya Magavana ya Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA)
Mwaka jana, shirika hilo lilipitisha azimio dhidi ya Iran likidai haitekelezi wajibu wake wa kudhibiti usambazaji wa silaha za nyuklia. Iran ililaani hatua hiyo kama ya kisiasa.
Marekani haiwezi kulazimisha kufutwa kwa maazimio hayo moja kwa moja, lakini inaweza kushawishi washirika wake.
10. Kufutwa kwa maazimio yote ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa dhidi ya Iran
Kumekuwa na maazimio kadhaa dhidi ya Iran, hasa kuhusu nyuklia. Mwaka uliopita, Umoja wa Mataifa ulirejesha vikwazo dhidi ya Iran kwa kukiuka makubaliano ya mwaka 2015.
Marekani inaweza kujaribu kushawishi washirika wake, lakini hilo litahitaji makubaliano mapana zaidi na Iran.