ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, May 8, 2026

WAZIRI MCHENGERWA ALIVYOIKOMALIA VITA YA SERIKALI DHIDI YA VIFO VYA MAMA NA MTOTO NCHINI TANZANIA

 NA ALBERT G.SENGO/MWANZA

Afya ya mama na mtoto ndiyo msingi wa taifa lenye nguvu. Kila maisha yanayopotea wakati wa ujauzito, kujifungua au baada ya kujifungua ni kengele inayotukumbusha wajibu wetu kama jamii na wataalam wa afya. Ndiyo maana vikao vya mara kwa mara kwa wahudumu na wataalam wa afya vinaendelea kuwa silaha muhimu katika kupunguza vifo vya mama na mtoto nchini Tanzania. Leo tunaangazia sababu 10 zinazoonesha kwa nini mikutano hii ya kitaalam ni muhimu katika kuokoa maisha, kuboresha huduma na kujenga kizazi salama kwa taifa letu. Moja kati ya sababu hizo ni pamoja na kuhuisha maarifa na miongozo ya tiba Sekta ya afya hubadilika mara kwa mara kutokana na tafiti na maboresho ya kitabibu. Vikao huwasaidia wahudumu wa afya kuendelea kutumia mbinu sahihi za kuhudumia wajawazito, wajifungua na watoto wachanga. 2. Kupunguza makosa ya kitabibu Kukumbushana wajibu, taratibu na tahadhari muhimu husaidia kupunguza uzembe, kuchelewa kutoa huduma au maamuzi yasiyo sahihi ambayo yanaweza kusababisha vifo. 3. Kuimarisha huduma za dharura za uzazi Kupitia vikao, wahudumu hukumbushwa namna ya kushughulikia haraka changamoto kama kutokwa damu nyingi, kifafa cha mimba, uchungu wa muda mrefu na matatizo ya mtoto mchanga. 4. Kujenga ushirikiano wa timu Huduma za mama na mtoto zinahitaji ushirikiano wa madaktari, wauguzi, wakunga, maabara na famasia. Vikao huongeza mawasiliano mazuri na mshikamano kazini. 5. Kuchambua sababu za vifo vilivyotokea Kupitia tathmini za vifo vya mama na mtoto, wataalam hujifunza makosa yaliyotokea ili yasijirudie tena katika vituo vingine vya afya. 6. Kuongeza uwajibikaji kazini Vikao huwafanya wahudumu wa afya kukumbuka kuwa maisha ya wananchi yako mikononi mwao hivyo kuwajibika zaidi katika utoaji wa huduma. 7. Kuboresha huduma kwa wananchi Elimu na ukumbusho wa mara kwa mara huwasaidia wahudumu kutoa huduma zenye utu, upendo na kuwahudumia wajawazito kwa haraka na usalama zaidi. 8. Kusaidia kufikia malengo ya taifa na dunia Tanzania inaendelea kupambana kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa mujibu wa malengo ya maendeleo endelevu (SDGs). Vikao ni sehemu muhimu ya kufanikisha azma hiyo. 9. Kuibua changamoto za vifaa na mazingira ya kazi Kupitia mikutano, wahudumu hupata nafasi ya kueleza changamoto kama uhaba wa dawa, damu salama, vitanda au watumishi ili hatua zichukuliwe mapema. 10. Kujenga moyo wa kujituma na kupeana hamasa Wataalam wanapokutana mara kwa mara hupata hamasa mpya, kubadilishana uzoefu na kuendelea kufanya kazi kwa ari ya kuokoa maisha ya mama na mtoto.

WAZIRI MKUU ATAKA WATENDAJI SERIKALINI WATUMIE USHAWISHI BADALA YA UDHIBITI KWA WAWEKEZAJI


_Azindua Hoteli ya Mikumi Wildlife

_Asema Serikali imetoa sh. bilioni 35 kuboresha uwanja wa Kikoboga, Mikumi

Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amewataka watendaji katika taasisi na mamlaka za Serikali wawe tayari kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti ili wavutiwe kuwekeza zaidi na zaidi.


“Nitoe wito kwa taasisi na mamlaka za Serikali, tumieni muda mwingi kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti. Washawishini waongeze uwekezaji badala ya kuwafanya waonekane wanaomba. Tumieni vivutio zaidi ili washawishike zaidi na zaidi,” amesema.


Ametoa wito huo leo (Ijumaa, Mei 8, 2026) wakati akizungumza na wadau waliohudhuria uzinduzi wa hoteli ya Mikumi Wildlife katika Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, wilayani Kilosa, mkoani Morogoro.

Amesema hoteli hiyo ambayo zamani ilikuwa inamilikiwa na serikali lakini ikapata janga la kuungua moto, ina historia ya miaka mingi; na ana imani na uwekezaji uliofanyika kwani umesaidia kuongeza ajira na kipato kwa wananchi.


“Sina shaka uwekezaji huu utaongeza mvuto kutokana na viwango vilivyopo kwenye hoteli hii. Viwango vya hoteli hii ni vya juu sana, ninaamini vitasaidia kuongeza muda wa watalii kukaa ndani ya hifadhi na uwepo wa malazi mazuri pia utaongeza idadi ya watalii,” amesema.


Akielezea juhudi za serikali kuboresha hifadhi ya Mikumi, Waziri Mkuu amesema Serikali imetoa sh. bilioni 35 za kuboresha uwanja wa ndege wa Kikoboga na ifikapo Oktoba mwaka huu, utakuwa umekamilika.


Amezitaka Wizara ya Maliasili na Utalii, TANAPA washirikiane na mamlaka nyingine za Serikali na kutumia fursa ya stesheni ya Kilosa ili kufungua njia na kuboresha miundombinu itakayorahisisha watalii kuingia katika Hifadhi ya Mikumi na hivyo kuongeza idadi ya watalii.


Ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii iendelee kubuni mikakati ya kwa kuhamasisha sekta binafsi iwekeza katika maeneo ya utalii huku akizitaka taasisi zote za umma ikiwa ni pamoja na mikoa yenye maeneo yaliyo na fursa za utalii ziendelee kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi. “Suala hili litekelezwe sambamba na kutangaza vivutio vilivyopo.”


Waziri Mkuu amewataka wadau wa utalii waweke mipango ya kuendeleza mazao mapya ya utalii yatakayochochea ongezeko la watalii na kuwahamasisha kuchagua kutembelea vivutio vilivyopo katika Kanda ya Utalii Kusini.


Ametumia fursa hiyo kumwelekeza Waziri wa Maliasili na Utalii aangalie namna ya kuongeza programu za utalii kwenye Chuo cha Ufundi (VETA) kilichopo Mikumi. “Waziri wa Utalii tuongeze programu nyingi za utalii ili vijana wa hapa wanufaike na rasilimali zilizopo katika eneo lao. Kwa maono ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, alitaka hivi vyuo vinapojengwa viweke programu kulingana na shughuli za kiuchumi za eneo husika kama vile utalii, uvuvi ili viwasaidie vijana wa maeneo husika.”


Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji alisema miaka ya nyuma hifadhi ya Mikumi ilikuwa ikipokea watalii 60,000 kwa mwaka lakini mwaka jana idadi ya watalii iliongezeka sana kufikia 174,808.


“Mapato yanayotokana na utalii yalikuwa sh. milioni 2.5 lakini nayo kwa mwaka jana yaliongezeka na kufikia sh.milioni 9.81. Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026 idadi ya watalii waliofika kwenye hifadhi ya Taifa ya Mikumi walikuwa 151,275 na mapato yaliyokusanywa yalikuwa yamefikia sh. milioni 10.12,” alisema.


Alisema tayari sh. bilioni nne za kujenga geti upande wa Kilosa zimeshatolewa na ziko hifadhini tayari kuanza kazi hiyo ambapo mtu akishuka Kilosa kwa treni ya SGR atatumia dk.20 tu kuingia hifadhini.


Naye Bw. Simon Nguka, akisoma taarifa kuhusu mradi huo, alisema ujenzi na ukarabati wa hoteli hiyo yenye vyumba 48 na ambayo inamilikiwa na Watanzania kwa asilimia 100, umetumia sh. bilioni 26.8.


Alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi 24 waliyonayo. Wellworth Group inamiliki mahoteli, loji, resorts na kambi za kitalii zenye uwekezaji wa thamani ya sh. bilioni 640.




Monday, May 4, 2026

SERIKALI KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA TAASISI ZA DINI KUIMARISHA AMANI NA MAADILI NCHINI

▪️︎ Asema dini ni nguzo muhimu ya malezi na mshikamano wa Taifa

▪️︎ Asisitiza jamii kuendelea kuombea na kulinda amani ya nchi


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za dini nchini ili kuimarisha maadili, mshikamano wa kijamii na kudumisha amani ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya Taifa.


Amesema hayo leo Jumapili, Mei 3, 2026, aliposhiriki ibada katika Kanisa Kuu la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mufindi, lililopo Mafinga Mjini, mkoani Iringa.

FT: SIMBA 2 - 2 YANGA

 A

Dabi ya Kariakoo kati ya Simba na Yanga nchini Tanzania imeendelea kuthibitisha ukubwa wake, safari hii ikichezwa katika mazingira ya kipekee, kwenye uwanja wa kambini ama jeshini, Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.

Sare ya mabao 2-2 haikuwa tu matokeo, bali ilikuwa picha halisi ya ushindani, ubora na presha ya mechi kubwa. Simba walianza kwa kasi na dhamira ya wazi ya kutawala mchezo mapema. Mabao ya Libasse Gueye na Clatous Chama yaliwapa faida ya mapema na kuonyesha mpango wao wa kushambulia kwa nguvu.

Lakini Yanga walirejea kwa utulivu na uzoefu. Kupitia Prince Dube na nahodha Bakari Mwamnyeto, walionyesha uthabiti na kupambana hadi dakika ya mwisho, japo matokeo yalisalia kuwa sare.

Sare hiyo inaacha pengo la alama tano likiendelea kuwepo, lakini zaidi ya hilo, imeacha mjadala mpana kuhusu kiwango cha dabi, mazingira ya mchezo na mchango wa wachezaji binafsi. 

Sunday, May 3, 2026

SERIKALI KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA TAASISI ZA DINI KUIMARISHA AMANI NA MAADILI NCHINI


▪️︎ Asema dini ni nguzo muhimu ya malezi na mshikamano wa Taifa

▪️︎ Asisitiza jamii kuendelea kuombea na kulinda amani ya nchi


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za dini nchini ili kuimarisha maadili, mshikamano wa kijamii na kudumisha amani ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya Taifa.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 3, 2026, aliposhiriki ibada katika Kanisa Kuu la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mufindi, lililopo Mafinga Mjini, mkoani Iringa.


Akizungumza na waumini, Dkt. Nchemba amesema taasisi za dini zina mchango mkubwa katika kujenga jamii yenye maadili mema, inayozingatia misingi ya haki na uwajibikaji.


“Serikali inaendelea kusisitiza Watanzania wote kuwa wadau wa kuombea na kusimamia amani ya nchi yetu,” amesema.


Ameongeza kuwa mafanikio ya mipango ya maendeleo ya Taifa yanategemea uwepo wa amani.


“Pasipokuwa na amani, hata malengo binafsi ya mtu mmoja mmoja ya Mtanzania mmoja mmoja hayawezi kufikiwa,” amesema.


Waziri Mkuu pia ameeleza mabadiliko ya mazingira ya dunia na changamoto zinazoweza kujitokeza.


“Kuna aina mpya ya mapambano, na mapambano hayo ni ya rasilimali na kila palipo na rasilimali mara nyingi huwa kunavutia maadui na hupenda kupitia migawanyiko ya raia wa nchi hizo husika,” amesema.


Katika hatua nyingine, amepongeza juhudi za Kanisa katika malezi ya watoto na vijana.


“Maandalizi ya watoto hivi si tu manufaa kwa Kanisa, ni manufaa pia kwa Taifa tunalolitaka,” amesema.


Kwa upande wake, Askofu wa KKKT Dayosisi ya Mufindi, Dkt. Anthony Kipangula, ameipongeza Serikali kwa kazi ya kuwahudumia wananchi na kusisitiza kuwa ziara za Waziri Mkuu zimeonesha uongozi unaowagusa wananchi moja kwa moja.


“Nimeona juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuwajali wananchi mtu wa ngazi yako kushuka mpaka kusikiliza kesi ya mwananchi na kumruhusu ajieleze, niliona ni maajabu kabisa,” amesema.



Ameongeza kuwa Kanisa litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha maadili mema, kutoa ushauri na kuliombea Taifa ili kudumisha amani na ustawi wa jamii.




Friday, May 1, 2026

DKT. MWIGULU ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI NJOMBE


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 1, 2026, ameshiriki Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) yaliyofanyika mkoani Njombe.

Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.


Akizungumza katika maadhimisho hayo, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ametoa wito kwa wafanyakazi wote nchini kuwa wavumilivu na kuto kata tamaa katika majukumu yao ya kazi ili kufikia mafanikio ya pamoja.


Kadhalika, Dkt. Mwigulu amewaasa waajiri kujenga mazingira chanya yatakayowafanya wafanyakazi wajisikie kuthaminiwa, jambo linalosaidia kuongeza mshikamano na ustahimilivu wa kiutendaji.


Kaulimbiu ya maadhimisho hayo ilikuwa: “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050.”




Thursday, April 30, 2026

Tanzia : MWANDISHI WA HABARI EDITHA KARLO AFARIKI DUNIA

 



Mwandishi wa habari wa mkoa wa Kigoma, Editha Karlo, amefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mfupi.

Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na Kaimu Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari mkoa wa Kigoma, Jacob Ruvilo, aliyesema kuwa marehemu alifariki Jumatano mchana Aprili 28,2026 akiwa nyumbani kwao wilayani Kasulu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kabla ya umauti wake marehemu alikuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Kifo cha Editha Karlo ni pigo kwa familia, ndugu, marafiki na tasnia ya habari mkoani Kigoma na nchini kwa ujumla.

R.I.P Editha

Wednesday, April 29, 2026

NI YANGA DHIDI YA SIMBA KOMBE LA MUUNGANO 2026

 


Michuano ya Muungano Cup 2026 inafikia tamati leo kwa mchezo wa Fainali kupigwa katika dimba la New Amaan.


Ni Yanga SC dhidi ya Simba SC.


Mechi hii itachezwa kuanzia saa 2:15 usiku na kuruka mbashara AzamSports1HD.


Je, Yanga SC ambae ni bingwa mtetezi atalitetea Kombe ama kuvuliwa Ubingwa na Mnyama?


#MuunganoCup

Monday, April 27, 2026

SIKU YA UHURU WA AFRIKA KUSINI.

 


Kwa niaba ya Serikali na wananchi wa Jamhuri ya Afrika Kusini, napenda kutoa salamu za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Serikali na wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, raia wa Afrika Kusini wanaoishi Tanzania, makampuni ya Afrika Kusini, pamoja na washirika na marafiki wetu wa Kitanzania tunapoadhimisha Siku ya Uhuru wa Afrika Kusini tarehe 27 Aprili 2026.

Mwaka huu inatimia miaka 32 tangu Waafrika Kusini walipotumia haki yao ya kidemokrasia kupiga kura kwa uhuru kwa mara ya kwanza mwaka 1994, hatua iliyofungua enzi mpya iliyojengwa juu ya utu, usawa, kutokuwepo kwa ubaguzi wa rangi, kutokuwepo kwa ubaguzi wa kijinsia, na utawala wa sheria. Siku ya Uhuru inaendelea kuwa kumbukumbu muhimu ya kujitoa mhanga kwa wale waliopigania ukombozi na haki, na kwa ajili ya Afrika Kusini ya kidemokrasia inayowahusu wote wanaoishi ndani yake.

Mwaka huu pia inatimia miaka 30 tangu Mahakama ya Katiba ilipoidhinisha Katiba tarehe 4 Desemba 1996, mafanikio makubwa yaliyoweka msingi wa dola ya kidemokrasia inayozingatia utu wa binadamu, usawa na uhuru. Katiba inaendelea kuwa sheria kuu ya Jamhuri yetu na nguzo muhimu katika kukuza utawala unaowajibika, kulinda haki za msingi, na kuimarisha taasisi za kidemokrasia.

Tunapoadhimisha tukio hili muhimu hapa Tanzania, tunafanya hivyo kwa kuthamini kwa kina uhusiano wa kihistoria na wa kudumu kati ya mataifa yetu mawili. Tanzania ilichangia kwa kiasi kikubwa katika mapambano ya ukombozi ya Afrika Kusini kwa kuunga mkono harakati za ukombozi na kuonesha mshikamano wakati wa nyakati ngumu. Historia hiyo ya pamoja inaendelea kuunda uhusiano unaojengwa juu ya heshima ya pande zote, Uafrika (Pan-Africanism), na dhamira ya pamoja ya amani, maendeleo na ustawi.

Leo, Afrika Kusini na Tanzania zinafurahia ushirikiano imara katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni, pamoja na mahusiano ya watu kwa watu, unaoonesha maono ya pamoja ya umoja wa Afrika, ushirikiano wa kikanda, na ukuaji jumuishi. Afrika Kusini inaendelea kujitolea kufanya kazi kwa karibu na Tanzania ili kuimarisha zaidi uhusiano wa pande mbili na kuchangia kwa maana katika Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika pamoja na ajenda ya maendeleo ya kimataifa.

Ninatoa shukrani zangu za dhati kwa wenyeji wetu, washirika wetu, na jamii ya Waafrika Kusini nchini Tanzania kwa kuungana nasi katika maadhimisho haya muhimu.

Heri ya Siku ya Uhuru.

Mheshimiwa Noluthando Mayende-Malepe
 Balozi wa Jamhuri ya Afrika Kusini hapa nchini Tanzania

UWANJA WA BENJAMIN MKAPA KUKAMILIKA MIEZI SITA IJAYO.

Uwanja Benjamin Mkapa kuboreshwa kisasa

 Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, ametangaza kuanza kwa maboresho makubwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa uliopo jijini Dar es Salaam.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Msigwa amesema maboresho hayo yanahusisha sehemu ya kuchezea (pitch), ambayo inatarajiwa kufikia viwango vya kisasa ndani ya kipindi cha miezi sita.

Ameeleza kuwa lengo ni kuwa na uwanja wenye viwango vya kimataifa, sambamba na kuboresha maeneo mengine ikiwemo sehemu za wageni maalum (lounges), vyumba vya kubadilishia nguo, ubao wa matokeo pamoja na mwonekano wa jumla wa uwanja.

Aidha, ameomba radhi kwa mashabiki wa soka kwa kutoweza kuutumia uwanja huo katika dabi ya Kariakoo iliyopangwa kufanyika Mei 3, 2026.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa baada ya maboresho kukamilika, uwanja huo utakuwa katika hali bora zaidi na utadumu kwa matumizi ya muda mrefu.


NI SIMBA NA YANGA FAINALI YA MUUNGANO 2026

 


Timu ya Simba SC imefanikiwa kwenda Fainali ya Kombe la Muungano baada ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya wenyeji, Mlandege FC usiku wa jumapili ya tarehe 26 Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar. 

Mabao ya Simba SC yamefungwa na mshambuliaji mzawa, Suleiman Abdallah Mwalimu ‘Gomez’ dakika ya 61, winga Muivory Coast, Alain Anicet Oura dakika ya 76 na kiungo wa Kimataifa wa Afrika Kusini, Neo Gift Maema dakika ya 89.

Simba SC itakutana na mtani wake, Simba SC katika Fainali ya Kombe la Muungano 2026 Jumatano, Aprili 29 kuanzia Saa 2:15 usiku hapo hapo New Amaan Complex.

Ikumbukwe juzi mabingwa hao, watetezi, Yanga SC walifanikiwa kwenda Fainali ya Kombe la Muungano baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC hapo hapo Amaan Complex.

Hii ni maana yake miamba hiyo ya soka nchini italutana mara mbili ndani ya wiki moja, kwani Mei 3 watamenyana katika mechi ya marudiano ya Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara kuanzia Saa 12:00 jioni Uwanja wa Meje Jenerali Isamuhyo, Mbweni, Dar es Salaam. 

Sunday, April 26, 2026

YANGA WATINGA FAINALI, MACHO SASA KWA DABI NZITO INAYOFUATA?

 


Mabingwa watetezi, Young Africans SC wamefanikiwa kutinga Fainali ya Kombe la Muungano 2026 baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC katika mchezo wa nusu fainali uliopigwa usiku wa Jumamosi, Aprili 25, 2026 kwenye dimba la New Amaan Complex, Zanzibar.

Yanga walionyesha dhamira mapema baada ya mshambuliaji wao raia wa Zimbabwe, Prince Mpumelelo Dube kufungua ukurasa wa mabao dakika ya 9 akiitungua timu yake ya zamani. Kiungo mahiri raia wa DR Congo, Maxi Mpia Nzengeli akaongeza bao la pili dakika ya 25, akiipa Yanga utulivu wa mchezo.

Kwa upande wa Azam FC, kiungo mshambuliaji Feisal Salum Abdallah alifunga bao la kufutia machozi dakika ya 78, naye akiiumiza klabu yake ya zamani, lakini halikutosha kuizuia Yanga kusonga mbele.

Sasa Yanga wanasubiri kumjua mpinzani wao wa fainali atakayepatikana katika mchezo wa nusu fainali ya pili kati ya Simba SC na Mlandege FC utakaopigwa leo kuanzia saa 2:15 usiku, uwanja huo huo wa Amaan.

Fainali ya Kombe la Muungano 2026 imepangwa kupigwa Jumatano, Aprili 29, saa 2:15 usiku katika Uwanja wa Amaan .

Hata hivyo, macho ya mashabiki wengi tayari yanaelekezwa mbele zaidi kwani siku tatu tu baada ya fainali hiyo, kunatarajiwa kuchezwa dabi kubwa ya watani wa jadi, Simba SC dhidi ya Young Africans SC mchezo unaotarajiwa kuwa na presha, ushindani mkali, na huenda ukaathiriwa moja kwa moja na matokeo ya fainali ya Muungano.

'LEO WANAUME WA MWANZA MMEFIKIWA' KARIBU KIKAONI

 NA ALBERT G.SENGO/MWANZA

Jumapili hii, yaani LEO - tarehe 26 Aprili 2026, jiji la Mwanza linakuwa kitovu cha mjadala muhimu unaomhusu mwanaume wa kizazi cha sasa. Ndani ya Ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT – Capri Point), tukio maalum la Mwanza Wanaume Summit 2026 linafanyika, likiwaleta pamoja wanaume kutoka pande mbalimbali za Kanda ya Ziwa na kwingineko. Kuanzia saa 8 mchana hadi saa 12 jioni, washiriki watapata fursa ya kipekee ya kujifunza, kuhamasishana na kujenga mtazamo mpya unaoendana na changamoto na fursa za maisha ya leo kuanzia majukumu ya kifamilia hadi mchango wao katika jamii na taifa. Katika mazungumzo haya yenye uzito, Maxwell Stanslaus Shing’oma, Rais wa Taasisi ya Wanaume Tanzania (Men At Work Global), anafungua pazia kwa kueleza kwa kina dhamira ya kongamano hili na kwa nini ni muhimu kwa maendeleo ya mwanaume wa kizazi hiki.......

Friday, April 24, 2026

SIMBA WALEEEE NUSU FAINALI KOMBE LA MUUNGANO 2026

 


TIMU ya Simba SC imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya Kombe la Muungano baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mafunzo usiku wa tarehe 23 Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

Bao pekee la Simba SC katika mchezo huo limefungwa na mshambuliaji wake tegemeo kwa sasa, Suleiman Abdallah Mwalimu ‘Gomez’ dakika ya 54.

Simba SC sasa itakutana na Mlandege FC katika Nusu Fainali Jumapili, baada ya mabingwa watetezi, Yanga kucheza na Azam FC katika Nusu Fainali ya kwanza Jumamosi, mechi zote zikianza kuanzia Saa 2:15 usiku hapo hapo Uwanja wa New Amaan Complex 

Mlandege FC imetinga Nusu Fainali baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars mchezo uliocheza jioni ya tarehe 23 April 2026 hapo hapo Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

Mabao ya Mlandege yamefungwa na Omar Juma’Samatta’ dakika ya 28 na Mussan Hassan ‘Mbappe’ dakika ya 45’+1, baada ya Mishamo Daudi kuanza kuifungia Singida Black Stars dakika ya tisa.

Wakati Yanga iliitoa Muembe Makumbi City FC kwa kuichapa mabao 4-0 juzi, Azam FC iliitupa nje KVZ FC KWA kuichapa mabao 2-0 hapo hapo Amaan Complex.

BETIKA WAZINDUA JEZI YA MSIMU WA 10 WA TULIA MARATHON MBEYA

 


KAMPUNI ya ubashiri, Betika Tanzania ikishirikiana na Taasisi ya Tulia trust kupitia Betika Mbeya Tulia Marathon imezindua rasmi jezi ambayo itatumika Msimu wa 10 wa Mashindano Jijini Mbeya mwaka huu.

Akizungumza na Wanahabari  Jijini Dar es Salaam Meneja Mkuu wa Betika Tanzania Samuel Mcheru amesema Betika inathamini sana michezo na itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa kupitia Taasisi ya Tulia trust Kuhakikisha mbio hizo za Betika Mbeya Tulia Marathon zinafanyika kwa ufanisi mkubwa.

Hata hivyo, ameongeza kuwa mashirikiano hayo yanalenga kuwaweka wananchi karibu na kushiriki michezo ili kuweka miili yao imara zaidi,kurudisha tabasamu kwa jamii na kutoa fursa za kibiashara kwa Wananchi wa Jiji hilo.

Mcheru ametoa wito kwa Makampuni mengine yawe yenye tija katika jamii kwani uwepo wa Betika Tulia Marathon ni kiashiria tosha kuwepo kwa ongezeko la kipato kila inapofanyika kutokana na jamii kukusanyika eneo moja hivyo inawapa fursa betika pia kujitangaza zaidi na Wafanyabiashara kuendesha shughuli zao.

Kwa upande wake Mbunge wa Mbeya na Spika wa Bunge Mstaafu Dkt.Tulia Ackson amesema Kampuni ya Betika imekuwa na mchango mkubwa wa kuhakikisha mbio hizo zinafanyika kwa ufanisi mkubwa hasa kwa mchango wao wa vifaa vya kushiriki mbio hizo pamoja na miundombinu mbalimbali pindi linapokuja shindano hilo kutokana na kuweka udhamini wao kwa zaidi ya Miaka mitatu.

Ackson amesema kwa mwaka huu shindano hilo linatimiza miaka 10 tangu kuanzishwa kwake na kwa mwaka huu wanategemea kukusanya kiasi cha fedha shilingi milioni 300 ili kugusa Maeneo ya Kijamii mbalimbali ikiwemo Kuboresha makazi ya Wahitaji, eneo la Afya hususani kujenga baadhi ya wodi hitajika, vifaa pamoja na eneo la Elimu Mashuleni.

Hata hivyo amesema Mbio hizo za kipekee zilizopewa chachu na hali ya hewa ya jiji hilo itatimua vumbi Mei 15 na 16 zikiambatana na burudani mbalimbali.

Aidha amevipongeza vyombo vya habari kwa kuendelea kutoa habari juu ya Taasisi ya hiyo ambayo kutokana na michango ya wadau mbalimbali katika kujikita kusaidia jamii.

Pia ametoa wito kwa Watanzania kujiandikisha kushiriki katika mbio hizo kupitia Ofisi zilizopo Jijini Mbeya pamoja na kujisajili mtandao kwenye kurasa za Taasisi hiyo.

Nae Afisa Habari wa Kampuni ya Betika Juvenalius Rugambwa aliongeza kuwa Jezi hiyo iliozinduliwa itatumika rasmi kwenye mbio hizo huku akisherehesha kuwa jezi hizo zimepambwa na rangi zenye mvuto zaidi zenye michoro ya vivutio vilivyopo Tanzania ikiwemo bendera ya Taifa.

Thursday, April 23, 2026

SAKATA LA MAHANDAKI MWANZA: MFANYABIASHARA AKAMATWA KWA UJENZI USIOFUATA SHERIA.

 news

Katika tukio linalozua maswali ya kiusalama na ufuatiliaji wa shughuli za ujenzi, mfanyabiashara Evance Bisesagu (47), mkazi wa Bupumula, Kata ya Nyamhongolo, Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kuchimba mahandaki sita kinyume cha sheria.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, mtuhumiwa huyo alikamatwa jioni ya Aprili 22, 2026, kufuatia taarifa za wananchi waliokuwa na hofu juu ya uwepo wa mahandaki hayo karibu na makazi yao. Wananchi hao walieleza kuwa shughuli hizo zilikuwa zikifanyika kwa siri na bila maelezo ya wazi, jambo lililozua wasiwasi mkubwa wa usalama.

Uchunguzi wa Polisi Wabaini Ukiukwaji wa Sheria

Akizungumza Aprili 23, 2026, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa, alisema uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa ujenzi huo ulikuwa unafanyika bila vibali halali kutoka mamlaka husika.

Mbali na mmiliki wa eneo hilo, watu wengine wawili Ngasa Kasuka na Hamad Kashinje pia wanashikiliwa wakidaiwa kuwa walikuwa wakifanya kazi kama vibarua katika mradi huo.

 “Msako unaendelea kuwatafuta mafundi na watu wengine wote waliohusika katika shughuli hizi,” alieleza Kamanda Mutafungwa.


Hofu ya Usalama kwa Wananchi

Tukio hili limeibua mjadala mpana kuhusu usalama wa makazi ya wananchi, hasa pale shughuli za ujenzi zinapofanyika bila uwazi na ufuatiliaji wa karibu. Mahandaki kama hayo yanaweza kusababisha hatari kubwa, ikiwemo kuporomoka kwa ardhi au majengo, pamoja na uwezekano wa kutumika kwa shughuli zisizo halali.

Wito kwa Viongozi na Mamlaka

Jeshi la Polisi limetoa rai kwa viongozi wa serikali za mitaa na mamlaka za ujenzi kuhakikisha wanafuatilia kwa karibu shughuli zote za maendeleo katika maeneo yao.

Kamanda Mutafungwa alisisitiza kuwa ni lazima kila ujenzi ufuate taratibu zote za kisheria, ikiwa ni pamoja na kupata vibali vinavyohitajika kabla ya kuanza kazi yoyote.

 “Hatutavumilia ujenzi holela. Kila anayekiuka sheria atachukuliwa hatua kali,” alionya.


Wednesday, April 22, 2026

ALIYEMUUA MUMEWE BAADA YA FUMANIZI AHUKUMIWA KIFUNGO CHA NJE.

 Mahakama

ELIZABETH Sylvester maarufu kama Sosomo, mkazi wa Kijiji cha Chudeko, Wilaya ya Songwe, amehukumiwa kifungo cha nje cha miezi 18, baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kumuua mumewe, Ally Masanja, bila kukusudia.

Hukumu hiyo imetolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songwe, imemhukumu Katika kesi hiyo namba 7304/2026, mshitakiwa alikiri kosa la kuua bila kukusudia kinyume na vifungu vya  195 na 198 vya kanuni ya adhabu, Sura ya 16, kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2023.

Kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo na wakili wa Serikali, Elbariki Mpinga, tukio hilo lilitokea Januari 3, 2026 katika Kijiji cha Chudeko, wilayani Songwe, ambapo mshitakiwa alimchoma mumewe kisu ubavuni wakati wa ugomvi uliotokana na wivu wa mapenzi.

Ilielezwa kuwa ugomvi huo ulizuka baada ya mshitakiwa kumkuta mumewe akiwa  nyumbani kwa mwanamke anayedaiwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi. 

Hali  hiyo  iliyoibua ugomvi kati yao watatu hao, hadi kufikia  kwenye shambulio hilo lililosababbisha mauti ya mwanaume huyo. 

Akisoma hukumu Aprili 21, 2026, Jaji Mfawidhi wa mahakama hiyo, Jaji Gabriel Malata, amesema mahakama imezingatia mazingira ya tukio, ikiwemo hali ya mshtakiwa kabla, wakati na baada ya tukio pamoja na ungamo lake.

Alisema mahakama ilimtia hatiani kwa kosa hilo na kuamua kumpa adhabu hiyo ya kifungo cha nje cha miezi 18 kwa kuzingatia masharti ya kisheria.

Kwa mujibu wa hukumu hiyo, mshitakiwa hataruhusiwa kutenda kosa lolote la jinai katika kipindi hicho, na endapo atakiuka masharti hayo atalazimika kutumikia kifungo hicho gerezani.

Kesi hiyo ni miongoni mwa kesi tatu za mwanzo kutolewa hukumu na Mahakama Kuu Kanda ya Songwe tangu kuanza rasmi kwa shughuli zake za kimahakama Machi 30, 2026.

Awali, Wakili wa utetezi, Moses Mwampashi, aliomba mahakama imuonee huruma mshitakiwa, akieleza kuwa hilo ni kosa lake la kwanza na halikupangwa bali lilitokana na mazingira ya tukio.

Aliongeza kuwa mshitakiwa ana watoto wanne aliowazaa na mumewe,ambao kwa sasa  ndiye mtu wa kuwalea na wanamtegemea, hivyo kuiomba mahakama izingatie maslahi yao katika utoaji wa hukumu.

KONGAMANO LA WANAUME (MEN AT WORK) KUFANYIKA MWANZA

 

Men at Work ni jukwaa maalum linalowakutanisha wanaume kutoka maeneo mbalimbali kwa lengo la kujifunza, kujadili na kujengeana uwezo katika safari ya maisha. 

Kupitia kongamano hili, washiriki hupata fursa ya kuimarika katika nyanja muhimu kama uchumi, ndoa na mahusiano pamoja na kukuza nidhamu binafsi na uwajibikaji katika nafasi zao kama wanaume ndani ya familia na jamii kwa ujumla.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2015, Men at Work imeendelea kuwa chachu ya mabadiliko kwa wanaume wengi, ikiwa imefanikiwa kuandaa makongamano yenye tija ndani na nje ya Mwanza. 

Athari yake imekuwa kubwa kiasi cha kuibua majukwaa mengine yenye mwelekeo sawa, ikiwemo "Kikao cha Wanaume", lakini chimbuko lake ni Men at Work. 

Ushuhuda wa mafanikio na mabadiliko ya maisha ya washiriki ni mwingi na unaendelea kuongezeka kila mwaka na unatarajiwa kutolewa katika kongamano la wanaume jijini Mwanza.

Kongamano hilo la wanaume (Men at Work) linatarakiwa kufanyika jumamosi tarehe 26 Aprili 2026 katika ukumbi wa Chuo cha BOT, Capripoint jijini Mwanza kuanzia saa mbili asubuhi.

Mwandaaji wa kongamano hilo, Maxwell Chaila amesema jukwaa hilo ni linatoa fursa kwa wanaume kufahamiana na kujifunza safari ya mabadiliko chanya katika maisha yao.

Men at Work- Mwanaume Bora, Jamii Imara.