ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, March 30, 2024

TEMESA TANGA YAZIDAI TAASISI ZA SERIKALI MADENI ZAIDI YA BILIONI 1.8 ,YAMO MADENI SUGU

 

Na Oscar Assenga,TANGA.

WAKALA wa Ufundi na Umeme nchini (TEMESA) Mkoani Tanga umesema kwamba unazidai Taasisi za Serikali madeni sugu ya zaidi ya Bilioni 1.8 ambao walikwenda kutengeneza magari yao katika karakana ya wakala huo ambapo mengine ni ya muda mrefu.

Hayo yalisemwa na Meneja wa Temesa Mkoa wa Tanga Mhandisi Jairos Nkoroka wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ambapo alisema wanaziomba taasisi hizo kulipa madeni yao ili kuuwezesha wakala huo kuendelea kutekeleza shughuli zao kwa ufanisi.

Meneja huyo aliziomba taasisi hizo nazo ziweze kulipa madeni yao kutokana na kwamba nao pia wanadaiwa Bilioni 1.4 na wazabuni ambao wamekuwa wakipeleka vifaa kwa ajili ya kutengeneza magari

“Tunawakumbusha watulipe ili tuweze kuendelea kuwapa huduma kwani kutokufanya hivyo kunaweza kusababisha kutokupata huduma kwa wakati “Alisema

Aidha alisema kwamba madeni mengi ni ya nyuma ambayo wameyarithi na mengine wameyapeleka makao makuu yao kwa utaratibu mwengine na ya mwaka huu wanaendelea kuwadai kuhakikisha wanalipa

“Tumeanzia kitengo cha mahusiano kupitia mabalozi kwa kujenga mahusiano na hivyo kuzaidia wanaodaiwa kuanza kulipa madeni yao na tunaamini tutaendelea kupata mafanikio”Alisema

Aidha alisema ili kuweza kukabiliana na wadai hao sugu Temesa umeingia mkataba na wazabuni wakubwa (40) wa vipuri vya magari mkoani Tanga ili kuondoa ucheleweshaji ambao ulikuwepo hapo awali badala ya kuanza taratibu za manunuzi ambazo siku za nyuma zilikuwa zinawachelewesha.

Alisema wameamua kufanya hivyo ili kuweza kuhakikisha wanaondokana na ucheleweshwaji huo na kwa sasa wanachukua muda mfupi baada ya siku mbili.

Alisema mpango huo utasaidia kuwawezesha kupata vifaa ambavyo walikuwa hawana na vile vyengine ambavyo kwa hiyo kwa sasa ivi magari ya serikali yanayokwenda kufanyiwa matengenezo yanachukua muda mfupi sana na hatimaye kuruhusiwa kuendelea na shughuli zao.

“Hivi sasa tumeingia mikataba na wazabuni wakubwa na matengenezo ya magari ya Serikali yanatakiwa kutengenezwa na Temesa na tukishindwa kutengeneza kutokana na kitaaluma au vifaa kuna utaratibu ambao unafahamika na tunatoa vibali kwenda kwenye karakana nyengine na yanatrngezwa chini ya usimamizi wao”Alisema

“Katika ishu ya vifaa vya matengenezo ya magari tunatumia muda mfupi kulikagua gari na kubaini changamoto zake kutokana na uwepo wa vifaa vya kisasa “Alisema Jairos

Friday, March 29, 2024

AJALI YAUWA MASHABIKI WAWILI WA SIMBA KAMANDA AZUNGUMZA

VICTOR MASANGU/PWANI WATU wawili wamepoteza maisha na wengine watatu kujeruhiwa vibaya baada ya gari dogo la abiria aina ya Costa kupata ajali kwa kugongana na Lori katika eneo la Vigwaza Mizani Halmashauri ya Chalinze Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Pius Lutumo amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo majira ya saa 12:15 asubuhi ya leo. Kamanda Lutumo ameongeza kuwa katika ajali hiyo basi dogo lililokuwa likitokea Mkoani Mbeya kuelekea Jijini Dar es Salaam lilikuwa limebeba mashabiki wa klabu ya Simba. Aidha Kamanda Lutumo aliwataja marehemu katika ajali hiyo kuwa ni Oleison Mwakasila, anaekadiriwa kuwa na miaka 42-45, mkazi wa Kiwila mkoani Mbeya na Dereva wa gari hilo dogo aitwaye Moses Mwaisela mwenye umri wa miaka (40,). Ikumbukwe siku ya jana katika eneo la bonde la mto Ruvu Wilayani Kibaha kulitokea ajali nyingine iliyohusisha magari matatu kugongana na kupelekea vifo vya watu watatu.

MASHABIKI WA SIMBA WAPATA AJALI MMOJA AFARIKI

 


Na Victor Masangu,Vigwaza


Mtu mmoja ambaye ni shabiki wa Klabu ya Simba anahofiwa kufariki dunia katika ajali ya gari aina ya coaster iliyokuwa imebeba mashabiki wa Simba ikitokea Mbeya kupata ajali ya  kugongana na Lori leo alfajiri majira  katika eneo la Vigwaza mizani Mkoa wa Pwani.


Taarifa za awali ambazo zimethibitisha na Mwenyekiti wa kijiji cha Vigwaza  zinaeleza kuwa gari hiyo iliyokuwa imebeba mashabik wa Simba ilikuwa inatokea MkoaniMbeya kuelekea Jijini Dar es Saalam.

MV MWANZA HAPA KAZI TU YAFIKIA ASILIMIA 96 KUANZA SAFARI ZAKE AFRIKA MASHARIKI HIVI KARIBUNI

 NA ALBERT G. SENGO/MWANZA

Meli Mpya ya kubeba Abiria na Mizigo ya MV Mwanza hapa kazi tu, kwa mara ya nyingine imefanya safari ya majaribio ya kiufundi katika Ziwa Victoria. Mara baada ya majaribio ya siku 3, Waziri wa Uchukuzi Makame Mbarawa anaongoza zoezi la ukaguzi wa Mv Mwanza Hapa Kazi Tu, iliyoondoka katika Bandari ya Mwanza Kusini ikiwa na jopo la wadau, wakiwemo Wahandisi, Wakandarasi, Wandishi wa Habari pamoja na Wataalam waliokuwa wakiijenga meli hiyo. Eric Hamisi ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Huduma za Meli Nchini na hapa anaeleza zaidi ni yapi yaliyosalia kwa ujenzi wa meli hiyo ili kuanza safari zake. Meneja Mradi wa Ujenzi wa Meli ya MV. Mwanza hapa kazi tu Vitus Mapunda amesema majaribio hayo ni ishara ya kukamilika kwa Ujenzi wa Meli hiyo, nao wakiwa na dhamana ya kuilinda na kuitunza. Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya huduma za Meli MSCL Meja Jenerali Mstaafu John Mbungo amesema Watanzania wanapaswa kuona fahari kubwa ya ushiriki wao katika Ujenzi wa Meli hiyo. Wakazi wa Jiji la Mwanza wameipongeza Serikali kwa kukamilisha Ujenzi wa Meli hiyo. Meli ya MV. Mwanza hapa kazi tu yenye uwezo wa kubeba Abiria 1,200, Tani 400 za Mizigo, si chini ya Magari Madogo 28 na Malori Matatu unatarajiwa kukamilika ndani ya Mwaka huu ambapo Ujenzi wake ulianza Mwaka 2019 ukitekelezwa na Mkandarasi kutoka Korea ya Kusini zikishirikiana na Suma JKT ya Tanzania, Mradi huo umegharimu zaidi ya Shilingi Bilioni 127 za Kitanzania.

Happy Mbuya - AONAAA! (Official Music Audio)

 

 
"Nimeachia Wimbo wangu unaitwa ONAA! Nitakutumia link unisaidie kushare , usisahau kususcribe na comments.  Nitafurahi sana uki saport huduma hii iweze kuenea Tanzania na kwingineko duniani. Mungu akubariki sana mpendwa"

Thursday, March 28, 2024

MADUDU RIPOTI YA CAG, "NCHI TUNAIUA SISI WENYEWE"


Rais Samia Suluhu Hassan amewataka watendaji wa Serikali, kusimamia vema rasilimali za nchi kwa kutumia mifumo na kuweka nidhamu, akisema kinyume na kufanya hivyo ni sawa na kuiua nchi yetu wenyewe.


Mkuu huyo wa nchi ameeleza hayo wakati akifafanua kuhusu uzembe wa upitishaji wa baadhi ya mikataba inayoigharimu Serikali kwa kuweka ama kuruhusu vifungu vya kisheria visivyostahili kuwepo.

Kauli yake hiyo inatokana na kile kilichobainishwa kwenye ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2021/22 na taarifa ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwa, Serikali inadaiwa tozo na riba ya zaidi ya Sh418 bilioni kutokana na ucheleweshaji wa malipo au mikataba.


Katika hotuba yake aliyotoa Ikulu ya jijini Dar es Salaam jana, baada ya kupokea ripoti hiyo ya CAG na ile ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Rais Samia alisema kuna mambo ya hovyo yanafanyika.

Alisema kumekuwa na upitishwaji mikataba mibovu inayoigharimu nchi, sambamba na kucheleweshwa kwa malipo kunakozalisha riba kubwa kwa Serikali.

Huku akionekana kukerwa na kuwakaripia watendaji wazembe, alieleza pamoja na kufahamika kila mkataba unavyopaswa kuwa, baadhi ya watendaji wanapitisha ambayo ina vifungu visivyostahili.

“Dhambi ni sisi wenyewe. Tunaua nchi yetu sisi wenyewe. Unaruhusu vifungu vya ajabu vinaingia kwenye mitakaba isiyopaswa, kwa hiyo huko kwenye mikataba angalieni vizuri.

“Mikataba hii ina aina zake, unajua kabisa mkataba wa aina hii hauwezi kuwa na vifungu hivi, lakini unakuta kuna kifungu cha ajabu ajabu kipo ndani ya mkataba,” alieleza Rais akionyesha kukasirika na kuongeza: “Kinachoshangaza ni njia ulizopita mkataba huo na ukafanyiwa kazi bila hata vifungu hivyo kuonekana.


“Umepita njia zote na mkataba ukaenda ukafanya kazi na sasa waliofanya kazi wanadai ni kimkataba, sasa unawapa watu wengine hebu someni huu mkataba wanakwambia mama hivi vifungu havikupaswa kuwepo ndani ya mkataba, unawauliza ilikuwaje vikaingia, wanaangaliana machoni,” alisema.


Ucheleweshwaji malipo

Kuhusu ucheleweshwaji wa malipo kwa makandarasi, Rais Samia alisema unafanywa na baadhi ya watendaji kwa makusudi kwa kuwa kuna wanachokipata kupitia tozo na riba hizo.

“Kuna malipo ya riba Sh418 bilioni, bilioni hizi tungezipeleka kwenye umeme, tungepeleka kwa watu wangapi, watu wapo tu hawana uzalendo.

“Hawajali, wanatengeneza riba wanalipa wapate na cha kwao, kikupeleke wapi, utazikwa nacho?” alihoji Rais kwa hisia.

Kwa mujibu wa CAG Charles Kichere, riba hiyo ya Sh418.77 bilioni ilitokana na kucheleweshwa kwa mikataba katika taasisi mbalimbali ikiwemo Serikali Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa (Tamisemi) na mashirika ya umma.

“Ucheleweshaji huo umetokana na mchakato wa malipo kuchukua muda mrefu bila kuzingatia matakwa ya kimkataba,” alisema Dk Kichere.


Upigaji mikopo ya halmashauri

Wakati wabunge na madiwani wakiibana Serikali na watendaji kuhakikisha wananchi wananufaika na mikopo hiyo ya asilimia 10 inayotokana na mapato ghafi ya halmashauri, CAG amebaini kuwepo kwa urejeshaji duni wa mikopo hiyo. Kwa mujibu wa ripoti ya CAG kiasi cha Sh88 bilioni zilizokopeshwa kwa makundi ya wanawake, vijana na walemavu, hazijarejeshwa. Kutokana na hilo, Rais Samia alisema sababu kubwa ya kushindwa kukusanywa kwa mikopo hiyo ni namna ya ukopeshaji.


Alieleza mikopo hiyo imegeuka kuwa mfuko wa siasa kwa madiwani na hata zinapokopeshwa, wananchi huamini wamepewa na madiwani wao, hivyo hawaoni haja ya kurejesha ili wengine wanufaike.

“Huku nako kunataka marekebisho makubwa, mbinu hii tunayoichukua kupitia halmashauri haitafanya kazi siku zote, tutatoa fedha na haitarudi,” alisema.

Alitaka mfumo wa kibenki uingizwe kuratibu mikopo hiyo, akisema kila halmashauri ikusanye fedha na kupeleka kwenye benki itakayokubalika na wakopaji waende huko.

“Vijana, wanawake, wenye ulemavu watakopa benki na kule utake usitake utalipa, tukifanya hivi wanaochukua watalipa na tutaondoa ile tabia ya madiwani kufanya wanavyotaka.

“Fedha yote hii iliyotoka Sh88 bilioni kama ni vituo vya afya vingapi? Imekwenda imepotea, sadaka madiwani wametoa kwa wapiga kura wao, hii fedha kwenye bajeti ya mwakani iundiwe mfumo mpya,” alisema.

Mfumo huo alioshauri kuanza kutumika mwaka wa fedha ujao 2023/24, ndio unaotumika kwa Zanzibar, ambapo Serikali iliingia makubaliano na taasisi za fedha kukopesha wajasiriamali kwa masharti nafuu lengo likiwa ni kuwa na mfumo mzuri wa ufuatiliaji.


Kasoro utekelezaji wa miradi

Licha ya uwepo wa wasimamizi wa miradi katika kila wizara, alisema bado kumekuwepo na kasoro kwenye utekelezaji wa miradi.

Alisema kwenye miradi mikubwa bado kuna matatizo na wasimamizi wanapaswa kuonea uchungu fedha ya Serikali.

“Kama upotevu huu ni faida kwa wanaosimamia basi imetosha, mmeshachukua ngapi, kwa hiyo tumechelewa kwenye kuchukua hatua, wakichukuliwa hatua wataacha,” alisema. 


 Alitolea mfano kwenye ununuzi wa vishikwambi akisema kuna ziada ya Sh10 bilioni fedha ambayo imepotea bila tija.

Rais Samia alisema katika ununuzi wa vishikwambi 300,000 uliofanywa kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, ambapo Machi 2022 ilipewa jukumu hilo kwa ajili ya Sensa ya Watu na Makazi na ilianzisha mchakato wa zabuni.

Alisema zabuni hiyo iligawanywa katika sehemu sita kila moja ikiwa na vishikwambi 50,000 wizara ilisaini mikataba na wazabuni watatu wa kuleta vishikwambi 300,000 vyenye thamani ya Sh123.7 bilioni.

Katika mchakato huo, alisema wajumbe wa bodi walipendekeza wazabuni wanne kati ya 14 wawili kati yao walishinda zabuni, ilhali si kazi ya bodi ya zabuni kupendekeza wazabuni.

Pia, alisema bodi ya zabuni ilibadilisha vigezo vya ubora bila kuwasiliana na idara tumizi na kuondoa vifaa vya kutunzia umeme, wazabuni walipewa siku mbili tu kujibu nyaraka za zabuni badala ya 14 zinazotakiwa huku 10 kati ya 14 wakijibu kwa wakati.“Idara tumizi haikuhusika katika kamati ya wajumbe walioteuliwa kutathmini na waliteuliwa bila mapendekezo ya idara ya ununuzi ambayo ni kinyume cha sheria,” alisema.

“Haya yapo mengi mawaziri tusaidiane huko, wasiwadanganye, tunaomba tufanyie kazi na ili tuendelee kuna kazi ya kufanya inahitajika,” alisema.


Kwenye miradi ya maji nako balaa

Awali, akizungumza kuhusu hilo, CAG Kichere alisema katika ukaguzi wake, alibaini upungufu katika utekelezaji wa mradi wa uboreshaji na usambazaji wa maji wa Sami-Mwanga wenye thamani ya Sh263.67 bilioni.

 Katika mradi huo unaotekelezwa na Wizara ya Maji kwa ufadhili wa Serikali ya Tanzania na Shirika la Maendeleo, alisema ulianza kutekelezwa Desemba 17, 2014 na ulitarajiwa kukamilika Machi 4, 2021 lakini hadi sasa mradi haujakamilika.

Alisema kulikuwa na makandarasi wawili wanaotekeleza mikataba mitatu ya mradi huo yote ilisitishwa Desemba 2020 na miwili ilisitishwa baada ya Wizara ya Maji kujiridhisha kwamba, mkandarasi alighushi dhamana ya benki ya malipo ya awali na dhamana ya fedha za zuio alizowasilisha wizarani.

“Mkataba mmoja ulisitishwa kwa kuwa mkandarasi hakuhuisha dhamana ya utekelezaji wa mradi, baada ya kuisha muda wake na baada ya kukumbushwa mara kadhaa bila mafanikio,” alisema.

Baadaye, alisema Wizara ya Maji iliingia mikataba miwili yenye thamani ya Dola milioni 13.95 za Marekani na Dola milioni 3.61 za Marekani, kwa ajili ya kumalizia kazi ya kusambaza mabomba na kumalizia kazi ya kujenga matenki mtawalia.

Alisema kabla mkandarasi mpya hajaanza kazi, Wizara ya Maji ilifanya mabadiliko kwenye mkataba wa kujenga matenki na kuongeza gharama za mkataba kutoka Dola milioni 3.61 za Marekani na kuwa Dola milioni 5.9 za Marekani sawa na ongezeko la Dola milioni 2.3 za Marekani sawa na asilimia 61.


Tanapa na fedha za Uviko-19

Rais Samia alitaka kujenga utaratibu wa kuunda bodi zenye sifa ya kufanyakazi kwenye maeneo kama Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa).

“Huku nako kukatizamwe vizuri, lakini Tanapa hawa wamepata fedha za Uviko-19 nendeni mkazitazame zimefanya nini,” alisema.

Ili kufanya rasilimali za nchi zitumike inavyopaswa, alisema kuna haja kufanyia kazi hasa kwa kutumia mifumo na kuweka nidhamu.

“Tukilegalega kwenye nidhamu na hatusimamii nidhamu kwa sababu sisi wenyewe ni wanufaika, tusingenufaika tungesimama, lakini kwa sababu tunanufaika hatusimamii.

“Niwaombe sana nchi hii kama tutasimamia rasilimali zetu, huko mbele tutapunguza shughuli za mikopo, tutakopa kama kuna umuhimu, tutakopa kwenye miradi mikubwa ya ndani, lakini mambo mengi tutaweza kufanya wenyewe,” alisema.


Mifumo TRA, TPA kutosomana

Katika ripoti ya Takukuru iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Kamishna Salum Hamduni alisema kutosomana kwa mifumo ya Mamlaka ya Bandari (TPA) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ni moja ya viashiria vya rushwa.

Kutokana na hilo, Rais Samia alisema tatizo la mifumo katika bandari limekuwepo kwa siku nyingi na alishaagiza lirekebishwe, lakini anashangazwa mpaka sasa bado halijafanyiwa kazi.

Alisema kutokana na hilo, ametoa ruhusa TPA kufanya kazi kwa kushirikiana na sekta binafsi ili kuongeza ufanisi wa huduma na ukusanyaji wa mapato huku akiamini jambo hilo linafanywa kwa makusudi.

Alisema hakuna sekta binafsi itakayoweka fedha yake ikaacha mifumo iendelee kubaki kama ilivyo, kwa vyovyote itaimarisha isomeke vema ili fedha zikusanywe.

“Na kuna reservation upande mwingine huko nao wana wasiwasi na hilo, tutakuja kulizungumza baadaye lakini kuna umuhimu kuimarisha bandari, mifumo, teknolojia,” alisema.

Alieleza bandari ni lango kubwa la uchumi lenye uwezo wa kuchangia hata nusu ya bajeti ya Serikali, lakini inashangaza pato lake haiinuki.

“Na watetezi mpo wengi tu, hapana sekta binafsi isiende mifumo sijui nini… mimi nasema sekta binafsi ikaribishwe twende tukaimarishe kwa masharti tutakayokubaliana kupitia Mwanasheria Mkuu atushauri bandari iimarishwe,” alisema.


Mapato halmashauri

Kuhusu fedha za halmashauri, Rais Samia alisema upotevu mkubwa husababishwa na mifumo akidokeza uwepo wa tabia ya baadhi ya watumishi kuondoka na mashine za ukusanyaji wanapotenguliwa.

“Huu mfumo ambao mtu anaweza kuondoka nao na ukawa haki yake hapana, hebu itazameni vizuri,” alisema na kuongeza: Tatizo lingine ni ulaji wa fedha mbichi katika halmashauri ambao alitaka ukomeshwe. Waziri (Angela Kairuki) tumezungumza hapa majuzi na ukaniambia unakwenda kufanya kitu, naomba tulifanye sasa ili kudhibiti ulaji wa pesa mbichi kwenye hizi halmashauri.

Walichosema wachambuzi

Mchambuzi wa siasa na uchumi, Gabriel Mwang’onda alisema Rais Samia yupo sahihi katika maeneo mengi aliyoyagusia katika hotuba yake. Hata hivyo, alisema tatizo sio mfumo pekee bali hata uendeshaji wa kawaida hasa wadau wa mashirika ya Serikali yanayotoa huduma kama TPA.

“Nakupa mfano mmoja unaweza kuleta mzigo wako ukamalizana na TPA na TRA, lakini jioni watu wa bandari wapo, huku wahusika wa taasisi kadhaa hawapo wameshafunga ofisi. Licha ya kuzungumzia mfumo lakini Rais Samia amependekeza pia ushirikishwaji wa sekta binafsi, hili jambo la msingi.

“Kitu kikiwa cha Serikali kinakwenda kiserikali, hakuna mtu anayejali, lakini kukiwa na sekta binafsi kunakuwa na uchungu katika utendaji kazi. Mapato ya TPA ni makubwa, sasa suala la mifumo likiangaliwa kwa upana litaleta tija,” alisema Mwang’onda.


Naye Mhadhiri Msaidizi wa Fedha, Uhasibu na Kodi wa Chuo cha Serikali za Mitaa, Dodoma, Charles Matekele alisema baadhi ya wataalamu hawajawajibika katika utekelezaji wa majukumu yao, ndio TRA wana mifumo mingi wanayoifanyia kazi, lakini wanaibadilisha mara kwa mara.

“Ni vema viongozi wa TRA na TPA kukaa chini na kuangalia maslahi ya Taifa, lakini ninaamini Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania na (TCRA), pamoja na Serikali mtandao wakikaa pamoja kazi zitakwenda vizuri.

“Kama unataka mafanikio hasa kwa bandari na TRA, lazima kutumia mifumo na ushirikiano wao na sekta binafsi katika mifumo utaleta ufanisi kwenye utekelezaji wa majukumu yao,” alisema Matekele.


CHANZO: MWANANCHI.

MIAKA MITATU YA RAIS SAMIA ,TANROAD TANGA YAJIVUNIA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA MAENDELEO

 Menejaa wa Wakala wa Barabara nchini (Tanroad) Mkoa wa Tanga Mhandisi Dastan Singano akizungumza na waandishi wa habari ambao hawapo pichani.



Na Oscar Assenga, TANGA.

SERIKALI kupitia Wakala wa barabara nchini (Tanroad) Mkoani Tanga imetengewa Bilioni 294 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya barabara inayoendelea kwa sasa ikiwemo barabara ya Tanga-Pangani.

Hayo yalisemwa na Meneja wa Wakala wa Barabara Mkoani Tanga (Tanroad) Mhandisi Dastan Singano wakati akielezea miaka mitatu ya Rais Dkt Samia Suluhu ambapo alisema wanajivunia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Ambapo alisema Serikali ya awamu ya sita imejikita kuleta Maendeleo ya Miundombinu ya barabara kwa Mkoa wa Tanga na katika barabara hizo kuna miradi inayoendelea.

Aliitaja miradi hiyo kuwa ni ule wa Barabara ya Tanga-Pangani ikiwemo Daraja la Mto Pangani mpaka Tungamaa kuelekea Mkwaja hadi Makange pamoja na Barabara ya Handeni-Mafleta.

Aidha alisema kwamba miradi hiyo inaendelea na utekelezaji wake na kwa sasa imefikia asilimia 73 vilevile Daraja la Pangani na barabara zake mradi inaendelea kutekelezwa kwa tija kubwa

“kwa kweli kwa kipindi cha miaka mitatu ya Rais Dkt Samia Suluhu sisi kama mkoa wa Tanga tunajivunia uwepo wa miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo mradi wa Tanga-Pangani-Daraja la Mto Pangani -Tungamaa kwenda Mkwaja mpaka Makange barabara inaedelea kutekelezwa”Alisema Meneja Singano.

Meneja huyo alisema pia kwa sasa wanaendelea na utekelezaji wa barabara ya Handeni –Mafleta iliyopo chini ya Mkandarasi huyo amepata kipande kingine cha Mafleta kwenda Kweleguru hata hivyo mradi kutoka kwaleguru utakwenda hadi Kibirashi mpaka kule mpakani mwa Manyara hiyo barabara mpaka Singida inatekelezwa kwa utaratibu huo na utaona miradi mikubwa inaendelewa.

Akizungumzia kuhsu namna walivyojipanga kukabiliana na uharibifu wa muondombinu hususani katika kipindi cha mvua alisema wamejipanga kukabiliana na changamoto za barabara na Bajeti ya matengenezo ni zaidi ya milioni 12.6 imetengwa .

“Lakini pale panapotokea dharura kuna fedha za dharura ambazo wanazitumia kwa ajili ya sehemu ambazo zimepata itilafu ya kukatika kwa barabara kwa lengo la kuondosha changamoto hizo”Alisema Mhandisi Singano.

Meneja huyo alisema kwa sasa matarajio yao ni kuanza mradi wa barabara ya Soni hadi Bumbuli mpaka funta wilayani Lushoto wenye kilomita 20 na wanandelea na upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwemo barabara ya Old Korogwe-Kwamkoro-Maramba mpaka Mabokweni.

Alisema barabara hiyo pia wanakamilisha usanifu ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami na wana mpango wa kujenga barabara kutoka njia ya panda kiomoni kwenda mpaka Bamba wilayani Mkinga kutokea Mlingano wilayani Muheza .

“Kwa hiyo utaona namna gani serikali ya awamu ya sita imejikita kuleta Maendeleo ya Miundombinu ya barabara kwa Mkoa wa Tanga zitakazokuwa na tija ya kuchochea kufungua maendeleo na kukuza uchumi”Alisema

DKT. SHEMWELEKWA AWAPIGA MSASA WATUMISHI KIBAHA MJI

 NA VICTOR MASANGU KIBAHA 


Mkurugenzi mtendaji mpya wa  Halmashauri ya Mji Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa amefanya kikao kazi na watumishi kwa lengo la muweza kufahamiana,pamoja na  kujitambulisha rasmi ikiwa sambamba  na kutoa mwelekeo wa utekelezaji wa majukumu.

Dkt.Shemwelekwa aliyeteuliwa rasmi  na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan tarehe 13 Machi,2024 kuwa Mkurugenzi wa Kibaha Mji.

Mkurugenzi huyo  amesifu mifumo mizuri iliyowekwa na watangulizi wake akiwemo Bi.Jenifa Omolo ambaye kwa Sasa ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mhandisi Mshamu Munde aliyehamishiwa Halmashauri ya Nanyamba na kwamba kazi yake Sasa ni kutengeneza kemia mpya itakayotumika ili kufikia malengo ya Serikali ya kuwahudumia wananchi 

Dkt.Shemwelekwa amewataka watumishi kutoa huduma Bora kwa wananchi wakiwa na furaha,kuondoa hofu,woga na wasiwasi na kwamba unapokuwa ofisini mwananchi ana matumaini makubwa nawe ya Kusikilizwa na kutatuliwa changamoto zake.

Aidha,Dkt.Shemwelekwa amewaasa watumishi kuwa wanyenyekevu kwa wananchi,kutumia lugha za staha,kuheshimiana,kushirikiana,kupendana na kusaidiana ili kufanya kazi zenye matokeo na zinazoacha alama za kukumbukwa huku akikemea vikali tabia za kufanyakazi kwa mazoea zisizokuwa na tija kwa Taifa letu.

"Watumishi wa Umma tuache kulalamika,tujielekeze kwenye kuondoa malalamiko na kero za wananchi.Tuwasikilize vizuri na kuwahudumia tukiwa na furaha"...amesema Dkt.Shemwelekwa.

Akizungumzia ukusanyaji wa Mapato ametoa rai kwa watumishi wote kushiriki na sio kuwaachi Kitengo cha fedha na Divisheni ya Biashara pekee kama ilivyozoeleka huku akitoa rai ya kuongeza uadilifu,uaminifu na kuziba mianya yote inayovujisha ama kuchepusha Mapato na kwamba atakayefanya hivyo hata mvumilia.
"Ndugu zangu tukakusanye Mapato kwa uaminifu na uadilifu ili yatumike kwa Maslahi mapana ya watu wote,atakaye thubutu kwenda kinyume atakumbana na mkono wa sheria" ameongeza

Dkt.Shemwelekwa amekumbusha watumishi kuwahi Kazini kama sheria,Kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma zinavyoelekeza na kwamba hiyo sio hiari ni takwa la Kisheria linalomtaka mtumishi kufanya kazi kwa saa nane kwa siku

Mary Chimoto na Hassan Ngonyani  wamesifu utaratibu mpya kiutendaji wa Mkurugenzi Dkt.Shemwelekwa na kwamba kilichobaki ni utekelezaji 

Mkuu wa Divisheni na Utumishi na rasilimali watu Dibogo Protas amesema kazi yake kwenda kutafsiri sheria,Kanuni na taratibu kwani watumishi Sasa wamekumbushwa upya wajibu wao.

Dkt.Rogers Shemwelekwa ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutumiza miaka mitatu Madarakani kwa kuendelea kuwekeza kwenye Miradi mikubwa ya Kimkakati nchini ikiwemo Kibaha Mji ambayo imenufaika na Soko kubwa lenye thamani ya Bilioni nane

Tuesday, March 26, 2024

KOKA AWASHUKURU KWA DHATI WANA CCM NA WANANCHI WA KIBAHA MJI KWA USHINDI WA MSANGANI

 


NA VICTOR MASANGU,KIBAHA

Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka kwa dhati wanachama wa ccm pamoja na wananchi wa Kata ya Pangani kwa kuweza kumchagua Yohana Gunze kuwa  diwani wa Kata ya Msangani katika uchaguzi mdogo uliomalizika hivi karibuni.


Koka ameyasema hayo wakati wa kikao màalunu  cha Halmashauri kuu ya chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mji chenye lengo la kujadili agenda mbali mbali kimaendeleo  pamoja na kujiandaa na chaguzi mbali mbali ikiwemo uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu.

Alisema Koka aliwapongeza viongozi mbali mbali kuanzia ngazi zote za chini hadi ngazi za juu kwa ushirikiano wao wa  dhati katika kipindi chote cha kampeni za uchaguzi wa udiwani hadi uchaguzi mwenyewe. 

Koka alisema kwamba amefarijika sana kuona wanachama na wananchi kukiamini chama cha mapinduzi na kumchagua kwa kishindo  mgombea udiwani wa kata ya Msangani kwa kushinda kwa kishindo kwa asilimia 99.20

"Nawashukuru sana wanachama wenzangu wa ccm pamoja na wananchi wote kwa ujumla wa kata ya  Msangani kwa kuweza kukiamini chama cha mapinduzi na kuibuka na ushindi mkubwa katika kata ya Msangani hii inaonyesha ni jinsi gani tulivyokuwa na mshikamano,"alisema Mbunge Koka.

"Ni kweli nilikuwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu zaidi lakini nashukuru kwa dhati viongozi na wananchi wa Jimbo la Kibaha kwa dua zenu na nashukuru Mungu nimerudi na nipo nanyi ili kuendeleza gurudumu la maendeleo,"aliongezea Koka.


Kadhalika Koka alibainisha kwamba wana CCM wote kwa sasa wanatakiwa kuwa na umoja na ushirikiano na kujipanga katika kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa pamoja na uchaguzi mkuu  ili kuweza kushinda.

Pia alisema pamoja na kuwa nje ya nchi lakini amekuwa akiendelea kufanya shughuli mbali mbali ikiwemo kushirikiana bega kwa bega katika kushauliana mambo ya maendeleo na kijamii,"alisisitiza Koka.
Katika hatua nyingine Koka alitoa pongezi kwa Rais wa awamu ya sita Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbali mbali ya kimaendeleo katika Jimbo la Kibaha mjini.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi (CCM) Mwalimu Mwajuma Nyamaka amesisitiza umoja na mshikamano kwa lengo la kuweza kukiimarisha chama.

Kikao maalumu  cha halmashauri kuu ya (CCM) Wilaya ya Kibaha mji imeweza kukutana na kujadili mambo mbali mbali ikiwemo kujiandaa na chaguzi mbali mbali za serikali za mitaa pamoja na uchaguzi mkuu.