ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, November 22, 2025

CLEMENCE MWANDAMBO ASHIKILIWA NA JESHI LA POLISI

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limethibitisha kumkamata mwalimu wa shule ya awali ya Saint Clemence, baada ya madai ya kusambaza maneno yanayodaiwa kuwa ya uchochezi kupitia mitandao ya kijamii. 

Taarifa hiyo imetolewa rasmi na Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, ikisema kuwa tukio hilo limefanyika tarehe 21 Novemba 2025 katika eneo la Uzunquni “A”, jijini Mbeya.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mtuhumiwa alikamatwa majira ya saa 5:20 asubuhi, kufuatia malalamiko yaliyowasilishwa polisi kwamba alikuwa ametumia kurasa zake za “Facebook” na “Instagram” kuchapisha taarifa zilizodaiwa kuhamasisha taharuki na kuweza kusababisha uvunjifu wa amani. Polisi wamesema mara baada ya kupokea taarifa hizo, waliendesha uchunguzi wa haraka ambao ulipelekea hatua ya kumkamata kwa ajili ya kuendelea na mahojiano.

Jeshi la Polisi limeeleza kuwa mitandao ya kijamii imeendelea kuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa mbalimbali, hivyo wananchi wanatakiwa kutumia majukwaa hayo kwa uangalifu na kufuata sheria za nchi. 

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, hatua kali zitachukuliwa kwa watu wote watakaobainika kutumia mitandao ya kijamii kuchochea vurugu, kuhatarisha usalama wa raia au kusambaza taarifa zisizokuwa sahihi zinazoweza kuathiri ustawi wa jamii.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa uchunguzi bado unaendelea na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika. 

Hata hivyo, polisi wamesisitiza kuwa hatua hii haikusudiwi kuzuia uhuru wa raia kujieleza, bali inalenga kuhakikisha uhuru huo unatumika kwa kufuata misingi ya sheria na kuheshimu haki za watu wengine.

Aidha, Jeshi la Polisi limewahimiza wananchi kutoa ushirikiano pindi wanapobaini matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii, ikiwemo uchochezi, uongo, matusi, au taarifa zinazoweza kuleta mgawanyiko katika jamii. 

Lengo lao ni kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa nchi yenye amani na utulivu, huku maendeleo ya teknolojia yakitumika kwa manufaa.

Kukamatwa kwa mwalimu huyo kumeibua mijadala mitandaoni, baadhi ya wananchi wakisema kuwa vyombo vya habari na mamlaka zinapaswa kufafanua zaidi kuhusu ni aina gani ya maneno yanaweza kufasiriwa kama uchochezi ili kuepusha mkanganyiko. 

Wengine wamepongeza hatua za polisi wakisema zinasaidia kudhibiti matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii ambayo yameongezeka kwa kasi katika miaka ya hivi karibuni.

Hadi sasa, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limesisitiza kuwa litatoa taarifa zaidi endapo kutakuwa na maendeleo mengine kuhusu kesi hiyo, huku likiwataka wanachama wa mitandao ya kijamii kuzingatia maadili na sheria wakati wa kuchapisha au kushiriki taarifa mtandaoni.

HAKIMU AKATAA KUTUPA JELA MWANAFUNZI ALIYEFIKISHWA KORTINI KWA KUIBA POMBE.


 
Mahakama ya Thika imevuta hisia za umma baada ya Hakimu Mkuu Stella Atambo kukataa kumhukumu kijana anayedaiwa kujaribu kuiba pombe ya whisky. 

Mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 23, alidaiwa kujaribu kuiba pombe yenye thamani ya KSh1,800 kutoka kwa Duka Kuu la Naivas. Uamuzi wa Hakimu Mkuu Atambo ulifuatia mazungumzo mafupi yaliyojaa maswali, ushauri, na msukumo wa suluhu la vitendo badala ya adhabu. 

Kwa nini Hakimu wa Thika alikataa kumtia hatiani mwanafunzi? Alipouliza kuhusu thamani ya whisky, mwendesha mashtaka alijibu kuwa ni KSh1,000 kabla ya kusahihisha na kugundua kuwa KSh1,800 zilionekana kwenye karatasi ya mashtaka. 

Alimkumbusha kijana huyo kwamba kosa dogo mara nyingi hukua na kuwa mzigo wa muda mrefu mara moja linaporekodiwa kama hatia. 

Baada ya kuuliza na kuthibitisha umri wake, Atambo alimwambia bado ana maisha marefu na aepuke makosa ambayo yamesalia kwenye faili rasmi. "Wameandika KSh1,800. Unajua ikifika kwa charge sheet inakuwa more expensive. Si uwalipe tu, tuachane na story nyingi, ju hii itakuwa record of previous conviction. Uko na miaka mingapi? Miaka 23, bado wewe ni mchanga sana," alisema.

Mwanafunzi huyo aliiambia mahakama kuwa alipendelea kulipa pesa hizo badala ya kufungwa jela, lakini alikosa pesa kwa vile hakuwa na kazi. Alipouliza ikiwa kuna mtu yeyote alikuja kumsaidia kulipa dhamana ya pesa taslimu, alisema binamu yake alikuwa akielekea kortini.

Kisha akabadilisha mjadala, akieleza kwamba alitaka kumtia hatiani kwa kutumia chupa ya whisky ya John Barr. "Je, hutaki ulipe pesa za duka kuu sasa. Nikuwachilie. Wamesema KSh 1,800; whisky inaitwa nini? Unajua hii inaitwa John Barr Whisky. Sitaki ujibu maombi yako na kukuhukumu kwa sababu ya chupa ya whisky," Atambo aliambia mahakama. 

Jinsi gani Hakimu wa Thika alimwokoa mwanafunzi kutoka katika hatia Akiwageukia mawakili waliokuwepo kortini, Atambo alihoji wangeweza kumfanyia nini kwani alikuwa kijana anayehitaji mwelekeo. 

Mawakili hao walisema walikubaliana na hakimu, wakieleza kuwa kiasi hicho kilitakiwa kumalizwa na duka kubwa. 

Hakimu Atambo aliwakazia zaidi na kuwakumbusha madai yao ya mara kwa mara kuhusu kuwashauri vijana. "Wakili unamfahamu huyo? Humjui. 

Lakini huyu hapa mtoto wa kiume mwenzako. Unaweza kumfanyia nini?" aliuliza. Hakimu huyo alionekana kuhalalisha kitendo cha mwanafunzi huyo, na kuongeza kuwa kuna uwezekano alitaka muda mfupi wa kupumzika na akaishia kufanya uamuzi mbaya. 

Kundi la mawakili lilikubali kukusanya pesa ili kupata KSh1,800 huku wakisubiri binamu kuwasili. 

Wakili mmoja alisema maafisa wangemrejesha kwenye seli huku wakishauriana jinsi ya kulipa kiasi hicho. 

Hakimu Atambo alitumia muda huo kumtia moyo kujifunza kutokana na usaidizi ulioonyeshwa na wataalamu wakubwa katika chumba hicho. 

Alimweleza mwanafunzi kwamba hatia ingechafua rekodi zake na kupunguza fursa za siku zijazo. "Unaona sasa hawa ni kaka zako wakubwa. Wanajua maana yake unapoiba whisky tu ili upate wakati mzuri na kupumzika. Wakufanyie kitu maana nikikutia hatiani itachafua rekodi yako. Ona ni sawa," aliongeza. 

Alimwagiza awasiiane na binamu yake na akamhakikishia kwamba mawakili walikuwa tayari kumsaidia kulipa kiasi hicho. Mpangilio huo ulimaanisha kuwa mwanafunzi angefidia duka kuu bila kupokea rekodi ya uhalifu. 

MABASI YA ESTER SIO YANGU WALA MKE WANGU: MWIGULU

Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba

 Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amevunja ukimya kuhusu uvumi unaoenezwa na baadhi ya watu kwamba mabasi ya kampuni ya Ester ni mali yake akisema jambo hilo sio la kweli na kuwataka Watanzania kutokubali kila wanachoelezwa.

“Siku hizi watu hawaogopi hata kusingizia jambo unakuta mtu hafanyi hata utafiti juu ya mtu anayetaka kumsema, juzi juzi nikasikia tumechoma magari ya Ester ya mbunge wa Iramba Magharibi, magari yake yanaitwa Ester ameyaita Ester jina la mke wake,”…

“Mke wangu mimi haitwi Ester anaitwa Neema, wanasema basi kama sio ya mke wake yatakuwa ya mama yake mama yangu binti wa kiislamu anaitwa Asha Ramadhani Mohamed,”


Dk.Mwigulu ambaye ametoa ufafanuzi huo IJUMAA ya Novemba 21, 2025 wakati akizungumza na mamia ya wananchi kwenye viwanja vya Bombadia Manispaa ya Singida, amesema yeye amezaliwa katika familia ya kifugaji ambayo huruhusiwi hata kufanya biashara ya miwa hivyo hajawahi kufanya biashara yeyote.

“Nimeingia huku serikalini uwekezaji mkubwa ninaoufanya ni kusomesha watoto na nina kundi la watoto zaidi ya 500 ninaowasomesha, nimewekeza kwenye huduma za watu,”amesema Dk.Mwigulu.

MBUNGE JIMBO LA KIBAHA VIJIJINI ATUA KWA KISHINDO NA KUTEMA CHECHE KWA WANANCHI

 


NA VICTOR MASANGU, KIBAHA 


Mbunge wa Jimbo la Kibaha vijiji Homoud Jumaa ameahidi  kutekeleza ilani ya chama cha mapinduzi (CCM)  kwa vitendo  ikiwemo kusimamia suala zima la kuwahudumia wananchi ipasavyo katika  mambo mbali mbali  kwa ajili ya kuwaletea chacu ya maendeleo katiika nyanja tofauti.

Jumaa ameyabainisha hayo wakati wa halfa fupi ya kumpokea rasmi kutokea Mkoani Dodoma ikiwa ni siku chache  zimepita baada ya kuapishwa rasmi kuwa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini  ambapo sherehe hiyo imehudhuliwa na na viongozi wa chama cha mapinduzi, wananchama pamoja na wananchi kutoka maeneo tofauti.

Mbunge huyo amesema kwamba kwa sasa uchaguzi umeshamalizika na kwamba kitu kikubwa amewaomba wanachama wote na wananchi kuhakikisha kwamba wadumisha hali ya amani na utulivu wa nchi na kuepukana na vurugu ambazo hazina maana na badala yake washikamane katika kukijenga chama pamoja na kushiriki kikamilifu katika mambo ya kimaendeleo.

"Nawashukuru kwa dhati viongozi wangu wa chama cha mapinduzi, wanachama wa ccm pamoja na wananchi wote kwa kuweza kuniamini kwa mara nyingine na kuweza kunipitisha tena kuwa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini kitu kikubwa ambacho ninaweza kuwaahidi ni kuendelea kutoa ushirikianio wa hali na mali katika kuhakikisha  ninawaletea maendeleo mbali mbali,"amesema Jumaa.  

Katika hatua nyiingine   Mbunge huyo amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. kwa kuweza kuchaguliwa kwa kishindo pamoja na kuweza kutoa hotuba yake nzuri ambayo imelenga kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo kwa wananchi katika sekta mbali mbali.

Kwa upande wake Diwani mteule wa kata ya Kwala Mansuri Kisebengo amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kibaha vijijini kwa kuweza kuchaguliwa kwa kishindo na wananchi na kwamba ana imani kubwa wataweza kuwatumikia wananchi na kuwaletea chachu ya maendeleo.

Nao baadhi ya wananchi ambao wamepata fursa ya kuhudhulia katika halfa hiyo wamesema kwamba wana imani kubwa na serikali mpya  ya awamu  ya sita  pamoja na kumpongeza Mbunge wa Jimbo hilo la Kibaha vijijini  Hamoud Jumaa kwani ataweza kuleta mafanikio ya kimaendeleo  kwa wananchi wake.

 Mbunge wa Jimbo la Kibaha vijijni Mhe. Hamoud Juma amepokelewa kwa kishindo kikubwa na viongozi CCM, wananchama pamoja na wananchi sambamba na madiwani  mbali mbali za Jimbo la KIbaha vijijini.