ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Sunday, January 11, 2026

MASHABIKI WA SIMBA USO KWA USO NA MASHABIKI WA PAMBA JIJI


 Ni Januari 12, 2026… Mwanza inawaka moto wa sherehe!!

Katika kuadhimisha Siku ya Mapinduzi ya Zanzibar, jiji la Mwanza linawaletea burudani ya kipekee, mechi ya kirafiki ya kihistoria… Mashabiki wa Simba vs Pamba Jiji!

Watachuana mastaa wa zamani waliowahi kung’ara kwenye timu hizi mbili maarufu nchini – ni kumbukumbu, ni burudani, ni hadithi za mpira zinazofufuka tena!

Na si mpira tu! Kutakuwa na michezo ya kina dada, kina mama, zawadi kibao na burudani ya nguvu kwa familia nzima!

Jumatatu ya tarehe 12 Januari 2026, kuanzia saa nane mchana, pale Uwanja wa Nyamagana – usikose kushuhudia historia ikiandikwa upya!

MAPINDUZI DAY – Mwanza inasherehekea kwa mshikamano, amani na burudani ya kufungia mwaka!

Mgeni rasmi: Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mh. Said Mtanda

GGML YATOA MSAADA WA MILIONI 50 KUSHEREHEKEA MWAKA MPYA NA WATOTO YATIMA

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) Bw. Duan Campbell (kati kati) akipeana mikono na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mh.Martine Shigela (wa tatu kutoka  kulia) baada ya kukabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni 50 kwa kituo cha Watoto Yatima cha Moyo wa Huruma kilichopo mkoani Geita mwishoni mwa wiki. Kituo hicho kimeanzishwa kwa ushirikiano wa pamoja kati ya GGML , Halmashauri ya Geita na Kanisa Katoliki . Wa pili kwa upande wa kulia ni Askofu  Flavian Kasala wa Jimbo Katoliki la Geita.

 Na Mwandishi Wetu, Geita

Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya uwajibikajo kwa jamii kwa kutoa msaada wa hundi ya shilingi milioni 50 kwa kituo cha kulelea watoto yatima cha Moyo wa Huruma wakati wa sherehe za kuukaribisha mwaka mpya 2026 zilizofanyika kituoni hapo, mkoani Geita  mwishoni mwa wiki.


Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mfano wa hundi hiyo kwa uongozi wa kituo hicho, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Bw. Duan Campbell, amesema uwepo wa GGML katika moa wa Geita haujikiti tu katika uchimbaji wa dhahabu bali pia katika kuigusa jamii kwa kujenga jamii yenye afya, matumaini na fursa hasa kwa Watoto walioko katika mazingira magumu.


“Kujenga jamii yenye afya na yenye matumaini ni sehemu ya jukumu letu kama kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini. Uwekezaji wetu katika maendeleo ya kijamii unaendelea kuwa kichocheo cha ukuaji wa ndani, kikanda na kitaifa. Tunajivunia kushirikiana na Moyo wa Huruma na kuona jinsi maisha ya Watoto yanavyobadilika kwa misaada na fursa wanazopata.


“Tunajisikia fahari kuona watoto wanaolelewa katika kituo hiki wanapata mafanikio, ikiwemo wale wanaohitimu katika vyuo vikuu,”


“Hivyo, kama wadau wa maendeleo ya jamii, GGML tutaendelea kuhakikisha kuwa kituo hiki kinapata mafanikio zaidi na kushirikiana na Serikali katika kutokomeza watoto wa mitaani,” amesema Bw. Campbell. 


Kituo cha Moyo wa Huruma kilianzishwa mwaka 2006 kupitia ushirikiano kati ya GGML, Jimbo Katoliki la Geita na Halmashauri za Serikali ya mkoa wa Geita, kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kukabiliana na changamoto za watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu—ikiwemo watoto waliopoteza wazazi kutokana na VVU/UKIMWI.


Kupitia mfuko wa GGML Kili Challenge Against HIV & AIDS, GGML imekuwa ikishirkiana na wadau mbalimbali ikiwemo Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) kukusanya rasilimali kwa kupanda Mlima Kilimanjaro kwa lengo la kusaidia watu wanaoishi na VVU pamoja na taasisi zinazohudumia makundi yaliyo katika hatari, ikiwemo Kituo cha Moyo wa Huruma. Juhudi hizi zimewezesha kujengwa kwa kituo hicho ambacho kimeweza kukua kutoka kulea watoto 12 mwaka 2006 hadi kuwahudumia zaidi ya watoto 100 kwa sasa, wakiwemo wahitimu wa vyuo vikuu na watumishi wa umma.


Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mh. Martine Shigela ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, ameipongeza GGML kwa kuendelea kusaidia makundi mbalimbali katika jamii.


“Napenda kuwapongeza GGML kwa ibada hii ya kulea kituo hiki chenye watoto wakiwemo watoto wadogo na wakubwa ambao baadhi yao ni wahitimu wa vyuo vikuu mbalimbali wanaosomea masomo ya Sayansi na wale walioajiriwa Serikalini ambao wamepitia katika kituo hiki,” amesema RC Shigela


Akizungumza katika hafla hiyo, Askofu wa Jimbo Katoliki la Geita, Askofu Flavian Kasala amesisitiza umuhimu wa jamii kuendelea kushirikiana katika kujiepusha na kuzuia vyanzo vinavyopelekea ongezeko la watoto wanaoishi katika mazingira magumu ambao hukosa msaada na hatimaye kutapakaa mitaani.


“Matatizo mbalimbali katika jamii ikiwemo changamoto zinazotokana na uzazi katika umri mdogo, maambukizi ya Virusi vya UKIMWI na ugumu wa maisha yamepeleka uwepo wa watoto wa mitaani wenye uhitaji kutoka katika jamii”


“Hivyo, kituo kama hiki, kinatupa somo la kuwapa faraja watoto wenye uhitaji na kuweka jitihada za makusudi za kuzuia ongezeko la watoto hao wanaoishi katika mazingira magumu,” amesema Askofu Kasala.


Akizungumza mara baada ya hafla ya kukabidhi hundi, Mwakilishi wa GGML kutoka idara mahusiano Mussa Shunashu ameeleza majukumu ya GGML katika kituo hicho kilichoanzishwa kwa ushirikiano kati ya GGML, Jimbo Katoliki la  Geita na Halmashauri za Mkoa wa Geita.


“GGML katika kuanzisha na kuendeleza kituo hiki, ilikuwa na wajibu wa kutoa fedha na halmashauri wakati huo ilikuwa na wajibu wa kutoa eneo na Jimbo Katoliki la Geita lilikuwa na wajibu wa kusimamia malezi bora na tunashukuru mpaka leo hii kituo hiki kinaendelea kutoa huduma,” 


“Kama ilivyo katika mikoa mingine, mkoa wa Geita pia una watoto yatima, ambao walipoteza wazazi/ walezi kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ugonjwa wa UKIMWI, hivyo, tuliamua kuwa na kituo hiki kwa msaada wa malezi na elimu kwa watoto wenye uhitaji,” amesema.


Katika hafla hiyo ya kuadhimisha Mwaka Mpya 2026, GGML pia ilitoa zawadi mbalimbali, kuandaa burudani, michezo na chakula kwa watoto na walezi wao, pamoja na mazungumzo ya faraja yaliyoimarisha dhana ya malezi ya pamoja na mshikamano wa kijamii.


Mmoja wa watoto wanaolelewa katika kituo hicho (jina limehifadhiwa) amesema msaada unaotolewa na GGML na wadau wengine umewapa nguvu ya kuota ndoto kubwa.


“Tunajisikia kama tupo nyumbani. Tunathamini sana kuona kuna watu wanaojali maisha yetu na mustakabali wetu,” amesema mtoto huyo.


Hatua hii inaendelea kuonesha utekelezaji wa sera ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) ya GGML, inayolenga kuimarisha afya, elimu na ustawi wa watoto na familia katika mkoa wa Geita na Tanzania kwa ujumla, kwa kutambua kuwa maendeleo endelevu huanza na uwekezaji kwa watu.

MADAKTARI IRAN WADAI KUZIDIWA NA WAGONJWA

 


Huku maandamano nchini Iran yakiendelea na mamlaka ya Iran ikitoa maonyo yaliyoratibiwa kwa waandamanaji, daktari na muuguzi katika hospitali mbili waliiambia BBC kwamba vituo vyao vya matibabu vilikuwa vimejaa watu waliojeruhiwa.

Daktari mmoja alisema hospitali ya macho ya Tehran ilikuwa iko katika hali ngumu, huku BBC pia ikipokea ujumbe kutoka kwa daktari katika hospitali nyingine ikisema haikuwa na madaktari bingwa wa kutosha kukabiliana na ongezeko la wagonjwa.

Siku ya Ijumaa, Rais wa Marekani Donald Trump alisema Iran ilikuwa katika "matatizo makubwa" na akaonya "ni vyema isianze kufyatua risasi kwa sababu sisi pia tutaanza kufyatua risasi".

Katika barua kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Iran iliilaumu Marekani kwa kuyageuza maandamano hayo kuwa kile ilichokiita "vitendo vya uasi na uharibifu mkubwa".

CHANZO BBC SWAHILI

MISRI YAWAVUA UBINGWA IVORY COAST NA KUTINGA NUSU FAINALI AFCON

 

TIMU ya Misri imefanikiwa kwenda Nusu Fainali Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya mabingwa watetezi, Ivory Coast usiku wa jana Uwanja wa Adrar mjini Agadir nchini Morocco. 

Mabao ya Mafarao jana yamefungwa na mshambuliaji, Omar Khaled Mohamed Abdelsalam Marmoush wa Manchester City dakika ya nne, beki Ramy Hisham Abdel Aziz Mostafa Rabia wa Al Ain ya Falme za Kiarabu (UAE) dakika ya 32 na kiungo mshambuliaji, Mohamed Salah anayekiputa Liverpool dakika ya 52.

Kwa upande wao mabingwa wa Fainali za 2023 nyumbani, Ivory Coast mabao yao yalifungwa na beki wa kushoto wa Zamalek,  Ahmed Mohamed Abou El Fotouh Mohamed aliyejifunga dakika ya 40 na beki wa kulia wa Strasbourg ya Ufaransa alikozaliwa dakika ya 73.

Kwa matokeo hayo, Misri itakutana na Senegal katika Nusu Fainali Jumatano ya Januari 14 kuanzia Saa 1:00 usiku Uwanja wa Tangier Grand mjini Tangier, wakati Nusu Fainali nyingine wenyeji, Morocco watamenyana na Nigeria siku hiyo hiyo kuanzia Saa 4:00 usiku Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat.

NIGERIA YAICHAPA ALGERIA 2-0 NA KUTINGA NUSU FAINALI AFCON

 

TIMU ya Nigeria imefanikiwa kwenda Nusu Fainali Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Algeria usiku huu Uwanja wa Marrakech Jijini Marrakech nchini Morocco.

Nigeria ilipata ushindi wa 2-0 dhidi ya Algeria katika robofainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 Uwanja wa Marrakech Jumamosi, na kujikatia tiketi ya kutinga nusu fainali dhidi ya wenyeji Morocco Jumatano saa 9 alasiri. (saa za ndani) katika Uwanja wa Rabat wa Prince Moulay Abdellah.

Victor Osimhen alitangulia kufunga katika dakika ya 47, akitumia vyema mpira wa Alex Iwobi. Mshambulizi huyo aliipita ngome ya Algeria kabla ya kumtungua kipa Alexandre Zidane na kuwapa Super Eagles bao la kuongoza mapema kipindi cha pili.

Dakika kumi tu baadaye, Akor Adams alifunga bao la Nigeria mara mbili katika dakika ya 57. Osimhen tena alichukua jukumu muhimu, kutengeneza nafasi na kutoa pasi nzuri kwa Adams, ambaye alimaliza kwa utulivu mbele ya Zidane na kufanya matokeo ya mwisho kuwa 2-0.

Algeria, inayojulikana kwa safu duni ya ulinzi katika michuano hiyo, imefungwa kwa mara ya kwanza kwenye mechi hii.

HAYA HAPA MATOKEO YA KITAIFA WA KIDATO CHA PILI , DARASA LA NNE 2025

 

Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) limetangaza rasmi matokeo ya Upimaji wa Kitaifa wa Kidato cha Pili (Form Two National Assessment – FTNA 2025) pamoja na Upimaji wa Kitaifa wa Darasa la Nne (Standard Four National Assessment – SFNA 2025).

Matokeo hayo yametangazwa Januari 10, 2026, na Katibu Mtendaji wa NECTA, Profesa Said A. Mohamed, wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaam.