ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, April 16, 2022

Msalabani (Official Live Music) - Neema Gospel Choir (AICT Chang’ombe)

 Alama ya ukombozi wetu. Kwa upendo mkuu Yesu alijitoa kufa kwa mateso na aibu ili sisi wanadamu tuokolewe dhambini na kupatana na Mungu tena.

1Kor 1:18 π—Ÿπ˜†π—Ώπ—Άπ—°π˜€: Msalabani pa Mwokozi, (At the cross of our savior) Wapatikaana ukombozi. (There’s redemption) Ni kazi ya thamani yake Yesu (It’s the precious work of Jesus) Msalabani pa Mwokozi (At the cross of our savior) Msalabani pa Mwokozi, (At the cross of our savior) Wapatikaana ukombozi. (There’s redemption) Ni kazi ya thamani yake Yesu (It’s the precious work of Jesus) Msalabani pa Mwokozi (At the cross of our savior) Tumesamehewa dhambi hatuna deni, (Pardoned our sins, we are dept free) Amelipa yote Bwana hatuna deni , (He paid it all, we are dept free) Ni kazi ya thamani yake Yesu (It’s the precious work of Jesus) Msalabani pa Mwokozi (At the cross of our savior) Unyenyekevu uvumilivu na upendo (Humility, perseverance, and love) Huruma nyingi na fadhili kwetu (For his mercifulness to us) Ni sifa za thamani zake Yesu (It’s the precious attribute of Jesus) Msalabani pa Mwokozi (At the cross of our savior) Tumesamehewa dhambi hatuna deni, (Pardoned our sins, we are dept free) Amelipa yote Bwana hatuna deni , (He paid it all, we are dept free) Ni kazi ya thamani yake Yesu (It’s the precious work of Jesus) Msalabani pa Mwokozi (At the cross of our savior) On this 3rd drop Msalabani from π—¦π—œπ—‘π—š π—ͺπ—œπ—§π—› π—§π—›π—”π—‘π—žπ—¦π—šπ—œπ—©π—œπ—‘π—š (Worship in Spirit) Project held on 03 December 2021 at CCC Upanga Auditorium, We would like to thank God for the whole team, The Song Leader Minister - Samwel Limbu, Our Church - AICT Chang’ombe, The Committee, Our Sponsors & All contributions and support from everyone. Song Written by Fredrick Masanja Credits: Video, Directed & Edited by: Johnson Amigo Audio - Captured, Mixed & Mastered by: Frester’s Record (Fredrick Masanja) FOH and Backline Provided by;: ABE Professional Sound Sound Engineer; Jeddy DC Ass. Sound Engineers; Greyson Bruno & George Shoo Lights: Allan Lights Stage: Hugo Domingo

MAOFISA BOT WABAINIKA KUPIGA Tsh 3.99 BILIONI ZA NOTI CHAKAVU.

 


Kukosa uadilifu na upungufu wa udhibiti ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kumesababisha hasara ya Sh3.99 bilioni kwa noti ambazo hazikuwa na vigezo vya kuwa chakavu kati ya Januari 2019 hadi Septemba 2019.


Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya Serikali Kuu ilisema noti 399,392 zenye thamani ya Sh3.99 bilioni hazikuwa na vigezo vya kupewa noti mpya na zilipewa noti mpya kwa udanganyifu. Noti hizo ni zaidi ya asilimia 95 ya noti zote chakavu katika kipindi hicho.


“Katika kipindi hcha Januari 2019 hadi Septemba 2019, nilibaini BoT ilipokea noti za Sh4.17 bilioni ambazo ni noti 417,006 za Sh10,000 ambazo zilidaiwa kuwa ni chakavu, ili zibadilishwe na kutolewa noti mpya.


“Udanganyifu uliofanywa na maofisa wawili na watunza fedha wanne wa Benki Kuu,” ilieleza ripoti hiyo.


Ripoti iliendelea kuchanganua kuwa noti 1,427 zenye thamani ya Sh14.27 milioni zilikuwa safi na zilifaa, hivyo hazikuwa na sifa ya kuwa noti chakavu.


“Nilibaini kuwa noti 16,187 zenye thamani ya Sh161.87 milioni zilikidhi vigezo vya kurejeshwa Benki Kuu na kutolewa noti mpya,” ilisema ripoti hiyo.


Ripoti hiyo ilieleza kuwa asilimia 95 ya fedha zilibainika hazikuwa chakavu, wahusika walifanya udanganyifu kwa kukata noti safi 199,696 vipande vilivyotoa noti takribani 399,392 vyenye thamani ya Sh10,000 kila kimoja kuvibandika kwenye karatasi nyeupe kisha wakadai noti mpya.


Kutokana na ubadhirifu huo, Benki Kuu ilipata hasara ya Sh20.68 milioni ya kuchapisha na kutoa noti 199,696 zilizotumika katika udanganyifu huo.


Dosari nyingine iliyobainika ni kutokutunza daftari la wateja waliokuwa wanabadilisha fedha chakavu, hivyo CAG hakuwatambua wateja waliobadilisha fedha chakavu katika kipindi husika.


Licha ya kikwazo hicho, alisema “nilibaini wateja 24 walikuwa na mtindo wa kutembelea Benki Kuu mara kwa mara kwa ajili ya kufanya miamala ya noti chakavu, ambao wamehusishwa kushirikiana na wafanyakazi wa benki hiyo kutekeleza mpango huo.”


CAG alipendekeza Gavana wa BoT achukue hatua stahiki za kinidhamu dhidi ya wafanyakazi waliohusika katika ubadhirifu huo na kuhakikisha kunakuwapo usimamizi madhubuti wa miamala yote ya noti chakavu zinazobadilishwa Benki Kuu na kwenye Benki zote za Biashara.


Ubadhirifu maofisa Uhamiaji KIA

Katika ripoti hiyo, CAG alieleza kuwa Serikali imepata hasara ya Sh2.42 bilioni kutokana na stika 21,208 za viza zinazodaiwa kughushiwa na kumbukumbu zake kufutwa kwa makusudi kwenye Mfumo wa Maombi ya Viza (VAS) na maofisa uhamiaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).


Ilielezwa kati ya Januari mosi 2019 hadi Juni 30, 2019 ukaguzi ulibaini Watanzania 41 na wageni 107,119 waliwasili nchini kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).


Wageni 33,558 waliwasili kupitia KIA, ingawa taarifa zao ambazo ni pamoja na stakabadhi za mapokezi ya fedha (ERV), fomu za kuingia nchini, pamoja na taarifa za uwekaji fedha benki hazikuweza kupatikana.


Kutokana na sababu hiyo, ripoti hiyo ilieleza CAG hakujua ni kiasi gani cha mapato ambayo Serikali ilipaswa kupata kutoka kwa wageni hao.


“Katika uchunguzi zaidi, niligundua taarifa za stika 21,208 za viza za wageni waliowasili nchini kupitia KIA zilifutwa kutoka kwenye kanzidata ya mfumo wa ‘VAS’.


“Stika hizo zilizoondolewa ziliwahusu wageni ambao walipaswa kulipa viza walipowasili, lakini maofisa 32 wa Idara ya Uhamiaji KIA walifanya njama na kuwapatia wageni hao stika za viza za kughushi na kujipatia Sh2.42 bilioni kutoka kwao,” ilieleza ripoti hiyo.


Hivyo, alipendekeza Idara ya Uhamiaji ichukue hatua stahiki za kisheria na kinidhamu dhidi ya maofisa 32 wa idara hiyo kituo cha KIA ambao wanahusika kuisababishia Serikali hasara.

VIGOGO WATATTU WAFYEKA 215 MILIONI ZA POSHO.

 


Ukaguzi uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Charles Kichere katika Bohari ya Dawa (MSD) umebaini taasisi hiyo ya umma kutumia jumla ya Sh215.99 milioni kulipa watumishi watatu posho ya kujikimu walipokwenda China.


Mbali na hilo, CAG alibaini taasisi hiyo kushindwa kwa asilimia 66 kutimiza mahitaji ya bidhaa za dawa na vifaatiba kwa wateja, ununuzi usiozingatia sheria pamoja na kuwepo kwa mikataba iliyosainiwa bila kupekuliwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.


Katika ripoti yake kwenye ukaguzi na ufanisi uliofanywa MSD, Kichere alibaini barua yenye Kumb. Na. CEA.169/178/03/18 ya Oktoba 13, 2020 ya uteuzi wa maofisa watatu kwenda China kwa ajili ya kutafuta watengenezaji ili kusambaza mashine 71 za kusafisha damu kwa wagonjwa wa figo ‘hemodialysis’ na kutoa ushauri kwa Serikali juu ya ununuzi wa mashine hizo.


Alisema mchakato huo haukuhusisha kitengo cha usimamizi wa ununuzi na bodi ya zabuni, bali mchakato mzima ulifanywa na watu watatu wakiwa China kwa Sh2.79 bilioni. “Nilibaini kuwa, ili kuwezesha ununuzi wa mashine hizo, MSD ilitumia Sh215.99 milioni kulipa watumishi watatu posho ya kujikimu kwa siku 61 pamoja na gharama za usafiri kwenda China kwa madhumuni ya mazungumzo na kutafuta viwanda. Nina shaka na mchakato mzima wa ununuzi na matumizi ya fedha za umma,” alisema Kichere.


Kiwanda cha Idofi

Katika ripoti ya mapitio ya uwekezaji katika mashirika ya umma, Kichere alieleza kuchelewa kuanza uzalishaji kwa viwanda vinavyomilikiwa na mashirika ya umma huku akigusia uanzishwaji wa kiwanda cha kutengeneza glovu bila kufanya upembuzi yakinifu wa kibiashara.


Alisema baada ya kupitia muhtasari wa mkutano wa 157 wa Bodi ya Wadhamini ya MSD, iliibua wasiwasi wa upembuzi yakinifu na kuiagiza taasisi hiyo kueleza kwa uwazi uwezo wao katika masuala ya fedha, utaalamu, teknolojia na kuonyesha chanzo cha asilimia 10 ya malighafi kwa ajili ya uzalishaji kutoka vyanzo vya ndani.


CAG alibaini ripoti ya upembuzi yakinifu ya MSD ya Septemba 2020 juu ya kuanzishwa kwa eneo hilo la viwanda haikujumuisha mchanganuo wa biashara pamoja na mpango wa kina ulioandaliwa ili kupata hoja za kuanzisha mradi na kutathmini faida, gharama na vihatarishi vya biashara.


Ununuzi

Katika ripoti hiyo, Kichere alisema taasisi hiyo ilifanya ununuzi wa bidhaa bila mikataba wenye thamani ya Sh9.90 bilioni na Dola 1.42 milioni za Marekani kinyume na kanuni ya 233(1) (2) na kanuni ya 75 ya kanuni za ununuzi wa umma za mwaka 2013.


Katika hatua nyingine, CAG amebaini mikataba yenye thamani Sh17.92 bilioni iliyotolewa na kusainiwa bila kupekuliwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kinyume na kanuni ya 59 (1)(2) na kanuni ya 2 ya kanuni za ununuzi wa umma za mwaka 2013.


Hata hivyo, CAG Kichere alisema katika ukaguzi wa ununuzi alibaini utekelezaji wa mikataba sita ya ununuzi ya Sh43.98 bilioni katika bohari hiyo ambayo haikuwa katika bajeti wala kujumuishwa katika mpango wa ununuzi wa mwaka.


Akichangia mada bungeni Aprili 13, mbunge wa Handeni, Reuben Kwagilwa alisema kuna haja kwa sheria ya ununuzi wa dawa irekebishwe kwa kuwa inatoa mianya mitatu mibaya inayosababisha dawa kununuliwa kwa bei isiyo halisi.


Akijibu hoja hiyo, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu alisema, “sheria inaweza kuwa na changamoto, tatizo lililo MSD siyo sheria ya ununuzi ya umma, lakini mipango mibaya ya utekelezaji, MSD hiyohiyo kwa sheria hii hii tulianza kufanya vizuri, sheria tunayo lakini tunaweza kubadilisha sheria, lakini kama hatuna mipango mizuri hatutafanikiwa, Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo tunalifanyia kazi.”

BAKWATA, KIVULINI waendesha kongamano la maadili wilayani Misungwi

 

Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Mkoa Mwanza kwa kushirikiana na shirika la kutetea haki za wanawake na watoto (KIVULINI) limeendesha kongamano la kuhamasisha maadili katika jamii wilayani Misungwi ili kusaidia kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Kongamano hilo limefanyika Jumamosi Aprili 16, 2022 katika Msikiti Mkuu wa Waslamu Misungwi na kuhudhuriwa na waumini mbalimbali wa dini hiyo ambapo lengo ni makongamano ya aina hiyo kufanyika katika Wilaya zote za Mkoa Mwanza.

Sheikh wa BAKWATA Mkoa Mwanza, Sheikh Hassan Kabeke amesema kongamano hilo la Malezi Bora, Tabia Njema na Misingi ya Ndoa linalenga kujadili na kuandaa mapendelezo yatakayoeleza sababu za kuporomoka kwa maadili katika jamii na kuwasilishwa serikalini kwa ajili ya hatua za utekelezaji.

Amesema kuporomoka kwa maadili katika jamii kunasababisha ufa katika ndoa ambapo matokeo yake ni kuibuka kwa wimbi la watoto wanaokimbilia mtaani kwa sababu ya kukosa malezi bora.

Sheikh Kabeke amekemea tabia ya wazazi hususani akina baba kukosa muda wa kulea watoto akisema wako ‘busy’ na kuacha watoto kulelewa na akina mama pekee ambapo matokeo yake ni kuibuka kwa ufa uitwao liwatwi (ulawiti).

“Baada ya maadili kuporomoka, watoto wadogo wa kindagate, shule za Msingi, Sekondari na vyuo wanaangukia kwenye hatari ya kuingiliana kinyume na maumbile, mbaya zaidi imefika hatua baadhi ya familia wanawaalika hadi mashoja kusherehesha sherehe zao, je ni kweli tumeupokea ushoga? (sauti zinasikika hapa), huo ni ufa kwenye ndoa” anaonya Sheikh Kabeke.

Sheikh Kabeke ameongeza kuwa kukosekana kwa maadili katika jamii pia kumesababisha unyanyasaji wa kijinsia kwenye ndoa ambapo imekuwa kawaida mme kumnyanyasa mke na mke kumnyanyasa mme.

“Imefika mahali wanaume hawafanyi kazi wanabaki kwenye kahawa, wanawake ndio asubuhi utakutana nao kwenye daladala wanahangaika na mabeseni kwenda kutafuta hela ya kutunza familia, mme akirudi jioni anaanza kuhoji chakula” Sheikh Kabeke amekemea tabia hiyo akiwataka wanaume kuwajibika katika ndoa zao.

Pia Sheikh Kabeke ametoa rai kwa wanandoa kuwa na muda wa kukaa pamoja na kuzungumza masuala ya kulea familia, akisema “Mwanamke ananatumia kanga kufikisha ujumbe kwa mmewe kwa sababu hakuna muda wa kuongea, inabidi avae kanga, utamaliza mabucha yote lakini nyama ni ile ile. Hivi ni sawa tuwasiliane kwa mfumo huo wa kanga? Tena ndoa za kiislamu? Wanandoa wanawekeza muda mwingi kwenye simu kuliko kukaa pamoja na kujadili masuala ya ndoa.

Katika hatua nyingine Sheikh Kabeke amelipongeza shirika la KIVULINI kwa jitihada zake kubwa za kusaidia kurudisha maadili kwenye jamii, kuwasiaidia watu waliodhalilishwa na wenye matatizo mbalimbali yanayohusiana na vitendo vya ukatili wa kijinsia.

“ Mungu awape nguvu tuzunguke nao Mkoa mzima wa Mwanza. Tunataka baada ya Ramadhan tutoke na andiko litakalosaidia maadili katika ndoa kwani sisi BAKWATA tunapinga watoto wa mitaani, Kivulini wanapinga na Misungwi naamini mnapinga” amesema Sheikh Kabeke.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la KIVULINI, Yassin Ally amesema wimbi kubwa la ndoa zinazofungwa mwezi wa Shaban linapaswa kujadiliwa kwani nyingi hazidumu na matokeo yake zinakuwa chanzo cha ongezeko la watoto wa mitaani.

“Unakuta mwanaume anatafuta mwanamke wa kumtumikisha, ampikie futari, akijinasibu kwamba funga yake itapokelewa. Inabidi wafungisha ndoa, masheikh wetu hili nalo tulijadili, huenda kuna mapungufu mengi katika misingi ya kuzilea na kuzifuatilia hizi ndoa ndio maana hazidumu” amesema Ally.

Yassin pia amewasihi wanandoa kuishi kwa furaha na kutaniana kwani ukali umezidi miongoni mwa wanandoa tofauti na wapokuwa nje na nyumbani. “unakuta mwanaume akiwa kwa mama ntilie anamtania, leo umependeza ila akiwa kwa mkewe ni mwendo wa kumuamrisha, wewe njoo hapa, chakula kiko wapi” amedokeza Ally.

Lakini pia Ally amesisitiza kuwa jukumu la kulea watoto ni la wazazi hivyo ni vyema wakaishi kwa maelewano na kuwalea watoto katika misingi ya maadili inayozingatia kumcha Mungu, kuwapa haki za msingi ikiwemo kupata elimu kwani Serikali imeboresha mazingira ya kuhakikisha kila motto anakwenda Shule.

Kwa upande wake Sheikh wa Wilaya Misungwi, Sheikh Hussein Hussein amesema wanandoa wanapokuwa na uchumi imara, watoto wanaepuka hatari ya kukimbilia mitaani na hivyo kushauri vijana wa kiislamu kutobweteka na kuunda vikundi vya uzalishaji mali.

Baadhi ya washiriki wa kongamano hilo akiwemo mzee Hussein Manyilizu wamesema ndoa nyingi hazidumu kwa sababu vijana hukutana kwenye mitandao ya kijamii na kuoana tofauti na zamani ambapo wazee walikuwa wakifanya utafiti wa familia ya kuoa, akisema “siku hizi wanaangalia utajiri na siyo maadili, matokeo yake ndoa hazidumu”.

Naye Ibrahim Mhebi amewaasa vijana wenzake kufanya kazi badala ya kuamkia kwenye vijiwe vya kahawa na michezo haramu ya kubashiri kwani inadhorotesha uchumi wao na kuzikimbia familia. “Una elfu 50 unaamkia kwenye michezo ya ku-BET unaliwa yote, hapo ndoa Sheikh lazima uikimbie. Mimi naomba BAKWATA ije na mifumo ya kutusaidia vijana kujikwamua kiuchumi hatua itakayotusaidia kutunza familia” ameomba Mhebi.
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Sheikh wa BAKWATA Mkoa Mwanza, Sheikh Hassan Kabeke (katikati) akifungua kongamano la Malezi Bora, Tabia Njema na Misingi ya Ndoa lililofanyika wilayani Misungwi. Kulia ni Sheikh wa BAKWATA Wilaya Misungwi, Sheikh Hussein Hussein na kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji shirika la KIVULINI, Yassin Ally.
Sheikh wa BAKWATA Wilaya Misungwi, Sheikh Hussein Hussein (kulia) akizungumza kwenye kongamano hilo. Katikati ni Sheikh wa BAKWATA Mkoa Mwanza, Sheikh Hassan Kabeke na kulia ni Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally.
Washiriki wa kongamano hilo ambao ni waumini wa dini ya kiislamu wakimsikiliza Sheikh wa Wilaya Misungwi, Sheikh Hussein Hussein.
Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally akichangia mada kwenye kongamano hilo lililoandaliwa na BAKWATA Mkoa Mwanza kwa kushirikiana na KIVULINI.
Washiriki wakifuatilia kongamano hilo.
Mmoja wa washiriki wa kongamano hilo, Ibrahim Mhebi akichangia mada kwenye kongamano hilo.
Kongamano hilo, pamoja na mambo mengine linalenga kuhamasisha wanajamii kuzingatia maadili bora, kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia na kusomesha watoto/ kuondoa utoro mashuleni ambapo baada ya kutamatika katika wilaya zote za Mkoa Mwanza, BAKWATA itaandaa mapendekezo yatakayowasilishwa serikalini kwa ajili ya utekelezaji.
Mmoja wa washiriki akichangia mada kwenye kongamano hilo.
Mshiriki akichangia kongamano hilo.
Washiriki wakiwa kwenye kongamano hilo lililofanyika katika Msikiti Mkuu wa BAKWATA wilayani Misungwi.
Jumbe mbalimbali kuhusiana na kongamano hilo.

Friday, April 15, 2022

KCB BANK YAFUTURISHA MWANZA NA KUTOA MIKOPO BILA RIBA


WITO umetolewa kwa viongozi wa Mashirika, Taasisi na Idara zote zilizo na wafanyakazi walioajiriwa kutoa ruksa za ibada kwa wafanyakazi wao waliokwenye mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ili watumishi hao wazidi kuthamini ajira walizo nazo na kuzitumikia kwa ufanisi.

Hayo yamesemwa na Sheikh wa Mkoa wa Mwanza Hassan Kabeke mara baada ya kushiriki iftar iliyoandaliwa na Benki ya KBC Tawi la Mwanza na kuwafuturisha wateja wake wa Kanda ya Ziwa, huku benki hiyo ikitumia mwanya huo kutambulisha huduma yake ya mikopo isiyo na riba yaani SAHL BANK. "Unaonaje wewe bosi, wewe kiongozi kwenye taasisi au shirika flani ukawa na mfanyakazi mwenye kumweshimu na kumwogopa Mungu?, Bila shaka mfanyakazi huyo atakuwa msaada mkubwa kwako" amesema Sheikh Kabeke

MAJANGA MIKOPO YA ELIMU YA JUU.

 


Dosari katika mifumo ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) zimesababisha baadhi ya wanufaika kuzidishiwa, wengine kupunjwa huku watoto kutoka kaya maskini pamoja na mayatima wakinyimwa kabisa.


Dosari hizo zinaanzia kwenye utambuzi wa wanufaika, upangaji wa viwango vinavyotakiwa kutolewa mpaka kwenye ugawaji wa fedha zinazotakiwa kutolewa kwa wanafunzi wanaostahili.


Kwenye ukaguzi wa ufanisi alioufanya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere kwa HESLB, amebaini dosari tatu kwenye utoaji wa mikopo hiyo. Makosa hayo ya kimfumo yamesababisha baadhi ya wanafunzi kuzidishiwa fedha kuliko wanavyostahili huku wengine wakipewa kiasi kidogo kisichotosheleza mahitaji na wengine wakikosa kabisa, licha ya kukidhi vigezo vilivyopo.


Waliostahili wakakosa mkopo

Kwa miaka mitano mfululizo, ukaguzi huo umebaini bodi ilitoa mikopo kwa wastani wa asilimia 72, ikimaanisha asilimia 28 ya wanafunzi waliostahili kila mwaka, walikosa mkopo hivyo kuhatarisha uhakika wao wa kuipata elimu ya juu.


“Timu ya ukaguzi ilibaini mwaka 2020/21 wanafunzi 43,053 waliokidhi vigezo walikosa mkopo. Wanafunzi hao waliihitaji Sh124.92 bilioni na katika kipindi cha miaka mitano, wanafunzi 192,039 waliotakiwa kupata Sh569.5 bilioni walikosa mkopo japokuwa walikidhi vigezo,” amesema Kichere.


Miongoni mwa maofisa wa bodi waliozungumza na CAG walisema ugawaji wa mikopo hutegemea upatikanaji wa fedha kutoka serikalini, wakimaanisha kuna wakati hutolewa kidogo ikilinganishwa na wanafunzi wanaostahili.


Aliyewahi kuwa Kiongozi wa Mtandao wa Wanafunzi wa Vyuo Vikuu Tanzania (TSNP), Abdul Nondo alisema ufinyu wa bajeti ni tatizo la siku nyingi ambalo wanafunzi hulipigia kelele.


“Bajeti inatakiwa kuongezwa na Serikali iwe na mfumo mzuri wa kuwatambua wahitaji wanaostahili,” alisema Nondo.


Yatima, Tasaf nao wachinjwa

Kati ya kundi linalopewa kipaumbele ukiacha wale wanaosoma masomo ya sayansi, ni wanafunzi wanaotoka kaya masikini au waliofiwa na wazazi wao kwani wengi hukosa msaada wa fedha kuwawezesha kulipia shahada zao.


Tofauti na ukweli huo, CAG anasema jumla ya wanafunzi 95 walioomba mkopo kati ya mwaka 2017/18 na 2020/21 ambao ni yatima waliowapoteza wazazi wa wote wawili, hawakupewa fedha walizozihitaji.


“Mwaka 2020/21 wanafunzi mayatima 12 waliohitaji Sh50.23 milioni hawakupewa fedha walizoomba kutokana na dosari ya mfumo na ugawaji wa mikopo,” amesema CAG.


Ukiacha mayatima hao, ukaguzi wa Kichere na wenzake uligundua wanafunzi 22 ambao familia zao zinanufaika na ruzuku inayotolewa na Serikali kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini Tanzania (Tasaf), licha ya kuwekwa kwenye kundi la wenye uhitaji wa hali ya juu lakini walikosa.


“Wanafunzi hao walihitaji Sh84.48 milioni kati ya mwaka 2019/20 na mwaka 2020/21,” amesema CAG.


Akizungumza na Mwananchi, yatima mmoja mhitimu wa chuo kikuu mwaka 2016 ambaye hakutaka kutajwa jina, alisema alikosa mkopo kwa miaka yote mitatu licha ya kukata rufaa kila mwaka.


“Nilihangaika sana wakati naanza mwaka wa kwanza lakini nilikosa mkopo, nilijaza upya mwaka huo ila nilikosa pia. Nilirudia tena nikiwa mwaka wa pili nikakosa, nilisoma kwa shida sana,” alisema mwanafunzi huyo liyejiunga chuo kikuu akiwa na diploma.


Kuhusu wanafunzi waliohitimu diploma kabla ya kwenda chuo kikuu, Nondo alisema ni kikwazo kwao. “Unakuta mwanafunzi amesoma diploma au QT (mfumo unaotumiwa na walioikosa elimu ya sekondari) anakosa mkopo kwa kigezo cha kwamba alikuwa katika mfumo binafsi hata kama ni mtoto wa maskini,” alisema Nondo.


Wazidishiwa, wapunjwa ada

Chuo kikuu, kila kozi ina gharama zake na mwanafunzi hupewa mkopo kwa kuzingatia shahada anayosoma. Kwenye ukaguzi wake, CAG alibaini mwenendo tofauti, kwani baadhi ya wanafunzi walipewa fedha nyingi za ada kuliko kiwango kilichopangwa na chuo husika, huku wengine wakiambulia kiasi kidogo kisichotosha ada wanayotakiwa kuilipa.


Idadi ya wanafunzi walioongezewa, ripoti inaonyesha walikuwa zaidi ya mara mbili mwaka 2020/21 wakilinganishwa na wa mwaka wa nyuma 2019/20.


Mwaka 2020/21, Kichere amesema jumla ya wanafunzi 4,839 walipokea kiasi kikubwa zaidi ya walichostahili. Idadi hiyo iliongezeka kutoka 2,097 waliokuwapo mwaka 2019/20.


Licha ya mwenendo huo, thamani ya mikopo iliyotolewa ilipungua kwa asilimia 30 katika kipindi hicho kutoka Sh4.71 bilioni mpaka Sh3.32 bilioni katika kipindi hicho.


Kwa miaka mitano iliyopita, Kichere amesema jumla ya Sh13.7 bilioni zilizidishwa kwa baadhi ya wanafunzi waliopokea mkopo wa HESLB.


“Upangaji mikopo zaidi ya kiwango stahiki au chini ya kiwango ulitokana na dosari za mifumo ya upangaji na ugawaji wa mikopo wakati wa zoezi la upangaji na ugawaji wa mikopo kwa wanafunzi,” inasomeka sehemu ya maoni ya CAG.


Mkakati wa kupunguza tatizo

Akizungumzia dosari zilizoainishwa na CAG kwenye ripoti ya mwaka 2020/21, Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru alisema wanaboresha mifumo yao ili kila mwanafunzi apate kadri anavyostahili.


“Wakati mwingine national database zinakuwa hazijaunganika vizuri kupitia mfumo wa Gasi. Kuna wanafunzi wanastahili lakini wanakosea kujaza taarifa zao hivyo mfumo unamkataa,” alisema Badru.


Ofisa Mawasiliano wa HESLB, Veneranda Malima alisema viwango vinavyotolewa ni kulingana na utafiti walioufanya katika mwaka husika wa masomo kwa kushirikiana na vyuo vikuu vinavyopokea wanafunzi.


“Tunaangalia hali ya maisha kwa kipindi husika ndio maana huwa tunabadilisha kila baada ya muda fulani. Viwango vya ada tunafuata vinavyotumika kwenye vyuo vya umma na hata inapotokea vyuo vinaongeza gharama ya programu fulani wanatushirikisha,” alisema Veneranda.


Kwa kutambua uwepo wa wanafunzi wengi wanaokosa mikopo kwa sababu mbalimbali, hasa kukosea kujaza fomu, Veneranda alisema bodi inaendelea kutoa elimu kwa wahusika kwa kuwafuata shuleni, wanapukuwa kwenye kambi za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kwa mafunzo ya kijeshi hata kupitia vyombo vya habari.


“Tumepunguza mifumo na hatua za kujaza fomu za mikopo, ikiwamo kuondoa baadhi ya nyaraka zilizotakiwa kuambatanishwa ili kupunguza idadi ya wanaokosea kwa sababu hizo,” alisema.


Bajeti ya mkopo

Kasoro zinazowanyima haki baadhi ya wanafunzi wanaostahili zinatokea, licha ya Serikali kuongeza bajeti kwa ajili ya mikopo hiyo kila inapobidi.


Katika mwaka wa fedha 2020/21 kwa mfano, Serikali ilitenga Sh464 bilioni kwa ajili ya wanafunzi 145,000 ambazo ni sawa na ongezeko la Sh14 bilioni ikilinganishwa na Sh450 bilioni zilizotengwa mwaka 2019/20 kuwanufaisha wanafunzi 128,285.


Serikali pia iliongeza fedha hizo kwa asilimia 23 mwaka huu wa fedha na kufika Sh570 bilioni.


Waziri wa mikopo wa serikali ya wanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Daruso), Miseyeki Kijana alisema wanazo njia mbili za kuwaunganisha upya wanafunzi waliokosa mkopo wa bodi na inapobidi hufanya fundraising (uchangishaji wa hiari) kwa wadau, ndani na nje ya chuo.


“Mwaka huu 2021/22 kwa mfano, karibia asilimia 90 ya wanafunzi wa chuo hiki hawakupata mkopo kwa asilimia zote, lakini tuliwaunganisha kufanya maombi upya kwa HESLB na tumepata majibu. Kesho (leo) wanafunzi 300 wameongezewa viwango walivyotakiwa kupata,” alisema Kijana.


Waziri huyo alifafanua kwamba wanaokosa kabisa mkopo wa HESLB, huchangishiwa. “Utaratibu huu umewanufaisha zaidi ya wanafunzi 100 waliolipiwa ada mwaka huu,” alisema Kijana.


Naibu waziri wa mikopo na fedha wa serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Tuamaini (Tudarco), Isaack Msenya alisema wanafunzi wanaokosa mkopo licha ya kuwa na vigezo, huwasiliana na bodi.


“Tunachokifanya tunapopokea malalamiko tunawaunganisha na bodi japo hiyo haitoi guarantee (uhakika) wa kupata ingawa wapo wanaofanikiwa,” alisema Msenya.

KAULI YA HAJI MANARA BAADA YA KUONGEZA MKE WA PILI.

 


Msemaji wa Klabu ya Yanga Haji Manara ameweka wazi kwamba haikuwa kazi rahisi kuoa tena mke wa pili lakini anamshukuru Mungu kwa kufanikisha jambo hilo.


"Haikuwa Rahisi lakini kila jambo lina utaratibu wake vile Muumba wetu alivyolijaalia. Thanks Baba na Mama yangu kwa baraka zenu kwetu, karibu Mke wangu Rubynah Binti Salum kwenye familia yetu". ameandika Haji Manara


Taarifa za Manara kuoa mke wa pili zimetoka jana usiku baada ya kushea picha kwenye page yake ya Instagram huku baadhi ya mastaa wa kike kama Hamisa Mobetto, Zamaradi Mketema, Batuli Actress na Esha Buheti wakihudhuria harusi hiyo.

WAZIRI NDAKI AVUNJA UKIMYA KUHUSU ENEO LA CHIBE

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (kushoto) akiwaeleza wawakilishi wa wananchi wa vijiji vinavyozunguka lililokuwa eneo la kupumzishia mifugo la Chibe lililopo mkoani Shinyanga sababu za kuwaondoa kwenye eneo hilo muda mfupi baada ya kuwasili hapo leo (14.04.2022).
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Sophia Mjema (kulia) akiteta jambo na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki muda mfupi kabla ya Mhe. Ndaki kuanza ziara ya ukaguzi wa shughuli mbalimbali zinazohusu  sekta ya Mifugo mkoani humo leo (14.04.2022).
Mkaguzi Mkuu wa Nyama kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga Bw. Ernest Nigo (wa pili kutoka kushoto) akimuonesha Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) namna moja ya mitambo ya kusindika nyama iliyopo kwenye Machinjio ya Manispaa hiyo inavyofanya kazi  muda mfupi baada ya Mhe. Ndaki kufika Machinjioni hapo leo (14.04.2022). Kushoto ni Meneja wa Shamba la Mifugo la Mabuki lililopo mkoani Mwanza, Bi. Lynn Andey.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki (kushoto) akitoa maelekezo ya namna ya kutumia lililokuwa eneo la kupumzishia Mifugo la Chibe lililopo Mkoani Shinyanga  kwa msimamizi wa eneo hilo ambaye pia ni Meneja wa Shamba la Mifugo la Mabuki lililopo Mwanza Bi. Lynn Andey (kulia)  leo (14.04.2022).

 
Sasa kutumika kuzalishia na kunenepeshea mifugo

Baada ya sintofahamu ya muda mrefu  kuhusu hatma ya matumizi ya zaidi ya ekari 5000 za eneo  lililokuwa likitumika kupumzishia mifugo “holding ground”  la Chibe lililopo mkoani Shinyanga  , Hatimaye Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ameamuru wananchi  wote wanaofanya shughuli mbalimbali za kibinadamu kwenye eneo  hilo kuondoka ifikapo Agosti 30  mwaka huu.

Mhe. Ndaki ameyasema hayo leo (14.04.2022) mara baada ya kufika na kukagua eneo hilo ambapo amewataka wananchi wanaolitumia  kwa shughuli za kilimo kuhakikisha wameondoka mara baada ya mavuno ya mazao yao ambayo kwa wakazi wa mkoa wa Shinyanga huwa ni  kati ya mwezi Aprili hadi Agosti.

“Kwanza ni lazima mfahamu kuwa hili ni eneo la Serikali na mnaishi humo kimakosa na naona tayari mmelima aina mbalimbali za mazao tena bora mngeishia kulima tu, mmeamua kujenga na makazi kabisa, sasa serikali tunataka kulitumia na kwa kuwa hatutaki muone kama mmenyang’anywa mazao yenu ninawapa mpaka mwezi wa 8 muwe mmeshavuna na kuondoa mazao yenu” Amesema Mhe. Ndaki.

Aidha Mhe. Ndaki amemuelekeza Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga kufanya operesheni ya kuwaondoa  watu wote ambao watakuwa hawajaondoka kwenye eneo hilo baada ya muda uliowekwa ili Serikali kupitia Wizara yake iweze kuanza kulitumia  kwa ajili ya kuzalisha na kunenepeshea ng’ombe na mbuzi wa nyama watakaouzwa kwenye viwanda  vilivyopo hapa nchini.

“Tunataka kuendelea kuongeza mauzo yetu nje ya nchi hivyo mbali na Serikali kulitumia eneo hili kwa ajili ya kuongeza tija kwenye mifugo yetu hivyo tutawakaribisha pia wafanyabiashara binafsi na vikundi vya ushirika kuleta mifugo yao hapa kwa ajili ya kuiongezea thamani na kuiuza kwenye viwanda vyetu ambavyo vipo kama vitano hivi lakini vyote vinafanya kazi chini ya uwezo wake kwa kukosa malighafi” Ameongeza Ndaki.

Akizungumza kwa niaba ya viongozi na  wananchi wa vijiji vinavyozunguka  eneo hilo,Mwenyekiti wa Kijiji cha Chibe ambacho ni moja ya vijiji vinavyotumia shamba hilo Bw.  Masalu Malale amekiri wao kuvamia  eneo hilo ambapo alibainisha kuwa yeye na wananchi wake wataondoka kwa hiyari ndani ya muda waliopewa kwa sababu uwepo wao hapo ulitokana na eneo hilo kutotumiwa na Serikali  kwa shughuli yoyote ya kiuchumi.

“Kwenye kijiji changu kuna kaya kama 10 ndani eneo hili na baada ya kutambua kuwa tupo kwenye eneo la Serikali tulikubaliana kuwa pindi ikitaka kutumia eneo hili tutaondoka bila tatizo lolote” Alisema Masalu.

Mbali na  kufika kwenye eneo hilo, Mhe. Ndaki alipata fursa ya kutembelea machinjio ya Manispaa ya Shinyanga ambapo baada ya kukagua namna shughuli zinavyofanyika kwenye machinjio hiyo aliuagiza uongozi wa Manispaa hiyo kuwahamasisha wafugaji waliopo Mkoani Shinyanga kwenda kuchinja mifugo yao kwenye machinjio hiyo ili kuiongezea uwezo wake wa kufanya kazi badala ya hivi sasa ambapo  jumla ya mifugo 36 pekee inachinjwa kwa siku badala ya mifugo 500 ambayo ingekidhi uwezo uliosimikwa wa machinjio hiyo.

“Tutashirikiana kutafuta wawekezaji watakaokuwa na uhakika wa kupata ng’ombe na mbuzi wa kutosha na masoko ya mifugo hiyo japo mmeniambia mmeshaanza mazungumzo na mtu mwenye nia ya kuwekeza hapa ila naomba muwe makini sana kwa sababu pale Machinjio ya Dodoma tulipata mwekezaji ambaye ametuletea ugomvi mkubwa sana kiasi cha kuifanya machinjio yetu kutofanya kazi yake kwa ufanisi” Amesema Ndaki.

Mapema kabla ya kuanza ziara yake Mhe. Ndaki alifika kumsalimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Sophia Mjema ambapo alipokea taarifa ya mkoa huo inayohusu  utekelezaji wa shughuli mbalimbali za sekta za Mifugo na Uvuvi.

Thursday, April 14, 2022

MAHAKAMA YAZUIA MALI ZA ROMAN ABRAMOVICH ZENYETHAMANI YA DOLA BILIONI 7

 


Roman Abramovich amelazimishwa kuuza klabu ya Chelsea FC na kuihahamisha mashua yake ya kifahari nje ya maji ya nchi za Muungano wa ulaya.


Mali za birionea wa Mrusi Roman Abramovich zenyethamani ya dola bilioni 7 (£5.4bn) zinazohusiana naye zimefujwa na mahakama yaJersey.


Jumanne, polisi ya Jersey ilisaka eneo linaloshukiwa kuwa na shuguli za kibiashara zenye uhusiano na Bw Abramovich katika kisiwa hicho, Maafisa wa idara ya sheria ya walisema.


Bilionea Abramovich yuko katika orodha ya vikwazo vya Uingereza vinavyohusiana na vita vya Urusi katika Ukraine.


Kisiwa cha Channel Island Jersey kinafuata sera ya Uingereza na kuwawekea vikwazo watu walioko kwenye orodha hiyo ya Uingereza.


"Mahakama hiyo pia iliweka amri rasmi tarehe 12 Aprili, inayofahamika kamasaisie judiciaire, juu ya mali zinazofahamika kuwa na thamani ya zaidi ya dola bilioni 7 za Kimarekani ambazo zinashukiwa kuwa na uhusiano na Bw Abramovich na ambazo zinapatikana Jersey au zimeingizwa katika taasisi zaJersey," Maafisa idara ya sheria wa Jersey walisema.


Bw Abramovich alikuwa ni miongoni mwa matajiri Warusi walioongezwa mwezi uliopita kwenye orodha ya uingereza na muungano wa Ulaya ya vikwazo , ambao tayari wamekwishachukuliwa hatua ya kuchukuliwa kwa mashua zao za kifahari na mali zao nyingine za kifahari.


Bilionea huyo alijaribu kuuza klabu ya soka ya Chelsea katika mwezi March, lakini mchakato huo uliondolewa mikononi mwake na serikali baada ya kuwekewa vikwazo.


Mapema mwezi huu, taifa la Caribbean la Antigua and Barbudalilisema liko tayari kuisaidia Uingereza kushikilia mashua zinazomilikiwa na Abramovich.


Boti hizo za kifahari zilizohusishwa na mfanyabiashara Abramovich, kwa pamoja zina thamani inayokadiriwa kuwa ya dola bilioni 1.2 na kwa sasa zimetia nanga kusini mwa Uturuki, nje ya eneo la Muungano wa Ulaya na uingereza.

TAARIFA YA ULIPO MSIBA WA MAUNDA ZORRO.

 


Msanii Banana Zorro ametoa taarifa ya kinachondelea kwenye msiba wa dada yake Maunda Zorro kwa kueleza kwamba kwa sasa msiba upo Maweni Kigamboni kwa Mzee Zorro na taarifa zaidi kuhusu msiba huo zitatolewa baadaye.


Taarifa ya Maunda Zorro kufariki dunia zimetoka usiku wa kuamkia leo huku chanzo cha kifo chake ni ajali ya gari iliyotokea Kigamboni Dar es Salaam.

Wednesday, April 13, 2022

'MWANZA YENYE MAJI YA KUTOSHA IPO NJIANI' - RC MWANZA

 

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel (wa pili kushoto) akiwasili kwenye eneo la ujenzi wa chanzo kipya cha maji cha Butimba. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi MWAUWASA, Mhandisi Leonard Msenyele

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel akielekeza jambo wakati wa ziara yake kwenye ujenzi wa mradi wa chanzo kipya cha maji cha Butimba, Mkoani Mwanza.

Hatua mbalimbali za ujenzi wa chanzo kipya cha maji zikiendelea

Ujenzi wa Machujio ya Maji katika Mradi wa Maji Butimba

Eneo la mradi wa chanzo kipya cha maji na Tiba ya maji Butimba, Mkoani Mwanza

………………………………………….

Na Mohamed Saif

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel ameridhishwa na hatua za ujenzi wa mradi wa chanzo kipya cha maji katika eneo la Butimba wenye thamani ya shilingi bilioni 69 na utakaonufaisha zaidi ya wakazi 400,000.

Mhandisi Gabriel ameeleza hayo Aprili 12, 2022 wakati wa ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miradi inayotekelezwa kwa fedha za Serikali Kuu ikiwemo mradi huo wa chanzo hicho kipya cha majisafi cha Butimba.

“Nimeridhishwa na shughuli inayoendelea hapa; ikumbukwe kwamba huu ni mradi wa kimkakati ambao Serikali imewekeza fedha nyingi ili kutatua adha ya upungufu wa upatikanaji wa huduma ya majisafi kwa wakazi wa Jiji la Mwanza,” alisema Mhandisi Gabriel.

Alisema anatambua uwepo wa mgawo wa huduma ya maji kutokana na hali halisi ya mahitaji ambayo ni makubwa kuliko uzalishaji wa maji wa sasa wa MWAUWASA; hata hivyo alibainisha jitihada mbalimbali za Serikali ya awamu ya sita inayooongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha huduma ya majisafi inaimarika zaidi.

“Tunamshukuru sana Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa dhamira yake ya dhati ya kumtua mwanamke ndoo ya maji kichwani, fedha za miradi zipo na zinafika kwa wakati na miradi inaendelezwa kwa kasi,” alisema Mhandisi Gabriel.

Mhandisi Gabriel alisema wananchi wamekuwa na hofu ya muendelezo wa ujenzi wa miradi na hivyo kupitia ziara yake hiyo kwenye mradi wa chanzo kipya cha maji eneo la Butimba anawathibitishia hatua za kimapinduzi zinazochukuliwa na Serikali ya awamu ya sita.

“Niwasihi wananchi waendelee kuwa na subira kwa niliyoyashuhudia hapa ninasema yajayo yanafurahisha. Mkandarasi nimemkuta site, kazi zinaendelea na mradi ni mkubwa ninawapongeza sana Wizara ya Maji kupitia MWAUWASA; ninaiona Mwanza yenye majisafi ya kutosha ni suala la muda tu, kazi inaendelea,” alisema Mhandisi Gabriel.

Akizungumzia utekelezwaji wa mradi, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA), Mhandisi Leonard Msenyele alisema mradi unatekelezwa na Mkandarasi Kampuni ya SOGEA SATOM na VINCI GRAND PROJETS kutoka Ufaransa.

“Shughuli za usanifu na ujenzi zilianza rasmi Februari, 2021 na tunatarajia ifikapo Februari 2023 mradi utakuwa umekamilika,” alibainisha Mhandisi Msenyele.

Mhandisi Msenyele alisema mradi unahusisha ujenzi wa chanzo kipya na kituo cha tiba ya maji chenye uwezo wa kusafisha na kuzalisha majisafi kiasi cha lita milioni 48 kwa siku.

“Chanzo hiki kitakapokamilika kitaboresha huduma ya upatikanaji wa majisafi kwa wakazi zaidi 400,000 katika jiji la Mwanza na maeneo ya pembezoni kama vile Usagara, Kisesa, Buhongwa Mashariki, Lwanhima, Sahwa, Fumagila, Kishiri, Igoma na Buswelu,” alisema Mhandisi Msenyele.

Mhandisi Msenyele alisema mradi unatekelezwa kwa mfumo wa kusanifu na kujenga na kwamba hadi kufikia Machi 2022, utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 90 kwa kazi ya usanifu na asilimia 12 kwa shughuli ya ujenzi.

ZAIDI YA WANAJESHI 1,000 WA UKRANE WAJISALIMISHA HUKO MARIUPOL - URUSI

 

Urusi inadai wanajeshi 1,026 wa Ukraine wameweka silaha chini katika mji unaozingirwa wa Mariupol.


Bandari ya kusini imekuwa ikishambuliwa kwa wiki kadhaa na inaaminika kuwa inaelekea kuanguka mikononi mwa Urusi.


Kikosi hicho, cha 36 cha Marine Brigade, lilisemekana kujisalimisha karibu na kiwanda cha kutengeneza mabati na vyuma cha Ilyich Iron and Steel.


Msemaji wa wizara ya ulinzi ya Ukraine Oleksandr Motuzyanyk amesema kwamba hajapokea taarifa kuhusu ripoti hizo.


Mapema wiki hii, naibu meya wa Mariupol alitaja kuwa "feki"chapisho la Facebook lililodai kuwa wanajeshi wa kikosi hicho walikuwa wameishiwa na risasi na kwamba wamekosa uungwaji mkono.


Huku hayo yakijiri familia ya Muingereza anayepigana nchini Ukraine imesema amewaambia kwamba atalazimika kujisalimisha kwa vikosi vya Urusi.

AVUNJWA MIGUU NA MIKONO BAADA YA KUFUMANIWA

 


Na Amiri Kilagalila, Njombe

Kijana anayefahamika kwa jina Benard Mkolwe mkazi wa kata ya Madilu,wilaya ya Ludewa mkoani Njombe,amepigwa na kuvunjwa mikono na miguu baada ya kukutwa na msichana Sara Mgohole anayedaiwa kukutana naye nyumbani kwao kwa lengo la tendo la ndoa ikiwa ni siku ya kwanza tangu waanze mahusiano wiki mbili zilizopita.


Kijana huyo amekili kuwa na mahusiano na msichana huyo na kudai kuwa mahusiano yao yalikuwa yakuwasiliana kwa simu pekee na yana muda wa wiki mbili toka wayaanzishe hivyo siku ya tukio hilo ilikuwa ni siku yao ya kwanza kukutana kwa lengo la kufanya tendo la ndoa.


“Wakati wananipiga wakaniambia kwanini unatembea na binti yetu nikawaomba samahani nimekosa lakini hawakutaka kunielewa”alisema Benard Mkolwe


“Waliofanya tukio ni baba zake wadogo wa yule binti yule binti ni kama wiki mbili tuko kwenye mahusiano lakini sijawahi kufanya kitu chochote kile tulikuwa ni marafiki wa kuchati na ile siku alivoniita nahisi ndio ilikuwa siku ya kuelekea kwenye tendo lakini sikufanya kitu chochote”aliongeza Mkolwe


Kijana huyo anafanyiwa matibabu katika hospitali ya St. Jon's huku Daktari wa zamu wa hospitali hiyo Zainabu Said akieleza kuwa kijana huyo ameumizwa na sasa anaendelea na matibabu katika hospitali hiyo.


Mkuu wa wilaya ya Ludewa Andrea Tsere ambae pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo amethibitisha kutokea kwa tukio hilo sambamba na kupinga vikali vitendo vya wananchi kujichulia sheria mkononi.


“Labda kuna visa vya awali,huu ni ukatili wa kijinsia unaotokana na binti kusuka mpango kumuonea huyu kijana,yeye amekubali kuchati halafu wanakuja kumpiga na kama alikuwa hana uhitaji wa kukutana na huyu kijana angemkatalia toka mwanzo”alisema Tsere