ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, March 28, 2024

MADUDU RIPOTI YA CAG, "NCHI TUNAIUA SISI WENYEWE"


Rais Samia Suluhu Hassan amewataka watendaji wa Serikali, kusimamia vema rasilimali za nchi kwa kutumia mifumo na kuweka nidhamu, akisema kinyume na kufanya hivyo ni sawa na kuiua nchi yetu wenyewe.


Mkuu huyo wa nchi ameeleza hayo wakati akifafanua kuhusu uzembe wa upitishaji wa baadhi ya mikataba inayoigharimu Serikali kwa kuweka ama kuruhusu vifungu vya kisheria visivyostahili kuwepo.

Kauli yake hiyo inatokana na kile kilichobainishwa kwenye ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2021/22 na taarifa ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwa, Serikali inadaiwa tozo na riba ya zaidi ya Sh418 bilioni kutokana na ucheleweshaji wa malipo au mikataba.


Katika hotuba yake aliyotoa Ikulu ya jijini Dar es Salaam jana, baada ya kupokea ripoti hiyo ya CAG na ile ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Rais Samia alisema kuna mambo ya hovyo yanafanyika.

Alisema kumekuwa na upitishwaji mikataba mibovu inayoigharimu nchi, sambamba na kucheleweshwa kwa malipo kunakozalisha riba kubwa kwa Serikali.

Huku akionekana kukerwa na kuwakaripia watendaji wazembe, alieleza pamoja na kufahamika kila mkataba unavyopaswa kuwa, baadhi ya watendaji wanapitisha ambayo ina vifungu visivyostahili.

“Dhambi ni sisi wenyewe. Tunaua nchi yetu sisi wenyewe. Unaruhusu vifungu vya ajabu vinaingia kwenye mitakaba isiyopaswa, kwa hiyo huko kwenye mikataba angalieni vizuri.

“Mikataba hii ina aina zake, unajua kabisa mkataba wa aina hii hauwezi kuwa na vifungu hivi, lakini unakuta kuna kifungu cha ajabu ajabu kipo ndani ya mkataba,” alieleza Rais akionyesha kukasirika na kuongeza: “Kinachoshangaza ni njia ulizopita mkataba huo na ukafanyiwa kazi bila hata vifungu hivyo kuonekana.


“Umepita njia zote na mkataba ukaenda ukafanya kazi na sasa waliofanya kazi wanadai ni kimkataba, sasa unawapa watu wengine hebu someni huu mkataba wanakwambia mama hivi vifungu havikupaswa kuwepo ndani ya mkataba, unawauliza ilikuwaje vikaingia, wanaangaliana machoni,” alisema.


Ucheleweshwaji malipo

Kuhusu ucheleweshwaji wa malipo kwa makandarasi, Rais Samia alisema unafanywa na baadhi ya watendaji kwa makusudi kwa kuwa kuna wanachokipata kupitia tozo na riba hizo.

“Kuna malipo ya riba Sh418 bilioni, bilioni hizi tungezipeleka kwenye umeme, tungepeleka kwa watu wangapi, watu wapo tu hawana uzalendo.

“Hawajali, wanatengeneza riba wanalipa wapate na cha kwao, kikupeleke wapi, utazikwa nacho?” alihoji Rais kwa hisia.

Kwa mujibu wa CAG Charles Kichere, riba hiyo ya Sh418.77 bilioni ilitokana na kucheleweshwa kwa mikataba katika taasisi mbalimbali ikiwemo Serikali Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa (Tamisemi) na mashirika ya umma.

“Ucheleweshaji huo umetokana na mchakato wa malipo kuchukua muda mrefu bila kuzingatia matakwa ya kimkataba,” alisema Dk Kichere.


Upigaji mikopo ya halmashauri

Wakati wabunge na madiwani wakiibana Serikali na watendaji kuhakikisha wananchi wananufaika na mikopo hiyo ya asilimia 10 inayotokana na mapato ghafi ya halmashauri, CAG amebaini kuwepo kwa urejeshaji duni wa mikopo hiyo. Kwa mujibu wa ripoti ya CAG kiasi cha Sh88 bilioni zilizokopeshwa kwa makundi ya wanawake, vijana na walemavu, hazijarejeshwa. Kutokana na hilo, Rais Samia alisema sababu kubwa ya kushindwa kukusanywa kwa mikopo hiyo ni namna ya ukopeshaji.


Alieleza mikopo hiyo imegeuka kuwa mfuko wa siasa kwa madiwani na hata zinapokopeshwa, wananchi huamini wamepewa na madiwani wao, hivyo hawaoni haja ya kurejesha ili wengine wanufaike.

“Huku nako kunataka marekebisho makubwa, mbinu hii tunayoichukua kupitia halmashauri haitafanya kazi siku zote, tutatoa fedha na haitarudi,” alisema.

Alitaka mfumo wa kibenki uingizwe kuratibu mikopo hiyo, akisema kila halmashauri ikusanye fedha na kupeleka kwenye benki itakayokubalika na wakopaji waende huko.

“Vijana, wanawake, wenye ulemavu watakopa benki na kule utake usitake utalipa, tukifanya hivi wanaochukua watalipa na tutaondoa ile tabia ya madiwani kufanya wanavyotaka.

“Fedha yote hii iliyotoka Sh88 bilioni kama ni vituo vya afya vingapi? Imekwenda imepotea, sadaka madiwani wametoa kwa wapiga kura wao, hii fedha kwenye bajeti ya mwakani iundiwe mfumo mpya,” alisema.

Mfumo huo alioshauri kuanza kutumika mwaka wa fedha ujao 2023/24, ndio unaotumika kwa Zanzibar, ambapo Serikali iliingia makubaliano na taasisi za fedha kukopesha wajasiriamali kwa masharti nafuu lengo likiwa ni kuwa na mfumo mzuri wa ufuatiliaji.


Kasoro utekelezaji wa miradi

Licha ya uwepo wa wasimamizi wa miradi katika kila wizara, alisema bado kumekuwepo na kasoro kwenye utekelezaji wa miradi.

Alisema kwenye miradi mikubwa bado kuna matatizo na wasimamizi wanapaswa kuonea uchungu fedha ya Serikali.

“Kama upotevu huu ni faida kwa wanaosimamia basi imetosha, mmeshachukua ngapi, kwa hiyo tumechelewa kwenye kuchukua hatua, wakichukuliwa hatua wataacha,” alisema. 


 Alitolea mfano kwenye ununuzi wa vishikwambi akisema kuna ziada ya Sh10 bilioni fedha ambayo imepotea bila tija.

Rais Samia alisema katika ununuzi wa vishikwambi 300,000 uliofanywa kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, ambapo Machi 2022 ilipewa jukumu hilo kwa ajili ya Sensa ya Watu na Makazi na ilianzisha mchakato wa zabuni.

Alisema zabuni hiyo iligawanywa katika sehemu sita kila moja ikiwa na vishikwambi 50,000 wizara ilisaini mikataba na wazabuni watatu wa kuleta vishikwambi 300,000 vyenye thamani ya Sh123.7 bilioni.

Katika mchakato huo, alisema wajumbe wa bodi walipendekeza wazabuni wanne kati ya 14 wawili kati yao walishinda zabuni, ilhali si kazi ya bodi ya zabuni kupendekeza wazabuni.

Pia, alisema bodi ya zabuni ilibadilisha vigezo vya ubora bila kuwasiliana na idara tumizi na kuondoa vifaa vya kutunzia umeme, wazabuni walipewa siku mbili tu kujibu nyaraka za zabuni badala ya 14 zinazotakiwa huku 10 kati ya 14 wakijibu kwa wakati.“Idara tumizi haikuhusika katika kamati ya wajumbe walioteuliwa kutathmini na waliteuliwa bila mapendekezo ya idara ya ununuzi ambayo ni kinyume cha sheria,” alisema.

“Haya yapo mengi mawaziri tusaidiane huko, wasiwadanganye, tunaomba tufanyie kazi na ili tuendelee kuna kazi ya kufanya inahitajika,” alisema.


Kwenye miradi ya maji nako balaa

Awali, akizungumza kuhusu hilo, CAG Kichere alisema katika ukaguzi wake, alibaini upungufu katika utekelezaji wa mradi wa uboreshaji na usambazaji wa maji wa Sami-Mwanga wenye thamani ya Sh263.67 bilioni.

 Katika mradi huo unaotekelezwa na Wizara ya Maji kwa ufadhili wa Serikali ya Tanzania na Shirika la Maendeleo, alisema ulianza kutekelezwa Desemba 17, 2014 na ulitarajiwa kukamilika Machi 4, 2021 lakini hadi sasa mradi haujakamilika.

Alisema kulikuwa na makandarasi wawili wanaotekeleza mikataba mitatu ya mradi huo yote ilisitishwa Desemba 2020 na miwili ilisitishwa baada ya Wizara ya Maji kujiridhisha kwamba, mkandarasi alighushi dhamana ya benki ya malipo ya awali na dhamana ya fedha za zuio alizowasilisha wizarani.

“Mkataba mmoja ulisitishwa kwa kuwa mkandarasi hakuhuisha dhamana ya utekelezaji wa mradi, baada ya kuisha muda wake na baada ya kukumbushwa mara kadhaa bila mafanikio,” alisema.

Baadaye, alisema Wizara ya Maji iliingia mikataba miwili yenye thamani ya Dola milioni 13.95 za Marekani na Dola milioni 3.61 za Marekani, kwa ajili ya kumalizia kazi ya kusambaza mabomba na kumalizia kazi ya kujenga matenki mtawalia.

Alisema kabla mkandarasi mpya hajaanza kazi, Wizara ya Maji ilifanya mabadiliko kwenye mkataba wa kujenga matenki na kuongeza gharama za mkataba kutoka Dola milioni 3.61 za Marekani na kuwa Dola milioni 5.9 za Marekani sawa na ongezeko la Dola milioni 2.3 za Marekani sawa na asilimia 61.


Tanapa na fedha za Uviko-19

Rais Samia alitaka kujenga utaratibu wa kuunda bodi zenye sifa ya kufanyakazi kwenye maeneo kama Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa).

“Huku nako kukatizamwe vizuri, lakini Tanapa hawa wamepata fedha za Uviko-19 nendeni mkazitazame zimefanya nini,” alisema.

Ili kufanya rasilimali za nchi zitumike inavyopaswa, alisema kuna haja kufanyia kazi hasa kwa kutumia mifumo na kuweka nidhamu.

“Tukilegalega kwenye nidhamu na hatusimamii nidhamu kwa sababu sisi wenyewe ni wanufaika, tusingenufaika tungesimama, lakini kwa sababu tunanufaika hatusimamii.

“Niwaombe sana nchi hii kama tutasimamia rasilimali zetu, huko mbele tutapunguza shughuli za mikopo, tutakopa kama kuna umuhimu, tutakopa kwenye miradi mikubwa ya ndani, lakini mambo mengi tutaweza kufanya wenyewe,” alisema.


Mifumo TRA, TPA kutosomana

Katika ripoti ya Takukuru iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Kamishna Salum Hamduni alisema kutosomana kwa mifumo ya Mamlaka ya Bandari (TPA) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ni moja ya viashiria vya rushwa.

Kutokana na hilo, Rais Samia alisema tatizo la mifumo katika bandari limekuwepo kwa siku nyingi na alishaagiza lirekebishwe, lakini anashangazwa mpaka sasa bado halijafanyiwa kazi.

Alisema kutokana na hilo, ametoa ruhusa TPA kufanya kazi kwa kushirikiana na sekta binafsi ili kuongeza ufanisi wa huduma na ukusanyaji wa mapato huku akiamini jambo hilo linafanywa kwa makusudi.

Alisema hakuna sekta binafsi itakayoweka fedha yake ikaacha mifumo iendelee kubaki kama ilivyo, kwa vyovyote itaimarisha isomeke vema ili fedha zikusanywe.

“Na kuna reservation upande mwingine huko nao wana wasiwasi na hilo, tutakuja kulizungumza baadaye lakini kuna umuhimu kuimarisha bandari, mifumo, teknolojia,” alisema.

Alieleza bandari ni lango kubwa la uchumi lenye uwezo wa kuchangia hata nusu ya bajeti ya Serikali, lakini inashangaza pato lake haiinuki.

“Na watetezi mpo wengi tu, hapana sekta binafsi isiende mifumo sijui nini… mimi nasema sekta binafsi ikaribishwe twende tukaimarishe kwa masharti tutakayokubaliana kupitia Mwanasheria Mkuu atushauri bandari iimarishwe,” alisema.


Mapato halmashauri

Kuhusu fedha za halmashauri, Rais Samia alisema upotevu mkubwa husababishwa na mifumo akidokeza uwepo wa tabia ya baadhi ya watumishi kuondoka na mashine za ukusanyaji wanapotenguliwa.

“Huu mfumo ambao mtu anaweza kuondoka nao na ukawa haki yake hapana, hebu itazameni vizuri,” alisema na kuongeza: Tatizo lingine ni ulaji wa fedha mbichi katika halmashauri ambao alitaka ukomeshwe. Waziri (Angela Kairuki) tumezungumza hapa majuzi na ukaniambia unakwenda kufanya kitu, naomba tulifanye sasa ili kudhibiti ulaji wa pesa mbichi kwenye hizi halmashauri.

Walichosema wachambuzi

Mchambuzi wa siasa na uchumi, Gabriel Mwang’onda alisema Rais Samia yupo sahihi katika maeneo mengi aliyoyagusia katika hotuba yake. Hata hivyo, alisema tatizo sio mfumo pekee bali hata uendeshaji wa kawaida hasa wadau wa mashirika ya Serikali yanayotoa huduma kama TPA.

“Nakupa mfano mmoja unaweza kuleta mzigo wako ukamalizana na TPA na TRA, lakini jioni watu wa bandari wapo, huku wahusika wa taasisi kadhaa hawapo wameshafunga ofisi. Licha ya kuzungumzia mfumo lakini Rais Samia amependekeza pia ushirikishwaji wa sekta binafsi, hili jambo la msingi.

“Kitu kikiwa cha Serikali kinakwenda kiserikali, hakuna mtu anayejali, lakini kukiwa na sekta binafsi kunakuwa na uchungu katika utendaji kazi. Mapato ya TPA ni makubwa, sasa suala la mifumo likiangaliwa kwa upana litaleta tija,” alisema Mwang’onda.


Naye Mhadhiri Msaidizi wa Fedha, Uhasibu na Kodi wa Chuo cha Serikali za Mitaa, Dodoma, Charles Matekele alisema baadhi ya wataalamu hawajawajibika katika utekelezaji wa majukumu yao, ndio TRA wana mifumo mingi wanayoifanyia kazi, lakini wanaibadilisha mara kwa mara.

“Ni vema viongozi wa TRA na TPA kukaa chini na kuangalia maslahi ya Taifa, lakini ninaamini Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania na (TCRA), pamoja na Serikali mtandao wakikaa pamoja kazi zitakwenda vizuri.

“Kama unataka mafanikio hasa kwa bandari na TRA, lazima kutumia mifumo na ushirikiano wao na sekta binafsi katika mifumo utaleta ufanisi kwenye utekelezaji wa majukumu yao,” alisema Matekele.


CHANZO: MWANANCHI.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.