ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, November 22, 2019

SERIKALI YAMPA SIKU 14 MKANDARASI KUKAMILISHA MRADI WA MAJI MAGU

 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (kulia) akijadiliana jambo na Mbunge wa Jimbo la Magu, Boniventura Kiswaga wakari wa ziara ya kukaga ujenzi wa mradi wa maji wa Mji wa Magu.
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (kulia) akimsikiliza Msimamizi wa ujenzi wa mradi wa maji mji wa Magu, Mhandisi Wilbert Bujiku akielezea hatua zilizofikiwa za ujenzi wake.
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (katikati) akitoa maelekezo wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa ujenzi wa mradi wa maji Magu. Kushoto ni Mbunge wa Jimbo la Magu, Boniventura Kiswaga na kulia ni Msimamizi wa ujenzi wa mradi, Mhandisi Wilbert Bujiku.
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (kulia) akitoa maelekezo wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa ujenzi wa mradi wa maji Magu. 
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (kushoto) na ujumbe aliyoambatana nao wakimsikiliza msimamizi wa mradi, Mhandisi Wilbert Bujiku (hayupo pichani) akiuelezea mradi.
Eneo la chanzo cha maji cha mradi wa Mji wa Magu ambapo kuna mitambo ya kuvutia maji yanayotoka ziwani.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga ametoa muda wa siku 14 kwa Mkandarasi China Civil Engineering Construction Corporation (CCECC) kukamilisha ujenzi wa mradi wa maji Mji wa Magu.

Ametoa agizo hilo Novemba 22, 2019 alipofanya ziara kwenye mradi huo Wilayani Magu, Mkoani Mwanza ili kujionea hatua ya ujenzi iliyofikiwa sambamba na kuzungumza na Mkandarasi.

Mara baada ya kutembelea eneo la chanzo cha maji na kituo cha tiba ya maji cha mradi, Mhandisi Sanga alibainisha kuwa ameridhishwa na ujenzi wa mradi na kwamba tayari wananchi wameanza kupata huduma ya maji lakini yapo maeneo machache ambayo bado hayajakamilika inavyopasa na hivyo kumtaka Mkandarasi kuhakikisha anayakamilisha kwa muda aliyopangiwa.

“Mradi unaridhisha umejengwa vizuri ila tu shida ninayoiona hapa kuna maeneo machache bado hayajakamilishwa vizuri ambayo kitaalam tunaita 'snags' kama kuna pipe imechomoka, koki, kurudishia rangi,  na vingine vidogo vidogo.  Maelekezo yangu ni kwamba ndani ya wiki mbili kuanzia leo maeneo haya yakamilike,” alisisitiza Mhandisi Sanga.

Aliongeza kuwa Mkandarasi amekwishafanya kazi kubwa na kwamba hizo chache zilizobaki ahakikishe anazikamilisha haraka na kwamba baada ya siku hizo 14 awe amekabidhi mradi kwa Mamlaka ya Maji Mji wa Magu na awe ameondoka kwenye eneo la mradi ili kuondokana na gharama mbalimbali za usimamizi wake.

“Hata kama hatumlipi mkandarasi kwa hizi kazi zilizobakia lakini gharama bado zitakuwepo tu ikiwa ni pamoja na kulipa watendaji wetu ambao ni wasimamizi wa mradi fedha za kujikimu na gharama zingine zikiwemo za usafiri wa kuja kukagua kazi mara kwa mara na hivyo kutumia mafuta,” alisema Mhandisi Sanga.

Aliongeza kuwa fedha za ujenzi wa mradi ni za wananchi kwani zilitolewa na wadau wa maendeleo ambao aliwataja kuwa ni Benki ya Maendeleo ya Ulaya na Shirika la Maendeleo la Ufaransa kama mkopo wa masharti nafuu ambao Serikali inapaswa kulipa.

Alitahadharisha kwamba Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Dkt. John Pombe Magufuli haipo tayari kushuhudia matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi na kwamba haitowavumilia wakandarasi wanaochelewesha miradi kote nchini bila sababu za msingi.

“Namshukuru sana Mhe. Rais ambaye kimsingi ndio mtoaji wa fedha, tunasema fedha imetolewa na wafadhili lakini ni mkopo wa masharti nafuu na hivyo zitalipwa kwa kodi za wananchi, kwa hiyo tutahakikisha hata shilingi ya mwisho inatumika vizuri na hatuwezi kumtazama Mkandarasi afanye anavyojisikia yeye wakati wa kukamilisha mradi,” alisema Mhandisi Sanga.

Akizungumzia maeneo ambayo hayajafikiwa na mradi na uhitaji upo, Mhandisi Sanga alielekeza Mamlaka ya Maji Mwanza (MWAUWASA) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji Magu (MAUWASA) pamoja na Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) wayafanyie kazi na kwamba kwa maeneo yatakayokuwa nje ya uwezo wao wayawasilishe wizarani ili wananchi wote waliokusudiwa waweze kunufaika na mradi huo. 

Aidha, alishukuru uongozi wa Mkoa wa Mwanza na Wilaya ya Magu kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Magu, kwa ufuatiliaji na usimamizi mzuri wa mradi na kwa uhamasishaji walioufanya kwa wananchi waliokuwa wakidai fidia.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Magu, Boniventura Kiswaga aliipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa ujenzi wa mradi huo mkubwa wa maji ambao aliuelezea kuwa ni mwarobaini wa kero ya muda mrefu ya upatikanajni wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wake.

Naye msimamizi wa mradi kutoka MWAUWASA, Mhandisi Wilbert Bujiku aliahidi kusimamia vyema utekelezaji wa maelekezo ya Naibu Katibu Mkuu na kwa wakati kama ilivyoelekezwa.

Aidha, akiwasilisha taarifa ya mradi kwa ujumla, Mhandisi Bujiku alisema mradi utanufaisha zaidi ya wananchi 120,000 na kwamba hadi hivi sasa jumla ya kaya 4,911 tayari zimeunganishwa na wanapata huduma ya maji na kwamba vituo 21 vya kuchotea maji pia vimejengwa maeneo mbalimbali kulingana na idadi ya wakazi wa maeneo husika.

Aliongeza kuwa mradi umehusisha ujenzi wa tenki la lita milioni mbili za maji, ulazaji wa bomba kuu kutoka ziwani hadi kwenye tenki umbali wa kilomita 10.9 na bomba za usambazaji kwa wananchi umbali wa kilomita 67 na kwamba umegharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 16.


Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.