ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, June 29, 2019

DAR KUCHEZA NA MWANZA ROBO FAINALI SOKA WASICHANA UMITASHUMTA



Na Mathew Kwembe, Mtwara

Timu za soka za wasichana za mikoa ya Dar es salaam na Mwanza zimetinga hatua ya robo fainali ya michuano ya UMITASHUMTA na zinatarajiwa kucheza leo katika viwanja vya chuo cha ualimu Mtwara.

Dar es salaam imefikia hatua hiyo baada ya kuibuka kinara katika kundi A na hivyo itachuana na mshindi wa pili kundi C Mwanza katika hatua ya robo fainali. Pambano lingine la robo fainali litazikutanisha timu za mikoa ya Manyara ambao iliibuka mshindi wa kwanza kutoka kundi B watakaochuana na mshindi wa pili kundi D timu ya soka ya wasichana kutoka mkoa wa Mara.

Mshindi wa kwanza kutoka kundi C, timu ya soka wasichana kutoka mkoa wa Kagera imepangwa kuchuana na mshindi wa pili kundi B, Simiyu huku mshindi wa kwanza kundi D Morogoro watachuana na mshindi wa pili kundi A, Kilimanjaro.

Kwa upande wa soka maalum wavulana, michuano hiyo pia imefikia hatua ya robo fainali na inatarajiwa kuchezwa leo katika viwanja vya chuo cha ualimu Mtwara ambapo mshindi wa kwanza kundi A Kilimanjaro atachuana na mshindi wa pili kundi C Dodoma. Mshindi wa kwanza kundi B Tabora atachuana na mshindi wa pili kundi D Ruvuma. Mchuano mwingine mkali utahusisha mshindi wa kwanza kundi C, Mtwara atachuana na mshindi wa pili kundi B, Kagera huku mshindi wa kwanza kundi D, Dar es salaam atachuana na mshindi wa pili kundi A, timu ya soka maalum wavulana kutoka mkoa wa Shinyanga.

Kwa upande wa soka wavulana, michuano hiyo bado inaendelea katika hatua ya makundi na inatarajiwa kuchezwa hatua ya robo fainali tarehe 1, julai, 2019 ambapo mshindi wa kwanza kundi A atacheza na mshindi wa pili kundi C, mshindi wa kwanza kundi B atachuana na mshindi wa pili kundi D, mshindi wa kwanza kundi C atacheza na mshindi wa pili kundi B na mshindi wa kwanza kundi D atachuana na mshindi wa pili kundi A.

Matokeo ya michezo iliyochezwa kundi A kuanzia tarehe 24 juni hadi tarehe 28 juni, 2019 katika soka wavulana inaonyesha kuwa Tanga imeifunga Singida 4-0, Dodoma wameichapa Mara 2-1, Dar es salam imetoka sare na Kilimanjaro 1-1, Singida imetoka suluhu na Kilimanjaro 0-0, Mara imefungwa na Dar es salaam 0-1, Tanga imeifunga Dodoma 2-1, na Dodoma imefungwa pia na Dar es salaam 2-3.

Kilimanjaro  iliifunga Tanga 1-0, Singida iliichapa Mara 2-0, Dodoma nayo iliifunga singida 2-1, Mara ikaichapa Kilimanjaro 2-1, Dar es salaam ikatoka suluhu na Tanga, Tanga ikaifunga Mara 3-0, Singida ikachapwa na Dar es salaam 0-3 na Kilimanjaro pia ikachapwa na Dodoma 0-3.

Matokeo ya kundi B soka wavulana, Mbeya ilichabangwa na mwanza 2-5, Pwani iliibugiza Iringa 4-0, Lindi nayo ikaichapa Mtwara 2-0, Mwanza ikaifunga Pwani 3-0, Simiyu ikaifunga Iringa 2-0, na Mbeya ikaichapa Mtwara 1-0, Lindi ikatoka suluhu na Simiyu, Mtwara ikafungwa na pwani 0-3, Iringa nayo ikabugizwa na Mwanza 1-5 na Mbeya ilipata kipigo kutoka Simiyu 0-1, Mwanza imeichapa Mtwara 4-0, Pwani ikatoka sare na Lindi 1-1, Iringa ikapata kipigo kutoka Mbeya 0-4, Mtwara nayo ikafungwa na Simiyu 1-3 na Mwanza ikatoka sare na Lindi 1-1.

Matokeo ya michezo ya kundi C yanaonyesha Geita iliichapa Kigoma 1-0, Manyara iliifunga Njombe 2-1, Shinyanga ilikubali kichapo kutoka kwa Ruvuma 0-2, Kigoma iliifunga Ruvuma 1-0, na Njombe ikaifunga Shinyanga 4-1. Pia Geita ikaifunga Manyara 2-0, Manyara ilikubali kipigo kutoka kwa Shinyanga 0-5, Ruvuma nayo ilifungwa na Geita 0-2, Kigoma ikaifunga Njombe 1-0, Manyara ikaichapa Kigoma 4-0, Njombe na Ruvuma zikatoka suluhu, Shinyanga ikafungwa na Geita 0-1, Geita ikaichapa Njombe 4-0, Kigoma ikatoka sare na Shinyanga 1-1 na Ruvuma ikakubali kichapo kutoka kwa Manyara 1-3.

Katika michezo iliyochezwa kundi D soka wavulana, matokeo yanaonyesha Katavi ilifungwa na Kagera 1-2, Morogoro ilichapwa na Tabora 1-2, Rukwa ikaifunga Songwe 3-1, Morogoro ikatoka sare na Rukwa 1-1, Kagera ikaichapa Arusha 3-0, huku Katavi na Tabora zikitoka suluhu ya bila kufungana. Matokeo mengine Songwe ilichapwa na Kagera 0-2, Tabora na Rukwa zikatoka suluhu, Arusha ikachapwa na Morogoro 1-3, Arusha pia ilibugizwa na Songwe 1-7, Katavi ilifungwa na Rukwa 0-1, Morogoro ilifungwa na kagera 1-2, Arusha ilifungwa na katavi 0-2, Tabora ilichapwa na Kagera 0-3 na Morogoro na Songwe zilitoka suluhu ya bila kufungana.

Michuano hiyo inatarajiwa kuendelea leo na kesho ili kukamilisha ratiba kwa timu za soka wavulana kutoka makundi A hadi D kwa soka wavulana ili kukamilisha ratiba ya michuano hiyo kabla ya kuchezwa hatua ya robo fainali kesho kutwa katika viwanja hivyo hivyo vya chuo cha ualimu Mtwara.

 Lidya Daudi wa timu ya soka ya wasichana Geita (mwenye jezi ya bluu) akichuana vikali kugombea mpira na mchezaji Eneck Daud wa Mbeya (jezi nyeusi) wakati timu hizo zilipocheza hivi karibuni.

Mshambuliaji hatari wa timu ya soka wavulana ya mkoa wa Lindi Omari Mohamed akifunga goli la pili kwa njia ya penati dhidi ya timu ya Mtwara huku golikipa wa timu hiyo Benard William  akijaribu kuchupa bila mafanikio wakati timu hizo zilipokutana hivi karibuni. Lindi iliifunga Mtwara 2-0.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.