ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, February 19, 2026

KAMATI YA BUNGE YAITA WAWEKEZAJI UJENZI WA VITUO VYA GESI ASILIA ILIYOSHINDILIWA (CNG)

 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, kupitia Mwenyekiti wake Mhe. Subira Mgalu, imetoa wito kwa wawekezaji kuunga mkono Serikali katika ujenzi wa vituo vya gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG) ili kurahisisha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi katika Jiji la Dar es Salaam na mikoa mingine ikiwemo Morogoro na Dodoma.

Wito huo umetolewa tarehe 19 Februari 2026 wakati Kamati hiyo ilipotembelea Kituo Mama cha Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG) kilichopo eneo la Mlimani jijini Dar es Salaam.

“Tumeona Serikali tayari ina mpango wa kuongeza ujenzi wa vituo hivi kutokana na uhitaji wa wananchi kuendelea kuongezeka pamoja na unafuu unaopatikana ukitumia CNG kwenye vyomvbo vya usafiri kama vile magari na bajaji, kwani gharama zinapungua kwa asilimia 40 ukilinganisha na mafuta. Hii hii ni fursa kwa sekta binafsi kushirikiana na Serikali kujenga vituo vingi zaidi,” amesema Mhe. Mgalu

Aidha, kamati hiyo imetoa wito kwa Serikali kufunga mfumo wa CNG katika magari yake, jambo litakalosaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa vyombo hivyo vya usafiri.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini pia imeipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa uwekezaji inaoufanya katika ujenzi wa vituo vya CNG na kupelekea vyombo vya usafiri vipatavyo 15,000 kutumia CNG.


Vilevile, imepongeza shughuli za utafiti na uendelezaji wa gesi asilia zinazoendelea; ikisema kuwa upatikanaji wa gesi asilia ya kutosha utawezesha kuendelea kuboresha huduma nyinginezo ikiwemo kupikia majumbani na viwandani.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema tangu kuanza kwa vituo vya CNG nchini, Serikali imekuwa ikiona tija yake na ndiyo maana inaongeza kasi ya usogezaji wa huduma hiyo kwa wananchi kwa kuhusisha pia sekta binafsi mfano ukiwa ni uzinduzi wa hivi karibuni wa kituo cha CNG cha Puma kilichopo Salasala ambacho kwa Afrika ndicho kituo kikubwa.

Amesema Serikali pia katika mwaka huu wa fedha imeagiza magari makubwa matano yatakayobeba gesi asilia iliyoshindiliwa na kuisambaza katika vituo vilivyopo katika maeneo ya mbali ikiwemo Dodoma, Morogoro, Arusha na Tanga, lengo likiwa ni kuhakikisha huduma hiyo inapatikana kutoka eneo moja kwenda jingine.

Kuhusu kubadilisha mfumo wa magari ya Serikali kwenda kwenye CNG, ameeleza kuwa, tayari Serikali imeanza kufanyia kazi suala hilo na moja ya vielelezo ni mabasi mapya ya mwendo kasi ambayo yote yanatumia mfumo wa CNG, jambo ambalo limefanya utoaji wa huduma kwa abiria kuboreka.

Kituo cha CNG Mlimani kina uwezo wa kujaza gesi asilia kwenye magari 1,200 kwa siku huku kikiwa na pampu maalum tatu kwa ajili ya kujaza magari maalum ya kusafirisha CNG kwenda kwenye vituo vidogo vya kujaza gesi kwenye magari (Offline CNG Filling Stations), viwandani, katika taasisi na majumbani.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment