ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, August 13, 2025

KAMATI YA MTAKUWWA MWANZA YATAKIWA KUTIMIZA WAJIBU WA KULINDA JAMII DHIDI YA UKATILI

 


Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza ndugu Balandya Elikana amewataka wajumbe wa kamati ya ulinzi wa wanawake na watoto (MTAKUWWA) mkoani humo kushirikiana na serikali kuhakikisha wanatambua na kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazokabili makundi hayo na kuwaondoa kwenye ukatili.

Ndugu Balandya amesema hayo leo Agosti 13, 2025 wakati akizindua mafunzo ya siku tatu kwa kamati ya Mkoa ya kupinga na kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto NPA-VAWC 2024/25- 2028/29 II.

Amesema ni lazima mwanakamati azunguke kwenye jamii ili kubaini changamoto mbalimbali zinazowakwamisha katika kushiriki kwenye kujenga uchumi wao na kuhakikisha wanaweka misingi ya kuondoka changamoto hizo.

"Ukatili kwa wanawake na watoto unazuia maendeleo kwa jamii na nchi kwa ujumla kwani serikali inalazimika kuahughulika na majeraha ya ukatili kama kutibu na kunasihi, hivyo wajumbe nawaomba mkatekeleze wajibu wenu." Amesema Balandya.


Ameongeza kuwa mchanganyiko wa wajumbe kutoka kwenye taasisi na madhehebu ya dini mbalimbali umelenga kuyafikia makundi mbalimbali na kuhakikisha jamii yote inafikiwa na kupatiwa elimu dhidi ya ukatili.

Akizungumzia watoto wanaoishi mtaani, Katibu tawala amesema kila mmoja kwenye eneo lake ahakikishe anafikisha ujumbe kwamba ni vibaya kuwahudumia watoto wanaoomba pesa mtaani kwani inapelekea kuwafanya waendelee kuwepo.


Akimuwakilisha Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt Gabriel Mashauri amebainisha kuwa kwa siku tatu wajumbe watapitishwa katika maeneo 8 ambazo ni afua za kufuata na mwisho wa mafunzo hayo kila mjumbe atajua majukumu yake ya kila siku katika kuhakikisha watoto na wanawake wanakingwa na ukatili.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment