ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Sunday, June 23, 2024

TFS WAPONGEZWA UHIFADHI WA MISITU NA UTUNZAJI WA MAZINGIRA

 

Mmoja ya viongozi wa shamba la miti Sao Hill wilaya ya Mufindi mkoani Iringa akisoma taarifa kwa viongozi wa mwenge wa uhuru kitaifa  Mwenge wa uhuru ukiwa ukiwa katika shamba la miti la Sao Hill wilaya ya Mufindi mkoani Iringa 
Shangwe za Mwenge wa uhuru katika shamba la miti Sao Hill wilaya ya Mufindi mkoani Iringa 

 Na Fredy Mgunda, Iringa.


Mwenge wa Uhuru 2024 watembelea na kukagua shughuli za uhifadhi wa misitu na utunzaji wa mazingira Shamba la Miti SaoHill

Mbio za Mwenge wa Uhuru zimepita na kukagua mradi wa Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira TFS - Shamba la Miti Sao Hill uliopo Tarafa ya Pili ya Shamba Ihefu katika Safu ya Nyololo Wilayani Mufindi.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru 2024 Ndg.Godfrey Eliakimu Mnzava amewapongeza Wakala wa Huduma Misitu Tanzania -TFS kwa kazi kubwa ya utunzaji wa Shamba la Saohill kwani limekuwa chanzo kizuri cha mapato kwa serikali na wananchi.

"Tunaelekea katika biashara ya hewa ukaa naamini kupitia msitu huu biashara hiyo itakuwa kubwa" Amesema Ndg Mnzava

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mhe Dkt Linda Salekwa amesema kuwa Shamba la Miti Saohill limekuwa ni msingi mkubwa katika shughuli za utunzaji wa mazingira na pia limekuwa likichangia kutatua changamoto za ajira kwani wananchi wengi wanafanya kazi katika msitu huu. 

Akiwasilisha taarifa ya mradi huo Mkuu wa Kitengo cha Maliasili na Hifadhi ya Mazingira Wilaya ya Mufindi Ndg. Gilbert Ngailo amesema kuwa Shamba la Miti Saohill limekuwa mchango mkubwa katika utunzaji wa uhifadhi wa mazingira kwani limekuwa likichangia katika utoaji wa elimu ya uhifadhi kwa wananchi na pia limekuwa likiandaa vitalu vya miche ya miti, upandaji wa miti pamoja na usimamizi dhidi ya majanga ya moto.

"Mbali na kuchangia mapato makubwa katika Serikali kuu na Halmashauri Shamba hili linatoa ajira kwa wananchi, kuhifadhi mazingira, kuelimisha wananchi juu ya ufugaji wa nyuki, kukarabati miondombinu ya barabara na kuchangia shughuli za maendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa mabweni na ugawaji wa madawati katika shule mbalimbali" ameongeza.

Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2024 zinaongozwa na kauli mbiu isemayo "Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Ujenzi wa Taifa Endelevu"

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.