ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, July 5, 2022

TFS WAPONGEZWA KWA KUPAMBANA NA MATUKIO YA MOTO

 

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Balozi Dkt.Pindi Chana akisalimiana na baadhi ya watumishi wa wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) shamba la miti la Sao Hill wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa.
Baadhi ya watumishi wa wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) shamba la miti la Sao Hill wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa.
Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Balozi Dkt.Pindi Chana wa katikati alipowasili katika ofisi za mkuu wa wilaya ya Mufindi kwa ajili ya ziara ya siku moja.
Baadhi ya watumishi wa wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) shamba la miti la Sao Hill wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa katika kitengo cha moto.

 

 Na Fredy Mgunda,Iringa. 

WAZIRI wa Maliasili na Utalii Mhe.Balozi Dkt.Pindi Chana amewapongeza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa kuweka mkakati wa kupambana na majanga ya moto na kuendeleza utamaduni wa kulinda kwa kutoa elimu ya uhifadhi wa misitu kwa wananchi ambao wanayazunguka mashamba ya mimi ya TFS.


Akizungumza wakati wa ziara ya siku moja katika ofisi za Shamba la Miti SaoHill wilayani Mufindi mkoani Iringa Balozi Dkt.Chana alisema kuwa anatoa pongezi kwa uongozi na wafanyakazi wa TFS kwa kuendelea kutoa elimu ya majanga ya moto na amekikipongeza kitengo cha moto kwa kukabiliana vilivyo na majanga ya moto.


Dkt.Pindi Chana amewataka watumishi wa TFS kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kwa ajili ya kuendelea kulinda hifadhi za misitu


Alisema kuwa licha ya kazi kubwa wanayoifanya kulinda misitu lakini bado wamefanikiwa kutoa ajira zaidi ya 4000 katika shamba la miti ya kupanda la Sao Hill jambo ambalo linasaidia serikali kuendelea kutoa ajira kama ilivyokuwa kwa serikali kuwa ajira limekuwa swala la kipaumbele katika awamu hii ya sita ya uongozi.


Dkt.Pindi Chana aliwapongeza TFS  Sao Hill kwa kufanikiwa kutatua migogoro kumi na mbili na kubakiwa mitatu ambayo anaamini kuwa watatafuta nyia ya kuimaliza migogoro hiyo kama ambavyo wamefanya kwenye kutatua migogoro mingine.


Lakini pia Dkt.Pindi Chana aliwata TFS Sao Hill kuanza kutafuta bidhaa mpya za zao la misitu ambayo yatakuwa na faida kwa wananchi na taifa kwa ujumla.


Katika ziara hiyo Balozi Dkt.Chana ametembelea kiwanda cha kuchakata mazao ya nyuki kilichopo Shamba la Miti SaoHill na kuipongeza TFS kwa kazi nzuri ya uzalishaji wa mazao yanaotokana na misitu ikiwemo asali.


Kwa upande wake Kamishna wa Uhifadhi TFS Prof.Dos Santos Silayo amesema katika kuunga mkono juhudi za serikali kwenye sekta ya utalii TFS imeandaa mpango wa kuzifanya hifadhi kuwa ni sehemu ya utalii


Prof.Silayo alisema kuwa katika shamba la miti la Sao Hill wamekuwa wakifanya utalii wa kutembea kwa miguu,utalii wa pikipiki na baiskeli akaongeza kuwa wamejipanga kuhakikisha wanaanzisha utalii wa farasi jambo ambalo wanaamini litakamilika hivi karibuni.


Naye Mbunge wa Mafinga Mjini Mhe. Cosato Chumi amesema  sekta ya Misitu ina mchango mkubwa kwa wananchi hasa wa Mafinga kwa kutoa  ajira nyingi na mchango mkubwa kwenye Mapato ya Halmashauri hiyo kwa asilimia 60,  hivyo yeye kama mwakilishi wa wananchi ataendelea kushirikiana  na Wizara katika uhifadhi wa Maliasili hiyo.

Chumi alisema kuwa asilimia 85 ya wananchi wa wilaya ya Mufindi na Jimbo la Mafinga Mjini wanategemea mazao ya misitu kukuza uchumi wa wananchi wa Mufindi


Alisema kuwa anawapongeza TFS kupitia shmba la miti la Sao hill kwa kuwa wamekuwa na mchango mkubwa wa kimaendeleo kwa kusaidia ujenzi kwenye sekta ya afya elimu na biashara kwa kuboresha miundombinu katika maeneo hayo.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.