ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, November 12, 2021

MIAKA 6 TU NA UFANISI MKUBWA HOSPITALI YA BENJAMIN MKAPA.

 

Na WAMJW-DOM 

Waziri wa afya Dkt Dorothy Gwajima ameupongeza uongozi wa hospital ya Benjamin Mkapa kwa mafanikio makubwa waliyoyapata kwa kipindi cha miaka sita.

Dkt. Gwajima ametoa pongezi hizo leo jijini Dodoma katika hotuba yake ya uzindunzi wa bodi ya hospitali hiyo, shughuli iliyofanyika katika viwanja vya hospitali hiyo Jijini Dodoma. 

Kwa kiasi kikubwa, Dkt.  Gwajima amefurahishwa na utendaji wa wataalamu wazawa kwa kuthubutu kutoa huduma za upandikizaji wa figo bila kujali vinasaba, pamoja na kutibu magonjwa ya moyo pasipo kufungua kifua ambapo imepunguza gharama kwa wananchi kwenda kutibiwa nje.

Pamoja na hayo Dkt. Gwajima amewataka bodi, menejimenti na watumishi wajitume kwa weledi, maadili na nidhamu ya hali ya juu maana wameteuliwa kwa kuzingatia sifa, uzoefu na uchapa kazi.

 "Nipende kusema kuwa ninyi ni miongoni mwa hazina ya wachapakazi wa taifa hili", alisema Dkt Dorothy Gwajima.

Aidha, Dkt. Gwajima amesema tayari  wagonjwa 25 wamepandikizwa figo ndani ya kipindi cha miaka mitatu, na sasa Hospitali hii imepandikiza figo pasipo kujali vinasaba.

 "Kwa taarifa nilizonazo wagonjwa 25 wamepandikizwa figo ndani ya kipindi cha miaka mitatu, na sasa nimesikia mmepiga hatua zaidi kwenye eneo hilo kwa kupandikiza figo pasipo kujali vinasaba, hii ni hatua kubwa hongereni sana."Amesema Dkt Gwajima. 

Hata hivyo Dkt. Gwajima amesema kuwa, huduma zimeendelea kuongezeka katika hospitali hii hususan huduma za Ubingwa Bobezi.

Kwa kipindi kifupi cha miaka sita tu, mmeweza kupandikiza figo, kutibu magonjwa ya moyo pasipo kufungua vifua na kwa kufungua vifua, mmeweza kutoa huduma za upasuaji wa nyonga na magoti, uvunjaji wa mawe kwenye figo pasipo upasuaji, upasuaji Ubongo na uti wa mgongo. Ameendelea.

Mbali na hayo, Dkt. Gwajima amesema kuwa, mafanikio haya tunayojivunia hapa yanatokana na utekelezaji wa sera nzuri na madhubuti za Serikali ya awamu ya Tano na Sita katika Sekta ya afya.

Pia, ameipongeza Bodi iliyopita na Menejimenti ya Hospitali ya Benjamin Mkapa kwa kuleta mabadiliko makubwa ya huduma na kukidhi lengo la uanzishwaji wa Hospitali hii kwa ndani ya muda mfupi wa miaka sita tu.

Hata hivyo ametoa rai, kwa Bodi Mpya aliyoizindua kuhakikisha inasimamia kwa karibu utoaji wa huduma bora kwa wananchi huku akielekeza kuweka namba za simu wazi ili wapate mrejesho wa moja kwa moja kutoka kwa wananchi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.