ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Sunday, November 28, 2021

DKT. GWAJIMA SASA AGEUKIA MAPATO NA MATUMIZI VITUO VYA AFYA.

 Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amewaagiza viongozi wa hospitali zote ngazi ya Taifa, Mkoa, Wilaya kuunda Kamati ndogo za ufuatiliaji wa mapato ya fedha za uchangiaji kila siku toka vitengo vyote ili kufahamu bayana kiasi kinachokusanywa maana imebainika viko vitengo ambavyo makusanyo yake ya fedha za uchangiaji ni madogo kuliko kilichochangiwa au kilichotarajiwa kuchangiwa. 


Aidha, ameelekeza Kamati hizo pia zihusike na kuchambua iwapo matumizi ya kwenye eneo la dawa na vipimo au bidhaa za afya kiwango kinafikia asilimia 50 au zaidi kama ilivyoelekezwa kwenye mwongozo wa wizara.

Dkt. Gwajima ametoa maagizo hayo leo 28.11.2021 wakati akizungumza na watumishi wa Hospitali ya Rufaa Mkoa Kitete Mjini Tabora ambapo amesema kuwa iundwe Kamati hiyo ndogo ya kusimamia mapato ya fedha ili kudhibiti upotevu wa fedha za umma na utumiaji wa kiasi kidogo cha fedha za uchangiaji kwenye kununua vifaa tiba ikiwemo dawa.


Dkt Gwajima amesema kuwa usimamizi mzuri wa wa uendeshaji wa vituo kwa ujumla wake pamoja na usimamizi mzuri wa uwajibikaji kwenye matumizi ya raslimali zote ikiwemo fedha ni muhimu na ni chachu katika kuboresha huduma na kuvutia wateja wa makundi yote ya uchangiaji huduma ili dhana ya uendelevu wa huduma kwa uchangiaji na hususan Bima za Afya itimie kwa ukamilifu wake.


Kutokana na kulegalega kwa upatikanaji wa huduma za vipimo na dawa mara nyingi wateja hasa wenye uwezo wa kuchangia huduma wamekuwa wakihama baadhi ya vituo na vituo hivyo kuanza kujenga hoja kuwa havina fedha za uendeshaji kwa kuwa wanaotibiwa hapo ni wale wasio na uwezo wa kuchangia. Hii siyo dhana sahihi amesema Dkt Gwajima kwani wateja wenye bima kwa jumla wake ni asilimia 14 ya watanzania wote na waliobakia wasio na bima ni asilimia 26 tu ndiyo hawana uwezo. Je waliobaki wenye uwezo wanaochangia huduma wanatibiwa wapi? Ni Dhahiri kuwa vituo vikiboresha huduma na usimamizi wa raslimali uwiano wa wateja utakuwa kama ilivyokusudiwa kwenye miongozo ya afya kuwa kwa uwiano huo na kwa bajeti inayoletwa na serikali basi hata wasio na uwezo wa kuchangia inawezekana kuhudumiwa.



Dkt. Gwajima amesema zipo tafiti za kutosha ambazo takwimu zake zinaonesha bayana kuwa mapato ya uchangiaji huduma kwenye vituo vingi yanavuja kiasi cha kuathiri uendeshaji wa vituo hivi na hasa upatikanaji wa bidhaa za afya zikiwemo dawa na vipimo vya maabara na hivyo kuathiri makundi mbalimbali yakiwemo ya wanaotakiwa kupata huduma kwa msamaha.


 Amesema hali hii inasababishwa na baadhi ya watumishi wazembe na wabadhilifu na uongozi usio na makali ya kuchukua hatua kwenye ngazi husika na kufumbia macho mambo haya au kukosa mbinu na nguvu za kufuatilia na kuchukua hatua.


Aidha Dkt Gwajima amewataka watumishi kushirikiana katika utendaji kazi kwa kuwa na umoja wa dhati huku akimpongeza Mtumishi wa kujitolea anayepambana kikamilifu kusimamia mapato Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Tabora Ndg. Mohamoud Ramadhan ambaye hupita kila eneo la huduma na kuhakikisha uchangiaji wa huduma umefanyika hali iliyosababisha kuchukiwa na watumishi wasiyo waadilifu wakihofia kufichuliwa. Dkt. Gwajima amesema watu wenye moyo kama hawa wanatakiwa wapewe nafasi kwenye ajira kwani sifa zingine zote wanazo.


Aidha amemuagiza mganga mkuu wa mkoa wa Tabora  Dkt Hororatha Rutatinisibwa kusimamia kuhakikisha Ngg. Ramdhani anapata motisha ya na uwezekano wa kuajiriwa ajira ya kudumu badala ya mkataba kwani ameonesha uzalendo wa hali ya juu ulioleta mapinduzi makubwa ya kudhibiti upotevu wa fedha za uchangiaji na ameonesha yale ambayo yalikuwa yanasitiriwa na wajanja na ameisaidia serikali kudhibiti mapato yanayopotea kutokana na baadhi ya watumishi ambao hawatekelezi wajibu wao kwa kujali maslahi yao Binafsi.


Awali Afisa Mapato wa kujitolea katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Tabora Kitete Mohamudu Ramadhani amemwambia Waziri wa Afya Dkt Gwajima kuwa baada ya kubaini upotevu wa Fedha za umma na dawa alishauri wakuu wa idara zote kutoa taarifa ya mapato kila siku kwa kulinganisha na idadi ya wagonjwa wanaopokelewa ila baada ya kutoa maagizo hayo baadhi ya wakuu wa idara hawakuwa tayari kutoa ushirikiano kwake bila sababu za msingi. Dkt. Gwajima amesema amepokea na hao wasiotaka kutoa ushirikiano watakutana na sheria, kanuni na taratibu za serikali.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.