ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, April 13, 2019

DAWASA KUFUFUA VISIMA VYA PEMBEZONI KWA MJI DAR ES SALAAM NA PWANI

Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) Neli Msuya (mwenye kofia) akitoa maelezo kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja (wa kwanza kushoto) mara baada ya kutembelea mradi wa Kisima cha Maji cha Gezaulole kichojengwa kwa muda mrefu na kimekuwa kikitoa huduma kwa watu wachache tu. Picha zote na Cathbert Kajuna - Kajunason/MMG.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja akimsikiliza Msimamizi wa Miradi ya Pembezoni Mhandisi Gonsalves Rutakyamirwa wakati akimuonyesha ramani ya mtandao wa maji utakavyokuwa wakisambaziwa wananchi na Gezaulole.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja akimsikiliza Msimamizi wa Miradi ya Pembezoni Mhandisi Gonsalves Rutakyamirwa wakati akimuonyesha genereta inayotumika kufua umeme kwa ajili ya kusambazia wakazi wa Gezaulole.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja akiwasha mashine.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja akionyeshwa mashine zilizokuwa zikitumika kuvuta maji.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja akimsikiliza Msimamizi wa Miradi ya Pembezoni Mhandisi Gonsalves Rutakyamirwa wakati akimuonyesha kisima cha maji kinachotumika kusambazia wakazi wa Vijibweni, Kigamboni.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja akitoa maelekezo kwa msimamizi wa mradi.
Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja  akitoa maelekezo.

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.

Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Mkoa wa Dar es Salaam (DAWASA) imeanza mchakato wa kuvifufua na kuvirejesha visima vilivyojengwa na  Serikali na kuachwa kwa muda mrefu bila kutumika kwa ajili ya kuhudumia wananchi wa pembezoni mwa mji.

Akizungumzia mchakato huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kuna maeneo ambayo hayana mtandao wa maji ya bomba kwahiyo wameamua kuvifufua visima vilivyojengwa muda mrefu na serikali au wahisani ili viweze kuhudumia wananchi wa maeneo hayo na yaliyokaribu.

Amesema, kuna kisima kilichopo Gezaulole na Vijibweni tayari wameshaanza kuvifanyia tathmini na vinatarajia kuanza kutoa maji kwa wananchi wa maeneo hayo na yaliyokaribu nao.

“Visima hivi vilijengwa kwa muda mrefu sana, katika maeneo ambayo hayana mtandao wa DAWASA tumeamua kuwapelekea huduma ya maji kwa kutumia visima hivi ambavyo maji yake ni safi na salama,”amesema Luhemeja.

“Ninapoongelea asilimia 85 ya wananchi wanaotumia maji safi na salama ndani ya mkoa wa Dar es Saalaam namaanisha na huduma hii ya visima, na lengo letu ni kuhakikisha kuwa ifikapo Juni 2020 tunataka Watu wote wawe wanapata maji,”

Msimamizi wa Miradi ya Pembezoni Mhandisi Gonsalves Rutakyamirwa amesema bado wanaendelea na tathmini ya kufahamu visima hivyo vina uwezo wa kuhudumia wananchi wa ngapi pamoja na kujenga tenki la kuhifadhi la maji.

Nao Wananchi wa eneo la Gezaulole wamefurahi kuona wanatarajia kupata maji safi na salama kwakuwa kwa kipindi kirefu wamekuwa wanatumia maji ya visima ambapo ni vifupi na kuhatarisha maisha yao kiafya hususani ifikapo kipindi cha mvua, visima huchafuka na kuchanganyika na udongo.

Kwa sasa Mkoa wa Dar es Salaam unapata maji Lita Milion 502 kutoka kwenye vyanzo vya Ruvu juu, Ruvu Chini na Mto Kizinga.

Ziara hiyo itaendelea tena kesho kwa kutembelea miradi mingine ikiwemo maunganisho mapya ya wateja, mradi wa Maji Chalinze na Miradi mingine inayoendelea kujengwa kwa kutumia fedha za ndani za DAWASA ambapo takribani Bilion 3 zinatumika kila mwezi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.