ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, March 22, 2018

KOREA YA KUSINI YAONGOZA KUWA NA WAFANYAKAZI WAPENDA KAZI KUPITA KIASI.


Serikali nchini Korea Kusini imeanzisha mpango wa kuwalazimisha wafanyakazi kuondoka kwa wakati baada ya kumalizika kwa zamu yao.

Mpango huo unahusisha kuzimwa kwa lazima kwa kompyuta za wafanyakazi hao afisini saa mbili usiku kila Ijumaa.

Lengo la mpango huo ni kujaribu kufikisha kikomo "utamaduni wa kufanyakazi muda wa ziada".

Wafanyakazi nchini humo hufanya kazi muda mwingi zaidi kwa siku ukilinganisha na wafanyakazi wengine nchi nyingine duniani.

Wafanyakazi wa serikali Korea Kusini kwa kawaida hufanya kazi saa 2,739, muda ambao ni saa 1,000 zaidi ya muda wanaofanya kazi watumishi wa umma katika mataifa yaliyoendelea.

Mpango huo wa kuzima kompyuta kwa lazima utaanza kutekelezwa na serikali ya jiji la Seoul kwa awamu tatu katika kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Utaanza kutekelezwa mnamo 30 Machi, ambapo kompyuta zote zitakuwa zinazimwa saa mbili usiku.

Awamu ya pili itaanza Aprili kwa kompyuta kuzimwa saa moja unusu usiku Ijumaa ya pili na ya nne ya mwezi.

Kuanzia Mei, mpango huo utaanza kutekelezwa kikamilifu ambapo kila Ijumaa saa moja jioni kompyuta zitakuwa zinazimwa kwa lazima.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa serikali ya jiji la Seoul, wafanyakazi wote wataathiriwa na mpango huo, ingawa baadhi wanaweza kuepushwa kukiwa na hitaji maalum.

Hata hivyo, si wafanyakazi wote wanaofurahia mpango huo.

Serikali hiyo inasema 67.1% ya wafanyakazi wa serikali wameomba kutoshirikishwa kwenye mpango huo.

Mapema mwezi huu, bunge la Korea Kusini lilipitisha sheria kupunguza saa za kufanya kazi kila wiki kutoka saa 52 hadi saa 68.

Katika mataifa mengi, watu hufanya kazi saa 40 kwa wiki.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.