ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, February 8, 2011

WADAU WA SANAA WAIOMBA SERIKALI KUINGIZA RASMI SOMO LA SANAA KATIKA MITAALA YA ELIMU NCHINI.

Mkufunzi wa Bendi ya Jeshi la Polisi, Damas Mpepo akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kuhusu Mchango wa Majeshi Katika Kuthamini Ajira za Sanaa. Kutoka kushoto ni Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego, Afisa wa Bendi ya Polisi Bw. Mayalla na Mratibu wa Jukwaa hilo, Ruyembe C.Mulimba.(picha na Sufiani Michuzi)

Na Mwandishi Wetu

Serikali kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imeombwa kuliingiza rasmi somo la Sanaa kwenye mitaala ya elimu kutoka ngazi ya awali ili kujenga vipaji vya vijana katika tasnia hii na baadaye kuweza kujiajiri.

Ombi hilo limetolewa Jumatatu ya wiki hii na wadau wa sanaa wakati wakichangia mada kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) iliyohusu Mchango wa Majeshi Katika Kukuza Ajira za Sanaa nchini iliyowasilishwa na Mkufunzi wa Bendi ya Polisi Damas Mpepo ambapo wengi walikunwa na jinsi majeshi yetu yanavyoenzi sanaa na kuwa mstari wa mbele kuiimarisha tasnia hii.

“Majeshi yetu yamekuwa yakifanya vizuri katika tasnia ya Sanaa kwa kuwa kuna elimu wanayoipata katika tasnia hii. Ni lazima Wizara ya Elimu iamke sasa na itambue kwamba tasnia ya sanaa ni kimbilio la vijana wengi kwa sasa hivyo lazima uwekwe utaratibu wa kujenga vipaji vya sanaa toka ngazi ya awali ili kukuza tasnia hii inayoajiri vijana wengi kwa sasa” alichangia mdau.

Hoja hii iliungwa mkono na Mkufunzi Mpepo wa Bendi ya Polisi ambapo aliweka wazi kwamba, wizara haina jinsi kwa sasa zaidi ya kuliingiza somo la sanaa kwenye mitaala ya elimu badala ya ilivyo sasa ambapo limekuwa halitahiniwi na vijana wengi mashuleni wamekuwa wanalikuta mitaani baada ya kumaliza shule.

“Sanaa inaajiri watu wengi sana, hata Jeshi la Polisi limeajiri wasanii karibu 500, tatizo lililopo sasa ni kwamba somo la Sanaa halifundishwi na hivyo ujuzi katika tasnia hii ni tatizo kubwa. Wizara ya Elimu lazima sasa ione haja ya kuliingiza somo la sanaa kwenye mitaala ya elimu toka ngazi ya awali na litahiniwe kwenye mitihani ya shule na taifa” alisisitiza Mpepo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Jukwaa la Sanaa ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Mfuko na Uwezeshaji BASATA Ruyembe Mulimba alisema kwamba, hoja ya somo la sanaa kufundishwa toka ngazi ya awali ya elimu ilichukua muda mwingi kwenye Kikao cha Nane cha Sekta ya Utamaduni kilichomalizika hivi karibuni jijini Mwanza ambapo wadau walitoka na azimio la kushawishi somo hili kuanza kufundishwa na kutahiniwa kama masomo mengine.

“Kauli mbiu ya kikao cha nane cha sekta ya utamaduni ilikuwa ni Sanaa ni Ajira Tuithamini lakini wadau wengi walisikitishwa na somo la sanaa kutokufundishwa toka ngazi ya awali na walitaka wizara ya elimu kusikia kilio hicho kwani tasnia hii kwa sasa inaajiri vijana wengi sana wanaokadiliwa kufika milioni sita.

Katika kikao hicho cha Jukwaa la Sanaa, Jeshi la Polisi kupitia Bendi yake lilitoa taratibu za kuajiri wasanii na sifa zinazohitajika ambapo jumla ya wadau 157 waliohudhuria walipata wasaa wa kuelimishwa kazi mbalimbali za Bendi ya Jeshi la Polisi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.