
Akizungumza leo Alhamisi Mei 21, 2026 wakati wa uzinduzi rasmi wa Siku ya Ziwa Victoria na kufunga kilele cha maadhimisho ya kwanza yaliyofanyika katika Viwanja vya Nanenane Nyamhongolo jijini Mwanza, Dkt. Nchemba amesema Ziwa Victoria si mali ya taifa moja pekee bali ni hazina ya pamoja inayounganisha nchi za Afrika Mashariki kiuchumi, kijamii na kimazingira.
Amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo isemayo “Maji Yetu, Mustakabali Wetu: Tuungane kwa Uendelevu wa Bonde la Ziwa Victoria” inapaswa kuwa chachu ya kuongeza uwajibikaji wa pamoja katika usimamizi wa rasilimali za maji, ulinzi wa mazingira pamoja na kuimarisha mshikamano wa kikanda.
“Ziwa Victoria ni uti wa mgongo wa maisha ya watu wetu. Linatoa ajira kupitia uvuvi, usafiri wa majini, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi, hivyo ni lazima tulinde mazingira yake kwa nguvu zote,” amesema Dkt. Nchemba.
Aidha amesema Serikali itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kuimarisha usalama majini, kudhibiti uharibifu wa mazingira na kutumia teknolojia za kisasa katika usimamizi wa shughuli zinazofanyika ndani na pembezoni mwa ziwa hilo.
Katika hotuba yake, Waziri Mkuu pia amesisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo ya uokoaji majini ili kuzuia ajali pamoja na matumizi ya mifumo ya kidijitali kufuatilia shughuli za uvuvi, ubora wa maji na athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo zimeendelea kuwa tishio kwa mazingira ya Ziwa Victoria.
Kadhalika, ametoa rai kwa taasisi za utafiti na wadau wa mazingira kuendelea kufanya tafiti zitakazosaidia kupatikana kwa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazoikabili Ziwa Victoria ikiwemo ongezeko la magugu maji, uchafuzi wa mazingira na uharibifu wa vyanzo vya maji.
“Sote tunawajibika kuhakikisha Ziwa Victoria linaendelea kuwa salama na lenye manufaa kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo,” amesisitiza Dkt. Nchemba.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema Tanzania itaendelea kuwa mstari wa mbele katika juhudi za kulinda na kuhifadhi Ziwa Victoria kutokana na mchango wake mkubwa katika uchumi, usalama wa chakula na maendeleo ya wananchi wa ukanda wa ziwa.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha viongozi wa Serikali, wadau wa mazingira, taasisi za utafiti pamoja na wananchi kwa lengo la kujadili namna bora ya kuhifadhi na kutumia kwa uendelevu rasilimali za Bonde la Ziwa Victoria.

Tupe maoni yako
0 comments:
Post a Comment