ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, October 11, 2023

WAZIRI MHAGAMA AZINDUA WIKI YA VIJANA KITAIFA SAMBAMBA NA KITABU CHA MWONGOZO WA UWEKEZAJI MKOANI MANYARA

 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama (kulia) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa kitabu cha Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Manyara sambamba na Wiki ya Vijana katika Wilaya ya Babati Mkoani Manyara. Kushoto kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbert Sendiga.

Na Cathbert Kajuna -MMG/Kajunason, Manyara.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama amezindua kitabu cha Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Manyara sambamba na Wiki ya Vijana katika Wilaya ya Babati Mkoani Manyara.
Muongozo huo unaelezea kwa kina fursa mbalimbali za kiuchumi zilizopo Mkoani Manyara na Dira ya Mkoa kwenye eneo la Uwekezaji na Maendeleo.
Uzinduzi huo uliofanyika katika Wiki ya Vijana Kitaifa 2023 iliyoanza Oktoba 8, 2023 inatarajiwa kumalizika Oktoka 14, 2023 ambapo itaenda Sambamba na Uzimaji wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa katika mkoa huo.

Akizungumza katika Uzinduzi huo Waziri Mhagama ambaye alimwakilisha Waziri Mkuu Mhe. Khasim Majaliwa amefurahishwa na mwamko wa Vijana jinsi walivyojitokeza kuhudhuria katika Wiki yao inayowapa fursa ya kutambua mambo mbali mbali yanayofanywa na vijana wenzao Tanzania nzima.

"Binafsi nimefurahishwa na muamko wa vijana jinsi mlivyojiyokeza na kuonyesha kazi zenu, nimepita katika mabanda mbali mbali nimejionea kazi zenu za mikono na kwakweli vijana ni nguvu kazi ya Taifa letu," amesema Waziri Mhagama.

Waziri Mhagama alitoa pongezi kwa Viongozi wa Mkoa wa Manyara unaoongozwa na Mkuu wa Mkoa Mhe. Queen Cuthbert Sendiga kwa jinsi walivyojipanga kusimamia na kufanya maandalizi ya shughuli mbalimbali za kiserikali ikiwemo Wiki ya Vijana, Ibada ya Kitaifa ya kumbukizi ya Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbert Sendiga amesema kuwa mkoa wa Manyara unamaono makubwa sana katika kupambanua fursa zilizopo hivyo ni vyema vijana wakawa msitari wa mbele katika kuchangamkia fursa hizo.

"Nawashukuru timu nzima ya Mkoa wa Manyara kwa kazi nzuri na kubwa tulioshirikiana kwenye uzinduzi wa jarida hili, tunaweka mazingira rafiki kwa kila atakayetaka kuwekeza ndani ya Mkoa wetu wa Manyara, tumeanza kutangaza fursa hizi kwa vijana wetu waliofurika mjini Babati kutoka pande zote za Tanzania," amesema Mhe. Queen.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali, Chama ,Taasisi, na Dini.

Wiki ya Vijana Kitaifa 2023 yanayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu yakiwa na Kauli mbiu, "Vijana na Ujuzi Rafiki wa Mazingira kwa Maendeleo Endelevu"
Wageni mbali mbali ikiwemi wakuu wa taasisi za kiserikali na binafsi pamoja na mashirika ya maendeleo waliohudhuria hafra hiyo.
Wanahabari.
Meza kuu.
Wadau wa maendeleo wakipokea kitabu cha Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Manyara
Wanafunzi wa Shule ya Msingi Kateshi "A" (Wanafunzi wenye mahitaji Maalumu) wakitoa ujumbe kwa viongozi ikiwa ni maadhimisho ya Wiki ya Vijana Kitaifa 2023 yanayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu yakiwa na Ujumbe "Vijana na Ujuzi Rafiki wa Mazingira kwa Maendeleo Endelevu"
Msanii Shoro Mwamba akitumbuiza.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.