ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, January 27, 2022

DKT. GWAJIMA KUANZISHA MADAWATI YA KIJINSIA VYUO VIKUU

Na WMJJWM-DSM

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe Dkt.Dorothy Gwajima amesema kuwa Serikali imejipanga kukabiliana na changamoto za ukatili wa kijinsia zinazowakabili Baadhi ya Wanafunzi waliopo Vyuo Vikuu hapa nchini ili kunusuru kushuka kwa ufanisi wa masomo.


Amebainisha hayo jijini Dar es salaam katika Uzinduzi wa Dawati la Jinsia kufuatia utekelezaji wa mradi wa kutetea haki za Jinsia wa unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO ). 


Dkt. Gwajima  amesema kuwa Serikali ya awamu ya Sita inayo ongozwa na Mhe.Rais  Samia Suluhu Hassan imejipanga kupambana na Ukatili wa Kijinsia.


"Kuna matukio mengi ya ukatili wa kijinsia kwenye jamii ikiwemo Vyuoni na shuleni hivyo kuna haja ya kuweka mikakati madhubuti ya kuanzisha Madawati ya Jinsia yanayofanya kazi kwa  mfumo wa kupima ufanisi wake ili isije ikawa tumefungua kwa mazoea yakakosa tija" amesema. Dkt. Gwajima.

Aidha Dkt Gwajima amesema, Serikali imetekeleza mambo mengi katika kupambana na ukatili wa kijinsia mathalani kukuza uelewa wa wananchi kutoa taarifa za matukio, Madawati ya Jinsia 420 yameundwa kwenye Vituo vya Polisi na 153 kwenye Jeshi la Magereza, Kamati 18,186 za Ulinzi wa Wanawake na Watoto zimeanzishwa nchini, Vituo vya huduma kwa wahanga vimeanzishwa kwenye hospitali 14, Sheria ya msaada kwa wahanga na 1 ya mwaka 2017 imetungwa na mambo mengine mengi.


Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mhe.Omari Kipanga, amesema kuwa mradi wa ‘03plus’ utanufaisha Vyuo Vikuu vya Dar Es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) Serikali ya awamu ya sita imejipanga kikamilifu kuondoa changamoto ya ukatili wa kijinsia.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mwakilishi wa UNESCO nchini Tirso Santos amesema kwamba lengo la kuleta mradi huo ni kutaka kuona wanafunzi wa kike waliopo vyuo vikuu wanasoma kwa kujiamini


Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.