ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, June 25, 2019

MRADI WA MAJI LAMADI WAFIKIA HATUA ZA MWISHO

Washirika wa maendeleo wakiwa katika picha ya pamoja na watendaji Serikalini. Katikati waliokaa ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Emmanuel Kalobelo; kulia kwake ni Ofisa Mradi kutoka AFD, Katell Rivolet na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Jijini Mwanza (MWAUWASA), Mhandisi Anthony Sanga na kushoto kwake ni Mkuu wa Msafara wa AFD, Claire Fargeaudou na Mratibu mradi kutoka EIB, Raoul Pedrazzani.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Emmanuel Kalobelo akisisitiza jambo wakati wa majadiliano ya utekelezaji wa miradi ya maji ya LV WATSAN. Kulia kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Jijini Mwanza (MWAUWASA), Mhandisi Anthony Sanga na Naibu Mkurugenzi, Idara ya Usambazaji Maji wa Wizara ya Maji, Mhandisi William Christian.
Ujumbe wa washirika wa maendeleo ulitembelea maeneo mbalimbali ya mradi. Pichani ni sehemu ya eneo la Tiba ya Maji.
Washiriki wa mkutano wakikagua miundombinu ya tiba ya maji kwenye mradi wa Maji wa Lamadi. Wa kwanza ni Mratibu mradi wa LV WATSAN kutoka EIB, Raoul Pedrazzani.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Jijini Mwanza (MWAUWASA), Mhandisi Anthony Sanga akizungumza jambo wakati wa mkutano. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Emmanuel Kalobelo. Kushoto kwake ni Naibu Mkurugenzi, Idara ya Usambazaji Maji wa Wizara ya Maji, Mhandisi William Christian.
Muonekano wa baadhi ya maeneo ya mradi wa maji wa Lamadi ambao ulitembelewa na ujumbe wa washirika wa maendeleo.
Ujumbe wa washirika wa maendeleo wakiwa katika picha ya pamoja na Watendaji kutoka Serikali kwenye eneo la chanzo cha maji cha maji mradi wa Lamadi.


Serikali imesema imeridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa maji wa Lamadi uliopo Wilaya ya Busega Mkoani Simiyu ambao utekelezaji wake umefikia asilimia 93.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Emmanuel Kalobelo alisema hayo hivi karibuni wakati wa ziara yake kwenye mradi huo.
Katika ziara hiyo Mhandisi Kalobelo alifuatana na washirika wa maendeleo wanaowezesha utekelezaji wa miradi ya maji kupitia Programu ya Uboreshaji wa Huduma ya Majisafi na Usafi wa Mazingira ijulikanayo kama LV WATSAN ambao ni Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB) na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD).
Mhandisi Kalobelo alisema amefarijika kushuhudia hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa mradi na aliongeza kuwa hadi kufikia Agosti mwaka huu utakuwa umekamilika kwani shughuli iliyopo kwa sasa ni ya ufungaji wa pampu na baada ya hapo maji yataanza kutoka.
Kwa upande wake Mratibu mradi kutoka EIB, Raoul Pedrazzani alisema miradi inayotekelezwa chini ya Programu ya LV WATSAN imeonyesha mafanikio makubwa na aliipongeza Mamlaka ya Maji Mwanza (MWAUWASA) ambayo inajukumu la kusimamia miradi hiyo kwa niaba ya Wizara ya Maji kwa usimamizi mahiri wa utekelezaji wake.
Pedrazzani alisema EIB ina nia ya dhati ya kupanua ushirikiano na Serikali ya Tanzania katika siku zijazo kwani imeridhishwa na namna ambavyo Serikali inatekeleza miradi maeneo mbalimbali kote nchini.
Naye Afisa Miradi kutoka AFD, Clement Kivegalo akizungumza kwa niaba ya ujumbe alioambatana nao, alisema wameridhishwa na hatua ya utekelezaji wa mradi na kwamba AFD itaongeza udhamini kadri itakavyohitajika kufanya hivyo.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Busega, Tano Mwera ambaye alikuwa mwenyeji wa ugeni huo wilayani hapo, alisema mradi unatarajiwa kuleta mabadiliko makubwa kwenye wilaya na hususan katika mji wa Lamadi na alitoa wito kwa wawekezaji kujitokeza kwani maji ya yhakika yamepatikana na kwamba miundombinu mingine ipo vizuri ikiwemo barabara na umeme wa uhakika.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa MWAUWASA, Mhandisi Anthony Sanga akiuelezea mradi alisema unafadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia mia moja kupitia mkopo wa masharti nafuu kutoka EIB na AFD kwa gharama ya Shilingi Bilioni 12.83.
Mhandisi Sanga alisema mradi utazalisha lita Milioni 3.3 za maji kwa siku ambayo ni mara mbili ya mahitaji ya sasa ya wananchi wa Lamadi na maeneo jirani hasa ikizingatiwa kwamba mradi umebuniwa kuhudumia wananchi zaidi ya 60,000.
Aliongeza kuwa hatua ya kwanza ya maunganisho kwa wananchi; mradi utaunganisha kaya zipatazo 5000 na aliwataka wananchi kuchangamkia mradi ili kujiletea maendeleo.
Kabla ya ziara hiyo, washirika hao wa maendeleo walifanya mkutano Jijini Mwanza na watendaji kutoka Serikalini kwa ajili ya majadiliano na tathmni ya hatua za zilizofikiwa kwenye ujenzi wa miradi ya maji inayotekelezwa chini ya Program ya LV WATSAN.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.