ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, November 13, 2018

MAMLAKA YA MAJI MWANZA WAPIGWA MSASA NA JUMUIYA YA KIMATAIFA YA MAJI

 Mkurugenzi Mtendaji wa MWAUWASA, Mhandisi Anthony Sanga (kulia) akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uandaaji wa Mpango wa Usalama wa Maji yanayotolewa kwa wafanyakazi wa MWAUWASA na  Jumuiya ya Kimataifa ya Maji (IWA)
 Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa Mpango wa Usalama wa Maji yanayotolewa na  Jumuiya ya Kimataifa ya Maji (IWA) wakimsikiliza Mhandisi Anthony Sanga (hayupo pichani). Wa pili kulia ni Mkufunzi kutoka IWA, Kizito Masinde.
 Washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa Mpango wa Usalama wa Maji yanayotolewa na  Jumuiya ya Kimataifa ya Maji (IWA) wakifuatilia mafunzo.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa Mpango wa Usalama wa Maji yanayotolewa na  Jumuiya ya Kimataifa ya Maji (IWA) wakimsikiliza Mkufunzi Kizito Masinde (hayupo pichani).

Washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa Mpango wa Usalama wa Maji yanayotolewa na  Jumuiya ya Kimataifa ya Maji (IWA) katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jijini Mwanza (MWAUWASA), Mhandisi Anthony Sanga (mbele katikati)  mara baada ya ufunguzi wa mafunzo.


Watumishi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jijini Mwanza (MWAUWASA) wametakiwa kuzingatia  Mpango wa Usalama wa Maji kila wanapotekeleza shughuli zao ili kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama kwa ubora unaotakiwa.

Wito huo umetolewa Novemba 12, 2018 na Mkurugenzi Mtendaji wa MWAUWASA, Mhandisi Anthony Sanga wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uandaaji wa Mpango wa Usalama wa Maji yanayotolewa kwa wafanyakazi wa MWAUWASA na  Jumuiya ya Kimataifa ya Maji (IWA). 

Mhandisi Sanga alisisitiza umakini kwenye usimamizi wa mnyororo mzima wa utoaji huduma ya maji kuanzia kwenye chanzo, uzalishaji hadi yanapomfikia mtumiaji ambapo alisema ni wajibu wa kila mtumishi kuhakikisha maji yanayozalishwa yana ubora unaokubalika Kitaifa na Kimataifa.

Aliongeza kuwa suala la usalama wa maji ni nyeti na linapaswa kupewa kipaumbele cha kipekee na kila mtumishi ili kutimiza wajibu wa kuwapatia wananchi huduma wanayostahili kupata.

"Watumishi mliopata nafasi ya kuhudhuria mafunzo haya, mkitoka hapa hakikisheni mnawaelimisha na wale ambao hawakufanikiwa kushiriki," alisema Mhandisi Sanga.

Aliwataka waliohudhuria mafunzo hayo kuuliza maswali na kufuatilia kwa umakini ili mara baada ya mafunzo hayo waboreshe Mpango wa Usalama wa Maji uliopo.

Mafunzo hayo ya siku Tano yameanza Tarehe 12 na yatamalizika Tarehe 16 Novemba, 2018 lengo likiwa ni kuwawezesha wataalam wa Mamlaka kuhakikisha ubora wa maji wanayosambaza kwa wananchi kuanzia mahala yanapozalishwa hadi yanapofika kwa mtumiaji.

Kwa mujibu wa Mkufunzi kutoka IWA, Bwana Kizito Masinde alisema MWAUWASA ndiyo Mamlaka pekee miongoni mwa Mamlaka za Maji Nchini ambayo imepewa kipaumbele cha mafunzo hayo.

Kizito aliongeza kwamba matarajio ya IWA ni kuona wataalam wa MWAUWASA wakitoa mafunzo ya namna hiyo kwa Mamlaka zingine kote nchini.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.