Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi Angelina Mabula akikabidhi hati za kimira kwa wananchi wa kijiji cha Lupembelwasenga Wilaya ya Iringa Vijijini mkoani Iringa
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi Angelina Mabula akiwa na mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela,mbunge wa viti maalum mkoa wa Iringa kupitia chama cha mapinduzi CCM Ritta Kabati pamoja na viongozi wa LTA wakati wa ugawaji wa hati za kimila
Wananchi 2,587 wa kijiji cha
Lupembelwasenga Wilaya ya Iringa Vijijini wamekabidhiwa Hati za Hakimiliki ya
Kimila chini ya Mradi wa LTA Uliofadhiliwa na wadau kutoka Marekani wa Feed the
Future USAID.
Akizungumza wakati wa kukabidhi Hati hizo Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na
Makazi Angelina Mabula alisema kuwa katika miaka miwili ya utekelezaji,Mradi
huo umeweza kutoa jumla ya Hati za Hakimiliki ya Kimila 35,286 katika vijiji
26.
Mabula alisema kuwa hati hizo zitawasaidia kutenga maeneo kwa ajili ya matumizi
mbalimbali kwa kuzingatia uwezo wa ardhi kuhimili idadi hiyo na kasi ya
ongezeko la watu na mifugo kwa miaka mingi ijayo.
Mabula aliongezea kuwa,hatua hiyo itasaidia kupunguza migogoro ya ardhi
kwa kuimarisha usalama wa miliki za ardhi na kuongeza thamani ambayo
itawawezesha hata kukopesheka katika taasisi za kifedha zikiwemo benki.
“Usajili wa
ardhi ni muhimu kwasababu unaongeza ulinzi wa umiliki wa ardhi, unawezesha
uwekezaji, unaongeza thamani ya ardhi na unapunguza migogoro ya ardhi,” alisema Mabula
Mabula aliupongeza mpango huo akisema utasaidia kupunguza eneo kubwa la ardhi
ya Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ambayo haijapimwa.
Aidha Mabula aliwaomba Feed The Future wautanue mradi huo angalau
ufike umalize kupima vijiji vyote vya Halmashauri ya Wilaya ya
Iringa huku akivikumbusha vijiji vyote vya wilaya hiyo kuendelea
kutoa ushirikiano kwenye miradi ambayo inasaidia kukuza maendeleo ya
nchi.
“Tunataka
katika kipindi ambacho Mradi wa Urasimishaji Ardhi (LTA) unaofanywa chini ya
mpango wa Feed The Future kwa ufadhili wa Shirika la Misaada la Marekani
(USAID) tuhakikishe tunapima ardhi na mipango ya matumizi bora na ipimwe ili
kila mwenye kipande chake cha ardhi awe na hati yake,” alisema Mabula.
Alisema kwa
kupitia sera hiyo, kutakuwa na usimamizi zaidi wa ulinzi wa ardhi ya watu
masikini ili kupunguza uporaji wa rasilimali hiyo unaofanywa na matajiri.
“Marekebisho
ya sera hiyo ya ardhi yatawezesha pia kufanyika kwa mrekebisho ya sheria
mbalimbali za ardhi ili ziendane na sera na mazingira ya sasa,” alisema Mabula.
Mabula aliwataka wanakijiji wa kijiji hicho ambao hawajapimiwa maeneo yao kwa
sababu mbalimbali ikiwemo ubishi na migogoro ya kifamilia kutumia vizuri muda
ambao bado mradi huo upo katika wilaya hiyo na kuhakikisha nao wananufaika na
zoezi hilo.
Wanakijiji ambao hawajapimiwa maeneo yao wanaweza kuendeleoa kuzalisha
migogoro ambayo haina tija kwa maendeleo yao na kusababisha waendelee kuwa
masikini kwa kuwa hawatakuwa na dhamana ya kwenda kukopa
Mabula alimalizia kwa kuwataka wananchi wote waliopokea Haki hizo
kutambua na kuheshimu wajibu wao kwa jamii na Taifa kwa ujumla katika matumizi
na usimamizi mzuri wa Ardhi.
Naye Naibu Mkurugenzi wa Mradi huo Ndugu Malaki Msigwa alisema kuwa
mradi huo umefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa kutoa Hati kwa usawa Wanawake na
Wanaume.
Msigwa aliwapongeza wataalamu wa mradi huo kwa kuhakikisha wanawasaidia
wananchi wa kijiji cha Lupembelwasenga kupima maeneo
yao na kupata hati miliki za kimila ambazo zitakuwa msaada mkubwa kwenye
maendeleo ya kiuchumi.
“Baadhi ya miradi imeibuliwa wakati wa upimaji wa ardhi hivyo ni fursa
sasa kwa wananchi wenyewe kuitumia vizuri ardhi waliyopimiwa na kupewa hati
miliki za kimila na kwa kuwa asilimia fulani kijiji hiki kimepimwa hivyo
wanaweza kuwa kijiji cha mfano kwa kuwapa maendeleo hata wawekezaji wazuri kwa
faida yao” alisema Msigwa
Msigwa alisema kati ya vijiji hivyo 41 vitakavyotayarishiwa mipango ya
matumizi bora ya ardhi na kila mwenye ardhi kupimiwa na kupewa hati miliki za
kimila, vijiji 36 vipo wilayani Iringa na vitano vipo wilayani Mbeya.
“Baada ya kukamilisha zoezi la upimaji mashamba na urasimishaji wa
kijiji chote cha Lupembelwasenga, hivi sasa
mradi unaendelea na upimaji mashamba katika vijiji vya mradi ambavyo vipo
wilayani Iringa” alisema Msigwa
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa,
Robert Masunya aliupongeza Mradi wa Urasimishaji
Ardhi (LTA) unaofanywa chini ya mpango wa Feed The Future kwa ufadhili wa
Shirika la Misaada la Marekani (USAID) kwa kuzingatia jinsia wakati walipokuwa
wanaendesha zoezi la upimaji ardhi katika kijiji hicho.
“Hongera sana LTA kwa kuwapa elimu wanawake na wanaume na kuhakikisha
kuwa wanapa haki zao sawa bila kuwa na mgogoro wowote tofauti na ilivyokuwa
hapo awali,maana miaka ya nyuma mwanamke alikuwa anabaguliwa kwenye kila kitu
wala alikuwa haruhusiwi hata kumili ardhi” alisema Masunya
Masunya aliongeza kwa kusema kuwa wanakijiji wa kijiji cha Mlanda baada
ya kupata elimu ya kumiliki ardhi kumepunguza sana migogoro ambayo ilikuwa
inaleta chuki kwenye familia.
“Kwa sasa ardhi ya kijiji hiki imepanda dhamani kwa kiasi kikubwa na
tayari ishapimwa na mmepata hati miliki za kimila ambazo zitawasaidia katika
maendeleo yenu ya kiuchumi” alisema Masunya
Akitoa shukrani kwa niaba ya wananchi wa Lupembelwasenga Mshauri wa
Kijiji Ndugu Titus Maketta ameshukuru Msaada wa Marekani uliofadhili Mradi wa
urasimishaji wa Ardhi LTA kwa kuwawezesha kupata Hati za Hakimiliki za kimila
zitakazowaondolea migogoro ya Ardhi.
Zoezi la ugawaji wa Hati za Hakimiliki ya Kimila Kijiji cha
Lupembelwasenga umeambatana na Naibu waziri Mhe. ANGELINA MABULA kufungua
Masjala ya Ardhi Kijijini hapo.
Tupe maoni yako
0 comments:
Post a Comment
Note: Only a member of this blog may post a comment.