ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, July 25, 2018

ZANTEL YAINGIA MAKUBALIANO NA MABENKI 9 KUWEZESHA EZYPESA KUFANYA MIAMALA YA KIBENKI

 Mkuu wa Zantel Zanzibar, Mohamed Khamis Baucha mkutano na waandishi wa habari  (hawapo pichani) mjini Zanzibar kwenye hafla hiyo. Kushoto ni Meneja wa Huduma za wateja wa NMB, Salim Kimweri, Mkuu wa Kitengo cha masoko, Abdalla Jabir wa benki ya watu wa Zanzibar na Mkuu wa masoko na mawasiliano wa Zantel, Sakyi Opoku (kulia). Picha zote na Cathbert Kajuna - Kajunason/MMG, Zanzibar.
 Baadhi ya waandishi wa habari wa habari na wageni waalikwa wakifuatilia matukio.
Picha ya pamoja ya Maofisa wa Zantel na baadhi ya wafanyakazi wa mabenki  mara baada ya kumalizika kwa hafla hiyo.

Na Cathbert Kajuna - Kajunason/MMG, Zanzibar.

Kampuni ya mawasiliano ya Zantel imeingia makubaliano na mabenki tisa nchini kuwawezesha watumiaji wa huduma yake ya fedha ya Ezypesa, kufanya miamala ya kibenki kupitia simu zao za mikononi wakiwa mahali popote nchini Tanzania.

Mabenki hayo ni; Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) ya Zanzibar, NBC, NMB, Barclays, Amana Bank, Equity Bank, Access Bank, Exim Bank na BOA.

Hatua hii ni mapinduzi makubwa kwa matumizi ya teknolojia kurahisisha huduma za kifedha nchini, hivyo Zantel imejipanga kuhakikisha wateja wake hawaachwi nyuma katika mapinduzi haya na imejipanga kuhakikisha wateja wake wanafanya miamala yao ya kibenki kirahisi na kw usalama.

Akiongea kwenye mkutano na waandishi wa habari mjini Zanzibar, Mkuu wa Zantel Zanzibar, Mohammed Khamis Mussa (Baucha) alisema kampuni ya Zantel kwa muda mrefu imekuwa ikifanyia kazi suala hili la kushirikiana na mabenki ili kuhakikisha huduma ya Ezypesa inaenda sambamba na maendeleo ya kiteknolojia ya kufanya miamala kwa njia ya simu na kimtandao.

“Katika mchakato wa kushirikiana na mabenki kutoa huduma za kifedha, mwanzoni tulianza kushirikiana na Benki ya Watu wa Zanzibar pekee lakini baadaye tukaona kuna umuhimu kuingia makubaliano na mabenki mengine 8 ili kuwawezesha wateja wetu kufanya miamala ya kifedha kwa urahisi na bila mipaka,” alisema Baucha.

Baucha alisema Zantel, imejipanga kuleta mapinduzi ya teknolojia kupitia simu za mkononi kuwarahishia maisha wateja wake ambapo mbali na huduma za kibenki, watumiaji wa Ezypesa vilevile wanaweza kufanya malipo kwa taasisi mbalimbali za serikali ya mapinduzi ya Zanzibar na serikali ya Muungano wakati wowote.

“Ili kufanya malipo ya kiserikali mteja ataingia kwenye menu ya Ezypesa kwa kubonyeza *150*02#, halafu atachagua namba 8 itakayomuweza kuchagua kati ya Zan e-pay (kwa malipo ya serikali ya mapinduzi ya Zanzibar) au UnionGov e-epay (kwa Tanzania bara),” alisema Baucha.

Baadhi ya malipo ya kiserikali yanayoweza kufanyika kupitia EzyPesa ni faini zinazotozwa na Polisi, malipo ya tozo za uhamiaji na malipo kwenye Wizara mbalimbali kwa mujibu wa sheria za nchi.

Akiongea kwa niaba ya taasisi za fedha zilizoingia makubaliano na Zantel,Bw. Salim Kimweri,ambaye ni Meneja wa Huduma za wateja wa NMB, alipongeza ushirikiano huo  na kuongeza kuwa utawarahishia wananchi huduma za kibenki na kuleta mapinduzi ya huduma za kifedha nchini.

Katika mkakati wa kuboresha huduma zake nchini, hivi karibuni Zantel iliwekeza katika kuimarisha mtandao wake wa huduma za mawasiliano ya intaneti nchini na kuzindua kampeni ya “Tunaliamsha Kivingine” inayowezesha wateja wake kupata intaneti yenye kasi kubwa na kwa gharama nafuu.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.