ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, May 3, 2018

JAFO ATUA IRINGA NA KUTOA AHADI HII KWA SHULE YA WASICHANA.



Serikali yaahidi kuikarabati Sekondari ya Wasichana Iringa
Na Atley Kuni      OR TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo ameahidi kuwa shule ya sekondari ya Wasichana Iringa iliyopo mkoani Iringa itafanyiwa ukarabati ikiwa ni muendelezo wa serikali katika kuzikarabati shule zake kongwe hapa nchini.
Waziri Jafo alitoa kauli hiyo jana wakati akiwa njiani kurudi Dodoma akitokea mkoani Iringa ambapo pamoja na kuhudhuria sherehe za Mei Mosi alihudhuria pia ufunguzi wa hospitali ya Wilaya ya Kilolo.
Ilimlazimu Waziri Jafo kufanya ziara ya kushtukiza shuleni hapo, ili aweze kujionea miundombinu mbalimbali katika shule hiyo iliyo anzishwa toka mwaka 1967.
Akizungumza na walimu, watumishi wasio walimu pamoja na wanafunzi wa shule hiyo mara baada ya kujionea hali ya miundombinu ya shule hiyo, Mhe. Jafo alieleza kuwa shule hiyo ni miongoni mwa shule kongwe zilizo kwenye mpango wa ukarabati mkubwa ili kuwa na mazingira bora ya kusoma na kujifunzia.
“Katika mwaka wa fedha wa 2017/18 tulikarabati shule kongwe 43 na katika mwaka huu wa 2018/19, shule hii pamoja na zingine kongwe 45 hapa nchini zitakuwa katika mpango kamambe wa kukarabatiwa kama tulivyokwisha fanya kwenye shule kama 43 za awali ambapo shule 89 zote kongwe tuwe tumezimaliza” alisema Waziri Jafo.
Aliongeza kuwa shule ya Wasichana Iringa imekuwa ni moja ya shule bora na hivyo kufanya wanafunzi wengi kupenda kuhamia kwenye shule hiyo.
Sambamba na ukarabati huo Mhe. Jafo ameahidi kuzifanyia kazi changamoto zote ambazo ziliainishwa mbele yake ikiwepo upungufu wa walimu wa Fizikia na Hisabati pamoja na stahiki za walimu.
“Mama yetu Nkondola amewasilisha changamoto za walimu wa Hesabu na Fizikia lakini pia maslahi ya walimu, naomba nieleze kuwa suala hilo nimelichukua lakini niwaahidi kutuma wataalam kutoka kwenye wizara yangu pamoja na wizara nyingine za kisekta kuja kufanya tathmini ya kina juu ya haya mliyoniambia,” alisema waziri Jafo.
Aliwataka wanafunzi hao kusoma kwa bidii huku akitoa ahadi  kwa jumuiya hiyo kuwa endapo katika mitihani yao ya mwisho ya kidato cha sita watapata daraja la kwanza (DV.1) zaidi wanafunzi ya 30 atawandalia sherehe ndogo ya kujipongeza na wale watakaopata daraja la kwanza kati ya pointi 3-5 wataalikwa bungeni kwa gharama zake yeye Mhe.Jafo.
Mhe. Jafo akiwa katika ziara hiyo, alikagua miundombinu ya shule ikiwapo Mabweni, Vyoo, Bwalo la Chakula, Jiko na Ofisi za Walimu na kisha kufanya mazungumzo na walimu, watumishi wasio walimu wanafunzi sambamba na wananchi wanaozunguka eneo la shule hiyo. 
Huo umekuwa ni utamaduni wa kiongozi huyo mwenye dhamana na OR TAMISEMI kila anapopata fursa kutembelea mikoani kutembelea shughuli za maendeleo kwa wananchi na sekta zote ili kujionea maendeleo ya watu na shughuli zao.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.