ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, December 16, 2016

MWENYE NYUMBA WA MSAIDIZI WA MBOWE AELEZA ILIVYOKUWA.

Dar es Salaam. Mmiliki wa nyumba anayoishi kada wa Chadema, Ben Saanane aliyepotea katika mazingira ya kutatanisha mwezi mmoja uliopita, Evance Mrosso amesema waligundua kuwa amepotea baada ya siku nne kupita bila kuonekana.
Mrosso aliyekuwa akiishi na Saanane maeneo ya Tabata Dampo, jana alifunguka kuwa haikuwa kawaida yake kukaa kimya kwa muda mrefu kwani ni mtu wa mawasiliano kwa ndugu zake, marafiki na majirani.

“Saanane ni mtu wa kutoka asubuhi na kurudi usiku na inaweza ikapita siku mbili tusionane kutokana na mwingiliano wa shughuli zangu na zake, lakini tunawasiliana kwa simu, ” alisema Mrosso.

Hata hivyo, Mrosso alisema hali ilikuwa tofauti baada ya kupita siku hizo nne ndipo aliamua kuwauliza jirani zake kama wamemuona na walimjibu kuwa hawajamwona.

“Nimeishi na Saanane kwa muda wa miaka mitano.Mara ya mwisho tulionana na kuwasiliana Novemba 12, wakati wenzangu tunaoishi nao walimuona kuanzia tarehe hiyo hadi 14, hata wao walishangaa kutomuona kwa sababu siyo kawaida yake,” alidai Mrosso.

Alisema baada ya kujibiwa hivyo, alichukua uamuzi wa kumtafuta kumpigia simu katika namba zake mbili alizokuwa akitumia lakini hazikupatikana.

Alisema baadaye aliamua kumpigia simu mmoja wa dada zake anayeishi Mbeya ili kumweleza suala hilo na kama aliwasiliana naye hivi karibuni.

“Dada yake akaniambia hawajawasiliana na Saanane kwa muda sasa. Hivyo alinishauri nitoea taarifa polisi. Lakini kabla ya kwenda polisi, nilienda ofisini kwake Chadema (Kinondoni) kumuulizia, nilimkuta mlinzi akanieleza kuwa hajaonekana kwa siku kadhaa ofisini hapo,” alidai Mrosso.

Juzi, Mwanasheria wa Chadema, Tundu lissu aliitaka Serikali kueleza kama inamshikilia kada huyo ambaye alikuwa msaidizi wa Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe.

Sanjari na hilo, Lissu aliitaka Serikali kufuatilia ujumbe wa vitisho aliowahi kutumiwa Saanane kupitia simu yake ya mkononi na mtu ambaye bado hajafahamika.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala, Salum Hamduni alisema polisi bado inaendelea na upelelezi.

“Taarifa zilizopo ni za kipelelezi hatuwezi tukaziweka hadharani, wakati uchunguzi wa tukio hili ukiendelea,” alisema Kamanda Hamduni.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.