ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, October 15, 2016

KONGAMANO LA KUMUENZI MWALIMU J.K NYERERE LAFANYIKA WILAYANI IKUNGI

  Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akiwa amembeba mmoja ya mwanafunzi wa shule ya Msingi Ikungi mchanganyiko
 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akikabidhi mahitaji kwa wanafunzi walemavu mara baada ya kuwasili shule ya msingi Ikungi mchanganyiko
 Baadhiya washiriki wa Kongamano wakisikiliza kwa makini mada zikiwasilishwa kwenye mdahalo

 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akiwa na baadhi ya viongozi wa ngazi ya Wilaya wakati kongamano likiendelea

 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akimsalimu Bi Fumbo Shishiwa aliyejifungua salama mtoto wa kiume na kumuita Magufuli
 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akisalimiana na wanafunzi wenye ulemavu katika shule ya msingi Ikungi mchanganyiko
 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akishiriki kuandaa bustani kwa ajili ya mbogamboga zitakazotumiwa na wanafunzi wa shule ya msingi Ikungi mchanganyiko
Katibu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Ikungi akichangia mada iiliyokuwa inajadiliwa kwenye Kongamano la Kumuenzi Mwalimu J.K Nyerere kwenye Ukumbi wa Shule ya Sekondari Ikungi
 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akisalimia na Bi Faidha Athumani mara baada ya kumkuta akisubiri matibabu katika Kituo cha afya Ikungi
 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akishiriki kuandaa bustani kwa ajili ya mbogamboga zitakazotumiwa na wanafunzi wa shule ya msingi Ikungi mchanganyiko
 Baadhi ya washiriki wakifatilia kwa makini Kongamano

 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akikagua Chumba cha kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya Ikungi

 Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akikagua Mashine ya vipimo vya magonjwa mbalimbali ikiwemo ini katika kituo cha afya Ikungi
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akimuelekeza Mganga Mkuu wa kituo cha Afya Ikungi kuhakikisha anasimamia ujenzi wa upanuzi wa chumba cha kuhifadhia maiti


Na Mathias Canal, Singida

Uongozi wa Wilaya ya Ikungi Mkoani Singida umeungana na Watanzania kote ulimwenguni kuadhimisha kumbukizi ya miaka 17 ya kifo cha Mwasisi wa Taifa na Rais wa Kwanza wa Tanzania hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyefariki dunia Octoba 14, 1999 katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas huko Uingereza.

Katika Kongamano hilo lililofanyika katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Ikungi limejumuisha Viongozi wa kada tofauti wakiwemo viongozi wa serikali, Viongozi wa Dini, Viongozi wa Vitongoji na vijiji, Viongozi wa siasa, Wazee wa mji wa Ikungi, Maafisa Tarafa na Watendaji, Madiwani, Walimu na wanafunzi ambapo wote kwa pamoja wamepata nafasi ya kuchangia mada na kupitisha maadhimio zaidi ya kumi na tano yatakayotoa taswira ya namna ya kumuenzi Mwalimu Nyerere mwakani.

Mgeni rasmi katika Kongamano hilo Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu amewasihi wananchi kwa umoja wao kumuenzi Mwalimu Nyerere katika matendo makubwa na muhimu aliyokuwa anayafanya hususani misingi ya Haki, Ukweli na uwajibikaji.

Amewataka watanzania kuishi katika matakwa ya Mwalimu Nyerere ikiwa ni pamoja na kutokubali kutoa na kupokea Rushwa kwani hayo ni miongoni mwa mambo mengi aliyoyahubiri wakati akiwa waziri Mkuu kabla ya kujiuzulu nafasi hiyo na hatimaye kuyahubiri na kuyaishi kipindi akiwa Rais wa kwanza wa Tanzania.

Dc Mtaturu alisema kuwa Tanganyika wakati wa uhuru ilikuwa na changamoto mbalimbali ikiwemo maradhi yatokanayo na magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza, Pia kulikuwa na ujinga uliosababishwa na ukosefu wa elimu bora kwa kiasi kikubwa kwani watanganyika wasiojua kusoma, kuandika na kuhesabu walikuwa ni zaidi ya asilimia 90.

Alisema kuwa sambamba na hayo pia kulikuwa na umasikini mkubwa na uliokithiri kwani asilimia kubwa ya watanzania walikosa mahitaji ya msingi kama vile malazi, Chakula, na Mavazi ambapo Mwalimu Nyerere alifanikiwa kupingana na maadui hao watatu kwa kuongeza udahili kwa kiasi kikubwa katika shule muhimu za Sekondari Kilakala, Kibaha na Mzumbe.

Mtaturu alisema kuwa pia Mwalimu Nyerere alitaifisha taasisi zote za watu binafsi ili kuleta usawa katika jamii pamoja na kuimarisha upatikanaji mzuri wa huduma za afya katika zahanati,  vituo vya afya, na Hospitali ili kuboresha afya za watanzania na kuwafanya kuweza kufanya kazi vizuri na kwa ufasaha.

Dc Mtaturu Amewataka washiri wote wa Kongamano hilo na watanzania kwa ujumla kuendelea kuwa viungo muhimu katika kudumisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Kudumisha Lugha ya Kiswahili, Kukuza Utu na uadilifu katika kazi na jamii inayotuzunguka.

Zaidi amesisitiza wakulima kwa kushirikiana na maafisa kilimo kulima kilimo chenye tija ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ili kuhakikisha wanakuwa na mavuno mengi yenye faida kubwa na kuwaongeza uchumi wao kwani wastani wa pato la Mtanzania aishie Wilaya ya Ikungi ni shilingi elfu mbili kwa siku ambapo kwa mwezi ni shilingi elfu sitini.

Hata hivyo Dc Mtaturu amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa vitendo hususani kusimamia vyema mapato ya serikali, Kupambana katika misingi ya utu, haki na usawa kwa kila Raia wa nchi hii, Kupinga Rushwa na matumizi mabaya ya fedha za Umma.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Tawala wa Wilaya ya Ikungi Ndg Dandala Mzunguor ameyataja baadhi ya maadhimio yaliyojadiliwa katika kongamano hilo kuwa ni pamoja na Kupata viongozi wa Haki na halali katika chaguzi zetu, Jamii kuwa na moyo wa uzalendo na kujitolea katika kufanya kazi.

Mengine ni kuepuka kejeli na dharau katika maisha ya kila siku, Kuboresha mazingira ya kufundishia, Jamii na viongozi kuweka miiko ya uongozi, Kudumisha umoja na mshikamano wa Taifa letu.

Naye katibu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Ikungi Aluu Segamba amempongeza Mkuu huyo wa Wilaya kwa kuamua kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa kufanya kongamano kwani imekuwa taswira njema kwa wakazi wa Wilaya hiyo ambao hawajawahi kushiriki katika kongamano kama hilo tangu kuanzishwa kwa Wilaya hiyo.

Baadhi ya wachangiaji katika kongamano hilo la kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wamependekeza kuwa na siku moja ambayo Mkuu wa Wilaya atakutana na wananchi wote kwa ajili ya kujadili kwa pamoja namna ya kuiboresha Wilaya hiyo ikiwa ni pamoja na shughuli za kijamii hususani kuboresha kilimo, Uchumi na Miundombinu.

Wengine wamependekeza bendera kupeperushwa nusu mlingoti ni kuenzi na kutoa heshima kubwa kwa Baba wa Taifa kwani kufanya hivyo itakuwa njia sahihi ya kuongeza uwajibikaji na nidhamu ya Taifa.

Kabla ya Kongamano hilo mkuu huyo wa Wilaya ya Ikungi akishirikiana na viongozi wote wa Wilaya pamoja na kamati ya ulinzi na usalama alitembelea Shule ya Msingi mchanganyiko Ikungi ili kutoa baadhi ya mahitaji kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu wakiwemo Wenye ulemavu wa ngozi, Walemavu mchanganyiko na wasioona.

Sambamba na hayo pia amewatembelea wagonjwa katika Kituo cha afya Ikungi kwa kuzuru katika wodi za wanawake waliojifungua, sambamba na Wodi ya wanaume na Wanawake.

Dc Mtaturu amemuagiza mganga Mkuu wa Zahanati hiyo kuhakikisha anafanya utaratibu wa kujenga Sehemu ya kuhifadhia maiti kutoka na sehemu iliyopo kuzidiwa kwani ina sehemu mbili tu za kuhifadhia maiti.

Aidha Dc Mtaturu alipotembelea kituo cha Afya cha Ikungi alipitia maagizo yake aliyowahi kuyatoa hivi karibuni ya kupanua chumba cha maabara na kuagiza kutengenezwa kwa mashine ya kupimia magonjwa mbalimbali ndani ya muda mfupi ili kuboresha huduma ya afya kwa wananchi wanaotumia kituo hicho kwa ajili matibabu.

Akifunga Kongamano hilo Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu amesisitiza kuwa katika kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni lazima kuhakikisha huduma za Afya, Elimu, Uchumi, Kilimo na Miundombinu zinaboreshwa.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.