ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, February 22, 2024

COREFA KIBAFA YAMFAGILIA MBUNGE KOKA KUSAPOTI MASHINDANO YA KIBAFA VIJANA CUP

 


NA VICTOR MASANGU,KIBAHA 

Uongozi wa chama cha soka Mkoa wa Pwani (COREFA) pamoja na chama cha soka Wilaya ya Kibaha (KIBAFA) umempongeza Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka kwa kuamua kujitoa kwa hali na mali   kusapoti sekta ya michezo hasa kwa vijana.

Akizungungumza wakati wa halfa ya kufunga rasmi mashindano ya Kibafa Vijana Cup chini ya umri wa miaka 25,Makamu Mwenyekiti wa Corefa Mohamed Lacha alisema kwamba mbunge Koka ameweza kusapoti michuano hiyo kwa asilimia mia moja.

Lacha alisema kwamba amefarijika sana kuona sapoti kubwa ambayo ameweza kuitoa mbunge huyo kwa lengo la kuweza kufanikisha mashindano hayo ya vijana yaweze kufanyika na kwamba yamefanikiwa.

"Kwa kweli mimi kwa nafasi yangu kama Makamu mwenyekiti wa Corefa nipende kwa dhati kabisa kumshukuru Mbunge wa Jimbo la kibaha kwa kutoa fedha kwa ajili ya kudhamini mashindano haya,"alisema Lacha
Kadhalika aliongeza kuwa kauli mbiu yao kubwa ni kwamba  mpira lazima uchezwe katika Mkoa wa Pwani kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wa mchezo wa soka.

"Tunashukuru mashindano haya yamemalizika salama na timu zote zimeweza kupatiwa zawadi zao ambazo zimetolewa na mdhamini mkuu ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka,"alifafanua Lacha.

Kwa upande wake .mjumbe wa kamati ya utekelezaji ya chama cha soka Wilaya ya Kibaha (KIBAFA) Jeremia Komba alisema kwamba Mbunge huyo amekuwa mstari wa mbele katika kushiriki kikamilifu katika kusaidia sekta ya michezo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji Kibaha Mussa Ndomba aliwataka viongozi wa vyama soka kuendelea kumpa sapoti Mbunge huyo kwani ameweza kutumia zaidi ya milioni sita katika kudhamini michuano hiyo.

Pia na sisi kama halmashauri tumejipanga vilivyo katika kutenga maeneo ya viwanja kwa michezo ili kuweza kutoa fursa zaidi ya vijana kupata ajira kupitia michezo.

Nao baadhi ya wachezaji na wadau wa mchezo wa kabumbu walisema jambo ambalo amelifanya Mbunge Koka la kudhamini michuano hiyo kwa asilimia 100 linatia moyo katika nyanja ya kukuza mchezo wa soka  hasa kwa vijana.

Waliongeza kuwa kitendo ambacho amekifanya Mbunge Koka cha kuziwezesha timu 16 kwa kuzipatia jezi  pamoja na mipira ikiwemo na kutoa zawadi kwa washindi watatu kimewapa faraja sana katika medani ya soka.

Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka amekuwa ni nguzo kubwa ya kuwasaidia vijana katika kuibua na kukuza vipaji walivyonavyo ambapo safari hii amekuwa mdhamini mkuu wa michuano ya Kibafa vijana Cup kwa asilimia mia moja.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.