ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, May 8, 2023

POLISI: HAKUNA MTOTO ALIYEFUFUKA, WAZAZI WALITAKA KUMUIBA.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa

"Hakuna mtoto aliyefufuka" ndiyo kauli aliyoitumia Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mutafungwa kuelezea majibu ya uchunguzi wa tukio la mtoto, Mabirika Wilson (8) kudaiwa kufariki, kuzikwa kisha kuonekana akizurura kwenye majaruba yaliyoko kijiji cha Mwangika Wilaya ya Kwimba mkoani humo. 

Mtoto huyo ambaye ni Mkazi wa Kijiji cha Salong'we Wilaya ya Magu mkoani Mwanza alifariki Aprili 16 mwaka huu nyumbani kwao baada ya kuugua maradhi yanayodhaniwa kuwa ni homa na kuzikwa nyumbani kwao Aprili 17 mwaka huu.

Siku 13 baada ya maziko ya mtoto huyo, Jeshi la Polisi mkoani humo lilitoa taarifa ya kuibuka sintofahamu kuhusu kifo cha mtoto huyo kufuatia wazazi wa Mabirika, Wilson Bulabo (35) na Helena Robert (32) kudai kwamba mtoto aliyeokotwa ni wao jambo lililoibua taharuki na kuwalazimu polisi kufukua kaburi ili kuchukua sampuli kwa ajili ya kipimo cha Vinasaba (DNA).

Akizungumza na Waandishi wa habari leo Jumamosi Mei 5, 2023 Kamanda Mutafungwa amesema uchunguzi wa awali wa vinasaba uliofanyika kwa watu wanne wakiwemo wazazi, babu wa marehemu na mtoto aliyeokotwa umeonyesha wazazi hao wa marehemu Mabirika hawana Unasaba (uhusiano) na mtoto aliyeokotwa katika kijiji cha Mwangika bali wazazi hao walitaka kumuiba. 

"Uchunguzi wa Vinasaba tulioufanya kwa mtoto aliyeokotwa tumebaini siyo mtoto wa wazazi hao badala yake mtoto wao ni aliyefariki. Hivyo, tunawashikilia wazazi hao ambao walidanganya na kuzua taharuki kuwa mtoto aliyeokotwa ni wa kwao amefufuka tukikamilisha uchunguzi tutawafikisha Mahakamani kwa tuhuma za kuibua taharuki na kutaka kuiba mtoto," amesema Mutafungwa

Kuhusu mtoto aliyeokotwa, Mutafungwa amesema baada ya kumfanyia mahojiano chini ya usimamizi wa Ofisi ya Ustawi wa Jamii amejitambulisha kwa jina moja la Mussa (8) huku akiwaomba wazazi ambao mtoto wao amepotea kufika Kituo Kikuu cha Polisi mkoani humo kwa ajili ya kumtambua mtoto huyo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Salong'we, Geremanus Masala amewataka wakazi wa mkoa huo kuacha kuzusha taarifa za imani potofu na kishirikina kuwa mtu akifa anaweza kufufuka jambo linaloweza kuzua taharuki kwa Umma.

"Nitawafikishia ujumbe wakazi wa kijiji changu cha Salong'we kuachana na imani potofu, watambue kuwa mtoto huyu siyo aliyefariki na pia tunaenda kukemea imani potofu," amesema Masala

Mtoto huyo ambaye aliokotwa anaendelea kuwa chini ya uangalizi wa Jeshi la Polisi na Ofisi ya Ustawi wa Jamii mkoani Mwanza wakati akisubiria utambuzi wa wazazi ama ndugu zake kujitokeza.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.