ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, April 25, 2023

'ENERGY DRINKS' TISHIO KWA AFYA


Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), imetoa angalizo kwa wale wanaopenda kutumia vinywaji vya kuongeza nguvu mwilini maarufu 'Energy drinks'.

Imesema katika utafiti wake mpya umebaini unywaji wa vinywaji hivyo kwa wingi unaweza kuleta madhara kwenye mishipa ya moyo ya kuziba ghafla na hata kusababisha vifo vya ghafla.

Hivyo, imeonya kuwa mtu asinywe zaidi ya kopo moja lenye ujazo wa mililita 250 ndani ya saa 24, huku ikisisitiza kama kuna uwezekano wa kuviepuka, ifanyike hivyo kulinda afya ya mhusika.

Baadhi ya vinywaji hivyo ndani yake kuna maji, sukari, ladha, caffein, mitishamba, tauline (amino acid), protini, vitamini, madini. Inaelezwa kuwa caffeine pamoja na mambo mengine, inafanya kazi ya kuzuia uzalishwaji wa kichocheo cha mwili kinachohusika na kulala ama kuhisi uchovu.

Utafiti huo wa kisayansi umehusisha unywaji wake na matatizo ya moyo na mishipa kuziba ghafla inayowakumba watu wa rika zote wanaovitumia hivi sasa.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na Mkuu wa Kitengo cha Utafiti na Mafunzo JKCI, Pedro Palangyo alisema utafiti huo uliochapishwa juzi katika jarida moja maarufu la kisayansi nchini Marekani, unamhusisha kijana wa Kitanzania ambaye mshipa wake mkubwa wa moyo uliziba ghafla.

Hata hivyo, alisema miezi ya hivi karibuni JKCI imekuwa ikipokea vijana wengi hospitalini hapo wanaofika kutibiwa wakikabiliwa na changamoto mfanano na hizo, huku wakiwa na historia ya kutumia vinywaji hivyo.

Ongezeko la matumizi

Dk Pedro alisema matumizi ya vinywaji vya kuongeza nguvu yamekuwa makubwa katika jamii na yanaongezeka huku vijana wengi wakivitumia si kwa sababu ya kujipa nguvu, bali kwa kupenda ladha yake.

"Energy drinks husababisha damu kuwa nzito kuliko inavyopaswa na ikiwa nzito inaweza kusababisha damu kuganda kama ilivyokuwa katika kisa hiki, kwa hiyo ni muhimu kuendelea kupaza sauti kwa jamii zetu na kwa wale wanaviotumia ni vizuri wakaacha kabisa," alisema Dk Pedro.

Alisema takwimu za hivi karibuni za taasisi hiyo zinaonyesha wanapata wagonjwa wengi wa mishipa kuziba kwa watu wenye umri mdogo ambao katika hali ya kawaida ya ugonjwa huo umri mdogo ni mtu yeyote chini ya miaka 45.
 

Ukubwa wa tatizo

Wanamichezo, wanafunzi na watu wanaofanyakazi ngumu ndiyo wanaotajwa zaidi kutumia vinywaji hivyo wakiamini huwaondolea usingizi, uchovu na kuwapa nguvu zaidi.

Wapo wanamichezo ambao hutumia saa chache kabla ya kuingia mchezoni au mara baada ya kucheza wakiamini itawafanya kupata nguvu za ziada na kucheza kwa kiwango.

Huku wanafunzi na madereva wakivitumia siku za mitihani ili kuuondoa usingizi na wanywaji wa pombe kali aina ya spiriti na whiskey hutumia kuchanganyia.

Hata hivyo, wataalamu walisema iwapo mwili umechoka na unaulazimisha kwa kutumia visaidizi ina madhara.

"Ni kweli caffein husisimua mfumo wa fahamu na kumfanya mtumiaji kuhisi kuchangamka na kuondoa uchovu. Caffein huainishwa kisayansi kama kundi la opiod yaani dawa ya kulevya aina ya kichangamshi kiwango chake katika vinywaji hivi kinakubalika ni salama kwa matumizi ya binadamu lakini unapoulazimisha mwili unauchosha zaidi na unapozidisha lazima upate madhara na hatushauri kuchanganya na pombe kali ina madhara makubwa," anasema daktari wa bingwa wa magonjwa ya moyo, Enock Erick.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.