ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, September 12, 2018

MACHINGA MJINI BABATI WALIA NA SERIKALI BAADA YA KUTIMULIWA.



Na John Walter-Babati

Halmashauri ya mji wa Babati imeanza zoezi la kuwaondoa Wafanyabiashara wadogo wadogo [Machinga] wanaofanya shughuli zao kwenye maeneo yasiyo rasmi.

Hata hivyo baadhi yao waliozungumza na Muungwana Blog, wamesema kuwa wanafanyia biashara nje ya maeneo rasmi yaliyotengwa kwa biashara kwa sababu ya ukosefu wa wateja hali inayowalazimu kutembeza kuwatafuta mitaani.

Wafanyabiashara hao wamesema baada ya kufukuzwa hawajui waelekee wapi huku wakiomba serikali ya Rais John Magufuli iwasaidie kwani wanadaiwa pesa za mikopo na ndio tegemezi kwenye familia zao.

Baada ya malalamiko ya wafanyabiashara hao kituo hiki kikazungumza na  mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Babati Fortunatus Fwema ambaye amesema wameamua kuwaondoa wafanyabiashara hao baada ya kukiuka agizo lililotolewa muda mrefu kuhamia katika maeneo yaliyotengwa.

Amesema kwamba  wanatekeleza agizo la serikali la kuwatafutia wafanyabiashara maeneo ya biashara lakini cha kushangaza hawataki kuyatumia na badala yake wanapanga bidhaa zao kwenye maeneo ambayo hayajaidhinishwa.

“Ni wajibu wetu kama halmashauri kuhakikisha mji unapangika na katika kutekeleza hilo lazima tuwatafutie wafanyabiashara wanaouza mboga mboga na wengine maeneo maalum ya kufanyia shughuli hizo,na kwa kuzingatia hilo tumejenga soko  darajani  na Silent Inn ambalo limezinduliwa na mbio za mwenge mwaka jana” alisema Fwema.

Mji wa Babati ambapo ndipo makao makuu ya mkoa wa Manyara tangu mwaka 2012, ni moja kati ya miji inayokuwa kwa kasi kubwa ambapo kwa sasa idadi inazidi kuongezeka maradufu tofauti na takwimu za awali za sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 iliyoeleza kuwa kulikuwa na wakazi  wapatao 93,108.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.