ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, September 19, 2023

MAKTABA YABOMOLEWA KUJENGWA MPYA YA KISASA MWANZA NA CHATO


 NA. ALBERT G.SENGO/MWANZA

Huku akionesha na kuelekeza kwa mkono kupitia picha kubwa ya kwenye bango la ukumbi wa mkutano, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Huduma za Maktaba Tanzania (TLSB) Dkt. Mboni A. Ruzegea anasema "Kama umepita sasa hivi eneo ambalo kulikuwa na maktaba ya mkoa wa Mwanza, imebomolewa na ujenzi unaendelea"
"Na hii hapa ndiyo picha ya jinsi jengo litakavyokuwa kwa Maktaba ya Mwanza, pindi litakapokamilika, mnaletewa kitu kizuri sana na Serikali ya awamu ya sita ya Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, kizuri ni kwamba pesa zake zilishaidhinishwa kwenye Bajeti ya 2023-2024" na kisha Dkt Ruzegea akaendelea kwa kusema. "Vilevile tutakuwa na maktaba kumbukumbu ya aliyekuwa Rais wa awamu ya 5 Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ambayo inajengwa pale Chato, maktaba kubwa nzuri ya mfano itakayobeba kumbukumbu zote za viongozi wa nchi yetu" Taarifa hii imetoka leo Septemba 19 katika Kongamano la Tatu la Kitaifa la Huduma za Maktaba, Tamasha la Vitabu na Usomaji, linalofanyika katika Ukumbi wa Mikutano BOT Kapri Point, Jijini Mwanza. Lengo kuu la Kongamano na Tamasha hili ni kutoa fursa kwa wadau wote wa huduma za maktaba nchini kushiriki, kujadili, kuchangia na kuamua kwa pamoja upatikanaji na utumiaji wa huduma bunifu za maktaba na teknolojia za kisasa nchini kunavyosaidia kujenga ari na utamaduni wa kujisomea. Kongamano hili ni la siku 3, hivyo litadumu kuanzia leo 19 hadi 21 mwezi Septemba 2023. Kauli mbiu ya Kongamano hilo kwa mwaka huu 2023 ni 'Waandishi na Wachapishaji Tukutane Maktaba'

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.