ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Friday, May 12, 2023

KOKA AJIPANGA KUWASAIDIA WANAFUNZI KUONDOKANA NA DIVISHENI ZERO.

 


Na Victor Masangu,Kibaha

Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka amewahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii na kuwa na nidhamu katika masomo ili kuongeza kiwango cha ufaulu na kuondokana kabisa  na changamoto ya kupata divisheni zero.

Koka ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wanafunzi na walimu wa shule ya sekondari Visiga iliyopo katika halmashauri ya mji Kibaha wakati wa sherehe maalumu ya kuwakutanisha wadau wa elimu wakiwemo wazazi na walezi ijulikanayo Kama Visiga day.

Mbunge huyo alibainisha kwamba anachukizwa sana na baadhi ya watu kuziita shule za kata majina mabaya yasiyofaa kabisa wakati serikali inatenga kiasi kikubwa kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu hivyo kunahitajika juhudi za makusudi ili wanafunzi wafanye vizuri katika masomo yao.

"Kimsingi ndugu zangu Mimi Kama Mbunge wenu wa Jimbo la Kibaha mjini uwa nachukizwa sana shule zetu za kata kuitwa majina ya kayumba hii sio sawa kabisa kwa sababu uwezo wa kuwafanya wanafunzi wetu wafanye vizuri tunao na kuondokana kabisa na kupata alama ya divisheni zero kukibwa ni kuongeza juhudi,"alisema Koka.

Aidha aliwataka walimu na wazazi kuweka maazimio ya pamoja katika kuweka mikakati madhubuti ambayo itaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kutokomeza kabisa divisheni zero kwa wanafunzi wa shule ya sekondari Visiga pamoja na shule nyingine za kata zilizopo katika Jimbo lake.

Alifafanua kwamba katika kulifanikisha hilo ataendelea kutoa michango yake ya hali na mali ikiwemo kusaidia viti na meza pamoja na kuboresha miundombinu ya vyumba vya madarasa lengo ikiwa ni wanafunzi waweze kusoma katika mazingira rafiki.

Pia alisema kuwa ana Imani kubwa endapo wazazi,walezi pamoja na walimu wakishirikiana kwa pamoja wataweza kuwasaidia Wanafunzi hao kufanya vizuri katika masomo yao na kuondokana kabisa na kupata alama mbaya.

Abasi Kikonyo ambaye ni mkuu wa shule ya visiga alisema kwa sasa shule hiyo inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo uchakavu wa madarasa pamoja na mahitaji mengine ambayo yakifanyiwa kazi yatasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza kiwango cha ufaulu.

Nao baadhi ya wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo ya Visiga waliahidi kuyafanyia kazi yale yote ambayo wameekekezwa kuyafanya na Mbunge huyo wa Jimbo la Kibaha mjini ili waondokane kabisa na kupata alama ya divisheni zero.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.