ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Saturday, March 3, 2018

RPC MWANZA, ASISITIZA ASKARI WAKE KUEPUKA UBAMBIKAJI KESI

 KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Mwanza Naibu Kamishina wa Polisi Ahmed Msangi amewasisitiza askari kuepuka ubambikaji kesi kwa wananchi, rushwa na ubabaishaji pia akiwataka askari kufanya kazi kwa utii, nidhamu na maadili kama ambavyo Jeshi la Polisi Tanzania linavyoelekeza. Hayo yamejiri tarehe 28/02/2018 wakati Kamanda Msangi alipokutana na askari wa Wilaya ya Sengerema katika ukaguzi anaoendelea kuufanya katika Wilaya na Vikosi vyote hapa Mkoani Mwanza.

Amewataka askari kukomesha vitendo vya ubabaishaji kwa wananchi na ubambikaji kesi kama vipo, mfano kesi ya madai inabadilishwa kuwa kesi ya jinai jambo ambalo linanyima haki wananchi na kuchafua sifa nzuri ya Jeshi la Polisi. Hivyo ubabaishaji wa aina hiyo uepukwe na yeyote atakaye bainika anafanya hivyo hatua za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake.

 Sambamba na hilo Kamanda Msangi amewataka askari wa kila kitengo kusimama vyema katika nafasi zao, ambapo alisema kila askari akiwa vizuri katika utendaji kazi hakutakuwa na malalamiko yeyote toka kwa wananchi hivyo ni jukumu la kila askari kuhakikisha dhamana aliyopewa na serikali ya kulinda wananchi pamoja na mali zao  anaisimamia vizuri bila ubabaishaji wa aina yeyote ile.

Pia aliwataka askari wawe na utaratibu mzuri wa upokeaji, utunzaji na uondoshaji wa vielelezo katika vituo vya Polisi, kwani katika baadhi ya vituo vya Polisi lipo tatizo la utunzaji wa vielelezo hivyo hataki kuona tatizo hilo linaendelea kuwepo. Vilelele aliwataka Maofisa wa Polisi wa Wilayani hapo kuzingatia taratibu zilizowekwa kisheria za uondoshaji wa vielelezo katika vituo vya Polisi.


Hata hivyo alisema hategemei kuona mlundikano wa vielelezo katika vituo vya Polisi ambavyo vimekaa vituoni mwaka mmoja au zaidi. Kwani madhara yake vinaweza kuharibika, kupoteza ubora au kupotea alafu baadae liwe deni kwa Jeshi. Hivyo aliwataka askari kutekeleza maamuzi ya mahakama haraka juu ya uondoshaji wa kielelezo/vielelezo baada ya kesi kumalizika mahakamani.

Kwa upande wa upelelezi alisema kumekuwa na tatizo la kuchelewesha upelelezi wa kesi nyingi. Jambo ambalo linawanyima wananchi haki. Hivyo alimtaka Mkuu wa Upelelezi Wilayani hapo kushughulikia suala hilo mapema lisiwepo katika himaya yake ili haki ipatikane haraka bila uonevu wa aina yeyote.

Pia aliwapongeza askari wa Wilaya hiyo kwa utendaji mzuri wa kudhibiti uhalifu, aliwataka waongeze juhudi kwa yale maeneo yenye vibaka na uhalifu mwingine mdogomdogo kwani anaamini wanaweza. Ushirikiano ulipo na Viongozi wa ulinzi na usalama Wilaya, Wananchi na vyombo vingine vya ulinzi na usalama udumishwe ili Sengerema iwe salama zaidi kwani amani ikiwepo maendeleo yatapatikana zaidi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.