ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Thursday, April 28, 2011

MRITHI WA TIDO TBC APATIKANA

RAIS Jakaya Kikwete amemteua Clement Mshana kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Tido Mhando.Taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, imesema kwamba Mshana ambaye kabla ya uteuzi huo alikuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo). Anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Dunstan Tido Mhando ambaye amemaliza muda wake wa utumishi kwa mujibu wa mkataba wake.

Hata hivyo, Tido aliwahi kukaririwa akilalamika kwamba licha ya mkataba huo kumalizika, hakupewa fursa ya kujadiliana na mwajiri wake ili kuuongeza.

Mbali ya uteuzi huo, Rais Kikwete pia amewateua manaibu katibu wakuu 10 katika wizara mbalimbali. Miongoni mwa walioteuliwa ni Bashir Mrindoko ambaye sasa anakuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji. Kabla ya uteuzi huo, alikuwa Kamishna wa Nishati na Mafuta ya Petroli.

Pia amemteua Mhandisi John Ndunguru kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi. Awali, alikuwa ni Mkurugenzi wa Ufundi na Umeme wizarani hapo.Wengine walioteuliwa na nafasi zao za zamani katika mabano ni Charles Pallangyo, Naibu

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Mkurugenzi wa Uratibu wa ofisi hiyo). Mhandisi Mwamini Malemi, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi (Msaidizi wa Makamu wa Rais, Maendeleo ya Jamii na Uratibu wa Malalamiko ya Wananchi).

Mhandisi Musa Iyombe, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi (Mkurugenzi wa Miundombinu ya Usafiri, Wizara ya Ujenzi). James Mngodo, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Uchukuzi (Mkurugenzi wa Uhakika wa Chakula), Anna Maembe, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto (Mkurugenzi wa Mazingira na Habari wa Baraza la Taifa la Mazingira-NEMC).

Sihaba Nkinga, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, (Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Uchukuzi.) Aphayo Kidawa, Naibu Katibu Mkuu, Ikulu (Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi). Habib Mkwizu, Naibu Katibu Mkuu, Menejimenti ya Utumishi wa Umma (Karani katika Baraza la Mawaziri). Kwa mujibu wa taarifa hiyo. Uteuzi huo ulianza juzi Aprili 21, mwaka huu.

Wakati huohuo, Rais Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa watu walioathirika na mafuriko mkoani Morogoro na kukosa mahali pa kuishi baada ya nyumba zao zaidi ya 200 kuharibiwa vibaya. Mvua hizo zilinyesha katika Milima ya Udzungwa na Mahenge kati ya Aprili 19 na 25, mwaka huu.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.