ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Tuesday, March 29, 2016

RAIS DK MAGUFULI AGIZA KUFUNGULIWA KWA BARABARA YA AIRPOT - IGOMBE (km7) ILIYOFUNGWA TANGU 2014 KUPISHA UPANUZI WA UWANJA WA NDEGE WA MWANZA.

Ndege iliyomleta Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Magufuli ikiwa katika harakati za kutua kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Magufuli akishuka uwanja wa ndege wa Mwanza.

NA. PETER FABIAN 
G.SENGO BLOG
RAIS Dk John Magufuli, ameamuru kufunguliwa kwa barabara ya Airpot-Igombe hadi Kayenze yenye urefu wa km.7 iliyofungwa kupisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa mwanza tangu mwaka 2014 na kusababisha usumbufu kwa wananchi waliokuwa wakiitumia wilayani Ilemela mkoani Mwanza.

Salaam salaaam........!!!
Kauli hiyo ya Rais Dk Magufuli ameitoa leo alipotua katika uwanja wa ndege wa Mwanza kabla ya kuelekea nyumbani kwake wilayani Chato mkoani Geita kwa mapumziko wakati akizungumza na viongozi wa serikali mkoa, vyama vya siasa, madhehebu ya dini, wananchi na waandishi wa habari waliokuwepo kumpokea.

“Nafahamu suala linalowaumiza wananchi la kufungwa kwa barabara hii ya Airpot-Igombe (km7), sasa naagiza kuanzia sasa (leo) kufunguliwa kwa barabara hiyo ili wananchi watumie kupita ili kuondoa usumbufu wa kuzunguka kule maeneo ya Nyakato hadi maeneo ya TX Kata ya Bugogwa, Kata ya Sangabuye,”alsema.

Rais Dk. Magufuli amesema kwamba, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongela, natumia fursa hii kukuagiza kufunguliwa kwa barabara hii ambayo natambua inapita pembezoni mwa uwanja huu lakini serikali itaangalia juu ya kuupanua zaidi kuelekea eneo la mashariki ili kutoa nafasi ya barabara kutumiwa na wananchi wa maeneo haya.

“Serikali katika bajeti yake ya mwaka 2016/2017 tumepanga kutoa fedha kwa lengo la kuhakikisha ujenzi wa uwanja huu unaoboreshwa kuwa wa kisasa ili kuwezesha ndege kubwa kutua kwa wingi lakini pia kutumiwa kimataifa na nchi za Maziwa Makuu kama tulivyoahidi wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa 2015,”alisema.

Rais Dk Magufuli pia amesisitiza kwa kusema kuwa “kamwe sitaki kusikia tena uwanja huu umefungwa na uongozi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini (TAA) kuangalia kuupanua zaidi kwenda mashariki ili barabara hii pia waitumie wananchi na tutatoa fedha ili ijengwe kwa kiwango cha lami hata kama ni kwa awamu,”alisisitiza.

Asalimia Abiria.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida mara baada ya kusalimiana na viongozi mbalimbali waliofika kumpokea alipowasili majira ya saa 5:15 asubuhi uwanjani hapo ghafla alikwenda eneo walipokuwa wamesimama watumishi wa uwanja huo na kuwasalimia kwa kushikana nao mikono.

Wakati akiongozwa na maafisa wa Idara ya Usalama kuelekea mlango wa VIP ili kuongea na baadhi ya viongozi wa mbalimbali wa Mkoa wa Mwanza, Rais Dk Magufuli ghafla  alielekea mlango wa chumba cha kupumzikia abiria na kulazimisaha kufunguliwa mlango ili kusalimiana nao na kuacha mshangao kwa wananchi na viongozi.

Abiria waliokuwa wakisubiri kusafiri na ndege kuelekea jijini Dar es salaam na Bukoba na kwingineko walifurahi kumuona Rais Dk Magufuli na kuchangamkia kusalimiana kwa kushikana naye mikono na kuonyesha furaha kwa kitendo hicho cha kumuona kiongozi wao huku baadhi wakidai ni jambo lisilo la kawaida.

Rais Dk Magufuli aliwapongeza kwa sala na dua viongozi wa madhehebu kwa kuendelea kumuombea ili kuweza kuwatumikia wananchi bila kuwabagua kwa itikadi zao za kisiasa na kusisitiza kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa kufanya kazi bila kuchoka ili kila mtanzania aweze kunufaika na rasilimali zilizopo nchini kisha kuomba ushirikiano kwa wananchi wote ili kufikia malengo.
  
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na mkewe Mama Janeth Magufuli pamoja na viongozi wa mkoa wa Mwanza wakijipatia chakula cha mchana katika mgahawa wa Victoria uliopo nye ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza alipopumzika kwa muda kabla ya kuelekea nyumbani kwake Chato mkoani Geita kwa mapumziko mafupi. Pamoja nao mezani hapo ni Meya wa Ilemela Mstahiki Renatus Mulunga, Meya wa jiji la Mwanza Mstahiki James Bwire, Mkuu wa Mkoa wa MWanza  Mhe John Mongella na Mwenyekiti wa CCM Mkoa huo Ndg Anthony Diallo.
Ala chalula mghahawa wa nje ya uwanja.
Baada ya kuzungumza na baadhi ya viongozi wa mkoa ndani VIP, ghafla alitoka nje na kuelekea eneo la mighahawa iliyopo nje ya uwanja wa ndege wa Mwanza na kuingia katika moja ya mghahawa na kusalimiana na wateja na wananchi waliokuwa katika maeneo hayo kisha kuagiza chakula na kutoa ofa ya Sh 100,000/= ili wapewe soda na maji kwa watu wote waliokuwepo.

Rais akiwapungia mikono wananchi waliojitokeza kumlaki uwanja wa ndege Mwanza mara baa ya kutoka kupata chakula cha mchana kwenye mgahawa mdogo wa Victoria Catering,
Kutokana na tukio hilo mmoja wa wasimamizi wa mghahawa huo aliokaa Rais Dk Magufuli na baadhi ya viongozi wakiwemo madhehebu ya dini na serikali, alieleza kufurahishwa kwake na kuahidi kubadilisha jina la mghahwa wake na kuupatia jina la Dk Magufuli Cafe ili kuenzi kufika kwake na kula chakula hapo ukizingatia kuwa ni kiongozi mkubwa wanachi.

Huku viongozi wa madhebu ya dini wamuombea sala na dua ili kuendelea kuwatumikia watanzania bila kuchoka na kuhakikisha amani na umoja wa taifa unaendelea kuwa tunu, lakini pia katika dua na sala zao wamemuhakikishia Rais Dk Magufuli kuendelea kumuombea na kumpatia ushirikiano wao ili aweze kutekeleza majukumu yake akiwa na nguvu na afya njema.
Victoria Catering ni mgahawa aliokula chakula cha mchana Rais Magufuli na Mkewe, ghafla umegeuka kuwa maarufu.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongela akizungumza mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Magufuli, uwanja wa Ndege wa Mwanza.
RC Mongela anena
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongela, mara baada ya Rais Dk Magufuli kuondoka katika uwanja wa ndege wa mwanza kuelekea nyumbani kwake wilayani Chato mkoani Geita kwa mapumziko, alieleza kutekeleza agizo la Rais la kufunguliwa kwa barabara ya Airpot-Igombe kwa kufika maeneo hayo ya wananchi katika Kata ya Bugogwa kufikisha ujumbe huo.

“Baada ya kuondoka Rais mimi na viongozi wa Kamati ya Ulizi na Usalama Mkoa, Wilaya pamoja na uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Meneja wa Tanroad Mkoa wa Mwanza na viongozi wa CCM wilaya ya Ilemela tunaongozana kuelekea eneo la TX Kata ya Bugogwa ili kufikisha ujumbe uliotolewa na Rais Dk Magufuli ili wananchi watumie barabara hii kuanzia sasa,”alisema.

Mongela alipongeza kamati ya amani ya mkoa inayoongozwa na viongozi wa madhehebu ya dini pamoja na viongozi wa serikali na vyama vya siasa vilivyoshiriki katika tukio la mapokezi wakiwemo wananchi wa Wilaya za Ilemela na Nyamagana na kuonyesha ushirikiano ambao ameomba uendelee.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.