ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, March 16, 2015

MWILI WA SYLVESTER MARSH WAWASILI JIONI HII JIJINI MWANZA KUZIKWA KESHO ALASILI

Badrudian Nsubuga aliyeteuliwa kuwa mwenyekiti wa Kamati ya Mazishi (kushoto akiweka mipango mezani mbele ya wanakamati wenzake Jumanne Shengelo ambaye ni Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Mkoa wa Mwanza MZFA (kulia), Mr. Sado na mdau wa viongozi toka Ofisi za halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Nyumbani kwa marehemu Marsh . 
HATIMAYE mwili wa aliyekuwa Kocha Msaidizi wa Timu ya Taifa ya Mpira wa miguu Sylivester Marsh umewasili jioni ya leo ukitarajiwa kuagwa kesho katika Uwanja wa Mirongo Jijini Mwanza, kabla ya kwenda kuzikwa katika katika makaburi ya Igoma Jijini hapa.
BOFYA PLAY KUSIKILIZA TAARIFA 

Badrudin Nsubuga ambae ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mazishi ya Marehemu Marsh, amesema kuwa shughuli ya kuuaga mwili wa marehemu unatarajiwa kufanyika kesho kuanzia majira ya saa 06:00 asubuhi hadi saa 12:00 mchana katika Uwanja wa Shule ya Msingi Mirongo, ambapo kuanzia muda huo mwili huo utapelekwa nyumbani kwao Igoma kabla ya kwenda kupumzishwa katika nyumba yake ya Milele katika Makaburi ya Igoma.
Mjane wa Marehemu Marsh Bi.Asha Sylivester Marsh (wa pili kutoka kushoto) akiwa na watu wake wa karibu waliofika msibani kumpa pole.
Mjane wa Marehemu Marsh Bi.Asha Sylivester Marsh ameelezea kupokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa Marehemu Mars ambapo amebainisha kuwa bado alikuwa akimhitaji zaidi Marsh kwa ajili ya malezi ya watoto ambao bado ni wadogo na wanasoma.

Zaidi amewahusia wanamichezo nchini kufuata nyayo za Marehemu Marsh katika utendaji wake wa kazi sanjari na kuwapenda na kuwashauri vyema watu wote kubwa zaidi kupenda kuibua na kuendeleza vipaji kwa wanamichezo kama Marehemu Marsh alivyokuwa akifanya.

Nae Jumaine Shengelo ambae ni Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Mkoa wa Mwanza MZFA amemuelezea Marehemu Mwalimu Marsh kuwa katika enzi za uhai wake wakati akicheza mpira, alikuwa ni kijana mtulivu na mwenye nidhamu uwanjani ambae alikuwa na mwamko wa kimichezo hali iliyomsukuma pia kuanzisha kituo cha michezo pamoja na Timu ya Soka ya Marsh Athletic Academy.

Aidha ameongeza kuwa jambo ambalo angependa kuliweka wazi ni kwamba Timu ya Marsh Athletic Academy haitakufa, kwa sababu ameacha watu ambao wataweza kuiendeleza kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Nae Samiry Omary ambae ni Mchezaji wa timu ya Soka ya Marsh Athletic Academy amesema kuwa wachezaji wa timu hiyo wameupokea kwa masikitiko makubwa msiba wa Marehemu Mwalimu Marsh kwa kuwa bado walikuwa wakimhitaji na walikuwa wameahidiana mambo mengi ya kimichezo ambapo wamewaomba wadau michezo wajitokeze katika kuiendeleza aliyoiacha ya Marsh Athletic Academy.
Blogger George Binagi (kulia) akifanya mahojiano na baadhi ya wanakamati wa mazishi kutoka kushoto ni Chaku Master, Mr. Hamza Yusuph Shido, Badrudin Nsubuga ambae ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mazishi, Almasi Moshi Almasi.
Akizungumza kwa masikitiko Makubwa Hamza Yusuph Shido ambae ni Mdau wa Michezo na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Utemini Kata ya Mirongo ulipo Msiba wa Marehemu Mwalimu Marsh, amesema kuwa wanamichezo wamesikitishwa kwa kitendo cha mwili wa Marehemu Mwalimu Marsh kusafirishwa kwa njia ya barabara (Kwa gari/ Coaster) kutoka Jijini Dar es salaam ukilinganisha nafasi aliyokuwa nayo katika Soka la Tanzania.

Amesema amesikitishwa namna Chama cha Soka Mkoani Mwanza MZFA pamoja na Shirikisho la Soka nchini TFF walivyoshindwa kumuenzi Marehemu Mwalimu Marsh hususani kwa namna mwili wake ulivyosafirishwa sanjari na katika michezo ya ligi kuu ya Tanzania bara iliyochezwa jana kushindwa kuonyesha ishara ya aina yoyote ya kumuenzi marehemu Marsh.
Mchezaji wa zamani wa Yanga Africans Edibilly Jonas Lunyamila (kushoto) akiwana rafiki yake wa dhati ambaye pia ni mchezaji wa zamani toka klabu ya Pamba na Taifa Stars Juma Amir Maftah.


Marehemu Mwalimu Sylivester Marsh alizaliwa mwaka 1960 na alifariki juzi jumamosi March 14 alfajiri akiwa katika Hospitali ya Taifa Mhimbili kwa ajili ya Matibabu ya Saratani ya Koo ambapo enzi za Uhai wake aliwahi kuwa mchezaji wa timu mbalimbali za soka hapa nchini ikiwa ni pamoja na Kufundisha Klabu kadhaa za Soka ambazo ni pamoja na Kagera Sugar pamoja na Azam FC ambapo pia amewahi kuwa Kocha Msaidizi wa Timu ya Taifa ya Soka.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.