ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Monday, July 23, 2012

WAZAZI WANAODAIWA KUWATELEKEZA WATOTO WAJISALIMISHA Polisi

Na Shomari Binda
Musoma,

Wazazi wanaodaiwa kuwatelekeza watoto wao watatu na kuwasababishia kuishi maisha ya kutangatanga mitaani leo wamejisalimisha katika kituo kikuu cha Polisi mjini Musoma kitengo cha dawati la jinsia na watoto baada ya vyombo vya Habari kutangaza tukio hilo huku kila mmoja akimtupia mwenzake lawama kwa kile kilichosababisha watoto hao kuishi maisha hayo.

 Akizungumza mbele ya jopo la wana dawati pamoja na waandishi wa habari,mama wa watoto hao Paulina kichere alimshushia lawama mzazi mwenzake Kichere Sangi kwa kile alichokieleza mara baada ya kutaarikiana mwaka 2007 mahakama ilimtaka kukaa na watoto hao kutokana na mama kutokuwa na uwezo wa kuwatunza lakini mara baada ya mzazi mwenzake kuoa wanawake wengine wawili watoto hao wamekuwa wakilalamika kutokuwa na malezi mazuri.

Amesema mara kadhaa watoto hao wamekuwa wakimfata na kulalamika kupewa kazi zinazowazidi uwezo mara baada ya kutoka shuleni huku watoto wengine ambao mwanaume huyo amezaa na wanawake wengine aliowaoa wakipata muda wa kusoma na kushindwa kufanya kazi nyingine za nyumbani.

Paulina amesema licha ya mji ambao waliangaika kuujenga kwa pamoja katika maisha yao ya ndoa kuuacha kwa ajili ya malezi ya watoto anashangaa kitendo cha mzazi mwenzake kuacha watoto wakiteseka mtaani huku akijua yeye kwa upande wake hana uwezo wowote wa kuwatunza kutokana na kutokua na kazi ya kumuingizia kipato chochote.

Amesema yeye kwa upande wake hawezi kuangalia watoto wake wakiishi maisha ya kuangaika kama angekuwa na uwezo wa kuishi nao na kuomba vyombo vya sheria viweze kuliangalia suala hilo kwa mapana ili kuwaepusha watoto hao na maisha ya mitaani.

Kwa upande wake baba wa watoto hao Justine Kichere (14) James Kichee (13) na Gerald Kichere (12) Kichere Sangi amesema licha ya kuwa anashinda katika shughuli zake muda mwingi hana uhakika kama watoto hao wanaishi maisha ya kuteswa kutokana na kutokupata taarifa hizo.

Amesema licha ya kutengana na mama wa watoto hao amekuwa akiishi nao bila kubaguliwa na kudai kuwa watoto hao waliondoka nyumbani bila yeye kuwa na taarifa na alijua walikuwa wamekwenda kwa mama yao kama ambavyo wamekuwa wakifanya mara kwa mara.

Afisa mmoja katika kitengo cha dawati la jinsia na watoto kutoka jeshi la Polisi ambaye hakutaka kutajwa jina lake kwa kuwa sio msemaji amesema baada ya kufika kwa wazazi hao katika ofisi hiyo walizungumza nao huku kila mmoja akimlushia lawama mwenzake juu ya malezi ya watoto hao na walichokiamua cha kwanza ni kulipeleka suala hilo katika ofisi ya afisa Maendeleo ya Jamii kwa hatua zaidi juu ya malezi ya watoto hao.

Amesema licha ya kulipeleka suala hilo katika ofisi ya afisa Maendeeo ya Jamii wataendelea kulifuatilia kwa karibu kujua hatima ya watoto hao na malezi yao ili kuweza kupunguza ongezeko la watoto wa mitaani na ofisi ya dawati la jinsia na watoto halita sita kuwafungulia mashitaka wazazi wote ambao bila sababu za msingi wanazalisha wtoto wa mitaani.

Siku tatu zilizopita Watoto hao watatu waliwafikisha wazazi wao katika kituo kikuu cha Polisi Mjini Musoma kitengo cha dawati la jinsia na watoto wakidai kutelekezwa na kuwafanya kuishi maisha ya kutangatanga mitaani ili hali wazazi wao wakiwepo na kuendelea na maisha ya kila siku bila kujua wao wanaishi vipi.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.