ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, September 7, 2011

IGUNGA MAMBO YAMEIVA....!! SEIF WA CUF ATUA JIMBONI HUMO KUONGEZA NGUVU

Amesema uzoefu unaonyesha shughuli za siasa hasa zinazoratibiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), zimekuwa zikiingiliwa na vyombo hivyo jambo ambalo siyo sahihi.

Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), aliyasema hayo mjini Igunga baada ya kuwasili akitokea Tabora. Alipokewa na Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Fatuma Kimario.

“Hivi sasa macho ya Watanzania wote yapo Igunga kuangalia nini kitatokea na nimeambiwa vyama tisa vya siasa vimeweka wagombea kushiriki uchaguzi huu.

“Ninaiomba Kamati ya Ulinzi na Usalama kuwa makini katika kusimamia jukumu zima la usalama kwa kipindi chote cha kampeni hadi uchaguzi utakapofanyika.

“Mara nyingi hisia zimekuwa zikionyesha vyombo hivi vinaingilia uchaguzi. Ninakuomba Mkuu wa Wilaya hili lisitokee kwani hata sisi tutakusaidia lisitokee,” alisema Seif.

Pamoja na maelezo mengi aliyotoa, mwanasiasa huyo alionyesha hofu kwa kusema kuwa matatizo wakati wa uchaguzi mara nyingi hutokea wakati wa kujumlisha kura kwa kuwa wakati huo ndiyo baadhi ya watu hutaka kufanya hujuma.

“Hatupendi kuona vyombo mnavyoviongoza vikiingilia uchaguzi na hata kulazimika kutumia nguvu kubwa ya mabomu kuwatisha wananchi kwa sababu matatizo mara nyingi hutokea wakati wa majumuisho ya kura,” alisema.

Akizungumzia vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi huo, alivitaka kufanya kampeni za ustaarabu kwa kufuata taratibu zilizowekwa na NEC kwa kuwa kila chama kina ratiba ya uchaguzi huo.

Katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu wa CUF Tanzania Bara, Julius Mtatiro, alimtambulisha mgombea wa chama hicho, Leopold Mahona.

Katika hali isiyotarajiwa, jana mchana misafara ya wafuasi wa vyama vya CUF na CHADEMA, iligongana njiani wakati wagombea wa ubunge walipokuwa wakirudisha fomu katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya ya Igunga.

Baada ya misafara hiyo kugongana, wafuasi wa vyama hivyo walirushiana maneno ya kejeli huku kila upande ukisema utashinda katika uchaguzi huo.

Katika tukio hilo, mgombea wa Chadema alikuwa amepita njia tofauti kuelekea ofisini kwa Mkurugenzi na mgombea wa CUF alikuwa amepita njia nyingine lakini wakakutana katika makutano ya barabara.

Baada ya kurushiana maneno kwa muda, misafara hiyo ilitengana njia lakini pande hizo mbili zilikutana tena katika ofisi za Mkurugenzi.

Pamoja na kurushiana maneno, pande hizo zilianza kuelewana baada ya viongozi wa misafara hiyo kuzungumza kirafiki.


Hisani ya MTANZANIA.

Tupe maoni yako

0 comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.